Ushirikiano kati ya Benki za Exim za China na Afrika kutoa msukumo kwenye ushirikiano wa kibiashara kati ya China na nchi za Afrika

ldleo

JF-Expert Member
Jan 9, 2010
1,010
1,036
VCG111201494807.jpg


Benki ya Exim ya Afrika (African Export-Import Bank) na Benki ya Exim ya China (China Export-Import Bank) wamesaini makubaliano yanayoifanya Benki ya Exim ya China kutoa mkopo wa dola milioni 600 kwa Benki ya Exim ya Afrika, kwa ajili ya kufadhili mikopo na miamala ya fedha za biashara. Hatua ya benki hizi mbili inalenga kuipa sekta ya biashara msukumo zaidi, sawa na ule unaonekana kwenye sekta nyingine za ushirikiano kati ya China na Afrika.

Ushirikiano kwenye miradi mikubwa kati ya China na nchi za Afrika, ni jambo ambalo si geni kwa watu wanaofuatilia mambo ya ushirikiano kati ya China na Afrika. Karibu kila nchi ya Afrika ina alama nyingi ambazo ni ushahidi wa matokeo ya ushirikiano kwenye eneo hilo. Iwe ni kwenye bandari, reli, barabara, viwanja vya michezo, majengo makubwa nk. Lakini ushirikiano kwenye sekta ya biashara, hasa biashara ndogo ndogo kati ya pande mbili, bado una safari ndefu.

Kutokana na maendeleo makubwa ya sekta ya viwanda, na kutoka na ukubwa wa tabaka la kati nchini China, ni wazi kuwa bidhaa nyingi ndogondogo za mtaji kwa ajili ya kuendeleza shughuli za ujasiriamali zinaweza kupatikana nchini China, na hata soko kwa ajili ya bidhaa ndogo ndogo iwe ni pamoja na za sanaa za mikono, vyakula vya kusindika visivyo vibichi kama chai, ufuta, maharage, korosho nk vinapatikana nchini China.

Hata hivyo hali halisi ni kwamba licha ya kuwa mazingira ya pande mbili yana msingi mzuri wa fursa za ushirikiano, uhalisia ni tofauti kabisa. Si kila mwafrika ana uwezo wa kununua bidhaa za mtaji za bei nafuu kutoka China au kufikisha bidhaa zake kwenye soko la China. Na sio rahisi pia kwa mteja wa China kununua bidhaa ya Afrika kwa urahisi kama hazijafika kwenye soko la China. Makubaliano yaliyosainiwa na benki hizo mbili yanalenga kuondoa changamoto hiyo.

Makubaliano haya yamesainiwa muda mfupi baada ya mkutano mkuu wa tatu wa “Ukanda Mmoja, Njia moja”, na yanatajwa kuwa ni matokeo ya mkutano huo. Mkuu wa Benki ya Exim ya Afrika Profesa Benedict Oramah alisema baada ya kusainiwa kwa makubaliano hayo, kuwa yatasaidia kuchochea ufadhili wa biashara kati ya China na nchi za Afrika, na hivyo kuimarisha mtiririko wa bidhaa kutoka Afrika kuja China, mtaji na teknolojia kutoka China kwenda Afrika. Pia amesema Benki ya Afrika Exim kupitia mpango mkakati wake wa sita, ulioanza mwaka 2022 na utatekelezwa hadi 2026, inafanya kazi kupanua nafasi yake katika ufadhili wa biashara ndani ya Afrika na inaendelea kuona fursa nyingi za ushirikiano miongoni mwa nchi za Afrika.

Pamoja na kuwa kimsingi makubaliano haya yanalenga kuimarisha biashara kati ya China na nchi za Afrika, hali halisi ni kuwa pia yatahimiza biashara miongoni mwa nchi za Afrika kwenye muktadha wa Eneo la biashara huria la Afrika (AfCFTA). Ikiwa ni miaka 10 sasa tangu pendekezo la “Ukanda Mmoja, Njia Moja” lihimize ujenzi wa miundo mbinu barani Afrika, usafirishaji wa bidhaa kutoka mji mmoja hadi mwingine, na hata kutoka nchi moja hadi nchi nyingine unazidi kuboreka.

Mkuu wa benki ya Exim ya China Bw, Shengjun Ren, pia ameyataja makubaliano hayo kuwa yatahimiza utekelezaji wa programu tisa zilizo chini ya Mfumo wa Baraza la Ushirikiano kati ya China na Afrika (FOCAC) katika utoaji wa mikopo ya biashara, uwekezaji wa hisa, uendeshaji wa soko la mitaji, fedha za biashara, kubadilishana wafanyakazi na kubadilishana maarifa, ili kutoa mchango kwenye ushirikiano wa kiuchumi na biashara ndani ya Afrika, pamoja na maendeleo endelevu ya kiuchumi na kijamii ya nchi za Afrika.
 
Back
Top Bottom