SERIKALI ya Tanzania imebwagwa katika rufaa yake iliyokata dhidi ya uamuzi wa mahakama ya Afrika Mashariki ya kuzuia ujenzi wa barabara ya Musoma-Serengeti-Arusha baada ya kitengo cha Rufaa cha Mahakama hiyo jana kuamua kuwa uamuzi huo ulikuwa sahihi.Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa serikali ya Tanzania ilipinga hati hiyo kwa madai kuwa mahakama haikuwa na mamlaka ya kufanya hivyo kisheria.Kupitia kwa Wakili Mkuu wa Serikali, Gabriel Malata serikali ya Tanzania ilidai mbele ya jopo la majaji watatu wa mahakama hiyo wakiongozwa na Rais wao, Jaji Harold Nsekela, Jaji James Ogoola na Jaji Emilie Kayitesi kuwa hati hiyo iliyotokana na shauri lililofunguliwa dhidi yake na taasisi isiyo ya kiserikali inayoshughulikia haki za wanyama ya Africa Network for Animal Welfare (ANAW) ya nchini Kenya inayopinga mradi huo haikuwa halali kisheria.Wakili Malata alidai licha ya mahakama hiyo kuwa na uwezo wa kusikiliza na kuamua shauri, suala hilo linahusu mambo ya ndani ya Tanzania na yalistahili kuwasilishwa na raia wa Tanzania au NGO ya Kitanzania mbele ya mahakama iliyo ndani na chini ya mamlaka ya nchi ya Tanzania.Maombi hayo ya Tanzania yalipingwa na wakili Saitabao Kanchory Mbalelo anayewakilisha walalamikaji aliyedai mahakama hiyo ina uwezo na mamlaka ya kutoa hati ya kuzuia utekelezaji wa mradi huo na kuomba mahakama kutupilia mbali rufaa hiyo.Akisoma uamuzi wa jopo hilo kwa niaba ya wenzake jana, Jaji Ogoola alisema kifungu cha 9 cha mkataba wa Jumuiya ya Afrika Mashariki kinaipa mamlaka, haki kisheria Mahakama ya Afrika Mashariki kutoa hati ya zuio na hivyo kutupilia mbali rufaa ya serikali ya Tanzania.Pamoja na mambo mengine taasisi hiyo ya Kenya kwa kushirikiana na taasisi zingine za ndani ya nchi wanaoungwa mkono na baadhi ya nchi wafadhili na mashirika ya kimataifa ya fedha wanapinga ujenzi wa barabara hiyo kutoka Musoma-Mugumu-Ngorongoro hadi Arusha mjini kwa madai kuwa utafanya magari mengi kupitia njia hiyo na hivyo kuathiri ikolojia ya wanyama wanaohama kutoka hifadhi ya Serengeti nchini Tanzania kwenda hifadhi ya Masai Mara nchini Kenya kila mwaka
ANGALIZO:
Ø Kwa mtindo huu wa kenya kuingilia mambo ya ndani ya Tanzania kila wakati na kizivuruga nini maana yake?
Ø Ikumbukwe pia walishawahi kuvuruga tana pale tanzania ilipoomba kibali cha kuuza meno ya temba na wakafanikiwa.
Ø Mbona sisi hatukuwaingilia pale walipoomba kibali cha kujenga bandari ya lamu?
Ø Kwa mtindo hu,nini manufaa na faida ya kuwa na east africa community kama wenzetu wanakua wanafiki na kinyume na sisi kila wakati?