Utajiri wa damu

Utajiri wa damu

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Joined
Feb 3, 2009
Posts
43,037
Reaction score
34,741
Ilikuwa ni kazi nzito kwa polisi waliokuwa wakisumbuliwa na wimbi la mauaji ya kimyakimya yaliyokuwa yakifanywa na mtu ambaye hawakumjua.

Polisi walijua kuwa mtu huyo hakuwa wa kawaida kutokana na aina ya vifo vilivyokuwa vikiwakumba watu katika Jiji la Dar es Salaam.
Maiti ya kwanza waliikuta imening'inizwa kwenye mti lakini inawezekana wauaji kwa harakaharaka walimtundika marehemu mtini wakiamini watu watadhani amejinyonga bila kujua kwamba uzito wa mtu huyo waliyemuua na mti ni tofauti.
Mara baada ya kumtundika marehemu huyo kwenye tawi la mti, lilipinda na maiti ikawa imegusa chini baada ya muda mfupi ikawa imepiga magoti ardhini.
Hali hiyo ilimfanya Inspekta Ado aliyekuwa akifuatilia kifo hicho, aamini kwamba mtu huyo hakujiua kwa kujinyonga bali aliuawa kusikojulikana na pale aliletwa akiwa ameshafariki dunia akatundikwa mtini.
"Wauaji hawa walidhani mti huu ni imara, hivyo asubuhi watu wangemkuta ananing'inia, kumbe tawi lenyewe siyo imara hivyo limepinda," alisema Inspekta Ado huku akiwaangalia askari kanzu wake aliokuwanao eneo la tukio jirani kabisa na kota za wafanyakazi wa machimbo ya madini wa Kampuni ya Lumesule.
Kulikuwa na kundi kubwa la watu waliokuwa wameizunguka maiti wakati askari wakifanya uchunguzi wao na hakuna hata mmoja aliyekuwa akionekana kumfahamu marehemu huyo.
Inspekta Ado aliwageukia raia waliokuwepo na kuwaangalia mmoja baada ya mwingine kabla ya kuwauliza.
"Ndugu zangu, kuna mtu yeyote hapa ambaye anamjua marehemu huyu?"
"Hakuna," alijibu mtu mmoja aliyekuwa amevaa kofia aina ya pama.
"Jibu lako unawakilisha watu wote au ni wewe ndiye humjui huyu marehemu?"
"Afande nimejibu hivyo kutokana na sababu ninazozijua."
"Sababu gani hizo?"
"Kwa vyovyote kungekuwa na watu ambao wanamjua au ndugu wa marehemu kwanza kama ni wanawake basi wangeangua kilio na usingekuwa na sababu ya kutuhoji na kama ni mwanaume, asingesita kujitokeza na kujitambulisha," alisema mtu huyo.
Inspekta Ado alijiuliza kimoyomoyo busara za mtu huyo kama zinagonga ubongo wake? Akajijibu kuwa alikuwa sahihi.
Akaachana naye na kugeukia umati.
"Ndugu zangu kuna yeyote ambaye atatusaidia yaani kama kuna mtu wa jirani na hapa ambaye aliliona gari likileta mwili huu usiku?"
Swali hilo liliwafanya watu kuangaliana bila kujibu lolote.
Inspekta Ado alichomoa simu yake ya upepo ambayo alikuwa ameining'iniza kwenye mkanda mkubwa kiunoni.
"Haloo, hebu hakikisheni mnatuma gari la wagonjwa hapa haraka liwe na daktari," aliamuru.
Wakati hayo yanafanyika mimi Che-Priska Ajigale nilikuwa naangalia kwa umakini mkubwa na nilikuwa nimesimama jirani kabisa na Inspekta Ado.
Nilikuwa natetemeka kwa mbali sana lakini nilijitahidi ili watu wasiweze kugundua mwili wangu unatetemeka.
Nilikuwa nimeshika tawi la mti huohuo ambao maiti ilikuwa imening'inizwa kumbe Inspekta Ado akagundua natetemeka baada ya kuona majani yakitikisika, aligeuka kabla na kuniangalia kwa macho makali.
"Wewe msichana kwa nini unatetemeka na unaitwa nani?" aliniuliza Inspekta Ado.
"Naitwa Che-Priska Ajigale
"Kwa nini unatetemeka?"

Haya tena kwa wale wanaopenda kuwa ni Matajiri wasome hii hadithi ya kusisimuwa kama utapenda niendelee weka ( Like)
 
UTAJIRI WA DAMU - 2-
ILIPOISHIA
Nilikuwa nimeshika tawi la mti huohuo ambao maiti ilikuwa imening'inizwa kumbe Inspekta Ado akagundua natetemeka baada ya kuona majani yakitikisika, aligeuka na kuniangalia kwa macho makali.
"Wewe msichana kwa nini unatetemeka na unaitwa nani?" aliniuliza Inspekta Ado.
"Naitwa Chepriska Ajigale…"
"Kwa nini unatetemeka?"
SONGA NAYO

Swali hilo lilinipa wakati mzito kwa sababu sikujua nimjibu nini.
"Nimekuuliza kwa nini unatetemeka?" aliniuliza tena nami akili ikafanya kazi harakaharaka na kumjibu:
" Sijawahi kuona mtu akiwa amekufa tena kwa kujinyonga ndiyo maana natetemeka."
"Aliyekuambia kuwa huyu kajinyonga ni nani?"
"Hakuna aliyeniambia, ni akili yangu tu, si nimeona ana kamba shingoni?"
"Mtu akiwa na kamba shingoni ina maana amejingonga?"
"Mimi ndivyo nilivyoona."
Baadaye Inspekta Ado aliniacha akawa anaendelea kuandika kwenye kitabu chake kidogo huku polisi mpigapicha akiifotoa maiti mara kwa mara.
Baada ya muda kidogo lilikuja gari la wagonjwa kwa mwendo wa kasi sana huku king'ora kikilia.
Lilisimama hatua chache kutoka tulipokuwa tumesimama na wa kwanza kushuka alikuwa daktari aliyekuwa amevaa glovus mikononi na kidude cha kusikilizia mapigo ya moyo kilikuwa kinaning'inia shingoni.
"Chepriska hujambo?" alinisalimia dereva wa gari lile la wagonjwa na kusababisha watu wote wageuke na kuniangalia mimi.Nilimjibu kuwa sijambo, aliiangalia maiti kisha akanigeukia.
"Pole sana."
Pole hiyo ilimfanya Inspekta Ado atugeukie na kutuuliza maswali mengi sana.
"Kwani marehemu ni nani kwako?"
"Ni mtu ninayemfahamu tu na tumekuwa tukikutana mara kwa mara katika baa mbalimbali, tukazoeana."
Inspekta Ado aliandika alichoniuliza kisha akamgeukia dereva wa ambyulensi.
"Umempa pole huyu dada, kwani huyu ni ndugu yake?"
"Sijui, lakini kama alivyosema mwenyewe nilikuwa nawakuta mara kwa mara kwenye baa wakinywa, sasa uhusiano wao siujui."
"Mara ya mwisho uliwaona wapi?"
"Mara ya mwisho niliwaona baa jirani na hapa."
"Wewe huyu marehemu unamjua kwa jina?"
"Simjui kwa jina isipokuwa kwenye ulevi tulikuwa tukimtania kwa kumuita bwana mafegi."
"Kwa nini?"
"Kwa sababu alikuwa akivuta sigara sana."
Inspekta alifikiri kwa dakika moja huku akiwa ameuma kalamu yake na alikuwa akiniangalia bila kupepesa macho kwa sekunde kadhaa.
Ilibidi niiname na kuangalia chini kukwepa macho inspekta ambaye alikuwa akionekana kuniwazia.
"Koplo Joyce, huyu binti yupo chini ya ulinzi. Mshikilie mpaka tutakapomhoji kwa kina."
Baada ya Inspekta Ado kutoa amri hiyo askari mwanamke alinikamata na kunifunga pingu kisha kinipakia kwenye Land rover 110 Discovery.
Nilijilaumu kwa nini nilikwenda kuiona maiti ya marehemu yule.
Daktari aliichunguza maiti kuanzia shingoni hadi mwilini huku akipepesa macho kuwaangalia watu waliokuwa wameizunguka.
"Uchunguzi wa awali unaonesha marehemu hakufa kwa kujinyonga maana shingo yake ni nzima, haijavunjika. Kwa kawaida mtu akijinyonga shingo yake ni lazima ivunjike kutokana na uzito mwa mwili," alisema daktari huku akimuangalia Inspakta Ado aliyekuwa akiandikaandika kile alichokuwa akizungumza mtaalamu huyo wa tiba.
Baadaye maiti ilibebwa na kuwekwa kwenye gari la wagonjwa.
"Dereva ipeleke maiti hiyo hospitali lakini ukiifikisha omba ruhusa uje Kituo cha Polisi Kijitonyama."
"Afande nije kwani mimi nahusika na kifo hiki?"
"Nani kakuambia kuwa unahusika? Acha kujichulia. Nimekuambia uje kituoni wewe unaongeza kujihisi kuwa unahusika na kifo hiki, aliyekuambia hivyo ni nani?"
Dereva wa ambyulensi aliwasha gari na kuondoka huku nyuma polisi nao waliamuru mjumbe na mwenyekiti wa serikali ya mtaa huo wajitokeze na wakafanya hivyo.
"Nyinyi ni viongozi, wote nitawachukua hadi kituoni ili nikapate maelezo yenu kwa sababu tukio la mauaji limetokea katika maeneo yenu, sawa?"
Nilifarijika kuona watuhumiwa na msiba huu tunazidi kuongezeka, sasa kwenye lile gari la polisi tulikuwa watatu.
Lakini cha ajabu ni kwamba miongoni mwetu ni mimi pekee nilikuwa nimefungwa pingu mikononi.
Gari la polisi liliwashwa na kutimua mbio huku nikiwa nimeng'ang'ania vyuma vilivyowekwa nyuma na askari wengine wenye silaha wakiwa wamesimama kutulinda, dereva wa gari hilo alikuwa na mbwembwe kwani wakati wa kuondoka aliwasha king'ora kana kwamba alikuwa akisafirisha mtu mahututi.

Je Chepriska anahusika na kifo cha mtu huyo? Nini kitatokea akifikishwa polisi? Fuatilia baadae...
 
UTAJIRI WA DAMU - 3-

"Nyinyi ni viongozi, wote nitawachukua hadi kituoni ili nikapate maelezo yenu kwa sababu tukio la mauaji limetokea katika maeneo yenu, sawa?"
Nilifarijika kuona watuhumiwa wa msiba ule tuliongezeka, sasa kwenye lile gari la polisi tulikuwa watatu.
Lakini cha ajabu ni kuwa kati ya watatu tuliokuwa humo ni mimi tu ambaye nilikuwa nimefungwa pingu mikononi.
Gari la polisi liliwashwa na kutimua mbio huku nikiwa nimeng'ang'ania vyuma vilivyowekwa nyuma na askari wengine wenye silaha wakiwa wamesimama kutulinda, dereva wake alikuwa na mbwembwe kwani wakati wa kuondoka aliwasha king'ora kana kwamba alikuwa akisafirisha mtu mahututi.
SONGA NAYO..

Tulifika kituoni na kushushwa kwenye gari. Kabla ya chochote tulivuliwa mikanda na mimi kilemba changu kilitolewa na tukakabidhi kila kitu kwa askari aliyekuwa ‘mapokezi' ya polisi kisha tukatupwa rumande.
Mimi nilitupwa rumande ya wanawake baada ya kufunguliwa pingu niliyokuwa nimefungwa mikononi. Wale wenzangu wawili ambao ni viongozi wa eneo lile, hawakupelekwa mahabusu badala yake waliambiwa waketi kwenye benchi lililokuwa pale mapokezi.
Sikujua wenzangu walikaa kwenye lile benchi kwa muda gani lakini mimi nilikaa kwa dakika ishirini kule mahabusu kisha nikasikia jina langu likiitwa.
"Chepriska."
"Afande. "Nilishitukia nikijibu hivyo kana kwamba mimi ni askari.
Nilitolewa rumande na kuingizwa katika ofisi moja ya upelelezi ambapo nilikutana na askari mmoja wa kike ambaye sikujua jina lake mara moja.
Nilipoingia kwenye ofisi hiyo niliwakuta wale akina baba ambao tuliletwa pamoja katika kituo hicho tukitokea eneo la tukio.
"Nyinyi wazee mnaweza kuondoka, tukiwahitaji tena tutawaita," alisema yule askari wa kike huku akifunika kile alichokiandika kutokana na maelezo ya watu wale.
Aliniangalia mimi huku akichambua makaratasi mapya ambayo yalikuwa hayajaandikwa chochote. Aliyabananisha na kuyaweka kwenye jalada lililokuwa na maelezo ya wale wazee wawili walioachiwa huru muda mfupi uliopita.
"Jina lako tafadhali," alisema.
"Chepriska Ajigale."
"Una miaka mingapi?"
"Thelathini na mbili,"
"Dini yako?"
"Mkristo."
"Kabila lako?"
"Myao."
"Hebu niambie, yule marehemu anaitwa nani na ulimfahamuje?"
"Yule marehemu mimi simfahamu kwa jina lakini tulikuwa tunakutana mara kwa mara kwenye baa usiku."
"Kiongozi wangu afande Ado amesema kwenye tukio kwanza ulikana kumfahamu lakini baadaye dereva wa gari la wagonjwa alipokukuta aneo la tukio alikupa pole, kwa nini alifanya hivyo kama huna uhusiano naye marehemu?"
"Kama nilivyokuambia, sina uhusiano naye. Nadhani yule dereva ama alidhani marehemu ni ndugu yangu au anajua labda nafanyanaye kazi, kunikamata mimi ni kunionea tu."
"Hapana siyo kukuonea, huu ni upelelezi kwani umetiwa hatiani?"
"Sasa kama ni upelelezi kwa nini mimi nilifungwa pingu? "Achana na hayo jibu maswali yangu na siyo wewe uniulize mimi."
Kilipita kimya cha dakika kama mbili huku tukitizamana na askari huyo, nadhani alikuwa akinisoma kuona kama nahusika na kifo kile au laa.
"Sasa inawezekana mkakutana kwenye baa na kunywa kila siku bila kuwa na uhusiano wowote hata kama siyo wa kindugu ukawa ni wa kibiashara?"
"Inawezekana sana na ndivyo ilivyokuwa kwangu na huyu kaka."
"Nani alikujulisha kuwa amefariki dunia asubuhi ya leo?"
"Hakuna aliyenijulisha. Nikiwa nyumbani kwangu nilisikia watu asubuhi wakisema kuna maiti inaning'inia kwenye muarobaini, ikabidi niende kushuhudia."
"Ulipoiona ukafanya nini?"
"Nikaona ni ya mtu ninayemfahamu. Nikashangaa kwa sababu jana usiku tulikuwa wote tukinywa pombe pale Chambilecho Baa."
"Mliachana saa ngapi na marehemu?"
"Wala sikukaa sana. Mimi baada ya kunywa bia mbili niliondoka."
"Marehemu ulimuacha akiwa na nani?"
"Nilimuacha akiwa na msichana mmoja na wanaume wawili."
"Unaweza kunitajia majina yao?"
"Siwajui kwa majina. Kama ilivyo kwa marehemu simjui kwa jina lakini tulizoeana kwa ajili ya kukutana Baa ya Chambilecho."
Wakati anaendelea kunihoji katika redio yake ya upepo tulisikia Inspekta Ado akiambiwa kuwa kuna mwanaume mwingine amekutwa ananing'inia kwenye mti akiwa amenyongwa.
"Khaa, mwingine tena?" alisikika akisema yule askari aliyekuwa akinihoji na akawa anasikiliza kwa makini majibizano kati ya askari wa doria na Inspekta Ado.

Je, nani huyo aliyeuawa? Msichana huyo anahusika na vifo hivyo? Fuatilia baadae kidogo.....
 
Mzizi endelea basi jamani ikiwezekana iishe kabisa.
hii stori ni ndefu mno,ukiwa na haraka utamfanya mwandishi aifupishe bure na kutunyima uhondo,endelea kuwa mstahamilivu utazidi kuipenda.
Nalog off
 
UTAJIRI WA DAMU - 4


LIPOISHIA
Wakati anaendelea kunihoji katika, redio yake ya upepo tulisikia Inspekta Ado akiambiwa kuwa kuna mwanaume mwingine amekutwa ananing'inia kwenye mti akiwa amenyongwa.
"Khaa, mwingine tena?" alisikika akisema yule askari aliyekuwa akinihoji na akawa anasikiliza kwa makini majibizano kati ya askari wa doria na Inspekta Ado.
Endelea...

Askari huyo wa kike alionekana kuchanganyikiwa na kuanza kuwapigia simu watu mbalimbali ambao nihisi walikuwa ni wapelelezi.
Baadaye aliniambia kuwa mahojiano yetu yametosha lakini akaniambia ni lazima nirudi rumande kwa kuwa yeye hakuwa na uamuzi wowote kuhusu kuniachia huru.
"Lakini kwa maelezo yangu afande unaona nina hatia?"
"Mimi siwezi kujua."
"Una uzoefu, tafadhali nieleze maana si ni nyinyi ndiyo mnatayarisha mashitaka?"
"Hapana, siku hizi anayetayarisha mashitaka ni ofisi ya mkurugenzi wa mashitaka."
"Ina maana kuna siku atakuja hapa kunihoji?"
"Hapana, tunachokifanya siku hizi ni kwamba sisi polisi tunampelekea jalada hili ofisini kwake kisha yeye akishalipitia anaona kama kuna kosa anaandaa shitaka au mashitaka."
Wakati anaendelea kunifahamisha, ghafla aliingia Inspekta Ado huku akiwa na simu yake mkononi. Alikuwa akizungumza na mtu fulani ambaye upande huo wa pili wa simu yake nilikuwa sisikii maneno aliyokuwa akiyasema.
"Umesema ameuawa na ananing'inia kwenye mti?"
Baadaye alimuamuru yule askari aliyekuwa akinihoji anirudishe rumande.
"Chepriska hakuna namna rudi ndani tukashughulikie hili tukio jipya," alisema askari yule huku akiniongoza kwenda kunifungia mahabusu.
Kilichoendelea huko walikokwenda sikukijua kwani mimi nilikuwa ndani huku giza likiwa limetanga na mbu wakilia kutaka kunyonya damu yangu japokuwa usiku ulikuwa haujaingia.
***
"Cheprisca, nakuachia, unajidhamini mwenyewe kwa kuwa nimesoma maelezo kwenye jalada, nimeona hakuna kitakachonifanya niendelee kukushikilia lakini tukikuhitaji, tutakuita, sawa?" Alisema Inspekta Ado
"Sawa."
Niliachiwa na nikaenda moja kwa moja kwa Bwana Mitimingi. Huyu alikuwa tajiri aliyekuwa akinituma mara kwa mara kazi zake, zingine ni za kijinga kabisa, kama vile kumletea mavi ya tembo au takataka za kwenye kona.
Niliamini kwamba alikuwa akinituma vitu vile ili avifanyie mambo ya kishirikina na nilihakikisha hilo baada ya kumuona siku moja akiweka kipande cha mavi ya tembo niliyompelekea kwenye siti ya dereva ya moja ya mabasi yake.
Lakini siku nyingine alinituma nimpelekee yai la bundi ambalo nililinunua kwenye maduka ya dawa za asili kwa bei mbaya. Sikujua yai lile alilifanyia nini.
Kuna siku alinituma nimletee nyasi zilizo kwenye makutano ya barabara, baada ya kuzileta nilimuona akiziweka chini ya kiboksi cha fedha za mauzo.
