Simulizi ya maisha: KABURI LA MSOMI

Simulizi ya maisha: KABURI LA MSOMI

TULIPOISHIA.
Mazungumzo hayo yalikuwa na maana kubwa sana kwake, aliiona nafasi kubwa ya kupata ukweli kuhusu mauaji ya hotelini kupitia wanawake wale walioonekana kumjua vizuri kijana aliyeuawa hotelini.
ENDELEA,,
Mpaka muda huo wazo la kwenda kukagua chumba cha mauaji ndani ya Kiwala Hoteli lilikuwa lishafutika kichwani mwake. Aliona kulikuwa na namna sahihi zaidi ya kumjua kijana aliyeuawa na hatimaye kuujua ukweli zaidi wa chanzo na sababu ya mauaji kupitia wale wanawake, kilichobakia ni kupanga namna gani afanye kupata neno la kila mmoja wao. Macho yake yalivutiwa zaidi na gari iliyokuwa mbele yake. "Gari la kijana aitwaye Morisi, kijana aliyekuja kuliegesha mahali hapa kisha akaingia ndani ya hoteli, gari lililomleta eneo la kifo chake, gari la kijana aliyeuawa." Mawazo hayo yalimfanya kushawishika kulipekua kwanza lile gari akiamini lazima kuna chochote atakipata ama kumhusu Morisi au muuaji. Ni baada ya kujilidhisha kuwa hakuna aliyemtilia shaka miongoni mwa watu waliokuwa eneo lile ndipo aliamua aende pale lilipokuwa lile gari akitembea kwa umakini sana na kwa namna isiyo rahisi kwa yeyote kumtilia shaka. Alifanikiwa kuifikia gari, akazungukia upande ambao asingeonekana moja kwa moja na msichana aliyekuwa dukani. Jaribio lake la kuufungua mlango wa gari liligonga mwamba, gari lilikuwa limefungwa kwa funguo hivyo pasipokuwa na funguo hizo asingeweza kulifungua kwa namna ya kawaida. Kulihitajika ama funguo au itumike namna nyingine nje ya utaratibu wa kawaida jambo ambalo hakuliona kuwa sahihi kwa mazingira yale maana isingekuwa rahisi kufanya hivyo bila kutengeneza kelele ambayo ingewajaza watu eneo lile. "Inamaana hawa wanawake watakua na funguo za gari! Itakuwa hivyo maana bila ya kuwa na funguo wasingeharakisha kumtafuta dereva kabla ya kutafuta namna ya kufungua gari."

Mawazo yalikuwa yakipishana kichwani mwake, akiwaza hile na lile katika namna ya kupata mwafaka wa kipi afanye kwa wakati ule. Kuwapata wanawake wale aliona kama bahati ya mtende. Kama Askari alijua namna gani ilivyo ngumu kufanya upelezi wa kesi ya kariba ile. Upelelezi ambao kwa kawaida huwachukua zaidi ya masaa ishirini na nne kumpata shahidi mwenye taarifa za mojakwamoja kuhusu tukio la mauaji ya kupanga. Ndiyo maana alitamani kufanya kila linalowezekana na kukusanya kila taarifa mhimu zinazohusiana na tukio lile. Gari iliyotumiwa mara ya mwisho na marehemu lilikuwa muhimu sana katika kuchunguza kifo chake ndiyo maana licha ya mazingira kutokuwa rafiki hakuwa tayari kumruhusu mtu yeyote kuingia ndani ya gari lile kabla yake. "Lazima niwe wa kwanza" Ndiyo kauli ya mwisho aliyoitoa kufuatia uamuzi alioufanya. Kwa sababu ya umhimu wa kulikagua lile gari, aliamua sasa kutumia mamlaka yake kama Askari, yaani sasa asingefanya kwa kujificha tena bali angefanya kwa wazi kama Askari polisi na kutumia mamlaka yake kulifungua lile gari na kuwahoji wale wanawake. Hakuwa na namna nyingine zaidi ya kufanya vile ingawaje tokea mwanzo halikuiona hilo kuwa sahihi.

Ni wakati akisimama ndipo alipomuona binti muuza duka akitembea kwa mwendo wa haraka kuja upande alipo. Salma aliyekuwa akiongea na mtu kupitia simu aliyoishikilia sikioni alitembea mpaka lilipokuwa gari la Morisi na kuanza kuifungua milango ya gari lile lakini haukufunguka. Alifanya hivo kwa awamu tatu mfululizo lakini bado hakufanikisha lengo lake.
"Wewe njoo kwanza tuone tunafanyaje, usije ukaleta dereva wakati huna ufunguo, mimi sitaki kuitwa mwizi" Ndiyo kauli ya mwisho aliyoisikia toka kwa binti aliyefika na kujaribu kuufungua mlango wa gari. Mda huo yeye alikuwa kajificha uvunguni mwa gari ndiyo maana hakuonekana. Alipata ahueni baada ya kugundua hata wanawake wale hawakuwa na funguo za gari. Akaamini sasa atapata mda zaidi wa kushughurika kwanza na gari lile kabla ya wanawake wale. Haukupita mda mrefu alionekana Jenita akitembea mwendo wa harakaharaka sana kwenda pale dukani. Alisubiri mpaka mteja alipoonda ndipo akaongea na Salma.
"Wewe kwahiyo tunafanyaje kama funguo hauna"
"Mimi sijui tunafanyaje"
"Sasa kwanini hukumwambia akuachie funguo na wewe"
"kwani mimi nilijua nini kitatokea." Jenita alikuwa na mshawasha wa ajabu kiasi cha kuuliza maswali yaliyomchanganya rafiki yake.
"Ndiyo maana nilikwambia tokea mwanzo tutoe taarifa polisi waje walichukue maana sisi wenyewe hatuwezi kulitoa hapa. Na huwa hairuhusiwi kulaza chombo cha usafiri mahali hapa bila taarifa rasmi kwa walinzi" Salma aliongea kauli ambayo ilipingwa vikali na mwenzake.
"Tulia wewe, lazima nitafute namna ya kulitoa hapa, siwezi kuacha hela eti kisa polisi, kwani unafikiri wao wakilichukua watalipeleka wapi zaidi ya kuliuza wagawane hela!" Alijibu Jenita mda huo akitoka pale dukani na kwenda kulitazama lile gari. Alisogea mpaka pale lilipokuwa gari na kujaribu kufungua milango kwa nguvu bila mafanikio, aliendelea kufanya hivo kwa mda mpaka pale aliposikia sauti ya nyuma yake.
"kwahiyo ndiyo unafanyaje hapa." Aliuliza Salma baada ya kufika mahali pale, "nawaza nitafute mtu wa kunisaidia kuuvunja huu mlango" alijibu kwa sauti kavu bila kugeuka akionekana kumaanisha kile alichokisema.Salma aliishia kumshangaa rafiki yake kwa mipango aliyonayo.
"Yaani unataka tuharibu gari la watu kwa sababu ya hela tu."
"Kwahiyo wewe unaona tufanyaje"
"Tutafute njia nzuri ya kuufungua mlango."
"Nani kakudanganya utajiri hupatikana kwa njia nzuri, wewe endelea kujifanya mama mchungaji, utaendelea kunyanyaswa na mabosi wako mpaka akili ikukae sawa. Yaani hela inakuja mpaka mkononi mwako unashindwa kijiongeza, utakuwa umelogwa wewe siyo bure." Anita aliongea kwa hasira sana kitendo kilichomfanya Salma kunyong'onyea kabisa. Akaamua kurudi kule dukani. Dangi aliweza kusikiliza yote yaliyozungumzwa, malumbano ya wanawake wale yalimshawishi kufanya kitu zaidi, aliiona bahati ikiwa upande wake hasa baada ya Salma kuondoka na kumwachia nafasi aliyoitamani sana. Alijinyanyua toka uvunguni mwa gari kwa kujiamini sana akiwa na uhakika na kile anachoenda kukifanya maana alishaijua akili ya Jenita. Asingemsumbua.

