SIKU moja baada ya baadhi ya vigogo wa chama kipya cha kisiasa cha CCJ kutimkia Chadema, katibu mkuu wa chama hicho, Renatus Muabhi amesema uamuzi wa waliohama unatokana na uchu wa madaraka.
Akizungumza na Mwananchi jijini Dar es Salaam jana Muabhi alieleza kuwa uamuzi wao hautakiua chama hicho kilichoanzishwa kwa kishindo lakini kikakosa usajili wa kudumu kukiwezesha kushiriki uchaguzi wa mwaka huu.
Alisema kitendo cha viongozi hao kutangaza kugombea ubunge kwa tiketi ya Chadema kinaonyesha kuwa walijiunga na CCJ kutafuta umaarufu binafsi na uchu wa madaraka.
Kwa mujibu wa Muabhi kama vigogo hao wangekuwa na dhamira ya kweli ya kujenga siasa zilizoanzishwa na sera nzuri ya CCJ, wasingehama chama hicho.
Kuhusu hatua ya viongozi hao kumlalamikia Msajili wa Vyama vya Siasa, Muabhi alisema madai yao hayana msingi kwani usajili wa chama hufanywa kwa mipango na sio kukurupuka.
"Chama cha Jamii (CCJ) hakikuanzishwa kwa ajili ya kushiriki uchaguzi mkuu wa mwaka huu pekee; ni chama chenye malengo mengi na ya muda mrefu. Sisi baada ya kuondoka hao, tutakutana, tufanye uchaguzi ili tuendelee na taratibu za kukisajili chama chetu," alisema Muabi.
Muabi alieleza dhamira ya CCJ kurejesha misingi bora iliyoachwa na Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere bado ipo na chama kinaendelea kuhakikisha kinafikia lengo hiyo.
"Ingawa uamuzi wa mtu kujiunga na chama chochote cha sisasa ni haki yake, kikatiba hawa ndugu zangu wamepoteza mwelekeo kwa kuchagua njia ya mkato ya kujitafutia madaraka," alisema Muabi.
Juzi CCJ ilimpoteza mwanachama wake maarufu, Fred Mpendazoe baada ya mbunge huyo wa zamani wa Kispahu kutangaza kujiunga na Chadema.
Pia mwenyekiti wa chama hicho, Richard Kiyabo, naibu katibu mkuu, Nickson Ng'ihily na msemaji wa CCJ, walikabidhiwa kadi za Chadema jijini Dar es Salaam na mwenyekiti Freeman Mbowe.
Muda mfupi baada ya kupokea kadi hizo, viongozi hao walitangaza nia kugombea ubunge katika majimbo tofauti nchini kwenye uchaguzi mkuu uliopangwa kufanyika Oktoba 31.
Mpendazoe ametangaza nia ya ubunge wa jimbo la Segerea, wakati Kiyabo atagombea Bukene na Ng'ihily anagombea jimbo la Temeke.
source: gazeti la mwananchi