Shairi

Shairi

Mokes Junior

Member
Joined
Aug 20, 2022
Posts
7
Reaction score
0
CHINI YA MPARACHICHI.

1 Kivuli chake kitamu, mfaidi hafaidi
parachichi zake tamu, wengine wanafaidi
matunda yake ni sumu, tiba yao makuadi
Chini ya mparachichi, nadondokewa na mawe.

2 Matunda yakikomaa, mzee huwa mkali
unaweza kulemaa, ukimwambia ukweli
maisha ya ujamaa, yalishakwenda na meli
Chini ya mparachichi, nadondokewa na mawe.

3 Sifa zake naskia, matunda wakisifia
wanadai yavutia, matamu kuyabugia
mdomoni kuyatia, sijawahi ambulia
Chini ya mparachichi, nadondokewa na mawe.

4 Majaniye kudondoka, taka taka kuongeza
fagio wenye mashaka, kusafisha naumiza
maneno nayo sadaka, ukweli unajiweza
Chini ya mparachichi, nadondokewa na mawe.

5 Anajali marafiki, wanae kutudhihaki
hataki tukate keki, rafiki hababaiki
watoto twalia dhiki, lawama hazikwepeki
Chini ya mparachichi, nadondokewa na mawe.

6 Mkweli hawezi dumu, daima kumdhulumu
ukweli hatari sumu, darasa bila kalamu
kushindia vuta ndumu, daima kosa nidhamu
Chini ya mparachichi, nadondokewa na mawe.

7 Urithi wetu shakani, hatuoni ahueni
uhuru wetu shambani, unasubiri hisani
hakuna kwenda sokoni, mfadhili mlangoni
Chini ya mparachichi, nadondokewa na mawe.

8 Barafu siyo kinywaji, hata ukila hushibi
tunataabika maji, nyumbani shamba la bibi
tunashindwa pata uji, kelele zenu kinubi
Chini ya mparachichi, nadondokewa na mawe.
 
Back
Top Bottom