BONUS PART
New York Police Department.
Saa Mbili Asubuhi
Afisa mmoja wa polisi alifika katika ofisi ya mpelelezi akiwa ameshikilia bahasha kubwa ya kaki.
Afisa huyo, mwembamba mrefu, mwendo wake wa kikakamavu, alikuwa na macho ya kizungu mithili ya paka. Sura yake ilikuwa ya kazi, na kofia yake aliyoishusha mpaka kwenye nyusi ilizidi kumfanya atishe.
Alimkabidhi mpelelezi bahasha kisha akamwambia kuwa hicho ndicho walikipata kwa kupitia kitengo maalum za 'CCTV Surveillance'. Baada ya hapo alienda zake asingoje hata maneno ya ziada. Alikuwa ni mjumbe tu.
Mpelelezi alikagua bahasha ile aliyoletwa akakuta maelezo kadhaa na picha vilevile. Miongoni mwa picha hizo alikuwapo Ferdinand na gari walilolikodisha siku ambayo tukio la mauaji lilitokea The DL.
Maelezo yalieleza ya kwamba bwana huyo, pamoja na mwenzake ambaye alikuwa mwanamke, waliutumia usafiri huu wa uber kufika kwenye makazi yao ambayo bado hayajajulikana.
Mpelelezi alijikuta anatabasamu. Sasa aliona kazi yake imeelekea ukingoni mwa ushindi.
Mara moja, kwa kupitia maelezo aliyoyapata, haswa ya gari, alinyookea kwenye ofisi za kampuni ya Uber inayopatikana katika jiji hili kubwa.
Huko aliingia makaoni akataka taarifa, katika mfumo mzima wa Uber, za mtu aliye-request uber yenye 'plate number' zilizopo pichani, saa fulani kutoka kweye bar ya The DL. Alikuwa anataka kujua kila kitu, ikiwemo na ramani ilionyesha gari hilo lilipeleka wateja wapi.
Kuwasababu ya ithibati ya polisi, kampuni haikuwa na namna zaidi ya kuingia kwenye data kusaka kinachodaiwa. Ndani ya muda mfupi, mpelelezi akawa amepata karibia ya kila anachohitaji.
Kabla ya 'move' yoyote ya kusogelea walengsa wake, alimtafuta dereva aliyehusika na kuwasafirisha watu hao, yeye akamhoji maswali kadhaa haswa juu ya haiba ya wateja hao ambao alimkumbushia kwa kutumia picha.
Alipomaliza hapo, alirejea kwenye ofisi yake, akaketi akiyapanga mambo kichwani kwa ustadi wake alobarikiwa na ujuzi wake aliosomea.
Alihoji kila taarifa aliyopata. Kwanza, kwanini watu hawa walifanya mauaji? Kwanini mwaname yule aliingia hapo bar akiwa amejificha na kofia ina maana alidhamiria kuja kufanya tukio? Kwanini walitumia usafiri wa uber, si usafiri binafsi au daladala?
Kwanini taarifa anazozitumia mtu aliye-request uber, si sahihi kwa maana ya kwamba namba yake ya taifa na taarifa zingine alizozianisha hazikuwepo kabisa kwenye mfumo wa serikali?
Na kwanini watu hao walishukia njiani, si mbele, karibu au ndani ya jengo la makazi ambalo ni rahisi kubainika?
Maswali haya alijiuliza akiitazama picha ya mwanamke ambayo alipewa na mfumo maalum wa utambuzi wa serikali. Punde alipoweka namba ambazo mteja yule alikuwa amejisajili nazo, zilimletea hiyo picha.
Ilikuwa ni picha ya mwanamke mdogo, makamo ya miaka ishirini na moja mpaka ishirini na tano hivi. Amebana nywele zake anatabasamu.
Mpelelezi alinyanyua simu yake ya mezani akaagiza mtu fulani kufika ofisini kwake upesi. Punde kidogo, alifika afisa mmoja mnene aliyekuwa amening'iniza 'badge' yake shingoni, amevalia miwani na 'form six' nyekundu.
Mpelelezi alimkabidhi bwana huyo picha ile aliyokuwa anaitazama akamwambia atafute taarifa zote kuihusu alafu amletee mara moja.
Bwana huyo alipotoka, akaingia tena yule afisa aliyekuja mwanzoni. Saa hii alikuwa na bahasha nyingine. Alimkabidhi mpelelezi akamwambia kuwa hiyo ni taarifa kuhusu kesi ya mauaji ya Afisa Parker, nayo taarifa ilikuwa imetoka kwenye kitengo cha 'CCTV Surveillance'.
