Urais 2010 waitikisa Zanzibar
na Mwandishi Wetu, Zanzibar
Tanzania Daima~Sauti ya watu
KILE kilichotokea wakati wa mchakato wa kumtafuta mgombea urais wa Zanzibar kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) mwaka 2000, kinaelekea kujirudia tena baada ya kuwepo kwa baadhi ya matukio yanayoshabihiana na yaliyotokea wakati huo.
Wakati mwaka 2000, aliyekuwa rais za Zanzibar, Dk. Salmin Amour alijaribu bila mafanikio kungangania madarakani, tukio kama hilo limeanza dalili za kujirudia tena baada ya kundi la wazee wa CCM kumtaka Rais wa sasa Zanzibar, Amani Abeid Karume, kubadili katiba ili agombee tena urais kwa kipindi cha tatu.
Hali hiyo ilidhihirika kuwepo baada ya kundi la wazee katika kampeni za kujenga wagombea kueleza msimamo wa kutetea ushauri wa kutaka katiba ifanyiwe marekebisho, ili imuwezeshe Rais Karume kugombea tena nafasi hiyo mwaka 2010 baada ya kumaliza muhula wa pili wa urais wake.
Hata hivyo, katika kile kinachoonekana kuwa umakini wa kusoma alama za nyakati, Rais Karume tayari amekwishatoa tamko kuhusu nia hiyo ya wazee kuwa hana mpango wa kuwania tena urais baada ya kumaliza kipindi chake cha miaka kumi.
Rais Karume alikaririwa wakati akizungumza katika mkutano wa hadhara kwenye Uwanja wa Demokrasia, Kibanda Maiti kuwa, kuna wazee walimfuata na kumshauri kuangalia uwezekano wa kubadili katiba, ili agombee tena nafasi hiyo, lakini aliwajibu kuwa hilo haliwezekani, kwa kuwa ndani ya CCM wapo watu wengi wenye uwezo wa kushika nafasi hiyo.
Wakati hali ikiwa hivyo kwa baadhi ya mashabiki wa Rais Karume, idadi ya wana CCM wanaotajwa kujiandaa kumrithi atakapomaliza kipindi chake mwaka 2010 sasa wamefikia 10, wakiwemo wanasiasa wakongwe na vijana, ambao wamekuwa wakipanda ngazi za uongozi haraka haraka.
Uchunguzi wa Tanzania Daima Jumapili, umebaini kuwepo kwa makundi yanayoendesha kampeni za kujenga wanasiasa wanaotaka wawe viongozi wa visiwa hivyo mwaka 2010, ambao baadhi yao wamehamia Tanzania Bara baada ya ngome ya Zanzibar kugawanyika kwa kiwango kikubwa.
Uchunguzi umebaini kuwa kundi linaloonekana kuwa na nguvu hasi sasa na ambalo limekwishaonyesha nia ya wazi na ya dhati ya kutaka kuingia ikulu ya nchi hiyo baada ya kuondoka kwa Rais Karume ni lile linalomuunga mkono Waziri Kiongozi mstaafu, Dk. Mohamed Gharib Bilal.
Kundi hili ndilo linalotajwa kuwa lina baraka za Rais mstaafu wa Zanzibar, Dk. Salmin Amour Juma, mwenye maskani yake eneo la Migombani, mjini hapa.
Hata hivyo, kundi hili limeanza kupata upinzani kutoka kwa wanasiasa wengine wanaowania nafasi hiyo baada ya kuwepo kwa dalili za wazi za Dk. Bilal kutengwa au kubaguliwa na baadhi ya wanasiasa waliopo sasa madarakani, kiasi kwamba baadhi ya makada wa CCM wamekuwa wakiogopa kusalimiana naye au kukaa naye karibu.
Uchunguzi zaidi wa gazeti hili umebaini kuwa Dk. Bilal amekuwa akijikuta katika wakati mgumu, hasa anapohudhuria mikusanyiko mbalimbali ya sherehe za kitaifa, ambapo amekuwa akishindwa kusalimiana vizuri na watu wanaotajwa kutaka kuwania urais, kwa kuhofia kuonekana kwamba wanamuunga mkono au wanaunga mkono kundi fulani.
Hali hiyo ilidhihirika wazi wakati wa Baraza la Idd el Fitr lililofanyika Jumatano, baada ya baadhi ya viongozi (majina yao tunayo) kulazimika kumkwepa Dk. Bilal kwa kuhofia kuonekana kuwa wanamuunga mkono kiongozi huyo anayeonekana kuwa na nguvu na ushawishi mkubwa miongoni mwa wana CCM.
Zanzibar tuna siasa za unafiki mkubwa, leo hii watu wanapita nyuma ya mgongo wa Dk. Bilal kwa kuhofia kuhusishwa na makundi ya watu wanaotaka kuwania urais, alisema mwanasiasa mmoja wa siku nyingi aliyeomba asitajwe gazetini.
Hata hivyo, alisema ni jambo la kushangaza kuwa wale wanaomkwepa hadharani Dk. Bilal ndio hao hao wanaohudhuria vikao vya kampeni vya baadhi ya wagombea vinavyofanyika nyakati za usiku katika maeneo mbalimbali ya Zanzibar.
Mbali na Dk. Bilal, kundi jingine linaloonekana kuanza mikakati ya kuhakikisha linaweka mtu wake katika nafasi hiyo mwaka 2010, ni lile linalotajwa kuwa la makada wa CCM wanaomuunga mkono mwanasiasa machachari wa visiwani hapa, Ali Juma Shamuhuna, ambaye ni Naibu Waziri Kiongozi na Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo wa Zanzibar.
Shamuhuna anaokena kuwa na nguvu zaidi kwa sasa baada ya kuonyesha msimamo wake ambao umekuwa ukitofautiana na viongozi wenzake wengi ndani ya chama chake, kuhusu masuala yanayoihusu Zanzibar.
Mbali na vigogo hao, makundi mengine yanayotajwa kuhaha kujipanga kwa ajili ya mwaka 2010 ni lile linalomuunga mkono Waziri Kiongozi wa sasa, Shamsi Vuai Nahodha.
Wanasiasa wengine wanaotajwa kuwa na makundi yaliyo katika jitihada za kuwania nafasi hiyo ni Waziri wa Ulinzi, Dk. Hussein Mwinyi (aliyechaguliwa Mbunge wa Kwahani baada ya kuliacha la Mkuranga, (Tanzania Bara), na Kamishna wa Umoja wa Afrika (AU) mjini New York, Amina Salum Ali.
Wengine ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais wa Zanzibar, Dk. Mwinyihaji Makame, Naibu Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mohammed Aboud Mohammed, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Zanzibar, Haroun Ali Suleiman, Jaji Mkuu wa Zanzibar, Hamid Mahmoud na Balozi wa Tanzania nchini Italia, Ali Abeid Amani Karume, ambaye ndiye pekee aliyetangaza wazi nia ya kugombea nafasi hiyo katika uchaguzi mkuu ujao.
Baadhi ya makada wa CCM waliozungumza na gazeti hili, walieleza kuwa nafasi ya urais wa Zanzibar isipochukuliwa kwa umakini inaweza kuigawa tena CCM kama ilivyokuwa mwaka 2000 baada ya Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) kumteua Karume kugombea nafasi hiyo badala ya Dk. Bilal, aliyepewa alama nyingi dhidi ya Karume aliyepata alama chache katika mikutano ya uteuzi.
Makada hao walieleza kuwa vitendo vilivyotokea vya kuzungumzia matabaka na asili za watu watokao Pemba, Ngazija, Tumbatu, Makunduchi na kwingineko, ni mambo yaliyokumbatiwa na watu kama silaha ya kisiasa katika harakati za kutafuta kuwa wagombea wa chama hicho mwaka 2010.
Walidai pia kuwa, hata hatua ya kusambazaji vikaratasi vinavyomkashifu Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais wa Jamhuri (Muungano), Muhammed Seif Khatib, kuwa ni mwanzo wa kuipeleka CCM kubaya na ni kwenda kinyume cha misingi ya waasisi wa chama hicho.
Akizungumzia kuhusu kampeni za kuwania nafasi hiyo kuanza kujitokeza mapema, Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Saleh Ramadhani Ferouz, alisema chama hicho kinaongozwa na kanuni, hivyo mwanachama yeyote anayezikiuka atachukuliwa hatua wakati utakapofika.
Alisema chama kinafuatilia matukio yanayohusisha wanachama wake na wakati wa uchukuaji fomu wote watakaobainika kufanya kampeni kinyume na maadili, watajadiliwa na kushughulikiwa kulingana na taratibu zilivyo.
Wakati huo huo, taarifa nyingine kutoka Zanzibar zinaeleza kuwa askari wastaafu wa vikozi vya SMZ wanaodai kupunjwa mafao yao wametishia kufichua siri jinsi walivyotumika katika uchaguzi mkuu wa 2000 na 2005 Zanzibar.
Wakizungumza jana na gazeti hili, walisema wanatoa wiki mbili mapendekezo ya mafao yao mapya kuwa yamezingatiwa na Wizara ya Fedha na Uchumi ya Zanzibar.
Hapa kinachoonekana hawathamini mchango wetu, tumetumika sana kwenye uchaguzi na tunajua mambo mengi, hiki ni choyo cha watendaji wa Wizara ya Fedha, alisema ofisa mmoja mstaafu ambaye alifikia cheo cha juu katika Kikosi cha KMKM.
Wastaafu hao walisema kwamba inashangaza kuona watendaji wa Wizara ya Fedha wamekuwa na kinyongo na mafao yao wakati baadhi yao wameajiriwa hivi karibuni wakiwa wanamiliki mali nyingi, yakiwamo majumba na magari.
Mapema wiki iliyopita, Katibu Mkuu Wizara ya Nchi Afisi ya Rais Tawala za Mikoa na Vikosi vya SMZ, Hassan Haji Wambi, alisema mapendekezo ya mafao ya askari hao wastaafu yamekwama baada ya kutokea mgongano wa kisheria kati ya sheria ya Tume ya Uajiri namba 7 ya mwaka 2007 na sheria ya fedha ya mwaka 2005.