Simulizi: Mke Wangu Juliana

Simulizi: Mke Wangu Juliana

Sehemu ya 34

Jumatatu, 15/08/2016: Nilimpelekea Deborah zawadi ya samaki nyumbani kwao lakini kwa bahati mbaya sikuweza kumuona, hivyo nikaiacha zawadi hiyo mahali hapo.

Bado moyo wa John ulikuwa kwa msichana Deborah, kwake mtu huyo alionekana kuwa kila kitu, alimpenda na alikuwa tayari kufanya lolote lile kwa ajili yake.

Sura ya msichana huyo haikutoka akilini mwake, alivumilia mpaka siku ya Jumapili ambayo alikwenda kanisani lakini lengo lake kubwa likiwa ni kuonana na msichana huyo.
Alipofika, akasali, na huku ibada ikiwa inaendelea, msichana Deborah akafika na kuingia kanisani. Alikuwa vilevile, urembo wake ulikuwa ni wa juu kabisa, alionekana kupendeza na kuvutia kupita kawaida.

Wanaume kwa wanawake wakageuka na kuanza kumwangalia msichana huyo aliyekuwa akipiga hatua kuelekea sehemu ya kukaa na kama kawaida akapiga magoti na kuanza kumshukuru Mungu kwa kumfikisha salama kanisani hapo.

Macho ya John hayakutulia, alibaki akimwangalia Deborah tu, alitamani kumfuata na kuzungumza naye lakini alishindwa. Moyo wake ulikufa ganzi, alikuwa na mawazo tele na aliiona hiyo kuwa nafasi yake.

“Ngoja ibada iishe! Leo lazima niongee naye tena,” alijisemea huku akiendelea kumwangalia msichana huyo.

Ibada iliendelea huku kila wakati macho ya John yakiwa kwa Deborah, alimpenda kwa moyo wa dhati na alitamani sana muda ufike amfuate na kuzungumza naye lakini aliona kama akicheleweshwa kufanya hivyo.

Baada ya saa kadhaa, ibada ikamalizika na akasimama nje huku akimsubiri msichana huyo mrembo. Alisimama kwa dakika kadhaa, akashtuka kuona msichana mmoja akija mbele yake huku uso wake ukiwa kwenye tabasamu pana. Alikuwa Juliana.

“Bwana Yesu asifiwe!” alimsalimia msichana huyo huku lile tabasamu likiendelea kuwepo usoni mwake.

“Amen!” aliitikia lakini macho yake hayakuwa radhi kumwangalia Juliana muda wote, alikuwa akichunguliachungulia kanisani.
“Umependeza sana leo!”
“Nashukuru mno! Utukufu kwa Mungu aliye hai!” alijibu.

“Hivi unaishi wapi?”
“Nani? Mimi?” aliuliza.
“Ndiyo!”
“Nipo hapo mbele, karibu na makaburi!”
“Mwanga Makaburini?”
 
Sehemu ya 35

“Ndiyo! Nyum....” alisema Juliana lakini hata kabla hajamalizia sentensi yake, John akaingilia.
“Samahani kidogo!” alimwambia baada ya kumuona Deborah akiwa ametoka kanisa.
Akamfuata na kumsalimia.

Mapigo yake ya moyo yalikuwa yakidunda kwa nguvu, hakuamini kama alikuwa amesimama mbele ya msichana huyo kwa mara nyingine tena.

Uso wake ulikuwa kwenye tabasamu pana, kwake, kile kilichokuwa kikiendelea kilionekana kama muujiza fulani hivi. Hakujua ni kitu gani alitakiwa kumwambia, alimsimamisha, akamsalimia lakini hakujua ni kipi kingine alichotakiwa kuzungumza.
“Umependeza sana,” alimwambia.

“Nashukuru sana!”
“Juzi nilikuletea samaki, sijui ulipata?” aliuliza, hakutaka kuchelewa, ilikuwa ni lazima amfanye msichana huyo ajue kwamba yeye ndiye ambaye alipeleka wale samaki.

