Analogia Malenga
JF-Expert Member
- Feb 24, 2012
- 5,011
- 9,879
Akizungumza katika kikao kazi cha kutoa taarifa ya hali ya mawasiliano Kanda ya Ziwa kilichowajumuisha viongozi wa Jeshi la Polisi wilaya za Ilemela na Nyamagana, Ofisa Usajili kutoka Mamlaka ya Taifa ya Vitambulisho (Nida), watoa huduma wa makampuni ya simu na wanahabari, Mkuu wa Mamalaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) Kanda ya Ziwa, Francis Mihayo, alisema baada ya zoezi la usajili kuongezewa muda limeibuka kundi la vijana linaloingia mtaani kuwatapeli wananchi.
Aliongeza kuwa vijana hao wanakuwa wamevalia sare za watoa huduma kutoka kampuni za mitandao ya simu hupita majumbani, mitaani na sehemu za biashara na kuwalaghai baadhi ya wananchi kuwa usajili wa namba za simu kutumia alama za vidole unafanyika sambamba na uhakiki wa akaunti za benki, hivyo kusababisha watu wengi kuibiwa fedha zao kwa kutumia mitandao.
"Baada ya Rais kuongeza muda wa usajili tumebaini kuongezeka wimbi la utapeli unaofanywa na wakala wao wasio waaminifu, hivyo wananchi watambue zoezi linaloendelea ni la usajili wa laini za simu kwa njia ya kibiometria kwa kutumia kitambulisho cha Taifa au namba ya kitambulisho cha Taifa na siyo uhakiki wa akaunti za benki, hivyo akitokea mtu anayemtaka kufanya hivyo atoe taarifa mapema," alisema Mihayo.
Aidha, alisema, takwimu zinaonyesha hadi Desemba 31, mwaka jana idadi ya laini zilizosajiliwa ni 48,321,949, ambapo laini zilizosajiliwa kwa alama za vidole ni 24,021,757 sawa na asilimia 49.7 ya laini zote, huku laini ambazo hazijasajiliwa kwa alama za vidole ni 24,300,192.
Naye Mkuu wa Upelelezi Wilaya ya Nyamagana, Mrakibu wa Polisi Juma Jumanne, alisema, utapeli wa mitandao ya simu umeanza muda mrefu, na unabadilika kutokana na wakati, lakini usajili wa alama za vidole utasaidia kupunguza vitendo hivyo.
Hata hivyo, alisema baada ya siku za usajili kuongezwa, vitendo vya utapeli vimeongezeka, hivyo wananchi wachukue tahadhari na wawe makini.
Raphael Manase, Ofisa Msajili Mkoa wa Mwanza, aliwataka wananchi kuzingatia maelekezo wanayopewa na kufuata utaratibu uliopo pamoja na kutokukubali kupewa maelekezo mengine ya upotoshwaji, kitu ambacho kitasababisha kutapeliwa.
Chanzo: Nipashe