Salma alikuwa akiwaza sana juu ya kile alichoambiwa na Anita. Kwa namna fulani angekubaliana na maneno yake lakini bado hayakutosha kuirainisha roho yake kukubaliana na mpango ya kujimilikisha na kuuza gari lisilo la kwake. Ni kweli alikuwa na shida zake tena nyingi lakini kila akimkumbuka kijana aliyeuliwa hotelini, nafsi ilimsuta kufanya kile alichopaswa kufanya. Taswira ya Morisi ilimjiia kichwani, aliikumbuka sura ya kijana yule asiyekaukiwa utani na masihara kila afikapo pale dukani. Alikumbuka namna alivyozoeana naye kwa muda mfupi sana tokea alipopata kazi eneo hilo. Kila mala Morisi afikapo asingeacha kumtania.
"Wee Salma wewe" ilikuwa sauti ya Jenita ndiyo ilimkurupusha. Alishtuka sana na kuanza kuhema kwa nguvu mithili ya mtu aliyenusulika kugongwa na gari.
"Vipi wewe mbona huniachi nikatulia, unataka uniue kwa presha?" Alilalamika Salma akimwangalia rafiki yake aliyekuwa akijichekesha tu bila kujali namna alivyomuudhi mwenzake.
"Njoo" Aliongea Jenita akimvuta mkono.
"Nije wapi wewe, mbona unakuwa hivo" alilalamika Salma maana alivutwa kwa nguvu sana.
"Njoo uone mlango wa gari umefunguka" hapo Salma alipatwa na mshangao uliochanganyika na hamu ya kutaka kuona kilichokuwa kimetokea.
"Umewezaje kuufungua" aliuliza baada ya kuifikia gari.
"Wewe kaa kwa kutulia, mjini ujanja" Mda huo ndipo Salma aliweza kumuona mwanaume aliyekuwa ndani ya gari lile asimtambue.
"Vipi Jenita, gari inapelekwa wapi" aliuliza mwanaume yule swali liliomfanya Salma amwangalie Jenita asielewe nini kilikuwa kikiendelea.
"Mbona unanikodolea macho" Jenita alimwambia Salma na mda huo yule mwanaume aliliwasha gari na kupiga honi kwa mkupuo kama dereva aliyechelewa akiashiria uhitaji wa kuondoka.
"Unalipeleka wapi sasa" Aliuliza Salma ambaye hakuwa akielewa mpango wowote.
"Naona tulipeleke KIKOSO maana pale huwa kuna maegesho ya magari, tutaliacha pale kwa usiku wa leo harafu kesho tutaanza mchakato wa kilipiga bei" Salma hakuwa na pingamizi juu ya mpango wa rafiki yake hivyo maelekezo hayo ndiyo yalitolewa kwa mwanaume dereva.
"Nitaenda na huyu mwanaume mpaka KIKOSO nitaliacha pale kisha nitarudi, jiandae ili nikija tuondoke maana tayali utakuwa usiku sana." Aliongea Jenita akimuaga Salma kisha akaingia ndani ya gari na dereva akalitilia gia na kulitoa kwa mwendo wa taratibu.

Emmy alikuwa akikatisha mitaani taratibu taratibu akiwa ndani ya ndinga kali sana. Kila alikopita watu walibaki kulishangaa gari lake maana lilikuwa gari zuri sana tena gari jipya ndani ya mji ule maana hakukuwa na gari la aina hiyo kabla. Kitu hicho kilimpendeza sana Emmy, alifurahia sana vile mtaa ulikuwa ukimshangaa. "Safi sana Emiliana wangu, umekuwa mtoto mzuri sasa, kila aliyeko nje anatamani kukuona." aliongea akijipongeza. Aliyafurahia sana mandhari ya mji ule uliowashwa taa za kila aina kwa usiku ule na kuonekana kama moja ya miji ya kifahari sana. Mziki wa sauti ya juu ndio ulikuwa ukikiamlisha kichwa chake namna ya kuyumba na kujizungushazungusha yaani ilikuwa ni kelele tu ndani ya gari. Alionekana kufurahia kitu kile licha ya kuwa peke yake.

Tokea jioni mpaka usiku huu alikuwa amezurura kwa mda mrefu sasa, ni wakati ambapo aliwaza kutafuta sehemu yenye mgahawa ili apate chakula cha usiku. Maeneo kadhaa alikopita aliiona migahawa lakini hakujihangaisha nayo kwani hakuvutiwa na mandhari yake. Ijapokuwa alihisi njaa kali lakini asingeweza kuingia ndani ya mgahawa asioupenda. Mala zote akiona mgahawa na asiupende basi ungemsikia akisema; "Acha ujinga Emiliana, sahivi ni mda wako wa kufurahi, unatakiwa kufanya kiufurahishacho moyo wako." Maneno hayo ni kama yalikuwa yakimzidishia nguvu na ali ya kuendelea kutafuta sehemu nzuri zaidi aipendayo. Licha ya kutafuta sana hakufanikiwa kupata mgahawa uliomvutia, kila aliouona ulikuwa na kasoro. Huenda shida haikuwa kwa migahawa ile bali vigezo vyake vilikuwa vikubwa mno kiasi cha kutoendana na maendeleo ya mji ule. Hali hiyo ilimfanya kuchoka sana na kukata tamaa ya kufanikisha lengo lake, "Huna babati Emiliana, hutafanikiwa leo" ni maneno aliyoyatamka kuonesha kutowezekana kwa kusudi lake. Ile furaha aliyokuwanayo ilianza kumtoroka, uso wake haukuwa na tabasamu tena mpaka pale alipoliona jengo kubwa lililokuwa likiwaka taa za kungara usiku ule. Kilichomvutia zaidi ni baada ya kusoma maneno yaliyoandikwa kwenye bango kubwa lililobandikwa juu ya jengo lile agundua kumbe lilikuwa jengo la hoteli. "Siyo mbaya Emiliana, kama umekosa eneo zuri basi mahali hapa patakufaa sana, utapata kile ukipendacho." Aliongea maneno hayo kisha akakunja kona kuielekea hoteli ile lakini alisimama baada ya kubaini uwepo wa kizuizi cha polisi mahali pale.
ITAENDELEA.
 
TULIPOISHIA.
Kilichomvutia zaidi ni baada ya kusoma maneno yaliyoandikwa kwenye bango kubwa lililobandikwa juu ya jengo lile agundua kumbe lilikuwa jengo la hoteli. "Siyo mbaya Emiliana, kama umekosa eneo zuri basi mahali hapa patakufaa sana, utapata kile ukipendacho." Aliongea maneno hayo kisha akakunja kona kuielekea hoteli ile lakini alisimama baada ya kubaini uwepo wa kizuizi cha polisi mahali pale.

ENDELEA.
"Habari yako binti" alisalimiwa na Askari aliyesogea pale baada ya kuona ujio wa gari, Emmy alibaki kimya bila kuongea lolote. "Samahani sana binti, kwa sasa haturuhusu magari kuegesha mahali hapa." Kauli ile ilimuudhi sana Emmy aliyeamua kuwasha gari akatoweka mahali pale. "Huna babati Emiliana, hutafanikiwa leo" Maneno hayo aliyatamka kwa sauti ya kujirudia wakati akiliondoa gari lake mahali pale. Aliona ni kama siku hiyo alikuwa na mkosi na asingeweza kupata kile akipendacho kwa namna yoyote. Wakati huo hakutamani hata kuendelea kuendesha gari, kwa ufupi tukio lile lilimvuruga sana na kumuondolea utulivu wa akili, hata ile furaha aliyokuwa nayo mwanzo ilitoweka kabisa. Kadli sekunde zilivyosogea ndivyo hali yake ilikuwa ikibadilika kwa kasi kiasi cha kumfanya kushindwa kushikilia vema usukani wa gari lake. Sasa alikuwa akiendesha kwa kuweweseka, mikono ilikuwa ikimtetemeka sana hivyo alipokiona kituo cha mafuta mbele yake aliamua kuingia huko moja kwa moja kwa mwendo wa kasi sana kiasi cha kunusurika kupata ajali wakati akiikatisha kona ya kuingia ndani ya eneo lile.

Ulikuwa ni wakati ambapo Dangi alikuwa akitoka ndani ya eneo la kituo cha mafuta ndipo alipoweza kushuhudia ujio wa gari lililokuwa likipepesuka huku na huko likionekana kupoteza uelekeo wake. Alijitahidi sana kulikwepa ingawaje lilimkwaruza kidogo lakini hakukuwa na madhara zaidi hivyo hakujihangaisha nalo. Aliamua kuendelea na harakati zake maana bado alikuwa na kazi kubwa ya kufanya usiku huo.

Japo hakuwa katika hali ya utimamu wake lakini alijitahidi sana mpaka akafanikiwa kusimama sentimita chache mbele ya ukuta. Ilibakia kidogo tu augonge ukuta ule, "Huna babati Emiliana, hutafanikiwa leo," aliongea maneno hayo akiwa anatetemeka sana, jasho likiwa linamtoka mithili ya maji. Mda huo alikuwa kayafumba macho yake kwa nguvu akiwa kayaziba masikio yake kwa mikono na miguu kaikusanya pamoja mithili ya mtoto yatima aliyetelekezwa katikati ya balabala.

Salma ndiye mtu pekee aliyelishuhudia tukio lile kwa uzuri kabisa. Ilikuwa wakati amesimama nje ya duka lake akilitazama gari alilopanda rafiki yake likiondoka taratibu ndipo aliona gari jingine likingia kwa kasi sana uso kwa uso na gari alilopanda rafiki yake. Alishtuka sana akapiga yowe la hofu huku akifumba macho yake akiamini lazima ajari mbaya inatokea. "Hakuna kilichotokea" aliongea baada ya kayafumbua macho yake, hapo alilishuhudia gari lililosimama sentimita chache mbele ya ukuta wa duka lake, alipogeuka upande wa balabalani hakuiona lile gari alilopanda rafiki yake hivyo akaamini wameondoka salama. Alilisogea gari lilokuwa mbele ya duka lake akijaribu kuchungulia ndani bila mafanikio maana vioo vya gari ile havikuwa angavu kiasi cha kutoruhusu aliyepo nje kuona kilichopo ndani. Alitulia kidogo akavuta hewa nyingi ndani ya mapafu yake kisha akaanza kugonga kioo cha gari ile akihitaji kumjulia hali mtu aliyekuwa ndani. Alifanya hivo kwa muda bila mafanikio mwisho akaamua aachane nacho lakini wakati akitaka kuondoka alisikia sauti ya mlango wa gari ukifunguka, toka ndani alimuona binti aliyekuwa akihema kwa nguvu na kutetemeka sana.
"Pole sana dada, utakuwa umeumia sana!" Aliongea Salma kwa sauti iliyoonesha kujari sana akimtazama Emmy ambaye hakujihangaisha hata kumtazama mtu aliyekuwa akimuongelesha. Salma aliiewa hali ile hivyo akaingia dukani haraka akatoka na chupa kubwa ya maji ya kumywa akampatia Emmy ambaye mwanzoni alionesha kukataa lakini baadae aliyapokea maji yale na kayanywa.
"Pole sana" aliongea Salma baada ya kuona angalau mtu wake katulia lakini bado Emmy hakujibu chochote zaidi ya kumuangalia tu binti huyo aliyeonekana kumjari licha ya kutokumjua.
"Huna babati Emiliana, hutofanikiwa leo" aliongea tena maneno hayo kisha akashuka toka ndani ya gari lake. Alisimama wima kwa mda kidogo kabla ya kuyumbayumba, na kutaka kuanguka lakini Salma alimdaka na kumsaidia kukaa kwenye kiti cha plastiki kilichokua pale nje. "Unatakiwa utulie kwanza kizunguzungu kipoe" Bado Emmy aikuwa kimya, licha ya kusikia hayo hakujibu chochote.
Salma alibaki kumuangalia msichana mwenzake bila kumuelewa, aliwaza labda atakuwa ni bubu au kiziwi japo wazo hilo hakuliona kuwa sahihi. Angalau sasa Emmy alikuwa karudi kwenye utimamu wake baada ya kunywa maji. Alibaki kuiangalia chupa ya maji aliyoishikilia mkononi. Tumbo lilikuwa likiuma kwa njaa maana alikuwa hajapata chakula chochote cha maana toka asubuhi mpaka mda huu, hapo wazo la kutafuta chakula likamjia tena. Alinyanyuka baada ya kuona vitu alivyovipenda ndani ya duka lile, bila kuuliza akaanza kuchukua chochote alichoona kinamfaa kwa mlo wake na kuanza kutafuna hovyo bila kujali. Mwanzoni Salma hakuona hilo kuwa tatizo lakini baada ya kuona binti yule akichukua vitu vingi zaidi na kuvurugavuruga vitu ndipo aliamua kwenda kumzuia maana hakuliona lile kuwa jambo la kawaida tena kwani bidhaa zake zilikuwa zikivurugwa na kudondoshwa bila utaratibu.
"Wewe acha kubaribu hivo, usichukue vingi sana" Aliongea akijaribu kumzuia Emmy ambaye ni kama alikuwa amewehuka, alikuwa akitafuna hiki na kuacha, hiki anakibeba na kingine anatupa chini yaani sekunde kadhaa alizokaa mle ndani tayali ameshaharibu na kuvuruga mpangillio wa duka lile.

Alivyoona upinzani wa mwenyeji wake umezidi aliachana na vyote aliyokuwanavyo akatoka na kwenda ndani ya gari lake. Alirudi na pochi yake ya mkononi akaitupa juu ya meza kisha akaendelea kuchukua vitu. Salma alipotaka kumzuia tena hapo ndipo Emmy alinyoosha mkono kumuonyesha ile pochi aliyoitupia juu ya meza. Salma alitulia akaichukua ile pochi. Aliifungua na kukuta baadhi ya vitu vya kike, pamoja na pesa nyingi za kigeni zilizopangwa vizuri.
Wakati huo kuna gari iliingia kwa kasi sana maeneo yale. Walishuka wanaume watatu na kuingia dukani. Salma alivyowaona tu akaificha ile pochi, akihofia labda wanaweza kuwa watu wabaya. "Karibuni wateja." Hawakuwa na habari naye, moja kwa moja walimfata Emmy aliyekuwa bize kukusanya kila alichokipenda. Hakuelewa nini walimfanya mpaka akalegea vile ndani ya mda mfupi akionekana kutojiweza kabisa kiasi cha kushikiliwa na wanaume wawili waliombeba na kutoka naye wakampakiza ndani ya gari walilokujanalo wakatoweka eneo lile. Kilichotokea kilimchanganya asikielewe. Yule mwanaume wa tatu alibaki akikusanya vitu vyote vilivyokuwa vimedondoshwa na Emmy, kuanza na vile vyakula au hata visivyo vyakula vilivyodondoka ama kwa bahati mbaya au kwa makusudi. Alichukua mpaka vile vilivyokuwa eneo lake bila kudondoka ilimradi tu aliviona kutokuwa katika mpangilio mzuri kumaanisha kwamba vitakuwa viliguswa na Emmy wakati akichagua chagua vitu vya kubeba. Alivipakia ndani ya mfuko mkubwa ulioonekana sasa kama furushi zito maana vitu vile vilikuwa ni vingi sana. Alipomaliza alilibeba furushi lile akamfata Salma aliyekuwa akimshangaa tu asielewe kama ndiyo vinaibiwa au vinanunuliwa.
"Shika hii itakusaidia kufidia hasara" Aliongea akimpatia bunda la noti nyingi kisha akatoka na mzigo wake na kwenda kuupakiza ndani ya gari alilokujanalo Emmy kisha akaliondoa mahali pale akatoweka ndani ya eneo lile.

Salma alibaki kapigwa na butwaa asielewe namna mambo yalivyotokea kuanzia ujio wa gari la binti asiyeongea mpaka wale waliokuja kumchukua binti yule, aliona ni kama sinema vile, hata hivyo hakujali sana kuhusu namna yule binti alikuwa amelivuruga duka lake, maadamu amelipwa hakuona shida yoyote. Harakaharaka akaanza kulipanga tena duka lake katika mpangilio alioupenda kisha akalejea pale mezani na kuzihesabu zile pesa alizopewa kama fidia ya hasara na usumbufu uliojitokeza. Zilikuwa noti nyingi mpya zilizoonekana kana kwamba ndiyo zimechomolewa benki mda ule, na kilikuwa kiasi kikubwa kama malatano ya hasara iliyotokea, japo mwenyewe aliona hakukuwa na hasara yoyote zaidi ya gharama ya bidhaa zilizochukuliwa. Alishangaa sana kwa namna gani ameweza kupewa pesa zote hizo haliyakuwa bidhaa zilizochukuliwa zilikuwa za bei ya kawaida tu yaani maandazi na baadhi ya vitafunwa na vinywaji tu ndiyo vimelipiwa pesa nyingi kiasi kile. Kumbukumbu ya kauli aliyoambiwa na Jenita ilimjia hapo akakili bahati aliyokuwa nayo kwa siku ile kwamba Mungu kaamua kumpatia kwa namna ile. Baada ya kufanya mahesabu ya mauzo ya siku ile, aliitenga hesabu halali ya mwenye duka na kiasi alichobaki nacho kilikuwa kikubwa sana. Siku hiyo alijiona mwenye bahati ya kupata hela japo hakufurahishwa na kitu kile maana pesa zenyewe hakuwa amezifanyia kazi, hisia hizo zilimfanya kujipa onyo maana akithubutu kutamka hilo mbele ya rafiki yake wanaweza wakagombana kabisa maana rafiki yake hakuwa kama yeye. Salma alipenda kuwe na uhalali wa kila anachokifanya kujiingizia kipato lakini Jenita hakujali hilo yeye alichozingatia ni mapato tu akiitumia kila fursa inayojitokeza mbele yake kujipatia faida. "Ngoja aje nimsikie atasemaje, huenda leo akanipongeza kwa mala ya kwanza." aliwaza Salma akionekana kwa kiasi fulani kufurahia kile alichokipata. Mpaka hapo aliona siku imekwisha, alitamani kufunga duka ili aondoke lakini kwakuwa ni kazi ya mtu mwingine asingeweza kufanya hivyo maana mda wa kufunga haukuwa umefika. Alitakiwa amsubiri bosi wake afike, amkabidhi mauzo ya siku ile ndipo aondoke. Hata hivyo uwepo wa Jenita ndio ulimsaidia kwani mala zote Jenita humuombea ruhusa kwa bosi ili waondoke wote maana walikuwa wanaishi sehemu moja. Yeye hakuwa na ukaribu au mazoea na bosi wake hivyo alimtegemea rafiki yake kuongea na bosi kwa niaba yake.

