UCHU
TAFUTA UKWELI
Ilikuwa yapata saa saba unusu.
Musoke na Willy walipofika
nyumbani kwa Temu. Walimkuta
Temu akitembeatembea mbele ya
nyumba yake katika bustani huku
ameweka mikono yake nyuma.
Kwa vile nyumba ilikuwa juu
kwenye kilima, na wao
walimwona kabla hajawaona
mpaka walipopiga honi ya gari ili
kufunguliwa lango la mbele.
Alipoona ni gari la kukodi la
Musoke, mara moja alikimbia na
kulifungua lile lango hata askari
wake anayelinda nyumba yake
hakuwahi mbio za mzee huyu. Hii
yote ilionyesha shauku aliyokuwa
nayo Temu juu ya suala hili la
Rwanda.
"Shikamoo", Willy alimshalimia.
"Marahaba, karibu".
Temu alipeana nao mikono na
wote na kuwakaribisha kule uani
kwenye bustani ya nyumba.
"Wengine?", Musoke aliuliza.
"Saa nane watafika".
"Vizuri".
Walipokuwa wameketi kule
uawani kwenye kivuli kizuri cha
miti, Musoke alitumia nafasi hiyo
kuwafahamisha.
"Bwana Temu, huyu ni kijana
wetu, anaitwa Willy Gamba, sasa
hivi anafanyakazi za kujitegemea,
lakini alikuwa kwenye idara ya
upelelezi ya Tanzania kabla
hajaamua kuacha kazi ili
ajitegemee. Yeye ameombwa na
marafiki zetu wengine aje
atusaidie kwenye hili tatizo letu",
Musoke alieleza huku Temu
akionekana kushikwa na butwaa.
"Na bwana Gamba, huyu ni mzee
Temu na ndiye Mkuu wa PAM
upande wa Tanzania.
Willy aliinuka na kumpa Temu
mkono.
"Mimi siamini macho na masikio
yangu", Temu aliendelea
kuonyesha kama mtu
aliyeshituka sana. "Hivi kweli
Willy Gamba yupo! na ni wewe!
Hivi ni kweli baba yangu, ni kweli.
Mimi siku zote husikia habari za
Willy Gamba na huamini kuwa ni
hadithi tu, maana mambo
ambayo ameyafanya wakati wa
ukombozi wa nchi zilizo kusini
mwa Afrika tulifikiri ni
propaganda tu ya kamati ya
ukombozi ya OAU. Kumbe mtu
mwenyewe upo na ni kweli. Eehe,
ama kweli kuishi kwingi kuona
mengi. Basi bwana Musoke, kazi
yetu itafanikiwa", Temu alieleza.
"Huyu kijana wetu Mwenyezi
Mungu amemjaalia uwezo
mkubwa sana katika kazi hii ya
upelelezi. Hakuna mtu
unayeweza kumlinganisha naye
hapa Afrika, sijui huko Ulaya,
lakini hata majasusi wa huko
Ulaya ndiye aliyekuwa
akiyakomesha wakati wote huo.
Kwa kweli hata mimi niliposikia
amekubali na ni yeye anayekuja
basi roho yangu ilitulia, najuwa
tutafanikiwa. Hivi kwanini
wamekukubalia kustaafu
mapema hivi?", Musoke
alimuuliza Willy lakini kabla ya
kujibu, mhudumu wa pale
nyumbani alifika na kutaka
kujuwa watakunywa nini.
"Bwana Gamba unataka kunywa
nini?, kunywa kitu kidogo, maana
huko ndani wanatengeneza
chochote cha mchana, sisi
wachaga ndizi ndicho chakula
chetu, sijui wewe utapendelea?",
Temu aliuliza.
"Kinywaji naomba klabu soda, na
nitafurahia sana macharari", Willy
alijibu huku Temu akicheka na
kufurahi kusikia macharari.
"Kumbe unayajuwa eeh basi baba
yangu tutakula hayo maana
wanaandaa. Na wewe mzee
Musoke?".
"Mimi nitakunywa ki-wiski
kidogo, unajuwa sisi wazee
lazima ushituwe damu kidogo
upate joto".
"Sawa kabisa, nenda kalete
haraka", Temu alimwagiza
mhudumu wake.
"Ehe Willy, kwanini umeruhusiwa
kustaafu mapema hivi?, au kwa
sababu ya Afrika Kusini kupata
uhuru?", Musoke aliuliza tena.
"Hapana, mimi niliomba kustaafu
ili niweze kuoa na kuanza maisha
ya kifamilia maana kazi hii haifai
kama umeoa na una familia. Sasa
hivi nimeoa na mke wangu ni
mjamzito. Na hata kazi hii
nimekubali tu, kwanza kwa
sababu na mimi nimeumwa sana
na hali hii ya mauaji ya Rwanda
na pili kwa sababu Chifu alisema
nisipokwenda mimi atakwenda
yeye. Na unajuwa bwana Musoke,
mimi nisingependa hata kidogo
kuruhusu kitu kama hicho".
"Ni kweli kazi hii inahitaji kuweka
mawazo yako pamoja, usiwe na
fikira zingine, lakini ndivyo hivyo,
taifa bado linakuhitaji mara kwa
mara kama hivi, ingawaje si sana
kama ulivyokuwa jikoni", Musoke
alikubaliana na Willy. Mara
wakaona wenzao wengine
wanaingia na wote wakasimama
kuwasalimia.
Temu alichukuwa nafasi ya
kuwafahamishe wenzake kwa
Willy Gamba. "Hawa ni wana
PAM kutoka sehemu mbalimbali
za Afrika. Na wamekuja kwa ajili
ya kikao hiki cha kutathimini jinsi
mambo yalivyokuwa huko
Rwanda. Huyu ni bwana Kimani
kutoka Kenya, huyo ni Abakusi
toka Nigeria, huyu ni Makwega
toka Zambia na huyu kijana
mwenzio ni Malisa kutoka hapa
hapa Tanzania". Kisha akageuka
na kumgusa Willy. "Na huyu
ndiye mgeni tuliyemtarajia kwa
ajili ya kazi yetu. Bwana Willy
Gamba.
Kimanina Malisa waliwahi
kusikia habari zake nao
walishikwa na mshangao kama
wa Temu. Musoko alitumia nafasi
hiyo kunong'ona na Abakusi na
Makwega kuwaeleza Willy
Gamba hasa alikuwa mtu wa sifa
za namna gani. Bila hata kusema
mengi, alipoeleza kazi zake mbili
alizofanya na kuutingisha
ulimwengu kwa kuwazuia
majasusi wa Afrika Kusini tayari
wote wakamtambua na kupigwa
na butwaa vilevile.
"Wakati mwingine binadamu akili
inashindwa kuamini kitu. Mimi
nilisikia jinsi mpelelezi wa Afrika
alivyoyaangamiza majasusi kule
Kinsasa, Zaire, na nikaamini
kuwa zilikuwa hadithi tu. Sasa
namuona hapa mtu mwenyewe,
akili inashindwa kuamini.
Inashangaza", Abakusi alisema.
"Kama Willy Gamba ndiye huyu
kijana, basi mambo yetu
yameiva", Makwega naye alinena
na kutokwa na wasiwasi
aliokuwa nao usiku.
Bila kupoteza muda mkutano
uliendelea huku wakipata
huduma za vinywaji na chakula.
"Nafikiri wasiwasi wetu wote
sasa umepungua baada ya
kumpata kijana huyu?", Musoke
alisema kama vile akitoa maoni
ya mkutano.
Wote walitingisha vichwa kama
ishara ya kukubali.
Kwa vile kijana huyu yuko hapa,
tumpe maelezo tunataka
atufanyie nini. Nafikiri mimi
niendelee na kama mtu ataona
nimepwelea mahala naomba
asisite kuongezea, sawa".
"Sawa", wote walimjibu mzee
Musoke.
"Bwana Willy, wewe mwenyewe
naami unazo habari nyingi
kuhusu matukio ya Rwanda. Ila
sisi, kama wana PAM tungetaka
tupate undani zaidi wa mambo
yalivyotokea huko Rwanda mpaka
yakafikia yalipofikia na watu zaidi
ya milioni moja katika nchi ya
watu milioni tano kuteketezwa
kwa siku kadhaa tu. Kitu hiki
kinatisha na kama hakiwezi
kuangaliwa kwa undani na
kuthibitiwa inaweza kutokea tena
si Rwanda tu bali hata mahali
pengine Afrika. Sijui
unanielewa?", Musoke alimuuliza
Willy.
"Nakuelewa, ila nataka nijie ni
nini hasa mnataka mimi nifanye
maana kule sasa kuna serikali ya
RPF, kuna mashirika ya kimataifa,
kuna mashirika yanayotetea haki
za binadamu, mnafikiri mimi
nitafanya nini zaidi ya watu hawa
na wenye uwezo na mapesa
mengi nyuma yao, maana na wao
wanachunguza kwa kina maovu
yaliyotendeka Rwanda", Willy
alisema akitaka ufafanuzi zaidi.
"Sawa bwana Gamba, kitu
tunachotaka sisi ni uchunguzi
wetu wenyewe. Hawa watu
wengine wote wanaweza kuwa na
nia zao tofauti. Serikali ya RPF ni
mhusika kwa kiasi fulani.
hatuwezi kupata ukweli asilimia
mia toka kwao. Mashirika ya
kimataifa yenyewe yanaweza
kuwa na ajenda tofauti, tena
wanaweza kutoa ripoti kutokana
na ajenda yao. Wanaotetea haki
za binadamu nao wana mtazamo
wao kwa maana ya kuonyesha
kuwa kulikuwa na ukiukwaji wa
haki za binadamu Rwanda. Sisi
tunataka uende zaidi ya pale,
ujue kama haki za binadamu
zilikiukwa, na kwa nini zilikiukwa,
lazima kuna sababu.
Mauajiyaliyotokea nini kiini
chake, maana yanaonekana
yalikuwa yamepangwa toka
mapema. Na vilevile kwanini
Afrika na dunia kwa ujumla, ikiwa
kimya pamoja na nchi jirani kama
Uganda, Tanzania, Zaire na
Burundi hazikufanya chochote
kuzuia mauaji haya. Tukishajuwa
chanzo na sababu zilizofanya
mpaka binadamu akafikia kuwa
mbaya kuliko mnyama, nafikiri
tutakuwa tumejifunza; na hili
fundisho litatusaidia kuweka
mkakati wa kuzuia kitu kama
hicho kitakapotokea. Vilevile
tujue namna ya kukidhibiti kabla
hakijaleta maafa makubwa kama
haya", Musoke alijibu.
"Oke, nimeelewa nini mnataka,
nitajitahidi niweze kuchimbua
mambo uliyoyataja hapo ili nipate
vyanzo vyake", Willy alijibu.
"Lakini haitakuwa kazi lahisi,
lazima uwe macho maana ukweli
wa mambo haya unaweza kuwa
na athari nyingi kwa watu
mbalimbali ndani ya Rwanda na
pengineko duniani. Kwa hiyo
ikijulikana kuwa kuna mtu
anatafuta ukweli na ikaonekana
kuwa ataupata, basi ujuwe
masiha yako yanaweza kuwa
hatarini maana mpaka sasa
tunaamini kuna watu wanajaribu
kufukia ukweli usijulikane. Na
hawa watu watakuwa watu
hatari. Tafadhali, hadhari ni
lazima", Abakusi alimwasa Willy.
"Nitalitazama hilo", Willy alijibu
na kuendelea, "Na malipo yangu
yatalipwaje, maana sasa ni
mfanyabiashara na si mfanyakazi
wa serikali tena. Kazi hii
nimeichukua binafsi".
"Malipo utalipwa na PAM. Kwa
ajili ya kazi hii PAM iliwaomba
michango wafanyabiashara wa
kiafrika ambao wanaunga mkono
msimamo wa PAM na wametoa
michango mizuri sana na tukitoka
hapa tutapitia hotelini kwangu
nikupatie malipo yako. Sijui
utahitaji kiasi gani?", Musoke
aliuliza.
"Mimi vilevile, kama nilivyosema,
naunga mkono madhumuni ya
PAM, kwani ni mpaka pale
Mwafrika atakapojitambua kuwa
lazima azungumze na Waafrika
wenzake kupambana na ukoloni
mambo leo ndipo atakapokuwa
amejikomboa kutoka katika
umasikini, ujinga na maradh. Kwa
jinsi hiyo na mimi nikiwa
mshabiki wa PAM nitaomba
nilipwe gharama zangu tu
nitakazotumia, lakini utaalamu
wangu nautoa bure".
Makofi na kupeana mikono ya
shukrani vilisikika.
"Sijui hii kazi unafikiri itachukuwa
muda gani?", Kimani aliuliza.
"Mimi nitawafanyia kazi, nipeni
muda", Willy alijibu.
"Wiki mbili?", Makwega aliuliza
pia.
"Nitajitahidi".
"Basi tuonane hapa baada ya wiki
mbili", Musoke aliagiza.
"Sawa".
"Lakini Willy Gamba atakuwa
anawasiliana na mimi Kampala
kwa kila hatua atakayofikia.
Kama ikionekana kazi inakuwa
bado baada ya hizo wiki mbili,
nitawajulisha", Musoke alieleza.
"Sawa".
"Haya, asanteni sana wazee,
tutaonana Mwenyezi Mungu
akitujaalia baada ya wiki mbili.
Sasa hivi ngoja niende na mzee
Musoke akanikamilishie masuala
ya mapesa", Willy aliaga huku
akiwachekesha.
"Nilitaka kusahau. Tumekupatia
nafasi ya kulala Impala, ukienda
tu pale mapokezi watakupa
funguo, tumelipia kila kitu, kazi
kwako. Sijui kama utahitaji usafiri
kesho kukupeleka uwanja wa
ndege?", Temu alieleza na
kuuliza.
"Hapana, nitajitegemea kwenda
uwanja wa ndege".
Musoke alipoangalia saa ilikuwa
saa kumi na nusu. Willy alipewa
mkono wa heri na wajumbe wa
PAM huku kila mmoja
akimwombea mafanikio na
usalama. Willy aliupokea mkono
huo wa heri huku naye
kimoyomoyo akiomba sala zao
ziwe pamoja naye, kwani hawa
walikuwa watu wenye roho za
ubinadamu, ambao walikuwa
wakitumia muda wao kujaribu
kuwasaidia wengine bila malipo
ya aina yoyote. Kweli Mungu
awabariki.
Musoke na Willy aliondoka,
wakaelekea Maunt Meru.
"Kesho umesema ndege saa
ngapi?", Musoke alimwuliza Willy.
"Saa tatu asubuhi".
"Nije nikupeleke?".
"Hapana, nina marafiki wengi
hapa watanipeleka".
"Na leo jioni tunaweza kula
pamoja?", Musoke alimkaribisha
chakula cha usiku.
"Hapana, nitakwenda kwa dada
yangu jioni, alifiwa na mjukuu
wake na nilikuwa sijapata nafasi
ya kumsalimia na hii ndio nafasi
pekee niliyopata".
"Umeua ndege wawili kwa jiwe
moja".
"Bila shaka", Willy alijibu huku
akijuwa kabisa kuwa angeondoka
jioni ile. Willy kama kawaida
yake, aliendelea kuonyesha kama
angelala Arusha. Hii inaonyesha
jinsi ambavyo Willy hamwamini
mtu yeyote mara akishakuwa
kazini.
"Huwezi kujuwa, kikulacho ki
nguoni mwako, uzoefu wa siku
nyingi umenifundisha", Willy
alijisemea moyoni.
Walipofika Hoteli ya Mount Meru,
walikwenda chumbani kwa
Musoke na kuanza kuelezana
tena. Kwa vile Musoke naye
alikuwa na uzoefu wa siku nyingi
na kazi ya upelelezi alijuwa Willy
angetaka nini.
"Bwana Gamba, unajuwa kazi hii
inaweza ikawa ngumu na ya
hatari kuliko hata jinsi
tunavyotegemea. Hivyo,
jitayarishe kwa yote, nadhani
unanielewa?", Musoke
alimwuliza.
"Nakuelewa sana, kazi hii
naichukulia uzito uleule wa
kawaida, sintaipuuza hata
chembe. Kwa kawaida uzoefu
umenionyesha kuwa kwa
kawaida kazi rahisi ndio hugeuka
kuwa ngumu sana".
"Vizuri, mimi ninao wenyeji kule
Rwanda, ambao nafikiri
wanaweza kukusaidia kupata
fununu za awali", Musoke
alisema na kufungua mkoba wake
na kutoa kitabu chake cha
anuani. "Yuko rafiki yangu
ambaye kwa miaka amekuwa
akiipinga siasa ya chama cha
MRND. Yeye ni mwanajeshi.
Alikuwa kamanda katika jeshi la
kumlinda Rais, lakini kwa vile
hakukubaliana na sera yao,
aliacha na kuanza kwa siri
kueneza habari kwa vyombo
vinavyotetea haki za binadamu
jinsi serikali ya Rwanda
ilivyokuwa inavunja haki za
binadamu nchini humo. Wakati
Rais alipouawa Aprili 6, 1994,
yeye alikuwa Nairobi kuonana na
Katibu wa Chama cha kutetea
Haki za Binadamu ulimwenguni.
Hata hivyo, huku nyuma mke
wake na watoto wake sita na
wapwa wake wawili, wote
waliuawa tarehe 7, Aprili. Hii ina
maana angekuwepo Kigali na yey
vilevile leo angekuwa marehemu.
Anakaa Kimihurura nyumba
namba 168. Simu yake kwa
bahati ni moja ya chache
zinazofanyakazi sasa hivi na ni
namba 50486. Yeye ni Mhutu.
"Umeishazungumza naye?", Willy
aliuliza.
"Nitazubumza naye, tuna
uelewano mzuri, na yeye anajuwa
mengi kwa watu wachache
waliokuwa wanaipinga serikali
waliobaki. Na ujuwe huyu mtu
alikuwa karibu sana na serikali
ya Rwanda, na huenda karibu
sana na Rais mpaka kufikia kuwa
kamanda wa jeshi lake. Hivyo,
anajuwa serikali ilivyoondolewa
madarakani na RPF vizuri sana,
na ndio sababu vilevile kumtafuta
ili kumuua ili kuua ukweli wa
mambo".
"Vizuri, nikifika Rwanda
nitamtafuta kama nitamhitaji".
"Tumekupangia kwenye hoteli
iitwayo Des Mille Collines. Hoteli
hii ni maarufu maana wakati wa
mauaji watu wengi, hasa wa
mataifa ya nje, walijificha hapa
na hivyo hata wanyarwanda
waliokuwa wanatafuta ili kuuawa
kati ya walionusurika ni wale
waliobahatika kufika hoteli hapo.
Hivyo, nayo itakupa fursa nzuri
kupata fununu mbalimbali.
Vilevile ningependa umwone
Padre mmoja ambaye
tunafahamiana na yeye
alinusurika kimiujiza baada ya
mapadri, maburuda , watawa na
watu wote waliokuwa kwenye
kituo hicho cha dini kiitwacho
Centre Christus, kuuawa na
Wahutu wenye siasa kali. Padri
huyu anaitwa Jean Marie
Karangwa. Utapata mengi toka
kwake vilevile".
"Bado yuko kwenye kituo hicho?",
Willy aliuliza.
"Ndio yupo, na anajaribu
kukianzisha upya. Na wa mwisho
ambaye ningependa umwone
ikiwa unahitaji msaada, maana
huwezi kujuwa, unaweza kuwa
kwenye hatari ambayo inahitaji
msaada wa kiserikali, hasa
kijeshi. Huyu ni rafiki yangu
saana, tumekaa naye jirani mjini
Kampala na ni mmoja wa
makamanda wa RPF, mtu
shupavu kama wewe na msomi
kama wewe na kijana wa rika
lako. Naamini mkionana
mtashibana tu. ana roho safi
sana. Anaitwa Col Thomas
Rwivanga, namba yake ya simu
60314".
"Asante, nikihitaji msaada wake
nitamtafuta", Willy alijibu.
"Utaondoka lini na kwa njia
gani?", Musoke aliuliza.
"Mimi kesho kutwa nitakutafuta
Kampala nikiwa Kigali
kukujulisha nimefika".
Musoke hakuuliza zaidi maana
alielewa maana yake. Kisha
akatoa bahasha kubwa iliyokuwa
na pesa za dola za Kimarekani.
Idadi yake haikuzungumzwa,
lakini bila shaka ilikuwa maelfu
ya madola.
Baada ya kumpa mzigo huo
walisimama na kuagana.
"Haya, nakutakia safari njema na
kazi njema. Nakuombea heri",
Musoke alimshika mkono
akionyesha uchungu kidogo.
"Asante sana, tuombe Mungu",
Willy alijibu na kuondoka.
Willy alipoachana na Musoke
alikodi teksi pale nje ya Mount
Meru Hotel na kuelekea Impala.
Alipofika Impala alijitambulisha.
"Naamini nina nafasi ya chumba
hapa, naitwa Willy Gamba.
Msichana wa mapokezi aliangalia
kwenye orodha yake ya majina
kisha akaliona jina la Willy
Gamba.
"Ndio baba, chumba 212", alijibu
huku akitoa funguo na
kumkabidhi.
"Una mizigo?".
"Hapana, huu mkoba wangu una
kila kitu".
"Kila kitu?".
"Kila kitu nakuambia, utashangaa
nikiufungua, mrembo zaidi yako
atatokea".
Yule msichana akacheka na Willy
akapandisha ngazi. Alikifungua
chumba na kukuta kidogo lakini
kizuri sana. Aliangalia saa yake
akaona ilikuwa saa kumi na mbili
kasoro robo.
Alikwenda kitandani akatoa
blanketi, akaliweka pembeni na
kufunua shuka na kutengeneza
kama kwamba kulikuwa na mtu
aliyelala pale. Kisha, akauweka
ufunguo kwenye kufuli la mlango
kwa ndani, akachukua mkoba
wake. Akafungua mlango na
kuurudisha bila kuufunga na
funguo kwa vile aliziacha ndani
makusudi na kutelemka chini.
Alipoangalia pale mapokezi na
kuona wapokeaji wapo
shughulini, alichepuka na kutoka
nje. Akelekea kwenye maegesho
ya teksi na kukodi teksi kuelekea
uwanja wa ndege wa Arusha.
Ilikuwa yapata saa kumi na mbili
na robo alipofika uwanja wa
ndege na kukuta ndege imeshatua
tayari. Rubani wa ndege
alimfuata na kumpokea mkoba
wake.
"Habari za jioni?", Rubani
alimshalimia.
"Za jioni nzuri asante".
"Huna mzigo zaidi?".
Sina, ni huo huo".
Rubani aliufungua mlango wa
ndege hii ya Tanzanair, aina ya
Cessina Mark 4, na kumkaribisha
abiria wake huyu mmoja, ambaye
walikaa pamoja kwenye viti vya
mbele, na kisha akawasha injini
za ndege, na kuruka.
ITAENDEA