Usimamizi wa 'Mikopo ya Dharura kupitia simu' nchini Tanzania

Joined
Dec 18, 2023
Posts
59
Reaction score
10
Utangulizi
Kuwa kwa kasi kwa huduma za kifedha za kidijitali nchini Tanzania kumeleta mapinduzi makubwa katika upatikanaji wa mikopo na huduma za malipo kwa mamilioni ya wananchi. Miongoni mwa ubunifu huu ni kuibuka kwa huduma za mkopo wa dharura kupitia simu za mkononi, zinazojulikana kwa majina tofauti ya kibiashara ikiwemo Songesha. Huduma hizi huwezesha watumiaji kukamilisha miamala hata wanapokuwa na salio pungufu kwenye pochi zao za simu, hivyo kutoa mkopo wa muda mfupi papo kwa hapo kupitia majukwaa ya fedha kwa njia ya simu.

Ingawa huduma hizi zimeleta urahisi na kuboresha upatikanaji wa fedha kwa watumiaji, muundo wa bei, mifumo ya urejeshaji wa mikopo, na athari kwa walaji zimeibua mjadala na mashaka. Zaidi ya hayo, kumekuwa na maswali ya msingi kuhusu iwapo huduma hizi za mkopo kupitia simu zipo ndani ya wigo wa usimamizi wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), na iwapo zinazingatia sheria za fedha za kitaifa, hususan Sheria ya Mifumo ya Malipo ya Taifa ya mwaka 2015.

Makala hii inatoa uchambuzi wa kina wa kisheria na sera kuhusu huduma za mkopo wa dharura kupitia simu nchini Tanzania, kwa kutumia Songesha kama kielelezo, na kuchunguza iwapo huduma hizi zinasimamiwa ipasavyo chini ya sheria zilizopo kwa sasa.



Asili na Uendeshaji wa Huduma za Mikopo ya Dhuluma kwa Njia ya Simu
Huduma za mikopo ya dhuluma kwa njia ya simu (mobile overdraft facilities) hufanya kazi kwa kumpatia mteja kiasi fulani cha mkopo pale ambapo salio kwenye pochi yake ya simu hakitoshi kukamilisha muamala. Kiasi hicho cha mkopo hurejeshwa moja kwa moja kutoka kwenye malipo yoyote ya baadaye yanayoingia katika pochi ya mteja husika.

Kila muamala wa mkopo wa dharula huambatana na makato mawili ya kifedha. Kwanza, kuna ada ya usindikaji (processing fee) ambayo hukatwa mara moja pale mkopo unapotolewa. Pili, ada ya huduma ya kila siku (daily service fee) hutozwa kwa kila siku ambayo mkopo huo haujalipwa.

Ili kufafanua zaidi jinsi huduma hii inavyofanya kazi kwa vitendo, tuchukue mfano wa ujumbe uliopokelewa na mteja: “Umepewa mkopo wa dharula ya Tsh 653,870 ili kukamilisha muamala wako. Utatozwa ada ya usindikaji ya Tsh 22,885 na ada ya huduma ya kila siku ya Tsh 26,155.” Katika hali hii, mteja anapokea mkopo wa Tsh 653,870, anakatwa ada ya usindikaji ya Tsh 22,885, na atatozwa Tsh 26,155 kwa kila siku atakayoendelea kuwa hajarejesha mkopo huo. Endapo mteja atashindwa kulipa mkopo huo ndani ya siku 30, ada ya huduma itafikia jumla ya Tsh 784,650. Akijumlisha na mkopo wa awali na ada ya usindikaji, mteja atalazimika kulipa jumla ya Tsh 1,461,405.

Mpango huu wa mikopo kwa njia ya simu unazua maswali makubwa kuhusu uwezo wa wananchi kuimudu na usawa wake, hasa kwa watu wa kipato cha chini ambao mara nyingi hutegemea huduma hizi kufanikisha mahitaji yao ya kila siku.