Kama kuna kitu wakazi wa mji ule walijivunia sana basi ni kuwa na viongozi wenye maono ya namna gani mji ule uendelezwe kwani ndani ya miaka miwili tu ya uongozi mpya tayali kumefanyika mageuzi ya kutosha katika sekta mbalimbali za utawala bila kusahau maboresho na ujenzi wa miundombinu bora ya kutosha. Mwanzoni lilianza kama wazo tu lililotolewa na moja ya wagombea wakati akizinadi sela zake mbele ya umati mkubwa uliokusanyika kumsikiliza kipindi cha kampeni za uchaguzi. Sasahivi siyo wazo tena bali ni uhalisia unaovutia kwa kila atazamaye, "KIKOSO ZONE" lilikuwa jina maarufu miongoni mwa wakazi wa mji ule. Kutokana na ukuaji na maendeleo ya kasi kuliibuka wimbi kubwa la utitiri wa magari yaliyoegeshwa hovyo mitaani kiasi cha kuchafua taswira ya mji ule. Hali hiyo ilitokana na uhaba wa maeneo ya kuegesha vyombo vya moto kwani hata yale yaliyokuwepo mwanzo hayakutosha tena na kuna baadhi yalibadilishiwa matumizi. Hiyo ikawa changamoto kubwa iliyolalamikiwa na kila mtu kwani maegesho kidogo yaliyokuwepo yaligombaniwa, wenye nguvu zaidi ndio walijimilikisha. Serikali iliona umuhimu wa kujenga maeneo maalumu kwa ajili ya maegesho ya magari na vyombo vingine vya usafiri sawasawa na uhitaji uliokuwepo kwa wakati ule. Kulijengwa maegesho maalumu ndani na nje ya mji lakini KIKOSO ZONE ilipita mengine yote kutokana na sifa zake. Kwanza ilijengwa katikati ya mji eneo lililofikika kwa haraka na kila mtu, ikiwa na mazingira safi na kutoa huduma kwa usalama wa uhakika. Lilikuwa ni eneo zuri sana, kuanzia muundo wa ujenzi wake na mandhari yake hasa kwa usiku ule kulikuwa na mwanga wa kutosha ulipafanya kuonekana kama mchana. Tokea upande wa mashariki inaonekana gari moja ikija kwa mwendo wa kasi na kuingia ndani ya maegesho ya KIKOSO, anashuka Jenita akiwa na dereva wake ambaye bila shaka alikuwa ni Dangi mwenyewe. Waliliacha gari mahali pale kisha wao wakatafuta usafiri mwingine wa kuwarudisha walikotoka.
"Kwa hiyo kesho ndipo mumepanga kuliuza"
"Nimeshakwambia uache kunisumbua, gari haliuzwi hili ni mali yangu."
"Ni mali yako vipi wakati hukuwa hata na funguo zake na wala hujui kuliendesha?"
"Bwana ee!! Usinichanganye! Umeshafanya kazi yako subiri tufike nikulipe hela ushike hamsini zako, usitake kujua mambo yasiyokuhusu" Yalikuwa ni majibizano makali baina ya Jenita na Dangi. Licha ya Jenita kukubali msaada aliopewa na mwanaume yule lakini hakuwa tayali kumweleza kila kitu. Dangi alitamani kuweka ukaribu na msichana yule ili iwe rahisi kwake kupata taarifa azitakazo lakini hilo halikuwa jepesi hata kidogo maana Jenita hakuwa mtu wa kumwamini yeyote katika mipango yake.
Huenda fikra zake zilimpotosha tokea mwanzoni maana alivyomzania sivyo alivyokuwa, Jenita hakuwa mwepesi kuingilika hata kidogo. Kitu pekee alichomsikiliza na kukubali kuelekezwa ni juu ya kufungua milango ya gari na kulitoa kule sheli mpaka kikosa, tofauti na hapo hakuwa tayali kuongea chochote mbele ya mwanaume asiyemjua. Ukimya ulitawala mpaka pale walipofika ndani ya kituo cha mafuta. Hapo walishuka na Jenita alikuwa akitembea kuwahi kule dukani amchukulie pesa dereva wake.
"Sikiliza Jenita, najua hutaki nijue chochote kuhusu mpango ulionao wa kuliuza gari, hata mimi sitaki pia kujua kuhusu hilo lakin,,,, "
"Lakini nini, unataka kujua nini na kama nani hasa mpaka utake kujua!!" Jenita hakuwa mpole, alikabia juu kila mala dereva wake alipojaribu kuuliza chochote. Wakati huu walikuwa wamesimama wakitazamana mithili ya jogoo wanavyopandishiana manyoya wakijiandaa kuraruana, ukiwatazama wawili hawa ungezani hawakuwa ndani ya gari moja wakati wa kuondoka.
"Sikiliza wewe mwanaume, nikishakulipa hela yako sitaki tujuane tena, pita kushoto ukiniona kulia yaani sitaki tufatiliane la sivyo nitakuonesha cha mtema kuni." Kauli hii ilimshangaza sana Dangi, hakuamini mda huo alikuwa akipigwa biti na msichana aliyejiaminisha kummudu hapo kabla. "Ama kweli usihukumu kitabu kwa kuangalia kava yake." Alitafakari sana kujaribu kuelewa sababu ilikuwa ni nini hasa mpaka msichana yule kubadirika vile kiasi cha kuukataa ukweli ambao yeye mwenyewe aliusema mbele ya rafiki yake. "Labda amenichukulia kama wahuni wengine wa mtaani ambao hawaachi kukufata wakishaijua siri yako ili uwape chochote wao waendelee kukutunzia siri" Aliona hilo litakuwa sahihi kwamba kwa kuwa yeye ameijua siri ya Jenita ndiyo sababu anaonywa na kukalipiwa ukali namna ile. "Jenita ananiogopa" Baada ya kugundua hilo alijikuta akivutiwa na akiri ya msichana yule hasa ile namna alikuwa makini kwa kila hatua, "Hongera sana Jenita na karibu kwenye ulimwengu wa wenye akili." aliongea kauli hiyo akiamini angalau amemjua Jenita ni nani japo hakujihakikishia hilo kama alivyojidanganya mwanzo. Cha mhimu alichojiaminisha ni kuwa Jenita hakuwa msichana wa kawaida tu hivyo kumkabiri na kumshinda alipaswa kufanya zaidi ya kawaida. Aliwaza hayo akitabasamu pekeyake pale nje, akisubiri kuletewa hela kama malipo ya kazi aliyoifanya. Jenita alirudi akiwa kashikilia noti kadhaa mfukoni na kumkabidhi dereva wake.
"Mpaka hapa sina deni na wewe, zingatia nilichokueleza. Ninakutakia maisha mema" Jenita aliongea kisha akaanza kurudi kule dukani.
"Maisha mema kwako pia, na Uwe na bahati njema kesho utakapokuwa ukiliunauza gari la rafiki yangu" Kauli hiyo ilimshitua sana Jenita, alilazimika kugeuka kama mtu ambaye hajasikia vizuri kilichozungumzwa.
ITAENDELEA.
 
TULIPOISHIA
Ninakutakia maisha mema" Jenita aliongea kisha akaanza kurudi kule dukani.
"Maisha mema kwako pia, na Uwe na bahati njema kesho utakapokuwa ukiliunauza gari la rafiki yangu" Kauli hiyo ilimshitua sana Jenita, alilazimika kugeuka kama mtu ambaye hajasikia vizuri kilichozungumzwa.
ENDELEA,,,,,,,,

"Unasemaje wewe, nani rafiki yako" Aliongea kwa sauti ileile ya kukaripia lakini hakupata jibu lolote toka kwa dereva wake ambaye mda huo alikuwa bize kuhesabu pesa aliyolipwa.
"Naona bado hujaridhika! hujakoma kunichokonoa eti, bado unanitafuta kunijua mimi ni nani haya endelea, nitakuonesha mimi ni nani" Maneno yake ni kama yalipokelewa kwa namna ambayo hakuitarajia, alimuona dereva akitabasamu tu wakati akiitunza pesa yake. Jenita alijua nini anafanya kwa kuongea vile, alihitaji kumtia jambajamba yule mwanaume ili asimfatilie na kumvurugia mpango wake ndiyo maana alikuwa akitumia kauli ngumu sana kumuogopesha. Kitendo cha dereva kutabasamu tu, tena baada ya yeye kuongea vile haikuwa ishara nzuri kwake. Uoga ulianza kumuingia.
"Sina chochote nachotaka kujua toka kwako zaidi tu nataka kujua kuhusu rafiki yangu Morisi" Hapo Jenita alishtuka kiasi cha kutaka kukimbia, lakini alijikaza asionekane mdhaifu mbele ya mwanaume yule. Hata hivyo Dangi alibaini mabadiriko hayo kwenye uso wa Jenita japo mwenyewe alijitahidi kuficha hilo.
"Kwahiyo unataka kusemaje, Morisi ndiye kakutuma!"
"Sikiliza Jenita mimi sina shida na gari wala sitakuzuia kuliuza kama ulivyopanga lakini kuna vitu natamani kujua kuhusu rafiki yangu. Morisi ni rafiki yangu mkubwa tena wa mda mrefu ndiyo maana uliona sikupata tabu kulifungua gari lake licha ya kwamba sikuwa na ufunguo ni kwasababu ninalijua sana na nimekuwa nikiliendesha kwa mda mrefu. Mala ya mwisho aliniaga anakuja kwa demu wake eneo hili lakini taarifa za mtandaoni zinamuonesha akiwa ameuawa ndiyo maana nikalazimika kuja hapa kujua nini kimetokea. Sina maana mbaya lakini kama familia inahitaji kujua nini hasa kimetokea na hakuna mwingine wa kuwaambia hilo zaidi yangu maana mimi ndiye nilikuwa mtu wake wa karibu na familia yake inalijua hilo."
Maelezo hayo ni kama vile yalimvua nguo Jenita, alijihisi yupo uchi mbele ya mwanaume yule mpaka akaanza kulishikilia vizuri dera alilolivaa. Ule uoga uliochanganyikana na hofu sasa uliweza kuonekana vizuri usoni mwake hakuwa na nguvu za kuzuia tena hali hiyo. Hakuelewa afanye nini ndani ya sekunde zile alijiona kuwa katika wakati mgumu sana maishani mwake mithili ya mwizi aliyejificha kwenye shamba la karanga alikuwa akitapatapa asijue nini aongee kujitetea, aliishia kuchezea vidole vya mikono yake, akiviminyaminya. Mpaka hapo Dangi alikuwa akishangilia ushindi wa kimyakimya, alitamani wangekuwepo mashabiki awanyanyue kushangilia naye ushindi ule. "Sawa" ndilo neno pekee alilojibu Jenita kisha akamkaribisha dereva kwenye kiti kilichokuwa pale nje ya duka. Salma alifatilia kila kilichoendelea lakini hakuelewa nini hasa kilikuwa kikizungumzwa kwasababu hakuwa akisikia maneno yao yote kwa usahihi. Ghafla umeme ulikata, kukawa na giza eneo lile kabla ya mwanga kurudi tena baada ya jenereta za eneo lile kujiwasha. Dangi alikaa pale nje akimsubiri Jenita aliyeingia ndani kumuita Salma maana ndiye alijua zaidi kuhusu Morisi. "Safi sana Jenita, sasa utanisaidia mwenyewe kupata kila taarifa muhimu nitakayoihitaji toka kwa rafiki yako, huu ndiyo ulimwengu wa wenye akili na sheria yake ni moja tu, kula au uliwe" alitulia na kijiweka sawa baada ya kuhisi ujio wa watu wake.

Muumba angekuwa anafanya sawa na akili za mwanadamu huenda angemshawishi auondoe usiku ibakie asubuhi, mchana na jioni tu ili asipate adha kama ilivyokuwa sasa. Hakuwahi na mpaka sasa hakuwa anaupenda usiku hata kidogo maana ulibeba kumbukumbu nzito zisizofutika ndani ya maisha yake, kumbukumbu zilizomfanya kuuchukia usiku kulichukia sana giza akiamini ndicho chanzo cha yote yaliyotokea. Mala zote mwenyewe husema "haungekuwa usiku hayangetokea yote, ni usiku ndiyo sababu na giza ndicho chanzo." Maneno yake yalikuwa sahihi kabisa maana giza ndicho kiini cha usiku, hakuna usiku bila giza ndiyo maana giza lichelewapo watu husema usiku umekawia kuingia. Ili kuuepuka usiku ilimlazimu kuhakikisha analizuia giza kwa namna yoyote ile ili mladi wakati wote uwepo mwanga wa kutosha sehemu alipo na ndiyo maana licha ya kuwa ilikuwa nyumba yake ya kuishi lakini alihakikisha kunakuwapo mifumo ya umeme ya kutosha hivyo usiku ule umeme ulipokata mjini yeye hakupatwa na shida yoyote kwani sekunde ileile iliwaka jenereta na kuzalisha umeme kama kawaida. "Haya ndiyo mambo huwa sipendagi, yaani watu wanakatakata umeme namna wanavyojisikia" aliongea kwa hasira sana akionekana kuchukizwa na kitu kile. Wakati huo alikuwa ameketi juu ya kiti cha mbao akiwa kaipakata kompyuta yake ndogo akionekana ama kuandaa au kufuatilia kitu kilichouvuta umakini wake kwa kiasi kikubwa. Kuna video alikuwa akiiangalia kwa wakati huo akionekana kufurahia sana kile alichokuwa akikiona. "Hahahahaha!!!!! Hapa tumekukomesha mjinga wewe, sasa utajua nini maana ya maisha, nitahakikisha wa kwako wote wanauchukia usiku kama ilivyo kwangu. Giza ndicho kiini cha yote na lazima walijue hilo maana nitawakusanya niwafundishe mimi mwenyewe." Aliongea kwa sauti ya juu akichekelea kwa nguvu sana japo sura yake haikuakisi furaha aliyokuwa nayo. Ni kama aliigiza furaha mdomoni hali ya kuwa moyoni kulikuwa na huzuni iliyobeba uchungu mzito uliojaa kisasi ndani yake. Baada ya kumaliza kuiangalia video ile aliizima kompyuta yake akaiweka juu ya meza ya mbao iliyokuwa mbele yake kisha akanyanyuka na kuelekea ndani ya chumba chake cha kulala. Kilikuwa chumba kikubwa kipana kilichokuwa na taa nyingi zilizotoa mwanga wa kutosha, ukutani kulibandikwa picha kubwa iliyokuwa na taswira za watu watano. Wa kwanza alikuwa mwanaume aliyevalia suti safi ya kijivu, wa pili mwanamke mmoja aliyempakata mtoto mchanga akimwangalia kwa tabasamu, taswira ya tatu na ya nne zilikuwa za watoto mapacha waliokuwa wameshikana mikono wakiwa wamevalia sare za shule. Picha ilikuwa moja lakina taswira zilikuwa tofauti tena zilionekana kuwepo mazingira tofauti tofauti kumaanisha kwamba kila mmoja alipigwa picha eneo lake lakini ziliunganishwa namna ile na mtu aliyedhamiria kufanya vile. Taswira ya mwanaume ilijitenga peke yake, taswira za mama na mtoto ziliunganishwa na kuwekewa alama ya X iliyokolezwa kwa rangi nyekundu, taswira za watoto mapacha hazikua pamoja lakini mikono yao ilirefushwa na kushikana. Yule mwanamke alisimama akaitazama picha ile kwa kitambo kidogo kisha akachukua kalamu na kwenda kuchora alama ya X nyeusi juu ya taswira ya mwanaume. "Mda umeniishia Isaya wangu, sitaweza tena kuvumilia kukuona ukiteseka, nenda kwa amani, uliyoyaanzisha nitayakamilisha yote, nitawatafuta uliokuwa ukiwatafuta na nitakuletea wote wanaokuhusu. Ninakupenda sana" Alitamka maneno hayo kwa sauti iliyoakisi hisia nzito alizokuwa nazo juu ya mwanaume yale mpaka machozi yalimtoka kuonesha ni hisia gani alikuwa nazo. Baada ya kuachana na picha ile aliichukua simu yake akabonyeza namba fulani kisha akaipiga mahali. Alisubili mpaka pale ilipopokelewa na mtu wa upande wa pili ndipo akaongea "Niandalieni kaburi zuri, kesho kutwa nitamzika wakili msomi." Kisha akaikata simu ile na kwenda kujipumzisha kitandani.

Mchana wa siku ile alikuwa ametekeleza majukumu yake kwa wastani mzuri sana, hakuna alichobakiza katika yote aliyopaswa kuyafanya kwa siku ile. Aliikamilisha ratiba kwa ufanisi mkubwa sana jambo lililowafurahisha wakubwa wake kazini wakaahidi kumpa ulaji zaidi ya alivyokuwa akipata mwanzo. Hilo ndilo lilikuwa lengo lake tokea mwanzoni alipojiunga na jeshi la polisi, mala zote angefanya kazi kwa weledi na ufanisi wa hali ya juu akiamini ipo siku jitihada zake zitamlipa, na atafanikiwa zaidi. Tokea utotoni alipenda sana kuwa mwanajeshi japo hilo lilishindikana akaishia kuwa Askari polisi, hakuona hilo kuwa baya sana maana alijua siku zote simba akikosa nyama huwa mstaarabu na hujishibisha kwa majani hivyo alikubali kuwa Askari lakini lego lake halikuwa kubaki kuwa Askari tu bali kuwa Askari mkubwa mwenye cheo cha juu sababu aliamini Askari mwenye cheo kikubwa ni sawa mwanajeshi. Jitihada zake zilishamzalia matunda hapo kabla mpaka kufika nafasi aliyokuwa nayo sasa kama mkuu wa kitengo cha upelelezi, bado alifanya kazi kwa bidii akiamini atapita hapo alipo na kwenda juu zaidi. Ndoto yake ilikaribia kutimia siku ya leo baada ya kufanya kazi kubwa iliyosifiwa na wakubwa wakamuahidi kumpa heshima zaidi. Mpaka kufika mida ya jioni tayali alikuwa amekamilisha kila kitu,roho yake ililidhika na kazi nzuri aliyokuwa ameifanya ndipo akaamua kurudi nyumbani kwake mapema ili akajipumzishe, alikuwa amechoka sana. Ilikuwa mda wa saa nne kamili za usiku ndipo alishtuka toka usingizini baada ya kusikia mlio wa simu. Harakaharaka alinyanyuka na kwenda mezani kulipokuwa na simu zaidi ya ishirini akaichukua ile iliyokuwa ikitoa mlio. Alishtuka sana baada ya kumbukumbu sahihi za simu ile kumjia, huenda mwanzoni hakuweza kuung'amua haraka upekee wa mlio ule kwa sababu ya wenge la usingizi alilokuwa nalo lakini sasa tayali alisharudi kwenye utimamu wake. Aliiangalia mala mbilimbili simu ile asiamini kama kweli ndiyo ilikuwa ikiita usiku ule. Moyo ulidunda kwa kasi sana, kijasho chepesi kikaanza kumtoka bila kupenda, japo mikono haikutetemeka lakini aliishikilia kwa nguvu sana simu ile akayafumba macho yake kwa nguvu na kukinyanyua kichwa kuelekea darini akapiga kelele kwa sauti ya juu sana"Haaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaa!!!!!! Kisha akairusha ukutani simu ile ikapasuka vipande vipande kutokana na nguvu kubwa aliyoitumia.

Usingizi ulimpaa, ule uchovu aliokuwanao mwanzo hakuuhisi tena, damu ilichangamka sana ikawa inazunguka kwa kasi ndani ya mwili wake kitendo kilichopelekea mishipa yake hasa ile ya mikononi kututumuka sana ungezani ni mmoja wa mabondia wa masumbwi. Asingeweza kupata usingizi tena hata angejitahidi vipi kuutafuta hivyo aliamua kwenda nje akajaribu kuituliza akili yake. Hakuishia kukaa tu pale nje bali aliondoka kabisa ndani ya eneo lile kwa kutumia usafiri wa pikipiki. Baada ya nusu saa aliegesha pikipiki lake nje ya baa moja, akashuka na kuingia ndani. Wahudumu wa mahali pale walimjua vizuri hivyo walivyomuona akiingia mmoja alimfata na kumuuongoza mpaka chumba cha ndani kabisa ya jengo lile.
"Karibu sana Kaleli, sijui utahitaji nini nikuletee."
"Sihitaji chochote"
"Sawa lakini sijui nikisaidiaje sasa maana nakuona haupo sawa"
"Nimeijia simu yangu, niliisahau hapa mchana" Mhudumu yule ni kama hakumuelewa vizuri mteja wake maana simu anayoizungumzia yeye hakuwa ameiona na kwa shida kama hiyo basi hakupaswa kuingia mpaka chumba cha ndani kwani kule huwa wanafika watu wenye shida maalumu.
"Mbona unanishangaa"
"Hapana sikushangai wala ila sijakuelewa tu maana shida yako sio ya kukufikisha huku."
"Anhaaa!!!, wewe ni mgeni eneo hili"
"Hapana"
"Haina shida, wewe ondoka nitajihudumia mwenyewe" Kaleli hakutaka kuendelea kujibishana na mhudumu yule, kwanza alishatambua siyo mwenyeji wa baa ile pengine hata kazi yake hakuijua vizuri. Baada ya mhudumu kuondoka aliifata simu iliyokuwa juu ya meza na kuipiga sehemu akasubiri mpaka ilipopokelewa ndipo akaongea.
"Nimefika eneo lako la kazi sijakukuta, nimepokelewa na binti mhudumu; mgeni asiyeelewa chochote hivyo ameshindwa kunihudumia, sijapata huduma yoyote mpaka sasa, nimehuzunika sana. Umeniangusha sana mda huu. Kwa usiku wa leo nitavumilia huzuni hii lakini usiku wa kesho nahitaji huzuni hii ihamie kwake, umuhuzunishe kabisa.
"Sawa"
Baada ya kumaliza kufanya maongezi hayo alinyanyuka na kutoka nje akapanda pikipiki yake na kutoweka eneo lile. Binti mhudumu alibaki bila amani kabisa, aliogopeshwa na maneno aliyoyasikia "yaani anatoa taarifa kwa bosi ili na mimi nihuzunishwe kama alivyohuzunika yeye siku ya leo." Aliogopa sana akiwaza labda angefukuzwa kazini kesho yake maana aliisikia sauti ya bosi wake akiitikia kwa kukubaliana kile alichoelezwa na yule mwanaume. "Hapana, siwezi kukubali nikafukuzwa kidhembe wakati sijamkosea chochote. Kesho lazima niongee na bosi nimweleze kila kilichotokea asije akaamua tu bila kujua ukweli."

Osama alikuwa macho mpaka mda huu, hakuwa amepata usingizi kabisa baada ya kupokea ujumbe uliomwachia hisia mbili kwa wakati mmoja. Kwanza hisia ya furaha akiamini kwamba unaenda kuwa mwisho wa mchezo uliodumu kwa mda mrefu sasa, pili hisia ya huzuni akijua kesho na kesho kutwa zitakuwa siku ngumu sana kwake maana alitakiwa kuhakikisha ufanisi katika kila jambo litakalofanyika ndani ya siku hizo iwe lile atakalolifanya mwenyewe au litakalofanywa na vijana wake. Aliiwasha simu yake na kurudia kuusoma tena ujumbe aliotumiwa, "Hatima ya Msomi ipo kichwani mwako, kesho majira ya saa moja usiku, KIWILA HOTEL, Upper Floor. Room no, 23." Aliuelewa sana ujumbe huu kwani ni kariba ya jumbe nyingi anazotumiwa mala kwa mala na washirika wake. Kilichomkosesha usingizi siyo ugumu wa kazi iliyopo mbele yake bali mawazo kuhusu ujumbe aliotumiwa maana kuna namna hakuuelewa au alielewa lakini hakukubaliana nao. Jambo alilowaza ni ikiwa hatima ya msomi iko kichwani mwake basi siyo yeye atakayetakiwa kumaliza bali kutakuwa na mtu mwingine atakayeifanya hiyo kazi. "Mtu huyo ni nani na kwa nini siyo mimi" Ndilo swali alikuwa akijiuliza asipate majibu, aliamini yeye ndiye alistahili kufanya hilo wala siyo mtu mwingine.
ITAENDELEA.
 
