esther mashiker
JF-Expert Member
- May 29, 2018
- 616
- 552
TAASISI ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) imefanikisha kutopeleka mgonjwa wa moyo kwenda nje ya nchi kwa matibabu kwa mwaka huu. Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Mkurugenzi wa Idara ya Magonjwa ya Moyo wa taasisi hiyo, Dk Peter Kisenge alisema hayo ni mafanikio makubwa kwa taasisi hiyo kwani imesaidia kuokoa fedha nyingi za serikali ambazo hutumika kugharamia matibabu kwa wagonjwa ambao hupelekwa nje ya nchi.
Alisema mafanikio hayo yametokana na taasisi kuwa na vifaa vya kutosha vinavyohitajika kwa matibabu ya moyo na pia kuwa na wataalamu. Wagonjwa waliokuwa wakipelekwa nje ya nchi kwa matibabu kwa gharama za serikali imekuwa ikipungua mwaka hadi mwaka tangu kuanzishwa kwa JKCI. Kwa mwaka wa fedha 2016/17, wagonjwa wa moyo waliopelekwa nje ya nchi walikuwa ni 17. Mgonjwa mmoja kwenda nje ya nchi kwa matibabu gharama zake ni zaidi ya Sh milioni 30. Dk Kisenge alisema taasisi hiyo kwa sasa imekuwa na jina kubwa kutokana na matibabu ya kibingwa ambayo yanatolewa na pia wamekuwa wakitibu wagonjwa wa ndani ya nchi na pia Afrika Mashariki na Kati. Alisema kutibu wagonjwa kutoka nje ya nchi ina maana wana imani na huduma ambazo zinatolewa na taasisi hiyo.
Alisema kwa sasa taasisi inapokea wagonjwa wa nje 300 kwa siku, wagonjwa 10 hadi 15 ni wa rufaa na wagonjwa wawili ni kutoka nchi za Afrika Mashariki na Kati. Aidha, alisema JKCI pia inatoa mafunzo kwa madaktari mbalimbali ambao kwa mwaka madaktari hadi 20 wanapata mafunzo katika taasisi hiyo. Alisema hali hiyo ni tofauti na miaka ya nyuma ambayo madaktari walikuwa wakitumika kutibu wagonjwa mengi kutokana na kuwa na idadi ndogo ya madaktari, lakini kwa sasa hali ni tofauti. Dk Kisenge alisema taasisi hiyo hakuna mgonjwa ambaye anaweza kuka na asipatiwe huduma, wagonjwa wote wanatibiwa bila kujali hali zao kifedha.