Riwaya: Sala ya Sarah

Riwaya: Sala ya Sarah

RIWAYA : SALA YA SARAH.

MTUNZI : ALEX KILEO.

SEHEMU YA ISHIRINI NA MBILI.

ILIPOISHIA....................

Baada ya muda yule bwana aliyekuwa anatoa matangazo alikuwa amemaliza na sasa askofu akachukua kipaza sauti, kisha akawasalimu waumini waliohudhuria ibada, baada ya hapo akairudia ile sala iliyowahi kuombwa na Sarah miaka mingi iliyopita, wakati akiirudia ile sala, Taita alishtuka, tena uzuri alikuwa amekaa kiti cha mbele kabisa pamoja na Harry ambaye nae alipata mshtuko,

Masikio na mwili wa Taita vikapata ubaridi kwa pamoja wakati askofu akiirudia ile sala, Taita akakumbuka na ule ujumbe aliouona kwenye box upande wa chini, box ambalo kiliwekwa kichwa cha Toisa, ila bado Taita alisubiri kusikia ni kipi askofu ataongea baada ya kuirudia sala ile,

"Sasa baada ya kuirudia sala hii iliyowahi kuombwa na mtoto mdogo miaka kumi na Tisa iliyopita, leo hii huyu mtoto yupo hapa, namuomba asogee mbele" Askofu aliongea kisha Sarah akawa anajongea mbele huku waumini wakimpigia makofi. Sarah alipofika mbele akapewa kipaza sauti,

"Naitwa Sarah, Sarah Isack" Sarah aliongea kisha akatupia macho mahali walipokaa Taita na Harry na kuwaona namna walivyopata mshtuko, tena sio kidogo........

************ENDELEA***********

Sarah akatabasamu, halikuwa tabasamu alilolipanga, lilikuwa ni tabasamu lililokuja ghafla baada ya kuwaona maadui zake walivyopata mshtuko baada ya yeye Sarah kujitambulisha.

"Mimi ndiye yule mtoto niliyetoa sala miaka kumi na tisa iliyopita, na niliitoa nikiwa na maanisha kile nilichokiomba, sikuwa nasali tu ili mradi maneno yanitoke, nilitaka niwe mkubwa na niwe moto, tena moto kweli, nashukuru nimekuwa hivyo" Sarah aliongea na kufanya baadhi ya waamini wabaki na maswali, sio hao tu, mpaka askofu mwenyewe sura yake ilionesha ana swali,

"Umekuaje moto sasa?" Askofu alijikuta anauliza bila kutegemea,

"Na ninaposema nimekuwa moto simaanishi nawaka, hapana, maana yangu ni ule uwezo niliokuwa nao wa kushinda kila kikwazo kilichopo mbele yangu, na nadhani hiyo yote ni kutokana na Mungu kusimamia kila nifanyacho. Nawashukuru sana, maana mimi ni muongeaji sana, mnaweza shangaa naongea tu mpaka nachukua muda wa misa zote" Sarah alitania kisha waumini wakacheka, Sarah akarudisha kipaza sauti kwa askofu.

"Pia napenda kuwaambia habari njema kuhusu Sarah, Sarah ametoa ahadi ya kutoa mifuko mia moja ya cement kwa ajili ya kabisa" Askofu aliongea na waumini wakalipuka kwa furaha na huku wengine wakipiga makofi na vigele gele.

"Basi nadhani tutegemee kumuona hapa sarah mara kwa mara kwa maana amekuzwa na imani yetu" Askofu aliongea kisha akaweka kipaza sauti sehemu husika, kisha wakaongea kidogo na Sarah na baada ya hapo Sarah akawapa mikono mapadri na watumishi waliokuwepo mbele ya kanisa, kisha Sarah na askofu wakaanza kutoka kuelekea nje ya kanisa.

Walipokuwa wanatoka ndipo Sarah akayapeleka macho yake sehemu alipokuwa amekaa Taita, wakagongana macho, Sarah akatabasamu kisha akambinyia jicho Taita ambaye muda wote alikuwa amekamatwa na mshangao.

Sarah alitoka moja kwa moja mpaka ofisini kwa askofu,

"Sina muda tena was kukaa hapa, labda unisaidie tu namba ya account ya benk ambayo inatumiwa na kanisa" Sarah aliongea huku akimtupia jicho askofu ambaye alikuwa ameshika pen na akachukua karatasi akaandika namba ambayo Sarah anaihitaji,

"Mbona haraka hivyo" Askofu alimuuliza huku akimpatia ile karatasi,

"Kawaida, nitarudi siku chache zijazo baba askofu, ila pesa nitaiingiza kesho mapema kwenye account ya kanisa, kwa maana leo jumapili benki zimefungwa" Sarah aliongea huku akinyanyuka katika kiti,

"Sawa haina shida" askofu aliongea huku akipeana mkono na Sarah, kisha Sarah akaondoka zake.

Sarah alipotoka kwenye mlango was askofu, alipiga hatua za haraka haraka mpaka nje ya uzio wa kanisa na kwenda kuingia kwenye bajaj ambayo ndiyo ilimleta eneo lile la kanisa,

"Subiri kidogo, kuna mtu namsubiri" Sarah alimwambia dereva bajaj ambaye alitaka aiwashe bajaj yake,

"Sawa bosi" dereva bajaj alijibu na kutulia.

Baada ya dakika chache waumini walianza kutoka katika jengo la ibada kumaanisha kwamba misa imeisha, hapo ndipo Sarah aliweza kumuona Taita na Harry wakitoka, akashuhudia namna wanavyoangaza angaza macho wakiashiria kuwa kuna kitu wanatafuta.

Baada ya muda aliwashuhudia wakiongozana kuelekea ofisi ya askofu, Sarah akatabasamu peke yake,

"Haya washa bajaj tuondoke" Sarah alimwambia dereva Bajaj ambaye alitii na kuiwasha bajaj kisha wakaondoka taratibu na kupotea eneo lile la kanisa.

********************

Taita na Harry walielekea moja kwa moja mpaka mlangoni kwa askofu na kubisha hodi, askofu akaitikia na kisha wakaingia ndani, wakamsalimia askofu na kujikaribisha wenyewe kwenye viti,

"Samahani kwa kukuingilia" Taita aliongea huku akitabasamu,

"Bila samahani" Askofu alijibu,

"Nilikuwa nahitaji kuonana na yule binti, Sarah" Taita aliongea huku akimtazama askofu,

"Una maongezi nae labda, au kuna chochote?" Askofu alimuuliza Taita,

"Yule ni mtoto wa marehemu Dada yangu, baada ya Dada yangu kufariki miaka kumi na Tisa iliyopita, Sarah aliondoka na kwenda kusoma uingereza, sijawahi kubahatika kumuona tena mpaka leo" Taita aliongea,

"Kwa hiyo anakuita Mjomba?" Askofu alimuuliza,

"Ndio" Taita alijibu,

"Sawa, ila kwa bahati mbaya huyo Sarah ameshaondoka" Askofu alitoa jibu lililofanya Harry na Taita watazamane,

"Ameondoka muda mrefu?" Harry aliuliza,

"Sasa hivi tu" Askofu alijibu,

"OK, basi nisaidie namba yake ya simu" Taita aliongea huku akiitoa simu yake mfukoni,

"Bahati mbaya ameniambia kuwa hana simu" Askofu alitoa jibu jingine lenye ukakasi,

"Dah, hajasema hata eneo analoishi?" Taita aliuliza tena,

"Hapana, ila kama shida yako ni kuonana nae tu, mtaonana, maana atakuwa anakuja hapa mara kwa mara" Askofu akajibu,

"Sawa askofu, akirudi basi naomba unifahamishe, maana ni mtu muhimu sana kwangu" Taita aliongea,

"Sawa"'Askofu alijibu kisha Taita na Harry wakaondoka zao na kumuacha Askofu akiendelea na mambo yake.

Taita na Harry walielekea moja kwa moja kwenye gari walilokuja nalo na kumkuta Trigger akiwa anawasubiri ndani ya gari,

"Mbona ibada imeisha muda tu, alafu ninyi mnatoka sasa hivi?" Trigger aliwauliza huku akiwasha gari,

"Trigger moto umewaka sasa, ni jinsi gani tutauzima?" Taita aliuliza huku akijifuta jasho. ila swali alilouliza ni kwamba Trigger hakulielewa,

"Moto umewaka wapi?" Trigger aliuliza huku akimtupia jicho bosi wake huyo,

"Kumbe matukio yote tunayofanyiwa na mtu asiyejulikana, kumbe mtu huyo ni Sarah" Taita aliongea huku macho yakiwa mbele,

"Sarah kale kabinti ka kipindi kile, Dada ake vin?" Trigger aliuliza kwa mshangao,

"Ndio huyo huyo" Taita alijibu kinyonge,

"Yaani kale katoto ndio kamekuwa hatari hivyo?" Trigger aliuliza huku akitoa tabasamu lililoambatana na mshangao,

"Nadhani amekuja kulipa kisasi, sasa basi umakini uongezeke, jambo zuri ni kwamba tumeshamjua adui yetu" Taita aliongea,

"Jioni itabidi tuitishe kikao, lazima tujadili hili jambo" Harry aliongea,

"Ni kweli" Taita alijibu wakati gari ikiingizwa ndani ya uzio wa nyumba yake.

**"****************

Sarah alielekea moja kwa moja mpaka katika sehemu ambapo yanauzwa magari, akaingia ndani na kuwasalimia wahusika,

"Nimekuja kuangalia magari" Sarah aliongea baada ya salamu,

"Karibu, twende upande ule" Kijana aliyekuwa muuzaji aliongea huku akinyooshea kidole upande ambao anatakiwa aende.

Wakaelekea mpaka katika huo upande ambao kulikuwa na gari ndogo nyingi, Sarah akaanza kutafuta gari ambayo alihisi itamfaa. Baada ya dakika ishirini alisimama mbele ya gari ambayo ilionekana ameipenda, ilikuwa ni range rover sports, nyeusi.

"Bei gani hii" Sarah aliuliza huku akiikagua tairi zake, muuzaji akamtajia bei,

"Mnapokea cash au cheque?" Sarah akauliza,

"Tunapokea vyote, ila cash nadhani ndio haina mlolongo mrefu, ukishakabidhi tu unapatiwa gari, ila cheque ukikabidhi hupatiwi gari mpaka benki itoe uhakiki kuwa ni kweli account yako ina fedha hizo" Kijana muuzaji alitoa ufafanuzi,

"Sawa, nitatoa cash" Sarah aliongea huku akitabasamu,

"Ikague kwanza vizuri gari yako, alafu twende ofisini tukakabidhiane pesa" Kijana muuza magari aliongea huku akifungua mlango was ile gari na kisha Sarah akaanza kuikagua upande wa ndani, alipojiridhisha, walienda ofisini na kukabidhiana pesa, kisha Sarah akatoka na gari yake.

*****************

Mida ya saa kumi jioni, Taita na vijana wake walikuwa Vin hotel wakiendelea na kikao kizito kumuhusu Sarah,

"sasa mnaona kipi kifanyike kumdhiti au kummaliza kabisa Sarah?"Taita aliuliza,

"yaani suala la kumdhiti au kummaliza yote hayawezekani, kwa maana yeye anatujua vizuri sisi kuliko sisi tunavyomjua yeye" Tekso alijibu katika sauti ya utulivu,

"nadhani kumdhibiti tunaweza" Trigger aliongea kisha akachukua glass ya maji na kuipeleka kinywani na wenzake wakawa wanangojea kumsikiliza,

"tunamdhibiti vipi sasa?"Harry aliuliza baada ya kumuona Trigger yupo kimya ingali amemaliza kunywa maji,

"babu yake Sarah si yupo? nadhani tunatakiwa tumteke, alafu Sarah ni lazima ajue tu, akishajua ni lazima atatutafuta" Trigger aliongea na wenzake wakampigia makofi,

"hiyo ifanyike lini? " Taita aliuliza huku akitabasamu,

" leo hii, maana tukichelewa yule demu anaweza kutuzidi akili " Trigger alijibu,

"safi, nadhani muda huu Trigger chukua vijana na muende mkafanye hichi tulichopanga" Taita aliongea huku akimtazama Trigger.

********************

Mishale ya saa mbili usiku Sarah alikuwa yupo juu ya sofa ndani ya sebule yake akicheza game, play station, alikuwa akicheza game ya kivita, kitu ambacho hakukijua ni kuwa muda huo Trigger na vijana wake walikuwa wameizunguka nyumba ya babu yake.

Trigger baada ya kuizunguka nyumba ile na kujiridhisha hakuna kitu chochote cha kuwazuia, aliwahamrisha vijana wake na kuusogelea mlango, walipoufikia waligonga hodi, mlango ukafunguliwa na babu yake Sarah, ila cha ajabu alikutana na mdomo wa bunduki,

"eh!!! Shusha bunduki wewe" Babu Sarah alijikuta akitamka hayo maneno Bila kutegemea,

"Trigger akikunyooshea bunduki uwa haishushi chini mpaka risasi itoke" Trigger aliongea huku akitabasamu kisha akafyatua risasi kumuelekea babu yake Sarah................

**********ITAENDELEA***********

the Legend☆
 
RIWAYA : SALA YA SARAH.

MTUNZI : ALEX KILEO.

SEHEMU YA ISHIRINI NA TATU.

ILIPOISHIA.....................

Mishale ya saa mbili usiku Sarah alikuwa yupo juu ya sofa ndani ya sebule yake akicheza game, play station, alikuwa akicheza game ya kivita, kitu ambacho hakukijua ni kuwa muda huo Trigger na vijana wake walikuwa wameizunguka nyumba ya babu yake.

Trigger baada ya kuizunguka nyumba ile na kujiridhisha hakuna kitu chochote cha kuwazuia, aliwahamrisha vijana wake na kuusogelea mlango, walipoufikia waligonga hodi, mlango ukafunguliwa na babu yake Sarah, ila cha ajabu alikutana na mdomo wa bunduki,

"eh!!! Shusha bunduki wewe" Babu Sarah alijikuta akitamka hayo maneno Bila kutegemea,

"Trigger akikunyooshea bunduki uwa haishushi chini mpaka risasi itoke" Trigger aliongea huku akitabasamu kisha akafyatua risasi kumuelekea babu yake Sarah................

