Simulizi: Mke Wangu Juliana

Simulizi: Mke Wangu Juliana

SEHEMU YA 48

Moyo ulipenda, ulithamini na kujitoa kwa mwanaume mmoja ambaye hakuonekana kumtaka hata kidogo. Moyo ulichoma, ulikuwa na maumivu makali ambayo hakuwahi kuyafikiria hapo kabla.

Mawazo juu ya John hayakutoka kichwani mwa Juliana, alimpenda mwanaume huyo, alipatana nafasi ya kuongea naye lakini alishindwa kabisa kumwambia kile kilichokuwa kikiendelea moyoni mwake.

Hivyo akabaki akiumia kimya kimya, alipata maumivu pasipo dawa yoyote ile. Moyo wake ukavunjika, furaha ikamtoka hasa baada ya kusikia tetesi kwamba Deborah alikuwa akitoka kimapenzi na John.

Hizo zilikuwa tetesi tu zilizokuwa zikisikika kanisani, hazikuishia hapo bali wale wambeya waliwapa taarifa jinsi mapenzi hayo yalivyoanza, Deborah alivyomchukua John na kwenda kumuombea kazi ofisini kwao.
“Alikwenda kumuombea kazi?” aliuliza Juliana huku akionekana kutokuamini.

“Ndiyo! Yaani kweli kampenda mwanaume yule, au kwa sababu ametoka Dar es Salaam?” aliuliza msichana mwingine.

“Labda!”
“Lakini atawezana na Deborah”
“Kwa nini?”
“Jamaa nasikia masikini, hana hata pesa, amepanga, analala chini, yaani chumbani kwake hana hata ndoo ya maji,” alisema msichana huyo.

“Watawezana, si wamekubaliana lakini!”
“Mh Sidhani!”
Japokuwa Juliana aliendelea kusikia mambo kuhusu wawili hao lakini moyo wake ulikuwa na maumivu makali. Hakuamini kama yeye ndiye aliyekuwa akipitia mambo yote hayo, lile tonge alilokuwa akilitamani siku zote lilipokonywa akiwa karibu kabisa kulila.

Akakata tamaa kwamba asingeweza kumpata mwanaume huyo tena. Kila alipokwenda kanisani na kuwaona wawili hao wakiwa pamoja aliumia kupita kawaida, alitamani yeye awe na John lakini si kumuona akiwa na mwanamke mwingine.

Siku zikazidi kwenda mbele, mapenzi ya watu hao yalizidi kunoga. Deborah hakutaka kuona mambo hayo yakifanyika kimya kimya hivyo alichoamua ni kumshirikisha mama yake juu ya jambo hilo.

“Ni yule kijana wa Dar es Salaam?” aliuliza mwanamke huyo huku akionekana kushangaa.
“Ndiyo!”

“Nimesikia yule kijana ni masikini! Ni kweli?” aliuliza mama yake.
“Kwa maana gani?”
“Hana pesa! Amepanga, maisha yake ni hohehahe!” alisema mwanamke huyo.
 
SEHEMU YA 49

“Lakini mama.......”
“Ni kweli?”
“Ndiyo! Ila ninampenda!”
“Halafu atakulisha nini?”

“Mama lakiniiiiiiiiii....”
“Deborah! Hivi ni lini utakua?”
“Lakini mama kama watu wenye pesa wenyewe wamenitesa, waliniahidi kunioa na hawakufanya hivyo, kwa nini niendelee na kuwa watu wenye pesa?” aliuliza msichana huyo.

Mama yake alishindwa kuelewa, kwake haikumuingia akilini kwamba binti yake aliyekuwa akimpenda na kumtegemea alihitaji kuwa na mwanaume asiyekuwa na pesa.

Alijua ni kwa namna gani alikuwa msichana mrembo, kwa jinsi alivyokuwa tu alitakiwa kuwa na mwanaume aliyekuwa na pesa ambae angempa kila kitu alichokuwa akikihitaji.
Suala la John halikumuingia kichwani mwake hata kidogo, hakutaka kukaa nalo moyoni alichokifanya ni kumwambia mume wake juu ya kile kilichokuwa kikiendelea.

“Nilikuwa nasikia tu kanisani, kumbe ni kweli?” aliuliza mzee Abraham.
“Ndiyo! Ameniambia, moyo wangu umeteteka mno, hivi kweli Deborah anataka kuolewa na yule kijana, ambaye hana kitu kabisa?” mama yake aliuliza huku akionekana kushangaa.

“Haiwezekani! Nimemuhangaikia sana binti yangu, hawezi kuolewa na huyo kijana. Hebu niitie,” alisema mzee huyo huku akivua miwani yake na kuiweka mezani, kichwa chake kilichanganyikiwa, maneno aliyoambiwa alihisi kabisa yaliingia mpaka ndani ya moyo wake na kuuvunjavunja kupita kiasi.

*
*
*
Kama kupenda Deborah alimpenda sana John, alijitahidi kumuonyesha kila aina ya upendo lakini wazazi wake walimwambia hakutakiwa kuwa naye kwa sababu hakuwa na pesa.

Ni kweli John hakuwa na pesa lakini moyo wake ulijawa mapenzi mengi yaliyomfanya kuchanganyikiwa. Mwanaume huyo alitamani sana kumuoa lakini aliona kabisa jambo hilo lingeshindikana kabisa.

Alichokifanya ni kwenda kuzungumza na mchungaji ili amwambie kila kitu kilichokuwa kimetokea. Kweli akawasiliana naye na kuomba miadi ya kukutana na kuzungumza.
Wakakutana ofisini kwa mchungaji huyo na kuanza kumwambia kila kitu.

Mchungaji akakaa kimya, alikuwa akimsikiliza Deborah alivyokuwa akimwambia kuhusu maisha yake na John, jinsi mapenzi yalivyompelekesha kupita kawaida na wazazi wake kukataa kuolewa naye.
 
SEHEMU YA 50

Moyo wa mchungaji ulimuuma mno, hakuamini kama kweli bado kulikuwa na wazazi wa aina hiyo ambayo hawakutaka mtoto wao aolewe na fulani kwa kuwa tu hakuwa na maisha mazuri waliyokuwa wakiyahitaji.

“Nitazungumza nao!” alisema mchungaji.
“Hapana mchungaji! Wazazi wangu hawatojisikia vizuri!” alisema msichana huyo.
“Kwa hiyo unataka nifanye nini?” aliuliza.
“Uongee na John!”

“Nimwambiaje?”
“Kwamba wazazi wangu hawataki anioe!”
“Kwa nini usiende kuzungumza naye wewe mwenyewe?” aliuliza mchungaji.
“Siwezi! Nahisi nitaumia sana, sipendi kumuona akiwa kwenye moyo wa huzuni! Naomba unisaidie,” alisema msichana huyo, machozi yakaanza kujikusanya machoni mwake na hatimaye kuanza kulia.

Mchungaji alimbembeleza kumtaka anyamaze, aliyajua maumivu yake, jinsi alivyokuwa ameumia kwa wakati huo lakini alimtia moyo kwamba kuna siku wazazi wake wangekubaliana naye na hatimaye uchumba ungetangazwa na watu hao kuoana.

Baada ya kumaliza akaondoka, haraka sana mchungaji akampigia simu John na kuomba kuonana naye. Ilikuwa ni lazima iwe haraka kwa sababu muda huo alikuwa na hamu ya kuliongelea jambo hilo.

Kuonana haikuwa tatizo, kwa sababu ilikuwa ni Jumamosi, wakaonanana na kuanza kuzungumza. Walianzia mbali kabisa lakini mwisho kabisa akaanza kumwambia kila kitu kilichokuwa kimetokea.

John alikuwa kimya kumsikiliza, kile alichokisikia kiliuumiza moyo wake, alisikia maumivu ambayo aliamini hakuwahi kuyasikia hapo kabla.

Alijitahidi kutoa tabasamu usoni mwake lakini ukweli ndani ya moyo wake ulikuwa ukiuma, ulichoma kama pasi. Baada ya kukaa kwa dakika fulani na kuongea, John akaulizwa kuhusu msimamo wake.

“Kiukweli ninampenda sana Deborah!” alisema John huku akimwangalia mchungaji.
“Kwa hiyo tufanye nini?” aliuliza mchungaji.
“Naomba nikaonane na wazazi wake!”
“Kuonana na wazazi wake?”
“Ndiyo! Nitahitaji kuzungumza nao kuhusu jambo hili!” alisema John huku akimwangalia mchungaji.

Hilo halikuwa tatizo ila mchungaji alimuonya hakutakiwa kuzungumza jambo lolote baya la kuwakwaza wazazi wa msichana huyo.
 
SEHEMU YA 51

Siku hiyohiyo akampigia simu Deborah na kumwambia kila kitu alichoambiwa na mchungaji. Msichana huyo alijisikia uchungu sana, John alikuwa akiongea huku akilia, hakuamini kama kweli wazazi wa msichana huyo walimkataa kwa kuwa tu hakuwa na pesa.

“Nitakuja kuonana na wazazi wako!” alisema John.

“Lini?”
“Leo hiihii!”
“Leo?”
“Ndio! Hapa ninaongea nawe nipo njiani nakuja! Nataka kusikia msimamo wao, waniambie wao wenyewe,” alisema John na kukata simu.

Akatoka alipokuwa na kuanza kuelekea Mji Mwema, alihitaji kuonana na wazazi wa Deborah, kile alichoambiwa alihitaji kukisikia kwa masikio yake kutoka kwa wazazi hao.

Alipofika, akafunguliwa geti na kuingia ndani. Akapitiliza, na mtu aliyemkaribisha alikuwa huyo Deborah. Kwa sababu ilikuwa ni usiku, siku ya Jumamosi wazazi wote walikuwa hapo, akawasalimia kwa heshima na adabu zote huku uso wake ukiwa na tabasamu pana.

Akakaa kochini, walianza kupiga stori nyingine kabisa na baadaye kuingizia suala lake la kutaka kumuoa binti yao, alihitaji kupewa ruhusa ya kufanya harakati zote alizotakiwa kuzifanya.

“Unafanya kazi wapi?” aliuliza mzee Abraham huku akichukua juisi yake na kuanza kunywa.

“Nafanya naye kazi sehemu moja!” alijibu kwa kujiamini.
“Upo idara gani?”
“Idara ya usafi!”
“Unamaanisha mfagiaji?”

“Ndiyo baba!”
Mzee Abraham akakaa kimya, akamwangalia John, ni kweli kile alichokisema ndicho kilikuwa ukweli wenyewe kwani hata muonekano wake haukuwa wa mtu mwenye pesa kabisa.

Wakati huo Deborah alikuwa pembeni akisikiliza kila kitu, alimpenda John kwa sababu mwanaume huyo alijua mapenzi ni nini, alijua ni kwa namna gani alitakiwa kumpenda mwanamke na kumuonyesha mapenzi ambayo alitakiwa kuonyeshwa.

Mbele ya John, wazazi hao wakamkatalia, walimwambia kabisa kwamba hakuwa na hadhi ya kumuoa Deborah hata kidogo, na si kumuoa bali hata kumsogelea.

“Mzee! Pesa zinatafutwa, inawezekana mwenye pesa leo kesho asiwe na pesa, asiyekuwa na pesa leo akawa na pesa. Naomba mnipe ruhusa kuwa na binti yenu!” alisema John huku akimwangalia mzee huyo.
 
SEHEMU YA 52

“Kijana! Acha porojo, nenda katafute pesa. Huwezi kuwa na binti yangu halafu ukaenda kumchakaza na umasikini wako. Ninampenda binti yangu, sitopenda kuona siku moja akiwa kwenye maisha ya chini, nitahitaji aolewe na mtu mwenye pesa, muonekano mzuri na si wewe,” alisema mzee huyo.

Alikuwa Mkristo ambaye kila Jumapili alikuwa akienda kanisani, alikubalika lakini yeye huyohuyo leo hii alikuwa akimwambia John kwamba hakutakiwa kuwa na binti yake kwa kuwa tu hakuwa na pesa.

Hilo likamliza John, mbele ya wazazi wa Deborah na msichana huyo akaanza kutokwa na machozi. Hilo halikusaidia, msimamo wa wazazi hao ulikuwa uleule kwamba Deborah hakutakiwa kuolewa na mtu masikini kama alivyokuwa.

Deborah hakuvumilia kukaa sebuleni, akasimama na kwenda chumbani kwake, akajifungia na kuanza kulia mfululizo.

Moyo wake uliuma kwa kiwango cha juu kabisa. Ni kweli alimpenda mno John, hakutaka kuona akiondoka na kumuoa msichana mwingine, ndoto yake ilikuwa ni kuolewa na mwanaume huyo kwa kuwa tu alimuonyesha mapenzi ya dhati.

John alikaa sebuleni, mwili wake ulipigwa ganzi, alitamani kusikia wazazi hao wakibadilisha uamuzi wao na kumwambia walikubaliana naye lakini haikuwa hivyo.

Akainuka na kuondoka zake, akatoka nje huku akilia, aliuchukia umasikini aliokuwanao, alichukia maisha aliyokuwa akiishi kipindi hicho.

“Hivi kweli ninakataliwa kuoa kwa sababu ya umasikini wangu?” alijiuliza, alikosa jibu, akaanza kupiga hatua kuelekea nyumbani kwao.

Wazazi wa Deborah walikaa sebuleni, walikuwa wakizungumza kuhusu uamuzi waliokuwa wameamua siku hiyo. Walifurahi kuona hilo likitokea, walipongezana lakini wakiwa hapo, ghafla mlango ukafunguliwa, Deborah akatoka akiwa na begi lake la nguo na kuanza kwenda nje.

Wote wakashtuka, hawakuamini kile walichokiona, walimuita, hakuitikia, ni kama hakuwasikia vile, akafungua mlango na kuondoka zake.

Wazazi wake walikataa kuolewa na John lakini moyo wake ulimwambia ni lazima akaishi na mwanaume huyo.
 
SEHEMU YA 53

Maisha yake hayakuwa na thamani yoyote ile bila kuwa na mtu aliyekuwa akimpenda kwa moyo wa dhati.

“Deborah...we Deborah...” mama yake aliita, hakugeuka nyuma, akatokomea zake, akaanza kumuwahi John, pia ua ilikuwa ni lazima kwenda kuishi na mwanaume huyo.
*

* Juliana hakujua ni kitu gani kilikuwa kinakwenda kutokea, aliwaona John na Deborah wakiwa pamoja, walipendana lakini siku zote katika maisha yake aliamini mwanaume huyo angekuja kuwa nawe.
Kwenye maombi yake hakuacha kumuombea afanikiwe, awe na maisha mazuri mpaka siku ile ambayo angefunga naye ndoa na kuwa mume na mke.

Aliwahi kumwambia mama yake, wakati John akiwa na Deborah mwanamke huyo alikata tamaa ya kuona binti yake akiolewa naye lakini kitu cha ajabu kabisa Juliana aliendelea kumwambia kwamba kuna siku bado mwanaume huyo angekuja kuwa mume wake wa ndoa.

Walikiombea kitu ambacho hawakuona kama kilikuwa na dalili za kufanikiwa. Maisha yao ya kimasikini yaliendelea kama kawaida, kila siku walikuwa watu wa kupigwa na maisha na kila ilipoingia leo waliona ni afadhali ya jana kuliko leo.

Baada ya mwezi kupita tangu watu hao wawili wawe karibu ndipo tetesi zile zikawa kubwa kwamba watu hao walitarajiwa kutangaza uchumba kanisani.

Hilo lilimuuma kupita kawaida, kati ya vitu ambavyo hakupenda kuona vikitokea cha kwanza kilikuwa hicho.

Alijifungia chumbani kwake na kuanza kulia kwa maumivu makali, wakati mwingine alitamani sana kuona akikimbia, kwenda mbali kabisa ili asijue ni kitu gani kilikuwa kikiendelea lakini alishindwa kufanya hivyo.
“Nimesikia wazazi wa Deborah wamekataa,” alisema msichana mmoja, alikuwa akimwambia Juliana.

“Kukataa nini?”
“Deborah kuolewa na John! Yaani jamani mpaka nimeshangaa,” alisema msichana huyo.
Maneno yalianza kusikika kanisa kwamba wazazi wa msichana huyo walikataa kabisa kumruhudu binti yao kuolewa na kijana kama John.

Maisha yake hayakueleweka hata kidogo, alikuwa mwanaume masikini ambaye kwa kuangaliwa tu hakuonekana kama alikuwa na uwezo wa kumlisha Deborah ambaye alikuwa na maisha ya gharama sana.
 
SEHEMU YA 54

Watu wakapigiana simu, wakapeana taarifa hizo, kwa Juliana moyo wake ulikuwa na furaha kupita kawaida, ile nguvu ya kusali ikaongezeka kwani aliamini Mungu alikuwa kazini akipambania ndoto yake ya kuolewa na mwanaume huyo.

Jumapili ya pili baada ya tetesi hizo kusambaa, watu walikuwa kanisani wakiendelea na ibada kama kawaida, hawakuwa na hili wale lile lakini ghafla tu wakaona polisi kama kumi wakija na gari lao, wawili wakateremka na kuelekea lilipokuwa kanisa.

Wakasimama hapo na kuongea na wasimamizi, mashemasi na kuwaambia walifika hapo kwa kuwa walimuhitaji mtu mmoja aliyeitwa kwa jina la John.

“Wapo akina John wengi,” alisema shemasi.
Wakati wakiendelea kuzungumza na mtu huyo, mchugaji ambaye alikuwa mashabahuni aliwaona na hivyo kwenda huko kuzungumza nao. Alipofika, akaambiwa kwamba walikuwa mahali hapo kwa kuwa walikuja kumkamata mtuhimiwa aliyejulikana kwa jina la John.
“Amefanya nini?” aliuliza mchungaji.

“Amemtorosha binti wa watu usiku!” alijibu polisi.
“Amemtorosha binti wa watu usiku?”
“Ndiyo!”
“Binti gani?”
“Deborah Abraham.”

Mchungaji hakuamini alichokisikia, ikabidi arudi kanisani na baada ya sekunde chache akatoka akiwa na John, kabla ya watu hao kumchukua kwanza akaanza kuongea naye.
Alimwambia kile kilichokuwa kimetokea, kwamba Deborah aliondoka nyumbani kwao na kwenda kwake kwani alikasirishwa na maamuzi ya wazazi wake.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom