Wakuu nimerudi, laptop yangu imezingua lakini siyo sababu ya kuukosa uhondo wa safari hii ya kusisimua ndani ya Taxi. Tuendelee...
CC
the_legend Norshad bobefu zoefu Pablo PAKAYA Ibney blackstarline Bryece Tater Bigjahman moneytalk marybaby nipo2 ram kisukari Smart911 Madame S carbamazepine Astelia culture gal Prisoner of hope Mine eyes kuku mweus Thad hearly Shunie moneytalk Tumosa Mine eyes Kudo swahiba92 ludist Toyota escudo Clkey macson3 boga la kiangazi LEGE Smart911 Richard irakunda skfull popie Krizy Beat hearly nipo2 MWINDAJI HARAMU kakhulu Katavi Norami mbududa iron2012 popie Bughy Harry Mlenge Kacheda mjasiliamali Laki Si Pesa cocochanel kinusikwetu big jambo mludego Shupavu Kacheda mjasiliamali Mweweso Songa Heri esiankiki
Taxi - (55)
ILIPOISHIA
Sammy alimfuata yule bibi akionekana kuchangamka, akapokea lile begi dogo na ule mfuko wa plastiki, akafungua mlango wa nyuma wa gari lake na kuviweka kwenye siti. Kisha alimshika mkono yule bibi kwa upole na kumsaidia kuingia ndani ya lile gari, akaketi kwenye siti ya nyuma. Yule bibi alimtazama Sammy kwa jicho la shukrani.
“Asante sana mjukuu wangu,” yule bibi alisema huku akishusha pumzi za ndani kwa ndani.
“Usijali bibi… natakiwa kuwatendea wateja wangu kwa namna ambayo ningependa mama yangu atendewe,” Sammy alisema huku akifungua mlango wa dereva, akaingia na kuketi.
SASA ENDELEA NAYO...
“Wewe ni kijana mwema… sasa unaweza kunipeleka Karakata,” yule bibi alisema huku akiachia tabasamu.
“Hakuna tatizo bibi, shilingi elfu tano tu,” Sammy alimwambia yule bibi huku akigeuza shingo yake kumtazama.
“Sawa, lakini tupitie barabara inayoelekea Mnazi Mmoja,” yule bibi alisema huku akijiegemeza kwenye siti.
“Huko tutakuwa tunazunguka sana, bibi… ipo barabara rahisi ya kupitia Mnyamani halafu Vingunguti kisha tunakwenda kutokea Karakata…”
“Sijali kama tutakuwa tunazunguka, sina haraka,” yule bibi alisema huku akiachia tabasamu.
“Lakini gharama inaweza kuwa kubwa zaidi.”
“Usijali kuhusu gharama, wewe fuata maelekezo yangu.”
Sammy alimtazama yule bibi kwa makini kupitia kioo cha katikati cha gari kinachotumika kuangalia nyuma na kushusha pumzi za ndani kwa ndani. Yule bibi alitulia tuli huku akiwa amejiegemeza kwenye siti, alionekana kuchoka sana.
“Daktari wangu ameniambia kuwa ninahitaji kufurahi zaidi ili niweze kuishi muda mrefu kidogo, vinginevyo sina muda mrefu wa kuishi,” yule bibi alimwambia Sammy huku akishusha pumzi za ndani kwa ndani.
Sammy hakusema neno, alibaki kimya huku akimtupia jicho yule bibi kupitia kile kioo cha katikati cha gari kinachotumika kuangalia nyuma, alibana taya zake na kuwasha injini ya gari, akaliondoa gari lake taratibu akiingia katika barabara ya lami iliyokuwa ikienda kutokea hospitali ya Amana.
Walipita kwenye ile barabara iliyokatisha katikati ya majumba mazuri na makazi ya kisasa ya watu wenye ukwasi yaliyozungukwa na kuta zenye usalama wa uhakika. Na baada ya mwendo mfupi wa safari yao waliyafikia makutano ya barabara ile na barabara iliyoelekea Hospitali ya Amana.
Sammy alikata kona na kuingia upande wa kulia akaenda kuungana na barabara ya Uhuru katika eneo la Amana Vijana, kisha akakunja tena kuingia upande wa kushoto akiifuata barabara ya Uhuru.
Katika barabara ile ya Uhuru kulikuwa na msongamano mkubwa wa magari, hivyo safari yao ilikuwa ya taratibu. Yule bibi alikuwa hasemi kitu badala yake alikuwa amezama kwenye kutazama mandhari ya ile barabara ya Uhuru.
