...HALI YA HEWA TAYARI NI TETE!
Wapo wanaoombea msimu wa mvua uanze ili hali ya joto la Dar es Salaam ipungue, lakini kwa wakazi wengi huwa na maombi tofauti na wakati mwingine wingu jeusi linapotanda tu, taratibu za kuhama makazi yao huanza.
Ni maisha ya mguu ndani mguu nje. Katika maeneo mengi ukipita utaona magodoro na samani nyingine zimeanikwa nje au kuhifadhiwa juu ya paa.
Wanaoishi maeneo ya mabondeni huogopa kulala ndani wakihofu huenda wakasombwa na maji wakati wowote kwa kuwa hata kama mvua hazinyeshi kwenye maeneo yao, bado hufuatwa na maji kutoka maeneo mengine ambako mvua hunyesha.
Katika miaka ya karibuni mvua kidogo tu imekuwa ikisababisha kadhia mbalimbali kwa wakazi wa Jiji la Dar es Salaam, ikiwemo mafuriko na ongezeko la msongamano wa magari barabarani.
Ongezeko la watu, kuziba kwa mifereji ya kupitisha maji na kujenga katika njia za maji ni baadhi ya sababu zinazotajwa kuchangia kuwafanya wakazi wa Dar es Salaam hasa waishio mabondeni, kukosa usingizi katika kipindi hiki.
Gazeti hili lilifika katika baadhi ya maeneo na kushuhudia familia zikiwa nje ya nyumba zao. Wengine wakiwa wamefungia vitu vyao ndani na kuelekea maeneo mengine wakisubiri maji yakauke ili warudi kuendelea na maisha mabondeni.
Maisha kipindi cha mvua
Hivi sasa tunaishi kwa machale. Tukiona wingu au mvua imeanza kunyesha tunaondoka. Mali inaweza kutafutwa lakini sio uhai wa mtu, anasema Madande Jabir mkazi wa Gongo la Mboto.
Jabir anasema mvua ya saa mbili iliyonyesha juzi katika maeneo hayo imesababisha maafa makubwa, ikiwemo kubomoa kuta za nyuma, kuharibu samani na mazao yaliyokuwa shambani.
Kama isingekuwa machale, ina maana ile nyumba ilipobomoka ingeua watu, lakini tunaishi kwa kujihami na kujibanza popote salama unapoona mvua haiwezi kukubeba, anasema Jabir.
Wakazi wa Nyaishozi nao wanastaili nyingine ya maisha ambao inasababishwa na maji kujaa ndani ya nyumba zao.
Mwanahamisi Juma anasema maji yameingia mpaka ndani, lakini kwa kuwa si mengi sana, wanalazimika kuendelea na maisha ingawa hali hiyo ina hatarisha afya zao.
Nikiingia ndani kulala, mkononi ninashika kikombe chenye maji kwa ajili ya kunawa miguu. Yaani nakaa kitandani kisha najimwagia maji yaliyomo ndani ya kikombe kwa kuwa miguu huchafuliwa na maji yaliyojaa ndani, anasema Mwanahamisi.
Kauli ya wanaharakati
Mkurugenzi wa Haki Ardhi, Yusuph Myenzi anasema yapo mambo manne makuu yanayosababisha mafuriko jijini Dar es salaam, hasa katika kipindi hiki cha mvua.
Anasema pamoja na hali mbaya ya kimazingira inayojitokeza, ukweli ni kwamba Jiji la Dar es salaam halijawahi kupata mvua kubwa ambayo ikitokea, hali itakuwa mbaya zaidi.
Aliyataja mambo makuu yanayosababisha mafuriko kuwa ni ujenzi holela ambao huchangia kuziba kwa njia za maji.
Jambo la kusikitisha ni kwamba serikali ndio kinara katika hili. Mfano ujenzi uliofanyika eneo la Mikocheni, pale zilipo ofisi za Tanesco, eneo lile lote lilikuwa ni njia ya maji lakini Serikali imeweka majengo yake, tena kuna nyumba hata za viongozi wake, anafafanua.
Kwa hali hiyo watu wengine watafanyaje kama si kuiga? Si hivyo tu bali pia serikali imepeleka miundombinu kama vile maji na umeme, anasema Myenzi.
Anaongeza kuwa, uwekezaji hafifu wa miundombibu ya kupitishia maji ni suala jingine linalochangia mji wa Dar es Salaam kujaa maji.
Anafafanua kuwa sababu nyingine ni uchafu uliokithiri kwa wakazi wa Jiji la Dar es salaam akisema wamekuwa wakitupa taka hovyo, jambo linalosababisha kuziba kwa mifereji inayopitisha maji.
Kuna baadhi ya maeneo wala si hatarishi, lakini kwa sababu za uchafuzi wa mazingira yameingia katika mkumbo huo na hali huwa mbaya sana msimu huu, anafafanua.
Anasema kuzorota kwa upimaji wa viwanja kunaweza kuwa ni sababu kuu, inayosababisha matatizo yote hayo kwani kutokana na ukosefu au kusuasua kwa huduma hiyo, wakazi wengi hujikuta wakijiamulia wenyewe makazi ya kukaa.
Takwimu za kitaifa zinaonyesha wizara ina uwezo wa kupima viwanja 20,000 kwa mwaka nchi nzima. Hii ni sawa na wastani wa viwanja visivyozidi 1,000 kwa kila mkoa. Sasa pata picha kwa jiji kama la Dar es Salaam hali inaweza kuwaje? anahoji.
Kukosekana kwa utawala bora
Mkurgenzi wa Kituo cha Msaada wa Kisheria na Haki za Binadamu, Hellen Kijo Bisimba anasema matatizo yote yanayoambatana na makazi ni matokeo ya kukosekana kwa utawala bora.
Wala hawakukosea wale walioiweka Tanzania kwenye nafasi ya 102 katika suala la utawala bora, kwani ukweli ni kuwa licha ya viongozi serikalini kuyaelewa maeneo hatarishi, bado wanathubutu kutoa vibali vya ujenzi kwenye maeneo hayo na kuruhusu ufikishwaji wa miundombinu hiyo kwenye maeneo hayo, anasema.
Hivi unadhani hawayafahamu maeneo hayo? Ninachokiona mimi ni kwamba serikali imekuwa na watendaji wanaofikiria mambo kwa urahisi. Naamini kuna wataalamu mahiri kwenye Wizara na Idara za serikali, kinachofanyika hapa ni hawa viongozi kupuuza ushauri wa wataalamu wetu na kufanya vile wanavyotaka wao, anaongeza.
Anasema ili kuondokana na adha ya maafa mbalimbali sio tu ya mafuriko, kunahitajika kuwapo watu wanaojua na kuyafanyia kazi majukumu yao kwani haina maana viongozi kusubiri maafa yatokee ndio waanze kutoa matamko.
Ofisa uhusiano wa Wizara ya Ujenzi, Martin Ntemo anasema: Sidhani kama mifereji ya maji ndiyo chanzo cha mafuriko. Lakini kuongezeka kwa ujenzi holela kumechangia kuziba njia ya maji kuelekea baharini.
Akihutubia Bunge la Bajeti ya 2013/2014, Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka alisema kati ya changamoto zinazoikabili wizara hiyo ni uelewa wa wananachi juu ya haki na wajibu wao.
Alisema wananchi kutoelewa sheria zilizopo kunasababisha ugumu katika utendaji wa watumishi wa wizara hiyo.
Ni kauli ambayo inadhihirisha kuwa serikali inatambua maeneo hayo na kama haitafanyia kazi mvua zitaendelea kuwa jinamizi kwa wakazi waishio mabondeni.
mcl