***SURA YA AROBAINI NA SITA***
(MSIMU WA PILI)
*** SHETANI MPYA ***
Ilikuwa usiku wa saa mbili wakati Vitalis akiwa sebuleni anatizama taarifa ya habari runingani. Baada ya taarifa moja kukatiza ikiwa inaongelea ziara ya raisi wa Tanzania nchini China, ilifuatia taarifa iliyogutusha uso wa Vitalis. Aliona picha yake kwenye kioo cha runinga huku maelezo yakielezwa kama mshutumiwa nambari moja wa mauaji yaliyotukia ndani ya muda mfupi, waziri wa mambo ya nje na uhusiano wa kimataifa ameuwawa kwa kudidimiziwa kisu shingoni.
La haula!
Kitambulisho cha kazi cha Vitalis kilionyeshwa na kamanda wa kanda maalum akisema kwamba kimepatikana eneo la tukio. Na mtuhumiwa anashukiwa anaweza kuwa mhusika wa kundi linalotafutwa kwa udi na uvumba, WAGENI.
Vitalis alisimama akiwa ameshika kiuno na macho yake yakiwa yametoka nje. Alizunguka sebuleni kwa hatua kadhaa akienda na kurudi. Taarifa ya habari ilikuwa imepita na zingine zaendelea lakini kichwani kwake bado alikuwa anasikia jina lake kama mtuhumiwa wa kwanza kwenye mauaji ya mtu mkubwa serikalini.
“Nani kaniset kwenye haya mauaji? … Wametoa wapi kitambulisho changu? Ila si alikichukua OCD? …Kwanini waziri wa mambo ya nje?” Maswali yalimtafuna Vitalis.
Wakiwa kwenye kikao juu ya jambo hilo la mauaji, Bakari alitoa maono:
“Itatulazimu twende eneo la tukio, tunaweza tukapata jambo huko likatusaidia kusafisha jina lako kwa watu.”
“Ila unadhani itakuwa ni rahisi?” Jombi aliuliza, “Hilo eneo bila shaka litakuwa kwenye uangalizi mkubwa.”
“Si lazima tuingie eneoni.” Bakari alisema na kuongezea kwa kuuliza, “Kwani makazi ya marehemu ni wapi?”
“Msasani, ama tunaweza sema mpakani mwa Msasani na Oysterbay.” Vitalis alijibu. Bakari akavuta tanakilishi yake na kwenda kwenye ramani moja kwa moja, Vitalis akamuonyeshea makazi ya marehemu kwa kidole.
“Hapa!”
Bakari akatikisa kichwa, akavuta picha kwa ukaribu na kuitizama kwa umakini huku wenzake wakiwa wanamngojea aseme kitu.
“Tunaweza tukapata data.” Bakari alisema huku akihamisha macho yake toka kwenye tanakilishi mpaka usoni mwa Vitalis. “Pembeni kidogo ya jengo la makazi ya marehemu kuna duka kubwa la vifaa vya kisasa vya kompyuta.”
“Kwahiyo?” Miraji alidakia.
“Kwahiyo jengo kama hilo ni lazima tu litakuwa na kamera za ndani na nje. Tutatumia kamera za nje kutizama juu ya hilo tukio kwa kuzingatia muda wa tukio tuone kuna wageni gani walitembelea hapo muda mfupi kabla ya tukio.”
“Ni wazo zuri.” Sandra alichangia, “ila inabidi pia tufanye juhudi ya kuingia ndani, kuna mambo ambayo hatuweza kuyapata kwa kamera pekee.”
“Nitafanya hiyo kazi.” Vitalis alihakikisha, “Kazi hiyo kamera nitakuachia Bakari, Miraji na Jombi, najua hamtoniangusha.”
Saa nane mchana gari lililowabebelea Jombi, Bakari na Miraji lilitua kwenye kiwanja cha duka kubwa la vifaa vya tanakilishi. Wanaume walishuka wakiwa wamevalia ovaroli na kapero za bluu. Ndani ya dakika chache wakafika eneo la ulinzi, wakaketi kwenye viti nyuma ya tanakilishi zote za kamera baada ya kuwafunga wahusika midomo, mikono na miguu.
Bakari alirudisha video nyuma akaanza kuangalia yaliyotukia jana mida ya saa kumi ya jioni kwa mujibu wa kamera za nje zilizokuwa zinatizama jengo la marehemu waziri. Katika wasaa huo kwenye dakika za ishirini, wakaona gari aina ya Mark X nyeusi ikiwa inaingia ndani. Bakari alisimamisha video alafu akaivuta kwa ukaribu zaidi taratibu taratibu, akaandika chini namba za usajili na tarakimu: 25119-20, zilizokuwa zimeandikwa kwenye stika upande wa kushoto wa kibao cha usajili. Alijaribu kuvuta picha zaidi na zaidi lakini hakuona nyuso za waliomo ndani.
Baadae wakiwa ndani ya nyumba ya Vitalis, Bakari akaonyesha yale waliyoyapata. Vitalis aliweka karatasi ya nailoni mezani ndani yake kukiwa na risasi mbili na sigara kubwa.
“Haya ndiyo ambayo nimeweza kuyaokoteza ndani ya uzio wa nyumba ya marehemu.”
Bakari alishika karatasi ya nailoni akaipeleka machoni kwake kwa ukaribu. Aliitizama riboni kubwa nyeupe iliyoizunguka sigara ile kubwa, akasoma maandishi yaliyoandikwa hapo.
“Lugha gani hii?”
Kaguta alichukua huo ushahidi akausoma.
“Ni kiitaliano.” Alisema na kuongezea, “Imetengenezwa Italy, ni sigara ya watu wa daraja la juu.”
Bakari alipokea tena ushahidi huo akaupiga picha kisha akasogelea tanakilishi yake na kuiunganisha na kamera. Akatafuta majibu ya sigara mtandaoni.
“Hiyo sigara uliikuta wapi Vitalis?” Bernadetha aliuliza.
“Mlango wa kuingilia sebule ya marehemu.” Vitalis akajibu.
“Kwanini unadhani inaweza ikatusaidia?”
“Kwasababu naamini ni lazima itakuwa imeachwa na wauaji. Sidhani kama mwenye nyumba anaweza akavuta sigara na kuitupia mlangoni kwake.”
“Ni kutoka Italy!” Sauti ya Bakari ilipasua anga, wote wakamtizama. “Inatengenezwa Italy na inasafirishwa kwenda nchi chache sana Afrika. Wateja wake wengi wapo Ulaya na Marekani. Ni ghali mno, na ndio mana inachukuliwa kama ni ya watu wa tabaka la juu.”
“Kwahiyo kwa Tanzania inapatikana wapi?” Vitalis alidadisi.
“Kuna wakala mawili tu wanaouza hizo sigara kwa Dar es Salaam. Wote wapo Posta, wanauza pia na vinywaji vikali kama vile spirits, wines na whisky.”
“Nataka hayo maduka yafuatiliwe. Tupate majina ya wateja na makazi yao. Bakari, Jombi na Miraji, hiyo kazi naacha mikononi mwenu. Sandra na Kaguta nitawataka kesho muende msibani, Sandra, nitataka uwe karibu mno na mtoto mkubwa wa kiume wa marehemu, mchimbe unavyoweza. Najua tutapata kitu toka kwake. Naamini unaweza.”
Baada ya kupeana majukumu, walikula na kunywa. Kaguta na Sandra wakaondoka. Vitalis alitoka nje kuvuta hewa safi, Jombi akamfuata huko.
“Hatujapata muda wa kuongea tokea nimetoka maeneoni, mkuu.” Jombi alisema huku akitizama tizama mazingira. Vitalis alitabasamu akasema:
“Ni kweli.” Alivuta pumzi ndefu na matundu yake ya pua, akamgeukia Jombi.
“Naomba unipe mrejesho wa miradi. Inaendeleaje?”
“Inaendelea vyema tu. Baada ya kuwekeza pesa ile tuliyoikwapua kwa Isaac na Mr Wyne, imefufua na kuipa nguvu kubwa. Kwa sasa faida ni kubwa. Tunaweza tukafanya mambo yetu pasipo na shida kabisa.”
Vitalis akatabasamu.
“Hongera sana! Sasa tuna kazi moja tu ya kuusogeza huu mlima mbele yetu, baada ya hapo kila mtu akaishi maisha yake.”
“Tutaweza tu. Dhamira safi siku zote hushinda.” Jombi alikazia uzi.
Gari safi Toyota Rav4 modeli mpya rangi ya kijivu ilisimama kando kando ya uzio mkubwa wa nyumba ya marehemu waziri. Magari yalikuwa mengi mno watu pia. Sandra na Kaguta walishuka toka kwenye Rav4 wakiwa wamevalia nguo nyeusi na miwani ya rangi hiyo hiyo. Wakiwa wanaongozana wakaingia ndani na kuketi kwenye mojawapo ya viti vilivyokuwa vimetandazwa uwanja mzima. Shingo zao zilizungusha vichwa wakitizama kule na kule, Kaguta akamgusa Sandra.
“Yule pale.”
Alionyeshea kwa kutumia kichwa chake. Sandra akaelezea uso wake kule alipoonyeshewa, akamuona mwanaume mmoja mwenye uso mchanga wenye ndevu zilizojaa kidevuni.
“Anaitwa Morris. Ndiye tageti yetu.” Kaguta alieleza. Sandra akataka kunyanyuka, Kaguta akamzuia.
“Ngoja kwanza tusome mazingira.”
Waliendelea kutizama huku na kule. Kaguta akawaona wanaume wanne waliovalia suti na miwani zenye vioo vyeusi. Masikioni mwao walikuwa na viwaya vyeupe vilvyokuja mpaka mdomoni. Kazi yao ilikuwa kuperuzi peruzi huku na huko. Kaguta aliingiza mkono wake mfukoni akatoa miwani. Aliibinua akawatizama wanaume wale kwenye kioo akawaona kwa ukaribu zaidi, shingoni mwao walikuwa na tarakimu 25119-20.
“Utakapoenda, hakikisha unakuwa makini kuwatizama wale watu. Inaonekana wapo hapa kwa malengo fulani kinyume na ya kwetu.”
“Sawa.”
Sandra alinyanyuka akasogea mbele kidogo. Akasogea tena na tena kila alipoona walinzi hawamjali, mwishowe akamfikia Morris. Alimpa mkono wa kuume akisema:
“Pole sana, Morris.”
“Ahsante, nishapoa.” Morris aliitikia huku uso wake ukiwa umebebelea ka-wasiwasi.
“Samahani. Nakujua?” Morris aliuliza.
“Sidhani kama unanijua.” Sandra alijibu. “Ila mimi nakujua, wewe ni mtoto wa kwanza wa Mheshimiwa Johnson Machibya, aliyekuwa mfanyakazi mwenzangu kipindi tunafanya kazi pamoja ubalozini Australia. Ndani ya ofisi yake alikuwa ana picha kubwa ya familia yake, na huko ndipo nikaona uso wako, hata nilipokuona hapa nikakutambua.”
***
☆Steve