SIRI PART3: MTUNZI PATRICK CK
JASUSI/GAIDI
SEASON 2 : EPISODE 1
DAR ES SALAAM –
TANZANIA
Mataifa mbali mbali
duniani yaliendelea kutoa wito
kwa makundi ya kidini
yanayopigana kuacha mara
moja na kuitaka jumuiya ya
kimataifa kuchukua hatua za
haraka za kuzuia umwagikaji
mkubwa wa damu
unaoendelea katika eneo la
Afrika Mashariki .Vikosi vya
majeshi ya ulinzi vya nchi za
Afrika mashariki vikisaidiana
na vikosi vya jeshi la Marekani
viliendelea na juhudi za
kudhibiti mapigano yale
makubwa lakini pamoja na
juhudi zao bado hali iliendelea
kuwa mbaya.Mapigano
yaliendelea kushika kasi kila
uchao.Majengo mengi ya ibada
na yale ya serikali pamoja na
magari vilichomwa moto na
makundi ya watu
wanaopigana.
Nchini Tanzania
mawasiliano ya simu na
inteneti vilizimwa ili kuzuia
watu kuwasiliana na
kuhamasishana kushiriki
katika vurugu.Ni taasisi
muhimu tu za serikali ndizo
zilizoendelea kuwa na
mawasiliano.Licha ya
kutokuwepo kwa mawasiliano
ya simu,bado vurugu
ziliendelea na kuilazimu
serikali kuongeza ulinzi zaidi
katika sehemu muhimu kama
vile mahospitali,mitambo ya
kuzalisha umeme,mitambo ya
kusukuma na kusambaza
maji,mabenki na vituo vya
polisi ambako makundi ya
watu walikuwa wakivamia na
kupora silaha ambazo
walizitumia katika mapigano.
Saa tano na dakika kumi
za usiku,Rais Dr Fabian
alimaliza kikao na wakuu wa
vyombo vya usalama kikao
kilichoanza saa kumi na mbili
za jioni.Kwa muda wa siku
nzima Dr Fabian amekuwa
akifanya kikao baada ya
kingine katika kujaribu
kutafuta suluhu ya machafuko
yale.Baada ya kumaliza kikao
na wakuu wale wa vyombo vya
ulinzi na usalama akawa na
mazungumo ya faragha na
mkuu wa majeshi kwa
takribani dakika arobaini na
walipomaliza akataarifiwa
kwamba wakuu wa idara ya
SNSA walikuwa wanamsubiri
kwa ajili ya kuzungumza
naye.Rais akaelekeza
wapelekwe nyumbani kwake
ataenda kukutana nao huko
kwani bado alikuwa na
mazungumzo ya faragha na
mkuu wa idara ya usalama wa
taifa.
Saa saba kasoro dakika
tisa Rais akaingia sebuleni
kwake ambako aliwakuta Ruby
na Gosu Gosu wakimsubiri.
“Samahani sana vijana
wangu kwa kusubiri muda
mrefu” akasema Dr Fabian
“Usijali mheshimiwa
Rais,tunaelewa uzito wa
majukumu uliyonayo”
akasema Ruby
“Sikuwajumuisha katika
kikao cha wakuu wa vyombo
vya ulinzi na usalama kwa
kuwa idara yenu ni ya siri na
kazi zake zinafanywa kwa usiri
mkubwa hivyo msijisikie
kutengwa” akasema Dr Fabian
huku akilegeza tai yake
“Tunaelewa mheshimiwa
Rais” akajibu Ruby
“Kama hamtajali naomba
tukapate chakula kwani hivi
mnionavyo sijala chakula toka
nilipokunywa chai asubuhi”
akasema Dr Fabian na
kuongozana na akina Ruby
katika chumba cha chakula.
“Vijana wangu urais ni
mgumu sana.Nawashangaa
wale wanaong’ang’ania
madarakani.Sijamaliza hata
kipindi changu kimoja cha
urais lakini tayari nimeanza
kufikiria kutowania kuteuliwa
tena kipindi cha pili.Urais ni
mzigo mzito.Tazama hivi sasa
nchi imeingia katika
machafuko na watu wote
wananitazama
mimi.Nimeubeba mzigo mzito
mabegani mwangu kana
kwamba mimi ndiye
niliyeanzisha hizi vurugu.Toka
asubuhi sijapata hata nafasi ya
kupumzika ni kikao baada ya
kikao” akasema Dr Fabian
“Pole sana mheshimiwa
Rais.Ni kweli umebeba mzigo
mzito sana” akasema Ruby
“Tuachane na
hayo.Mnaendeleaje upande
wenu? Akauliza Dr Fabian
“Tunashukuru Mungu
tuko salama na tunashukuru
pia miundo mbinu yetu pia iko
salama.Jengo letu kuwa karibu
na ikulu imesaidia sana kwa
machafuko kutofika huku”
akasema Ruby
“Wafanyakazi wenu wote
wako salama? Akauliza Rais
“Ndiyo mheshmiwa Rais
wote wako salama.Tumeweka
kambi pale pale katika jengo
letu na sote tuko hapo hadi
pale hali ya amani
itakapokuwa nzuri” akasema
Ruby na ukimya mfupi ukapita
“Jioni ya leo
nimezungumza na Rais wa
Marekani akanitaka tusitumie
nguvu kubwa katika
kutawanya makundi ya
wanaopigana.Anadai idadi ya
watu wanaouawa na vikosi vya
ulinzi imekuwa kubwa hivyo
kuchochea machafuko zaidi.Si
yeye tu bali hata umoja wa
ulaya umetaka hivyo” akasema
Dr Fabian na kunyamaza
akaendelea kula halafu
akasema
“Nawashangaa sana hawa
viongozi wanaodai tusitumie
nguvu kubwa.Yawezekana
hawajawahi kukutana na
machafuko kama haya ya
kidini katika nchi zao ndiyo
maana inakuwa rahisi kudai
isitumike nguvu.Watu
wanavamia majengo ya
serikali,wanachoma majengo
ya
ibada,wanapora,wanaharibu
magari,wanachoma makazi ya
watu,wanaharibu miundo
mbinu halafu tusitume nguvu
kuwazuia?? Akauliza kwa ukali
“Huu ni upuuzi mkubwa
sana.Lazima tutumie nguvu
kuzuia machafuko haya
yasiendelee.Wanauawa watu
wasio na hatia.Wanawake na
watoto ndio wanaopata taabu
kubwa katika machafuko
haya.Tanzania tumezoea
kupokea wakimbizi kutoka
nchi nyingine lakini na sisi
yametukuta,hatuna kwa
kukimbilia.Tumeichezea
amani yetu na sasa tunayaona
madhara yake ! Naapa
kuendelea kutumia nguvu
kubwa kuhakikisha haya
makundi yanayochafua amani
yetu yanafutiliwa mbali !
akasema Dr Fabian na kuweka
kijiko chini hakuwa tena na
hamu ya kula chakula.Alizama
katika mawazo
“Mheshimiwa Rais”
akasema Ruby
“Suala hili linanikosesha
amani kabisa.Malizeni kula
twende katika mazungumzo”
akasema Dr Fabian.Ruby na
Gosu Gosu walimaliza kula Dr
Fabian akawachukua
wakaenda katika chumba cha
mapumziko
“Ni saa tisa sasa
mapambazuko
yanakaribia.Toka
mapambazuko ya jana
sijafumba jicho na ninawataka
ninyi wasaidizi wangu nanyi
pia msifumbe macho yenu
hadi pale tutakapohakikisha
balaa hili limepita” akasema
Dr Fabian halafu ukapita
ukimya
“Vijana wangu nimefurahi
kuwaoneni tena mkiwa
salama.Nataka kufahamu kile
kinachoendelea ndani ya SNSA
kwani toka zilipoanza vurugu
sijapata wasaa wa kukaa nanyi
tukazungumza yale
yanayoendelea katika idara
yenu.Vyombo vyote vya ulinzi
na usalama kuanzia jeshi
polisi,jeshi la
wananchi,zimamoto na
vingine vyote mnavyovifahamu
wamejielekeza katika kudhibiti
vurugu lakini mpaka sasa
hakujakuwa na mafanikio
yoyote vurugu bado zimeshika
kasi” akasema Dr Fabian
“Mheshimiwa Rais idara
yetu kama ilivyo jina lake
haijihusishi sana na masuala
ya udhibiti wa vurugu kwani
hiyo ni kazi ya jeshi la polisi
lakini katika suala hili sisi
tumejikita zaidi katika
kufahamu chanzo cha hizi
vurugu ni nini au ni nani?
Japo vurugu hizi zinatufanya
tushindwe kufanikisha jukumu
letu ipasavyo lakini kuna
mambo kadhaa
tumeyabaini.Katika uchunguzi
wetu wa awali tumebaini
kwamba vurugu hizi zinaweza
kuwa ni zaidi ya
tunavyofikiri.Yawezekana
ikawa ni zaidi ya chuki za
kidini”
“Kwa nini unasema
hivyo?Kuna kitu
mmekigundua? Akauliza Dr
Fabian
“Mheshimiwa Rais,kuna
chembe chembe za siasa ndani
ya vurugu hizi” akasema Ruby
halafu akanyamaza kidogo
“Muda mfupi baada ya
mkuu wa jeshi la polisi kutoa
tamko akiwa jijini Tanga
kuwataka watu waendelee
kuwa wavumilivu na kwamba
serikali inayafanyia uchunguzi
matukio yale ya mauaji ya
viongozi wa dini yaliyokuwa
yanaendelea jijini Tanga,katika
ukurasa wake wa twitter Karim
Abdallah ambaye anaongoza
chama cha siasa cha TPD
aliandika ujumbe akiwahimiza
waumini wa dini ya kiislamu
jijini Tanga kwenda
kuwatafuta wale ambao anadai
walimuua Sheikh mkuu wa
mkoa wa Tanga.Ujumbe huo
wa kichochezi haukukaa sana
akaufuta lakini tayari watu
wengi walikwisha usoma
kwani Karim ana watu wengi
wanaomfuatilia katika
mitandao ya kijamii.Kwa
mwanasiasa kama huyu
kuandika ujumbe kama ule
ambao una mlengo wa
uchochezi inatupa wasiwasi na
kutufanya tulione suala hili
kama lina chembe chembe za
siasa ndani yake.Ukichunguza
katika vurugu hizi utaona kuna
makundi yameibuka ambayo
yanalenga katika kuharibu
miundo mbinu muhimu vile
vile kuvamia na kuharibu
majengo ya taasisi za
serikali”akasema Ruby na Dr
Fabian akapandwa na hasira
“Namfahamu Yule kijana
ni mwanasiasa mchonganishi
na amekuwa akiandika mara
kadhaa jumbe za uongo na
uchonganishi kati ya wananchi
na serikali. Ruby kuna picha
nimeanza kuipata kufuatia
maelezo yako.Sikuwahi
kuusoma huo ujumbe wa
twitter aliouandika lakini
naamini kabisa lazima Karim
atakuwa na mahusiano na
vurugu hizi.Kijana mshenzi
sana Yule ! akasema kwa ukali
Dr Fabian
“Aliufuta ujumbe huo
ndani ya muda mfupi tu lakini
wengi tayari walikwisha
usoma” akasema Ruby
“Mmekwisha anza
kumfanyia uchunguzi huyu
jamaa??akauliza Dr Fabian
akionekana kuwa na hasira
kali
“Mheshimiwa Rais kuna
ugumu kidogo katika
kulitekeleza hilo.Kwanza
tumeshindwa kufuatilia
mawasiliano yake yote kwani
hakuna mawasiliano ya simu
wala intaneti.Pili ni ugumu wa
kumfuatilia nyendo zake kwani
huko mitaani kumetapakaa
vurugu na magari
yanachomwa.Barabara nyingi
zina vizuizi vya kuzuia magari
hivyo tumepata ugumu katika
kuifanya kazi yetu” akasema
Ruby
“Mngenieleza mapema ili
niangalie namna ya
kuwawezesha kutekeleza
majukumu yenu” akasema Dr
Fabian
“Ndiyo maana tuko hapa
mheshimiwa Rais kuleta
maombi yetu kwako”
“Nini mnakihitaji
Ruby?akauliza Dr Fabian
“Mheshimiwa Rais kwa
hivi sasa hakuna mawasiliano
ya simu hapa nchini isipokuwa
kwa ofisi nyeti za
serikali.Pamoja na kuzima
mawasiliano ya simu kwa
lengo la kuzuia watu
kuhamasishana kushiriki
katika vurugu,lakini bado
haijasaidia sana kwani bado
vurugu
zinaendelea.Tunashauri
mawasiliano ya simu
yarejeshwe kama kawaida”
akasema Ruby na Dr Fabian
akaonyesha mstuko kidogo
“Turejeshe tena
mawasiliano ya simu? Hali
itakuwa mbaya zaidi kwani
watu wanatumia simu
kuwasiliana na kuhamasishana
kushiriki katika vurugu na hili
ndilo lilipelekea tukaamua
kuzima mawasiliano yote ya
simu na intaneti na hii
itaendelea hivi hivi hadi pale
vurugu zitakapokoma kwani
tukirejesha mawasiliano
tutaendelea kuongeza chuki na
vurugu zitapamba moto !
Akasema Dr Fabian
“Mheshimiwa Rais pamoja
na nia njema ya jambo hilo
lakini kuna athari zake vile
vile.Siku hizi watu
wanategemea sana simu zao
katika shughuli mbali mbali
hivyo mkiwanyima fursa ya
kutumia simu zao ni
kuwafanya maisha yao yawe
magumu zaidi hata hivyo
sababu kubwa ambayo
tunashauri mawasiliano ya
simu yarejeshwe kama
kawaida ni ili kuwafanya watu
waone maisha yamerejea
kawaida wataamini kwamba
hali ya amani imeanza
kuboreka.Jambo lingine ni
kwamba mamilioni ya
watanzania sasa wanamiliki
simu janja.Tutazitumia simu
hizo kufikisha ujumbe kwa
wananchi kuhusu umuhimu
wa amani na kuepuka
kushiriki katika vurugu
zinazoendelea hivi
sasa.Mheshimiwa Rais
utalihutubia taifa na ili ujumbe
wako uweze kuwafikia watu
wengi zaidi na kwa haraka
tutatumia teknolojia ili hotuba
yako iweze kutazamwa na watu
wote wenye simu janja zao kwa
mara moja”akasema Ruby
“Inawezekana? akauliza Dr
Fabian
“Ndiyo mheshimiwa Rais
inawezekana.Simu janja zote
ambazo zitakuwa zimewashwa
muda huo zitapokea hotuba
yako moja kwa moja bila
mmiliki kujiunga sehemu
yoyote.Kwa mfano waweza
kuwa unawasiliana na mtu
Fulani au unafanya chochote
katika simu basi kila kitu
kitasimama kwa muda na
mtumiaji ataunganishwa moja
kwa moja na hotuba ya
Rais.Pale hotuba itakapokuwa
imemalizika basi mawasiliano
yao yataendelea kama kawaida
na ujumbe utakuwa
umewafikia karibu nusu ya
nchi na hii inaweza ikasaidia
sana kuwafanya watu
wakatafakari kuhusu hizi
vurugu na inaweza ikasaidia
zikapungua kama si
kumalizika kabisa” akasema
Ruby
“Hilo ni wazo zuri
Ruby.Sikuwa nimelifikiria
kabisa” akasema Dr Fabian
“Hilo linawezekana
mheshimiwa Rais na
itatusaidia hata sisi kupata
nafasi nzuri ya kumfuatilia
Karim kujua mienendo yake na
kufahamu mahala alipona
tutamchukua ili atueleze
alichomaanisha katika ule
ujumbe wake wa uchochezi”
akasema Ruby
“Nimekuelewa Ruby na
ahsante sana kwa wazo hili
nitalifanyia kazi.Hilo jambo
litatekelezwa kesho.” akasema
Dr Fabian
“Baada ya hotuba yako
hiyo unaweza ukawatafuta
viongozi wa dini mkakaa meza
moja kulijadili suala hili na
mnaweza kujikuta mmepata
muafaka kwani chanzo cha
vurugu zote ni masuala ya
kiimani” akasema Ruby
“Kuhusu hilo la kukutana
na viongozi wa dini nilikuwa
nafikiria kuwakamata viongozi
wote wakuu wa dini na
kuwafungia sehemu moja
niwaache wazungumze hadi
muafaka upatikane.Tukifaulu
kudhibiti makundi ya dini
tutakuwa tumelimaliza suala
hili kwani hayo makundi
mengine ya waporaji
yanajikinga na mwavuli wa
machafuko ya kidini” akasema
Dr Fabian
“Mheshimiwa Rais sidhani
kama hiyo ni njia nzuri kwa
sasa.Kuwakamata viongozi hao
wa dini kwa sasa itakuwa ni
kuongeza mafuta kwenye moto
kwani chanzo cha vurugu hizo
ni kuuawa kwa viongozi wa
kidini hivyo viongozi wengine
wakikamatwa hata kama ni
kwa nia njema basi vurugu hizi
zitaongezeka mara mbili”
akasema Ruby
“Ruby hawa viongozi
wanaweza wakawa na
mchango mkubwa sana katika
kutafuta suluhu ya vurugu
hizi.Umekuwa ni utamaduni
wetu kukaa mezani
kuzungumza kila pale
kunapokuwa na tofauti zozote
za kiimani naamini hata sasa
kama wakikaa pamoja basi
wanaweza wakazungumza
wanaweza wakafikia
makubaliano na
wakazungumza na waumini
wao kuwasihi waache vurugu”
akasema Dr Fabian
“Mheshimiwa Rais,nasema
haitakuwa rahisi kwa viongozi
hao wa dini kuwa na
maelewano hasa ukiangalia
chanzo cha vurugu
hizi.Ukiangalia namna vurugu
hizi zilivyoanza hapa kwetu
Tanzania ,aliuawa kiongozi
mmoja wa kanisa na waumini
wake kadhaa,usiku wa siku
hiyo hiyo akauawa sheikh
mkuu wa mkoa wa Tanga na
hii ilipeleka kila upande
kulaumu watu wa imani
nyingine kuhusika katika
mauaji yale ya viongozi na
vurugu zikaanzia hapo.Mbegu
mbaya ya chuki tayari
imekwisha pandwa miongoni
mwa waumini na viongozi wao
wa dini,kila upande
ukiwachukia wengine.Hata
ukiwaweka pamoja kila
upande utalaumu upande
mwingine kwamba ndio
chanzo cha vurugu.Njia pekee
ya kulitatua suala hili ni
kutafuta chanzo cha vurugu ni
nini au ni nani? Tunatakiwa
kufahamu nani waliomuua
yule kiongozi wa kanisa na
waliomuua Sheikh mkuu wa
Tanga? Tukifanikiwa
kuwafahamu watu hao basi
tunaweza kupata mwanga wa
vurugu hizi na hata
ukiwakutanisha viongozi wa
dini na ukawaeleza kuhusiana
na hiki tunachokifanya
wanaweza wakaelewa”
akasema Ruby
“Papo hapo tusisahau
kwamba vurugu hizi zilianza
Uganda na kuenea Tanzania
hadi Kenya.Tukitaka kupata
kiini cha vurugu hizi tuanze
kuchunguza namna
zilivyoanza nchini
Uganda.Huu ni kama ugonjwa
ambao umeibuka Uganda
ukaingia Tanzania na Kenya na
kama hakutakuwa na tiba ya
haraka basi ugonjwa huu
unaweza ukasambaa Afrika
nzima” akasema Gosu Gosu
“Uko sahihi Gosu
Gosu.Hali hii lazima idhibitiwe
kwa gharama zozote.Hatuwezi
kuacha hali hii
ikaendelea.Nchi imesimama
kutokana na vurugu hizi
ambazo ni kubwa hadi
kushindwa kudhibitiwa na
vikosi vyetu vya
ulinzi.Wamekuja wanajeshi wa
Marekani lakini bado
hawatoshi.Vurugu ni kubwa”
akasema Dr Fabian
“Mheshimiwa rais kwa
nini Marekani imetuma
wanajeshi wake Afrika
mashariki? Uliomba msaada
kwao? akauliza Ruby
“Sikuomba msaada
wowote kutoka Marekani.Rais
wa Marekani alilazimika
kutuma wanajeshi kwa ajili ya
kusaidia kuimarisha hali ya
amani vile vile kulinda raia wa
Marekani na wa nchi nyingine
za kigeni waliokwama Afrika
mashariki vile vile kulinda
balozi zake.Kama mnavyojua
ubalozi wa Marekani nchini
Uganda ulichomwa moto na
watu katika vurugu hizi
zinazoendelea hivyo
wamechukua tahadhari katika
balozi zao nyingine za Dar es
salaam na Nairobi.Vile vile
wanatusaidia katika ulinzi wa
miundo mbinu muhimu kama
vile bandari.Wameleta meli za
kijeshi katika bandari za Dar
es salaam na Tanga ambazo
zinasaidia katika ulinzi wa
bandari hizo.Huu ni msaada
mkubwa wametupa” akasema
Dr Fabian
“Mheshimiwa Rais,kubwa
lililotuleta kwako ni hilo
tulilokueleza kwamba
mawasiliano ya simu yarejee
kama kawaida ili kutuwezesha
kufanya shughuli zetu kwa
wepesi zaidi” akasema Ruby
“Hilo litafanyiwa kazi
kesho msihofu lakini
hakikisheni huyu kijana Karim
anapatikana tena ikiwezekana
achukuliwe ahifadhiwe katika
moja ya nyumba zetu ateswe
sana hadi aeleze alimaanisha
nini kuhusiana na ujumbe huo
wa kichochezi aliouandika
katika ukurasa wake wa
twitter.Nataka huu uwe ni
mwisho wa Karim ! akafoka
DrFabian
“Tunalifanyia kazi hilo
mheshimiwa Rais na
tutafahamu kila kitu” akasema
Ruby na kumtazama Gosu
Gosu
“Mheshimiwa Rais
umechoka sana naomba
tukuache upumzike hata
kidogo kwani inakaribia saa
kumi na moja za alfajiri sasa”
akasema Ruby
“Nitawezaje kulala wakati
wananchi wangu hawajalala
wanakesha kwa hofu na
wengine wakiishi katika
makambi kama wakimbizi
ndani ya nchi yao kwa hofu ya
usalama wao?Nitalala pale
ambapo vurugu zitakoma.Kwa
hivi sasa ninakwenda
kuzungumza na Rais wa China
katika simu.Nawashukuruni
sana kwa mawazo mazuri
mliyonipa.Nadhani hata
wasaidizi wangu nao pia
wamechanganyikiwa na haya
yanayoendelea ndiyo maana
hakuna hata mmoja wao
aliyenipa ushauri kama huu
mlionipa ninyi.Nendeni
mkaendelee na kazi
muhakikishe watu wenu wote
wanakuwa salama na vile vile
muhakikishe mnawapata
walioanzisha vurugu hizi”
akasema Dr Fabian akaagana
na akina Ruby wakaondoka
kurejea katika jengo la ofisi
yao ambalo halikuwa mbali na
Ikulu.Toka vurugu
zilipoanza,karibu wafanyakazi
wote wa SNSA waliweka kambi
hapo katika jengo la ofisi yao
kwa ajili ya usalama wao.
“Gosu Gosu tuna kazi
kubwa ya kufanya kuhakikisha
tunapata kiini cha vurugu
hizi.Naamini hazikuibuka hivi
hivi lazima wapo
waliozianzisha.Ni akina nani
na nini lengo lao? Hayo ndiyo
maswali ambayo tunahitaji
kuyatafutia majawabu”
akasema Ruby
“Nyakati kama hizi ndipo
humkumbuka sana Mathew
Mulumbi.Naamini huko aliko
anaona kile kinachoendelea
hapa nchini.I miss him so
much” akasema Gosu Gosu.
“Are you scared
Papii?akauliza Ruby
“I’m not scared.Mimi ni
mwanajeshi toka nikiwa
mdogo nimeishi katikati ya
mapigano makubwa hivyo
sijawahi ogopa hata mara moja
na sintoogopa kamwe”
akasema Gosu Gosu
“Good.Mathew hayupo na
jukumu hili ni
letu.Tutamshirikisha pia
Austin pale
itakapolazimu.Tuna kazi
kubwa ya kuhakikisha
tunauchimba mzizi wa
machafuko haya” akasema
Ruby na ukimya mfupi ukapita
halafu Gosu Gosu akasema
“Ruby kuna kitu nataka
kuuliza naomba tafadhali uwe
mkweli” akasema Gosu Gosu
“Siku zote nimekuwa
mkweli kwako.Uliza
nitakujibu”
“Ni kuhusu Mathew.Wewe
ndiye ulikuwa mtu wa mwisho
kuonana naye.Unafahamu
mahala alipo? akauliza Gosu
Gosu.Ruby hakujibu
akaendelea kuendesha
gari.Usiku huu hakuwa na
dereva yeye ndiye aliyeshika
usukani.
“Nijibu Ruby.Unafahamu
mahala alipo?
“Kwa nini unahitaji kujua
Gosu Gosu?
“Mathew ni kaka yangu,ni
mtu wangu wa
karibu.Nilipofumbua macho
na kumuona sikuamini macho
yangu kama kweli ni
yeye.Nilidhani labda ni mzimu
ninauona.Kumbe siku zote
hisia zangu kwamba hakuwa
amefariki ni za kweli.Kwa
bahati mbaya nilipata muda
mfupi sana wa kuwa naye
kisha akatoweka tena na
sijafahamu alikuwa wapi,nini
kilimtokea na amekwenda
wapi.Nahitaji kufahamu kama
kuna chochote alikwambia”
akasema Gosu Gosu.Zikapita
dakika mbili Ruby akasema
“Alinieleza kwa ufupi sana
kuhusiana na mambo
aliyoyapitia.Aliniambia
kwamba alitekwa na Mossad
na amepitia mateso mengi
sana.Ukimtazama mgongo
wake wote umejaa makovu
mengi ukionyesha namna
alivyopitia mateso
makali.Alikuwa makini sana
katika kueleza mahala
alipokuwa.Kuhusu mahala
alipo sasa sifahamu na
alinitaka atakapoondoka
nisimtafute ila aliweka ahadi
kwamba atarejea
tena”akasema Ruby
“Hakukueleza anakwenda
wapi? Akauliza Gosu Gosu
“Hapana hakunieleza na
alinitaka nisijaribu kumtafuta
lakini…….” Akasema Ruby na
kunyamaza kidogo
“Kuna nini Ruby?
“Kuna kitu nilikigundua”
akasema Ruby na kunyamaza
tena.
“Katika kipindi chote
alichorejea nilikuwa naye na
niligundua kuna mtu alikuwa
anawasiliana naye na kumpa
taarifa mbali mbali kuhusiana
na operesheni ile iliyomalizika
ya kumuua James Kasai”
“Alikuwa akiwasiliana na
mtu? akauliza Gosu Gosu.
“Ndiyo kuna mtu alikuwa
anawasiliana naye”
“Hukufanya uchunguzi
kujua alikuwa anawasiliana
nani?akauliza Gosu Gosu
“Hapana
sikuchunguza.Mathew hapendi
kuchunguzwa.Mtu huyo
alikuwa anawasiliana naye
usiku tu na alikuwa
anawasiliana naye akiwa
amejifungia ofisini kwake hii
ina maana kwamba hakutaka
mimi au mtu yeyote kufahamu
kuhusu mawasiliano yao na
mimi sikutaka
kuchunguza.Kila alipotoka
kuwasiliana na mtu huyo
alikuwa anakuja na taarifa
mpya.Mathew ana siri kubwa
sana anatembea nayo.Tufuate
vile alivyoelekeza na muda
utakapofika atarejea na
atatuweka wazi nini
kinaendelea katika maisha
yake.Sisi ni ndugu zake na
hataweza kutuficha kitu”
akasema Ruby
“Sawa Ruby
nimekuelewa.Ahsante sana
kwa kuwa muwazi” akasema
Gosu Gosu
“Naamini umeridhika kwa
haya niliyokueleza.Tunalifunga
suala la Mathew hadi pale
tutakaposikia chochote kutoka
kwake kwa sasa tujielekeze
katika kuuchimba mzizi wa
hizi vurugu zinazoendelea”
akasema Ruby.
Walifika katika jengo la
ofisi yao kuu.Ni watu
wachache tu waliokuwa ofisini
alfajiri hiyo wengi walikuwa
katika mahema
yaliyotengenezwa kwa ajili yao
pembeni ya jengo la ofisi.
“Gosu Gosu tutumie muda
huu mfupi uliosalia kabla ya
mapambazuko tupumzike
kwani tutakuwa na ratiba
ndefu sana siku ya leo”
akasema Ruby na kila mmoja
akaelekea katika sehemu yake
ya kulala
WASHINGTON DC –
MAREKANI
Ni saa tatu za usiku jijni
Washington DC
Marekani.Katika ikulu ya
Marekani Rais William
Washington na makamu wake
Mark Piller walimaliza
kutazama hotuba ya Rais
Armen Hijazi wa Iran.Ni
hotuba iliyosubiriwa kwa
hamu duniani,wengi wakitaka
kusikia msimamo wa Iran
kuhusiana na matamshi ya rais
wa Marekani William
Washington kwamba atalifuta
taifa la Iran.Katika hotuba
yake hiyo ya kumjibu William
Washington,Rais Armen Hijazi
aliionya vikali Marekani
kutothubutu kwa namna
yoyote ile kuvamia ardhi ya
Iran kwani watakachokipata
kitaingia katika historia ya
dunia.Kama haitoshi Rais
Armen alimtaka Rais wa
Marekani kufuta kauli yake
kwamba atalifuta taifa la Iran
kwani kauli yake hiyo
ingeweza kumrudia yeye na
taifa lake.Ilikuwa ni moja ya
hotuba iliyoleta hofu kubwa
kwa Marekani na dunia
wakihofia kuzuka kwa vita
kubwa kwani Rais Armen
aliweka wazi kwamba nchi
yake iko tayari kwa vita na
Marekani na alisistiza kwamba
wataishambulia Marekani
pamoja na washirika wake
watakaoisaidia na alitishia
kwamba baada ya vita hiyo
Marekani haitakuwa sawa tena
na itachukua zaidi ya miaka
hamsini kuijenga tena
Marekani.Katika kumalizia
hotuba yake Rais Armen
aliweka wazi mipango ya Iran
ya kuendelea na urutubishaji
wa madini ya Urani.
“Huu ni upuuzi mkubwa
sana ! akafoka Rais William
baada ya hotuba ile kumalizika
“Siwezi kuvumilia upuuzi
kama huu.Armen hawezi
kututamkia maneno kama
haya sisi ! akaendelea kufoka
William.
“Mheshimiwa Rais haya
maneno yote aliyoyazungumza
Armen ni upuuzi na ni maneno
ya mtu aliyeshindwa.Iran
haina uwezo wowote wa
kuipiga Marekani”akasema
Mark Piller
“Siwezi kuvumilia ujinga
wa namna hii.Marekani ni
taifa kubwa na hatuwezi
kukubali taifa kama Iran
kututolea vitisho vya namna
hii.Ninaapa lazima niishikishe
adabu Iran ! akaendelea
kufoka William ambaye ni
mwepesi sana wa kupandwa
na hasira
“Mheshimiwa Rais hiki
alichokisema Armen
kisikukoseshe amani.Hakuna
anachoweza kufanya
kwetu.Haya matamshi yake
aliyoyatoa leo dhidi yetu
hayatabadili mipango yetu
dhidi ya taifa hilo lakini
nashauri mheshimiwa Rais
huyu mtu tumuendee taratibu”
akasema Mark Piller
“Kiburi alichokionyesha
Armen hakiwezi
kuvumilika.Ameongea kwa
kujitapa kabisa kwamba nchi
yake itaendelea na
urutubishaji wa madini ya
Urani.Hatuwezi kuiacha Iran
ikaendelea na zoezi hili la
urutubishaji wa madini ya
Urani.Lazima tuchukue hatua
kali sana dhidi ya taifa hilo !
akaendelea kufoka William
Washington
“Mheshimiwa Rais suala
hili si jepesi na tunahitaji
umakini mkubwa sana katika
kulishughulikia.Armen ni Rais
mjanja sana.Ametoa matamshi
yale akitegemea kwamba
Marekani lazima itahamaki na
kuanza haraka kuchukua
hatua.Lazima tuwe makini
naye sana.Tumuonyeshe
Arman kwamba sisi ni taifa
kubwa na
hatukurupuki”akaksema Mark
Piller
“Mark hatuna muda wa
kumbembeleza huyu
mtu.Uvumilivu wangu umefika
ukomo.Kinachofuata ni
kumtandika vikali,kuharibu
vinu vyake vya nyuklia na
kumuondoa madarakani rais
Armen ! akasema William
“Mheshimiwa Rais,ni
mapema sana kufikia hatua
hiyo” akasema Mark lakini
William aliyekuwa amewaka
hasira akamgeukia
akamtazama kwa macho
makali na kusema
“Unataka huyu mtu
aendelee kutoa vitsho kwa
Marekani? Unadhani ni hofu
ya namnagani wameipata watu
wetu kufuatia matamshi yake
ya kuivuruga Marekani? Katu
hatuwezi kuwaacha wananchi
wetu waendelee kuishi kwa
hofu ya vitisho vya
Iran.Hawatatuelewa
tutakaposhindwa kuchukua
hatua zozote za
kuwalinda.Msuguano huu na
Iran umechukua muda mrefu
na sasa umefika wakati wa
kuumaliza.Niamini Mark
ninakwenda kulimaliza suala
hili .Siwezi kuipa nafasi Iran ya
kuendelea kuruubisha madini
ya Uran.Iran ikifanikiwa
kutengeneza bomu la nyuklia
hatutaweza kumdhibii tena na
eneo lote la Mashariki ya kati
litaingia katika hofu
kubwa.Lazima tuwahi angali
mapema na njia pekee ni
kuitandika kijeshi” akasema
William
“Mheshimiwa Rais
msuguano huu wa Marekani
na Iran umechukua muda
mrefu kwa sababu mpaka sasa
hatufahamu Iran anamiliki
silaha za namna gani.Mpaka
sasa hatufahamu kwa nini Iran
inakuwa na kiburi cha
kutunishiana misuli ya kijeshi
na Marekani.Hakuna taifa
katika zama hizi ambalo
limewahi kutamka
kuishambulia Marekani zaidi
ya Iran.Lazima kuna kitu
kinaipa kiburi Iran cha kuwa
tayari kuingia vitani na
Marekani hata
kesho.Nimekuwa katika
shirika la ujasusi CIA kwa
muda mrefu na tumekuwa
tukihangaika kujua Iran ina
silaha gani kali lakini mpaka
leo hatujafanikiwa kujua Iran
anamiliki silaha gani.Iran
wamekuwa wakidai kwamba
wana makombora ya masafa
marefu na wametishia
kushambulia nchi zote
washirika wa Marekani katika
Mashariki ya kati ikiwemo
Israel.Mpaka sasa hatuna
uhakika kama hiki
wanachokisema ni cha kweli
ndiyo maana nasema kwamba
hatuwezi kukurupka katika
suala hili.Tunao uwezo wa
kumtandika Iran lakini ni vipi
kama madai yake ya umiiki wa
silaha kali ni ya kweli.Vile vile
tukiivamia Iran kijeshi
tutakuwa tumeanzisha
mgogoro mwingine kwani Iran
na Urusi wana urafiki mkubwa
na wamekuwa wakisaidiana
kijeshi.Hatutapigana vita na
Iran pekee bali tutakuwa vitani
na Urusi pia.Usisahau vile vile
kwamba hivi karibuni Rais wa
Iran alifanya ziara nchini
China na mahusiano ya Iran
na China yameanza kuboreka
hivyo nchi hizi lazima
zitamuunga mkono Iran kama
tutaishambulia kijeshi.Tazama
namna Iran na Urusi
walivyoshirikiana kuiunga
mkono serikali ya Syria hadi
kuiwezesha kukomboa asilimia
zaidi ya tisini ya maeneo
yaliyokuwa yanashikiliwa na
waasi ambao tulikuwa
tunawaunga mkono.Suala hili
ni pana sana mheshimiwa Rais
na inahitaji busara kubwa na
mikakati mizito katika
kulishughulikia” akasema
Mark Piller
“Mark kauli yako ni
uoga.Siogopi kuipeleka nchi
vitani ili kuisambaratisha
Iran.Marekani si taifa la
kutolewa vitisho na taifa dogo
na dhaifu kama Iran !
“Mheshimiwa Rais
ninazungumza kama kachero
mbobezi.Kabla ya kufanya
maamuzi yoyote tunahitaji
kwanza kujiridhisha kuhusu
uwezo wa Iran kijeshi na aina
ya silaha ilizonazo.Tunahitaji
kujiridhisha kuhusu madai
hayo ya Iran kuwa na
makombora ya masafa
marefu.Tunahitaji kujiridhisha
kuhusu uwezo wake wa
kutengeneza bomu la
nyuklia.Tunahit………”
“Mark Piller ! akasema
Rais William na kumkatisha
Mark
“Umefanya kazi CIA
karibu nusu ya umri wako na
kwa muda huo wote mmekuwa
mkihangaika kupata taarifa
kuhusu mfumo wa
makombora na silaha za Iran
bila mafanikio.Itapita miaka
mingapi ili tuweze kupata
taarifa hizo za silaha za Iran?
Kama marais waliopita
walivumilia mimi sina
uvumilivu huo.Nataka
nilimalize suala hili.Iran awe
na makombora makubwa au
madogo lazima atandikwe !
akaendelea kusisitiza William
“Mheshimiwa Rais kuna
jambo muhimu naomba
nikueleze” akasema Mark
Piller
“Mark tunazungumzia
suala la Iran na
tutakapomaliza ndipo
utanieleza hilo unalotaka
kunieleza.Nataka mimi na
wewe tufike muafaka kwanza
kuhusu suala hili la Iran kabla
sijaomba ridhaa ya bunge !
“Mheshimiwa Rais
ninachotaka kukwambia ni
kuhusiana na suala hilo hilo la
Iran” akasema Mark na Rais
William aliyekuwa amesimama
akaketi
“Nini unataka kunieleza?
“Nimekuwa nikiandaa
mpango wa siri wa namna
tutakavyoweza kulishughulikia
suala hili la Iran” akasema
Mark
“Unaandaa mpango wa siri
? Akauliza William akionekana
kushangaa
“Ndiyo mheshimiwa
Rais.Sikuwahi kukwambia
suala hilo kwani maandalizi
yake hayakuwa yamekamilika
lakini kwa hapa tulipofika
inabidi nikueleze ukweli ili
mimi nawe tuwe katika
ukurasa mmoja.”
“Nakusikiliza Mark”
akasema William
“Kabla ya kukueleza
kuhusu mpango huo kuna
jambo ambalo nataka
ulifahamu ambalo naamini
hulijui ila halitakufurahisha”
“Nini unataka kunieleza
Mark? Akauliza
William.Ukapita ukimya mfupi
Mark akitafakari namna ya
kuanza kumweleza Rais kisha
akasema
“Kwa muda mrefu
Marekani tumekuwa
tunashirikiana na makundi
kadhaa ya kigaidi katika
mipango mbali mbali yenye
maslahi kwa
Marekani.Tumefanya hivyo
katika nchi mbali mbali kama
vile..” Mark akanyamaza baada
ya Rais William kuhamaki
“Kushirikiana na makundi
ya kigaidi?akauliza William
kwa mshangao
“Ndiyo mheshimiwa Rais”
akajibu Mark
“Marekani haiwezi
kushirikiana na magaidi hata
siku moja.Tumekuwa vinara
katika kupiga vita ugaidi
duniani.Ni kwa juhudi hizo za
kupamba na ugaidi
tulifanikiwa kumuua Osama
bin Laden kiongozi mkuu wa
Alqaeda kundi la kigaidi
lililokuwa hatari
duniani.Tumeendelea pia
kuvisambaratisha vikundi
mbali mbali vya kigaidi
sehemu mbali mbali
duniani.Nashangaa
unaponiambia kwamba
Marekani tunashirikiana na
magaidi !
“Mheshimiwa Rais, ni
kweli tunashirikiana na
makundi ya kigaidi lakini hili
ni suala la ndani mno na la siri
kubwa.Hata marais waliopo
madarakani huwa
hawafahamishwi jambo hili na
hawapaswi kulifahamu.Kwa
ufupi tu ni kwamba kuna
kitengo maalum cha siri ndani
ya CIA ambacho
kinashughulikia mahusiano na
mashirikiano na makundi ya
kigaidi kwa maslahi ya
Marekani.Kwa muda mrefu
sasa Marekani tumekuwa
tukivifadhili kwa pesa na
silaha vikundi mbali mbali vya
kigaidi ambavyo vimekuwa
vikitekeleza mashambulio ya
kigaidi sehemu mbali mbali
duniani kwa maslahi ya
Marekani”
“Mungu wangu ! akasema
William akimtazama Mark
Piller kwa macho ya woga
“Mheshimiwa Rais kama
nilivyokueleza kwamba jambo
hili ni la siri kubwa.Labda kwa
kukupa mfano ni kwamba
tumekuwa tukifadhili
operesheni mbali mbali za
kundi la kigaidi la IS sehemu
mbali mbali duniani na moja
kati ya operesheni ambazo
tumetumia kundi la IS ni
katika machafuko
yanayoendelea Afrika
Mashariki hivi sasa” akasema
Mark na Rais William
akasimama
“Machafuko ya Afrika
mashariki yameratibiwa na
Marekani kwa kuwatumia IS?!
Rais William akashangaa
“Ndiyo mheshimiwa
Rais.Ni mipango ya Marekani”
akasema Mark na Rais William
akasimama akamtazama Mark
kwa mshangao mkubwa
“Mark naomba uniambie
hiki unachonieleza si cha
kweli” akasema William
“Mheshimiwa Rais
ninachokueleza ni ukweli
mtupu na jambo hili lina
maslahi makubwa kwa
Marekani” akasema Mark
“Mark watu wanakufa
kama kuku Afrika Mashariki
hadi tumelazimika kutuma
vikosi vyetu kwenda kusaidia
kurejesha amani.Dunia
inashuhudia machafuko
makubwa kabisa ya kidini
kuwahi kutokea halafu
unaniambia kwamba ni kwa
maslahi ya Marekan…...”
“Mheshimiwa Rais !
akasema Mark na kumkatisha
Rais William.
“Kinachoendelea hivi sasa
Afrika Mashariki kina maslahi
makubwa kwa
Marekani.Tazama bei ya
mafuta ilivyopanda katika soko
la dunia baada ya nchi
wazalishaji wa mafuta kuweka
mgomo baridi na kuzalisha
kiwango kidogo cha mafuta
kuliko mahitaji ya dunia.Hii
imepelekea akiba yetu ya
mafuta kuanza kupungua na
wakati huo huo tuna migogoro
na nchi nyingi ambazo ni
wazalishaji wakubwa wa
mafuta duniani.Hatuna
mahusiano mazuri na
Venezuela,Mashirikiano yetu
na Saudi Arabia yametetereka
pia,Iran ambao nao ni
wazalishaji wakubwa wa
mafuta ni maadui zetu,Iraq
pia hatupati mafuta ya kutosha
kwani serikali iliyoko
madarakani hivi sasa haitaki
mashirikiano na
Marekani.Nchi nyingine kama
Urusi ambayo unafahamu
mahusiano yetu nao.Nchi
kamaLibya ambao wanashika
nafasi ya tisa kwa akiba kubwa
ya mafuta nako
kumechafuka.Kwa ujumla
mahusiano yetu na nchi
wazalishaji wa mafuta duniani
si mazuri na mafuta yetu hapa
nchini hayatutoshi hivyo kwa
namna yoyote ile tunahitaji
kuongeza akiba yetu ya mafuta
na Afrika Mashariki kuna kiasi
kikubwa cha mafuta.Nchi ya
Uganda inakadiriwa kuwa na
mafuta mengi zaidi kuliko nchi
zote katika bara la Afrika hivyo
mipango yetu kuhakikisha
tunapata mafuta kutoka
Uganda” akasema Mark Piller
“Mafuta? ! akauliza
William kwa hasira
“Mafuta yana thamani
kuliko uhai wa watu ?
Sikutegemea kabisa kama
Mark unaweza ukashiriki
katika jambo hili ovu !
akasikitika Rais William
“Mheshimiwa Rais mafuta
ni uchumi.Kuna mgomo baridi
kwa wazalishaji wa mafuta
duniani.Hizi ni njama za
wapinzani wetu dhidi ya
uchumi wetu.Lazima tutumie
kila njia kupata mafuta ndiyo
maana tumeyafuata Afrika
Mashariki.Mheshimiwa Rais
yawezekana haya
tunayoyafanya yasionekana
sawa lakini ni kwa ajili ya nchi
yetu.Marekani lazima iendelee
kuwa taifa kubwa lenye
uchumi mkubwa kuzidi yote
duniani hivyo kila aina ya
mbinu lazima itumike katika
kuhakikisha hilo linatimia”
akasema Mark
“Siamini kama ni wewe
kweli Mark unayezungumza
haya” akasema Rais William
“Mheshimiwa Rais,haya
yote yanafanyika kwa maslahi
ya Marek…….”
“Hata kama ni kwa
maslahi ya Marekani
hatukupaswa kusababisha
machafuko yale yanayoendelea
Afrika mashariki.Ule ni
unyama uliovuka mipaka ya
ubinadamu.Maiti za watu
zimesambaa mitaani huku sisi
tukifaidika kwa mafuta
ambayo Mungu amewajalia
wenzetu.Hili haliwezekani na
siwezi kulifumbia
macho.Lazima nichukue hatua
kalisana kwako na kwa
wenzako wote mlioshirikiana
kuandaa unyama wa namna
hii Afrika Mashariki na
kwingineko duniani ambako
mmekwisha fanya !! akafoka
William
“Mheshimiwa Rais
usithubutu kufanya chochote
kuhusiana na jambo
hili.Hukupaswa kulifahamu
suala hili lakini kwa kuwa u
mtu wangu wa karibu
nimeamua kukueleza kile
kinachoendelea lakini kwa
kwaida Rais hapaswi kabisa
kufahamu chochote kuhusiana
na mambo haya nyeti mno kwa
nchi” akasema Mark
“Mark huwezi ukanipangia
nini cha kufanya.Mimi ni Rais
wa Marekani na nitafanya kila
niwezalo kuhakikisha
ninakisambaratisha kikundi
hicho cha wauaji ndani ya
CIA.Siwezi kukubali
wakaendelea na haya
wanayoyafanya !
“Mheshimiwa Rais
narudia tena kukuonya
usithubutu kufanya
chochote.Utaendelea kuufunga
mdomo wako kama vile
hufahamu chochote
kinachoendelea !
“Mtanifanya nini wewe na
wenzako? Akauliza Rais
William
“Utauawa ! akasema Mark
na ukimya ukapita.William
Washington alionyesha woga
kwa kauli ile ya makamu wake
Mark Piller
“Mheshimiwa Rais
nakushauri fuata kile
ninachokuelekeza.Ukienda
kinyume chake basi sote
maisha yetu yatakuwa
hatarini”
“Kwa nini umenieleza
jambo hili Mark wakati
ukifahamu kuwa sipaswi kujua
chochote? Akauliza Rais
William
“Ni kwa sababu kuna
mpango mkubwa unaoendelea
kuhusu Iran ambao nataka
uufahamu ili usiendelee na
mipango yako ya kuivamia
kijeshi Iran hadi mpango huo
utakapokuwa umekamilika”
“Mpango gani
Mark?akauliza Rais William
akionekana kuanza kupunguza
hasira alizokuwa nazo
“Nitakurejesha kwanza
Afrika Mashariki.Mapinduzi
yale yaliyofanywa na jeshi la
Uganda yaliyomuondoa
madarakani Rais Jenerali
Akiki Rwamirama tuliyapanga
sisi tukishirikiana na Rais wa
Tanzania”
“Tanzania pia walishiriki
katika mapinduzi yale?!
Akauliza Rais William
“Kutokana na
mashirikiano yetu na IS
tuliweza kupata taarifa
kuhusiana na mpango
ulioshindwa kufanikiwa wa
kuwaua marais wa Tanzania
na jamhuri ya kidemokrasia ya
Congo kwa bomu la kujitoa
muhanga.Katika mpango huo
Jenerali Akiki pia
alishiriki.Baada ya kupata
taarifa hizo nilimtuma
mjumbe maalum kwa Rais wa
Tanzania akazungumza naye
kuhusu kumuondoa
madarakani Rais Akiki kwani
tuliamini lazima atakuwa na
hasira naye na ndipo
ukaandaliwa mpango wa
mapinduzi” akasema Mark
“Rais wa Tanzania naye
alikubali yatokee haya
yanaoendelea katika nchi
yake? Ni rais wa namna gani
huyu ambaye anakubali kuona
raia wake wakiuana namna
ile? Akauliza Rais William kwa
ukali
“Mpango wetu na
Tanzania ulikuwa ni
kumuondoa Jenerali Akiki
madarakani na kuuweka
utawala mpya.Baada ya
mpango huo kukamilika ndipo
tuliandaa haya machafuko
yanayoendelea hivi
sasa.Tulipanga kuanzisha
vurugu nchini Uganda ili
kuilazimisha serikali mpya ya
kijeshi kutumia nguvu kubwa
kuzima vurugu hizo na
kusababisha umwagikaji
mkubwa wa damu hali ambayo
ingepelekea kujengwa kwa
chuki kubwa kati ya serikali na
wananchi.Vurugu hizo
zingekuwa kubwa na hivyo
kuilazimisha Marekani
kupeleka vikosi vyake Uganda
na hapo ndipo tungepata
nafasi ya kudhibiti visima vya
mafuta na kuchukua kiasi cha
mafuta tunachokihitaji.Ili
kulifanikisha hilo tulihitaji
msaada wa Jenerali
Akiki.Haikuwa rahis kumfanya
jenerali Akiki akubali
kushirikiana nasi hadi
tulipotengeneza ajali ambayo
iliripotiwa kwamba familia
nzima ya Jenerali Akiki
waliokuwa wanaelekea Dar es
salaam walikoomba hifadhi
baada ya kupinduliwa na jeshi
walifariki”
“Subiri kidogo
Mark.Umesema mlitengeneza
ajali ambayo ilisadikisha watu
kuwa familia yote ya Akiki
walifariki katika ajali hiyo.Nini
unakimaanisha? akauliza
William
“Mheshimiwa Rais,familia
ya Jenerali Akiki iko salama na
hawakufariki katika ile ajali
kama ilivyodaiwa.Ajali ile
ulikuwa ni mchezo ili kumpa
hasira jenerali Akiki na
kumfanya akubaliane na
mpango wetu kwa nia ya
kulipiza kisasi kwa wale
walioua familia yake” akasema
Mark Piller na Willim
akaendelea kumtazama kwa
macho ya mshangao
“Mark siamini kama haya
maneno yanatoka katika
kinywa chako.Iko wapi familia
ya Akiki hivi sasa? Miili ile
iliyosafirishwa katika
majeneza kwenda Uganda ni
miili ya nani? Akauliza Rais
William
“Mheshimiwa Rais familia
ya Akiki kwa sasa iko sehemu
salama katika nchi Fulani
wakiishi kwa amani wakiwa
chini ya uangalizi wa
CIA.Wako salama kabisa
wanatunzwa vizuri na
wanapata kila
wanachokihitaji.Katika yale
masanduku kulikuwa na miili
lakini haikuwa ya familia ya
Akiki.Mheshimiwa Rais jambo
hili limefanywa kitaalamu sana
kiasi cha kutoweza kufahamika
hadi leo hii ninapokueleza”
“Dah ! akasema Rais
William halafu akainamisha
kichwa akafikiri kwa muda
kisha akamtazama Mark Piller
na kusema
“Mark ninajaribu
kuiaminisha akili yangu
kwamba ni wewe ninaye
kufahamu ndiye unanieleza
haya au ni Mark mwingine”
“Ni mimi mheshimiwa
Rais.Najua haya niliyokueleza
yamekustua sana lakini
naomba usistuke kwani yote ni
mipango kwa ajili ya nchi yetu”
akasema Mark na kunyamaza
kidogo
“Baada ya kumleta Akiki
hapa Marekani nilizungumza
naye akakubali kushirikiana
nasi kuanzisha vurugu Uganda
na akashauri njia pekee ya
kuweza kuleta machafuko
nchini Uganda ni kwa kutumia
dini.Alishauri kama tukiweza
kuwafarakanisha waumini wa
dini ya kikristu na kiislamu
lazima machafuko makubwa
yatatokea.Akiki alikwenda
mbali zaidi akashauri kwamba
kama tunataka kuchukua
mafuta basi machafuko ya
Uganda pekee hayataweza
kutusaidia bali tunahitaji
kueneza machafuko hayo hadi
nchini Tanzania kwani bomba
la mafuta linatoka Uganda
hadi Tanga nchini Tanzania
ambako ndiko meli zetu
zingeweza kupakia
mafuta.Tuliuchukua ushauri
huo na kuanzia hapo
tuliwahitaji IS ili waweze
kuanzisha choko choko za
kidini nchini Uganda na
Tanzania.Vile vile kwa msaada
wa Akiki tuliweza kuwapata
mwanasiasa mmoja wa
Uganda na mwingine wa
Tanzania ambao wangeweza
kuchochea vurugu hizo katika
nchi zao na wanasiasa hao
pamoja na wale viongozi wa
dini kwa sasa wako hapa
Marekani.Tulikubaliana baada
ya vurugu hizo kuanza
watakuwa wameimaliza kazi
yao na watakuja kuishi
Marekani.IS walifanya mauaji
ya viongozi wa dini na
kusababisha hasira na chuki
kubwa miongoni mwa
waumini wa dini hizo na Yule
mwanasiasa wa Uganda
akawachochea viongozi wa
dini ya kikristu kuanzisha
mashambulizi dhidi ya
nyumba za ibada za waislamu
na hapo ndipo machafuko
yalipoanzia.Vurugu zilipoenea
Uganda tulihamia pia Tanga
Tanzania ambako nako vurugu
zikaenea na kusambaa katika
sehemu mbali mbali za
Tanzania.Mheshimiwa Rais
hivyo ndivyo ilivyokuwa hadi
tukafanikiwa kupeleka vikosi
vyetu Afrika Mashariki na sasa
meli zetu zimepanga foleni
katika bandari ya Tanga nchini
Tanzania zinapakia mafuta na
hifadhi yetu ya mafuta
inaongezeka.Hatuna tena
sababu ya kusumbuka na
mafuta ya kutoka Mashariki ya
kati.Hadi vurug hizi
zitakjapomalizika tutakuwa na
akiba kubwa sana ya
mafuta.Pima mwenyewe
mheshimiwa Rais je hiki
kilichofanyika kina maslahi
kwa nchi yetu au hakina?
Akauliza Mark Piller na Rais
Wiliam akavuta pumzi ndefu
“Mark mlichokifanya kweli
kina maslahi makubwa kwa
nchi yetu kwani tunahitaji
sana mafuta lakini tatizo ni
njia mliyotumia.Tumemwaga
damu za watu kwa ajili ya
kujipatia mafuta.Machoni pa
Mungu hii si sawa hata
kidogo” akasema William
“Nakubali mheshimiwa
Rais lakini tumekuwa
tukifanya hivi kila mara na
hakukuwa na namna nyingine
ya kufanya kuweza kujipatia
mafuta zaidi ya kutumia njia
hii” akasema Mark Piller
“Kwa nini mkaniweka
kando kuhusiana na masuala
haya?Kama si wewe kuamua
kunieleza leo hii
nisingefahamu chochote
kuhusu kile
kinachoendelea.Niliposhauriw
a tupeleke vikosi vyetu Afrika
mashariki niliamini ni kwa nia
njema ya kuzuia mauji
kuendelea kumbe ni mpango
umetengenzwa ili tukachukue
mafuta”
“Mheshimiwa Rais kama
nilivyokueleza awali kwamba
mambo haya yanafanywa kwa
siri kubwa sana na Rais wa
nchi hatakiwi kabisa
kufahamu kitu chochote na
hata mimi kukueleza
nimevunja kanuni zetu kwani
iwapo nitagundulika nitauawa
hivyo ni jukumu lako kuufunga
mdomo wako ili mimi na wewe
tuendelee kuwa salama”
akasema Mark Piller na
ukimya ukatawala.
“Mheshimiwa Rais !
akasema Mark Piller na Rais
William aliyekuwa
ameinamisha kichwa akainua
kichwa akamtazama
“Katika mpango huu
unaoendelea Afrika Mashariki
kuna mpango mwingine
umezaliwa ndani yake ambao
nao una manufaa makubwa
sana ambao unahusiana na
Iran”
“Una mpango gani kuhusu
Iran?akauliza William
“Nilikueleza awali kwamba
kwa muda mrefu tumekuwa
tukiichunguza Iran kufahamu
silaha zake bila
mafanikio.Nimekuja na
mpango mpya ambao unaweza
ukatusaidia kufahamu kuhusu
silaha za Iran na vile vile
kulipua kinu kikubwa
ambacho Iran inakitegemea
katika kurutubisha madini ya
Urani” akasema Mark Piller na
ile mikunjo katika sura ya Rais
William Washington
ikatoweka
“Nieleze kuhusu mpango
huo.Nini umekibuni? Akauliza
Rais William
“Kuna mtu ambaye
tumekuwa tukimtumia katika
mipango yote ya kufadhili
vikundi vya kigaidi ambavyo
tuna mashirikiano navyo.Mtu
huyo ni mwanamama anaitwa
Habiba Jawad.Huyu ni raia wa
Saudi Arabia.Mume wake
ndiye tuliyekuwa tukimtumia
katika kazi hiyo lakini baadae
alionyesha mabadiliko na
tukalazimika kumuua.Baada
ya kuuawa mkewe akarithi
utajiri wote na akaendelea
kuifanya ile kazi aliyokuwa
anaifanya mumewe yaani
kufadhili makundi ya
kigaidi.Tulimuwezesha kimtaji
na utajiri wake ni mkubwa
sana.Ni mmoja kati ya
mabilionea wa Saudi Arabia na
mwanamama mwenye
heshima kubwa.Toka
alipochukua jukumu hili
amelifanya kwa ufanisi
mkubwa.Mpaka sasa yeye
ndiye anayetambulika kama
mfadhili mkuu wa kundi la IS
na makundi mengine madogo
madogo ya kipalestina
yanayopigana na serikali ya
Israel.Ni kwa sababu yake hadi
leo dunia haifahamu kama
Marekani ndio wafadhili
wakuu wa kundi la IS na
itabaki hivyo.Hata ndani ya IS
ni watu wachache tu
wanaolifahamu hilo”
“Sifahamu hayo yote
unayonieleza Mark”akasema
Rais William
“Hupaswi kuyafahamu
mheshimiwa Rais.Si wewe tu
bali rais yeyote wa Marekani
hapaswi kuyafahamu
haya”akasema Mark Piller
“Mheshimiwa Rais,Habiba
Jawad anakuja
Marekani.Ananiletea mtu
mmoja ambaye amekubuhu
katika masuala ya ugaidi.Mtu
huyo tutamtuma Iran”
“Sijakuelewa
Mark.Tutamtumaje gaidi
kwenda Iran?Tunamtuma
akafanye nini?
“Gaidi huyo ambaye
Habiba anakuja naye ndiye
atakayekwenda Iran
kuchunguza kuhusu silaha za
Iran na mfumo wake wa
makombora na vile vile
kuharibu kinu kikubwa
ambacho Iran inakitegemea
katika urutubishaji wa madini
ya Urani” akasema Mark na
Rais William akajikuta akitoa
kicheko
“Sikupaswa kucheka lakini
Mark umenifanya nicheke.Kwa
nini umtume gaidi Iran badala
ya majasusi wetu? Magaidi
hawana mafunzo yoyote wao
wanachofahamu ni kuua
tu.Mpango huo ni wa chini
sana kufanywa na taifa kubwa
kama la Marekani lenye
maelfu ya majasusi wenye
ujuzi wa hali ya juu mno.Tuna
shirika kubwa la ujasusi kuliko
yote duniani.Tuwatumie hao
kuliko kumtuma gaidi
akafanye kazi kwa niaba
yetu.Huu ni mpango wa aibu”
akasema Rais William
“Mheshimiwa
Rais,nimekuwa ndani ya CIA
kwa muda mrefu.Hakuna kitu
ambacho kinaumiza vichwa
vya watu wa CIA kama suala la
Iran na Korea
Kaskazini.Pamoja na kuwa na
majasusi wa kiwango cha juu
mno bado mpaka leo
hatujafanikiwa kufahamu
kuhusu mfumo wa
makombora wa Iran au silaha
inazomiliki.Na hili ndilo
ambalo limeleta ugumu mpaka
leo tunasita kuitandika Iran
kijeshi kwani hatuna uhakika
yawezakana akawa kweli
anamiliki silaha za
maangamizi makubwa kama
wanavyodai.Kwa kuwa
majasusi wetu wameshindwa
tunataka kujaribu njia ya pili
ambayo ni kumtumia gaidi”
akasema Mark Piller
“Hiki ni kichekesho
Mark.Gaidi anawezaje
akaingia Iran na kufanya
uchunguzi kuhusu silaha zake?
“Mpango uko hivi
mheshimiwa Rais” akasema
Mark Piller na kunyamaza
akanywa maji kulainisha koo.
“Gaidi huyo tutampeleka
Afrika Mashariki ambako
atalipua ubalozi wetu jijini Dar
es salaam”
“Kulipua ubalozi wa
Marekani ?! William
akahamaki
“Ndiyo mheshimiwa Rais”
“Hilo ni jambo
lisilowezekana
kabisa.Hatuwezi kumtuma
mtu akalipue ubalozi wetu na
kuua watu wetu ! akasema kwa
ukali Rais William
“Tayari tumekwisha fanya
hivyo jijini Kampala
mheshimiwa Rais.Ubalozi
wetu kule ulivamiwa na
kuchmwa moto ule ulikuwa ni
mpango maalum umepangwa
ili kuwafanya wamarekani
wakubaliane na hatua ya
kupeleka vikosi vyetu Uganda”
akasema Mark Piller
“Mungu wangu ! akasema
William akimtazama Mark
Piller kana kwamba ni mara ya
kwanza anakutana naye
“Mheshimiwa Rais”
akaendelea Mark
“Tutaulipua ubalozi wetu
jijini Dar es salaam kisha
tutamkamata huyo gaidi na
kumpeleka mafichoni”
akasema Mark na kunyamaza
kidogo
“Miaka sita iliyopita ndege
ya shirika la ndege la Qatar
ikitokea Moscow Urusi
kuelekea Tehran ikiwa na
abiria mia moja ishirini na
saba ndani yake ililazimika
kutua kwa dharura katika
uwanja wa ndege wa Almaty
nchini Kazakhstan kufuatia
hitilafu iliyojitokeza katika
mojawapo ya injini zake.Baada
ya kutua abiria wote
walishushwa ndegeni na
kupelekwa hospitali kwa
uchunguzi wa afya zao kufuatia
wengi wa abiria kupatwa na
mstuko mkubwa kutokana na
tukio lile.Mheshimiwa Rais sisi
ndio tuliotengeneza tukio lile
hadi ndege ikatua nchini
Kazakhstan.Tulikuwa na
sababu maalum” akasema
Mark na kunyamaza kidogo
halafu akaendelea.
“Miongoni mwa abiria wa
ndege ile,walikuwemo
wanasayansi sita wa Iran
wakitokea nchini Urusi
ambako walikwenda kupatiwa
mafunzo ya siri namna ya
kutengeneza bomu la
nyuklia.Tulizipata taarifa hizo
na kutengeneza mpango ule
kisha tutakafanikiwa kuwapata
wanasayansi hao ambao
tunaendelea kuwashikilia hadi
sasa tukiendelea kuwahoji japo
hawajasema chochote”
“Wako wapi hao
wanasayansi?
‘Tunaendelea kuwashikilia
katika mojawapo ya nyumba
salama za CIA” akajibu Mark
“Gaidi tunayekusudia
kumtuma kulipua ubalozi wetu
Dar es salaam atakamatwa
baada ya kutekeleza shambulio
hilo.Kisha kamatwa atakwenda
kuunganishwa na wanasayansi
hao mahala walikofichwa na
kujenga ukaribu nao.Baada ya
kuzoeana nao atasuka mpango
wa kuwatorosha wanasayansi
hao na wakifanikiwa kutoroka
wataelekea moja kwa moja
nchini Iran.Serikali ya Iran
itakuwa na kila sababu za
kumuamini huyo gaidi kwani
kwa wakati huo dunia nzima
itakuwa ikifahamu kitu
alichokifanya yaani kulipua
ubalozi wa Marekani na Iran
watampokea kama
shujaa.Akiingia Iran ndipo
atakapoanza kuifanya kazi yetu
tuliyomtuma” akasema Mark
Piller na ukimya ukatawala
mle ndani halafu Rais William
akasema
“Mark huo unaonekana ni
mpango mzuri sana lakini
tatizo ni huyo jamaa ambaye
unataka kumtumia katika
mpango huo.Hana mafunzo ya
kijasusi na hawezi kutekeleza
vyema kazi aliyotumwa na
nina wasi wasi anaweza
akagundulika kuwa ametumwa
na Marekani na akauawa hivyo
tukakosa kila kitu”Rais
William akaonyesha wasiwasi
mkubwa
“Hata kama akigundulika
kwamba ametumwa na
Marekani tutakana tuhuma
hizo na dunia itatuelewa
kwanza mtu huyo si raia wa
Marekani na kwa wakati huo
atakuwa anajulikana kama
gaidi ambaye anatafutwa na
Marekani kwa kulipua ubalozi
wake jijini Dar es salaam na
vile vile atakuwa anatafutwa
kwa kutoroka kutoka katika
mahala alipokuwa
anashikiliwa.Kwa sababu hizo
mbili tutakuwa tumejitoa
katika jambo hilo lakini kwa
namna mpango ulivyo uhakika
wa mtu huyo kugundulika ni
mdogo sana”
“Yawezekana mkawa
mmejipanga vizuri kabisa
lakini tatizo ni uwezo wa huyo
gaidi kutekeleza mpango
mkubwa kama huu.Jambo
kama hili linahitaji jasusi
mbobezi.Tunao wengi sana
majasusi wa namna hiyo
ambao tunaweza kuwatumia
katika mpango huo.Kwa nini
tusitafute mmoja wao
tukamtumia badala ya huyo
gaidi? Sijaukataa mpango huu
lakini sikubaliani na mtu
mnayetaka kumtumia.Ni
mpango mzuri sana na kama
ungeniambia kwamba
anayekwenda kuutekeleza ni
jasusi nguli wa Marekani basi
ningekubaliana nawe kwa
asilimia mia moja lakini kwa
gaidi kwenda kutekeleza
mpango huo nashindwa
kukubaliana nawe Mark”
“Mheshimiwa
Rais,hatutaki kumtumia raia
wa Marekani katika jambo
hili.Mtu huyo ambaye Habiba
anakuja naye ni raia wa Saudi
Arabia ambao hawana
maelewano mazuri na
Iran.Endapo misheni
itashindwa kufanikiwa na mtu
huyo akakamatwa basi mzozo
utakuwa ni kati ya Iran na
Saudi Arabia sisi
hatutahusika.Kwa mujibu wa
Habiba Jawad mtu huyo
anayemleta ni mtu mahiri na
sahihi kwa kazi
hiyo.Atakapokuja hapa
tutampima na kuona uwezo
wake lakini sina wasiwasi naye
hata kidogo.Ninamuamini
Habiba Jawad.Nina uhakika
mkubwa mtu anayemleta
atakwenda kuitekeleza vyema
kazi tutakayomtuma akaifanye
Iran”
“Mark nina wasi wasi sana
kuhusu jambo hili unalotaka
kulifanya.Sijui kwa nini
ninakuwa na wasiwasi
mkubwa namna hii” akasema
Rais William
“Naomba uniamini
mheshimiwa Rais.Nina
uhakika mkubwa sana na hiki
ninachokwenda
kukifanya.Tumekuwa
tukifanya mambo kama haya
sehemu mbali mbali na
tukafanikiwa.Mheshimiwa
Rais katika haya
yanayoendeleaAfrika
Mashariki tutaua ndege wawili
kwa jiwe moja.Tunaongeza
akiba ya mafuta na vile vile
kwa mara ya kwanza
tutafanikiwa kujua aina ya
silaha ilizo nazo Iran.Haya ni
mafanikio makubwa sana
mheshimiwa Rais” akasema
Mark Piller
“Mark katika suala la
mafuta japo mmetumia njia
ambayo si ya kibinadamu
lakini nataka
niwapongeze.Tunahitaji sana
mafuta na nchi za Mashariki
ya kati ambazo ni wazalishaji
wakubwa wa mafuta duniani
ziko katika mgomo baridi wa
kuzalisha mafuta kwa lengo la
kutukomoa sisi kutokana na
sera zetu za kuiunga mkono
Israel.Wamesahau kwamba
Marekani wana uwezo wa
kupata mafuta kutoka sehemu
yoyote ile wanayoitaka.Kwa
sasa mafuta kutoka Afrika
yanaendelea kumiminika
katika hifadhi zetu za
mafuta.Hongereni sana
Mark.Japo niliwekwa pembeni
katika jambo hili lakini lazima
niwapongeze.”
“Ahsante sana
mheshimiwa Rais” akasema
Mark Piller
“Kuna kitu nataka
kukiongeza hapo.Eneo hili la
ukanda wa Afrika Mashariki ni
tajiri sana.Lina utajiri mkubwa
wa madini mbali mbali
ambayo tunayahitaji mno.Kwa
mfano nchini Tanzania pekee
yanapatikana madini ya
thamani kubwa yanaitwa
Tanzanite ambayo
hayapatikani sehemu nyingine
yoyote duniani zaidi ya
Tanzania,yapo pia madini
mengine kama
dhahabu,almasi,na zaidi sana
madini ya Urani.Ukienda
Uganda kuna mafuta,ukienda
jamhuri ya kidemokrasia ya
Congo kuna madini mengi pia
ya thamani kubwa.Kwa ujumla
eneo hili lote limejaa
madini.Kwa kuwa tayari
tumekwisha ingia Afrika
Mashariki ni jukumu letu
kuhakikisha tunajiimarisha na
tunakwenda mbali zaidi ya
mafuta.Wekeni mikakati ya
kuhakikisha tunaongeza vikosi
zaidi Afrika Mashariki na
tunakwenda mbali zaidi kwa
kupeleka vikosi vyetu sehemu
zile zenye utajiri lakini jambo
hili lifanyike kwa ustadi na
umakini mkubwa kama
mlivyofanya katika haya
machafuko.Nataka hadi
tutakapoondoa vikosi vyetu
Afrika mashariki tuwe
tumefaidika na akiba kubwa ya
mafuta na madini mengine ya
thamani”akasema Rais
William
“Mheshimiwa Rais
ninashukuru kwa kuanza
kuelewa kile tunachokifanya
kwa ajili ya nchi yetu.Ili
tuendelee kujiimarisha na
kukaa muda mrefu zaidi Afrika
Mashariki inatulazimu
kutafuta namna ya kuongeza
machafuko katika ukanda huo
wa Afrika Mashariki.Nitakaa
na wenzagu tuone namna ya
kufanya lakini kuna kitu
ninakifikiria ambacho
kinaweza kutupa sababu ya
kuongeza vikosi vyetu na
tukaendelea kuchota
Rasilimali” akasema Mark
Piller
“Nini unakifikiria
kuhusiana na hilo wazo langu?
Akauliza William
“Kutoka katika machafuko
haya yanayoendelea Afrika
Mashariki ninafikiria
kuanzisha kikundi cha uasi
ambacho tutakipa nguvu na
kukifadhili silaha kali ambacho
kitasambaa katika nchi za
Tanzania na Uganda.Hatuna
shida sana na nchi ya
Kenya.Shida yetu ni
Tanzania,Uganda na jamhuri
ya kidemokrasia ya Congo nchi
ambazo zina utajiri
mkubwa.Kikundi hicho
ambacho kitasambaa katika
nchi hizo tatu kitawezeshwa
silaha nzito na kuendelea
kulifanya eneo la Afrika
mashari liwe ni eneo hatari na
sisi tutaongeza vikosi vyetu
Afrika Mashariki kulinda
amani.Nitazungumza na
Jenerali Akiki kuhusiana na
suala hili na tutaona nini
tukifanye lakini
nakuhakikishia mheshimiwa
Rais kwamba haya maelekezo
yako yatafanyiwa
kazi.Ninachokuomba niamini
na kila kinachoendelea
nitakujulisha lakini nakuomba
haya niliyokwambia iwe ni siri
yako asifahamu mtu mwingine
yeyote mambo haya.Narudia
kukupa angalizo mheshimiwa
Rais kwamba endapo haya
niliyokwambia yatavuja
utakuwa ni mwisho wetu.Hii
ni moja kati ya siri kubwa sana
ya nchi ya Marekani” akasema
Mark Piller
Mazungumzo yao
yalidumu kwa saa tatu kisha
wakaagana na Mark Piller
akaondoka zake.
DAR ES SALAAM –
TANZANIA
MAKAO MAKUU YA SNSA
Saa mbili za asubuhi
wafanyakazi wa idara ya siri ya
usalama wa ndani wa nchi
wakiwa katika ofisi yao kuu
wakiendelea na majukumu yao
katika ukumbi mkubwa
waliyaelekeza macho yao
katika runinga kubwa mbili
wakifuatilia picha kutoka
katika drone kubwa zilizokuwa
zinazunguka angani juu ya jiji
la Dar es salaam kufuatilia hali
inavyokwenda.Mitaa mingi
hata ile ambayo ilizoeleka
kuwa na msongamano
mkubwa wa watu ilikuwa
mitupu.Makundi ya watu
yakijiandaa kwa ajili ya
kuendelea na mapambano
yalionekana katika sehemu
mbali mbali za jiji.Vikosi vya
ulinzi viliendelea kufanya
doria katika baadhi ya mitaa
lakini barabara nyingi zilikuwa
zimefungwa kwa kuwekwa
mawe makubwa na kuchomwa
matairi.Katika baadhi ya picha
yalionekana majengo
yakiungua moto.Maiti za watu
zilionekana pia katika baadhi
ya mitaa.
Wakati wafanyakazi wale
wakiendelea kufuatilia picha
zile,katibu muhtasi wa Ruby
akamfuata na kumjulisha
kwamba Rais anataka
kuzungumza naye katika
simu.Haraka haraka Ruby
akaenda ofisini kwake na
kuinua mkono wa simu
“Mheshimiwa Rais
shikamoo” akasema Ruby
“Marahaba Ruby vipi
mnaendeleaje?akauliza Rais
Dr Fabian
“Tunaendelea vizuri
mheshimiwa Rais.Tunafuatilia
picha za drone kuona namna
hali ilivyo katika mitaa mbali
mbai ya jiji lakini hali bado ni
tete.Barabara nyingi
zimefungwa,majengo
yanaungua moto makundi ya
watu wanaendelea kujiandaa
kuingia mitaani katika
vurugu.Huduma hazipatikani
na maisha yanazidi kuwa
magumu” akasema Ruby
“Nimepokea taarifa
asubuhi hii kutoka kwa mkuu
wa jeshi la polisi kwamba bado
hali ni tete huko mitaani.Hata
hivyo nimekupigia kukujulisha
kwamba ndani ya dakika kumi
zijazo mawasiliano ya simu
yatarejeshwa kama ulivyokuwa
umeshauri na baadae
nitalihutubia taifa ili tuone
kama inaweza ikasaidia
kupunguza vurugu hata kwa
kiasi kidogo” akasema Dr
Fabian
“Ahsante sana
mheshimiwa rais kwa
kulifanya kazi suala hili.Nina
uhakika linaweza kuwa na
matokeo mazuri na watu
wakakuelewa” akasema Ruby
“Ruby kubwa ambalo
limenifanya nitake
mawasiliano ya simu
yarejeshwe ni ili kuwawezesha
kumfuatilia Karim.Mliniambia
kwamba kukosekana kwa
mawasiliano kumewafanya
mkashindwa kumfuatilia Yule
jamaa.Mawasiliano yatarejea
muda si mrefu nataka
mumfuatilie Karimu na
kuhakikisha mnafahamu kila
kitu kuhusu yeye na jioni ya
leo nipewe taarifa kama tayari
mmemkamata au vipi”
akasema Dr Fabian
“Mheshimwia Rais
tutalifanyia kazi suala hilo na
jioni ya leo nitakujulisha kile
ambacho tutakuwa tumekipata
katika uchunguzi wetu
kuhusiana na Karim Abdallah”
akasema Ruby na kuagana na
Rais kisha akakaa katika
kompyuta yake kwa dakika
tano akafanya kazi fulani
halafu akarejea katika ule
ukumbi mkubwa ambako
wafanyakazi wa SNSA
walikuwa wanaendelea
kufuatilia picha za Drone
kujua hali ilivyo katika mitaa
mbali mbali ya jiji la Dar es
salaam.
“Naomba tusikilizane
jamani” akasema Ruby na
watu wote wakawa makini
kumsikiliza
“Toka machafuko haya
yalipoanza mawasiliano ya
simu yalikatwa kwa lengo la
kuzuia watu kutumia simu
kuhamasishana kuhusu
vurugu.Pamoja na kukata
mawasiliano ya simu lakini
bado haijasaidia kupunguza
vurugu” akanyamaza kidogo
halafu akaendelea
“Muda mfupi uliopita
nimetoka kuzungumza na
mheshimiwa Rais na
amenieleza kwamba ndani ya
dakika chache zijazo
mawasiliano ya simu
yatarejeshwa” akanyamaza
baada ya watu kushangilia
“Jana usiku tulikuwa na
mazungumzo na Rais
tukamuomba aruhusu
mawasiliano ya simu
yarejeshwe na amekubali ombi
letu hivyo ndani ya muda
mfupi mawasiliano ya simu
yatarejea.Kubwa ambalo
lilinifanya nimuombe Rais
aruhusu mawasiliano ni kwa
ajili ya kumchunguza huyu
mtu” akasema Ruby na
kubonyeza kitanza mbali na
picha ya Karim Abdallah
ikaonekana runingani
“Anaitwa Karim
Abdallah.Ni mwenyekiti wa
chama cha siasa cha TPD.Kwa
nini ameonekana katika
runinga yetu? Huyu jamaa
kabla machafuko hayajaanza
aliandika ujumbe wa
uchochezi katika ukurasa wake
wa twitter akiwataka waislamu
wa mkoa wa Tanga waungane
wakawatafute wale waliomuua
Sheikh mkuu wa mkoa huo
aliyeuawa na watu
wasiojulikana.Ujumbe huo
japo aliufuta haraka lakini
tayari ulikwisha somwa na
watu wengi.Tunajiuliza nini
sababu ya kuandika ujumbe
kama ule? Kuna wasiwasi
machafuko haya
yanayoendelea yakawa na
chembe chembe za kisiasa
ndani yake hivyo nataka
mawasiliano yatakaporejea
tuanze kumfukua huyu jamaa
kufahamu kila taarifa
zake.Tunahitaji kujua mahala
alipo,kufahamu nani
anawasiliana nao na
wanawasiliana nini,marafiki
zake ni akina nani.Kwa ujumla
nataka tufahamu kila kitu
kumuhusu huyu jamaa.Sasa
kila mmoja aende mahala pake
na tuanze kazi mara moja”
akasema Ruby kisha akaelekea
ofisini kwake akaichukua simu
yake akaiwasha tayari
mawasiliano yalikwisha rejea.
“Ahsante Mungu.Sasa kazi
inaanza”akasema Ruby
RIYADH – SAUDI ARABIA
Toka Mathew alipoondoka
na Habiba kuelekea
Marekani,Najma hakutoka
ndani.Alikuwa amejifungia
chumbani kwake akiwa na
mawazo mengi sana.Pembeni
yake kulikuwa na simu ya
Mathew pamoja na kitabu
cheusi.Aliishika simu ile na
kuitazama halafu akairusha
pembeni
“Huyu Ruby ambaye Abu
ameandika namba zake za
simu katika kitabu chake cha
kumbu kumbu ni nani?Kwa
nini nilipomuuliza Ruby ni
nani alibadilika na haraka
haraka akaninyang’anya kile
kitabu? Akawaza Najma.
“Katika simu yake amepiga
namba za Ruby zaidi ya mara
tatu lakini kwa bahati mbaya
simu hiyo haikuwa
ikipatikana.Tatizo langu nina
wivu mbaya mno na hii ndiyo
sababu kubwa iliyonifanya
nikawa sitaki kuingia katika
masuala ya
mahusiano.Ninampenda sana
Abu Zalawi na sitaki awe na
mwanamke mwingine zaidi
yangu” akaendelea kuwaza
Najma
“Najilaumu sana kwa
kuingia katika mahusiano na
Abu Zalawi bila kuifahamu
historia yake ametoka wapi na
maisha yake yalikuwaje huko
alikotoka.Je alikuwa na mke
au na familia?Hata yeye
mwenyewe hajawahi kunieleza
chochote kuhusiana na
historia yake” Najma akainuka
kitandani na kukaa
“Lakini kwa nini niteseke
wakati namba za simu za huyo
Ruby ninazo? Kwa nini
nisimpigie kuufahamu
ukweli?Yawezekana akawa ni
rafiki yake au ni mtu ambaye
waliwahi kuifanya kazi
wote.Nimepata wivu kwa
sababu Abu hajawahi
kuonyesha kumafuta simuni
mwanamke kama alivyofanya
kwa Ruby jana” Najma
akaendelea kutafakari
“Hapana siwezi kuendelea
kuumia.Ngoja nimpigie simu
huyu Ruby nimfahamu vizuri
na nifahamu ana mahusiano
gani na Abu” akawaza Najma
na kubonyeza namba zile za
Ruby akapiga simu ikaanza
kuita akahisi kama mwili
unamtetemeka.
“Simu yake inaita”
akawaza huku akihisi woga
kwa mbali
“Hallow ! ikasema sauti ya
mwanamke upande wa pili wa
simu na Najma akasita kujibu
“Hallow ! ikaita tena sauti
ile
“Hallow ! akasema Najma
kwa lugha ya kiingereza
“Habari yako?akauliza
Yule mwanamke upande wa
pili
“Nzuri habari yako?
“Nzuri.Nazungumza na
nani kutokea wapi?
“Naitwa Najma niko
Riyadh Saudi Arabia”
“Riyadh ! Yule mwanamke
akaonyesha mshangao
“Ndiyo.Wewe uko
wapi?akauliza Najma na Yule
mwanamke akasita kidogo
“Hallow ! Najma akaita
“Najma
umenifahamuje?Umepata
wapi namba zangu za simu?
“Unamfahamu Abu
Zalawi? Akauliza Najma
“Abu Zalawi?yule
mwanamke akashangaa
“Ndiyo unamfahamu?
Najma akauliza
“Hapana simfahamu.Ni
nani huyo mtu?
“Ni mume wangu lakini
ana namba zako katika kitabu
chake cha kumbukumbu za
mawasiliano na jana alikupigia
simu mara tatu lakini simu
yako haikuwa ikipatikana”
akasema Najma
“Utanisamehe dada yangu
lakini simfahamu mtu mwenye
jina hilo na wala sijawahi kuwa
na rafiki mwenye jina hilo la
Abu Zalawi.Ni mara ya kwanza
ninalisikia”
“Abu ameandika namba
zako za simu katika kitabu
chake na alikupigia alionekana
ana jambo la muhimu sana
anataka kukueleza.Kwani
wewe si Ruby?akauliza Najma
na mwanamke wa upande wa
pili akasita
“Hallow? Najma akaita
“Nakuuliza kwani wewe si
Ruby?Najma akauliza tena
“Naweza kuzungumza na
huyo Abu Zalawi ” akauliza
Yule mwanamke
“Abu Zalawi amesafiri
Alfajiri ya leo.Naomba
tafadhali kama akikupigia tena
simu usimwambie chochote
kuhusu mimi kukupigia
simu.Ahsante sana nimefurahi
kuzungumza nawe japo
umekataa kunitajia jina lako”
akasema Najma na kukata
simu akashusha pumzi na
kutazama namba zile halafu
akaigiza namba za mwanzo
katika kompyuta yake ili kujua
namba zile ni za nchi gani na
majibu yakaja kuwa ni
Tanzania.
“Tanzania ! akasema
Najma na kuvuta pumzi ndefu
“Niliona kwa macho yangu
mawili katika kitabu chake
ameandika jina Ruby.Iweje
huyu mwanamke niliyempigia
ambaye japo amekataa
kunitajia jina lake lakini
naamini ni Ruby akane
kumfahamu Abu? Akajiuliza
Najma
“Au Abu ana jina lingine
anatumia tofauti na Abu
Zalawi?Amefahamiana vipi na
uyu mwanamke wa Tanzania?”
akawaza Najma
“Ninahitaji kumfahamu
Abu Zalawi kiundani na mtu
pekee ambaye anaweza
akanieleza kila kitu kuhusiana
na huyu mtu ni
mama.Atakaporejea katika
hiyo safari waliyokwenda
nitamtaka anieleze ukweli
kuhusiana na Abu Zalawi
kwani kuna mambo yameanza
kunipa mashaka sana
kuhusiana na huyu mtu.Mama
amefahamiana vipi na
Abu?Kuna kitu gani
wanakipanga? Nitafahamu kila
kitu watakaporejea” akawaza
Najma
DAR ES SALAAM –
TANZANIA
Ruby aliendelea kuishikilia
simu yake baada ya
kuzungumza na Najma.
“Abu Zalawi ! akajiuliza
“Ni nani huyo mtu?
Sijawahi kuwa na rafiki yeyote
mwenye jina hilo la Abu Zalawi
wala sina rafiki yeyote Saudi
Arabia sasa huyu mtu
amenifahamuje hadi ana
namba zangu tena
ninazotumia hapa Tanzania ?
Sijawahi kumpa namba za
simu ninazotumia Tanzania
mtu wangu yeyote wa nje ya
nchi,huyu Abu Zalawi
amezpata wapi?” akajiuliza
Ruby
“Au labda Uingereza
wamekwisha gundua kwamba
sikufariki katika ile ajali ya
ndege na sasa wanaanza
kunichunguza ili wapate
uhakika kama ni mimi?
Akaendelea kujiuliza
“Kwa nini nisimpigie simu
Najma na kumtaka anitumie
picha ya huyo Abu Zalawi
nimuone kama ninamfahamu?
Nadhani hilo litakuwa jambo
jema” akawaza na kuchukua
simu akampigia Najma kwa
kutumia zile namba
alizompigia.
“Hallow” akasema Najma
baada ya kupokea
“Najma samahani sana
kwa usumbufu,Unaweza
ukanitumia picha ya Abu
Zalawi nimuone kama ni mtu
ninayemfahamu?akauliza
Ruby
“Sawa ninakutumia muda
si mrefu” akasema Najma na
kupekua simu ya Mathew
lakini hakukuwa na picha hata
moja ya Mathew.Akapekua
katika simu yake lakini
hakukuwa na hata picha moja
ya Mathew akachanganyikiwa
“Haya mbona ni maajabu
makubwa.Picha zote
zimekwenda wapi? Tumepiga
picha nyingi sana tukiwa
katika mapumziko.Ni maelfu
ya picha lakini hakuna hata
picha moja na sielewi
zimekwenda wapi” akawaza na
kuchukua kamera yake
ambayo nayo pia alikuwa
anaitumia wakati wakiwa
mapumzikoni lakini hakukuwa
na picha hata moja.
“Mungu wangu haya
mbona maajabu? Akasema
kwa mshangao na kuchukua
kompyuta yake mpakato na
haraka haraka akafungua
sehemu ya kuhifadhi picha
ambako alikuwa anahifadhi
picha kila pale kadi ya
kuhifadhia kumbu kumbu
ilipojaa lakini akakutana na
kioja kwani zile picha zote
ambazo walipiga katika
mapumziko hazikuwepo.
“Jamani haya ni mambo
gani yanatokea?Tumepiga
maelfu ya picha kwa miezi
mitatu na hata jana nilikuwa
nazitazama nikichagua zile
nzuri kwa ajili ya kuweka
kumbu kumbu lakini ajabu leo
hii hakuna hata picha
moja.Hakuna picha katika
simu yangu,ya Abu,katika
kamera na hata katika
kompyuta.Zimekwenda
wapi?Nani amezifuta na kwa
nini?akajiuliza na mara simu
yake ikaita tena akazitazama
zile namba ni Yule mwanadada
aliyempigia kutoka Tanzania
“Nitamjibuje huyu dada?
Ataniona mwongo” akawaza
Najma halafu akaipokea ile
simu
“Najma samahani
umeipata picha hiyo ya Abu
Zalawi?akauliza
“Hapana
bado.Nitakutumia baadae
kidogo naomba unisubiri”
akasema Najma na kukata
simu.
“Haya ni maajabu ambayo
sijawahi kuyashuhudia”
akawaza na kuendelea
kupekua kompyuta yake kama
angeweza kupata picha zile
akini hakukuwa na picha
yoyote
“Humu ndani hakuna mtu
mwingine yeyote aliyeingia
zaidi yetu mimi na Abu.Kama
angekuwa mtu mwingine
ameingia ningehisi labda ndiye
aliyefuta picha hizo lakini
hakuna tulikuwa humu watu
wawili pekee.Ningeweza
kusema ni kirusi labda
kimefuta picha hizo lakini
picha zilizofutwa ni zile
nilizopiga na Abu pekee
nyingine zote zipo” akawaza na
kushika kidevuni
“Hapa kuna kitu
kinaendelea.Picha zile
hazijajifuta zenyewe bali
zimefutwa kwa sababu
maalum na aliyezifuta lazima
atakuwa ni Abu.Kwa nini
akafanya hivi? Amefuta muda
gani hizo picha? Najma
akapandwa na hasira
“Huyu Abu Zalawi ni nani
hasa?Mbona anaanza kunipa
mashaka? Nadhani nahitaji
kumfahamu kwa undani zaidi
ni mtu wa aina gani
huyu.Yawezekana
ninavyomfahamu sivyo alivyo”
akaendelea kuwaza Najma.