“Oh! Kumbe ni wewe?”
“Yeah! Ni mimi! Ulipata?” aliuliza.
“Ndiyo! Nashukuru sana Mungu akubariki!” alisema Deborah, akatoa tabasamu pana ambalo liliuvuruga moyo wa John kabisa.
“Amen.”

“Unauza samaki?” aliuliza.
“Ndiyo!”
“Una mtumbwi ama?” aliuliza.
“Hapana! Rejareja tu! Nanunua na kuwauza mitaani!”

“NA nilisikia umetoka Dar es Salaam!”
“Yeah! Ushawahi kufika?”
“Mara moja tu! Mwaka juzi, na sikukaa sana!”
“Oh!”

“Yeah! Nilikuwa huko kikazi kidogo, kwenye semina!” alijibu.
“Semina gani? Kampuni gani?”
“Kigoma Fishing Company,” alimjibu, John akashtuka.

“Kigoma Fishing Company?”
“Ndiyo! Unaijua?”
“Ndiyo! Mungu wangu kumbe unafanya kazi kwenye kampuni hiyo?” aliuliza John huku akijifanya kutokuamini.

“Ndiyo!”
“Mungu wangu!”
“Kwani kuna nini?”
“Ops! Siamini! Unafanya kazi kwenye kampuni hiyo?” aliuliza tena na tena.
Hilo likamfanya Deborah kushtuka zaidi, akajikuta akiingiwa na shauku ya kutaka kufahamu ni kitu gani kilichokuwa kikiendelea kwenye kampuni hiyo ambayo alijitolea kwa nguvu zote kufanya kazi usiku na mchana.

John hakutaka kumwambia sababu siku hiyo, alichomwambia ni kutafuta muda ambapo watakaa pamoja na kuzungumza kuhusu kampuni hiyo na sababu iliyomfanya kushtuka namna hiyo.

“Mh! Ila kuna nini?” aliuliza Deborah!
“Usijali! Nitakwambia! Kumbe kwenye kampuni hiyo? Aiseee!” alisema, maneno ambayo yalizidi kumtia msichana huyo kwenye maswali mengi.
 
Sehemu ya 36

Hiyo ilikuwa njia ya kwanza ambayo alitamani sana kumzoea msichana huyo. Hapakuwa na jambo lolote lile, alijua kwamba endapo angejifanya kuwa na kitu kuhusu kampuni hiyo basi msichana huyo angehitaji kujua na hivyo kumwambia waonane ili wazungumze zaidi.

Hilo ndilo alilolitaka, alihitaji kuzoeleka na msichana huyo, hiyo iwe mwanzo na mwisho kabisa wawe wapenzi kama alivyotaka iwe.
Alichokifanya ni kumuomba namba ya simu ili siku akiwa na muda ampigie, waonane na kumwambia mengi. Kwa kuwa Deborah alikuwa na hamu kubwa ya kutaka kujua, akamwachia namba yake na hivyo kuondoka zake.

Muda wote huyo Juliana alikuwa pembeni, macho yake hayakutoka kwa wawili hao, aliwaangalia, kwa jinsi John alivyoonekana tu ilionyesha ni kwa namna gani alimvutiwa na Deborah, hata ongea yake ilikuwa na maana kubwa sana kwa kile kilichokuwa kikiendelea moyoni mwake.

Baada ya kumaliza kuzungumza na John, Deborah akaomba kuondoka, akaruhusiwa na hapohapo Juliana kumfuata John ambaye alibaki akiwa amesimama akimwangalia msichana huyo.
“John!” aliita. John akageuka na kumwangalia Juliana.

“Naam!”
“Umeniacha solemba!”
“Oh! Samahani! Hivi unaitwa nani vile?”
“Juliana!”

“Oh! Sawa dada! Ulikuwa unasemaje?” aliuliza John huku kwa macho ya kuibia akimwangalia Deborah aliyekuwa akiingia ndani ya gari na kuondoka mahali hapo na familia yake.

“Nilitaka kukusalimia tu!”
“Oh! Ahsante sana dada yangu!” alisema John.

“Sawa. Mungu akubariki! Tutaonana Mungu akipenda!” alisema msichana huyo, akamuaga na kuondoka zake.
 
