Sehemu ya 14
Siku moja nikiwa faragha na mpenzi wangu nilishangaa kuziona sehemu zangu za siri zimeingia ndani nilishtuka sana. Hali ile ilinifanya nikose raha kwa kuamini zile zilikuwa njama za familia yangu kutaka kuona sifanyi mapenzi na mwanamke.
Katika kumbukumbu nilikumbuka siku moja kabla ya kutokea na tukio lile nilipokuwa na mpenzi wangu kuna kitu alinipaka kilichofanya nihisi kama kuwashwa baada ya kumaliza kufanya mapenzi. Na siku ya pili nilitokewa na tatizo lile, ilibidi nimbane kutaka kujua alinipaka kitu gani.
“Masalu juzi nilikutana na dada yako mkubwa aliniomba nikupake dawa hii, nilikataa lakini alinitishia kuniua. Unajua familia yako umeniandama sana kumbuka kuna wakati nikawa nakukimbia nawe ukaamua kutafuta mwanamke mwingine.
“Kitendo kile kiliniuma sana na kuamua kurudiana na wewe, ndipo juzi nilipokutana na dada yako aliyenipa dawa hii nikupake kabla ya kufanya mapenzi itasaidia kupunguza madhara yanayotokana na matatizo ambayo yangekupata.
“Nilikubali kuipokea kwa vile sikudhania kama dada yako angekufanyia kitu kibaya, kumbe nia yake ilikuwa hii ya kukufanya hivi.”
“Lakini kwa nini amenitenda hivi?” Nilijikuta nikilia kwa uchungu kwa kutendo cha dada yangu.
“Mpenzi sikuwa na nia mbaya kama ningekuwa na nia mbaya leo ningekuwepo hapa?”
“Ona jinsi ulivyonimaliza, hujui ugomvi wangu na familia yangu umekuwa kama mgeni unakubali kunimaliza, ona sasa,” nilisema kwa uchungu huku nikimuonesha sehemu zangu za siri zilizokuwa zimerudi ndani.
“Nisamehe Masalu sikujua yatatokea yaliyotokea.”
“Wameniweza,” nililalamika kwa uchungu.
Nilijikuta nikiapa kupambana nao, nilipanga sitakwenda tena dukani na nilikuwa nipo tayari kufa kwa njia yoyote ili tu niwaachie maisha yao.
“Masalu kwa nini usiende hospitali kuangalia afya yako kuliko kujikatia tamaa,” mpenzi wangu alinishauri.
“Hospitali haitasaidia kitu wameisha niweza kwa msaada wako, ona tena sina thamani ya wanaume, kimebakia kichwa kama kobe. Haya ni maisha gani ya kukoseshana raha.”
“Kama mambo ya kienyeji twende kuna babu mmoja namfahamu anaweza kazi hii.”
“Unanifikiri atanisaidia nini?”
“We, twende yote tutayajua huko huko.”
Nilikubaliana na mpenzi wangu niende kwa mtaalamu aliyekuwa akikaa Pasiansi kuvuka kota za benki. Sikutaka kupoteza muda tuliondoka muda ule ule kwenda kwa mtaalamu kuangalia tatizo langu kama linatatulika.
Kabla ya kwenda kwa mganga nilitulia ili nitafakali kama nitapata ufumbuzi wa tatizo langu bila kwenda huko. Baada ya sehemu zangu za siri kukosa nguvu nilipata mabadiliko mwilini kwa kidonda kuanza kutoaji maji upya huku biashara nazo zikifunguka.
Nilimtolea uvivu dada yangu kwa kumfuata kwenye duka lake na kumshutumu mbele ya wafanyakazi wake kwa kitendo chake cha kishrikina cha kumpa dawa ya kuniua sehemu za siri.
Dada alikimbia dukani huku watu wakiinishangaa, ugomvi wangu haukuishia pale nilimfuata kwake usiku akiwa na mume wake na kuendelea kumshtumu. Lakini dada alinisihi suala lile tukalizungumze kwa wazazi.
“Masalu utanilaumu bure mpango huo ni wa watu wengi si wangu peke yangu.”
“Kwa hiyo baada ya kunipa kidonda hamkuridhika mmeniua nguvu za kiume?”
“Lakini Masalu si ulielezwa madhara ya wewe kutembea na mwanamke?”
“Kuna madhara gani? Mbona ninyi mna wanaume na watoto au mnataka niwe shoga?”
“Hapana usifanye hivyo.”
“Nakuhakikishieni baada ya kuniua nguvu za kiume sasa natafuta mwanaume wa kufanya naye mapenzi,” nilisema kwa hasira.
“Masalu maneno gani hayo?’
“Tena kawaambie na wanga wenzako.”
“Masalu ukifanya hivyo utatudhalilisha.”
“Heri niwadhalilishe kuliko kunidhalilisha kuna faida gani ya mimi kuitwa mwanaume si bora niolewe?”
“Najua tumekukosea lakini unatakiwa ujue madhara yanayoweza kukupata, tumefanya vile kuokoa maisha yako.”
“Maisha yangu hamuwezi kuyaokoa ninyi si Mungu.”
“Hapana kutokana na kafara iliyofanywa ya utajiri, ukifanya kosa kama la Monika lazima wewe au baba mmoja wenu atakufa.”
“Wacha nife mimi kwani nina faida gani?”
“Hapana Masalu una faida kubwa kosa lako litagharimu mambo mengi katika familia yetu. Hatukuwa na jinsi imetubidi tufanye hivyo bila hivyo hali ilikuwa mbaya sana, muda wote huo baba alikuwa mgonjwa mahututi alikwisha anza kupooza sehemu moja.
Amini usiamini kuacha kwako kufanya mapenzi sasa hivi baba ndiyo ameanza kupata nafuu hata chooni anakwenda peke yake. Masalu hebu kuwa na huruma na baba hana nia mbaya sema ni kiburi cha Monika wala kidonda hiki kisingekuja kwako.”
“Ina maana Monika yeye alikuwa hana haja ya maisha mazuri kuwa na mtoto?”
“Maisha mazuri angeyapata tu, kidonda hivi kina muda wake ukikaa nacho kwa miaka ishirini hupotea na wewe kufanya mambo yako bila kipingamizi mtoto utapata tu mdogo wangu wala usijigeuze mwanamke.”
“Dada yaani nikae miaka ishirini bila kuwa na mwanamke nina mkataba na Mungu wa kuishi miaka yote hiyo?”
“Masalu usipofanya mapenzi utapungukiwa na nini?”
“Si swali la kuniuliza, kama inaona sipungukiwi na kitu mbona umemuhonga mwanaume gari?”
“Masalu sasa hayo maneno gani?”
”Huo ndiyo ukweli wenyewe, kila mwanadamu ameumbwa kufurahia mapenzi pia kupata watoto.”
“Najua ni kweli , lakini kumbuka lililotokea lilihatalisha maisha ya baba hatukuwa na jinsi.”
“Basi kama hamna jinsi niacheni niishi maisha niyatakayo.”
“Hapana mdogo wangu, hebu punguza munkari tukae kikao cha familia
Ili tutafute ufumbuzi wa tatizo lako.”
“Hakuna ufumbuzi wowote zaidi ya kuniongezea machungu, nakueleza ukweli sikupendi wewe na wote walionizunguka.”
“Masalu utatulaumu bure, kila kitu baba ndiye anayefahamu.”
“Sasa kama anafahamu kwa nini mnanitesa mimi si mgemuacha akafia mbali.”
“Masalu kuwa na huruma.”
“Niwe vipi na huruma wakati ninyi hamna huruma na mimi, mmemuua dada Monika bila kosa.”
“Masalu Monika kajiua mwenyewe, amekiuka masharti aliyopewa.”
“Muongo mkubwa, nina kila kitu mlichomfanyia, hivi dada kwa Mungu utamwambia nini ikiwa ulimtoa mtoto wako kafara ili upate mali?”
“Nani kakwambia?” Dada alishtuka kusikia vile.
“Nina siri ambazo hata wewe huzijui juu ya familia yetu inayoendekeza ushirikina.”
“Masalu una siri gani?”
“Ya wewe kumtoa mtoto wako ili upate utajili na kuwekwa ndani ya chumba.”
“Masaluu! Habari hizo umezitoa wapi?”
“Unaweza kuamini kuwa ni siri, kuna siri gani ikiwa dada Monika ndiye aliyekuwa akiipaka mafuta maiti ya mwanao.
“Wewee!” Dada alizidi kushangaa.
“Kibaya zaidi mmemuua dada Monika mmeshindwa kumzika na kumuweka ndani kama mwanao. Na wewe siku hizi ndiye unayempaka mafuta, hivi kwa mtindo huo kwa Mungu mtasema nini?”
“Masalu nani kakueleza yote hayo au mama?”
“Utamsingizia bure mama kama wewe, ninayo mengi ambayo wewe huyajui.”
”Masalu mambo gani?”
“Siwezi kukueleza muulize baba si ndiye anayefanya yote haya, hata hiki kidonda nilielezwa mapema kitanipata.”
“Na nani?”
“Na dada Monika, hata kifo cha alinieleza kitakavyompata.”
“Alijuaje?”
“Siku alipoondoka baba alimwambia lazima atakufa.”
“Monika muongo.”
“Kweli kabisa na hata alipotaka kufa alinieleza sema siku ya kufa nilikuwa shule kuna siri nzito alitaka kunipa lakini bahati mbaya sikuwepo. Hata mwanaume aliyekuwa akikaa naye hakumpa siri hiyo dada yangu amekufa na siri nzito hata sijui ni siri gani?”
“Wewe unamuamini?”
“Nisimuamini vipi hata bwana yake mmemuua.”
“Nani kakwambia tumemuua?”
“Najua kila kitu, mimi si mtoto ndiyo maana nimekueleza najua unayoyajua na usiyoyajua.”
Kila nililokuwa nikimueleza dada aliona kama maluweluwe, niliamua kuondoka huku nikiwa na akili kichwani mwangu.
Wazo la kwenda kwa mganga sikulitupa mbali japo lilikuwa mtihani kwangu. Lakini niliamini maisha yangu yananitegemea mimi mwenyewe si mtu mwingine.
Siku ya pili nilimpigia simu mpenzi wangu ili anifuate na anipeleke kwa mtaalamu huyo. Alinifuata na kunipelekwa kwa mtaalamu mmoja aliyekuwa maeneo ya Pasiansi nyuma ya kota za benki.
Tulipofika eneo la mganga tulikuwa kuna wagonjwa wengi kiasi, ile ilinipa moyo kuwa huduma za mganga ni nzuri.
Ilibidi tukae chini ya mti kusubiri wagonjwa wahudumiwe. Baada ya saa tatu ndipo tulipoitwa sisi muda ulikuwa ni saa kumi jioni. Tuliingia ndani na kuketi kwenye mkeka.