Kitengo hicho kilikuwa kimepewa jukumu la kutafuta chochote kile kinachohusiana na kesi ya mauaji ya Afisa Parker. Taarifa ambayo mpelelezi alikuwa anataka kuiwianisha na ile aliyoipata toka kwa majirani kuhusu wageni wanaotuhumiwa kufanya mauaji ya afisa huyo nyumbani kwake.
Zilikuwa ni picha kadhaa za gari lililohusika, picha ambazo kwake hazikuwa ngeni, alishazipitia nyingizo, lakini miongoni mwa picha hizo, kuna moja ilimvutia zaidi.
Ilikuwa ndiyo picha pekee ya karibu kushinda zote. Aliitazama picha hii kwa umakini akaona kivuli cha uso wa dereva wa gari lile lililohusika na mauaji.
Sura haikuwa wazi lakini alipata kitu zaidi. Umbo la kichwa na mabega ya aliyekuwa anaendesha yalionyesha jinsia ya kiume na pia mtindo wake wa nywele ulionekana.
Aliichukua picha hiyo akaigundisha kwenye ubao wake mdogo kwa kutumia pini, kisha akampigia simu mtaalamu wa michoro ndani ya kitengo hicho cha polisi.
Alimwambia mtaalamu huyo afike haraka katika ofisi yake. Ndani ya sekunde chache, bwana akafika. Alikuwa ni mtu mwenye makamo ya miaka arobaini. Mwanaume mwenye nywele nyeusi na nyeupe zilizojiviringita.
Alimsihi aitazame ile picha ubaoni na kisha askilize maelezo ya majirani kuhusu mtu waliyemuona kisha amtengenezee picha yenye walau ukaribu wa utambulisho wake.
Wataalamu hawa huwa wanatumika pale ambapo hamna namna yoyote ya kupata picha muhimu za mnato kumuhusu mhusika ila maelezo yao yapo kwa kupitia kauli za washuhudiaji.
Picha hizo zinazotengenezwa angalau hutoa nafasi ama mahali pa kuanzia endapo zikiwa na ukaribu wa angalau asilimia sabini na mhusika mwenyewe.
Basi wakati mtaalamu akiwa anachukua taarifa muhimu, Mpelelezi alijiveka koti lake akatoka ndani ya ofisi.
Alijiweka kwenye gari lake kisha akatimka kuelekea magharibi mwa eneo walilopo. Alikuwa amedhamiria kufika eneo lile ambalo wahusika wake wa mauaji ya The DL walishukia wakitoka kwenye usafiri wa uber.
Alipofika hapo, majira haya palikuwa na shughuli nyingi, watu wakikatiza huku na kule kila mtu na mambo yake.
Alipakagua kwa macho yake ya stadi, akasogelea moja ya fremu kubwa ya duka inayopatikana eneo hili.
Ndani alikutana na mwanaume na mwanamke mzee ambao ndo' wamiliki na wauzaji. Walimkaribisha na kumuuliza namna gani ya kumsaidia, bwana huyo akasema anahitaji rekodi ya kamera yao ya nje, kuna tukio muhimu anadhani huenda likawa limenaswa na macho hayo ya teknolojia.
Bila hiyana walimpatia.
Alifanya hivyo kwenye maduka kama matano ambayo aliyabahatisha kuwa na kamera za uangalizi.
Kwa mwenendo wa kamera hizo, akiunganisha matukio na hatua ya walengwa wake, alijikuta anamini kabisa kuwa wahusika walielekea kwenye jengo kubwa la kifahari la Halletts Point!
Hayo ndo' yalikuwa makazi ya watuhumiwa wa mauaji yaliyotokea The DL.
Kwa msaada wa data za kamera za barabarani, na hizi alizopata toka kwa watu binafsi, hatimaye kiu yake ya taarifa ilikata.
Alitabasamu akilitazama jengo hilo kubwa la kuvutia.
Akiwa anafanya yote haya, kuna mtu alikuwa anahakikisha anapata picha ya kila kitu kinachoendelea. Kila hatua aliyokuwa anaipiga bwana huyo na kila aliyekuwa anaongea naye.
Mtu huyo, mpiga picha, alikuwa ndiye yuleyule aliyefanya kazi hii kulekule kwenye makazi ya Afisa Parker wakati mpelelezi akifanya kazi yake ya uchunguzi.
Alizitazama picha zake na alipoona kila kitu ni chema, alipotea