Mfumo wa Kisheria Chini ya Sheria ya Mifumo ya Malipo ya Taifa ya Mwaka 2015
Sheria ya Mifumo ya Malipo ya Taifa ya mwaka 2015 ndiyo inayoweka msingi wa kisheria wa udhibiti wa mifumo ya malipo, watoa huduma za fedha kwa njia ya kielektroniki, zana za malipo, pamoja na huduma za kifedha zinazotolewa kupitia simu za mkononi nchini Tanzania. Kwa mujibu wa sheria hii, Benki Kuu ya Tanzania imepewa mamlaka mapana ya kudhibiti, kutoa leseni, kusimamia na kufuatilia kwa ukamilifu mifumo yote ya malipo ya kielektroniki na huduma zinazohusiana, ikiwemo mchakato wa usuluhishi wa malipo na matumizi ya zana za malipo, kama inavyoelezwa katika Kifungu cha 4 cha Sheria hiyo.

Aidha, Kifungu cha 15(1) kinakataza mtu yeyote kutoa zana ya malipo ya kielektroniki bila kupata leseni au kibali rasmi kutoka Benki Kuu ya Tanzania. Vilevile, Kifungu cha 24(1) kinazuia mtu au taasisi yoyote kutoa fedha za kielektroniki bila idhini kutoka Benki hiyo. Sheria hii pia inasisitiza juu ya ulinzi wa mlaji chini ya Kifungu cha 51, kwa kuwataka watoa huduma wa mifumo ya malipo kuweka masharti ya huduma yaliyo wazi, kuwa na muundo wa bei unaoendana na haki, na kuhakikisha kuwepo kwa mifumo madhubuti ya kutatua migogoro ya wateja.

Kwa kuzingatia masharti haya ya kisheria, huduma za mkopo wa dharura kupitia simu za mkononi kama vile Songesha, ambazo hutolewa kupitia mifumo ya fedha ya kielektroniki inayounganishwa na pochi za simu, bila shaka ziko chini ya usimamizi wa kisheria wa Benki Kuu ya Tanzania. Huduma hizi haziko nje ya udhibiti, wala si huduma zisizo rasmi au zisizo na utaratibu wa kisheria. Badala yake, zinahesabika kuwa ni huduma rasmi za malipo ya kielektroniki na matumizi ya zana za kifedha, ambazo lazima zizingatie masharti ya utoaji wa leseni, uwazi wa taarifa, na ulinzi wa watumiaji kama yalivyowekwa katika Sheria ya Mifumo ya Malipo ya Taifa ya mwaka 2015.

Masuala ya Kisheria na Kiuchumi
Ingawa huduma za mkopo wa dharura kupitia simu ya mkononi (mobile overdraft) zinakubalika kisheria endapo zitapatiwa leseni stahiki, mifumo ya bei inayotumika katika huduma hizi inazua maswali makubwa ya kisheria na maadili:

Ukosefu wa Uwazi Kuhusu Muda wa Marejesho
Huduma nyingi za mkopo wa dharura haziainishi wazi muda wa mwisho wa kurejesha mkopo. Ada ya kila siku inayotozwa hadi mkopo utakapolipwa, bila kuwepo ukomo wa muda wa kurejesha, husababisha mkopo kuwa mzigo wa kifedha wa muda usiojulikana kwa watumiaji.

Ada ya Kila Siku Kama Riba ya Siri
Ingawa ada ya kila siku haijaitwa rasmi kuwa ni “riba,” kiuhalisia hutumika kama riba. Mtumiaji anayeshindwa kulipa mkopo ndani ya siku 30 anaweza kujikuta analipa zaidi ya mara mbili ya kiasi alichokopa. Hili linafanana na mikopo ya kidijitali yenye gharama kubwa, jambo ambalo linaweza kutafsiriwa kama kandamizi au la unyonyaji, hasa kwa mujibu wa Kifungu cha 12 cha Sheria ya Mifumo ya Malipo ya Taifa (NPSA), kinachokataza vitendo vinavyoweza kuhatarisha uadilifu au ufanisi wa mfumo wa malipo.

Ukosefu wa Ulinzi wa Watumiaji wa Huduma
Katika hali nyingi, watumiaji hawapewi taarifa kamili kuhusu gharama ya jumla ya mkopo au matarajio ya marejesho. Hili linakiuka Kifungu cha 51(2) cha NPSA ambacho kinawataka watoa huduma kuwapatia watumiaji taarifa zilizo kamili, zinasomeka, na kueleweka kwa urahisi.

Ukosefu wa Kikomo cha Kisheria kwa Ada Zinazotozwa
Sheria ya NPSA haijaweka ukomo wa kisheria kwa ada za usindikaji au huduma zinazotozwa katika mikopo ya dharura kupitia simu. Hali hii huacha mianya ya kuendeleza mifumo ya bei yenye kasumba ya unyonyaji iwapo hakutakuwa na ufuatiliaji wa karibu.

Mlinganisho wa hoja
Tanzania inaweza kunufaika kwa kujifunza kutokana na uzoefu wa hivi karibuni wa Kenya katika suala la udhibiti wa huduma za mikopo ya simu. Kufuatia malalamiko kuhusu viwango vya juu vya ada za kila siku na masharti yasiyoeleweka ya huduma hizo, Benki Kuu ya Kenya ilianzisha mfululizo wa mageuzi muhimu ya kisheria. Mageuzi haya yalijumuisha kufutwa kwa ada za kila siku na badala yake kuwekwa kwa ada za kudumu, wajibu wa wakopeshaji kuweka wazi gharama zote za mkopo, pamoja na kuanzishwa kwa viwango vya ulinzi wa watumiaji vinavyolenga mahsusi huduma za mkopo wa kidijitali. Kwa pamoja, hatua hizi zimepunguza kwa kiasi kikubwa mzigo wa madeni kwa watumiaji na kuimarisha uadilifu na uaminifu wa huduma za mkopo wa simu nchini Kenya.

Mapendekezo ya Mageuzi ya Kisheria ya Udhibiti
Ili kuboresha usimamizi na kuwalinda watumiaji wa huduma nchini Tanzania, hatua zifuatazo zinapendekezwa:

Leseni za Lazima na Ukaguzi wa Uzingatiaji wa Sheria
Mashirika yote yanayotoa huduma za mkopo kupitia mfumo wa mkopo wa dharula kwa njia ya simu ya mkononi, ni lazima yapate leseni rasmi kama watoa huduma za fedha za kielektroniki au watoa huduma za mifumo ya malipo. Mashirika haya yakaguliwe mara kwa mara na Benki Kuu ya Tanzania (BoT) ili kuhakikisha yanazingatia viwango vya ulinzi wa watumiaji.

Uwazi katika Bei na Masharti
Kanuni zipaswa kuhitaji utoaji wa taarifa kamili kuhusu:​
  • Gharama zote za mkopo,​
  • Kipindi cha marejesho,​
  • Adhabu kwa kutotekeleza marejesho kwa wakati, na​
  • Njia rasmi za kushughulikia migogoro.​
Taarifa hizi zitolewe kwa muundo unaoeleweka kwa urahisi na mtumiaji wa kawaida wa simu ya mkononi.

Mapitio na Udhibiti wa Ada za Kila Siku
BoT inapaswa kuchambua uhalali wa utozaji wa ada za kila siku na kuzingatia uwezekano wa kuweka kikomo cha juu cha ada au muda wa neema (grace period) ambao ada haitoziwi. Hii inaendana na Kifungu cha 56 cha Sheria kinachompa Gavana wa BoT mamlaka ya kutunga kanuni kwa ajili ya kulinda maslahi ya umma.

Kuanzisha Mfumo Maalum wa Udhibiti kwa Mikopo ya Kidijitali
Kutokana na asili mseto ya huduma za mikopo ya dharula kwa njia ya simu ambazo ni sehemu ya kifaa cha kifedha na sehemu ya mfumo wa malipo kuna haja ya kuwepo kwa mfumo maalum wa kisheria unaojumuisha vipengele vya mifumo ya malipo na sheria za mikopo midogo (micro-lending).

Kwa kuhitimisha
Songesha na huduma nyingine za mkopo wa dharura kupitia simu za mkononi ni hatua mpya katika safari ya Tanzania kuelekea ushirikishwaji mpana wa kifedha. Huduma hizi zinatoa fursa muhimu ya upatikanaji wa fedha kwa mamilioni ya watu, lakini pia zinawaweka watumiaji katika hatari kubwa endapo hazitasimamiwa ipasavyo.

Benki Kuu ya Tanzania imepewa mamlaka ya kisheria pamoja na wajibu wa kusimamia huduma hizi kupitia Sheria ya Mifumo ya Malipo ya Taifa ya mwaka 2015. Kwa sasa, juhudi za kisheria hazipaswi tu kuishia kwenye kutambua uwepo wa huduma hizi, bali zielekezwe kuhakikisha kuwa zinatoa huduma kwa uwazi, haki, na kwa kuzingatia maslahi ya walaji.

Kadri mazingira ya huduma za kifedha kupitia simu yanavyoendelea kukua kwa kasi, ni muhimu kuweka mizani sahihi kati ya ubunifu wa kiteknolojia na uwajibikaji wa kisheria. Kufanya hivyo kutalinda watumiaji, kuimarisha imani ya umma, na kuifanya mifumo ya kifedha ya Tanzania kuwa imara na thabiti zaidi.​
 
Huo unyonyaji mdogo mdogo ndo unafanya watu wachini kubaki masikini.
 
Hili andiko inafaa mamlaka zilione na zilifanyie kazi ili kulinda walaji. Hapa kuna wizi wa waziwazi

Nilikopa songesha Tsh.50,000/= nikachelewesha kulipa kwa siku kadhaa, siku niliyotaka kulipa nikajikuta deni linasoma 175,000++. Nikajisemea kimoyomoyo, ya nini kuwatajirisha makampuni yaliyokwisha tajirika kwa kuwanyonya wanyonge??Hadi napoandika comment hii, huu ni kama mwaka wa pili na zaidi sijalipa hilo deni. Nadhani watakuwa wameshafikisha Milioni plus plus
 
Kuna mikopo inayotangazwa sana mtandaoni kuwa inatolewa fasta na Mohamed Dewji baada ya kuomba mkopo kupitia mtandaoni.

Unatakiwa kutanguliza karibu asilimia kumi ya thamani ya mkopo unaotaka kama dhamana.

Kwa waliowahi kushiriki aina hii ya mkopo naomba kufahamishwa je ni kweli mkopo wa aina hii hupo au ni Kanyabwoya.
 
Mo Dewj hana Mkopo wa namna hiyo. Hao ni wahuni kama walivyo kausha Damu.
 
Tatizo kubwa hapa ni Mfumo mgumu uliopo wa kupata Mkopo katika Taasisi Rasmi zenye Riba nafuu kama Benki.

Serikali imekuja na 200B za Samia na 10% za Halmashauri kwa sasa ni 15% though process ni ndefu na wasimamizi hawana weledi wa kutosha hasa watendaji wa mitaa ambao ni miongoni mwa team inayoenda kukagua makazi ya watu (kwa baadhi ya halmashauri hasa KINONDONI).

Kama usimamizi ungekuwa mzuri na kupunguza mchakato/muda wa kufuatilia hii Changamoto ya Mikopo chechefu ingepungua na Masharti kwenye Mabenki na hata Simu yasingekuwa ya kuumiza watu.

Kiufipi Gavoo ichukue hatua.
 
Ni wizi kiukweli huu. Waendesha mikopo riba zao ni kubwa na ongezeko la kila siku la kuchelewesha mkopo.
 
BOT wameshindwa kusimamia hii sekta na wameacha uholela wa kupitilza.

Wakati umefika sheria zitazamwe upya na kuwe na udhibiti kwenye hii biashara ya kukopesha .

Mikopo hii imekuwa chanzo cha kurudisha nyuma maendeleo ya watu na hata kusambaratisha ndoa za watu. Athari ni nyingi mno.
 
Cookies are required to use this site. You must accept them to continue using the site. Learn more…