Wakuu,
Naona tunatumia muda mwingi kusign hizi petition ambazo hazina athari zinazotakiwa. Nilipokuwa masomoni Marekani, nilifundishwa mbinu moja nzuri ya uanaharakati, lakini nawamegeeni hizi mbili, muweze kuzitumia kufanikisha lengo kuu.
Hit your enemy where it hurts the most: his pockets!
Tafsiri yake ni kwamba "Mpige adui yako mahali ambapo ataumia zaidi: kwenye mifuko yake." Tafsiri fupi ni kwamba, kama ana mapato, tafuta njia ya kumnyima mapato, kumtia hasara kubwa, ikiwezekana, mfilisi kabisa. Kwa hili tufanyeje? Badala ya kulalamika kwenye vyombo vya habari na kusign petition, tunachopaswa kufanya ni kuendesha mgomo baridi wa hata saa 24, kwa kuzima simu zetu za mkononi. Matumizi ya simu hizi, kisheria, na kibiashara, ni kwamba, mteja anaponunua line ya simu (SIM card) na kupewa namba ya simu ya mtandao wowote ule, anakuwa na hiari ya kutumia au kutotumia simu yake hiyo, na wala hapangiwi kiasi cha fedha anachopaswa kutumia. Kutumia aku kutotumia ni hiari yake; halazimishwi.
Hebu fikirieni, iwapo wakazi wa Jiji la Dar es Salaam, tena wale ambao wana kipato cha chini ambao ndio wenye matumizi makubwa zaidi, kwani mapato ya hizi kampuni za simu hupatikana zaidi kwenye SMS, na watumiaji hawa ni wengi zaidi kuliko matajiri, waamue kusitisha kutumia simu zao kwa saa 24 hadi 48, hasara watakayoipata wamiliki wa kampuni za simu itakuwa kubwa namna gani? Kampuni hizi zimeingia ubia haramu na Serikali yetu wa kuwanyonya Watanzania ambao wengi wao tayari ni maskini, ambao wengi wao kipato chao hakitoshi hata mlo mmoja wa siku. Ni ajabu walidunduliza MIAKA NGAPI hadi kupata uwezo wa kununua hizo simu zao za mkononi, kisha kununua line, na leo Serikali inakuja na kodi ya kinyemela kuwatoza Shs. 1,000 kwa mwezi? Dharau iliyoje? Basi na sisi (najua nitaitwa mchochezi lakini hizi ni harakati) tuwagomee huduma yao hii, kwa hizo saa 24 hadi 48. Najua wataleta vitisho kwamba kila atakayezima simu yake atafungiwa line yake hiyo, lakini hizo zitakuwa ni nguvu ya soda, kwani hakuna kampuni ya simu hata moja ya kuifungia line yoyote ile iliyosajiliwa kwa mujibu wa sheria, EPOCA, kwani sasa line hiyo ni chanzo cha mapato kwa Serikali.
Kampuni hizo haziwezi kukiuka mkataba wake na Serikali; tuzitie adabu, tuzitie hasara. Adabu isipotosha, mgomo huo (boycott) unarudiwa, mpaka Serikali na wabia wake haramu washike adabu, na waiondoe kodi hiyo haramu. Kwani wamiliki halali wa nchi hii ni nani kama sio sisi Watanzania, tena wanyonge, masikini, tulio wengi? Kwani viongozi wetu wanaolilia kututawala huja kuomba kura kwa nani wakati wa uchaguzi, kama sio kwetu sisi, ambao ndio tunaowapa dhamana hiyo ya kutwaa madaraka? Sasa cha kuogopa ni nini? Tukijipanga vizuri, tutafanikiwa. Hakuna kuogopa, zama hizo zimepitwa na wakati. Hata hivyo, kususia kutumia huduma hii ya simu SIO KOSA LA JINAI! NI HIARI! Tujipange! Inawezekana!
Put his dirty laundry out in the open!
Tafsiri ya mbinu hii ya pili ni "Anika nguo zake chafu hadharani!" Tafsiri fupi ni "anika siri zake za uhalifu/ufisadi hadharani". Kwa lugha ya Kiingereza, "dirty laundry" ina maana ya "uhalifu/ufisadi". Tukubali ukweli. Hakuna asiye na siri. Kampuni hizi za mawasiliano ya mkononi zimekuwa zikiwaibia (pasi na kuwa na ushahidi wa jinsi wanavyoibiwa) wateja wake kuwa miaka lukuki. Waajiriwa kwenye kampuni hizo, ambao ni Watanzania wenzetu, wamekuwa (kutokana na njaa zao) wakirubuniwa kushiriki kwenye wizi huu, pasi na kujua kwamba huu ni unyonyaji mkubwa kwa Watanzania, wengi wao ambao ni maskini.
Watanzania wengi wamekuwa wakilalamika jinsi pesa zao zinavyokatwa kinyemela pasi na kuwa na maelezo kwa sababu gani mambo haya yanafanyika. Kwa bahati mbaya, baadhi ya watendaji katika vyombo husika vya kusimamia sheria husika nao wameingizwa mtegoni, kwa kupewa ruzuku lukuki (bahasha za khaki), ambapo, kwa mfano, wanaposafiri nje ya nchi, hupangiwa masurufu makubwa ambayo kampuni hizi huhesabu kuwa "gharama ya uendeshaji kampuni ya ziada", au "overhead"/ Hapa tunahitaji kuwabembeleza Watanzania wenzetu wanaofanya kazi kwenye kampuni hizi kuwa wazalendo zaidi, na kutufunulia uchafu wote unaofanywa na kampuni hizi, kama ilivyofanyika kwa kampuni ambayo imekuwa ikiliibia taifa kwenye mapato ya matumizi ya umeme kwenye minara yake ya kurushia mawimbi, zaidi ya 1,700, na kusababisha hasara ya zaidi ya Bilioni 119 KWA MWEZI! Sasa harakati na ziendelee.
Tuanike nguo zao chafu hadharani, kila mtu azione: Tuifanye thamani ya kampuni zao iwe ndogo kabisa, kiasi kwamba wezi hawa washitakiwe kwa mujibu wa sheria, ikishindikana, wauze kampuni zao kwa wafanyabiashara wengine ambao wataogopa kutuibia, kwani watatambua kwamba, kwanza, wamenunua kampuni hizo kwa bei ya "kutupa", lakini pili, watatuheshimu Watanzania na kuogopa kurudia makosa ya wenzao.
Mbinu hizi mbili zinatosha. Acheni kuhangaika na hizo petition. Hazisaidii chochote. Mkitaka ushauri wa jinsi ya kuratibu harakati hizi, nitawapa, lakini msiniPM. Sitapokea PM ya mtu yeyote kuhusu hili, kwani najua miongoni mwetu humu wamo mandumilakuwili wengi tu. Siko tayari kumwamini mtu yeyote nisiyemjua kuhusu hili. Nitaweka mambo hadharani.
Kila la heri.
A luta continua!
P.S.: Moderators, nalazimika kuirudia post hii kwenye uzi wake, baada ya kuiweka chini ya post nyingine, kwa kuwa naona hata hao walioanzisha post hiyo ya kukusanya saini kupitia petition wameichoka. Nadhani wameelewa kwamba wanachokifanya hakina tija kwao.