TULIPOISHIA.
Jambo alilowaza ni ikiwa hatima ya msomi iko kichwani mwake basi siyo yeye atakayetakiwa kumaliza bali kutakuwa na mtu mwingine atakayeifanya hiyo kazi. "Mtu huyo ni nani na kwa nini siyo mimi" Ndilo swali alikuwa akijiuliza asipate majibu, aliamini yeye ndiye alistahili kufanya hilo wala siyo mtu mwingine.

ENDELEA,,
"Kwamba uwezo wangu hauaminiki" aliendelea kuwaza akionekana kuchukizwa sana na kitu kile mpaka akatamani kumpigia aliyemtumia ujumbe lakini alijionya kufanya vile maana ingekuwa kukiuka miiko ya kazi yake.
"Shiiiiiiiiiiiiiiiiiittt!!!!" alimaka kwa hasira akaachia ngumi nzito iliyoipasuapasua meza ya kioo iliyokuwa mbele yake. Hasira zilimpanda sana baada ya kumkumbuka Kipensi akiamini yeye ndiye atakuwa amepewa jukumu la kummaliza msomi. "Una bahati sana kichaa, wanakubeba sana na wanakudekeza mno. Ipo siku yako." Roho ilimuuma sana baada ya kupata wazo hilo, aliwaza namna Kipensi alivyokuwa akibebwa na kupendelewa na wakubwa licha ya uwezo mdogo alionao. Hakuuona mpango ule kuwa sawa kabisa yaani kazi ya heshima namna ile apewe mpuuzi tu ili aonekane kafanya kazi kubwa hali ya kuwa yeye ndiye huwa anahangaika mala zote kusuka mipango na kuhakikisha kila kitu kinafanyika kama kilivyopangwa. "Haina noma, kikubwa muamala wangu uendelee kusoma" Alihitimisha hivo kisha akaingia chumbani alale maana kesho yake alikuwa na ratiba ngumu.

Mithili ya gari la wagonjwa linalomuwahisha mgonjwa mahututi hosipitali, ndivyo lilivyokuwa likikimbia gari hili kwa mwendokasi sana, bahati nzuri ni kwamba tayali ulikuwa usiku mrefu sana hivyo hakukuwa na magari mengi balabalani. Dereva alikuwa makini sana kuuzungusha usukani akipanga na kupangua gia kadili mwenyewe alivyoona inafaa. Mwendo kasi ule haukuja kwa bahati mbaya tu au kujifurahisha kwa dereva bali kuna sababu maalumu ilipelekea hilo kutokea ndiyo maana hakusita kupunguza mwendo baada ya kulifikia gari jingine la aina ile lililokuwa likitembea kwa mwendo wa kawaida. Alipiga honi mala nne mfululizo kisha akaurejea mwendo wake wa awali ambapo alilikimbia kwa kasi sana akalipita lile la mwanzo ambalo nalo liliongeza kasi na kuanza kumfukuzia. Balabala ilikuwa tupu, hakukuwa na magari mengi usiku ule hivyo gari zile zilikimbia kwa kujidai, zikifukuzana kwa kasi sana. Safari ile ilikuja kuishia mbele ya nyumba moja iliyopo nje ya mji eneo lililojitenga kwa kiasi fulani na makazi ya watu. Toka ndani ya gari la kwanza alishuka mwanaume mmoja akaenda kufungua mlango wa nyuma wa gari lake akatoa furushi kubwa liloonekana kuwa zito. Ndani ya gari la pili walishuka wanaume wawili pamoja na msichana mmoja aliyeonekana kutojiweza kabisa, walimnyanyua na kuingia naye ndani ya nyumba. Walitumia dakika mbili tu kukaa ndani ya nyumba ile kisha wakatoka mala hii wakiwa wanaume tu bila yule mwanamke, wakaingia ndani ya magari yao wakayawasha na kuyaondoka kwa mwendo wa kasi sana.

Nyumbani kwa tajiri Isaya mambo yalikuwa shwari kabisa asubuhi ile. Nje ya nyumba wanaonekana walinzi waliovalia suti safi nyeusi zilizoichora vema miili yao iliyojaa kwa mazoezi, kila mmoja alikuwa makini kuhakikisha usalama hasa usalama wa watu waliokuwa ndani ya jumba lile. Sebuleni walionekana wanawake watatu waliovalia sare, walikuwa wafanyakazi wa ndani, wawili walikuwa wasichana na mmoja alionekana mwanamke wa umri wa makamo. Ndani ya moja ya vyumba vya jengo lile alionekana tajiri mwenyewe Mr Isaya aliyekaa kitandani peke yake akiwa kajiinamia na kushika tama kama mtu asiyekuwa na tumaini lolote ndani ya siku hii mpya. Mda huo mlango wa chumba ulifunguliwa akaingia yule mwanamke aliyekuwa sebuleni mkononi akiwa kashikilia sahani kubwa lililokuwa na baadhi ya vinywaji ndani yake.
"Umeamkaje"
"Niko salama sijui wewe unaendeleaje"
"Namshukuru Mungu angalau afya yangu inazidi kuimalika sasa ndiyo maana nikaona nije mwenyewe leo nimpumzishe binti yako."
"Ni habari njema kama unaendelea vizuri, na vipi halakati zetu zinaendaje kwa sasa! maana nimekuwa bize sana kiasi cha kushindwa kufatilia chochote."
"Bado kila kitu kipo sawa japo uwepo wako unahitajika sana, kwa sasa hali ya masoko siyo nzuri kabisa, ukijumlisha na hiki kinachozungumzwa sahivi soko limeshuka sana kaka yangu, bidhaa haziendi. Inatakiwa kufanyike jambo haraka kuweka mambo sawa maana tukisema tusubilie zaidi ndivyo tutakuwa tunajichimbia shimo la kujizika wenyewe."
"Sawa Esinati, kwahiyo wewe unawaza kipi kifanyike."
"Itatakiwa tuuze baadhi ya hisa tulizonazo kwenye makampuni ya nje ili angalau tuwe na pesa ya kutosha kuendeleza mapambano ya ndani maana bila kufanya hivo itakuwa ngumu kuwashawishi wabia wetu kuendelea kutuamini, lakini pia hatujui nini mahakama itaamua kwahiyo ni vizuri kuweka tahadhari ili hata likitokea lolote tujue namna ya kulikabiri."

Isaya alinyanyuka na kumkumbatia mwanamke yule tunayemfahamu sasa kwa jina la Esinati, "Najivunia sana kuwa na ndugu kama wewe umekuwa msaada mkubwa sana kwangu, licha ya aina ya maisha unayoishi lakini mala zote umekuwa msaada kwangu. Naahidi kukulinda mpaka dakika ya mwisho ya uhai wangu, si kwa sababu ya ahadi niliyomuahidi baba yetu kipindi kile bali ni kwasababu ya upendo wangu kwako. Nakupenda sana Esinati mdogo wangu, naomba unisamehe sasa kwa nyakati nilizowahi kukuudhi na kukuumiza." Tajiri aliongea kwa sauti ya uchungu akiwa kamkumbatia mdogo wake kwa nguvu sana, machozi yalikuwa yakimlengalenga machoni ishara ya hisia nzito alizokuwa nazo, Esinati hakujibu chochote, alikiwa mkimya akinaribu kumbembeleza kaka yake.
"Mda sio rafiki, unapaswa kuondoka mapema, kafanye kile ulichonieleza na mengine utaamua mwenyewe kwa wakati ambao sitakuwepo, nakuamini sana Esinati, wewe ni mwanamke jasiri sana. Nenda uendelee kuishi kama mwanzo, usije ukabadili mfumo wa maisha hata kama nitahukumiwa kunyongwa maana siku utakapobadilika itakuwa ndiyo mwanzo wa mwisho wako. Nenda usichelewe uwasalimie wanangu, wambie nawapenda sana" Isaya aliongea maneno hayo kisha akamfukuza mwanamke yule ambaye aliondoka akitokwa na machozi. Maneno aliyoambiwa na kaka yake yalikuwa mazito sana alitamani aendelee kuwepo eneo lile ili ahoji vizuri maana yake, lakini asingethubutu kufanya vile. Aliijua hatari ya kuendelea kuwepo eneo lile hivyo alijikaza akafuta machozi kujiweka sawa kisha akaondoka.

Tajiri Isaya alibaki akimwangalia mwanamke yule wakati akiondoka, alikuwa akikukumbuka matukio mengi ya siku za nyuma namna walivyokuwa wakiishi kwa amani wakiwa watoto wawili pekee wa familia ya mzee Akilimali. Maisha yao yalikuwa mazuri mpaka siku shetani la mabalaa lilipokosea njia na kuingia nyumbani kwao. Ni siku ambayo hataisahau, siku iliyoacha kumbukumbu mbaya zisizofutika akilini mwake. Ilikuwa ni siku ya jumapili siku ambayo kwa kawaida familia yao huamka asubuhi na mapema kujiandaa kwa ajili kwenda kanisani maana mama yao alipendelea kuhudhuria misa ya kwanza. Baba yao hakuwa mpenzi sana wa kuhudhuria kanisani, yeye angeenda mala chache sana hasa zile siku za matukio yanayomhusu kama vile siku ya ubatizo wa watoto wake. Asubuhi ile Isaya alidamka mapema sana si kwa sababu alipenda iwe hivo bali ni baada ya kuota ndoto mbaya iliyomshitua na hakufanikiwa tena kupata usingizi. Mda huo alitulia kitandani akawaza namna mama yake atakavyokuaja kumuamsha mala tu itakapofika saa kumi na moja kamili arufajiri. Siku hiyo alipanga kutokwenda kanisani ili aambatane na baba yake kwenda mgodini alikokuwa akifanyia kazi. Aliyakumbuka vema maneno aliyoambiwa na baba yake usiku wa jana yake alipomweleza mpango wake. "Wewe ni mwanaume, unatakiwa kujisimamia na kujitegemea mwenyewe, kama hujisikii kwenda kanisani kesho basi unatakiwa umweleze mama yako kama ulivyonieleza mimi, wala hatokuzuia" Ndivyo alivyojibiwa na baba yake wakati alipojaribu kumshawishi amuombee ruhusa kwa mama yake ili kesho asiende kanisani. Isaya alikuwa amemzoea na kumheshimu sana mama yake kiasi kwamba asingeweza kumbishia kwa chochote, tofauti na baba yake ambaye angeongea naye kawaida au hata kubishana naye maana mzee mwenyewe ndiye alimlea vile. Ilipofika saa kumi na moja kamili, aliweza kuusikia mlango wa chumba chake ukifunguliwa hapo akajua ni mama yake anaingia kumuamsha, aliigiza kupitiwa na usingizi akiwaza namna gani atamshawishi mama yake abaki nyumbani. Aliendelea kutulia akijiandaa kwa kupangilia vema maneno atakayomwambia mama yake mala tu atakapomgusa. Aliisikia vizuri sauti hafifu ya hatua za mtu akisogea kuja pale alipo, alitulia mpaka pale alipohisi kuguswa, "mama, mimi leo sijisikii kwenda kanisani" aliongea kwa kukulupuka huku akiling'ang'ania blanketi alilojifunika hata hivyo hakusikia sauti ya mama yake akijibu kile alichomwambia. Milio wa simu yake ndiyo ulimshitua toka kwenye dimbwi la mawazo yaliyokuwa yameuhamisha ulimwengu wake mda mfupi uliopita.

Haukuwa mwito wa simu bali sauti ya malamoja kuashiria kuingia kwa ujumbe. Iliichukua simu yake na kuufungua ujumbe ule akausoma,,
"Unaendeleaje Isaya wangu, leo nitahitaji tukutane tena kama tulivyokuwa tukikutana siku za nyuma, eneo lile lile saa na sekunde ileile. Nimekukumbuka sana mpendwa wangu, jitahidi ufike unifurahishe nami nitakufurahisha kwa kukuletea wanao, naamini umewakumbuka sana."
Ujumbe huo ulimshtua sana, mapigo yake ya moyo yaligonga kwa kasi kiasi cha kuufanya mwili mzima kuanza kutetemeka. Licha ya namba iliyotumika kuwa ngeni kwake lakini ujumbe ulioandikwa haukuwa mpya kabisa. Ni aina ya jumbe ambazo yeye mwenyewe hupendelea kuziandika. Yaani ujumbe uliokamilika na kujitosheleza unaeleweka kwa msomaji. Tajiri Isaya hakuwa mpenzi wa kuwasiliana kupitia njia ya ujumbe wa maandishi kwani aliona inampotezea mda mwingi kusoma na kujibu hivyo hata mala chache inapomlazimu kutuma ujumbe wa maandishi basi angetuma ujumbe uliokamilika ili mlemgwa atakapousoma aweze kuuelewa vizuri. Tabia hiyo amekuwanayo tokea ujanani na alishawaambukiza marafiki zake wengi hasa wale aliokuwa karibu nao. Aliishikilia vema simu yake kwa mikono miwili akisoma kwa kurudiarudia ujumbe aliotumiwa. Ni kama hakuamini kile alichokuwa akikisoma kama ndicho kilichoandikwa au ni macho yanamdanganya, lakini ulikuwa ndiyo uhalisia. Alipatwa na hisia mchanganyiko kwa wakati mmoja, sura yake haikueleweka kama anahuzunika ama anafurahi. Kila akisoma sentensi inayozungumzia watoto angejihisi furaha iliyochanganyika na shauku ya kutaka kuwaona wanae ama kweli aliyemtumia ujumbe huo alikuwa akimjua vilivyo na alijua kama amewakumbuka sana watoto wake na ana shauku kubwa ya kutaka kuwaona. Ujumbe ulikuwa mzuri wa kutosha kuifurahisha roho yake lakini kila anapomkumbuka mtumaji wa ujumbe moyo ulidunda kwa kasi mno, alipatwa na hofu sana. Alimkumbuka vizuri mtu aliyemtenga yeye na wanae. Licha ya utajiri mkubwa na umaalufu alionao, tajiri Isaya hajawahi kuishi kwa amani, hajawahi kuwa na raha au furaha ya kudumu katika maisha yake ya kifahari. Sio yeye tu bali hata ndugu zake wote waliojulikana walipitia wakati mgumu kama ilivyo kwake. Nyuma ya yote hayo alikuwepo mtu. Mtu aliyepotayari kufanya chochote kwa gharama yoyote kuhakikisha hayo yanatokea. Mtu Huyo ndiye muhusika na muumbaji halisi wa magumu yote anayopitia. Mtu huyo ndiye aliyemtumia ujumbe asubuhi ya leo.
Tajiri Isaya alikosa amani kabisa, licha ya kuwa na shauku ya kuwaona wanae lakini alikuwa na hofu sana, alihofia maisha yake maana alijua hatokuwa salama tena baada ya kukutana na mtu huyo. Aliuona mwisho wa simulizi yake tokea dakika ile atakapomtia machoni mtesi wake.
"Sijui nini kitanipata, lakini lazima niende kwa ajili ya wanangu, nitaenda niwaone hata kama hii ndiyo itakuwa mala ya mwisho. Liwalo na liwe." Alihitisha kwa kutoa kauli ya kiume kujitia moyo. Aliamua kwenda mahali alipoitwa. Aliukubali wito wa adui yake kwa ajili ya wanae. Alikuwa na shauku kubwa, shauku ya kuwaona wanae aliotenganishwa nao kwa miaka mingi. Shauku na hamu vilimzidia mpaka ile hofu aliyokuwanayo ikatoweka, mwili haukumtetemeka tena, mapigo ya moyo yakarudi kudundia kwenye mhimili wake, usoni alichanua tabasamu, tabasamu la ujasiri mkubwa sana. "Nitaenda. Ndiyo. Lazima niende." ,,,,,,,,,
ITAENDELEA.

😇😇😇
Tajiri Isaya ameamua kwenda alikoitwa, je nini itakuwa hatima yake?
Anaenda wapi?
Ana uhusiano gani na mtu aliyemuita?
Je, watoto wake wapo kweli na ni kina nani?
Kujua yote haya, usikose kufuatilia sehemu ijayo.
"KABURI LA MSOMI" JJ former.
Tukutane Jumanne mda na wasaa kama huu. ✍️✍️✍️
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom