Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe.
Maalim Seif Sharif Hamad, amewaongoza maelfu ya
waislamu katika mazishi ya sheikh maarufu wa
Mkoa wa Mwanza na mwanaharakati wa dini ya
Kiislamu marehemu sheikh Ilunga Hassan Kapungu.
Sheikh Ilunga amefariki dunia mjini Dar es Salaam
na kuzikwa katika makaburi ya Mwinyimkuu
Magomeni.
Katika uhai wake sheikh Ilunga Kapungu alikuwa
mwanaharakati ambaye mara nyingi alikuwa
akiendesha mihadhara ya wazi ya dini ya Kiislamu,
ambapo mwishoni mwa mwaka 2013 alikamatwa
kwa tuhuma za uchochezi mkoani Tabora na
baadaye kuachiwa huru.
Kwa mujibu wa taarifa za kimtandao, kabla ya
kukamatwa kwake na kuachiwa huru Disemba
mwaka 2013, marehemu sheikh Ilunga alikwenda
nchini India kwa matibabu baada ya kusumbuliwa
na matatizo ya figo pamoja na sukari.
Akizungumza katika mazishi hayo sheikh Basaleh wa
Dar es Salaam, amesema marehemu sheikh Ilunga
alikuwa mwanaharakati imara na ni mfano mzuri wa
kuigwa katika harakati za dini ya Kiislamu.
Mazishi yake yameweka historia baada ya maelfu ya
waislamu kujitokeza kushiriki kwao, hali iliyopelekea
mchanga wa kaburi lake kufukiwa kwa mikono
badala ya kutumia mapauro na majembe kama
ilivyozoeleka.
Masheikh kutoka Mikoa mbali mbali ya Tanzania
wameshiriki mazishi hayo akiwemo sheikh Kishki.
(HAKIKA YA SISI NI WAJA WA ALLAH NA NI KWAKE
YEYE TU MAREJEO YETU)
Allah tunakuomba umsameh madhambi yake na
umjaalie kuwa ni miongoni mwa waliofuzu na
umjaalie makaazi katika FIRDAUS