Simulizi: Baradhuli mwenye mikono ya chuma

Simulizi: Baradhuli mwenye mikono ya chuma

***SURA YA KUMI NA TATU***




(MSIMU WA 02)




Jua lilichomoza upande wake ule ule wa mashariki, watu wakaamka na kujiandaa kwenda makazini.


Juu ya kitanda cha Kaguta bado walikuwepo watu wawili wakiwa wamejilaza hawala hili wala lile. Nguo zilikuwa chini wao wakiwa uchi wa mnyama wamekumbatiana. Baada ya muda, Kaguta aliamka na kutizama saa yake ya ukutani, ilikuwa ni saa tatu yaelekea na nusu asubuhi.



“He! … Wewe Sandra, amka!”
Sandra alijivuta vuta kiulevi akamtizama Kaguta.
“Enh? …”
“Saa tatu na nusu hii!”



Sandra alitoa macho kama samaki majini. “Unasema? … Mungu wangu! … Mbona hukunamsha?”
“Mimi mwenyewe ndio naamka saa hii!”



Sandra alijitazama akashusha pumzi ndefu. “Hivi ulitumia kinga kweli?” Aliuliza. Kaguta akatikisa kichwa chake; “Hapana! Hatujatumia!”
“Mungu wangu! … Kwanini?”
“Sijui hata! … Mbona hukunikumbusha?”
“Mimi hata sikujielewa yani.”
“Pombe. Ile pombe tuliyokunywa ndio tatizo. Sasa itakuwaje?”
“Embu nipeleke ofisini kwanza.”



Walioga wakavaa. Kaguta alimpeleka Sandra nyumbani kwake akavaa wakaelekea ofisini. Mpaka wanafika ofisini ilikuwa ni saa tano ya asubuhi. Kaguta hakushuka wala kwenda kuwasalimia wakina Winner, alimpa Sandra salamu zake azifikishe huko, yeye akatembea kwenda nyumbani kwa inspekta.



Alipofika hakumkuta inspekta. Alipiga simu kumtafuta, inspekta akamuelekeza yupo kwenye canteen ya hospitali. Kaguta akaelekea huko na kumkuta inspekta akiwa na mama Miraji wanakunywa chai. Juu ya meza kulikuwa na tanakilishi mpakato ya inspekta.



“Karibu.”
“Ahsante, habari zenu?”
“Njema.”



Kaguta alikaa akaagiza chai, wakati anakunywa maongezi yalichukua nafasi.



“Jana hatukupata nafasi ya kuongea. Kuna mambo niliyapatakuyaona kwenye ile flash uliyoniletea nikaona si mbaya kumshirikisha na mama Miraji maana kuna mambo yanamhusu.”
“Ndio.” Kaguta aliitikia na kunywa fundo moja la chai.
“Wakati natizama tizama jana, niligundua kuna baadhi ya nyaraka ambazo zilimshirikisha mume wake, Mr Kim Salvatore, Mtemvu na wenzake kwa madhumuni ya biashara za magendo; kuteka na kusafirisha wanyama pori kwenda Italia. Kwa bahati nzuri, mikataba hiyo haikupata kutokea yani haikupata kutiwa sahihi na kutendeka. Kwa mujibu wa mama Miraji, mume wake alifanya kazi moja tu na hiyo ndio mwishoni iligundulika akauwawa.”
“Enhe…?”
“Sasa hapa ndio naanza kuunganisha doti … Naanza kupata kidogo mwanga kwanini Mr Kim alikuwa yupo nyuma ya mauaji ya Mtemvu pamoja na wenzake, yote ni kwasababu ya biashara walizokuwa wanafanya. Eidha walisalitiana ama kugeukana. Na kutokana na maelezo ya mama Miraji, mume wake hakusaini mkataba na Mr Kim, kwahiyo walikuwa wamemgeuka huyu bwana na hapo ndio ukawa mwisho wa biashara yao.”
“Aisee. Sasa tunafanyaje? … Unadhani tunaweza tukatumia nyaraka hizo kumtia Mr Kim nguvuni?”
“Hapana! Hizi haziwezi kutosha, zinaweza kukanushwa kiurahisi kwa kusema ni za kughushi. Ukiachana na hivyo, Mr Kim ni mtu mkubwa mno. Hatuwezi kumtia nguvuni kiurahisi.”
“Sasa tunafanyaje, Vitalis?”
“Inabidi tuwe waangalifu wakubwa mno. Mr Kim ana mtandao mpana mno kila sehemu. Ila itabidi twende Italy.”
“Italy!”
“Ndio. Ili tupate baadhi ya taarifa na vielelezo ni lazima twende huko. Kuna baadhi ya nyaraka hapa zinatuelekeza vizuri tu wapi pa kuanzia.”
“Haya, tutaenda. Ila barua ya maelezo utatuma wewe huko makaoni.”
“Haina shida. Ila unakumbuka kuhusu ile mipango ya mauaji kwenye zile barua?”
“Ndio!”
“Mojawapo ni leo. Umejiandaa?”
“Kujiandaa kivipi? … Anytime mimi niko ready. Alafu ndugu yangu, jana kuna mtu alikuwa ananifuatilia wakati nikiwa na yule binti wa kule Stationary. Alikuwa na pikipiki na ndiye jamaa anayetuma hizo barua za kifo, anaitwa Robinson.”
“Really?”
“Yap. Huyo demu niliyekuwa naye ameniambia huyo Robinson huwa hafikirii mara mbili kuua mtu. Na ndiye anahusika na usalama na usiri wa kampuni yao inayoitwa Mikmath yenye makao makuu posta mpya.”
“Siku ambayo mke na mtoto wangu waliuwawa, nilikuta nyayo za tairi za pikipiki kwenye uwanja wa nyumba.
“Bila shaka atakuwa ni huyo huyo.”
“Siku nitakayomkamata huyo mtu ataimba haleluya, ukweli nakuambia.”



Mama Miraji alitabasamu kidogo aliposikia hiyo kauli.



“Unadhani mama, nitamnyoosha kweli” Inspekta Vitalis alimwambia mama Miraji kwa msisitizo.
“Ila Vitalis.” Kaguta alidakia. “Kama nilivyokuambia kilichonitokea jana. Hudhani ni hatari kwa mama Miraji kuwa mbali na sisi labda? … ni mawazo tu.”
“Hapana, mimi nipo sawa tu.” Mama Miraji alisema kwa tabasamu kubwa.
“Kwangu mimi sidhanikama ni swala la usalama ndilo hoja, kumbuka mke wangu na mwanangu waliuwawa wakiwa palepale nyumbani pamoja na kuwa na askari.”
“Ni wazo tu.” Kaguta alisema kisha akanywa chai yake kama vile hakusema jambo. Mama Miraji na inspekta walitizamana kisha wakatabasamu.



Baada tu ya muda kidogo, inspekta na Kaguta walimuaga mama Miraji wakaondoka zao. Walielekea nyumbani kwao wakaweka silaha kwenye mkebe na kuvaa nguo za kazi. Inspekta alivalia traki nyeusi na shatinyekundu inayobana mwili. Kaguta alivalia traki ya kijivuna body nyeusi. Walijipaki kwenye gari wakaelekea mpaka maeneo ya Kawe, kama anwani ya mtu anayetakiwa kuuwawa inavyosema.



Walifika eneo husika wakaketi pembezoni kidogo mwa nyumba kubwa yenye uzio mpana. Macho yao yakiwa tenge na yaliyojaa tahadhari, walipepesa huku na huko mikononi mwao wakiwa wameshikilia bunduki.



Ghafla … Risasi tatu zilipiga kioo cha gari! Kaguta na inspekta waliinamisha vichwa vyao. Macho ya inspekta yalitizama kwenye sight mirror yakaona pikipiki mbili zinakuja kwa kasi kuwafuata. Upesi alimtizama Kaguta na kumuamuru;
“Endesha, wanakuja!”



Kaguta aliwasha gari na kuliondoa kwa kasi. Nyuma yao pikipiki ziliendelea kuwafuata huku risasi zikirindima. Walipofika konani, Inspekta alifunga mlango wa gari akatokea kwa chini akiwa amebebelea bunduki akamimina za haswa akiwalenga watu wawakimbizao, ndani ya sekunde tu chache wakawa wamewamaliza wale watu juu ya pikipiki, wote walikuwa chini.



“Sasa?” Kaguta aliuliza.
“Twende kwenye lile jengo tukamuone huyo aliyekuwa kwenye orodha ya kuwawa. Anaweza akatupa kitu juu ya Mr Kim.”
“Na vipi kuhusu hawa?”
“Wapigie simu polisi, waje wawabebe.”



Kaguta alivuta dashboard akatoa simu yake. Kabla hajapiga, namba mpaya ilijitokeza kwenye simu yake ikimpigia. Akapokea.
“Haloo!”
“Eeh … Al kareem, njoo upesi huku stationary, Robinson anampiga Sandra vibaya mno!”



Ilikuwa ni sauti ya Winner, mfanyakazi wa Rosemath stationary. Kabla Kaguta hajasema jambo, simu ilikata.



“Vipi tena?”



Inspekta aliuliza.



“Sandra, yule manzi wa kule stationary, anapigwa na Robinson!”
“Robinson?”
“Ndio!”
“Kwani Robinson hayupo pale chini?”
“Sidhani!”



Kaguta alisogeza gari kwa wale wanaume waliokuwa wamelala chini kwa kupigwa risasi wakashuka na kuwatazama.



“Hayupo Robinson hapa!” Kaguta aliduwaa.
“Tunafanya nini sasa?”
“Acha nikimbie huko stationary kukabiliana naye, we maliza hapa!”



Kaguta alikimbilia ndani ya gari akawasha na kutokomea. Ndani ya muda mfupi, magari ya polisi yalifika eneo la tukio, inspekta alitoa maelezo kisha akaelekea kwenye nyumba iliyokuwa inataka kushambuliwa, aligonga geti akamuonyesha mlinzi kitambulisho akimtaka aonane na mkuu wake.



Geti lilifunguliwa, inspekta akaingia na kukutana na mwenye nyumba. Mmama mmoja mnene kiasi mwenye mvi za kuhesabika kichwani. Waliketi kwenye viti vilvyo na meza yake bustanini wakapeana mikono;
“Karibu!”
“Ahsante. Naitwa inspekta Vitalis Byabata.” Inspekta alionyesha kitambulisho chake. “Bila shaka wewe ni bi Edna?”
“Ndio. Naitwa Edna Mshoke.”
“Nashukuru bi Edna. Nina maswali machache nataka kukuuliza, natumai nitapata majibu kutoka kwako.”
“Bila shaka inspekta, karibu. Lakini ningependa kujua hayo maswali yanahusu nini? Kampuni yangu, ama?”
“Ni kuhusu mahusiano yako na Mr Kim.”
“Mr Kim?”
“Yes.”
“Mr Kim Salvatore?”
“Exactly.”
“Okay. Unataka kujua nini, inspekta?”
“Wewe na Kim, mna mahusiano gani?”
“Mr Kim alikuwa business partner wangu. Kampuni yangu na yake zilikuwa kwenye ubia wa biashara.”
“Jina la kampuni yako?”
“Wonders Limited Company.”
“Na kampuni ya Mr Kim?”
“Mikmath Company.”
“Ubia wenu wa biashara ulikuwa unahusu nini?”
“Kampuni yangu inahusika na urembo wa wanawake. Kutengeneza lipstick, wanja, lipbam. Wigs, weaving na vitu kama hivyo. Mr Kim aliingia ubia na mimi wa kununua na kusambaza hizo bidhaa nje ya nchi kwa jina lake.”
“Kwanini atake kukuua?”
“Nani?”
“Kwanini Mr Kim atake kukua?”
“Umejuaje kama anataka kuniua?”
“Hujasikia milio ya risasi nje ya uzio wako?”
“Nimesikia.”
“Walikuwa ni watu wanaokuja hapa. Ni vijana wa Mr Kim. Kwanini anataka kukua?”



Bi Edna alishika kichwa chake akashusha pumzi ndefu. Alimtizama inspekta na macho yake ndani ya miwani akamwambia;
“Miezi michache ilyopita mimi na Mr Kim tulivunja mkataba. Sikutaka tena anunue bidhaa zangu, wala kuzisambaza kokote. Nlikuja kujua anachafua brand yangu kwa kutumia vitu vyangu kufanyia biashara yake haramu.”
“Biashara ipi?”




Kabla Bi Edna hajajibu, Ghafla milio miwili ya risasi ilivuma! Bi Edna alipiga kelele za maumivu, haraka inspekta aliingia chini ya meza risasi zingne zilizofululiza zikamkosa. Aliporusha macho yake juu ya uzio kutafuta risasi zinapotokea, alimuona mwanaume mwenye bunduki akiwa anachungulia, alikuwa ni Robinson.



Kufumba na kufumbua, Robinson alipotea, aliachia ukuta akadondoke huko nje. Haraka inspekta aliufuata ukuta akaurukia na kujidondoshea upande wa nje, alitazama kushoto na kulia akamuona Robinson akiwa anakimbia, naye akaanza kumfukuza kwa mbio pana.



Kila kona, inspekta aliibuka na Robinson. Kila uchochoro inspekta alizama na kuchomoza na mtu wake, hakumuacha hata chembe. Robinson alipiga kona za hapa na pale huku akijificha ficha kwenye miili ya wapita njia hali iliyomfanya inspekta ashindwe kutumia bunduki yake kumaliza kazi. Mara kwa mara, Robinson aligeuka na kufyatua risasi kumlenga inspekta lakini hakufanikiwa, risasi zilienda kombo ama kulenga watu wengine wasio na hatia.



Walipofika kwenye barabara ya lami, Robinsonalidandia daladalaaina ya DCM akaweka watu chini ya ulinzi na kumtaka dereva afuate maelekezo yake. Inspekta alikaa katikati ya barabara akasimamisha Noah, alipanda akaanza kufukuzia DCM iliyotekwa.



“Fasta, kanyaga mafutaa!” Robinson alimuamuru dereva huku macho na mkono wake wenye bunduki akiuelekezea kwa abiria. Dereva alikanyaga mafuta gari likazidi kupepea na kupepea. Nyuma yao, Noah alilomo inspekta nalo lilichochea moto kufukuza DCM.
“Haloo!” Robinson aliweka simu sikioni. “… Yes, nimeshamaliza kazi … nipo kwenye DCM la Kawe mbezi nakaribia kwenye kona ya kuelekea Mwenge … fanya fasta mwela ananikimbiza … yupo kwenye Noah nyeupe nyuma yangu … ”



DCM ilipofika konani kuelekea mwenge, yaliyotokea magari mawili kwa kasi nyuma ya Noah. Moja lilienda kushoto na lingine kulia, Noah likaekwa katikati. Gari lililokuwa upande wa kushoto lilibamiza kwanguvu Noah kwa ubapa, wakati Noah laenda kwa kasi upande wa kulia liliposukumiwa, gari lililokuwa upande wa kulia lilipiga breki kali na kuligusa tairi la Noah kidogo tu, Noah likapinduka na kubiringita mara mbili. Magari yale mawili yakapotea kwa kasi mno.



Mlango wa gari la Noah ulisukumwa na teke, inspekta akatoka nje akiwa anavuja damu kichwani, mkononi alikuwa kabebelea bunduki yake ndogo. Alitizama barabarani asione magari yale mawili wala DCM. Punde alianza kuhisi kizunguzungu akadondoka chini na kuzirai.



Macho ya inspekta yalipokuja kufunguka, alikuwa juu ya kitanda cha hospitali kichwani akiwa na bandeji kubwa. Aligeuza shingo yake kutizamapembeni akamuona Kaguta akiwa amesimama na daktari wanaongea lakini hakusikia nini kinaongelewa. Alifunga macho yake na kujaribu kukumbuka nini kilitokea, ghafla mpasuo wa maumivu ulipita kichwani kwake, akatoa sauti ya kulalamika. Kaguta na daktari wakamsogelea.



“Pole, inspekta.” Dokta alimwambia Vitalis.
“Ahsante.”
“Usihofu, ni jeraha la kawaida tu. Utarudi katika hali yako muda si mrefu. Kichwa kiligongwa kwanguvu.”
“Ahsante, daktari.”



Daktari alimeukia Kaguta akampa maelekezo; “Usimchoshe. Inabidi apumzike sana.” Kaguta aliitikia, daktari akaondoka na kuwaacha wawili.



“Pole, Vitalis.”
“Ahsante, nimeshapoa. Vipi kule ulipoenda?”



Kaguta alitikisa kichwa chake akasonya. “Hakuna kitu ndugu yangu. Sikukuta chochote.”



“Hukukuta chochote kivipi, Sandra hakuwepo?”
“Alikuwepo, ila Robinson hakuwepo. Nilivyouliza wakaniambia eti walikuwa wananipima.”



Inspekta alitikisa kichwa akatabasamu.



“Vipi, mbona umefurahi?”
“Tumeingizwa mkenge. Tumedanganywa na tukaingia kichwa kichwa. Robinson hakuwepo huko, Robinson alikuwepo kule uliponiacha na akatekeleza adhma yake ya kuua.”
“Ah! … Kweli tumepatikana.” Kaguta aling’ata kidole kwa kujilaumu.“Ilikuwaje sasa ukapata ajali, maana dokta kanambia ulipata ajali ya gari.”
“Ni wakati namkimbiza Robinson. Kuna magari mawili sijui yalitokea wapi yalipush gari nililokuwepo likapinduka.”
“Aisee! … Sandra na wenzake wanajikuta ni wajanja, sio?” Kaguta alijiuliza huku akitizama dirishani.
“You have to be careful, Kaguta. Huwezi jua wana mipango gani. Kumbuka, they are in the same team.”
“I am very sorry, Vitalis. I let you down.”
“Usihofu, tushukuru Mungu tupo wazima. Bado kazi yaweza kufanyika.”
“Ni kweli. Kuna kazi yoyote ya kufanya tena kule stationary?”
“Hapana. Kwa sasa cha kufanya ni kuwafuatilia wale watu waliokuwepo kwenye zile barua. Bahati mbaya tuliyempata kauwawa, alikuwa na taarifa nzuri na za muhimu sana.”
“Umepata taarifa gani?”
“Kuna kampuni inaitwa Wonders ya Bi Edna Mshoke inahusiana na bidhaa za wanawake, ilikuwa na mahusiano na kampuni ya Mr Kim. Lakini baadae walikata mahusiano kutokana na Mr Kim kuharibu brand ya Wonders kwa kufanya biashara haramu. Ila sijapata kujua hiyo biashara haramu ni ipi na ilikuwa inaharibuje brand ya Wonders kwani mwanamama huyo alipigwa risasi za kifua na Robinson akafa.”
“Umesema hiyo kampuni inaitwa Wonders?”
“Ndio.”
“Inatengeneza mawig na maweaving?”
“Ndio!”
“Dada yangu anafanya kazi hapo.”
“Kweli?”
“Ndio. Si unamjua Sarah?”
“Ndio.”
“Ndio huyo huyo!”
“Basi, anaweza akatusaidia kupata baadhi ya taarifa.”



Jioni ilipotinga, inspekta akiwa na bandeji yake kichwani aliongozana na Kaguta wakaenda hospitali kumuona Jombi. Walibeba chakula na maji makubwa. Walimjulia hali Jombi, wakaketi pembeni.



“Tumekuletea chakula, amka ule, kijana wangu.” Inspekta alisema huku akifungua mfuko aliokuja nao na kutoa hotpot la chakula. Jombi aliinuka akaketi kitako.



“Sasa hiki chakula kimepikwa na wanaume wenzako, kwahiyo unavyokula usianze kujudge judge sijui chumvi sijui mafuta … aah … aah!” Inspekta alitania wakacheka.



“Leo mama Miraji haji?” Jombi aliuliza.
“Hatujui, kwani huwa anakuja kila siku?” Inspekta aliuliza.
“Ndio, kila siku huwa anakuja.”
Ispekta alimsogezea hotpot Jombi akaanza kula.
“Mmmh … umepika wewe, inspekta?”
“Ndio, vipi?”
“Kitamu sana.”
Kaguta alicheka akapiga makofi; “Huwa hakosei huyu jamaa. Sijui kwanini alioa?”



Wote walicheka huo utani. Jombi alipiga matonge matatu, inspekta akaanza kuongea kiofisi;
“Jombi, kuna kitu kinanitatiza juu yako. Kwanini ulikuwa unawindwa uuwawe?”
“Siwezi kusema chochote, inspekta. Mimi ni mtu niliyefanya makosa, na nastahili kufungwa. Nilikuwa mtu muovu na mwenye kundi baya, nashangaa kwanini mnanijali kiasi hiki?”
“Usijali, Jombi. Sisi tuna dhumuni safi la kukusaidia. Ila hatuwezi kama hautotupa nafasi ya kufanya hivyo.” Inspekta alieleza.
“Natamani sana kusema na kujibu mnayouliza. Ila siwezi.” Jombi alisema na uso wake uliopoa.
“Tunajua ni kwasababu ya kiapo chako, si ndio?” Kaguta alimuuliza Jombi. Jombi alishtuka kidogo kusikia habari za kiapo.


***

☆Steve
 
****SURA YA KUMI NA NNE***


(MSIMU WA 02)







“Umejuaje kuhusu kiapo?”
“Wenzako wametuambia. Hawawezi kusema kitu kwasababu ya kiapo.”
“Ni kweli. Hatuwezi tukakiuka hilo. Tutakapofanya kinyume, ni kifo tu ndicho kitatuangamiza.”




Inspekta alimtizama Kaguta kisha akauliza;
“Ila Jombi, kwanini wenzako walikuwa wanakutafuta wakuue ingali wanajua ushakula kiapo na huwezi kufungua mdomo?”
“Hiyo ni kanuni. Mtu yeyote akikamatwa inabidi auwawe kabla hajasema chochote kwasababu …” Jombi alikatisha maneno. “Siwezi nikasema. Nitakufa.”



Inspekta alitikisa kichwa akamshika mkono Kaguta; “Tuondoke.”



Walinyanyuka Kaguta akainama na kumshika bega Jombi. “Ugua pole. Tutakuja kukuona siku nyingine.”




Waliondoka wakaelekea kwenye gari la Kaguta na kupanda.



“Tunaelekea wapi?”
“Kigamboni kwa Mr Bomba. Yule ambaye amepangiwa kuuwawa leo na Robinson. Leo ni kuchagua mawili, tumuokoe mtuhumiwa au tumkamate Robinson. Huyu ni mtu wa mwisho, Robinson akifanikiwa kumuua tutakuwa tumepoteza sana.”
“Usihofu, Vitalis. Tutamkamata.”



Kaguta aliondoa gari wakaanza safari ya kuelekea kigamboni. Walipofika kwenye nyumba husika, walishuka upesi na kuelekea ndani ya uzio wa nyumba. Walibisha hodi, lakini hakuna aliyeitikia. Kaguta alipiga mlango kwa teke kali, ukavunjika wakaingia ndani.




Walikuta mwili mwa mwanaume mnene mwenye kiwaraza ukiwa umejilaza chini panga pembeni, shingo imekatwa. Kabla hawajafanya chochote, ghafla, walisikia vishindo vya mtu nje ya nyumba. Haraka walitoka nje wakamuona mwanaume mmoja anakwea ukuta na kurukia nje ya uzio.




Kama upepo, inspekta na Kaguta walikimbilia ukuta na kuchumpia nje kama nyani. Kwa mbio zote walimfukuza yule mwanaume ambaye aligoma kabisa kugeuza shingo yake nyuma.




Inspekta alitoa bunduki yake akaifyatua kumlenga mwanaume yule mguuni mara mbili bila ya mafanikio. Kaguta alimpokonya inspekta bunduki akafyatua risasi kumlenga mguuni mwanaume wanayemkimbiza, akafanikiwa.




“Pumbavu!” Kaguta alipaza sauti. Huku akimnyooshea bunduki mwanaume aliyemlenga, walisonga karibu naye na kumuamuru aweke mikono juu. Walipomtizama waligundua ni Robinson.
“Oooh … Mr Robinson!” Kaguta alisema kama mtu atangazaye shughuli.
“Leo umeingia katika mikono yangu, mbwa wewe!” Inspekta alisema kwa hasira. Alimpiga teke kali Robinson tumboni. Kama hatoshi, alimpiga tena na tena. Kaguta alimtuliza inspekta akamsogeza kando.
“Utamuua sasa mapema yote hii!”




Walimnyanyua Robinson aliyekuwa anachechemea wakampeleka kwenye gari lao kisha wakaenda moja kwa moja kwenye jengo lao la mateso. Walimfungia Robinson mstimuni, miguu na mikono ikabanwa kwa kamba nene.



“Leo utaeleza kwanini popo hatagi?” Inspekta alitoa kitisho huku akivua shati lake na kubakia na kaushi, wakati huo Kaguta akiwa anatabasamu tu akimtizama inspekta.




Inspekta alimpiga ngumi Robinson mpaka akatoa damu mdomoni na puani. Inspekta akiwa anahema kwa kuchoka kurusha Makonde, simu yake iliita mfukoni. Ilkuwa ni namba private, alimuonyeshea Kaguta, Kaguta akapandisha mabega kuashiria hana la kusema. Inspekta alipokea akaweka simu sikioni.




“Haloo … eenh? … wewe! … “ Simu ilikata.
“Vipi?” Kaguta aliuliza.
“Wamemteka mama Mraji. Wapo nyumbani kwangu na wamesema niende na wewe pamoja na mtu wao.”




Inspekta na Kaguta wakiwa wanatizamana kwa mabumbuwazi, sauti ya kicheko ya Robinson iliwashtua.




“Mlidhani yanaisha, ndio kwanza yanaanza.” Robinson alisema kwa kebehi.
“Una uhakika wapo kweli na mama Miraji?” Kaguta alieleza shaka.
“Ndio! … Nimesikia sauti yake kabisa!”



Hakukuwa na jinsi, walimfungua Robinson wakampakiza garini na safari ikaanza ya kuelekea kwa inspekta.




“Sasa tunafanyaje, Vitalis?”
“Sijui hata. Kichwa kimegoma.”



Walifika nyumbani wakawakuta wanaume wanne mapande ya watu wakiwa wamemshikia bunduki mama Miraji. Robinson aliachiwa akaungana na wenzao, bunduki zikaelekezewa kwa inspekta na Kaguta.



“Tuna taarifa nzuri na mbaya kwenu. Taarifa nzuri kwenu ni kwamba, hatutowaua. Taarifa mbaya kwenu ni kwamba, kitu mlichokuwa mnakipinga na kukizuia, itabidi muungane nacho.” Alisema mwanaume mmoja mweusi kuliko wote.



“Sogea hapa, inspekta.” Mwanaume yule mweusi alimuamuru inspekta, inspekta akasogea kwa mwanaume mmoja aliyekuwa amekaa kwenye kochi. Mwanaume wa kochini akafunua mkono wa inspekta na kutoa mashine ya kuchora tattoo.
“Unataka kufanya nini?” Inspekta alipokonya mkono wake. Bunduki zikaelekezwa kwake.
“Toa mkono huo!” Amri ilitolewa. Inspekta hakutoa mkono wake. Bunduki ikaelekezwa kwa mama Miraji.
“Peleka huo mkono ama napasua kichwa cha huyu mama.”
Inspekta alirudisha mkono wake kwa mchoraji, mchoraji akaanza kazi yake. Alipomaliza, akafuatia Kaguta naye akachorwa tattoo. Tattoo zilipokamilika, upepo mkali ulipuliza watu wote wakadondoka chini.Ghafla giza lilitawala na Jitu likatokea! Mbele ya macho ya watu, jitu lilijigawa mara mbili na kuzama kwenye mikono ya Inspekta na Kaguta pale pale palipochorwa tattoo.




Zoezi hilo lilipokamilika, mwanga ulirudi ghafla. Inspekta na Kaguta walikuwa wamelala chini, hawakuwa na fahamu. Wale majambazi yalipeana ishara wakapotea lile eneo wakamuacha mama Miraji.




Mama Miraji aliisogelea mwili wa Kaguta na inspekta akilia. Aliita na kuita lakini wanaume hawakuamka. Walikuwa kimya, hata vifua vyao vilikuwa vinapanda na kushuka kwa mbali mno. Mama wa watu alikimbilia jikoni na kurudi na ndoo ya maji. Ajabu, hakuwakuta watu. Walikuwa wametokomea! Alitizama huku na kule asione chochote. Alifungua mlango akatoka nje ya nyumba akazunguka huku na huko asipate kuona kitu. Mwishowe alikaa chini akaanza kulia.



Katika ulimwengu mwingine mbali kabisa na ulimwengu wa nyama na damu, ndipo walipokuwepo inspekta na Kaguta. Kulikuwa ni kiza totoro. Inspekta na Kaguta walipeleka shingo zao kushoto na kulia lakini hawakuona chochote. Kwa mbali na ghafla, waliona mwanga wa moto. Bila ya kusemezana lolote na wakiwa kama watu wasiojitambua, walianza kusonga mbele kuufuata mwanga wa moto. Walipoufikia, walisimama na kusimamisha mikono yao ya kuume yenye tattoo wakasema kwa pamoja;




“Tumekuja hiji sisi tulio wapya. Tumekuja kula kiapo sisi tulio wapya. Tumekuja kujisalimisha sisi tulio wapya. Utuongoze na hekima yako. Utufunge mdomo na mioyo yetu tukapate kufanya kazi yetu vyema, kwa ufanisi na kwa siri.”




Baada ya kusema hayo, mwanga wa moto ulikuwa mkubwa ghafla na katikati yake akaonekana jitu la uteketezaji.Kufumba na kufumbua, jitu lilitoka kwenye moto na kuwazunguka haraka inspekta na Kaguta kisha likarudi motoni, mara mikono ya Kaguta na inspekta ikaanza kumwaga damu zikitoka eneo la tattoo. Wakati damu inamwagika wakawa wanaongea;




“Tunakula hiki kiapo kwa damu inayomwagika. Na tutakapokikiuka, tutaadhibiwa na damu inayomwagika mara nne zaidi!”




Maneno hayo yalipokoma, moto ulizima. Ghafla, inspekta na mwenzake walidondoka chini kama mizigo. Walipokuja kufungua macho walijikuta nje ya nyumba ya inspekta wakiwa uchi wa mnyama.




“Kaguta mbona upo uchi?” Inspekta alishangaa.
“He! Wewe je? … Hujioni?”




Walijitizama wakanyanyuka kukimbilia ndani, sebuleni walimkuta mama Miraji kalala kwenye kochi, haraka walifunga mlango wakatoka nje na kusogea mbali.




“Sasa tunafanyaje?” Kaguta aliuliza.
“Twende tupitie mlango wa nyuma!” Inspekta alishauri. Haraka walielekea nyuma ya nyumba wakafungua mlango na kuingia ndani.Walivaa nguo wakaketi juu ya kitanda.
“Tumekwisha, Vitalis. Hatuna ujanja tena!” Kaguta alilalamika huku akitikisa kichwa. Inspekta alishika tama, hakuwa na la kusema.
“Sasa tunafanyaje, Vitalis? … Tumeshawekwa chapa na kiapo tumekula. Sielewi hata ilikuwaje nikasema yale maneno.” Kaguta aliendelea kulalamika. Inspekta alikuwa kimya tu, kichwa chake kikibebwa na tama.
“Sasa mbona huongei, Vitalis?” Kaguta aling’aka.
“Sina hata cha kusema ndugu yangu. Sijui nitafanya nini sasa na tayari nieshaapa?
“Hapana! Inabidi tutafute cha kufanya, hatuwezi tukatulia tu hivi bila ya kuchukua hatua yoyote.”
“Kweli. Ila kwa sasa, nahisi kama kichwa changu kimepooza. Hakifikirii kabisa.”
“Najua. Lakini … ” Kaguta hakumalizia kauli yake mlango ukagongwa.
“Hodii! … Inspekta? Mpo ndani?”



Ilikuwa sauti ya mama Miraji. Inspekta na Kaguta walitazamana, Inspekta alinyanyuka na kuufuata mlango akafungua.



“Kumbe mpo ndani? … Mie nimewatafuta mpaka basi!” Mama Miraji alitanabahi kwa mshangao.
“Nakuja huko sebuleni muda si mrefu, mama.” Inspekta aliongea kwa upole. Mama Miraji alishika njia akaelekea sebuleni. Baada ya muda mfupi, inspekta pamoja na Kaguta wakaja sebuleni.
“Hao majambazi walikukamatia wapi?” Inspekta alimuuliza mama Miraji.
“Wakati natoka nyumbani, nilipotoka tu mlangoni lilikuja gari moja kwa kasi likasimama mbele yangu, walishuka wanaume watatu wakanikamata na kuniingiza garini wakanileta kwako.”
“Pole sana.” Inspekta alimpoza mama Miraji.
“Nimeshapoa. Ila nimeshindwa kuelewa, kwanini wale watu wamewachora tattoo mikononi? … Ilikuwa ina maana gani wao kunikamata ili tu wawachore nyie?” Mama Miraji aliuliza.
“Kusema ukweli hizi tattoo walizotuchora ni agano la kuwa katika kundi lao. Hawa majambazi ukiachana na kwamba shughuli zao hutumia mwili wa nyama, kuna ulimwengu wa kiroho unaowaongoza na kuhakikisha hawatoi siri za kazi zao, wala mkubwa wao.




Hiyo roho ili ipate kuingia kwenye mwili wa binadamu, lazima achore tattoo na ale kiapo cha damu. Atakapogeuka kiapo hiko, damu yake lazima imwagike, na inamwagika zaidi.” Inspekta alielezea. Mama Miraji akaachama mdomo kwa kushangaa.




“Kwani mmekula kiapo? … Si mmechorwa tu?”
“Tumekula na kiapo!” Kaguta alijibu.
“Saa ngapi?”
“Hatujui ni saa ngapi. Ila ninachokumbuka, ghaflatulitokea kwenye ulimwengu tusioufahamu. Kulikuwa ni giza na huko ndipo tulipokula kiapo. Sijui hapa tumefikaje, tulijikuta nje ya nyumba tena tukiwa uchi wa mnyama.” Inspekta alifafanua. Mama Miraji akazidi kuachama mdomo mithili ya pango.
“Mweh! … Baba sasa itakuaje?” Mama Miraji aliuliza huku akitumbua macho yake kama vile mtu aliyekabwa na tonge.
“Ila mimi sina hofu.” Kaguta alisema, mama Miraji na inspekta wakamtizama. “Mimi naona hii tattoo inadhuru pale tu mtu anapojaribu kutoa siri na si vinginevyo. Hakuna haja ya kuhofia.” Kaguta alidadavua.
“Una uhakika gani kama haina madhara kwa upande mwingine?” Inspekta aliuliza.
“Sidhani. Si unakumbuka Jombi mwenyewe alikuwa anataka kuuwawa na wenzake? … Sasa kama ingekuwa ni ishu ya tattoo wangewezaje kumdhuru au kutaka kumuua mwenzao? … ” Kaguta alimwaga maneno. Inspekta alifikiria kisha akatabasamu.
“You are right! … Sidhani kama itatuzuia kufanya kazi yetu.” Inspekta alikenua wakagongeshana mikono na Kaguta. Baada ya muda mama Miraji akaaga anataka kwenda nyumbani. Kabla hajaondoka, Kaguta alimuita inspekta pembeni wakateta jambo;
“Vitalis, hivi mpaka huyu mama afe ndio uone anahitaji kuwa na wewe? … Watamuua huyu nakuambia. We kaa naye si atalala hata vyumba vingine. Atakapokuja kufa utalalamika? … Utajilaumu kwasababu kwa njia moja ama nyingine utakuwa responsible for her death. Take this key kama utataka kumsindikiza.” Kaguta alisema kwa mkazo.
“Lakini, Kaguta … ”
“Lakini nini? … Sitokuambia tena hili swala.” Kaguta alisema kisha akaondoka zake kurudi sebuleni. Baadae kidogo, inspekta naye akaja sebuleni na kumtaka mama Miraji aongozane nayekwenda nje. Mama Miraji alimuaga Kaguta akatoka nje kuungana na inspekta aliyekuwa ameingia ndani ya gari la Kaguta. Alipoingia tu garini, inspekta aliwasha gari wakatoka lile eneo.
“Nataka kukupeleka ukamchukue mwanao huko shuleni.”
“Hatuendi nyumbani?”
“Tunaenda, ila nataka leo uhamie kwangu, wewe pamoja na mwanao.”
“Unasema?”
“Nataka uhamie kwangu, wewe pamoja na mwanao.”
“Kwanini?”
“Kwasababu ya usalama wenu. Si salama kukaa peke yako kwako.”
“Ila inspekta huoni kama … ”
“Sioni chochote. Nataka uwe karibu na mimi hapo tu ndipo nitahisi upo salama. Ntajitahidi kwa nguvu na akili zangu zote kukuhakikishia usalama. Sitaruhusu nifanye kosa lingine kama lile nililolifanya kwa mke na mtoto wangu.”
“Jamani inspekta … ”
“Nakuomba. Nakuomba uhamie kwangu. Sitasamehe nafsi yangu endapo utapata tatizo na sikufanya juhudi yoyote kukusaidia.”




Mama Miraji hakutia tena neno. Alihamishia macho yake nje akawa anatizama tu miti inavyokimbia. Kwa muda kidogo palikuwa kimya asiwepo wa kuongea. Baada ya muda, inspekta aliomba maelekezo kuelekeaa shule kumchukua Marietta. Walielekea huko wakamtwaa mtoto kisha wakaenda nyumbani kwa mama Miraji walipochukua baadhi ya nguo na kurudi kwa inspekta.





Siku iliyofuata ikiwa ni asubuhi ya saa mbili, Kaguta na inspekta waliongozana wakaenda kwa Sarah. Bahati mbaya hawakumkuta mwenyeji wao. Waliita na kubisha hodi lakini hawakupata majibu yoyote. Kaguta alitoa simu yake mfukoni akapiga.




“Sister upo wapi? … Mie nipo nyumbani kwako hapa … Ok, nakungoja basi.”





Alikata simu akamtizama inspekta; “Tumngojee anakuja muda si mrefu. Ametoka kidogo.” Inspekta alitikisa kichwa chake kwa masikitiko; “Sasa wewe kwanini hukumpigia tokea tupo nyumbani?”
“Nilisahau. Alafu nilijua nitamkuta coz hatokagi tokagi.”
“We mume wake mpaka ujue ratiba yake? … Umefanya mistake, tungoje tu.”




Punde Sarah akaonekana kwa mbali. Kaguta alimshtua inspekta na kumuonyeshea kule atokako Sarah.




“Yule anakuja, si nilikuambia anakuja sasa hivi?”
“Ndio yule mwenye hips nene?”
“Acha mambo yako basi, we umeona hips tu?”
“Aisee! … Ana vipisto!”
“Acha basi!”
“Eeeh … Wewe inakuuma enh? Lakini dada za wenzako … aah! aah!”




Sarah alipofika alimkumbatia kaka yake akawakaribisha wageni ndani, aliwaletea vinywaji wanavyotaka wakaketi na kuanza kuongea.




“Huyu anaitwa Sarah, ni mdogo wangu. Sarah huyu anaitwa Vitalis ni mfanyakazi mwenzangu.” Kaguta alitambulisha, Sarah na Vitalis wakapeana mikono punde tu Kaguta akawaachanisha.
“Inatosha!”




Inspekta na Sarah wakacheka. “Hujaacha tu wivu kwa dada yako?” Sarah alisema huku akitabasamu.



“Sasa anakushika muda mrefu hivyo?”
“Jamani, muda mrefu wapi?” Sarah alisema inspekta akadakia, “Mie mwenyewe nashangaa!”




Baada ya kutaniana kwa muda kidogo, walianza kuongelea mambo yaliyowaleta.



“Sarah, bado unafanya kazi kule Wonders?” Kaguta aliuliza.
“Hapana. Niliacha kitambo tu.”
“Kwanini uliacha?”
“Walikuwa wanazingua. Kwa muda mrefu tu hatukulipwa pesa zetu, nikaamua kusepa mie.”
“Kwanini hamkuwa mnalipwa?” Inspekta aliuliza.
“Kusema ukweli sijui. Ila kuna watu walikuwa wanasema kwamba yule mmama wa kampuni alikuwa kaiuza kampuni kwa mdosho fulani hivi ambaye alishindwa kuiendesha.”
“Mmmh … Ujue nilikutana na huyo mama anayemiliki hiyo kampuni, bi Edna. Akaniambia kwamba kampuni yake ilikuwa imeingia mkataba na mfanyabiashara fulani hivi mkubwa. Lakini akaja kuvunja mkataba baada ya kuona huyo mfanyabiashara anaharibu brand yake kwa kufanya biashara haramu. Ni kweli hayo?"
“Mmmh ... labda inaweza ikawa kweli. Ujue kuna kipindi fulani hivi kuna watu walikuwa wanatuletea vtu fulani hivi kama unga unga tuviweke kwenye masidiria, mawigi na maweaving. Tukimaliza wanachukua na kuweka kwenye mikoba yao wanaondoka. Wengine walikuwa wanasema eti ni madawa ya kulevya, lakini mie sina uhakika na hilo. Na huyo mama huyo bi Edna, mbona na yeye ndio alikuwa anakuja kila siku na kutuambia kwamba tufunge midomo yetu tusiseme chochote popote pale.”
Kaguta na inspekta walitizamana, inspekta akaguna.
“Kwahiyo bi Edna alikuwa anaunga mkono hiko kilichokuwa kinafanyika, sio?”
“Eeeh … Ndio!”
“Mlikuwa mnalipwa kiasi gani? Na mliacha lini kuweka hayo mavitu kwenye masidiria na hayo manywele?”
“Wakati tunaweka hayo maunga tulikuwa tunalipwa vizuri kweli, na ndio hapo nikajenga na hii nyumba mnayoiona. Ila baada tu ya kuacha hiyo kazi, ndio tukaanza kutokulipwa mpaka nikaondoka.”
“Sasa wewe mbona hukunambia?” Kaguta aliuliza.
“Si nimesema kwamba hatukutakiwa kusema lolote.” Sarah alijibu.
“Inaelekea kuna kitu bi Edna na mfanyabiashara mwenzake walikwaruzana.” Inspekta aliongea kama vile mtu mwenye uhakika. Sarah akadakia; “Ni kweli, maana ni ghafla tu lile zoezi lilikatizwa na hatukuliona tena. Alafu, nasikia yule mama kauwawa, tena yeye pamoja na kaimu wake.”
“Kaimu wake? … Yupoje?”
“Mbaba fulani hivi mnene mnene ana bonge la kibaraza kichwani.”
Inspekta alikunja sura akamtizama Kaguta.
“Kuna haja ya kwenda kwa yule mbaba?”
“Yupi?”
“Yule tuliyemkuta kauwawa. Ndio huyu ambaye Sarah anamuongelea.”
“Okay. Mie nipo tayari.”




Walinyanyuka wakaaga. Sarah aliwasindikiza mpaka nje ya nyumba, wanaume wakapanda gari na kuondoka kuelekea kwa yule mzee kaimu wa Wonders Limited.




***

☆Steve
 
***SURA YA KUMI NA TANO***



(MSIMU WA 02)





Ila wakiwa njiani, simu ya inspekta iliita. Alikuwa ni mama Miraji anampigia, inspekta alipokea akaiweka sikioni;
“Haloo … Enh? … Upo sehemu gani? …. Haya sawa nakuja sasa hivi … Hakikisha haukai sehemu yoyote peke yako …”



Simu ikakata.



“Vipi, kuna nini tena?”
“Mama Miraji! … Anasema kuna mtu anamfuatilia kwa nyuma tokea anampeleka mtoto shule! … Embu geuza haraka twende!”
“Wapi?”
“Mbele ya St Marry mbezi beach.”




Haraka gari liligeuzwa na kuanza kwenda Mbezi beach kwa mwendokasi mkali. Wakiwa wamekaribia kufika, inspekta alimpigia simu mama Miraji amuelekeze alipo, mama Miraji akafanya hvyo na ndani ya dakika Kaguta na inspekta wakawa wameshafika mbele ya mama Miraji.



“Yuko wapi?” Inspekta aliuliza kwa jazba.
“Yulee! … Yulee anakimbia! … Anakimbia!” Alikuwa ni mwanaume mwembamba aliyevalia suti. Aliwapa wakina inspekta mgongo huku akikimbia kwa kasi.
“Ingia kwenye gari, haraka!” Inspekta alimuamuru mama Miraji. Mama Miraji aliingia kwenye gari, gari likaondolewa kwa kasi kumfukuzia yule mwanaume akimbiaye. Yule mwanaume alipoona gari lamsogelea aliacha njia kuu akashika vichochoro.




Gari lilisimama kwa breki kali, inspekta akashuka na kuanza kumkimbiza mwanaume yule kwa kasi mno. Ndani ya sekunde chache, inspekta akawa tayari amemkaribia yule mwanaume, alimshika koti akamvuta akampa ngumi nzito ikampeleka mwanaume yule chini na kumvujisha damu puani.





“Wewe nani?” Inspekta aliwaka. Mwanaume yule hakujibu, badala yake alitabasamu na kumuonyesha inspekta ishara ya kidole cha kati. Inspekta alighafirika, alikunja mikono ya shati lake na kuacha tattoo yake wazi, mwanaume yule akaiona. Inspekta alimnyanyua mwanaume yule juu juu kwa staili ya kumkwida. Ajabu mwanaume yule hakuonyesha kupinga lolote, badala yake alipeleka mkono wake ndani ya suruali akawa anakunja na kunyoosha vidole kama mtu ajikunaye.





Ghafla, inspekta alimuacha mwanaume yule na kushika kichwa chake akilalamika maumivu. Mwanaume yule hakukoma, aliendeleza zoezi lake huku akionyeshwa kufurahishwa na ile hali aipitiayo inspekta ya kulalamika kichwa. Baada ya muda, inspekta alidondoka chini akapoteza fahamu. Mwanaume yule akapotea.




“Mbona harudi?” Mama Miraji aliingiliwa na hofu, Kaguta alishuka garini akaenda kumtafuta inspekta. Baada ya dakika kumi alimpata inspekta akiwa amelala hajielewi. Alimuita lakini hakuitika. Alimnyanyua akampeleka garini.
“Mungu wangu! Amefanya nini?” Mama Miraji aliuliza macho yakimtoka.
“Sijui! Tumuwahishe hospitali.”




Gari liliondoshwa kwa kasi na Kaguta kuelekea hospitalini. Inspekta akafanyiwa vipimo, daktari akawapasha majibu hakuna kitu chochote kikubwa alichopata kuona, labda tu mgonjwa alikuwa na uchovu wa jua kali. Kaguta na mama Miraji wakashangazwa na hayo majibu. Walingoja inspekta aamke warushe mashaka yao kwa njia ya maswali. Ikiwa lisaa limepita ndipo inspekta akaamka akirudi fahamuni.





“Vitalis, nini shida?” Kaguta alirusha swali, mama Miraji naye akaonyesha shauku kubwa la kutaka kufahamu.




Inspekta alishika kichwa chake akakunja sura. Macho yalikuwa yamemlegea akionekana kutawaliwa na uchovu. Alimtizama mama Miraji kisha akayarudisha macho yake kwa Kaguta.




“Kichwa kinaniuma.”
“Pole sana, inspekta.” Mama Miraji alisabahi.
“Vipi kwani ilikuaje?” Kaguta aliuliza.
“Sijui hata ilikuaje! … Wakati napambana na yule jamaa kichwa kilianza kuniuma ghafla kwa maumivu makali.” Inspekta alieleza, “Nilishangaa, badala ya yule adui kujilinda na kushambulia, alipeleka mkono wake ndani ya suruali hapo hapo kichwa kikaanza kunikata.”




Kaguta akaguna.




“Uliona alichokuwa anakifanya huko?”
“Hapana. Nashindwa kuelewa ni sayansi gani ilitumika. Tokea nianze mapambano na hawa watu sijawahi kukumbana na kitu kama hiki.”



Walitulia kwa muda kidogo wakifikiria Kaguta akalipuka na wazo; “Tattoo. Itakuwa ni tattoo.”
“Tattoo kivipi?” Inspekta aliuliza huku akirembua.
“Sijui kivipi, ila kwa njia moja ama nyingine itakuwa inahusiana na agano la mchoro.”




Baada ya masaa matatu ya kupumzika na kurudi kwenye hali yake ya kawaida, inspekta akiongozana na Miraji walielekea hospitalini kukutana na Jombi wakiwa wamebebelea chakula vya wagonjwa. Inspekta alimueleza Jombi kila kilichotokea, Jombi akaguna na kumtizama inspekta kwa jicho la mshangao.





“Inspekta, umechorwa tattoo?”
Inspekta na Kaguta wakatazamana.
“Ndio, tumechorwa wote wawili.” Inspekta alijibu na kuuliza, “Umejuaje?”




Jombi akatikisa kichwa chake kusikitika, “hilo huwa linatokea kwa wale tu wanaokuwa na tattoo hiyo. Unapokula kiapo maana yake unaridhia kufanya kazi ya mkuu kwa pamoja. Yeyote anayekuwa na hiyo tattoo hana uwezo wa kumshambulia mwenzake.





Endapo yule anayeshambuliwa atakapokuna au kukwangua sehemu ya tattoo na kufanya ichuruze damu, mshambuliaji atapata matatizo kama hayo yaliyokukuta wewe ukafikia hiyo hali.”




Inspekta aliweka mikono kichwani, “Mungu wangu. Sasa tunafanyaje?”
“Hapo kusema ukweli sijajua.” Jombi alijibu kwa sauti yenye lafudhi ya kukata tamaa, akauliza. “Wamewachora eneo gani?”
“Mkononi.” Kaguta aliwahi kujibu.
“Mkononi? … Kwanini?”
“Hatujui, kwani kuna utofauti wowote?” Kaguta aliuliza kwa pupa.
“Ndio. Kuna utofauti. Kuna wengine huchorwa kiunoni kama sisi, it means tupo grade ya pili. Walio juu yetu wao huchorwa mgongoni. Na wa juu zaidi, wanakuwa na tattoo shingoni.”
“Kwahiyo wewe ungepanda grade inayofuata wangekufuta hiyo ya kiunoni? Au?” Inspekta alipeleleza.
“Hapana, siwezi kufutwa. Hizi tattoo milele hazitoki. Na milele mimi nitabakia grade ya pili. Ni hivi, mtu wa grade ya kwanza ambao ni nyie wanaochorwa mkononi, wao huwa wamelazimishwa, si kwa matakwa yao. Grade ya pili, wanakuwa wameridhia kufanya kazi wakijua matokea yake. Grade ya tatu, ni wale wanaowafunda wote wa chini. Grade ya nne na ya mwisho, ni waanzilishi ama waasisi, mfano Mr Kim.”
“Umewezaje kusema hayo yote na ni ya siri?” Inspekta alidadisi.
“Si siri tena kwenu. Nyie mmekuwa wenzetu, kuwataarifu nyie si kuvujisha siri kwa kuwa nyie wenye agano ndio vinywa vyenu vimeuliza.”
“Naomba nirudie swali, Jombi. Kwanini wewe walitaka kukuua na ingali una tattoo huwezi kutoa siri?”




Jombi alitabasamu kwanza ndio akajibu, “Hiyo ni kawaida. Mtu anapokamatwa na kuwa chini ya adui, sharti auwawe, kwani akishatoa siri haijalishi tu ataangamizwa, bali siri inakuwa si siri tena.”





“Unatushauri tufanye nini sasa, Jombi?” Kaguta akauliza.
“Kama habari yenu ya kuwa na tattoo itakuwa imesambaa kote, hamtokuwa na la kufanya. Lakini kama sio, mnaweza mkaendelea na shughuli zenu. Ila ninachowashauri, kwa sasa inabidi msipige matawi ya miti, anzeni mizizi.”
“Kumaanisha?” Inspekta alidakia.
“Kumaanisha kwamba, nyie mnapambana na matawi ya miti lakini hamtafuti mizizi. Hamuwezi mkawamaliza wafuasi wa Mr Kim nchi hii, kila siku wanazalishwa wapya huko sehemu wanapopewa training. Inabidi muangamize kwanza hivyo viwanda, mengine ndio yafuate.”
“Unaweza ukatutajia hizo sehemu?” Inspekta aliuliza.
“Ndio, naweza nikawatajia. Ila sizifahamu zote, nitakutajia baadhi lakini mkae mkijua zipo kila mkoa wa Tanzania zikiendeshwa kwa siri mno. Kumbukeni hamuwezi mkaripoti hiki kitu popote pale, mkifanya hivyo utakuwa ni mwisho wenu.”
“Sawa. Nina swali la mwisho kwako.” Inspekta alisema.
“Uliza tu.”
“Ni kumhusu yule jitu. Mbona kwa sasa hapatikani? … Yani sioni wala sisikii akifanya mambo yake kama alivyokuwa akiwaendesha wakina Mtemvu. Kwanini watu wa Mr Kim wahangaike ingali jitu yupo?”




Jombi alishusha pumzi ndefu akajitengenezea kitako. Akamtizama inspekta.




“Kwanza awali ya yote, hakuna mtu awezaye kupambana na yule jinni. Ana nguvu mno na akidhamiriacho hakuna budi kutokea. Ila anaendeshwa, na anayemuendesha hupokea amri kutoka kwa mkuu juu ya nini cha kufanya. Mtu anayemuendesha huyo jinni anaishi Bagamoyo, anaitwa Alwatan Kombo, ni mzee maarufu sana ukimuulizia humkosi. Hayo mengine sifahamu.” Jombi alifunguka. Inspekta akaguna,
“Kazi ipo. Sijui hata tunaanzia wapi?”
“Popote pale.” Kaguta alitoa jibu jepesi.
“Ila kama mtahitaji, mnaweza mkaningoja. Tabibu amesema kesho nitaruhusiwa. Naomba niwarudishie fadhila kwa kuwasaidia.”



Inspekta alimtizama Kaguta, Kaguta akawahi kujibu; “Sawa, tutakungoja.”



Maongezi hayo yalipokoma, Kaguta aliwataka inspekta na mama Miraji waende kupumzisha akili zao ufukweni mwa bahari kwa kuwa ni mwisho wa wiki. Mama Miraji akapinga;



“Mimi siwezi, namsubiria mwanangu atoke shule.”
“Oooh! … Haina shida. Mpaka Jombi amalize kula muda muda utakuwa umeshawasili, tutamchukua mwanao alafu twende wote tukasahau ya ulimwengu kidogo.”



Mama Miraji akatabasamu, “Sawa, haina shida.”



Jombi alikula akamaliza, walimpitia pia Miraji kumjulia hali baada ya hapo wakaenda kumchukua Marietta shuleni akabadili nguo wakaelekea ufukweni mwa bahari ya indi. Ndani ya hoteli ya White sand ndimo walipokuwepo. Walipata chakula, kisha wakaenda jilaza kwenye vitanda vyembamba virefu vya ufukweni upepo ukiwa unawapuliza na simuliza za hapa na pale zikipigwa.



“Twendeni tukaogelee!” Inspekta alipendekeza.
“Tutaendaje sasa na hatujaja hata na nguo ya kuogelea?” Mama Miraji alisema, alikuwa amevalia suruali pana na top miguuni akiwa kavalia viatu vya wazi. Inspekta alikuwa amevaa pensi na tisheti jepesi wakati Kaguta akiwa kavalia bukta fupi juu ya magoti. Marietta alikuwa kavalia katop keupe na taiti nyeusi.
“Twende basi hata tukachezee maji tutoe kanuksi.” Inspekta alizidi kushawishi.
“Nyie tangulieni, nakuja.”
“Aaah jamani twendeni bana.” Kaguta alichochea.
“Kweli, nyie tangulieni naja.” Mama Miraji alisisitizia. Inspekta alinyanyuka pamoja na Kaguta, Inspekta akamnyooshea mkono Marietta, mtoto wa mwisho wa mama Miraji.
“Twendee!”
Marietta alimtizama mama yake kama mtu aombaye ruksa, mama akamruhusu aende. Inspekta alimnyanyua mtoto akamuweka mabegani wakayafuata maji. Wakiwa pamoja na Kaguta walichezea chezea maji kwa kurushiana rushiana.



Marietta alikimbia huku na huko wakifukuzana na inspekta. Walirushiana maji, wakalala kwenye michanga na kwenda tena kuoga. Mama Miraji alikuwa amekaa tu akiwatizama tabasamu likitambalia uso wake.



“Twende kwenye maji marefu!” Inspekta alimwambia Marietta huku akitabasamu.
“Akaa naogopa!”
“Kwanini?”
“Si n’tazama!”
“We ulishawahi kumuona mtu anazama?”
“Ndio! Tena kuleee!” Marietta alionyeshea kidole upande wake wa mashariki.
“Leo unaendaaa…!” Inspekta alisema kwa utani, Marietta akaanza kukimbia. Hao wakaanza kufukuzana huku na kule, “Njooo!”
“Sitakiii!”



Inspekta alimkamata Marietta akaanza kumrusha rusha juu juu. Wakiwa katika hilo zoezi, haraka Kaguta alikuja akitokea kwenye maji ya marefu alipokuwa anaoga.



“Vitalis, umeona kule?” Kaguta alielekezea uso wake kule alipokuwa amekaa mama Miraji. Inspekta alitizama akamuona mwanaume amejilaza juu ya kitanda alichokuwa amelala yeye.
“Nani yule?”
“Sijui! Nenda katizame.”



Inspekta alianza kusogea eneo la tukio mtoto akiwa kambebelea mgongoni. Macho yake alikuwa kayarusha kule aendapo akijitahidi kung’amua akionacho.



“Unaenda kumchukua mama?”
“Eeeh na yeye aje kucheza na sisi. Au hutaki?”
“Nataka. Alafu tukimchukua tunaenda kenye maji makubwa?”
“Ndio. Tunaenda kuleee kwa bluu.”
“Kule kwenye maboti?”
“Enhee huko huko!”
“Wewe huogopi?”
“Siogopi mimi.”
“Unajua kuogelea?”



Inspekta alikaa kimya, akili yake ilitekwa kidogo na kumtizama mwanaume aliyekuwa ameketi na mama Miraji kwani alikuwa tayari amekaribia na bado hajamng’amua ni nani hasa.



“Unajua kuogelea? Mbona hunijibu!” Marietta alipaza sauti yakekumuuliza inspekta.
“Eeeh najua kuogelea.” Inspekta alijibu huku akimtua Marietta ambaye moja kwa moja alimfuata mamaye.
“Habari yako?” Inspekta alimsalimu mwanaume yule aliyejilaza; alikuwa na kifua kilichotuna kwa kiasi chake wakati tumbo lake likiwa limepambwa na matuta. Nywele zake ndefu alizitia dawa zikawa zinameta meta.
“Njema tu, vipi?”
“Shwari. Unaweza ukanambia wewe ni nani?”



Mwanaume yule alitabasamu kidogo akalamba lips zake.



“Naitwa Hervey. Au unaweza ukaniita the handsome African. Vipi kwani?”
“Hapo unafanya nini?”
“Nimechil tu na mrembo hapa, kuna ubaya?”
“Wewe kuwa na adabu …” Mama Miraji aliingilia kati, inspekta akamtuliza na kuendelea kuongea na yule jamaa.
“Umechil ukiwa unataka kufanya nini?”
“Aaah bro, maswali gani hayo? Unauliza nini sasa?”
“Jibu swali langu.”
“Kwani vipi kaka?” Mwanaume yule alisimama. “Wewe ni bahasha wake nini huyu manzi. Mbona maswali ya kijinga jinga, si unasema tu unaeleweka.”



Inspekta alimtandika kofi la nguvu mwanaume yule akadondoka chini.



“Potea hapa!”
Mwanaume yule alinyanyuka kwa hasira akamtizama inspekta.
“Hivi wewe unanijua mi nani?” Alifoka huku akimfuata inspekta. Alirusha ngumi, inspekta akaidaka na kuiviringita kisha akamsukuma, mwanaume yule akadondoka chini.
“Ngoja sasa nikuonyeshe. Nisubirie hapo kama wewe mwanaume kweli.” Alisema mwanaume yule huku akitokomea. Inspekta alitikisa kichwa chake akamgeukia mama Miraji,
“Vipi upo sawa?”
“Nipo fresh tu. Alikuwa ananisumbua sumbua tu huyo mtu.”
“Pole sana. Twende basi tukatembee tembee hapa naona tumeshageuka kideo.”



Mama Miraji alinyanyuka na mwanae wakaongozana kuelekea kule alipo Kaguta. Inspekta alimbeba Marietta mabegani, mkono wake wa kulia akiwa amemshikilia mama Miraji. Kaguta alitoka kwenye maji akaungana nao, ila aliona jambo;
“Vitalis, kuna watu kama vile wanakufuata.”



Inspekta aligeuza shingo akaona wanaume wanne, mmoja wapo akiwa yule mwanaume aliyemzaba kofi. Inspekta alimshusha mtoto chini, akamtaka mama Miraji akae nyuma yake.



“Wakina nani hao?”
“Yule fala aliyekuwa amekaa na mama Miraji, kaenda kuita wenzake.”
“Wanataka nini?”
“Wanataka kuvunjwa vunjwa.”



Kaguta alitabasamu akaweka mkono wake kifuani mwa inspekta, “Niachie mimi. Sijanyoosha viungo muda kidogo.” Alisema kisha akasogea mbele kukutana na wanaume wale wanne.



“Tunaweza tukawasaidia?”
“Wewe nani wa kutuuliza hivyo? … Tunamtaka huyo mbwa mwenzako. Au amekutuma wewe umsaidie?” Mwanaume yula aliyezabwa kofi alitema cheche.



“Kwa ushauri tu wa bure. Kimbieni angali mnaweza.” Kaguta alisema huku akikuna kichwa chake. Wanaume wale walitizamana, mmoja akarusha teke, Kaguta alidaka kisha akammanua mwanaume yule na kupiga sehemu zake za siri kwanguvu, kamlio ka mbwa koko kakasikika … “Uuuuuu!” Wakati mwanaume yule akidondokea chini huku akiugulia. Mwaume mwingine alirusha ngumi, Kaguta naye akarusha ngumi zikakutana kwanguvu. Jamaa aliyerusha ngumi naye akatoa sauti yake kilio huku akiugulia kwa kuuning’iniza mkono wake mpaka chini alipodondokea.



Mwingine alinyanyua mguu akilenga kurusha teke lakini kabla halijafika popote, Kaguta alirudisha teke hilo kwa teke lake kama mtu anayesinya taka kisha akatoa teke lake sasa matata ambalo lilimkumba mwanaume yule kifuani akarukia kwenye maji. Sasa akabakia yule aliyeenda kuita wenzake.



“Njoo basi fasta, sina muda wa kupoteza.” Kaguta alimwambia yule mwanaume. Yule mwanaume akataka kukimbia, Kaguta alimshika akamvuta.
“Niliwaambia mkimbie wakati mnaweza.”



Mwanaume alirusha ngumi, Kaguta akarudisha uso wake nyuma ngumi ikavuka alafu akafunguka na ngumi yake kali iliyotua kwenye uso wa mwanaume yule na kumdondosha chini. Mwanaume aliyevunjwa mkono alinyanyuka, Kaguta akamrudisha chini na teke la kichwa lililomziraisha mlengwa.




“Vitalis, mbona umenipa visharobaro hivi havina hata changamoto!”
Inspekta alitabasamu; “Si uliwataka mwenyewe.” Muda huo watu walikuwa wamejazana wakitizama. Waliamua waondoke zao kufuata gari wakaondoka hilo eneo na kuelekea nyumbani.




Siku iliyofuata, ilikuwa tulivu na labda ilikuwa inatofautiana na jana yake kwa tarehe tu. Ila inspekta na Kaguta waliamka wakiwa tayari wamedhamiria kuifanya iwe ya pekee. Walimbeba Marietta wakampeleka shule, baada ya hapo wakaelekea hospitali na kumtwaa Jombi safari ikaanza kuelekea bagamoyo kwa Alwatan Kombo.





Baada ya lisaa na madakika kadhaa wakawa tayari wameshatia miguu yao ndani yabagamoyo. Walishuka garini wakaanza kumuulizia mzee Alwatan Kombo.




“Mmmh yule mzee amekwisha hama pale. Saa hii anakaa kuleeee … unapaona kulee!” Muelekezaji alionyesha kidole chake kisiwani. “Kule ndipo anakaa.”
“Kisiwani?” Inspekta alishangaa.
“Ndio, kisiwani. Nyie nendeni pale kwa wale wavuvi wanaweza wakawapeleka huko.”




Kaguta, Jombi na inspekta walishika njia wakaelekea huko walipoelekezwa. Walipowafikia wavuvi, inspekta akaelezea haja. Wavuvi walikuwa watano, wote waliacha kazi zao wakawatizama wageni.




“Hatuwezi kuwapeleka huko!”
“Kwanini?” Kaguta aliuliza.
“We jua hivyo, hatuendi.” Alijibu mvuvi mmoja kwa niaba kisha wakaendelea na kazi zao. Wengine wakipara samaki zao walizovua usiku, wengine wakitengenezea nyavu wapate kuanza safari.



Wakina inspekta walitizamana wakajadili cha kufanya, Kaguta akapata wazo;
“Tuwatajie pesa ya maana, watakubali tu.”
Wakakubaliana.
“Mnataka shilingi ngapi kutupeleka?” Kaguta alichombeza.
“Tumesema hatutaki. Hatuendi sisi huko! … Kha!” Aling’aka mvuvi mmoja kisha zogo likazuka miongoni mwao,
“Hawa jamaa vipi, wanataka wakatutoe kafara nini? … Nani aende kufa huko?”
“Nashangaa. Japo maisha magumu, hatutaki kufa.”
Wakina inspekta walitizamana kwa nyuso za maswali.
“Jamani kwani kuna nini huko?” Kaguta aliuliza. Inspekta akapandisha mabega yake juu. Jombi akabinua mdomo wake. Kaguta aliwageukia wavuvi akawashawishi tena;
“Kuna elfu hamsini hapa kwa atakayetupeleka.”



Wavuvi wanne wakaendelea kung’aka kwamba hawataki hata kwa pesa gani. Mmoja akasema;
“Twendeni. Ila tunawashusha na kugeuza papo hapo!” Wenzao wakamshangaa;
“We Bakari wewe wataka makubwa?”



Mvuvi yule hakujali, aliwapandisha wakina inspekta na safari ya kuelekea kisiwani ikaanza. Baada ya dakika ishirini, walifika. Mvuvi aliwashusha akadai pesa yake, Kaguta akampatia. Mvuvi alipogeuka apande mtumbwi wake alishangaa kuuona umesogea kwenda mbali kama vile kuna mtu ameusogeza.



****

☆Steve
 
mkuu endeleza basi

Ahsante mkuu nitashukuru maana dah nahofia kuitesa nafsi ya moyo Wangu kutaka kitu kisichowezekana

Kila ukiingia unaongea hivyo

Story safi napata na pickup lines basi mubashara kabisa.

Dah story nzuri sana haichoshi kuisoma

Asee Mkuu, endelezea mzigo. Inazidi kunoga haswaa.

Haichoshi kuisoma. Thanks Steve
Nimeiendeleza maradufu (mara tatu). Karibuni jamvini.
 
Hebu nisaidieni jamani.maana ya mubashara ni nini?naona nalisikiasikia tu humu mitandaoni.Mimi nipo vijijini huku
 
Hebu nisaidieni jamani.maana ya mubashara ni nini?naona nalisikiasikia tu humu mitandaoni.Mimi nipo vijijini huku
Kwa Mujibu wa BAKITA (Baraza Kuu la Kiswahili la Taifa) MUBASHARA maana yake ni TUKIO linalotokea na kupewa airtime na chombo cha habari.

Mfano: matangazo ya mpira, baadhi ya matukio kama pale Ikulu, n.k.

Kama upo na mpenzi wako kitandani, mnafanya yenu, hapo neno MUBASHARA haliwezi kutumika kwa vile hakuna chombo cha Habari kilichofanya live coverage.

Mtu akishuhudia ajali kwa macho yake, au tukio lolote lile, bado sio sahihi kusema MUBASHARA.

Ili iwe MUBASHARA, lazima chombo cha habari kihusike!
 
mbona umepotea hivi au ni hyo avatar uliyochange inanivuruga mzee wa fursa umelikimbia kwa nn
Labda Avatar inakuvuruga mamaa. Jukwaa lile nimeshindwa kulihimili. Hhaha! Mambo mazito alafu hamuonyeshi ushirikiano.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom