Simulizi: Mke Wangu Juliana

Simulizi: Mke Wangu Juliana

Sehemu ya 104.

Martin alikuwa jamaa yake tangu walipokuwa chuoni, walipanga mambo mengi likiwemo la kuishi pamoja hapo baadaye. Alimpenda sana kijana huyo, walifanya mambo mengi lakini kubwa zaidi likiwa ni kumtambulisha kwa wazazi wake kwamba alikuwa mpenzi wake ambaye alipanga kuoana naye.

Alimpenda, ndiyo, lakini mwanaume ambaye alimfuata kipindi hicho alikuwa tofauti. Achana na uzuri wake, zile pesa alizokuwanazo zilimchanganya akili yake kupita kawaida.

Akakaa kati, akawa kama fisi, tamaa ikamuingia, alitamani wanaume wote awamiliki lakini alishindwa, mmojawapo alitakiwa kuwa bora zaidi ya mwingine.

“Sasa hapo unataka nikushauri nini?” aliuliza Christina huku akimwangalia rafiki yake, alikuwa na wivu mkali lakini uso wake ulikuwa kwenye tabasamu pana kana kwamba alifurahia alichokuwa akiambiwa.

“Niwe na nani hapa?” aliuliza Amanda.
“Wewe unampenda nani?”
“Nawapenda wote!”
“Wa zaidi?”

“Martin jamani! Si unajua tumeanzia mbali! Hivi nikimuacha itakuwaje?”
“Sasa hapo ni kumpenda ama kumuonea huruma?” aliuliza Christina.

“Yaani hata sijui nisemeje!”
“Na huyo mwingine?”
“Ana pesa sana. Jana kanichukua kunipeleka pale Hyatt, ilikuwa balaa, sijui yule kaka anamliki visima vya mafuta!” alisema huku akijifanya kujifikirisha.

“Kwani wewe katika maisha yako unahitaji nini hasa?” aliuliza Christina huku akimwangalia rafiki yake huyo.
“Maisha mazuri!”

“Basi kuwa na huyo mpya!”
“Ila sasa...daah! Martin....” alijisemea.
“Basi achana na huyo jamaa mpende Martin, si ndiye unampenda kwa moyo wa dhati!” alisema Christina.

Amanda akanyamaza, ni kweli mbele yake kulikuwa na mtihani mzito, hakujua ni uchaguzi gani alitakiwa kufanya. Alimpenda Martin lakini kijana huyo hakuwa na maisha yoyote yale.

Alimaliza naye chuo, na wakati huo kama alivyokuwa yeye hata kijana huyo alikuwa akitafuta ajira, aajiriwe na kuendelea na maisha yake lakini hiyo ilikuwa tofauti na John.

Mwanaume huyo alionekana kuwa na maisha mazuri, alikuwa na pesa na alikuwa akifanya alichokuwa akikitaka kwa wakati wowote ule.
 
Sehemu ya 105.

Kitu kilichokuwa kikimsumbua moyoni mwake ni kuujua ukweli wa John, ni kweli alikuwa akimpenda kwa mapenzi ya dhati ama alihitaji kumfunua na kuondoka zake.
Alitakiwa kufanya uamuzi sahihi lakini kabla ya yote alitakiwa kufanya uchunguzi kwa hali ya juu. Alipofika hatua hiyo ndipo akajilaumu kwa nini alimwambia Christina mapema hivyo.

Alitakiwa kujiamulia mwenyewe kwamba ni uchunguzi ndiyo uliotakiwa kufanyika na mambo mengine yaendelee. Walizungumza mengi na baada ya kumaliza akachukua elfu thelathini na kumpa rafiki yake huyo.
“Hizi alikupa yeye nini?”

“Yaani wewe acha tu! Alinipa laki mbili za matumizi ya wiki hii!” alijibu Amanda.
Moyo wa Christina ukazidi kuuma, aliumia kwa kuwa mwenzake alikuwa na mwanaume mwenye pesa ambaye angemaliza matatizo yote aliyokuwanayo.

Wakati mwenzake akiwa na bahati hiyo, yeye alikuwa akihangaika usiku na mchana kutafuta wanaume wa namna hiyo. Aliishia kuchukuliwa na kutumiwa usiku mmoja na wanaume wenye vipesa na kumuacha kwenye mataa.

Aliagana na Amanda huku akiwa na hasira moyoni mwake, moyo uliwaka kwa wivu mkali uliomfanya mpaka kuhisi kama muda wowote ule angeweza kufariki dunia.

Hakutaka kukubali, hakutaka kuona mwenzake akiwa na mwanaume mwenye pesa halafu yeye abaki na wale kapuku, alitaka kupambana kuhakikisha anampata mwanaume huyo na kumpa kila kitu alichokihitaji, yakiwemo mapenzi matamu kitandani ili aachane na Amanda.

Hakujua ni kwa namna gani angeweza kupata namba yake ya simu. Hakutaka kujua alikuwa na sura gani, doa gani lakini kuwa na sifa ya kuwa na pesa tu kwake ilitosha kabisa kulala na mwanaume huyo.

Akajifanya kuwa karibu zaidi na rafiki yake, Amanda huku kila siku akionekana kucheka kumbe moyoni mwake akiwa na wivu mkali uliokuwa ukimtafuna kadiri siku zilivyozidi kwenda mbele.
 
Sehemu ya 106.

Wakati yeye akiwa kwenye hali hiyo kwa Amanda ilikuwa tofauti kabisa, msichana huyo aliendelea kujiona kuwa mtu mwenye bahati, mbele yake alikuwa na wanaume wawili, wote walikuwa wakimpenda kwa mapenzi ya dhati na wakati huo ilikuwa ni uamuzi wake ni yupi ambaye alitakiwa kuwa naye.

John alimpenda sana Amanda, alimuhitaji msichana huyo, mara kwa mara alikuwa akimpigia simu na kumjulia hali, hakutaka kuomuona akiwa kwenye hali ya huzuni, alitamani kumpa kila kitu kilichokuwa kikihitajika kwa msichana huyo.

“Natamani sana kupendwa kama ninavyokupenda,” alisema John kwenye simu.
“Nitakupenda kama unavyotaka!”

“Nitashukuru sana! Naomba nikuulize kitu!”
“Uliza tu mpenzi!”
“Kuna mtu una-date naye kwa sasa?” aliuliza.

Swali hilo hakulitegemea hata kidogo, lilimshtua, hakuwa amepanga jibu la haraka haraka la kumpa. Kumwambia alikuwa aki-date na mtu fulani ilimaanisha huo ungeweza kuwa mwisho wao.

Alijiona kuwa msichana asiyekuwa na akili hata kidogo kama tu angekubaliana naye ndiyo kulikuwa na mwanaume mwingine, angezipata vipi pesa hizo? Yale maisha mazuri angeyapata wapi? Akaamua kumdanganya.
 
Sehemu ya 107.

“Hapana! Nipo singo now! Nyie wanaume wabaya sana ndiyo maana sitaki kuwaamini tena,” alisema Amanda.
“Ila naomba uniamini!”
“Sawa haina shida. Ila kwa nini umeniuliza hivyo?”

“Ninahitaji kufahamu kabisa kama kuna mtu, haimaanishi nitakwambia uachane naye, hapana, sitokwambia ila nitatakiwa kujua kuna mtu mwingine hivyo nina kila sababu ya kumuonyesha mtu huyo nampenda mpaka niuteke moyo wake kwa asilimia mia moja kabisa na huyo mwingine atoke moyoni mwake,” alisema John.
“Mh!”

“Ndiyo hivyo! Kila mwanamke mzuri unayemuona ana mwanaume, hivyo tunapofanikiwa kumpata mwanamke wa mtu basi tumpende kwa dhati, tumuonyeshe mapenzi makubwa, yule mwingine ataachwa tu,” alisema John.
“Kumbe!”

“Ndiyo! Kama mtu kwenye uhusiano wake kila siku anapigwa, anadharauliwa, ananyanyaswa na kufanyiwa mambo ya kishenzi halafu wewe ukaingia na kumuonyesha mapenzi ya dhati, ukamjali, kumsikiliza na mambo mengine, kwa nini usiuteke moyo wake? Ni rahisi Amanda,” alisema John. “Nimekuelewa!”

“Na kitu gani hupendi kufanyiwa na mpenzi wako?” aliuliza.
“Mengi! Zaidi kusalitiwa!”
“Sawa! Sitokusaliti!”
“Na wewe?”

“Sipendi kudanganywa! Ujinga wote unaanzia kwenye uongo. Mtu anapotaka kusaliti ni lazima aanze kudanganya, ajifanye anapenda sana kumbe nyuma ya pazia kuna kitu kingine. Uongo ndiyo dhambi ya kwanza duniani, si unalijua hilo?” alisema John na kuuliza.

“Ndiyo!”
“Basi ndiyo maana uongo ninauchukia sana. Inawezekana kama yule nyoka asingemdanganya Hawa pale bustanini na kuwafanya wale tunda, leo hii tungekuwa tunakula bata tu,” alisema John na kuanza kucheka.

“Yaani wewe!”
“Amanda mpenzi! Naomba usinidanganye, hata kama kitu kitaniumiza sana, naomba usinidanganye kwa sababu nikiujua ukweli baadaye na wakati umenidanganya, nitaumia sana,” alisema John.

“Usijali! Sitokudanganya!”
“Una uhakika?”
“Ndiyo mpenzi!”

|
|

Je, nini kitaendelea?
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom