University of Dodoma (UDOM)
Public Institution
- Feb 24, 2024
- 48
- 52
Timu ya wafanyakazi wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) imeanza kwa mafanikio makubwa ushiriki wake katika mashindano ya michezo ya watumishi wa umma nchini Tanzania (Mei Mosi 2026), kwa kuibuka na ushindi wa kishindo katika mchezo wa kwanza.
Katika pambano la mpira wa wavu kwa wanaume lililochezwa leo, timu ya UDOM iliibuka na ushindi wa seti 2–0 dhidi ya timu ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT), matokeo yaliyoonyesha uimara na maandalizi thabiti ya kikosi hicho.
Akizungumza mara baada ya ushindi huo, Mkufunzi Mwandamizi wa Michezo wa UDOM, Bw. Patrick Mwani. alisema mafanikio hayo yametokana na maandalizi ya kina pamoja na nidhamu ya hali ya juu ya wachezaji.
“Tumefanya maandalizi ya kutosha na wachezaji wameonyesha nidhamu kubwa uwanjani. Huu ni mwanzo mzuri, na tumejipanga kuendeleza kiwango hiki katika michezo inayofuata,” alisema Bw. Mwani.
Mashindano hayo ya kitaifa yanayofanyika mkoani Njombe yanaleta pamoja watumishi wa umma kutoka taasisi mbalimbali nchini, yakilenga kuimarisha afya, mshikamano na ushirikiano kazini kupitia michezo.
Mbali na mpira wa wavu kwa wanaume na wanawake, timu ya UDOM pia inashiriki katika michezo mingine ikiwemo bao, riadha, karata na draft, ikiwa na matumaini ya kufanya vizuri katika mashindano yote.
Ushindi huu wa awali unaweka msingi imara kwa UDOM katika harakati zake za kuwania nafasi za juu kwenye mashindano hayo ya Mei Mosi 2026.