Chama cha wafanyakazi wa serikali kuu na afya (TUGHE) kimemlaani Mh Zitto Kabwe kwa kuweka hadharani mishahara ya wabunge, mawaziri, waziri mkuu na rais.
Lengo la Zitto kutaja mishahara ya vigogo lilikuwa kuonyesha jinsi gani wanasiasa wanavyojilipa mamilioni ya pesa za walipakodi huku wafanyakazi, hasa wa kada ya nchini (walimu na wengineo) wakilipwa mishahara midogo ambayo haizidi hata posho ya mbunge kwa siku moja!
TUGHE ni chama kinachopaswa kutetea maslahi ya wafanyakazi, hasa madai ya nyongeza ya mishahara, kupandishwa vyeo, madai ya pesa za nauli, posho, nk. Kwa hiyo, TUGHE hawakupaswa kumlaumu Zitto bali wangemsifu kwa kuanika hadharani mishahara ya vigogo, ambao hutumia zaidi ya nusu ya pesa zinazotengwa kwa ajili ya mishahara ktk nchini nzima. Yaani kikundi kidogo cha watu wasiopundukia 500 wanalipwa zaidi ya nusu ya mishahara ya serikali!
Ulipaji mishahara wa ovyo kama huu, usiozingatia usawa, ndio unapelekea serikali kugoma kuwaongeza wafanyakazi mishahara kwani sehemu kubwa ya pesa ambazo zingetumika kuongezea mishahara huishia matumboni mwa kikundi kidogo cha wateule wachache--ambao ni peke yao tu waliobarikiwa kuishi maisha bora.
Kwa hali kama hii nilitegemea kwamba TUGHE wangemuunga mkono Mh Zitto kuibana serikali iboreshe mishahara ya wafanyakazi wa kada ya chini badala ya kuzidi kuwalundikia posho wabunge, mawaziri, makatibu wakuu na wakurugenzi huku wafanyakazi ngazi ya chini wakizidi kufa njaa kila kukicha. Nina wasiwasi kama kweli TUGHE wanatetea masilahi ya wanachama wao au kama wanatetea masilahi ya serikali inayowakandamiza wafanyakazi wataalam huku ikiwabeba wanasiasa. Sina imani tena na chama hiki katika kutetea maslahi ya wanachama wake. Hiki ni chama cha kinafiki na kindumilakuwili na kamwe hakiwezi kutegemewa kuwatetea wanyonge ikiwa viongozi wake wana mawazo mgando na tabia za kifisi kama hizi. Wanachama wa TUGHE mtakuwa mmeng'amua aina ya chama mnachokitegemea kuwatetea dhidi ya ukandamizaji wa serikali. Hiki ni chama cha ovyo kabisa kuwahi kuwapo katika ardhi hii ya Tanzania.