JUMATATU, OCTOBA 08, 2012 06:06 NA BAKARI KIMWANGA, DAR ES SALAAM
*Akitaka chama hicho kijitafakari zaidi
*Awachana viongozi wanaogawa fedha
*Asema watu wa aina hiyo ni wezi, mafisadi
*Ambeba Lowassa, asema hana ugomvi naye
HATIMAYE Waziri Mkuu mstaafu, Frederick
Sumaye, avunja ukimya na kuamua kueleza ya moyoni baada ya kushindwa nafasi ya U-NEC kupitia Wilaya ya Hanang'.
Sumaye ametoa tahadhari kuhusu mwenendo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na kusema kuwa chama hicho kikongwe kinasumbuliwa na rushwa ambayo sasa imekithiri.
Alisema vitendo vya rushwa vilivyotawala ndani ya CCM vinaweza kuiangamiza amani ya nchi na kutoweka na kuliacha taifa katika matatizo makubwa.
Sumaye alikuwa akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, ambapo pamoja na mambo mengine, alizungumzia kushindwa kwake katika uchaguzi wa NEC.
Katika uchaguzi huo, Sumaye ambaye alikuwa waziri mkuu kwa miaka 10 mfululizo, aliangushwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji na Uwezeshaji), Dk. Mary Nagu.
Sumaye ambaye pia alikuwa Mbunge wa Hanang' kwa miaka 15 na baadaye kumwachia Nagu, alisema rushwa na mtandao wa watu ndivyo vilivyomwangusha katika nafasi hiyo.
Alisema hatua yake ya kuangushwa katika uchaguzi huo wa ni jambo la kawaida na limetokea kwa vigogo wengi katika maeneo mengi nchini, isipokuwa matukio hayo yanatofautiana kutokana na sura na viwango vya watu.
Sumaye, ambaye muda wote alikuwa akizungumza kwa kujimini katika mkutano huo, alisema uchaguzi huo uligubikwa na matumizi makubwa ya fedha, hali ambayo alisema inaweza kukiangamiza chama hicho.
"Tatizo la rushwa linazidi kuota mizizi, binafsi nimekuwa nikilizungumzia mara kadhaa, mfano Oktoba 10, 2010, nikiwa wilayani Same. Nilisema wazi kuwa hivi sasa inaonekana kuwa hapa kwetu huwezi kushinda uchaguzi bila kuwahonga wapiga kura.
"Kwa maana nyingine unakuwa kiongozi wa watu si kwa sababu ya watu wanakupenda, bali ni kwa sababu umewanunua.
"Kiongozi anayepatikana kwa njia ya rushwa basi yeye mwenyewe ni mwizi na fisadi, maana vinginevyo hizo fedha za kuwahonga angezipata wapi?" alihoji Sumaye na kuendelea:
"Kiongozi mtoa rushwa, huyo ni mali ya watu fulani, yaani wale waliompa fedha kisha fedha zile akazigawa kwa kuwanunua watu.
"Siku zote mtu anayemlipa mpiga zumari ndiye anayechagua wimbo, aidha huwatendei haki unaowawakilisha kwa sababu haoni jambo japokuwa macho anayo.
"Hana huruma kwa wananchi kwa sababu kwake wananchi ni sawa na bidhaa sokoni na akiwa madarakani kazi yake kubwa ni kutafuta fedha kwa ajili ya kuwahonga wananchi.
"Julai 7, mwaka 2011, nikiwa mkoani Kilimanjaro katika sherehe za miaka 35 ya kuzaliwa CCM, nilisema rushwa ni adui wa haki.
"Kama ilivyo katika mataifa mengi, rushwa ni tatizo kubwa katika nchi na kwenye chama chetu ni gonjwa ambalo halikuanza leo na limekuwa likiota mizizi.
"Ndugu zangu wanahabari hadi leo (jana), tunavyoongea hali ya rushwa wakati huu wa uchaguzi imekuwa mbaya zaidi, kwani katika uchaguzi wa kidemokrasia wapiga kura humchagua mtu wanayemtaka.
"Hivi sasa hali imetoka kwenye kuhonga ili achaguliwe katika eneo lake na badala yake hutoa rushwa za kimtandao ambapo mtu hutoa fedha katika maeneo mbalimbali nchini ili watakaochaguliwa wawe wafuasi wake mbele ya safari atakapokuja kuwahitaji.
"Kwani watu watakaochaguliwa kwa utaratibu huu utumishi wao na uwakilishi wao sio kwa wapiga kura ila kwa wapiga mihuri (wajumbe) waliomuidhinishia zile kura.
"Tunakuwa na uwakilishi wa mhuri bali si wa mtu, ninaomba Watanzania wote tulio CCM na vyama vingine vya siasa tupige vita hali mbaya inayodhihaki na kudhalilisha demokrasia na utu wa wananchi wetu," alisema.
Alivyoshindwa Hanang'
Akizungumzia uchaguzi wa Hanang', alisema kuwa uchaguzi huo uligubikwa na matumizi makubwa ya fedha, vitisho vingi pamoja na uharamia wa kuhamisha wapiga kura usiku.
"Maovu mengine mengi ambayo hayasemeki yalifanywa. Jambo la msingi mimi sijakata tamaa wala sitopeleka malalamiko ndani ya chama changu kwa sababu yaliyokuwa yanatendeka yanafahamika.
"Narudia tena mimi nitabaki kuwa mwanachama mwaminifu wa CCM. Nchi nyingi zenye demokrsia changa zimeingia katika vurugu na kuhatarisha amani na utulivu nyakati za uchaguzi.
"Naomba Tanzania tusichafue historia nzuri ya amani na utulivu kwa ajili ya uroho wa madaraka.
"Madaraka yatakuja tu kama wananchi wapiga kura wataona wewe ndiye utakayefaa na si kuwarubuni kwa fedha au jambo lolote kwa kutumia vibaya nafasi ya umaskini wao.
"Napenda nitambue kuwa haya ninayoyazungumza sio matamu masikioni kwa baadhi ya watu, lakini vema tukayasikiliza na kuchukua hatua chanya ili yasilete madhara zaidi katika jamii.
"Tusidiriki kuwanyamazisha watu wanaozungumza kwa uwazi, kwani hawa wanatuonyesha tahadhari iliyoko mbele kama taifa," alisema Sumaye.
Urais 2015
Akizungumzia suala la kugombea urais mwaka 2015, Sumaye alisema kuangushwa kwake katika uchaguzi wa NEC kumempa nguvu ya kujiimarisha kisiasa akiwa nje.
"Hadi sasa sijatangaza kugombea urais mwaka 2015, kwa hili lililotokea Hanang, limenipa ujasiri zaidi na ikiwa nitatangaza nitashinda tena nafasi hiyo nikiwa CCM," alisema.
Sina ugomvi na Lowassa
Sumaye alikanusha taarifa zilizoripotiwa na chombo kimoja cha habari (si Mtanzania) kwamba yupo radhi kugombea urais 2015 iwapo Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa atagombea.
"Kama kuna watu wanasema kuna Lowassa amechangia kuanguka kwangu Hanang' mimi siwezi kuthibitisha hilo, labda muulizeni mwenyewe.
"Sitaki kumsemea mtu lakini nina uhusiano mzuri na ndugu yangu Lowassa. sina uhasama na Lowassa, nikiamua kugombea sitogombea kwa sababu ya mtu, bali kwa sababu ya maslahi ya nchi na si ya mtu.
"Kuna chombo kimoja kilikwenda mbali na kuandika eti Sumaye amtangazia vita Lowassa, ikiwa ataingia atamkabili kwa namna yoyote....'
"Napenda kusema kuwa hakuna mwandishi aliyezungumza na mimi kwamba nitapambana na Lowassa, hakuna mtu wa karibu yangu atakayezungumza kwa niaba yangu," alisema.
Akanusha kukutana na Chadema
Katika hatua nyingine, Sumaye alikanusha kukutana na Chadema kwa ajili ya kufanya nao mazungumzo kama ilivyoripotiwa katika baadhi ya vyombo vya habari.
Sumaye alikanusha vikali kuwa na mahusiano ya karibu na viongozi wa Chadema na kusema kuwa taarifa hizo zimejaa upotoshaji mkubwa kwa jamii.
"Baadhi ya taarifa katika magazeti zimeandika Sumaye kupasua jipu Dar, mengine yakaandika Sumaye kulipua bomu.
"Napenda kueleza kuwa hapa sina jipu wala bomu la kupasua. Katika hili la Chadema, mimi sijakutana na viongozi wa chama hicho ni taarifa za uwongo.