Wakuu kauli ya mwisho maana yake nini? Haipingwi au....? Au ni lazima itekelezwe ikishatolewa? Na kama haipingwi haipingwi na nani? Waliochini yake kiserekali au wananchi wote? Tusije tukawa tuna ongelea vitu tofauti. Tukumbuke kuna mahakama na bunge hata kama mkulu amesema yeye ndiye mtafutaji na mgawa mafungu.
Mkuu Masiya, kwa kawaida nchi zote duniani zinatawaliwa na mihimili mitatu ya
1.Serikali, (The Executive), kazi yake ni kutawala nchi, kutekeleza maamuzi ya Bunge na Mahakama.
2.Bunge (The Legislature),Kazi yake ni kutunga sheria zitakazotafsiriwa na Mahakama na kutekelezwa na Serikali. Bunge pia linaisimamia Serikali.
3.Mahakama(The Judiciary),kazi yake ni kutafsiri sheria zilizotungwa na Bunge na kutekelezwa na Serikali.
Kinadharia, mihimili hii mitatu inatakiwa kufanya kazi kwa uhuru bila kuingiliwa (Independence) na wakati huo huo kila mhimili ni mwangalizi wa mhimili mwingine usivuke mipaka ya mamlaka yake (checks &balance). Hii inaitwa "The Principles of Separation of Powers, Checks and Balance".
Wakuu wa mihimili hii, Rais, Spika na Jaji Mkuu, wanatakiwa kuwa huru na kutokuingiliwa. Na hata ikitokea rais wa nchi hayupo tena kwa sababu yoyote ile(Kifo, Kujiuzulu, Kufukuzwa, Ugonjwa, Incapacitation, insane, etc), yoyote kati ya wawili hao atashika urais hadi uchaguzi mwingine.
Lakini rais wa Tanzania ni Executive President, ambaye huteua Mkuu wa Mhimili wa Mahakama, ambaye ni Jaji Mkuu. Rais wa Tanzania ni sehemu ya Bunge, huteua mtendaji Mkuu wa Bunge ambaye ni Katibu wa Bunge, huliunda Bunge, hulivunja Bunge na huweza kulivunja Bunge wakati wowote akiamua.
Rais wa Tanzania ni sehemu ya Bunge kwa sheria zinazotungwa na Bunge, haziwi sheria mpaka rais atakapo ridhia (acent).
Rais wa Tanzania ni sehemu ya Mahakama, sio tuu kwa kuteua watendaji wakuu wa mahakama, majaji, bali rais kupitia mamlaka ya DPP, anaweza kuingilia kesi yoyote, ikiwa katika hatua yoyote na kuamua kuifuta (Nolle Proseque), hukumu ya kifo haitekelezwi bila rais kuridhia na ana mamlaka ya kusemehe wafungwa waliohumiwa vifungo.
Hivyo rais wa Tanzania ndio kila kitu, anatunga sheria, anatafsiri sheria na kutekeleza sheria hivyo kauli ya rais ni sheria. Ila sio kila anachosema rais ni sheria, bali kile rais anachosema na kisha kikaandikwa rasmi kuwa ni sheria na kutangazwa kwa waraka wa kiserekali, GN na kutangazwa kwenye gazeti la Serikali.
Rais akitangaza jambo fulani, kusipotolewa taarifa rasmi ya jambo hilo kupitia decree, jambo hilo linakuwa sio sheria.
Katazo la rais kuzitaka taasisi za umma kuweka fedha za makusanyo BOT, sio sheria na fedha zinazohifadhiwa BOT ni fedha za mapato tuu. Fedha za matumizi bado zinawekwa kwenye mabenki binafsi.
Paskali.