Shitambala aanza kuwananga CHADEMA
Na Charles Mwakipesile, Mbeya
ALIYEKUWA Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasi na Maendeleo (CHADEMA) mkaoni Mbeya ambaye sasa amejiunga na CCM, Bw. Sambwee Shitambala
ametangaza kuibomoa ngome ya chama chake za zamani mkoani Mbeya Mbele ya Mjumbe wa Kudumu wa Kamati Kuu, Dkt. John Malecela huku akitamba kuwa kwa kadri alivyokijenga chama hicho ndivyo atavyokibomoa kwa mikono yake mwenyewe.
Alisema kuwa anathamini kwa sehemu kubwa heshima aliyopewa na uongozi wa chama ukiongozwa na Rais Kikwete, baada ya kuamua mwenyewe kujiunga na chama hicho kutokana na usaliti anaodai alifanyiwa na uongozi wa CHEDEMA.
Alisema kuwa viongozi hao badala ya kufanya kazi kwa maslahi yao wamekuwa wakifanya kazi kwa ajili ya kutafuta umaarufu wao wenyewe.
Alisema wakati akiwa katika chama hicho walikuwa wakifanya kampeni kwa kutangaza wazi kuwa wakiingia madarakani watahakikisha kuwa wanaendesha nchi katika hali ya amani na utulivu, lengo likiwa ni kuwaunganisha Watanzania na kujipatia maendeleo yao wenyewe pasipo kufanya vurugu hali ambayo alisema kuwa imekuwa tofauti na makubaliano hayo.
Bw. Shitambala alisema kuwa kutokana na kuwa mpiganaji na msomi wa sheria alishangaa kuona viongozi hao ambao wengi wao ameshiriki kuwapa ubunge wakigeuza ajenda na kuamua kuanzisha maandamano nchi nzima na kutoka nje bungeni wakati Rais Kikwete akihutubia hali ambayo alisema ni utovu mkubwa wa nidhamu.
"Hatukukubaliana kufanya maandamano ya kuvunja amani wala hatukuwatuma waende wakatoke bungeni na kisha kurudi ukumbini kwa kujadili hotuba ya rais, nawaambia ndugu zangu hii ni sababu kubwa iliyonifanya nikaamua kuondoka katika chama hicho.
Alisema kuwa CHADEMA ni chama chenye watu wasioweza kufikiri kwa haraka kutokana na ukweli kuwa Watanzania wanazo akili za kutosha kujitambua na kutoyumbishwa wala kuamuliwa juu ya amani ya nchi yao.