Lowassa aishiwa uvumilivu
na Kulwa Karedia
ALIYEKUWA Waziri Mkuu, Edward Lowassa, ametangaza nia ya kulifungulia mashitaka gazeti la kila wiki la MwanaHalisi, kwa madai ya kumkashifu na kumchafulia jina.
Uamuzi huo wa Lowassa unatokana na habari yenye kichwa cha habari kisemacho: ‘Lowassa katika kashfa mpya', ‘Amesaini mkataba usiku', ‘Ni mradi wa UV-CCM' iliyochapwa katika toleo namba 107 la gazeti hilo la kila wiki lililoingia mitaani jana.
Lowassa alitangaza uamuzi huo wa kwanza kuutoa tangu alipolazimika kujiuzulu uwaziri mkuu Februari mwaka huu kupitia taarifa yake iliyotolewa kwa vyombo vya habari jijini Dar es Salaam jana na kusainiwa na yeye mwenyewe.
Uamuzi huo wa Lowassa unakuja baada ya jina lake kutajwa mara kadhaa likihusishwa na mkataba kati ya Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambao yeye ni Mwenyekiti wa Baraza la Wadhamini la jumuiya hiyo ya chama tawala.
Katika taarifa ya jana, Lowassa ambaye alilithibitishia Tanzania Daima kwa simu kuwa ni yake, alisema amefikia uamuzi huo kwa maelezo kuwa, gazeti hilo linalochapishwa na Kampuni ya Hali Halisi Publishers, limekuwa na utaratibu wa kumchafua katika matoleo yake mbalimbali. Hata hivyo hakutoa ufafanuzi kuhusu suala hilo.
"Kwa kuwa gazeti hili limekuwa na utaratibu wa kunichafua, nimewaeleza mawakili wangu wa Kampuni ya Rex Attorney, wawafungulie mashitaka mara moja ili wachukuliwe hatua za kisheria," alisema Lowassa katika taarifa hiyo.
Katika taarifa hiyo, Lowassa anasema anapenda kuifahamisha jamii kuwa, habari hiyo imeandikwa kwa majungu yanayopikwa, yakiwa na lengo la ziada.
"Wakati kichwa cha habari kinataja kuwa nimesaini mkataba usiku, ukisoma habari yenyewe ndani hakuna sehemu inapotaja iwapo nimesaini mkataba huo usiku kama walivyoandika," alisema Lowassa katika taarifa hiyo ya ukurasa mmoja.
Alisema katika taarifa hiyo kuwa, maelezo yaliyotolewa na Katibu Mkuu wa CCM, Yusufu Makamba, kuhusu mkataba huo, yalikuwa sahihi, ikiwa ni pamoja na kupeleka mkataba kwenye chama kwa ajili ya kusubiri maamuzi ya Kamati Kuu.
"Gazeti hili limethibitisha upungufu mkubwa katika taaluma. Namba yangu ya simu wanayo, na wanajua nipo bungeni, wangefika wakaniuliza, ila kwa nia ya kuendelea kutimiza malengo yao, hawakufanya hivyo," alisema Lowassa katika taarifa hiyo.
Lowassa aliongeza kuwa habari hiyo ilihamia ukurasa wa pili na kusisitizwa na makala ndefu kwenye kurasa za 8 na 9 iliyokuwa na kichwa cha habari: "Mradi wa UV-CCM; msumari wa mwisho katika ‘jeneza' la Lowassa.
Alisema habari na makala hiyo, vilikuwa vinazungumzia kiwanja namba 108/2, kilichopo jengo la UV- CCM, ambalo linadaiwa kuingia mkataba wenye utata.
Katika habari hiyo ya jana, MwanaHalisi lilieleza kuwapo kwa taarifa za Lowassa kusaini mkataba huo, tofauti na madai yaliyotolewa na Makamba wakati alipozungumza na waandishi wa habari wiki iliyopita aliposema suala hilo lilikuwa limepelekwa katika Kamati Kuu ya CCM kwa ajili ya maamuzi.
Gazeti hilo lilieleza pia kuwa, Lowassa akiwa Mwenyekiti wa Baraza la Wadhamini na Amos Makalla, wakati akiwa bado Katibu wa Baraza hilo, ndio waliosaini mkataba huo kwa niaba ya UV-CCM, wakati upande wa mwekezaji, waliosaini ni Shubhashbai M. Patel, anayejitambulisha kama Mkurugenzi Mtendaji wa makampuni ya MM.IS.ML na Jamila Adam, ambaye ni shahidi.
Akizungumza na Tanzania Daima kwa njia ya simu jana kutoka mjini Dodoma, anakohudhuria kikao cha Bunge, Lowassa alisema anachokifahamu ni kuwa Baraza la Wadhamani la UV- CCM ambalo yeye ni mwenyekiti wake, lilikuwa limesaini Hati ya Makubaliano (Memorandum of Understanding – MoU) na si mkataba.
Alisema hatua ya gazeti hilo kutumia neno ‘jeneza' la Lowassa, lilikuwa ni kielelezo kwamba lilikuwa limefikia hatua hata ya kumchulia kifo, kwa sababu ambazo alisema hazijui.
Akizungumza na Tanzania Daima kwa simu jana, Mkurugenzi Mtendaji wa Hali Halisi Publishers, Saed Kubenea, alisema walikuwa na uhakika na kile walichokiandika, kwani kabla ya kukichapa waliwasiliana na wanasheria waliobobea na wakawathibitishia kuwa walichokuwa nacho kilikuwa ni mkataba na si MoU kama anavyotaka ionekane Lowassa.
'‘Mwache aende mahakamani, tutaenda kukutana naye huko huko. Hatuna wasiwasi kabisa, kwani sisi tunao mkataba ambao Lowassa amesaini na ambao hata wanasheria wetu waliobobea walipoupitia walisema ule ni mkataba na si MoU kama anavyodai yeye," alisema Kubenea.
Alisema ushahidi mwingine unaowathibitishia kuwa kilichosainiwa ni mkataba ni ukweli kwamba, utekelezaji wa mradi ulioibua utata huu mzima, umeshaanza kutekelezwa kabla hata ya maamuzi ya Kamati Kuu ya CCM.
Mtu wa kwanza kuibua utata katika mkataba huo wa UV-CCM alikuwa ni kada kijana wa chama hicho, Nape Nnauye, wakati akichukua fomu za kugombea uenyekiti wa umoja huo wa vijana, katika uchaguzi utakaofanyika baadaye mwaka huu.
Nape, mtoto wa kada wa siku nyingi wa CCM, marehemu Moses Nnauye na ambaye pia ni mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM, alifikia hatua ya kumtaka Lowassa, Mwenyekiti wa Taifa wa Umoja wa Vijana, Emmanuel Nchimbi na Katibu Mkuu wa jumuiya hiyo kujiuzulu nyadhifa zao kutokana na kashfa ya mradi huo aliouelezea kuwa ni wa kinyonyaji.
Source: TANZANIA DAIMA.