Niliwahi kusikia kwenye ‘redio mbao' kuwa mzee huyu ni kigagula ambaye ana mbinu nyingi za kishirikina za kupata fedha, hivyo nilikuwa makini sana kwa kila alichokuwa akinituma.
Nilisikia watu wakisema utajiri wa mzee Mitimingi ulitokana na mambo ya giza na wengine walikwenda mbali zaidi kwa kudai kuwa alikuwa akiua watu na kuwageuza misukule.
Maneno hayo yalinifanya nisiwe na raha kwa sababu nami watu waliokuwa wakiniona niko naye karibu walikuwa wakinihusisha na imani za kishirikina na iliwahi kutokea mtu mmoja kuniambia laivu kuwa mimi ni mchawi.
Mawazo hayo niliyaweka kando nikawa nafikiria la kusema pindi nikionana na mzee Mitimingi kwani nilitaka anilipe fedha zangu kwa kuwa aliwahi kunipa kazi za kumtafutia nywele za watoto wachanga.
Ilikuwa ni dili, ilibidi niongee na kinyozi aliyefanikisha kunipa bunda la nywele hizo na akawa ananidai fedha nikawa ninamzungusha kwani mzee Mitimingi aliyekuwa bahili hakunilipa ujira wangu.
Kitendo cha kutomlipa fedha zake yule kinyozi kilimkera ndipo akaniambia:
"Usiponilipa fedha zangu nitakutangaza kwamba wewe ni mchawi."
"Hapana ndugu yangu usifanye hivyo, mimi zile nywele nilitumwa tu."
"Alikutuna nani kama na wewe siyo mchawi, nilipe fedha zangu Chapriska."
"Ndugu yangu usiwe na wasiwasi kuna mzee atanipa fedha zako na nitakuletea, naomba niamini."
"Nakuamini nakupa siku mbili uwe umenilipa, usinifanye mimi sijui fedha," alifoka kinyozi huyo.
Niliondoka kwenda kwa mzee Mitimingi nikiwa na wasiwasi mkubwa kwamba kwanza, siku alizonipa kinyozi zilibaki mbili maana moja niliipoteza nikiwa mahabusu.
Nilikuwa naomba Mungu mzee huyo nimkute na anipe fedha ili nimlipe kinyozi aliyegeuka kuwa mkorofi kwangu.
Nilipokaribia jumba la mzee Mitimingi nilisikia mbwa akilia.
Nilijiuliza kwa nini yule mbwa alikuwa analia kilio kilichoonesha alikuwa anapigwa.
Sikukosea kwani nilipokaribia geti niliona mzee Mitimingi akimpiga mbwa wake.
Kilichonishangaza zaidi ni kuona mzee huyo akisema na mbwa yule akimuambia anampiga kutokana na kutotii alichomuagiza.
"Nitakupiga sana kwa sababu umeniudhi." Alipotoa kauli hiyo alikuwa akimpiga mbwa huyo kwa fimbo. Nilijitahidi kuchungulia nikamuona mbwa kafungwa kamba kichwa kikiwa kibandani na sehemu ya mapaja yake yakiwa nje.
Nilipigwa na butwaa kwani ilikuwa mara yangu ya kwanza kushuhudia jambo kama lile!

Je, kwa nini anaongea na mbwa? Fuatilia ujue siri hiyo..........Baadae...........
 
UTAJIRI WA DAMU - 5-

ILIPOISHIA
Nilijiuliza kwa nini mbwa huyo alikuwa analia kilio kilichoonesha kuwa alikuwa anapigwa. Sikukosea kwani nilipokaribia geti niliona Bwana Mitimingi akimpiga mbwa yule.

Kilichonishangaza zaidi ni kuona mzee huyo akimuambia yule mbwa anampiga kutokana na kutotii alichomuagiza.
"Nitakupiga sana kwa sababu umeniudhi." Alipokuwa akisema maneno hayo alikuwa akimpiga mbwa huyo kwa fimbo. Nilijitahidi kuchungulia nikamuona mbwa huyo kafungwa kamba kichwa kikiwa kibandani na kubaki nje sehemu ya mapaja.Nilipigwa na butwaa!


SASA SONGA NAYO...

Niligonga mlango wa geti huku nikimuangalia mzee Mitimingi kupitia tundu la kwenye lango hilo. Alishituka na akaacha kumpiga.
Nilimuona akija getini harakaharaka na fimbo aliyokuwa anatumia kumpiga mbwa wake akaitupa chini.
Alichukua kitambaa chake cheupe na kufuta uso. Nilisogea nyuma kidogo ya geti ili asijue kama nilikuwa nikimchungulia wakati anamfanyia ukatili mbwa yule ambaye hakuwa na uwezo wa kujitetea.
"Nani?" aliuliza baada ya kulikaribia geti.
"Ni mimi Chepriska Ajigale."
"Ahaa, karibu, ngoja nikachukue ufunguo ndani," alisema nami nikarudi kwenye tundu nikawa naendelea kumchungulia.
Badala ya kuingia ndani, alikwenda kwenye banda la mbwa na kumfungia ndani tena kwa kufuli. Baada ya kufanya kazi hiyo alikwenda kwenye mlango mkubwa wa nyumba yake akaingia ndani.
Baada ya dakika chache alitoka huku akiwa na funguo nyingi zilizokuwa zimefungwa kwenye rundo moja, alikuwa akizitikisatikisa.
Kama ada, nilisogea hatua moja kutoka kwenye geti ili asigundue mchezo wangu wa kumchungulia yaani kupiga chabo!
"Karibu ndani," alisema huku akifungua geti hilo kubwa.
Niliingia ndani na tukawa tunaongozana kuelekea kwenye kibaraza kilicho mbele ya nyumba yake. Hatukuingia ndani kwa sababu sikuwa na mzigo wowote ambao alikuwa amenituma.
Tuliketi kwa kuangaliana.
"Jana sikukuona na nilitegemea sana kuwa ungefika."
"Nilipatwa na tatizo."
"Tatizo gani?"
Nilimueleza kila kitu, akashangaa.
"Sasa kwa nini hukuniita nikuwekee dhamana?"
"Polisi walininyang'anya simu na wakaniambia hawataki niwasiliane na mtu yeyote mpaka upelelezi wao utakapoisha."
"Sasa wamemaliza huo upelelezi?"
"Sijui, lakini kuhusu mimi nahisi hawakuniona kuhusika ndiyo maana nikajidhamini mwenyewe. Mzee si unajua kuwa kesi za mauaji hazina dhamana, naamini maelezo yangu yaliwatosheleza kwamba sihusiki hata kidogo."
"Pole sana lakini pia una bahati kwa sababu kesi kama hizo kuchukuliwa na kutolewa kesho yake huwa ni nadra, labda siku hizi polisi wameendelea au uongozi wa IGP Mwema umesaidia kuwafanya wawe shapu."
Kilipita kimya cha dakika mbili hivi kwani mzee Mitimingi aliingia ndani bila kuniaga. Sikujua alikwenda kufanya nini nami sikumuuliza kwani mzee huyu huwa hakawii kutibuka ukimkorofisha.
Baada ya dakika mbili alikuja na glasi mbili za juisi.
"Tunywe juisi, karibu, " alisema huku akinipa glasi iliyojaa juisi, kwa kuwa nilikuwa nimechoka kutokana na kuswekwa ndani, sikutaka kumchelewesha nikaanza kumdai fedha zangu.
"Mzee nimekuja kuchukua fedha zangu zile za nywele za watoto maana kinyozi ananidai sana," nikasema huku nikiangalia chini.
"Wewe umesema umelala kituo cha polisi, huyo kinyozi amekuona saa ngapi?"
"Kabla sijakamatwa alikuwa akinisumbua sana kwa simu zake, akasema kama sitampatia leo atanitangaza kwa watu kuwa mimi ni mchawi kwani nimekusanya nywele za watoto wao."
Nilimuona mzee Mitimingi akitoa macho baada ya kumueleza hivyo na harakaharaka akadakia:
"Looh hatari sana. Kwa nini hukunipigia simu baada ya kukupa vitisho hivyo?"
"Nimeshakuambia kuwa nilikamatwa na polisi na meseji hiyo ilikuwa ya mwisho, baada ya hapo nikafunga simu."
"Polisi hawakukagua simu yako?"
"Waliikagua lakini kila meseji ya kinyozi ikiingia nilikuwa naisoma na kuifuta haraka."
"Nitakuongezea fedha ili ukampe naye za ziada. Kwa kuwa ulisema anakudai shilingi elfu ishirini, kampe thelathini nawe chukua laki moja, sawa?" Akanyanyuka kufuata fedha.
Ghafla yule mbwa aliyekuwa akipigwa akawa amesimama nyuma yangu, ajabu ni kwamba alikuwa na sura ya binadamu na muda wa sekunde yule mzee alirudi na baada ya kumuona mnyama huyo akawa anatetemeka. Mbwa naye akawa analia kama afanyavyo mtu! Nilishituka sana.

Je, kwa nini mbwa ana sura ya mtu? Fuatilia leo jioni.....
 
Back
Top Bottom