diana chumbikino
JF-Expert Member
- May 29, 2018
- 428
- 368
HOSPITALI ya Taifa ya Muhimbili, tawi la Mloganzila, imeendelea na ongezeko la asilimia 17.8 la wagonjwa wa nje wanaopata matibabu licha ya kuwapo na changamoto mbalimbali
Katika kipindi cha robo ya kwanza ya mwaka, wamehudumia wagonjwa 20,173 ikilinganishwa na kipindi kama hicho mwaka uliopita walipohudumia wagonjwa 17,116. Kaimu Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili-Mloganzila, Dk. Julieth Magandi, aliyaeleza hayo juzi katika kikao cha bodi ya uongozi wa MNH kujadili mafanikio na changamoto za tawi la Mloganzila katika kipindi cha robo ya kwanza ya mwaka wa fedha. Dk.
Magandi alisema upande wa wagonjwa waliolazwa kulikuwa na ongezeko la asilimia 29.6 kutoka wagonjwa 1,459 hadi 1,891, wakati upande wa huduma za upasuaji jumla ya wagonjwa 649 walifanyiwa upasuaji ukilinganisha na upasuaji wa wagonjwa 267 katika robo ya kwanza ya mwaka huu wa fedha ambalo ni ongezeko la asilimia 143 .
Kwa upande wa huduma za tiba shirikishi inayojumuisha maabara na huduma za radiolojia alisema maabara ilipokea jumla ya sampuli za vipimo mbalimbali 28,907 kwa wagonjwa waliolazwa na wa nje ukilinganisha na sampuli 16,233 katika robo ya kwanza ya mwaka .
Dk. Magandi alisema katika huduma za radiolojia zinazojumuisha vipimo vya CT Scan, MRI na X-ray kulikuwa na ongezeko la asilimia 47 na vipimo 5,221 vilipimwa katika kipindi hicho ukilinganisha na vipimo 3,541 na huduma katika maeneo yote ya hospitali zinaendelea kuimarishwa siku hadi siku. Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya MNH, Prof. Charles Majinge, iliupongeza uongozi wa hospitali hiyo kwa kuboresha huduma za afya kwa wananchi tawi la Mloganzila
“Nafahamu kumekuwa na changamoto kadhaa katika hospitali hii ya Mloganzila, lakini nafurahi kuona kila siku menejimenti inavyotatua changamoto hizo na hivyo wananchi kuitikia wito wa kutumia huduma zinazopatikana hapa,” aliema Prof. Majinge.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Muhimbili, Prof. Lawrence Museru, alisema pamoja na hospitali hiyo kukabiliwa na changamoto mbalimbali, menejimenti imejipanga kuhakikisha inatoa huduma za kibingwa na za kibobezi kama ilivyokusudiwa. Oktoba 3, mwaka 2018, serikali iliiweka Hospitali ya Taaluma na Tiba ya Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MAMC) Mloganzila chini ya Mamlaka ya Usimamizi na Uendeshaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili.
Hospitali ya Mloganzila ina vitanda 608 na inatoa huduma za tiba za kibingwa na kibobezi, mafunzo na utafiti na ilifunguliwa Novemba 25, mwaka 2017 na Rais John Magufuli.