Sababu iliyomfanya kukataa kupigia kura Mlima Kilimanjaro; Viongozi wasome waelewe!

Mzito Kabwela

JF-Expert Member
Nov 28, 2009
18,857
7,617
SIKUPIGA kura kwenye mtandao ili Mlima Kilimanjaro uwe miongoni mwa maajabu saba ya asili ya dunia. Sikujaribu kuwahimiza wengine wafanye hivyo. Ulikuwa ni uamuzi wa kiakili japo uliniuma kwa sababu nilitamani na mimi ningefanya hivyo ili nijisikie vizuri. Sikutaka kushiriki kwenye kitu ambacho nilijua mapema kuwa kisingewezekana.


Baada ya matokeo kutoka kuwa Mlima Kilimanjaro haukuwa mojawapo ya maajabu hayo saba mapya ya dunia maelezop yalitolewa kuelezea kwa nini ilishindikana huku maelezo ya haraka yakisema ati ni kwa vile watu wetu hawana intaneti kama hizo nchi nyingine.


Kwa kadiri tarehe ya mwisho ya kupiga kura ilivyokaribia tuliweza kushuhudia watu mbalimbali na hasa viongozi wakijitokeza kuhimiza watu wapige kura. Tumeona Mzee Mwinyi, mama Salma Kikwete na hata Waziri Mkuu Pinda walivyojitahidi kuhimiza watu wapige kura kwenye simu zao kwa kutuma ujumbe wa sms au waingie kwenye mtandao na kufanya hivyo. Niliwaonea huruma kwa kweli! Niliwaonea huruma kwa sababu walikuwa wanajaribu kusukumiza gari bovu kwenda mlimani!

Ninaamini kwamba wengi waliokuwa wanafanya kampeni hii walikuwa wanafanya hivyo wakiamini kuwa kwa Mlima Kilimanjaro kutangazwa kuwa ni miongoni mwa maajabu saba mapya ya asili ya dunia basi kungeitangaza Tanzania na hivyo Tanzania kujulikana zaidi duniani. Hapa ndipo lilipokuwepo kosa kubwa zaidi – walitaka kutumia kuwemo kwenye maajabu saba ya dunia kuitangaza Tanzania zaidi.

Lakini swali linabakia kwa nini kutumia njia ngumu na nzito ya kutangaza Tanzania wakati njia nyepesi ipo? Ninaamini kabisa kuwa hakuna njia yenye gharama rahisi kuliko kutangaza kwa kutumia michezo. Tanzania na vivutio vyake vyote vinaweza kujulikana kwa urahisi zaidi kwa kupitia michezo na mashindano mbalimbali. Hivi majuzi kulikuwa na mashindano ya riadha ya dunia huko Daegu huko Korea ya Kusini. Tanzania haikuwemo katika nchi ambazo ziling’ara na unaweza usiamini, lakini Tanzania iliwakilishwa na mwanariadha mmoja Zakia Mrisho ambaye alikuwa anashiriki mbio ndefu za mita 5000.


Sijui kama umenisoma vizuri nimesema kuwa tuliwakilishwa na mwanariadha mmoja! Fikiria juhudi zilizotumika kutaka watu waupigie mlima Kilimanjaro kura zingetumika kuhamasisha vijana kuingia katika riadha na fedha zilizotumika kuandaa matangazo hayo zingetumika kuwaweka kambini hao vijana tungeweza kweli kushindwa kuwakilishwa hata na wanariadha 20? Ati wanataka kuitangaza Tanzania bila kupanda, wanakinga mikono wavune! Nina uhakika Zakia angerudi na medali ungewaona wanavyojipanga uwanja wa ndege na kujichekesha chekesha kwa fahari!


Mashindano ya Olimpiki London 2012
Unaposoma gazeti hili zimebakia siku 250 kabla ya mashindano ya Olimpiki kufunguliwa katika Jiji la London Julai 27, 2012. Mashindano haya hayatokuja kwa kushtukiza kwani tulijua yanakuja kuanzia mwaka 2008 yalipofanyika mashindano ya Olimpiki yaliyofanyika kwa fahari kubwa Beijing huko China. Muda uliobakia ni sawa na miezi nane tu hivi. Lakini jiulize je Tanzania itawakilishwa na nani? Je itawakilishwa ili iwemo kwenye orodha ya watu watakaopita kwenye gwaride siku ya ufunguzi wakivaa nguo za rangi ya bendera ya taifa na sisi wengine tujisikie vizuri kuwa ‘tuliwakilishwa’? Au watawakilishwa wakiwa na lengo la kupata medali na kitu chochote chini ya hapo itakuwa ni kushindwa? Unafikiria Waingereza, Wachina, Wamarekani, Wakenya na Waghana wanataka kuwakilishwa tu au wanatarajia kurudi na medali?


Cha ajabu ni kuwa viongozi wetu uchwara ambao wamenogewa sifa za kisiasa wameshindwa kuonyesha uongozi wa kisiasa kwenye jambo kama hili. Hakuna mwamko wowote wa kuhamasisha wachezaji na kwa hakika kabisa hakuna kitu chochote cha kuwafanya wanariadha wetu wahamasike. Ati kitu pekee kinachotumiwa ni ile kadi iliyopitwa na wakati ya ‘uzalendo’. Ndugu zangu, uzalendo haulipi bili za watu, na wala haumtatulii mtu matatizo ya familia yake. Kwanini kijana aache kujihangaisha mjini hapa kutafuta maisha badala ya kwenda kufukuza upepo?


Kombe la Dunia Brazil 2014
Kuanzia sasa imebakia kama miaka minne hivi kabla ya mashindano makubwa kabisa ya soka duniani kufanyika nchini Brazil. Mwaka jana mashindano hayo yalifanyika Afrika kwa Mara ya kwanza na Afrika ilipewa nafasi tano Tanzania ikiwa haimo. Nchi karibu zote ambazo zina njozi za kushiriki mashindano ya Brazil tayari zimeanza maandalizi kwa sababu wanaongozwa na dhana kuwa ‘mwisho wa kombe la dunia moja ni maandalizi ya jingine”. Lakini Tanzania haina nadharia hiyo na viongozi wake wasio na maono wapowapo tu wakiombea timu ‘ifanye vizuri’


Mashindano ya awali ndio yameanza na Tanzania haikufanya vizuri sana lakini haiko pabaya sana kwani iliweza kushinda kwa mabao mawili kule Chad na kufungwa bao moja nyumbani. Japo siyo mazingira mazuri lakini ni mazingira ambayo tunaweza kuyajenga.


Kwenda Brazil hata hivyo hakuwezi kutokea hivi hivi. Kunawezekana lakini hakuwezekani kwa kuombea au kunuia. Kunawezekana kwa kuamua, kudhamiria, kujipanga na kwa pamoja kutekeleza lengo hilo la kwenda Brazil. Ikumbukwe kuwa wale wote wanaoenda Brazil 2014 ni binadamu waliozaliwa, kuishi na kusumbuka kwenye dunia hii hii.


Jua linaloangaza Marekani na China ni jua lilelile linaloangaza Morogoro na Tunduma! Kwa kifupi wanaoenda Brazil ni binadamu kama sisi wanaozaliwa na kufa kama sisi. Wanaweza kuwa na ngozi nyeupe au macho ya bluu, wanaweza kuzungumza lugha tusiyoielewa lakini mwisho wa siku ni binadamu wenzetu! Wanaoweza kushindwa na kuanguka kama sote tunavyojua! Au tumesahau siyo Ufaransa, Marekani, wala Uingereza iliyoondoka na Kombe la dunia mwaka jana Afrika ya Kusini?


Tufanye nini?
Jambo kubwa la kwanza mi kuwa tunahitaji viongozi wenye maono siyo hawa tulio nao ambao maono yao yameishia inapofika mikono yao! Tunahitaji viongozi wa kisiasa ambao wanaamini kuwa tunaweza kwenda na kufanya vizuri London na Brazil! Bahati mbaya sana hakuna viongozi vijana wenye maono ya namna hii kwa sababu na wao kama walivyo wale wazee wanafikiri kuwa ushindi unaweza kuja kwa kuombewa au kwa kutamania.


Hadi watakapojitokeza viongozi wenye maono ya kutaka Tanzania ifanye vizuri na ing’are na zaidi ya kung’ara hatuna matumaini! Kama ndio hawa tuliowaona wakihamasisha kutoka kwenye viti vyao vya enzi kupigia kura mlima Kilimanjaro basi imekula kwetu, tena imekula double hadi King!


Maandalizi
Lakini kama watatokea viongozi wenye uthubutu na maono ya kushinda – sifikiri kama wapo katika kundi la hawa wa sasa ambao wametumia siku tatu kulia na kulalamika Bungeni – basi kitu cha kwanza ambacho wanaweza kufanya ni kuweka mpango wa haraka wa maandalizi ya London 2012 ambao uwe umehakikisha tuna vijana wako kambini ifikapo Disemba 31, 2011. Sidhani kama Kikwete anaweza kutuongoza katika hili na kwa hakika kabisa simfikirii Nchimbi kuwa na maono ya namna hiyo! Sasa sijui ni nani maana kila mtu anaangalia Ikulu na wengine wanaangalia bungeni! Je kuna mtu yeyote nje ya Bunge? Je, CHADEMA na ile “People’s Power” wanaweza kutuongoza katika hili? Sina uhakika.


Maandalizi yanahitaji hela. Je kuna mtu serikalini anayeweza kusema tutenge siyo chini ya shilingi bilioni tano kuweka timu kambini sasa hivi na siyo chini ya bilioni 50 kuandaa timu ya 2012, 2014 na 2016? Maandalizi yana gharama na bahati mbaya sana kama tulivyoona kwenye suala la Kilimanjaro hatutaki kuingia gharama mapema hadi dakika za mwisho tukiamini uzalendo utatusukuma!


Motisha
Hakuna kitu muhimu katika kuelekea kushinda kama motisha kwa wachezaji na washiriki wetu. Je, tunatoa motisha gani kwa wachezaji wetu? Tunaweza kuwaahidi nyumba au shilingi milioni 50 kila mwanariadha atakayerudi na medali ya dhahabu? Je tunaweza kua ahidi kuwa kama Taifa Stars itafuzu kwenda kucheza Brazil mwaka 2014 kila mchezaji atapewa dola milioni 1 kwa kufuzu tu? Na kuwa kwa kila hatua wanayopiga wakati wa mashindano yale dau lao ilinazidi kupanda kiasi kwamba tukicheza fainali kila mchezaji kwenye ile timu ataondoka dola milioni 10 au zaidi? Oh najua, najua – sisi ni masikini hadi wa mawazo na maono.
 
binafsi nataka USIMAMIZI mzuri wa rasilimali zetu ndiyo nitashawishika kupigia kura vitu kama hivyo otherwise sipigii kura ULAJI wa mafisadi wakati akina Masawe,Shayo,Mushi,Kimambo na Manka wanaoishi chini ya mlima Kilimanjaro hawanufaiki na uwepo wa mlima huo hapo,Kikwete,Pinda,Maige,Luhanjo na familia zao waupigie kura wasitake kutufanya sisi wananchi 'their business entity' nimekuwa mpinzani mkubwa wa hili swala tangu mwanzo mpaka wengine wakaanza ku 'doubt' uzalendo wangu kwa mitazamo yao.
 
Back
Top Bottom