Simulizi: Baradhuli mwenye mikono ya chuma

Simulizi: Baradhuli mwenye mikono ya chuma

SURA YA ISHIRINI NA TANO:

Saa ya ukutani ilisema ni saa moja na nusu asubuhi, Mtemvu na inspekta Vitalis wakiketi sebuleni. Mezani kulikuwa na vikombe viwili vikubwa vilivyobebelea kahawa nyeusi ikifuka moshi. Pembeni kidogo ya vikombe hivyo kulikuwa na magazeti mawili yamejiweka hapo kana kwamba nayo yanafanya kikao.

Mtemvu alishika tama asionekane na dalili za kunywa wala kutaka kahawa. Inspekta alikuwa amekunja nne, mguu wake ulio juu akiutikisa tikisa kwa mbali. Taratibu yeye alikuwa anapeleka kahawa mdomoni akiinywa kwa tahadhari asiunguze mdomo.

“Yani sina amani kabisa. Nashindwa kufanya kazi zangu kwasababu ya kuwindwa mithili ya swala. Sijui nifanye nini?” Mtemvu alilalama akitikisa kichwa.

Inspekta alipeleka kwanza kahawa mdomoni ndipo akafungua kinywa;

“Usihofu, mkuu. Mimi nipo na nitajitahidi kadiri ya uwezo wangu kukuhakikishia usalama. Muda si mrefu nitawatia nguvuni kuna mipango nimekwishaipanga na nina uhakika lazima watanasa. Ninachokuomba tu ubaki nyumbani kwa majuma mawili. Yanatosha sana kumaliza kazi yangu.”

“Nitajitahidi kwa hilo, Inspekta. Sina mahala pa kwenda sasa tangu rafiki yangu pekee aliyekuwa amebakia, Pius, naye kuvamiwa na kuwawa.” Mtemvu alisema akiongezea:

“Ila nashukuru sana, Inspekta, hata hivyo unajitahidi sana. Naomba uwatie nguvuni hao watu haraka iwezekanavyo. Kuendelea kwao kuwa huru ni hatari kwa usalama wangu na wa watu wengine pia.”
“Ondoa shaka.” Inspekta Vitalis alisema kisha akanywa fundo moja la kahawa.
“Ila mkuu, nadhani huu ni wakati muafaka wa kunijuza kinaga ubaga kwanini mtoto wa rafiki yenu ahangaike kutaka kuwaua. Kuna nini kati yenu?” Inspekta Vitalis alidadisi.

Mtemvu alimtizama Inspekta alafu akajilazimisha kutabasamu. Kwa mara ya kwanza alinyanyua kikombe cha kahawa akanywa fundo moja.

“Sijajua kwanini. Mimi na baba yake tulikuwa marafiki mno tuliosaidiana kwa kila njia. Mpaka baba yake anakufa mie nilikuwa pembeni ya kitanda chake.”

Inspekta alitulia kwanza. Alikunywa mafundo matatu ya kahawa kisha akauliza:

“Unamkumbuka Jeniffer?”
Mtemvu akatikisa kichwa.
“Yes. Si yule mtoto wa K square aliyechora picha ya muhalifu?”
“Ndiye huyo.”
“Enhe …”
“Nilipata wasaa kidogo wa kuongea naye. Aliniambia muuaji kabla hajafanya mauaji, alidai amekuja kuchukua roho ya K square kama wao walivyoichukua roho ya baba yake, Malale. Unasemaje kuhusu hilo?”

Mtemvu alipaliwa na kahawa. Alikohoa kwa muda kidogo kusafisha koo lake kabla hajatia neno:

“Unajua vijana wa siku hizi sijui wamerukwa na akili. Sijui wanakula nini kinatibua bongo zao – nadhani ni bange tu. Miraji hajui aongeacho. Puuzia hayo maneno, fanya kazi yako. Umesikia Inspekta? Masikio hayalali njaa. Utasikia ya kila aina.”

Mtemvu alisema kwa mkazo kisha akanywa fundo la mwisho na kuaga anaelekea chumbani atarudi punde.

Inspekta alikunywa fundo moja akabinua mdomo wake akitikisa kichwa.

“Kuna kitu hakipo sawa.” Alisema na kuongezea:
“Ni lazima nijue.”

Muda mfupi mbele, Mtemvu alikuja akiwa amevalia suti wakaondoka na inspekta Vitalis kuelekea kituo cha polisi. Huko Mtemvu alikutana na Bernadetha aliyekuwa rumande, akaomba faragha apate kuongea naye.

“Unataka nini kwangu? Bado hujatosheka, sio?” Bernadetha aliongea kwa jazba.

Mtemvu alitabasamu akamwambia:
“Sijaja hapa kuzozana na wewe, Bernadetha. Ila nimekuja kukusaidia,”
“Wewe mwanahayawani unisaidie mimi?” Bernadetha alijikuta akitabasamu.
“Unataka kuonana na wanao, ama hutaki?” Mtemvu aliuliza. Bernadetha akamtizama kwa macho ya husda.
“Kama ukitaka kunijua mimi ni nani, gusa watoto wangu. Nitahakikisha nakuanika uchi hadharani!”
Mtemvu alitabasamu akitikisa kichwa.
“Nimekuambia sijaja kuzozana. Nataka nikuache uende ukakutane na familia yako. Hujammisi mwanao, Marietta? Je Miraji?”
Bernadetha alinyamaza kimya. Mara akaanza kulia.
“Shhh! Usilie. Nipo tayari kukupa nafasi nyingine ya kuonana nao.”
“Unataka nini, kwangu?” Bernadetha aliuliza. “Najua kuna kitu unataka, nini hiko?”
“Sasa hapo umeongea.” Mtemvu alisema akitikisa kichwa.
“Let us make a deal. Nakuachia huru ukaonane na wanao, ila kwa masharti mawili.”
Mtemvu aliweka kituo ameze mate, alafu akaendelea:
“Kwanza, ufunge mdomo wako kabisa. Sitaki kusikia unasema chochote kuhusu mimi na mumeo kwa yeyote yule. Pili, umwambie mwanao, Miraji, aache kunifuatilia, nami nitajitahidi kufanya sakata lake lipotee pasipo watu kugundua. La sivyo nitampotezea mbali kimya kimya. Tumekubaliana?”

Bernadetha hakujibu. Alimtizama Mtemvu na macho mekundu ya hasira.

“Tumekubaliana ama niondoke usiione familia yako milele?”

Bernadetha kimya. Mtemvu aligeuka akatishia anaondoka, mara Bernadetha akamuita.

“Sawa, nimekubali.”

Mtemvu akatabasamu na kuonya:
“Endapo utakiuka tulichokubaliana, nitakufanya kitu mbaya hutonisahau maishani mwako. Umesikia?”

Bernadetha hakujibu. Aliishia tu kumtizama Mtemvu kana kwamba anataka kummeza. Mtemvu alitabasamu akamuaga akimuahidi kutimiza walichoadhimia.

******

Muendelezo soma hapa
 
SURA YA ISHIRINI NA SITA

Ilikuwa inakaribia kumalizika majuma mawili tangu tukio la PWEZA LA VIDA lijiri na juma moja tokea Pius amekatwa pumzi. Vyombo vya habari viilivyokuwa havina habari mpya ya kuuza, viliendelea kujadili na kudadavua matukio hayo makubwa nchini kuwahi kutokea. Mbali na hapo kulikuwa tu tulivu, jiji la Dar es Salaam likielekea kutimiza majuma hayo bila mtu mwingine mzito kuaga dunia.

Ikiwa ni usiku wa saa nne, Mtemvu na mkewe: Mama Beatrice, walikuwa wanatizama marudio ya taarifa ya habari kwenye televisheni yao kubwa. Mama Beatrice alilala kwenye mapaja ya mumewe akijikunyata, Mtemvu akitizama simu yake mara kwa mara kana kwamba kuna kitu anategemea. Palikuwa tulivu usibashiri kama kuna jambo lolote linaweza kutokea kuharibu amani hiyo.

Dakika tatu mbele, nje ya nyumba ya Mtemvu kwa mbali kidogo, lilisogea gari wakashuka wanaume wawili wenye sura za kizungu wakibebelea mabegi migongoni. Walifuata uzio wa nyumba kwa tahadhari. Upesi walirusha kamba zao kutani wakapanda na kukata nyaya za umeme. Walidumbukia ndani ya uzio wakifikia kuchuchuma.

Simu ya Mtemvu iliita kamlio kadogo cha kushitua. Inspekta aliwabipu. Upesi Mtemvu na mkewe walitoka sebuleni wakakimbilia chumbani kujifungia. Ni kama vile ule mlio wa simu uliwaagiza wafanye hivyo.

Inspekta Vitalis alishuka kwenye mti mkubwa uliopakana na nyumba ya Mtemvu. Akatoa redio call akiongea;
“Kaa atensheni huko barabarani endapo watakimbia. Ova!”

Wakaonekana wanaume waliobebelea bunduki wakitapakaa barabarani umbali kidogo na nyumba ya Mtemvu.

“Sogea eneo la karibu, weka gari lao chini ya ulinzi. Ova!” Inspekta alitoa tena amri. Wanaume wengine watano wakatokea vichakani wakibebelea bunduki wakalizingira gari lililowaleta wavamizi.

Inspekta aliingia ndani ya uzio akisogea kuelekea ndani. Nyuma yake waliongezeka wanaume wawili wakimfuata lakini walijigawa, mmoja akaenda kushoto mwa nyumba mwingine akielekea kulia.

Wanaume wale wawili wenye sura za kizungu wakiwa koridoni wanajongea vyumbani, ghafula, walisikia vishindo nje nyumba. Walitizamana kitahadhari, mmoja wao akasema:
“Kuna watu nje. Tumeingia kwenye mtego, Miraji. Haukuwaua walinzi?”
“Hakukuwepo na mlinzi yeyote. Kibanda kilikuwa cheupe nikahisi labda watakuwa wametoka na tutamaliza kazi yetu haraka.”
“Umefanya uzembe, haiwezekani kukawa patupu. Watakuwa walijificha.”
“Sasa tunafanyaje. Hatuwezi tukapoteza nafasi hii tena.”
“Yes. Muda wa plan B.”

Haraka walichomoa mabomu mawili mabegini wakayapachika kutani wakiyaruhusu yasome tarakimu.

Mlango wa sebuleni ulifunguliwa akaingia inspekta Vitalis. Wanaume wale wawili wakasikia hilo. Wakati Inspekta anasogea kuja walipo, mmoja alilenga swichi kubwa ya umeme kwa risasi, umeme ukakata ndani ya nyumba kukawa giza totoro.

Vishindo vya miguu vilisikika vikitafutana milio ya risasi ikivuma. Sauti ya alarm ya bomu ililia kwanguvu, haraka inspekta Vitalis akarukia nje akipitia dirishani. Mabomu yalilipuka yakafanya nyumba iwe ghofu kufumba na kufumbua. Hakuna kilichobakia ndani.

Wanaume wale wawili wenye sura za kizungu walishatoka nje ya nyumba na tayari waliwamaliza wanaume wawili walioongozana na inspekta Vitalis. Walifuata ukuta haraka wapande, wasifanikiwe kumaliza, risasi ziliwalenga na kuwadondosha chini.

Mmoja alitulia kama aliyefariki tayari, mwingine akiugulia maumivu – alikuwa amejeruhiwa vibaya bega lake la kulia. Ila alinyanyua bunduki na mkono wa kushoto apambane. Kabla hajafyatua risasi, alijeruhiwa tena bega la kushoto akabaki analia kwa maumivu.

Inspekta alimsogelea karibu akamnyooshea mdomo wa bunduki, nyuma yake akiwa na wanaume wawili. Alivua sura bandia za mateka wao, akapata kuona sura ya Jombi na Miraji, Miraji akiwa yule mwanaume aliyetulia – mapigo yake ya moyo yalikuwa yanapiga kwa mbali akihema kwa kusita sita.

“Sali sala zako za mwisho.” Inspekta Vitalis alifoka akielekezea mdomo wa bunduki kwa Jombi.
“Usiniue, tafadhali. Usiniue!” Jombi alilia.
“Unaweza ukanipa sababu ya kuubakiza uhai wako?”
“Ndio!” Alisema Miraji na kuongezea; “Nitakuambia ukweli usiojua. Nitakuambia yule aliye nyuma ya mchezo huu.”

* MWISHO WA MSIMU WA KWANZA *

Kuanza msimu wa pili soma hapa
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom