Serikali kubana mali za mafisadi

BabuK

JF-Expert Member
Jul 30, 2008
1,845
329
SERIKALI imependekeza bungeni kutunga sheria inayotaka mali za watuhumiwa wa wizi na ufisadi kufilisiwa mara mtuhumiwa anapotoroka au akifariki dunia wakati kesi yake ikiendelea kusikilizwa mahakamani.

Mapendekezo hayo yamo katika Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali uliosomwa jana bungeni mjini hapa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema.

Muswada huo una sheria nane zinazotakiwa kufanyiwa marekebisho na Bunge.

Marekebisho hayo yalielezwa na Jaji Werema kuwa sheria ya sasa haitoi fursa kwa Mahakama
mtuhumiwa anapotoroka au anapofariki dunia kutoa amri ya kufilisi mali zake.

Katika eneo hilo, pia Jaji Werema alisema inapendekezwa Mahakama itoe amri ya kuzuia mtuhumiwa wa ufisadi wakati kesi yake ikiendelea kugawa mali au kuihamisha sehemu nyingine.

Alifafanua kuwa sheria hiyo inaelekeza namna Mahakama itakavyoteua msimamizi wa mali za
mtuhumiwa ambazo zitazuiwa na Mahakama wakati kesi itakapokuwa inasikilizwa.

Mwanasheria Mkuu alisema lengo la marekebisho hayo ni kuipa Mahakama mamlaka ya
kutaifisha mali iwapo mtuhumiwa anayepelelezwa atafariki dunia au kutoroka.

Alisema sheria hizo zimewasilishwa bungeni ili kutimiza mikataba ya Umoja wa Mataifa kuwa
watuhumiwa wa ufisadi wasifaidike na mali wanazopata zikitokana na vitendo vya ufisadi.

Sheria nyingine ambayo Jaji Werema alitaka Bunge liifanyie marekebisho ni ya Makosa ya
Usalama Barabarani, ambapo inatungwa sheria inayopendekeza kuwapo utaratibu wa leseni za
udereva kupewa alama maalumu kwa namba na mwenye leseni anapotenda kosa alama zipunguzwe na zikiisha hatimaye anyang’anywe leseni.

Lakini pia Serikali imewasilisha marekebisho ya Sheria ya Uhujumu Uchumi katika eneo la
dawa za kulevya, ambapo inapendekeza wafanyabiashara, wauzaji na watumiaji wafungwe maisha jela.

Katika sheria hiyo, pia inapendekezwa wamiliki wa nyumba na magari vinavyokamatwa vikiwa
vimehifadhi au kusafirisha dawa za kulevya nao wafungwe maisha.

Pia marekebisho mengine yatakayofanywa ni katika sheria ya ushahidi kuwa utaratibu wa
kutoa maelezo ya shahidi mahakamani ambaye hakupatikana na kutoa ushahidi wake ili yatumike kama ushahidi.

Wabunge wapinga
Lakini katika michango yao, wabunge walipinga mapendekezo hayo ya Serikali ya kutunga sheria ya kutaifisha mali za mtuhumiwa wa ufisadi, kubadilisha sheria ya usalama barabarani na ya uhujumu uchumi.

Pingamizi la kwanza lilitoka kwenye Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba, Sheria na
Utawala ambayo ilitaka Serikali iangalie kwa makini suala la leseni za udereva, kwa anayefanya
makosa pointi ziwe zinapunguzwa na Mahakama kwani wakiachiwa polisi linaweza kuchochea
rushwa.

Akisoma ushauri wa Kamati hiyo, Mjumbe John Lwanji, alisema Polisi ni eneo linalolalamikiwa
na wananchi kukithiri kwa rushwa, hivyo kuwaachia askari wapunguze hizo alama, ni
kuwawekea mradi wa rushwa.

Kamati pia ilishauri Waziri mwenye dhamana aweke kanuni na taratibu za wazi zinazoelekeza
aina ya makosa yatakayosababisha alama kupunguzwa kwenye leseni ya dereva.

Pia Kamati ilipinga mshitakiwa wa ufisadi ambaye kesi yake inaendelea anapofariki dunia
mali zake zitaifishwe na wakalitaka Bunge lirejee Katiba ya nchi ambayo inatoa misingi ya haki na kupiga marufuku mtu aliyeshitakiwa na kosa la jinai kuhesabika kuwa mkosaji kabla ya kutiwa hatiani.

Lwanji alisema Kamati inashauri mapendekezo hayo yaondolewe na sheria hiyo iangaliwe
upya, kwani yanaikiuka misingi ya haki, kwa kuwa kwa mujibu wa sheria, ushahidi kwenye
masuala ya jinai ni kwa anayeshitaki kuthibitisha pasipo shaka.

Mbunge wa Viti Maalumu, Faharia Shomari (CCM), alipinga eneo la mali ya mtu aliyekufa
wakati kesi yake inaendelea mahakamani kufilisiwa na kuonya kuwa hali hiyo inaweza kufanya
dhuluma kutendwa na vyombo vya sheria.

Shomari alisema warithi wa mali hizo hawatatendewa haki kwani hawajui kama mali hizo
mzazi wao alizipata kwa wizi.

“Suala hili liangaliwe upya, kwani linakiuka sheria za nchi,” alisema Shomari.

Mbunge wa Ubungo, John Mnyika (Chadema) alisema sheria za usalama barabarani ni nzuri,
tatizo ni askari ambao wamepewa dhamana ya kuilinda, kuendekeza rushwa.

“Tatizo la msingi hapa ni rushwa iliyokithiri barabarani, mfumo huu ni mkondo mwingine wa
rushwa, kwani hapa hatushughuliki na mzizi wa tatizo,” alisema Mnyika.

Kwa upande wa mali kufilisiwa, Mnyika alihoji ni mfumo gani utawekwa ili kulinda mali za
mtuhumiwa mara zinapokuwa zinashikiliwa na Mahakama wakati kesi yake ikiendelea kusikilizwa.

Mbunge wa Viti Maalumu, Pindi Chana (CCM) aliunga mkono askari kutopewa jukumu la kushughulikia alama za kuondolewa kwenye leseni badala yake kazi hiyo ifanywe na Mahakama.

Pia alipinga mali za mtuhumiwa wa ufisadi anayefariki dunia wakati kesi yake ikiendelea
kusikilizwa kutaifishwa, kwa maelezo kuwa wanawake ndio watapata shida zaidi iwapo
waume zao watafariki dunia na mali zao kutaifishwa.

Mbunge wa Mbulu, Mustafa Akoonay (Chadema), alisema kutokana na urasimu mahakamani, watuhumiwa wengi wanafariki dunia wakiwa gerezani wakati kesi zao zikiendelea kusikilizwa, hivyo kupitisha sheria ya kutaifisha mali zao ni kutowatendea haki.

Wapinzani nao wakataa
Ikichangia Muswada huo Kambi ya upinzani ilisema kuongeza adhabu za vifungo kwa watuhumiwa wa dawa za kulevya hakuwezi kumaliza au kupunguza tatizo hilo nchini badala yake Serikali iondoe uozo wa rushwa uliokithiri mahakamani.

Akisoma maoni ya Kambi ya Upinzani, Mbunge wa Viti Maalumu, Raya Ibrahimu alisema
kutokana na rushwa mahakamani ndiyo maana watuhumiwa wengi wanakamatwa lakini
wanaofungwa ni wachache.

Alisema pia kuwa takwimu kutoka Tume ya Kudhibiti Dawa za Kulevya inaonesha kuwa
watuhumiwa wanaokamatwa na dawa hizo idadi yao imepungua, lakini idadi ya dawa zinazoingizwa nchini inazidi kuongezeka.

Raya alisema takwimu zilizotolewa na T ume hiyo zinathibitisha kuwa mahakamani ndiko
kuna tatizo kubwa linalofanya biashara hiyo izidi kuongezeka kwani wanaoshitakiwa hawafungwi.

Vifungu vyaondolewa
Katika hatua nyingine, Serikali iliondoa bungeni vifungu vya marekebisho ya sheria mbalimbali vilivyokuwa vinahusu Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu ili kutoa fursa kwa wadau kutoa maoni yao na kuboresha zaidi muswada huo.

Mwanasheria Mkuu Jaji Werema alisema lengo ni kuhusisha wadau wote. “Muda mwafaka ukifika tutawasilisha sheria hii katika kikao kingine cha Bunge,” alisema Werema.

Sambamba na kuondolewa kwa kifungu hicho, Werema pia alisema kutokana na uamuzi
huo, vipengele vingine vya sheria ambayo vimeondolewa kwenye sheria hiyo ni Sheria ya Mafao ya Watumishi wa Mashirika ya Umma, Sheria ya Mafao ya Watumishi wa Serikali za Mitaa, Sheria ya Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii, Sheria ya Mamlaka ya Mapato Tanzania na Sheria ya Usajili wa Shughuli za Biashara.

Werema alisema sheria hizo zilizoondolewa zinamlenga mwanafunzi wa elimu ya juu anayepata mkopo kutoka Bodi ya Mikopo.
 
Naona hapa serikali ina mpango wa kuwapiga pini Rostam na Lowasa maana Rostam alishaanza kujiandaa kukimbia nchi maana tayari ameshaanza kuhamishia pesa zake Malaysia na kwingineko.
 
Zilipendwa...Mbona hata kukimbia hawakimbii lakini hakuna chochote kilichofanyika!
 
Ni blah blah za kawaida. Hivi tuna sheria ngapi za kuwabana mafisadi lakini hazitekelezwi ipasavyo. Niko hapoa Bungeni, leo nimesikiliza wenyeviti wa kama tatuz za mambo ya fedha, Zitto, Cheyo na Mrema. Kila mmoja amelalamikia wizi mkubwa wa mali ya umma, Mrema anasema ripoti za CAG zinakuwa na ushahidi wote kuhusiana na wizi huo, lakini si DPP, takukuru wala polisi wanaojihangaisha kuchukua hatua, na hata pale hatua zinapocukuliwa, upelelezi unaweza kuchukua miaka zaidi ya kumi, huku watuhumiwa wakiendelea kupokea mshahara kutoka serikalini
 
Naona hapa serikali ina mpango wa kuwapiga pini Rostam na Lowasa maana Rostam alishaanza kujiandaa kukimbia nchi maana tayari ameshaanza kuhamishia pesa zake Malaysia na kwingineko.
Ufisadi wa Rostam unajulikana kwa muda mrefu.Kama wameshindwa kumkamata hakiwa hapa nchini sasa hivi ni kitu gani kitawabadilisha waende kumkamata Malaysia siku zijazo?
 
Na hao wezi/fisadi watakaa kusubiri hayo marekebisho ya sheria hizo wasihamishe mali zao?
 
Kama mali zao zinaingiza income kwa familia zao , ukizibana ni kukosesha hao wanacnhi ajira
 
Back
Top Bottom