Na Mwandishi Wetu - Majira
KIZUNGUMKUTI cha uasisi wa Chama Cha Jamii (CCJ), kimeendelea kuwazunguka makada waandamizi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na
vigogo walioko serikali, ambapo 'muasisi' mwingine amejitokeza akiweka hadharani madai yake juu ya waliohusika katika mpango huo.
Daniel Ole Porokwa, ambaye alijitambulisha kuwa ni kada wa CCM, akizungumza jana na waandishi wa habari Dar es Salaam, alikiri kuombwa kuwa mmoja mwanzilishi wa CCJ, akidai kuwa alishawishiwa kufanya hivyo baada ya kukutana mara kadhaa na Bw. Nape Nnauye, Dkt. Harrison Mwakyembe, Bw. Fred Mpendazoe na Bw. Samuel Sitta.
Alidai kuwa katika mikutano zaidi ya mitano aliyofanya akiwa na Bw. Nnauye na Dkt. Mwakyembe, wenzake hao walimweleza mpango wao wa kuanzisha chama cha siasa kuwa umelenga kuondokana na utawala wa kiimla wa CCM, kwa hoja kuwa chama hicho kilipofikia hivi sasa, hakiwezi tena kuaminiwa kukabidhiwa madaraka kuongoza dola.
Kwa madai ya Bw. Porokwa, viongozi hao aliokuwa akikutana nao katika mipango ya kuanzisha CCJ, walisema CCM haiaminiki tena machoni mwa Watanzania na kimepoteza mvuto mbele ya umma, kwa sababu kimeacha misingi yake, iliyowekwa na waasisi wake, akiwemo Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere.
"Nimeamua kufanya hivi (kutoa madai hayo) kwa misingi miwili mikuu. Kwanza, sisi kama viongozi ni sharti tuwaoneshe wananchi wetu na wanachama wa chama chetu njia sahihi tunayotakiwa kupita, tuamini katika hiyo njia tunayoelekea. Pili, mmoja wa msingi mkuu wa chama chetu ni kusema ukweli...uongo na fitina ni mwiko.
"Ni kweli niliwahi kuombwa kuwa mmoja wa wanachama waanzilishi wa CCJ. Nilikutana mara kadhaa na Mheshimiwa Nape Nnauye, Mheshimiwa Dkt. Harrison Mwakyembe na Mheshimiwa Fred Mpendazoe.
"Aidha nilikutana mara moja na Mheshimiwa Samwel Sitta baada ya Mheshimiwa Nape na Mwakyembe kunitajia kuwa ni miongoni mwa waanzilishi wa CCJ, nami kutaka uthibitisho wa hicho walichonieleza. Naye Sitta alieleza kuwa nilichoelezwa na Nape na Mwakyembe hakina chembe ya mashaka," alisema Bw. Porokwa.
Aliongeza sababu nyingine ya kuamua kusema hayo ni baada ya kuwasikia Bw. Nape na Dkt. Mwakyembe wakimkana Bw. Mpendazoe, ambaye ndiye aliyeibua tuhuma hizo za vigogo wa CCM na serikali waliohusika kuanzisha CCJ, akijenga hoja kuwa itakuwa ni vigumu kwa chama hicho na serikali yake kuwatumikia wananchi;
Kama viongozi wake wamefikia hatua ya kusigana kiitikadi na kutokuwa wamoja katika masuala ya msingi ya utawala na uongozi wa nchi, kwa maslahi ya Watanzania wote.
Akijibu shutuma hizo baada ya kupigiwa simu na Majira, Bw. Sitta ambaye alisema alikuwa safarini kutoka Arusha, alijibu;
"Hivi waandishi wa habari hili suala...people can change parties let alone kuanzisha vingine...kwa hiyo amenizungumzia mimi...let us forget it, sisi tunashughulikia mambo makubwa zaidi ya hayo," alisema kisha akakata simu.
Naye Dkt. Mwakyembe alipoulizwa bila kufafanua alisema 'Muulizeni huyo Porokwa kama aliacha kugombea ubunge kwa sababu ya pesa, leo kapewa shilingi ngapi ili azungumzie suala hilo.