Ule mwendo wa wastani ulimruhusu yule bibi kuona vizuri mandhari ya nje. Alikuwa anaona vitu vikiwa vinapita mbele ya macho yake na kurudi nyuma taratibu wakati lile gari likiwa linakwenda, mara wakayapita mabanda yaliyotumika kama vyumba vya wasusi wa Kimasai.
Akiwa bado anayatazama yale mabanda ya wasusi wa Kimasai kwa makini wakaikuta barabara ya Mafao iliyokuwa ikiingia kushoto, wakaivuka na kulipita jengo refu zaidi maarufu kama
Mafao House. Yule bibi alilitazama lile jengo kwa makini na kuminya midomo yake.
Baada ya safari fupi hatimaye wakalifikia jengo la ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, eneo la
Ilala Boma. Yule bibi aliliangalia kwa makini lile jengo la ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam na kukohoa ili kusafisha koo lake, kisha akamuonesha Sammy jengo hilo.
“Enzi za ujana wangu nilifanya kazi hapo kama Katibu Muhtasi,” yule bibi alisema. Sammy alilitupia jicho lile jengo la Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam na kubaki kimya.
Muda huo walikuwa wamefika katika makutano ya barabara ya Kawawa na Uhuru kwenye taa za kuongozea magari barabarani. Bahati nzuri walimkuta askari wa usalama barabarani aliyekuwa akiruhusu magari na kuwaruhusu wapite.
Gari la Sammy likapita huku watu wakilisindikiza kwa macho yaliyoonesha kulishangaa na baadaye wakazipita daladala zilizokuwa zimesimama katika kituo cha daladala cha Karume. Kisha wakaikuta barabara ya Shaurimoyo upande wao wa kulia na kuipita, na hapo Sammy aliongeza mwendo na kuyapita majengo ya kiwanda cha bia (TBL).
Lile gari lilizidi kwenda mbele na kuvuka taa za kuongozea magari barabarani katika makutano ya barabara za Msimbazi na Uhuru, eneo la Kariakoo. Sammy aliendelea kuendesha gari kimya kimya akiifuata barabara ile ya Uhuru hadi walipozifikia taa za kuongozea magari barabarani katika makutano ya barabara za Uhuru na Lumumba.
“Endelea mbele hadi utakapofika Mtaa wa Indira Gandhi, kisha uingie kushoto kuufata mtaa huo,” yule bibi alimwambia Sammy huku akitupa macho yake nje na kushusha pumzi za ndani kwa ndani.
Sammy alitii na kuendesha akizivuka taa za kuongozea magari barabarani za makutano ya barabara za Uhuru na Lumumba, akakivuka kituo cha daladala cha Mnazi Mmoja, kisha akazivuka taa nyingine za kuongozea magari barabarani katika makutano ya barabara za Uhuru na Bibi Titi Mohammed.
Baada ya mwendo mfupi hatimaye wakaufikia Mtaa wa Indira Gandhi, Sammy akakata kuingia kushoto akiufuata ule mtaa hadi mbele kidogo walipoukuta Mtaa wa Aggrey uliokatiza mbele yao.
“Umeiona hiyo hoteli hapo mbele, ni hoteli ambayo mimi na marehemu mume wangu tulikuja kwa ajili ya fungate mara tu tulipotoka kufunga ndoa,” yule bibi alimwambia Sammy huku akimwonesha kwa kidole. Sammy aliiangalia ile hoteli akiwa hajui aseme nini.
“Unaweza kusimama hapo kando?” yule bibi alimuuliza Sammy, na bila kuchelewa alisimamisha gari lake kando ya barabara ya mtaa ule. Yule bibi alibaki kimya kabisa akilitazama lile jengo la hoteli kwa kitambo kirefu.
Sammy alionekana kukerwa kidogo lakini hakuwa na namna ya kufanya. Aliwaza: kama kazi ya kuendesha teksi ilikuwa na usumbufu kiasi kile ni heri angetafuta kazi nyingine ya kufanya. Alikuwa amepatikana! Kutoka Meneja Matukio katika hoteli kubwa yenye hadhi ya nyota tano hadi kazi ya kuendesha teksi! Haiaminiki kabisa!
Alitaka amweleze ukweli yule bibi kuwa hakupendezwa na kile kilichokuwa kikiendelea na ikibidi amtake atafute gari nyingine lakini alipokumbuka maneno ya yule bibi kuwa, “daktari wake alimtaka kufurahi zaidi ili aweze kuishi muda mrefu kidogo…” alishindwa kusema chochote.
Inaendelea...