TANZANIA KUADHIMISHA MIAKA 100 YA MWALIMU NYERERE
WIZARA ya Maliasili na Utalii kwa kushirikiana na wadau imeandaa na kuzindua programu ya Maadhimisho ya miaka 100 ya kuzaliwa Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ikiwa ni sehemu ya kuenzi na kusherehekea urithi wa maisha yake, itakayotumika kama zao jipya la utalii wa utamaduni.
Programu hiyo inayojulikana kama Mwl. Nyerere@100 ni sehemu ya mpango wa miaka 10 wa kuenzi na kusherehekea urithi wa maisha ya Mwalimu Nyerere ambao unalenga kuwashirikisha wadau ili kujenga uelewa wa pamoja kuhusu mchango wa Mwalimu Nyerere kitaifa na kimataifa.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa programu hiyo, Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Damas Ndumbaro amesema programu hiyo pia kutangaza, kumuenzi Mwalimu Nyerere na umuhimu wa kukusanya, kuendeleza, kuhifadhia na kutangaza rasilimali za urith wa Mwalimu Nyerere kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho ili kukuza na kuendeleza utalii.
" Kilele cha maadhimisho hayo kitakuwa Aprili 13 mwaka huu, Butiama mkoani Mara siku ambayo kama angekuwa hai angetimiza miaka 100, lengo likiwa ni kuenzi na kucherehekea mchango maridhawa wa Mwalimu Nyerere katika nyanja mbalimbali kitaifa na kimataifa."
Dkt. Ndumbaro amesema matukio yatakayofanyika wakati wa maadhimisho hayo kuanzia mwezi huu hadi kilele ni mikutano ya wadau, mashindano ya baiskeli, matembezi ya hiyari, ngoma za asili, Mwl Nyerere marathon, usiku wa Mwalimu Nyerere, Kalamu ya Mwalimu itakayohusiana na vitabu alivyoandika , maonesho, kughani mashairi na shindano maalumu ya kutengeneza nemba ya Mwalimu@100.
Akifafanua zaidi kuhusu mpango huo amesema Wizara yenye dhamana ya uhifadhi wa Malikale na matumizi yake ya Kiutalii imedhamiria kushirikisha wadau katika kuhifadhia na kutumia kiuendelevu urithi unaotokana na maisha ya Mwalimu Nyerere.
Amesema endapo Mpango huu utaweza kusimamia ipasavyo na kutekelezwa unategemea kuwezesha kutangaza nchi kwa kazi zikizofanywa chini ya Mwalimu Nyerere na pia viongozi wengine waliokuwa naye bega kwa bega.
Ameongeza kuwa kutakuwa na Makumbusho ya wapigania Uhuru ya kwanza Afrika ambayo itaitangaza Tanzania kwani kuna vioneshwa vya kutosha na urithi wa Mwalimu Nyerere utatambulika, kuhifadhiwa, kusherehekewa na kujulikana kwa watanzania wengi hasa vijana.
"Pia maeneo yenye historia ya Mwalimu Nyerere yatatangazwa, yatahifadhiwa kisheria lakini yatafunguliwa kwa ajili ya utalii na itakuwa ni utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi."