Watu wa kawaida pia wanaweza kuweka historia, hata kusafiri anga za juu

ldleo

JF-Expert Member
Jan 9, 2010
1,010
1,034
VCG111377820225.jpg


VCG111377860365.png


Aprili 16, wanaanga watatu wa China waliokwenda anga ya juu kwa Chombo cha Shenzhou No. 13 walirejea nyumbani salama wakiwa na hali nzuri kiafya. Katika kipindi cha miezi sita iliyopita, wanaanga hawa waliweka historia mbalimbali mpya katika sekta ya safari za anga ya juu ya China. Wanaanga hawa wanaotajwa na Wachina kama ni “mashujaa wa kitaifa” hawatoki katika familia za wazazi matajiri au wasomi, ila kinyume chake maisha yao ya utotoni yalikuwa magumu zaidi kuliko ya watu wengi wa kawaida.



Mwanaanga Zhai Zhigang alizaliwa Oktoba 1966, katika familia maskini, kaskazini mashariki mwa China. Kwa sababu afya ya baba yake ilikuwa mbaya, mama alimsomesha Zhai kwa kuuza mbegu za maboga barabarani mpaka alipomaliza shule ya upili. Lakini baadaye Zhai alipoomba kuacha shule ili kusaidia kuhudumia familia, alikataliwa na mama… "Unawezaje kufanikiwa bila ya kusoma?" Alipofikia umri wa miaka 19, Zhai aliingia katika chuo cha safari za anga. Katika muda wa miaka mitatu ya masomo, Zhai hakuzembea hata kidogo. Baada ya kuhitimu, alifanikiwa kujiunga na Kikosi cha Wanaanga cha Jeshi la Ukombozi la Watu wa China, kilichokuwa ndio kwanza kianzishwe wakati huo, na kuwa mmoja wa wanaanga 14 wa kwanza wa China. Baada ya miaka 10 ya mafunzo makali ya kila siku, hatimaye Zhai akawa mwanaanga wa kwanza wa China kutembea kwenye anga ya juu, jambo ambalo pia liliifanya China kuwa nchi ya tatu duniani kutimiza lengo hilo.



Wang Yaping ni mwanaanga pekee wa kike katika jukumu la Shenzhou No. 13. Alizaliwa katika familia ya wakulima wa kawaida, mashariki mwa China, na wazazi wake walimsomesha shuleni kwa kulima pilipili doria. Mwaka 2003, alipomwona Yang Liwei, mwanaanga wa kwanza wa China kufika kwenye anga ya juu, Wang Yaping alijisemea moyoni, “Kama China ina mwanaanga mwanaume, lazima awepo na mwanaanga wa kike pia.” Bila shaka, anga haina upole kwa mwanamke. Hata hivyo, Wang alitumia uwezo wake kuthibitisha msemo wa jadi wa Kichina, “wanawake wanabeba nusu ya anga”. Leo, amekuwa mwanaanga wa kwanza wa kike wa China kufika kwenye kituo cha anga za juu.



Ye Guangfu, mwenye umri sawa na Wang, anatoka katika familia ya wakulima magharibi mwa China. Ili kumsomesha shuleni, mama yake alibeba maji mlimani kwa ajili ya kumwagilia miti, ili kuchuma pesa zaidi za kuhudumia familia. Baada ya miaka zaidi ya 20 ya kusoma na kufanya kazi kama rubani na mwanaanga, mwaka 2016, akiwa mchina wa kwanza kushirikiana na wanaanga wa kimataifa katika mafunzo ya kimataifa, aliungana na wanaanga kutoka Marekani, Russia, Hispania na Japan kushiriki kwenye mafunzo ya utafiti wa pango yaliyoandaliwa na Shirika la Safari ya Anga ya Juu la Ulaya ESA. Baada ya kuwaongoza wanaanga wengine kugundua tawi jipya la pango, hatimaye ESA iliamua kuita tawi hilo kwa jina lake.



Kutokana na maisha ya Zhai Zhigang, Wang Yaping na Ye Guangfu, niliona upo uwezekano wa Wachina wa kawaida kutimiza ndoto zao. Wao wote wana kitu kimoja kinachofanana - walizaliwa katika maisha ya umaskini, lakini kupata elimu kwa usawa bila ya kuangalia historia, uchumi na uzoefu wa familia za watoto kumewaruhusu kupata “tiketi” ya kufika kwenye anga ya juu. Mwaka 1986, China ilitangaza Sheria ya Elimu ya Lazima, na kufanya upatikanaji wa elimu sawa kwa wote kufikia kwenye ngazi ya kitaifa. Mwaka 2001, China ilifikia lengo la kimsingi la elimu ya lazima ya miaka tisa kwa wote na kutokomeza tatizo la kutojua kusoma na kuandika miongoni mwa vijana na watu wazima kama ilivyopangwa, ambapo kiwango cha elimu ya lazima cha miaka tisa kilifikia 85%, na kiwango cha vijana watu wazima wasiojua kusoma na kuandika kilishuka hadi 5%, lakini kiwango hicho kilikuwa ni zaidi ya 80% mwaka 1949 wakati Jamhuri ya Watu wa China ilipoasisiwa. Kwa mujibu wa waraka wa "Maisha bora kwa pande zote China" uliotolewa mwaka jana na Baraza la Serikali ya China, mnamo mwaka 2020, kiwango cha kumaliza elimu ya lazima ya miaka tisa cha China kilifikia 95.2%, yaani 95.2% ya wanafunzi walioingia darasa la kwanza la shule ya msingi walihitimu kwenye shule ya upili; viwango vya uandikishaji kwenye shule ya sekondari ya juu na vyuo vikuu vilikuwa 91.2% na 54.4% mtawalia. Hii inaashiria kwamba kiwango cha elimu cha China kimeongezeka hadi kufikia kwenye ngazi ya wastani na juu duniani, na lengo la kuwezesha kila mtoto afurahie elimu ya haki na bora linabadilika kuwa hali halisi.



Wakati huo huo, usawa kati ya wanaume na wanawake umefanya mafanikio ya "Wang Yaping" yapatikane. Kwa hakika, vuguvugu la ukombozi wa wanawake wa China lilianza muda mrefu kabla ya kuanzishwa kwa taifa. Hayati mwenyekiti Mao Zedong alisema mwaka 1938 kuwa, “Siku ambayo wanawake wanainuka katika nchi nzima ndiyo wakati ambapo mapinduzi ya China yatashinda.” Katika miaka ya hivi karibuni, wanawake wa China wamestawi katika nyanja mbalimbali, na hivyo kuionyesha zaidi dunia uwezo wa wanawake. Tumemwona Tu Youyou, aliyeshinda Tuzo ya Nobel akiwa na umri wa miaka 85 kwa kuchangia juhudi za kutokomeza ugonjwa wa malaria duniani; Zhang Guimei, mwalimu ambaye amejikita katika maeneo maskini ya milimani kwa miaka 40 na kuwapeleka wasichana wengi waliotoka familia duni kwenye vyuo vikuu; Pia tumeona msomi mwenye umri wa miaka 73 Li Lanjuan, akiwa katika mstari wa mbele wa vita dhidi ya COVID-19 mjini Wuhan, na afisa mkuu wa fedha wa kampuni ya mawasiliano ya simu ya Meng Wanzhou, ambaye alizuiliwa kinyume cha sheria nchini Canada kwa miaka mitatu lakini hakukata tamaa, na mwishowe akarudi nyumbani hapa China.



Hatimaye, ningependa kusema kwamba kutoka kwa wanaanga hao watatu, tumeona kwamba umri, jinsia, na familia si visingizio vya sisi kuacha juhudi zetu; vilevile mafanikio ya jukumu la chombo cha anga ya juu cha Shenzhou 13 sio yao binafsi, pia ni safari ya kufikia nyota ambayo China imepata baada ya miaka mingi ya kazi ngumu. Ninaamini kwamba katika siku zijazo, watu wa kawaida zaidi watachangia mafanikio ya China katika masuala ya anga na nyanja nyinginezo.
 
Back
Top Bottom