Sehemu ya 37

John alikuwa na namba ya simu ya Deborah, kilikuwa kitu kizuri ambacho alitamani kuwa nacho kwa kipindi kirefu mno. Moyo wake ulikuwa na furaha tele, hakuamini kwamba hatimaye alikuwa akienda kufanikisha kile alichokuwa akikifikiria kila siku.

Hofu yake ilikuwa ni muonekano wake tu. Yaani yeye na Deborah hata kama walikuwa wakisimama pamoja walionekana kuwa watu wawili tofauti. Msichana huyo alikuwa wa kishua, aliyetoka kwenye familia ya kishua, msichana ambaye alikuwa na uwezo wa kumchagua mwanaume aliyekuwa akimtaka.

Hofu yake hiyo ilianza kutoweka baada ya kukumbuka kwamba alitoka jijini Dar es Salaam. Kilichoaminika ni kwamba wasichana wengi waliokuwa wakiishi mikoani waliwaona wanaume wa Dar kuwa tofauti fulani kuliko wa huko.

Wengi walihisi wana pesa, muonekano mzuri, jinsi walivyoongea waliongea vizuri na mambo mengine ambayo kila siku waliendelea kujidanganya nayo.

Hilo likamfanya kuhisi kwamba angeweza kumdaka msichana huyo ila alipokuja kukumbuka kwamba yeye alikuwa muuza samaki tu, mnuka shombo, moyo wake ukafa ganzi.

Akaondoka kanisani, alipofika nyumbani akatulia, akachukua simu yake iliyofungwa na ruber band na kuanza kuiangalia namba ya msichana huyo.

Moyo wake ulikuwa na shauku ya kumpigia na kuzungumza naye, hata asikie sauti yake tu ili moyo wake uridhike. Alivuta pumzi kwa dakika chache tu, hatimaye akaamua kumpigia simu msichana huyo.

Wakati simu ikianza kuita, moyo wake ulikuwa na presha kubwa, ulikuwa unadunda kwa nguvu kama ulitaka kuchomoka kutoka kifuani. Baada ya sekunde chache, ikapokelewa.

“Bwana Yesu asifiwe!” ilikuwa salamu ya kwanza aliyoitoa, alifanya hivyo kwa makusudi kabisa, alihitaji kumuweka sawa ili ajue alikuwa akiwasiliana na mwanaume aliyeokoka.
“Amen! Habari yako!” alisikika msichana huyo.

“Nzuri tu! John hapa!”
“John yupi?”
“Wa kanisani!”
“Oh! Mdar es Salaam!” “Yeah!” alisema John huku akijisikia fahari kuitwa hivyo.
 
Sehemu ya 38

Wakaanza kuzungumza. Lengo kubwa la kumpigia simu msichana huyo lilikuwa ni kumzoea, kabla ya mambo mengine kuendelea kwanza ilibidi wawe karibu kwa kipindi fulani ili hata kama kitakuja kipindi cha kumwambia kwamba alimpenda kusiwe na tatizo lolote lile.

Alikuwa mcheshi, alimchekesha msichana huyo, hakumpa pumzi ya kuongea sana kwa sababu watu wengi walipenda kuwasikia watu wa Dar es Salaam kwa jinsi walivyokuwa wakiongea kwa mapozi, kama cherehani.

“Umenifurahisha sana!” alisema Deborah.
“Ni wajibu wangu kukufurahisha!” alisema.
“Na Dar ulikuwa unaishi sehemu gani?” aliuliza.

“Tandale!”
“Tandale?”
“Ndiyo! Ushawahi kufika?”
“Hapana! Huwa nikienda nafikiaga Mwenge kwa baba mdogo!” alijibu.
“Oh! Basi ninaishi huko! Kwa wajanja!”
“Kwa akina Diamond?”

“Yeah! Alikuwa jirani yangu, yaani nyumba yao ile kule, yetu hii,” akajiongeza kidogo.
Wakazungumza kwa dakika kadhaa na walipomaliza, simu ikakatwa na kuendelea kufanya mambo yake. Hapo kidogo moyo wake ukatulia, akawa na furaha, alijiona kuwa mshindi na pia ua ilikuwa ni lazima msichana huyo aingie mikononi mwake.

Wakati akijifikiria hayo, mara simu yake ikaanza kuita, haraka sana akahisi ni Jumanne, akaichukua, kuangalia jina, akashangaa kuona ni Deborah. Moyo ukaanza kudunda tena.

“Niambie bosi wangu!” alisema.
“Eti bosi wangu! Sasa nina ubosi gani?” aliuliza msichana huyo huku akicheka.
“Wewe ni bosi tu! Nimewaona wanawake wengi Kigoma, ila kwako, daah! Mungu kakubariki sana,” alisema.

“Hahaha! Aya ahsante! Nimekupigia kutaka kukuuliza kitu!” alisema.
“Kitu gani?”
“Kuhusu kampuni yetu!”

“Oh! Husahau! Sasa hatuwezi kuongea kwenye simu!”
“Mpaka?”
“Tuonane!”
“Basi nitakutafuta baadaye! Ama utakuwa bize?” aliuliza msichana huyo.

“Hapana! Nitakuwa na muda!”
“Sawa!” alisema na kukata simu.
Furaha aliyokuwanayo haikuweza kuelezeka hata kidogo. Moyo wake ulichanganyikiwa, hakuamini kama kweli Deborah alihitaji kuzungumza na yeye.

Haraka sana akakurupuka kutoka kwenye godoro lake na kuufungua mfuko wake wa nailoni na kuanza kuangalia nguo zake, alihitaji kuvaa nguo fulani maridadi kwa lengo la kumvutia msichana huyo.
 
Sehemu ya 39

“Hii hapana! Nitaonekana wa kuja!” alijisemea na kuiacha.

Alikuwa na mtihani mkubwa wa kuchagua mavazi ya kuvaa huo muda ambao angekutana na Deborah. Alifanya uchaguzi kwa dakika kumi na tano ndipo akajua ni mavazi gani ambayo alitakiwa kuyavaa.

“Haya yanafaa!” alijisemea.
Ilipofika majira ya saa 10:15 jioni akapigiwa simu na msichana huyo, haraka sana akaipokea na kuanza kuzungumza naye.

Alimwambia alikuwa tayari kama vipi walitakiwa kuonana sehemu na kuzungumza.
Hilo halikuwa tatizo, wakapanga kuonana katika mgahawa wa Bijou uliokuwa Mjini karibu na Shule ya Msingi ya Kigoma ambapo hapo wangekaa na kuzungumza.

Baada ya nusu saa wakaonana huko. Kwa jinsi Deborah alivyovaa, John akabaki hoi, alimwangalia msichana huyo, alivutia, alikuwa mrembo kupita kawaida. Akachanganyikiwa na mapenzi juu yake yakazidi kuongezeka zaidi na zaidi.

Watu walikuwa wakimwangalia, hawakuamini kama kulikuwa na msichana mrembo kama alivyokuwa huyo Deborah. Ni kama alikamilika, alionekana na sifa zote ambazo alikuwanazo mwanamke aliyeitwa kwa jina la mrembo.

Akasimama, akamsogelea na kumsogelea kisha kumkumbatia, alinukia vizuri, alitamani kumng’ang’ania ili na yeye aichukue harufu ya manukato ya msichana huyo.
“Unanukia vizuri!” alisema John.

“Nashukuru sana!”
Akamvutia kiti na kukaa. Hakuzungumza kitu, alibaki akimwangalia tu, alinoga kupita kawaida, muda wote huo Deborah alikuwa akiachia tabasamu pana.
“Wewe ni mrembo sana!” alisema John huku akimwangalia Deborah.

“Oh! Nashukuru sana!”
Kabla ya kuzungumza kile kilichowafanya kuwa mahali pale, wakaanza kuzungumza mambo mengine kabisa. John aliamua iwe hivyo kwa sababu alihitaji kumzoea kwanza, wawe marafiki wa kutosha na ndipo wazungumze mambo mengine ya msingi.

Walikuwa katika hilo kwa dakika kadhaa ndipo hasa wakaanza kuzungumza kile kilichowafanya wapigiane simu na kuitana mahali hapo.
“Kuna nini kwenye kampuni hii?” aliuliza Deborah.
.
.
.

Je, nini kitaendelea?

Tukutane week ijayo
 
Sehemu ya 40

John hakuwa na jibu zuri la kumpa ila alichokifanya ni kuanza kumwambia kuhusu mambo mengine tu ya kuunga unga, jinsi alivyowahi kwenda kwenye kampuni hiyo kuomba kazi, akatolewa nje kwa sababu tu hakuwa na muonekano mzuri.

“Yaani kisa muonekano?” aliuliza Deborah.
“Ndiyo! Niliumia vibaya mno, nadhani ndiyo moja ya sababu iliyonifanya nije Kigoma kutafuta maisha!” alisema John huku akimwangalia Deborah, sura yake aliiweka katika hali ya kuonewa huruma.
“Umekuja Kigoma kutafuta maisha?” aliuliza Deborah.

“Ndiyo! Na bahati nzuri nimekutana na wewe,” alisema John.
Deborah alishangaa lakini hakutaka kugundulika, akampa pole kwa mambo yote yaliyokuwa yametokea huko Dar es Salaam na alimtia nguvu kwamba alitakiwa kupambana kwani maisha yalikuwa popote pale.

Walizungumza mengi, John hakutaka kujificha, alimwambia msichana huyo kuwa alihitaji sana kupata ajira yenye mshahara mzuri kwani biashara ya kuzunguka mitaani akiwa na kapu la samaki ilimchosha mno.
“Una elimu gani?” aliuliza Deborah huku akimwangalia John.

“Nilisoma mpaka kidato cha pili, wazazi wakakosa ada hivyo nikabaki nyumbani!” alijib.

“Pole sana! Nitaangalia nitakusaidia vipi! Ungependa kuwa na kazi ipi?”
“Kiukweli yoyote ile, najua siwezi kupigwa na kiyoyozi, kazi yoyote nitashukuru Mungu!” alisema John.

Deborah akajisikia huruma sana, moyo wake ulichoma kupita kawaida. Alimwangalia John, ni kweli alinyesha kuhitaji msaada mkubwa.
Hata kwa jinsi aivyovaa, alionekana kuwa na maisha ya chini mno. Akajiahidi kumsaidia kwa hali na mali, hivyo wakaagana na kurudi majumbani kwao.

Siku hiyo Deborah akaanza kumfikiria John, hakuamini kama mwanaume huyo alitoka jijini Dar es Salaam. Aliwafahamu watu wa huko, wanapokwenda mikoani huwa tofauti, wanaringa, wanajiona wao ndiyo wao, maisha mazuri lakini huyu ambaye alikutana naye kipindi hicho alikuwa tofauti kabisa.
“Kwa nini amekuwa hivyo?” alijiuliza.
 
Sehemu ya 41

Siku iliyofuata akaondoka na kwenda kazini, alipofika huko, kitu cha kwanza kilikuwa ni kuzungumza na bosi na kumwambia kilichokuwa kikiendelea kwamba alifanikiwa kuonana na kijana mmoja ambaye aliguswa sana kumsaidia hivyo kama kulikuwa na kazi yoyote ile ya kufanya hapo, alikuwa tayari.

Bosi huyo, Bwana Masako alimwamini sana Deborah, alikuwa mfanyakazi muaminifu, aliyekuwa akijituma kuliko hata wafanyakazi wengine, na ili kumfurahisha, akamwambia basi azungumze na kijana huyo, kulikuwa na kazi ya kufagia katika jengo la kampuni hiyo kwa sababu mtu aliyekuwa akiifanya kazi hiyo alitarajiwa kuondoka kuelekea jijini Mwanza kwa ndugu zake.

“Nashukuru sana bosi! Nitawasiliana naye na kesho tu atafika mahali hapa,” alisema Deborah huku akionekana kuwa na furaha tele.

Alipotoka tu kitu cha kwanza kilikuwa ni kumpigia simu John na kuanza kuzungumza naye. Alimwambia kilichokuwa kimeendelea, kwamba kazi ilipatikana na hivyo alitakiwa kufika huko kwenye kampuni hiyo kwa lengo la kuanza ajira yake mpya.

John alichanganyikiwa, alipagawa, hakuamini alichokisikia, aliuliza mara mbilimbili kama ni kweli ama Deborah alimdanganya, msichana huyo alimwambia ni kweli na hivyo alitakiwa kwenda huko.
“Mungu akubariki sana!” alisema John.
“Amen!” alisema Deborah.

Siku iliyofuata asubuhi na mapema John alikuwa ofisini hapo hata kabla ya wafanyakazi. Kwa jinsi alivyokuwa kila mmoja aliamini alikuwa na maisha mabovu mno, alivaa kama jamaa fulani la mitaani na si kama wao ambao waliingia huku wakiwa na suruali za vitambaa, mashati huku wakichezesha funguo za magari.

Pamoja na umasikini wake lakini John alikuwa na heshima kubwa, kila aliyekuwa akiingia mapokezini, alisimama na kuwasalimia kwa kuwashika mikono. Alikuwa mnyenyekevu kiasi cha dada wa hapo mapokezi kushangaa.

“Unaitwa nani vile?” aliuliza dada huyo.
“John Chagala!”
“Unaishi wapi?”
“Mwanga Makaburini!”
“Sawa!”
 
Sehemu ya 42

Baada ya hapo, dada yule akaendelea na kazi zake mpaka muda ambao Deborah akaingia ofisini humo. Alipomuona tu, akaonyesha tabasamu, haraka sana John akasimama na kumsalimia kwa kupeana naye mikono.

“Umefika muda sana?” aliuliza.
“Kabla ya mtu yeyote humu?” alijibu John huku akiwa na furaha tele.
“Umehudumiwa?”
“Yeah! Nashukuru nimehudumiwa vizuri!”

“Na umekula?”
“Hapana!”
“Hebu twende nje tukale!” alisema Deborah.
Akamchukua kijana huyo na kuondoka naye kwenda kwenye mgahawa uliokuwa hapo na kunywa chai. Alishangaa, ni kweli aliwahi kuishi na watu wengi lakini kwa jinsi msichana huyo alivyokuwa mnyenyekevu kulimfanya kuwa na mshangao mkubwa mno.

Alichokuwa akikiamini ni kwamba wanawake wengi warembo walikuwa na mapozi, maisha fulani ya nyodo lakini lililomshangaza kabisa ilikuwa ni tofauti na huyo Deborah.
“Ila utatakiwa kufanya kazi sana,” alisema Deborah huku akimwangalia John.

“Kwa hilo usijali dada yangu!”
“Ukiwa mvivu utaniondolea uaminifu kwa bosi, kujitoa kwako kwa nguvu kubwa kutanifanya nizidi kuaminika! Naomba usiniangushe,” alisema Deborah.

“Sawa haina shida. Ninakuahidi sitokuangusha!” alisema.
Walikunywa chai na walipomaliza, akamchukua na kumwambia amsubirie bosi ambaye alikuwa na kawaida ya kuchelewa kila siku.

Hilo halikuwa tatizo, John akamsubiri mapokezi na alipofika majira ya saa nne, akafuatwa na Deborah ambaye alimchukua na kumpeleka ofisini kwa bosi na kuanza kumtambulisha.

Alimmwagia sifa nyingi kwamba hakuwa mvivu, alikuwa mfanyakazi aliyejitoa ambaye kama angepewa nafasi kufanya kazi kwenye ofisi hiyo basi ingekuwa imepata mmoja wa wafanyakazi bora.

“Elimu yako?” aliuliza Bwana Msako.
“Kidato cha pili!” alijibu John.
“Yaani hukufika hata kidato cha nne?” aliuliza.

“Ndiyo bosi!”
“Sababu?”
“Wazazi hawakuwa na pesa!”
“Pole sana!”
“Ahsante!”

Siku hiyo ndiyo ambayo John akaanza kufanya kazi ya ufagiaji ndani ya kampuni hiyo. Ni kweli biashara yake ya samaki ilikuwa ikimuingizia kiasi kikubwa cha pesa kuliko mshahara ambao aliahidiwa hapo lakini hakutaka kujali sana, kiu yake kubwa ilikuwa ni kuwa karibu na msichana Deborah tu.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom