MADAI ya zawadi za suti tano na dola 1,000 za Marekani kupewa Rais Jakaya Kikwete yamezidi kukanushwa, safari hii kauli ikitoka kwa waliodaiwa kuhusika na utoaji wa vitu hivyo.
Kwa mujibu wa taarifa iliyosambazwa juzi kwa vyombo mbalimbali vya habari duniani kutoka kwa Mkurugenzi Mwendeshaji wa Kampuni ya Albwardy Investment ya Dubai inayomiliki hoteli za Kempinski, madai ya WikiLeaks dhidi ya Kikwete ni uongo mtupu.
Mkurugenzi huyo Philip DAbo, juzi aliandika kuwa katika maelezo yote yaliyomkariri Balozi wa zamani wa Marekani nchini Michel Retzer, ukweli pekee uliomo ni usahihi wa majina ya watu waliotajwa na hakuna mwingine zaidi ya huo.
Nikiwa nimefanya kazi kwa zaidi ya miaka 30 na Ali Albwardy, na sasa nikiwa Mkurugenzi Mwendeshaji wa kampuni zake, napenda kuweka sawa uongo huu uliopindukia na madai potofu dhidi ya Rais na bosi wangu.
Kwanza, Lisa Pile, alikuwa Meneja Mauzo na Masoko wa hoteli ya Kilimanjaro, nimeongea naye na amekanusha katakata kuzungumza na Balozi chochote kama anavyodai na anathibitisha kuwa hawezi kutamka neno lolote la Kiswahili, alisema DAbo katika taarifa yake.
Alisema hata siku moja Rais Kikwete hakuwahi kuomba au kupewa rushwa na Albwardy na wala bosi wake huyo hakuwahi kumlipia Kikwete tiketi ya ndege kwenda London au kumnunulia hata suti moja katika duka la Saville Row.
Huu ni utunzi na uzushi kama ilivyo katika madai ya kutoa dola milioni moja kwa CCM, kwani hakuna wakati hata mmoja kiongozi yeyote wa CCM aliomba fedha hizo kwa Albwardy, alisema DAbo.
Akizungumzia maombi ya bosi wake kuhusu ujenzi wa hoteli Zanzibar, DAbo alisema wakati wa uzinduzi wa hoteli yake ya nyota tano, Albwardy yawezekana kweli aliomba eneo kwa ajili hiyo Mji Mkongwe, na baada ya miaka mitano ya majadiliano, alinunua eneo. Juu ya hoteli ya Serengeti, taarifa hiyo ilisema baada ya miaka mitano ya makubaliano kusainiwa, hatimaye bosi wake alijenga hoteli katika mbuga hizo Bilila Kempinski.
Hata hivyo hizo zilikuwa enzi za Waziri wa Utalii na Maliasili, Zakia Meghji, chini ya uongozi wa Awamu ya Tatu ya Rais Benjamin Mkapa
kwa eneo la Ngorongoro, hadi leo maombi hayajakubaliwa hata licha ya Rais Kikwete kuwa madarakani kwa zaidi ya miaka mitano sasa, aliongeza DAbo.
Alisisitiza, kuwa kutokana na Pile kutozungumza Kiswahili hakukuwa na uwezekano wowote wa kufanyika mawasiliano na mtu yeyote, na pia alikanusha kama ilivyo kwa menejimenti ya Kempinski, dhidi ya vyumba vya hoteli hiyo kutumiwa na viongozi wa Serikali.
DAbo alisema kutokana na madai hayo, bosi wake anajisikia vibaya, kwamba uwekezaji wake katika nchi hii nzuri ya Tanzania, unaweza kuchafuliwa na uzushi kama huo kama ilivyo kwa Rais Kikwete ambaye naye anajisikia vibaya.
Wakati huo huo, Pile naye katika ujumbe wake kwa rafiki yake aliyetambuliwa kwa jina la Hasu Masrani, anaelezea kusikitishwa kwake na taarifa hizo, akisema huo ni uongo na ni uchafu na anajisikia kuchafuliwa hadhi yake.
Sikuwahi kuzungumza Kiswahili na sikuwahi kuonana na Rais wa Tanzania wala Rais yeyote duniani. Naamini nastahili kuombwa radhi kwa kashfa hii kama mimi binafsi lakini pia taaluma yangu, alisema Lisa.
Katika sehemu ya madai yake hayo, Balozi Retzer anakaririwa akisema baadaye Oktoba 18, tukila chakula cha usiku (hotelini Kempinski), mtu mwenye asili ya kihindi au kiasia, aliyeelezewa kuwa mbia wa kibiashara wa Albwardy, alimchukua Lisa kutoka mezani kwake na kwenda kuteta naye kwa Kiswahili.
Sina uhakika wa nini kilizungumzwa, lakini jina la Kikwete lilitamkwa mara nyingi na kisha akampa bahasha. Lisa aliniambia bahasha hiyo ilikuwa na dola 1,000 na zilikuwa ni kwa ajili ya kulipia mkutano wa Kikwete hotelini hapo baadaye mwezi huo.
Ikulu ilikanusha madai hayo pia na kuelezea kusikitishwa kwake na kuziita kuwa kampeni hizo ni upuuzi na uzushi wenye lengo la kuchafua jina zuri la Rais katika hadhi ya kimataifa. Akifafanua kuhusu hilo, Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu, Salvatory Rweyemamu, alisema: Tunasikitika kwa kuona jina la thamani la Balozi linahusishwa na ujinga kiasi hiki, alisema Rweyemamu.
Alisema Rais Kikwete tangu akiwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, hakuwahi kupelekwa na mtu yeyote London, Uingereza, kama inavyodaiwa, kununuliwa suti tano.
SOURCE: HABARILEO