Sehemu ya 101.
“Binadamu wote tunakosea, lakini wote tuna nafasi ya kujirekebisha! Inawezekana kabisa nikawa mwanaume mbaya sana kwako, ila haimaanishi nitakuwa mbaya hivyo milele, hakuna mtu anayetaka kuwa mbaya, ubaya unakuja ghafla, wakati mwingine unaondoka,” alisema John huku akimwangalia msichana huyo.
“Hujawahi kuona siku moja umechukua uamuzi mbaya wa kumuumiza mtu fulani halafu unaanza kujuta? Hutokea kwenye maisha yetu, na kama kungekuwa na mtu ambaye anakuona wakati unamfanyia mtu huyo ubaya huo, angesema wewe ni mbaya, kumbe ni hali tu ambayo imetokea na baadaye ulijuta kwa nini ulifanya hivyo,” alisema John.
“Unamaanisha nini?”
“Kitu cha kwanza unachotakiwa kujua ni kwamba mwanaume hajakamilika, sisi ni binadamu na si malaika. Mwanamke unapoamua kuingia kwenye uhusiano na sisi, unategemea kupata maisha mazuri milele bila kujua kuna wakati ubinadamu unatuingia na kuanza kufanya maamuzi ya kijinga kabisa,” alisema John.
“Unamaanisha usaliti?”
“Usaliti, wivu, hasira na mambo mengine ni ukamilifu wa binadamu. Leo nikikusaliti haimaanishi mimi ni mbaya sana kwa kuwa utampata mwingine naye atakusaliti vilevile. Kuna makosa tukiyafanya yanadhihirisha kwamba sisi ni binadamu,” alisema John.
“Mh!”
“Hakuna ndoa ambayo wanandoa hawatofautiani! Ni lazima hilo litokee, wanaonyesha ukamilifu wao kama binadamu. Inawezekana sisi tungekuwa malaika tusingekuwa na mambo kama hayo!” alisema John.
“Unamaanisha na wewe pia unaweza kusaliti?”
“Hahaha! Amanda! Kwenye ndoa usaliti upo, ila si unasaliti mpaka mwenzako anajua kwamba unamsaliti!” alisema John.
“Mh! Wanaume nyie!”
“Nisikilize Amanda! Mwanaume anaweza kusaliti na mke usijue, ila mwanamke anaposaliti anataka mwanaume wake ajue, huwa hamsaliti kwa kupenda, wakati mwingine mnafanya kwa makusudi kabisa, ili tujue, tuumie halafu muone tutafanya nini,” alisema John.
“Nyie wanaume si watu wa kuwaamini kabisa.”
“Ndiyo! Upo sahihi! Mimi mwenyewe sitaki uniamini tukiwa kwenye uhusiano!” alisema John.
“Kwa sababu gani?”