Posted Date::3/24/2008
Ubomoaji makazi ya watu Dar,Waziri Wassira asema hawezi kujiuzulu
Na Muhibu Said
Mwananchi
WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Stephen Wassira, amesema hawezi kujiuzulu wadhifa huo kutokana na kuvunjwa kiholela kwa nyumba 99 za wakazi wa Tabata Dampo, jijini Dar es Salaam, kwa vile hana sababu ya kufanya hivyo.
Kauli hiyo imetolewa na Wassira siku moja baada ya Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Chacha Wangwe, kumtaka ajiuzulu wadhifa huo kutokana na kuvunjwa kwa nyumba hizo kulikosababisha wakazi hao waendelee kuishi katika mahema kwa takriban mwezi sasa.
Wassira alisema anawashangaa Chadema kumshinikiza ajiuzulu wakati tayari kuna tume iliyoundwa kuchunguza na pia baadhi ya viongozi wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilala walishachukuliwa hatua za awali kutokana na kadhia hiyo.
Viongozi hao wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilala, ni pamoja na Mkurugenzi, John Lubuva na Mhandisi, Iddi Kisisa, ambao wote walisimamishwa kazi kwa nyakati tofauti hivi karibuni.
Wassira alisema yeye kama waziri anayeshughulikia Serikali za Mitaa, ametimiza wajibu wake kama msimamizi wa serikali hizo kwa kuunda tume kuchunguza sakata hilo na anasubiri ripoti ya tume hiyo.
Alisema Serikali za Mitaa zina mfumo wake wa uongozi na uwajibikaji na kwamba kuna Halmashauri za Wilaya 133 na Manispaa 10 hivyo kama waziri atawajibika kwa kila kosa linalofanywa na halmashauri au manispaa, basi kutakuwa na rundo la mawaziri watakaojiuzulu kwa mtindo huo.
"Waambie Chadema, ahsante sana nimewasikia. Lakini walie tu, hakuna mtu kujiuzulu. Kwanini nijiuzulu? Hakuna sababu ya mimi kujiuzulu. Kwani mimi nimebomoa nyumba ya nani?," alihoji Wassira alipozungumza na Mwananchi kwa njia ya simu kutoka wilayani Bunda, mkoani Mara, jana.
Aliibeza hoja ya Wangwe ya kumtaka ajiuzulu wadhifa huo kwa kumuiga Mbunge wa Monduli (CCM), Edward Lowassa aliyejiuzulu Uwaziri Mkuu kutokana na watendaji wake wa ngazi ya chini kuhusika katika kashfa ya Kampuni ya Kuzalisha Umeme wa Dharura ya Richmond.
Wassira alisema hawezi kuiga kujiuzulu kwa Lowassa na kuhoji kosa lililofanywa na Mbunge huyo wa Monduli.
"Lowassa alifanya nini?," alihoji Wassira alipokumbushwa na mwandishi kuhusu hoja ya Wangwe ya kumtaka ajiuzulu kama Lowassa alivyojiuzulu Uwaziri Mkuu, Februari 7, mwaka huu kutokana na makosa yaliyofanywa na watendaji wake wa ngazi ya chini.
Wassira alisema anashangaa watu wanaombana yeye ajiuzulu wadhifa huo, huku wakiacha kutoa shinikizo hilo kwa viongozi wa mkoa na wilaya wa Dar es Salaam.
"Kwani mkuu wa mkoa hayupo, mkuu wa wilaya hayupo? Why me? (Kwanini mimi?)," alihoji Wassira na kuongeza: "Mimi naendelea vizuri, niko Bunda".
Baada ya mazungumzo hayo, mwandishi aliagana na Wassira, lakini dakika chache baadaye, Wassira alimpigia mwandishi simu na kusema: "Mwambie Wangwe naye ajiuzulu kwa kuhama jimbo lake, haonekani muda mrefu, amewatapeli wananchi, kwani hawamwoni jimboni".
Wangwe ambaye ni Mbunge wa Jimbo la Tarime, mkoani Mara, alipoulizwa na mwandishi jana kuhusiana na madai hayo ya Wassira, alikanusha kuhama jimbo lake.
Alisema kinachomfanya awepo Dar es Salaam muda mrefu, ni majukumu yake ya chama ambayo alisema anatakiwa ayatekeleze kama Makamu Mwenyekiti wa Chadema.
Wangwe alisema sababu nyingine, inatokana na vyombo vya dola kumpiga marufuku kufanya mikutano jimboni mwake tangu Januari 10, mwaka huu ambapo kila alipojaribu kufanya mikutano ilisambaratishwa na askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) kwa mabomu ya machozi.
"Kila nikitaka kufanya mkutano jimboni mwangu, polisi wananiandikia barua kunizuia nisifanye wakisema kwamba, mpaka matatizo ya Kenya yaishe. Hata ukitaka nakala ya hizo barua naweza nikakuonyesha, kwani zote ninazo," alisema Wangwe.
Alisema wakati yeye akizuiwa kufanya mikutano jimboni mwake, Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimekuwa kikiruhusiwa kufanya mikutano kama kawaida na kwamba, kuna wajumbe zaidi ya 88 wa Halmashauri Kuu ya CCM (NEC) wamekwenda jimboni humo kuendesha kampeni kuanzia leo hadi Machi 29, mwaka huu, kwa nia ya kumdhoofisha kisiasa ili wachukue jimbo hilo katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010.
Wangwe alidai CCM wameamua kumhujumu kisiasa jimboni mwake kutokana na kukerwa na utekelezaji wa azimio la madiwani wa Chadema wilayani Tarime la kutumia Sh250 milioni za kodi inayokusanywa kutoka Kampuni ya uchimbaji madini ya Barrick, kusomesha bure watoto katika shule za sekondari wilayani humo.
Alidai jambo lingine, linalowaudhi CCM na serikali yake, ni kuchaguliwa kwake kushika wadhifa wa juu katika Chadema ambapo alidai baada ya kuchaguliwa, wananchi wa Tarime waliandaa mapokezi makubwa, lakini hayakufanikiwa kutokana na kusambaratishwa na FFU.
"Kwa hiyo, hii ni vita ya kisiasa wanayofanya. Hata hivyo, nasubiri CCM wamalize, niende jimboni," alisema Wangwe.
Alisisitiza kumtaka Wassira ajiuzulu wadhifa huo akisema kwamba: "Kama kuna collective responsibility (Uwajibikaji wa Pamoja), basi tunamtaka Wassira ajiuzulu kama alivyofanya Lowassa aliyejiuzulu kutokana na makosa yaliyofanywa na watendaji wa chini yake".
Pamoja na msisitizo huo, Wangwe alisema kuanzia leo wataungana na wananchi wa Tabata Dampo kwenda kuishi nao katika eneo hilo kwa hali yoyote itakayokuwa hadi hapo watakapopata haki zao.
"Kama ni kulala katika mikeka au majamvi, basi tutalala kuanzia kesho (leo), ili tupate tabu wanayoipata wananchi wale, hadi hapo watakapopata haki zao," alisema Wangwe.
Jana gazeti hili lilimkariri Wangwe akimtaka Wassira kujiuzulu wadhifa huo kutokana na kadhia hiyo, pia alilitaka Baraza la Madiwani la Manispaa hiyo, kujiuzulu kwa kuwa ndilo linalotoa maamuzi ya kisiasa katika mambo mbalimbali, ikiwamo uvunjwaji wa nyumba hizo.
Wangwe alisema kuwasimamisha kazi Mkurugenzi na Mhandisi wa Manispaa, ni kuwaonea.
Vilevile, alisema Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) linapaswa kujiuzulu kwa madai ya kuwaruhusu wakazi hao kugeuza eneo la Dampo kuwa sehemu ya makazi ya watu kwa vile kwa mujibu wa sheria, eneo kama hilo haliruhusiwi mtu kuishi hadi baada ya miaka 30 baada ya kukaguliwa na NEMC.
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Abbas Kandoro alikaririwa hivi karibuni akisema kuwa, uvunjwaji wa nyumba hizo ulikiuka haki za binadamu, utawala bora, taratibu na sheria za nchi.
Kutokana na hali hiyo, alishauri kufukuzwa kazi kwa viongozi wote wa manispaa hiyo watakaobainika kuhusika ama kuamuru au kubariki uvunjwaji wa nyumba hizo.
Alisema kadhia hiyo ilitokana na ama uzembe au kutowajibika kwao katika maamuzi yao, hivyo kusababisha uvunjaji wa haki za wakazi wa eneo hilo ambao nyumba zao zilivunjwa Februari 29, mwaka huu.
Alibainisha kuwa kitendo cha uongozi wa manispaa hiyo, kuwavunjia nyumba wakazi hao, siyo cha kiungwana kwa kuwa kimekiuka misingi ya haki za binadamu, utawala bora, taratibu na sheria.