Sehemu ya 12
“Mama nakupenda sana, lakini baba hatutendei haki.”
“Najua tuvumilie, hata wewe si unajua maisha yangu yalivyo?”
”Nayajua mama.”
“Sasa kwa nini unakuwa hivyo, hebu tuvumilie.”
”Sawa mama.”
Nilimkubalia mama lakini moyoni nikiwa na siri nzito ya kitendo nilichokifanya na mpenzi wangu usiku kucha.
Baada ya kujiandaa nilikwenda zangu dukani kwangu, nilipofika nilikuwa tayari wameisha fungua. Wahudumu wangu aliponiona walinieleza:
“Bosi mzee alikuja kukutafuta.”
“Amesemaje?”
“Kwa kweli haelewiki, sijui hukulala nyumbani.”
“Kama sikulala nyumbani mimi mtoto?”
“Tutajuaje, tumemkuta kabla ya kufungua duka, alipotuona tu alituuliza upo wapi, sisi tukamjibu tangia jana tulipoachana hatujui upo wapi?”
“Mzee yule anazeeka vibaya, sasa kasemaje?”
Tumemuona akitembea kona moja hadi nyingine kisha alitoweka bila kujua.”
“Achaneni naye.”
Nilisema huku nikikaa kwenye kiti changu, ajabu wafanyakazi walinishangaa jinsi nilivyoonesha sijali lolote. Haikuchukua muda baba aliingia huku akitweta.
“Masalu.”
“Naam baba, shikamoo”
“Marahaba, hebu njoo nje mara moja.”
Nilitoka nje kuzungumza na baba, baada ya kusogea pembeni baba aliniuliza.
“Masalu jana ulilala wapi?”
“Kwenye sherehe.”
“Sherehe ya nani?”
“Ya rafiki yangu.”
“Masalu kuna sherehe gani katikati ya wiki?”
“Birthday.”
“Hukulala na mwanamke wewe?”
“Mbona unaniuliza hivyo?”
“Masalu umelala na mwanamke,” baba alinilazimisha.
“Baba nimekueleza nilikuwa kwenye pati unanilazimisha nimelala na mwanamke,” nilijitia kujitetea.
“Masalu tusije laumiana ukirudia tena shauri yako.”
“Hivi baba kwa nini unanilazimisha kitu nisichokifanya, ulinikataza nisitembee na mwanamke si kufanya mambo mengine kama hili la jana nakushangaa unanitafuta kama mwizi.”
“Mmh sawa.”
“Baba mbona unataka kuninyima uhuru, niliyajua haya toka mwanzo ukabisha, ona sasa unanifuata kila kona,” nilijifanya kulalamika.
“Siyo hivyo, sipendi uingine kwenye matatizo.”
“Baba mi mtu mzima sasa vile vile najijali”
“Kama ni hivyo itakuwa vizuri, nisamehe kama nimekukwaza.”
“Nimekusamehe ila naomba uhuru sipendi nifuatwefuatwe”
Kauli yangu ilimfanya baba azidi kuomba msamaha, tulikubaliana asinifuatilie mambo yangu kwa vile nitajilinda mwenyewe.
Tokea siku ile hata nilipolala nje baba hakunifuatilia aliniacha niishi nitakavyo, mpenzi wangu alinishawishi nihame nyumbani ili tuweze kuwa naye siku zote.
Nilifikisha wazo kwa baba ambaye mwanzo alipinga lakini baada ya kumlazimisha alinikubalia kwa shingo upande. Nilipanga chumba maeneo ya Isamiro ambako nilipanga nyumba nzima. Niliendelea na tabia zangu za kufanya mapenzi na mchumba wangu ambaye alihamia kwangu kwa siri.
Siku moja baba alinifuata dukani na kuniita pembeni, baada ya kusogea pembeni aliniuliza.
“Masalu kwa nini hujiurumii.”
“Vipi?”
“Hebu nione kidonda chako?”
Nilimuonesha, kidonda changu, baada ya kukiangalia alisema:
“Si unaona!”
Nilishangaa sikujua alisema vile kumaanisha nini? Nilijikuta nikijiuliza kipi kilichomuonesha kitu kilichomshangaza.
“Kuona nini baba?”
“Ina maana huoni kidonda chako kinaonesha hujionei huruma maisha yako.”
“Bado sijakuelewa”
“Kidonda chako kinatoa maji?”
“Hapana.”
“Unajua kwa nini?”
“Hata sijui”
“Masalu unatembea na mwanamke wewe.”
“Baba mbona unang’ang’ania neno hilo?”
“Nakuomba uache, shauri zako.”
“Niache vipi wakati sifanyi”
“Masalu mimi baba yako nimewahi kuona jua kabla yako najua kila kitu, na sababu kubwa ya kuhama nyumbani ni kufanya uchafu wako. Huoni hata biashara sasa hivi zinadolola.”
“Baba tafuteni tatizo lingine siyo mimi”
“Mmh, haya mama yako asiye kunililia”
Baba aliondoka akiwa amechanganyikiwa, nami sikuwa tayari kuachana na mpenzi wangu, katika maisha niliamini raha ya mwanaume ni mwanamke na si wingi wa pesa. Siku hiyo hiyo ndugu zangu wote walikuja na kuniweka chini juu ya mimi kuwa na mwanamke.
“Masalu kwa nini hutaki kumsikiliza baba”
“Nimsikilize kwa lipi?”
“Juu ya wewe kuwa na mwanamke.”
“Mna uhakika gani?”
“Sisi hatuna uhakika ila kasema mwenyewe.”
“Ninyi mna wapenzi?” Niliwauliza.
“Tunao.”
“Sasa mimi nazuiwa na nini?”
“Si unajua hali yako haitaki uwe na mwanamke?”
“Kwa hiyo kidonda niwe nacho mimi maisha mazuri muwenayo ninyi, sikilizeni kila mtu ataubeba mzigio wake mwenyewe.”
“Masalu utakuja kuijutia kauli yako.”
“Sijuitii mbona dada Monika hakuijutia na mkiniua na ninyi mnafirisika kazi kwenu.”
Maneno yangu yaliwazima mdomo waliondoka na kuniacha wakiwa hawana hamu na mimi. Tokea siku ile nikawa adui yao mkubwa