*********ENDELEA***********

Risasi ilitoka moja kwa moja na kutua kwenye bega la kulia la babu yake Sarah, wenzake na Trigger wote wakapata mshtuko kwa maana hawakuambiwa wamdhuru yule mzee,

"umefanya kosa mkuu, hakutakiwa apigwe risasi huyu mzee" Strategic aliongea kwa upole,

"kosa sio langu, ni sheria tu nilizojiwekea ndio zimefanya nimpige huyu mzee" Trigger aliongea huku akimtazama babu yake Sarah aliyekuwa amelala sakafuni huku akiwa amepoteza fahamu,

"sheria gani hizo mkuu?" Strategic aliuliza huku akitabasamu,

"Trigger akikuelekezea bastola uwa haishushi mpaka itoe risasi" Trigger alijibu na kipindi hicho baba yake mdogo Sarah alikuwa akijongea sebuleni baada ya kusikia kelele za watu, alipotokezea tu sebuleni alikutana na mdomo wa bastola, ila hakunyooshewa na Trigger, alinyooshewa na Tekso,

"hatutaki kelele, Kaa chini" Tekso aliongea na kumfanya baba yake mdogo Sarah atii amri, ila alipotupa macho kwa mbele alimuona baba yake akiwa amelala sakafuni huku damu zikiwa zimetapakaa, Baba yake mdogo Sarah akanyanyuka na kukimbilia eneo alilokuwa amelala baba yake, alimpomfikia alimgeuza na kumuangalia kwa umakini huku akimuita baba yake,

"mmemfanyaje baba yangu" Baba yake mdogo Sarah aliuliza huku akinyanyuka kwa hasira, hakujali midomo ya bastola iliyokuwa inamuangalia,

"tulia hapo hapo, endapo utapiga hatua nyingine itakuwa umejitakia mwenyewe kifo" Trigger aliongea huku akiichomoa bastola yake iliyokuwa kiunoni, lakini baba yake mdogo Sarah hakuonekana kujali hilo onyo, alizidi kumsogelea Trigger, Tekso kuona hivyo, akapiga hatua moja ya haraka na kwa kutumia kitako cha bastola yake alimpiga kisogoni baba yake mdogo Sarah na kuanguka palepale, akapoteza fahamu.

Tekso alifanya hivyo kuhofia huenda Trigger anaweza kumnyooshea mdomo wa bastola baba yake mdogo Sarah na mwisho akamuua.

"mbebeni huyo mzee na mumpeleke nje kwenye gari" Tekso aliongea kwa ukali na kufanya vijana wamchukue babu yake Sarah na kumpeleka nje kwenye gari.

"na huyu tunamfanyaje" Strategic aliuliza huku akimuangalia baba yake mdogo Sarah aliyekuwa amelala chini,

"nae aingizwe ndani ya gari" Trigger alijibu huku akiipachika kiunoni bastola yake, vijana wakaubeba mwili wa baba yake mdogo Sarah na kuupeleka nje.

"tuikague nyumba kabla hatujaondoka" Strategic alitoa ushauri,

"hamna haja ya kukagua nyumba, wote tutoke nje" Trigger aliongea huku akielekea nje na kufanya wenzie wabaki wakitazamana na walionekana hawajamuelewa mkuu wao huyo,

"ebu tukague bwana, huenda huyo Sarah yupo humu" Tekso aliongea huku akianza kupiga hatua kuelekea vyumbani, ila ghafla alishuhudia moto mkubwa ukiwaka kupitia dirishani, akashtuka,

"tutokeni, kuna moto nje" Tekso aliongea huku akianza kupiga hatua kuelekea nje, wenzake wakamfuata na wote wakatoka nje na kumkuta Trigger akiwa ameshikilia kibiriti na pembeni yake kulikuwa na dumu la petrol,

"mnapoambiwa tokeni, muwe mnaelewa" Trigger aliongea kisha akawasha kibiriti na kukitupia mlangoni, moto ukashika zaidi na kuwaka kwa kasi na kufanya wenzake wazidi kushangaa,

"sasa mkuu ndani kama kuna watu wengine?" Strategic alimuuliza Trigger kinyonge,

"kawaokoe" Trigger alijibu huku akiingia ndani ya gari na kuliwasha,

"twendeni" Trigger aliongea huku akiwatizama wenzake hao, wakapanda kwenye gari na Trigger akaliondoa kwa kasi.

***************

Sarah wakati akiendelea kutazama runinga aliona kuna habari iliyokuwa ikirushwa muda huo, ni habari za papo kwa papo, ni habari iliyokuwa ikionesha nyumba ikiwaka moto na haikujulikana kama kuna watu ndani ya nyumba au lah, Sarah hakuitilia maanani sana ile habari, aliichukulia ni habari ya kawaida tu, akazima runinga na kuelekea chumbani kwake Kulala, ila alijihisi yupo tofauti sana usiku huo, alihisi kama ana hofu au wasiwasi fulani, akachukua simu yake na kuingia mtandaoni, akakuta habari inayozungumziwa ni ile ile ya nyumba kuungua, hakuona habari mpya, akaipuuza kisha akazima simu yake na Kulala.

*****************

Sarah aliamka asubuhi na kufanya mazoezi ya viungo, kisha akaelekea bafuni kujiswafi mwili, baada ya hapo akaenda jikoni na kutengeneza kifungua kinywa, alipomaliza alienda sebuleni na kuwasha runinga, akakuta habari ile ile ya nyumba kuungua, ikabidi ategee masikio ili kuisikiliza vyema ile habari, sasa hapo ndipo alichanganyikiwa, Sarah aligundua nyumba iliyoungua ni ya babu yake, ingawa habari ilieleza chanzo cha moto hakijajulikana, ila Sarah alihisi huenda ni kazi ya Taita, na alihisi Taita amefanya vile ili kumkomoa.

Sasa kwa mara ya Kwanza Sarah alihisi kuchanganyikiwa, aliona amefanya uzembe mkubwa sana kwa kujitambulisha kwa adui zake bila kuweka ulinzi kwa ndugu zake. Hata chai haikunyweka asubuhi hiyo, akataka aende eneo la tukio ila akaona itakuwa hatari zaidi, akahisi huenda vijana wa Taita watakuwa wapo maeneo hayo wanamwinda, akafikiri sana na mwisho akatabasamu, akaichukua chai yake na kuanza kuinywa, Sarah aliamua kupuuza hilo tukio, ndicho alichofundishwa jeshini, kuwa kama itatokea adui atataka kucheza na saikolojia yako, mpuuze, alafu athari kubwa itamrudia adui kama alitumia nguvu kubwa kukufanyia mchezo huo.

Sarah alipomaliza shughuli zake, alielekea mjini na gari lake, siku hiyo alipanga kuanza kufuatilia utaratibu wa kufungua kampuni yake ya kuingiza na kutoa mizigo nje ya nchi ili iwe kama kivuli cha kuficha matendo yake, hasionekana yupo mjini bure, siku hiyo alianzia TRA.

*******************

Ndani ya kituo cha polisi, mkuu wa polisi alikuwa juu ya kiti na mezani kulikuwa na makabrasha kadhaa ya kesi za zamani ambazo ziliachwa juu juu bila kufanyiwa kazi, kupitia hayo makabrasha sio aliamua tu, aliamua kutafuta kabrasha la nyumba iliyowahi kuchomwa moto huku ndani kukiwa na watu, alifanya hivyo baada ya tukio lililopita siku moja tu, la nyumba ya babu yake Sarah kuchomwa, akakuta hiyo nyumba iliyoungua siku iliyopita na ile nyumba iliyochomwa miaka 19 iliyopita, zote ni za mmiliki mmoja, ambaye ni Isack, Baba yake Sarah,

"inawezekana haya matukio yana uhusiano?" Mkuu wa polisi alijiuliza mwenyewe huku akijikuna kichwa, akaamua aangalie ni askari gani alipewa aifuatilie ile kesi ya nyumba iliyochomwa moto miaka 19 iliyopita, akakuta kuna jina Moses Mahenge, akaamua aendelee kusoma ni wapi askari huyo alipoishia katika upelelezi wake, akakuta upelelezi ulifungwa baada ya Moses Mahenge kupigwa risasi hospitali na watu wanaosemekana hawajulikani.

Akatabasamu baada ya kuona kesi iliamriwa kufungwa baada ya askari wa upelelezi kuogopa kuifuatilia ile kesi baada ya mwenzao kupigwa risasi,

"askari gani wa ajabu kiasi hiki?" Mkuu wa polisi alijiuliza mwenyewe kisha akachukua simu yake na kupiga namba anayoijua yeye, baada ya kuongea kwa sekunde tano, akakata simu.

Baada ya dakika moja aliingia kijana ndani ya ofisi ile ya mkuu wa polisi, alipoingia alionesha heshima kwa kupiga salute, kisha akaambiwa akae chini, akapatiwa makabrasha yote mawili yenye kesi za nyumba za mtu mmoja kuungua katika miaka tofauti, Yule kijana akapitia maelezo ya mule kwa muda wa dakika ishirini kisha akayarudisha mezani,

"umegundua nini hapo?" Mkuu wa polisi aliuliza,

"ni nyumba za mtu mmoja" Kijana alijibu,

"sasa nakupa hiyo kesi ya nyumba kuungua jana, uifuatilie kwa maana inasemekana kulikuwa na watu wanaishi mule ndani, ila hawajaonekana mpaka sasa hivi?" Mkuu wa polisi aliongea huku akimtazama yule kijana,

"sawa mkuu" kijana alijibu kikakamavu,

"unaanza kuifuatilia muda gani, leo au kesho?" Mkuu wa polisi alimuuliza,

"nitaenda kukagua usiku eneo la tukio labda naweza kupata chochote kitakachonipa mwanga" kijana alijibu kikakamavu,

"sawa, unaweza kuondoka" Mkuu wa polisi aliongea kisha kijana akapiga salute na kuchukua yale makabrasha mezani na kutoka nayo.

*****************

Usiku wa saa tano, Sarah alikuwa chumbani kwake akivaa, alivaa suruali nyeusi ya mpira iliyoushika mwili wake, na ilikuwa na mkanda mmoja kila paja, Sarah alipachika bastola mbili katika kila mkanda, juu alivaa blazia na koti kubwa jeusi, usoni alivaa half mask, yaani kinyago kilichoziba nusu ya uso wake, yaani kilianzia puani kushuka chini, macho yalikuwa wazi na nywele zake ndefu zilikuwa wazi, akaziachia zining'inie.

Sarah aliamua aende kwenye nyumba ya babu yake iliyochomwa moto, aliamua kufanya hivyo kama mtego huku akiamini anaweza kumkuta kijana yoyote wa Taita, na nia ya Sarah ilikuwa ni kumuua vibaya kijana yoyote wa Taita atakayemkuta eneo lile ili iwe fundisho na pia awatishe kambi ya Taita.

Mishale ya saa sita na nusu usiku, Sarah aliiegesha range Rover yake mtaa wa pili, kisha kwa umakini mkubwa akajongea mpaka kwenye nyumba ya babu yake, kwa jinsi alivyoiona alisikitika, aliikuta imeungua yote limebaki pagale, akaingia ndani ya lile pagale akaanza kuzunguka zunguka, kwa bahati nzuri akaona kuna kipande cha picha mbele yake chini, akainama na kukiokota, akakitia mfukoni, wakati anainuka alishangaa akishikwa mkono kwa nguvu,

"wewe ni nani" Sauti iliuliza kwa ukali huku akiwa bado ameushika mkono wa Sarah, alikuwa ni yule kijana polisi,

Sarah akutaka kujibu, aliamini huyo ni kijana wa Taita, Sarah aligeuka na kuuvuta mkono wake kwa nguvu kisha akaachia teke jepesi ila lina madhara makubwa, yule kijana akayumba lile teke likampiga shingoni, kijana akapepesuka kisha akakaa sawa. Yule kijana akaamini sasa huenda huyo binti anahusika na uchomaji wa hiyo nyumba, akaahidi moyoni mwake kuwa ni lazima amdhibiti.

Wakati kijana akiwaza hayo, huku Sarah alikuwa anatafakari namna pigo lake aliloliamini namna ambavyo halikumletea madhara yule kijana.

Sarah akakunja ngumi akairusha, kijana akainama kisha akamchota mtama mkali Sarah, wakati Sarah akiwa hewani, yule kijana alirusha buti kali lililomkuta Sarah mbavuni, Sarah akarushwa mbali na kujipigiza ukutani. Sarah akauma meno kwa maumivu, kisha taratibu akainuka huku akiwaza kuwa leo amekutana na fundi haswa, Sarah akakunja ngumi tena, akamuendea kwa mtindo ule ule alioutumia hawali, Sarah alimsogelea na kurusha ngumi, Kijana akainama tena, safari hii alivyoinama tu, alikutana na kifuti kizito kilichomkuta yule Kijana katika miwani yake, upande wa jicho la kushoto, kioo cha Miwani kikatia nyufa, kijana akahisi hilo pigo sio geni sana,

"Sarah?" kijana aliita huku akimtazama Sarah, Sarah kusikia huyo kijana anajua jina lake, akahisi kabisa ni Kijana wa Taita, Sarah hakuitika, akarudi nyuma na kuruka teke kali, kijana akamdaka mguu na kuachia ngumi kali iliyotua kwenye kifua cha Sarah, Sarah akadondoka chini na kukohoa, kijana kuona hivyo, akawa anamuendea kwa pupa Sarah, alipomfikia alimuinamia, kwa kasi ya ajabu sana, Sarah aliinua jiwe kubwa na kumtwanga nalo pale pale kwenye kioo cha miwani kilicho na nyufa upande wa kushoto wa miwani, kile kioo kikapasuka kabisa, yule Kijana akarudi nyuma na kuamua kuiondoa kabisa miwani machoni mwake, alipoitoa ile miwani ndipo alipoonekana vizuri, jicho lake la kushoto lilikuwa bovu, alikuwa na chongo..................

Naaam ndugu msomaji nadhani umeshamtambua huyo kijana askari.

************ITAENDELEA***************

the Legend☆
 
RIWAYA : SALA YA SARAH.

MTUNZI : ALEX KILEO.

SEHEMU YA ISHIRINI NA NNE.

ILIPOISHIA.............................

Wakati kijana akiwaza hayo, huku Sarah alikuwa anatafakari namna pigo lake aliloliamini namna ambavyo halikumletea madhara yule kijana.

Sarah akakunja ngumi akairusha, kijana akainama kisha akamchota mtama mkali Sarah, wakati Sarah akiwa hewani, yule kijana alirusha buti kali lililomkuta Sarah mbavuni, Sarah akarushwa mbali na kujipigiza ukutani. Sarah akauma meno kwa maumivu, kisha taratibu akainuka huku akiwaza kuwa leo amekutana na fundi haswa, Sarah akakunja ngumi tena, akamuendea kwa mtindo ule ule alioutumia hawali, Sarah alimsogelea na kurusha ngumi, Kijana akainama tena, safari hii alivyoinama tu, alikutana na kifuti kizito kilichomkuta yule Kijana katika miwani yake, upande wa jicho la kushoto, kioo cha Miwani kikatia nyufa, kijana akahisi hilo pigo sio geni sana,

"Sarah?" kijana aliita huku akimtazama Sarah, Sarah kusikia huyo kijana anajua jina lake, akahisi kabisa ni Kijana wa Taita, Sarah hakuitika, akarudi nyuma na kuruka teke kali, kijana akamdaka mguu na kuachia ngumi kali iliyotua kwenye kifua cha Sarah, Sarah akadondoka chini na kukohoa, kijana kuona hivyo, akawa anamuendea kwa pupa Sarah, alipomfikia alimuinamia, kwa kasi ya ajabu sana, Sarah aliinua jiwe kubwa na kumtwanga nalo pale pale kwenye kioo cha miwani kilicho na nyufa upande wa kushoto wa miwani, kile kioo kikapasuka kabisa, yule Kijana akarudi nyuma na kuamua kuiondoa kabisa miwani machoni mwake, alipoitoa ile miwani ndipo alipoonekana vizuri, jicho lake la kushoto lilikuwa bovu, alikuwa na chongo..................

Naaam ndugu msomaji nadhani umeshamtambua huyo kijana askari.

*********ENDELEA*********

Naam, huyu kijana askari alikuwa ni Sajenti Minja, yeye ndio alipewa hii kesi aifuatilie.

Sarah akabaki na kiulizo kuhusu huyu mtu, alishangaa uwezo wake wa kupambana ingali ana jicho moja. Sarah sasa kwa spidi ya mwanga, akachomoa bastola yake, Sajenti Minja kuona hivyo, akaruka hewani na kujipindua, kisha akaachia teke kali lililotua kwenye mkono wa Sarah, Sarah akaangusha bastola huku akirudishwa nyuma na lile teke na kumfanya apepesuke, Sajenti Minja akamuwahi na kumkamata shingo yake kwa kutumia mkono wa kushoto kisha akamnyang'anya na ile bastola aliyobaki nayo, Sarah ikambidi apoe, leo alikuwa amepatikana haswa.

Sajenti Minja akamuachia Sarah shingo, ila alimuelekezea bastola,

"wewe ni nani? Vua hicho kinyago" Sajenti Minja alimuuliza Sarah, sasa Sarah akapata mshangao, anajiuliza kwanini huyu mtu amuulize yeye ni nani wakati alimuita jina lake muda mchache uliopita,

"toa kinyago kwa hiyari yako au nikutoe mimi kwa maumivu?" Sajenti Minja alimuuliza tena baada ya kumuona yupo kimya, ila hata kipindi hiki Sarah hakujibu kitu,

"wewe si ni kiburi?" Sajenti Minja aliongea huku alimsogelea Sarah, Sarah akaona hiyo ni nafasi kwake ya kujitetea, Sarah akapiga hatua mbili za haraka kumsogelea Sajenti Minja, huku akijua kabisa ni lazima Sajenti Minja achanganyikiwe kwa ile kasi aliyomfuata nayo, na kweli, hicho ndicho kilichotokea, Sajenti Minja alishangazwa na wepesi wa yule binti, Sajenti Minja akakimbilia kubonyeza kifyatua risasi, alikuwa ameshachelewa muda tu, Sarah alishakishika kitako cha bastola na kukifungua, risasi zote zikamwagika chini, Sajenti Minja akiwa bado anashangaa, alipigwa ngumi ya mdomo, akarudi nyuma akatema mate, yalikuwa na damu, Sajenti Minja akatoa bastola nyingine aliyomnyang'anya Sarah,

"nakufumua ubongo, toa kinyago iko" Sajenti Minja aliongea kwa hasira,

"piga tu" Sarah aliongea kwa nyodo huku akiwa hajali, kuona hivyo Sajenti Minja akashusha bastola usawa wa miguu ya Sarah, akafyatua risasi, lakini haikutoka,

"unajua sana kufyatua risasi eeeh?" Sarah aliuliza kwa kejeli, Sajenti Minja akataka kuinama kuokota risasi zile zilizoanguka kwenye bastola ya hawali, Sarah hiyo ndio nafasi aliyokuwa anaitaka, aliupiga mkono wa Sajenti Minja, ile bastola ikaruka juu, Sarah akaidaka kisha akaachia teke kali lililomkuta, Sajenti Minja ubavuni, Sajenti Minja akarushwa kidogo, Sarah akainama na kuiokota ile bastola nyingine, kisha Akainama, akaruka dirishani na kuanza kukimbia, aliona mtu anayepambana nae hakuwa wa kawaida, aliona akiendelea kupambana nae anaweza kuotewa na akadhibitiwa,

Sajenti Minja kuona anakimbiwa, nae akanyanyuka na kuanza kumkimbiza, lakini Sarah alikuwa mwepesi zaidi, kila anapopiga hatua mbili, huku Sajenti Minja alipiga hatua moja, mwisho wa siku Sarah akalifikia gari lake na kupanda kisha akaliondoa kwa kasi, Sajenti Minja akakuta vumbi tu, ila aliambulia namba za gari, hiyo ilikuwa nzuri sana kwa upande wake.

Akatoa simu yake mfukoni na kuandika hizo namba, kisha akageuka nyuma na kurudi ndani ya lile pagale, alirudi na kuokota zile risasi zile zilizotoka kwenye bastola ya Sarah,

"huu nao ni ushahidi mzuri" Sajenti Minja aliongea huku akitoa mfukoni kimfuko kidogo cha nylon, kisha akaziweka zile risasi, akaiokota miwani yake na kuitia kwenye mfuko wake wa shati na kuondoka zake.

*************************

Sarah alipoingia ndani kwake, alijitupa juu ya kochi na kuingiza mkono katika koti lake na kuitoa ile pcha aliyoikota kule kwenye pagale, akaiangalia, ilikuwa ni picha ya familia yao, katika picha alikuwepo Sarah, sebastian na wazazi wao, Sarah akaitupa ile picha juu ya meza, akavua viatu vyake, kisha akashusha pumzi ndefu.

"yule bwege ni nani? naona Taita atakuwa amedhamilia kupambana na mimi. Pale kwa Taita hakuna kijana anaweza kupambana namna ile, itakuwa amemtoa nje ya nchi, ila mbona anaongea kiswahili kizuri? Nitamfuatilia vizuri" Sarah aliongea peke yake,

"na babu itabidi kesho nijue kama yupo salama au la" Sarah aliongea mwenyewe kisha akanyanyuka na kwenda kwenye droo ya kabati na kutoa dawa za kuchua, alifanya hivyo ili kujichua sehemu zenye maumivu aliyoyapata kutokana na mapigo ya Sajenti Minja.

"kesho nitaanzia polisi kwa ajili ya kufuatilia mambo yangu ya kampuni" Sarah aliongea huku akijipaka dawa.

******************

Hakuna kipindi Taita alichanganyikiwa kama hiki, maana alitegemea kupokea simu ya Sarah na Sarah hakupiga, sasa Taita usiku huu alikuwa amekaa amepoa, mawazo yalimtawala, aliwaza ni kipi Sarah awazacho, alihisi Sarah atakuwa anaandaa shambulizi baya sana.

"Trigger na wewe umekosea, kwanini uliichoma ile nyumba ya yule mzee?" Taita alimuuliza Trigger ambaye alikuwa amekaa mbele yake,

"hakukuwa na njia nyingine ya kufanya" Trigger alijibu kwa upole,

"kumbuka huyu tulimuhitaji kama chambo tu, lakini wewe hukuliona hilo, ukampiga risasi, ukachoma nyumba yake, wewe unadhani Sarah anaandaa kitu gani kwa ajili yetu" Taita alihoji huku akimuangalia Trigger, lakini Trigger hakuwa na jibu, akakaa kimya,

"mzee mmemuhoji nini?" Taita alimuuliza Trigger,

"tumemuuliza tu ni wapi Sarah alipo" Trigger alijibu,

"amejibu nini", Taita akauliza tena,

"amesema yupo uingereza" Trigger alijibu,


"hujamuuliza kama wameonana siku za karibuni?" Taita aliuliza,

"anadai mara ya mwisho kuonana na Sarah ni miaka kumi na tisa iliyopita, zaidi ya hapo uwa wanawasiliana kwa simu tu" Trigger alijibu,

"kazi ipo, basi huenda Sarah hajamwambia babu yake kama amerudi nchini" Taita aliongea na kumimina maji kwenye glass na kuyanywa,

"nadhani hatupaswi kufikiria sana, nadhani atatutafuta tu" Trigger Aliongea kwa kujiamini,

"mzee amejua ni mimi nimemteka?" Taita alimuuliza,

"si ulisema hatakiwi kujua, basi hatujamwambia" Trigger alijibu,

"na yule mtoto wake mmemuhoji?" Taita aliuliza,

"ndio, ila Majibu yake ni kama ya baba yake, labda inawezekana wanachoongea ni kweli" Trigger alijibu huku akijikuna kichwa,

"nasikia ulitafuta daktari na kumpeleka kule ndani kumtibu yule mzee?" Taita alimuuliza Trigger,

"ni kweli, maana hali ya mzee niliona ikibadilika ndio maana nikaamua kufanya hivyo" Trigger alielezea hali halisi,

"huoni hiyo ni hatari sana, au unafahamiana na huyo daktari?" Taita alimuuliza,

"hapana, nimemdanganya na pesa, na pia nimemtisha kuwa endapo atasema chochote, nitammaliza, ameogopa nadhani" Trigger alijibu,

"haya sawa, ngoja tusubiri mpaka kesho, kama Sarah asipotutafuta, nahisi tutakuwa na hali mbaya, itabidi niongezewe ulinzi" Taita aliongea huku akimaanisha anachosema,

"usiogope mkuu, akija atakuja kwa adabu tu" Trigger aliongea kwa kujiamini,

"we Kaa kimya, maana hujawahi kukutana nae, muulize Harry, maana anajua balaa la huyo mtoto" Taita aliongea huku akinyanyuka,

"siku nitakayokutana nae, ndio siku atakayokutana na Israeli mtoa roho" Trigger aliongea kwa kujiamini,

"ulishindwa kumuua akiwa mtoto, utamuweza muda huu akiwa tayari ni mkubwa, tena sio mkubwa tu, ni mkubwa anaewaka kama moto " Taita aliongea huku akiingia ndani kwake na kumuacha Trigger akitafakari maneno ya bosi wake,

"nitamuweza tu, nitamfanya kitu kibaya ili bosi arudishe imani kwangu" Trigger aliongea kisha akanyanyuka kutoka kwenye kochi na kuelekea nje.

***********************

Sajenti Minja asubuhi ya leo ilimkuta yupo ofisini kwake, alikuwa yupo makini na computer yake, alikuwa akizifuatilia zile risasi alizoziokota kule pagaleni, aliamua kuzifuatilia baada ya kukuta zimeandikwa kwa nyuma sehemu zilipotengenezewa.

Baada ya kuzifuatilia kwa muda, aligundua zile risasi zimetengenezwa na kampuni ya jeshi la kiingereza, na kwa maelezo aliyoyasoma pale, yalionesha kuwa risasi zile uwa zinatumika katika bastola zake ambazo ni maalum na zinatengenezwa na kampuni hiyo hiyo, na zaidi ni Kwamba hizo bastola hazitumiwi na watu tofauti zaidi ya wanajeshi wa uingereza. Kwa maelezo hayo tu, ilibidi Sajenti Minja agune,

"kwa hiyo yule mwanadada ni mwanajeshi wa uingereza, au ni Sarah amekuja kwa mission nyingine?" Sajenti Minja alijiuliza, ila Sarah aliyemdhania yeye sio huyu Sarah Isack, Sarah aliyemdhania yeye ni yule mwanadada komando aliyesumbuana nae kwenye riwaya ya MEMORY CARD.

"sasa yule ni mwanajeshi wa marekani, na huyu wa jana anaonekana ni muingereza, au ndio yeye ila ameamua kutumia vitu vya kiingereza?" Sajenti Minja aliendelea kujiuliza,

Wakati Sajenti Minja akiendelea kujipiga maswali, alishtuka baada ya kuiona Ranger Rover nyeusi ikipaki mbele ya kituo cha polisi, aliiona kupitia dirisha la kioo, akaikumbuka hiyo gari kuwa ndiye ile iliyomkimbia usiku uliopita.

Wakati akishangaa hiyo hali, alishuhudia mwanadada mrembo akishuka katika ile gari, alikuwa ni Sarah, alienda hapo kukamilisha mpango wake wa kufungua kampuni, alifika hapo kwa ajili ya kuongea na mkuu wa polisi ili apatiwe askari ambao watakuwa wakiboresha ulinzi nje ya geti la kampuni yake.

Sarah aliposhuka alienda moja kwa moja mpaka kaunta na kuomba kuonana na mkuu wa kituo, akaelekezwa ofisi ilipo na akaenda huko kuongea nae.

Baada ya nusu saa, Sarah alikuwa amemaliza kuongea na mkuu wa polisi, Sarah akaelekea nje huku akiwa ametinga baibui pana nyeusi.

Alipolifikia gari lake akafungua mlango, wakati anataka kuingia ndani ya gari, alishtuka akishikwa mkono kwa nyuma, Sarah akageuka na huku akijiuliza ni nani huyo aliyemshika,

"samahani" Sajenti Minja aliongea huku akiwa bado ameushika mkono wa Sarah kwa mkono wa kushoto na wakati huo mkono wake wa kulia aliutumia kuivua miwani yake, macho yakabaki wazi na kufanya jicho lake moja la kushoto lenye chongo lionekane vyema, hapo ndipo Sarah akachanganyikiwa kabisa, akaikumbuka ile methali isemayo "ndege mjanja hunasa kwenye tundu bovu"

***********ITAENDELEA*************

the Legend☆
 
RIWAYA : SALA YA SARAH.

MTUNZI : ALEX KILEO.

SEHEMU YA ISHIRINI NA TANO.

ILIPOISHIA......................

Baada ya nusu saa, Sarah alikuwa amemaliza kuongea na mkuu wa polisi, Sarah akaelekea nje huku akiwa ametinga baibui pana nyeusi.

Alipolifikia gari lake akafungua mlango, wakati anataka kuingia ndani ya gari, alishtuka akishikwa mkono kwa nyuma, Sarah akageuka na huku akijiuliza ni nani huyo aliyemshika,

"samahani" Sajenti Minja aliongea huku akiwa bado ameushika mkono wa Sarah kwa mkono wa kushoto na wakati huo mkono wake wa kulia aliutumia kuivua miwani yake, macho yakabaki wazi na kufanya jicho lake moja la kushoto lenye chongo lionekane vyema, hapo ndipo Sarah akachanganyikiwa kabisa, akaikumbuka ile methali isemayo "ndege mjanja hunasa kwenye tundu bovu"

**********ENDELEA***********

"bila samahani" Sarah aliongea huku akijitahidi kuficha mshtuko wake,

"habari yako" Sajenti Minja alitoa salamu kwanza,

"nzuri" Sarah alijibu huku akili yake ikimwambia asifanye kitu chochote cha ajabu,

"hii gari ni yako?" Sajenti Minja alimuuliza Sarah,

"ndio ni yangu, vipi kwani?" Sarah alijibu huku akimuangalia Sajenti Minja,

"naweza kuikagua?" Sajenti Minja aliuliza na kumfanya Sarah azidi kuhisi hatari,

"ruksa, ikague" Sarah aliongea na kufanya Sajenti Minja azunguke nyuma ya ile gari ili asome namba, ila alikuta namba ni tofauti na zile alizozinakiri usiku uliopita.

Sajenti Minja alirudi upande aliposimama Sarah,

"nashukuru kwa ushirikiano wako, nadhani nimefananisha gari" Sajenti Minja aliongea huku akitaka kuondoka,

"samahani, mbona unakagua tu gari yangu alafu unaondoka, hunipi hata sababu ya kuikagua?" Sarah alimuuliza Sajenti Minja huku akionesha hajakifurahia kitendo kile,

"nimeshakuambia kuwa nimefananisha gari" Sajenti Minja aliongea,

"sawa, hilo gari lilifanya kosa gani? " Sarah aliuliza,

"mwanamke acha maswali, Wewe elewa hivyo" Sajenti Minja aliongea huku akiondoka na kumfanya Sarah abaki anamuangalia tu.

Sarah akarudi ndani ya gari na kuiwasha kisha akaondoka zake,

"kumbe huyu jamaa ni askari, anajiamini sana alafu ana dharau" Sarah aliwaza peke yake wakati akiendesha gari yake, baada ya mwendo wa dakika tano, aliegesha gari yake kwenye duka kubwa, akashuka na kuchukua mahitaji yake ya nyumbani, baada ya hapo akaenda kulipia bidhaa alizonunua, kisha akatoka nje huku akiwa ameongozana na muhudumu wa pale ambaye alikuwa akimsaidia kusukuma kikapu cha matairi ambacho Sarah aliweka vitu vyake.

Baada ya Sarah kumaliza kuingiza vitu vyake ndani ya gari, na yeye aliingia ndani ya gari na kuiwasha kisha akaondoka zake, wakati akitoka eneo la dukani na kuingia barabara kubwa, aliweza kushuhudia gari aina ya harrier ikikatiza mbele yake, na ndani alimuona Trigger ambaye ndiye alikuwa dereva na pembeni ya Trigger alikaa binti mmoja mwembamba mwenye mwili kama Sarah.

Sarah akaona kuliko kwenda nyumbani, ni bora awafuate tu ili aone wanapoelekea.

Trigger aliendelea kuendesha gari huku hajui kama anafuatwa na adui yake, ile safari ya Trigger iliishia ndani ya majengo makubwa ya ghorofa ambayo Sarah hakusumbuka kujua pale ni hospitali.

Baada ya Trigger kusimamisha gari, alitelemka yule mwanamke ambaye alikaa pembeni ya Trigger, kisha akaingia ndani ya lile jengo, baada ya kupotelea ndani ya jengo, Trigger akageuza gari na kuanza kutoka kwenye eneo lile la hospitali, getini alipishana na gari la Sarah ambaye yeye alikuwa akiingia ndani ya eneo lile la hospitali.

Sarah aliingiza gari eneo la hospital na Kuliegesha, Sarah aliamua kudili na huyo dada tu, aliamini huyo dada huenda ana uhusiano na Trigger, iwe wa kimapenzi au ni ndugu, pia akahisi kama sio vyote hivyo, huenda huyo dada ni mmoja kati ya vijana wa Taita.

Sarah alitelemka na kuingia haraka haraka ndani ya jengo lile lile alipoingia yule dada, kwa bahati nzuri alimkuta yule dada akiwa bado eneo la mapokezi na alionekana akiongea kwa uchangamfu na yule dada wa mapokezi. Sarah akakaa katika kochi hapo na kujifanya anabonyeza simu yake.

"dokta pendo wahi bwana kuna wagonjwa wanakusubiri, ukiwa unatoka utanisimulia vizuri" Dada wa mapokezi alimwambia yule mwanadada aliyeletwa na Trigger,

a

"unajua leo natoka saa ngapi?" Mwanadada aliyeletwa na Trigger alimuuliza yule dada wa mapokezi,

"saa kumi na mbili kama kawaida, au?" Dada wa mapokezi alijibu,

"leo natoka saa mbili, maana nitamsaidia na dokta swai, kaniomba nimshikie mpaka muda huo ambao ndio ataingia hospitali" Mwanadada aliyeletwa na Trigger aliongea,

"mi natoka saa kumi na mbili, tutaongea kesho basi" Dada wa mapokezi aliongea,

"usijali shoga yangu" Dada aliyeletwa na Trigger aliongea huku akiondoka eneo hilo, na muda huo sasa Sarah ndio akaelewa kuwa yule dada ni daktari wa ile hospitali, akajua na jina lake anaitwa pendo, ila hivyo havikuwa vitu muhimu sana kwake, kwake kitu muhimu ambacho aliona amekiona, ni kujua muda wa kutoka wa yule daktari, hilo ndilo lilikuwa jambo muhimu kwake, sasa swali alilojiuliza ni kuwa huo muda wa huyo binti kuondoka, atafuatwa na Trigger au lah?

Sarah aliamua kuondoka muda huo, ila muda wote alikuwa akichekecha ubongo wake namna atakavyofanikisha mpango wako dhidi ya daktari yule wa kike, ajulikanaye kama Pendo.

Sarah alirudi nyumbani kwake, na kufanya shughuli zake ndogo ndogo za nyumbani huku akiwa makini na muda wake.

Baada ya shughuli zake kukamilika, hakutaka kuingia kusafisha mwili, alichofanya alibadili nguo na kuondoka, hakutoka na gari yake, aliamua kukodi boda boda iliyomfikisha mpaka mjini, kisha akamlipa dereva wa boda, alafu akakodi taxi ambayo ndio alipanga imfikishe hospitali anayofanyia kazi yule daktari wa kike.

Sarah alifanikiwa kupata taxi,

"nipeleke amani hospital" Sarah alimwambia dereva taxi huku akiingia siti za nyuma za taxi ile.

Dereva taxi akawasha gari na kuiondoa, njia nzima hakuna aliyemuongelesha mwenzake, Sarah alikuwa kimya na dereva taxi pia alikuwa kimya.

Dereva taxi akiwa yupo makini na barabara, alihisi kitu cha baridi kikigusa kisogo chake, dereva taxi akapata hofu kuu, kidogo agonge Kingo za barabara,

"simamisha gari, iweke pembeni" Sarah aliongea katika sauti laini na dereva taxi akatii ile amri,

"shuka na usizime gari" Sarah aliongea huku bastola yake ikiwa mkononi, ila dereva taxi akataka kuleta shida, alitaka kuchomoa funguo na kukimbia, Sarah akamuwahi kwa kumpiga na kitako cha bastola yake, dereva taxi akapoteza fahamu, Sarah akataka siti za nyuma na kuelekea mbele, akamsukuma dereva na kuanguka pembezoni mwa barabara, Sarah akawasha gari na kuiondoa mpaka nje ya hospitali ile.

Sarah alipofika alitelemka na kuanza kuchungulia kupitia katika uzio wa hospitali, alifika pale saa moja na nusu usiku, ila mpaka saa mbili na dakika tano hakumuona dokta Pendo akitoka, akasubiri nusu nyingine ila pia hakumuona dokta Pendo akitoka, akataka aingie ndani ndipo kwa mbali aliweza kumuona dokta Pendo akitoka. Dokta Pendo alipotoka, alienda kupanda coaster ambayo ilikuwa ndani ya uzio wa hospitali, hakuwa peke yake, aliongozana na kundi lingine la wafanyakazi wenzake ambao ilionekana muda wao wa kutoka ulikuwa umehitimu.

Sarah aliendelea kusimama pale pale mpaka alishuhudia ile coaster ikianza kusogea getini, na yeye akaenda kuingia kwenye ile taxi aliyokuja nayo.

Coaster ilipotoka nje ya geti, ilikamata barabara na kuondoka kwa mwendo wa wastani, Sarah akawasha gari na kuanza kuifuatilia kwa mbali, ile basi ambayo ilikuwa inawarudisha nyumbani wafanyakazi wa hospitali, iliendelea kuzunguka kupita kila mtaa na kumshusha kila mfanyakazi, mpaka ilipomshusha Dokta Pendo.

Dokta Pendo alipotelemka aliagana na wenzake, kisha akapiga hatua kuelekea kwenye nyumba iliyokuwa ikimtazama, zilikuwa ni nyumba za kota, Dokta Pendo alipoufikia mlango, alitoa funguo na kufungua mlango, alipoingia ndani, aliwasha taa na kujitupa katika kochi na kuanza kuvua viatu, wakati akiendelea kuvua viatu alisikia mtu akigonga hodi mlangoni kwake,

"watu wengine bwana, hata mtu hajatulia kwake wanakuja kumsumbua" Dokta Pendo alinung'unika huku akielekea mlangoni, alipofika alifungua mlango na kukutana na ngumi kali ya pua iliyomfanya apepesuke na kurudi nyuma,

"pole mrembo, naimani wewe ni dokta mzuri, utajitibu nikiondoka" Sarah aliongea huku akiingia ndani na kuufunga mlango, wakati huo Dokta Pendo alikuwa yupo chini huku damu ikimvuja puani.

"sijaja kwa ubaya, wala sina ubaya na wewe, nimekuja nina shida ndogo na wewe" Sarah aliongea huku macho yake yakitalii ndani ya sebule ya Dokta Pendo.

Dokta Pendo akajaribu kupiga kelele, Sarah akaruka na kutua mbele yake, kisha akampiga kofi kali sana, Dokta Pendo akajikuta analia badala ya kupiga kelele,

"Niue Niue" Dokta Pendo aliongea huku akilia,

"kwanini nikuue, mimi sijaja kukuua hapa, we ni mwanamke mwenzangu, na mimi ni mwiko kumdhuru mwanamke mwenzangu" Sarah aliongea kwa sauti tulivu,

"sema unataka nini?" Dokta Pendo aliongea kwa hasira,

"nilikuona mchana ukiwa kwenye gari aina ya harrier, ulikuwa na mwanaume, ni nani yako?" Sarah aliuliza huku akitabasamu,

"we mpuuzi nini, kumbe unanipiga kwa ajili ya mwanaume?" Dokta Pendo aliuliza kwa jeuri,

"naona hutaki kujibu, ila unataka tuulizane tu, itabidi nitumie hasira" Sarah aliongea huku akiitoa bastola na kuiweka mezani, hapo Dokta Pendo akapata uoga,

"yule ni mume wangu, je mna uhusiano nae?" Sarah aliuliza tena huku akimtazama,

"hapana, sina uhusiano nae", Dokta Pendo alijibu,

"mbona alikubeba kwenye gari na akakupeleka kazini? Kuwa mkweli, vinginevyo nitakuumiza vibaya mno" Sarah aliongea,

"nimeshakuambia Sina uhusiano nae" Dokta Pendo aliongea, na kufanya Sarah aikoki bastola yake na kumuelekezea,

"ni nini kinaendela kati yenu? Sitoona tabu kukuua endapo utakuwa hujibu ninavyotaka" Sarah aliongea na kumsogelea jirani kabisa,

"sawa, nitakujibu. Yule uliyeniona nae ni mtu ambaye aliniteka na kunilazimisha nimtibu mzee mmoja ambaye pia wamemteka" Dokta Pendo alitoa jibu lililomsisimua Sarah na kuhisi huyo mzee huenda ni babu yake,

"huyo mzee anaumwa nini?" Sarah aliuliza,

"ana jeraha juu ya bega, alipigwa risasi" Dokta Pendo alijibu,

"uwa anakufuata au unaenda mwenyewe?" Sarah alimuuliza,

"uwa ananifuata kila siku saa mbili asubuhi" Dokta Pendo alijibu,

"sawa" aliongea kisha akampiga kichwani na kitako cha bastola, Dokta Pendo akazimia, akambeba na kutoka nae nje, akamuingiza katika gari na kuondoka nae.

Sarah alipofika kwake, alimuingiza ndani Dokta Pendo, kisha akamuingiza katika chumba chake cha siri, akamlaza kitandani na kumpaka dawa anayojua yeye, alimpaka usoni, baada ya dakika moja ile dawa iliganda usoni kwa Dokta Pendo, Sarah akaibandua kama mask, kisha akaimwagia kemikali anayoijua yeye, alafu akaiingiza kwenye jiko la kukaushia, baada ya dakika tano akaitoa, ilikuwa ni mask ya sura ya Dokta Pendo, Sarah akaivaa usoni mwake, naam hicho ndicho alichokuwa anakitaka, alifanana kabisa na Dokta Pendo, Sarah akatabasamu.

********************

Mishale ya saa mbili asubuhi, Trigger aliegesha gari yake nje ya nyumba ya Dokta Pendo, kisha akapiga honi, baada ya dakika chache akatoka Sarah, ila ilikuwa ngumu kumtambua kutokana na ile mask aliyoivaa yenye sura ya Dokta Pendo.

Sarah akaingia ndani ya gari, akakaa pembeni ya Trigger,

"leo naona kama hips zako zimeongezeka" Trigger alimtania huku akitabasamu,

"macho yako tu" Sarah alijibu huku nae akitabasamu, kisha ukimya ukatawala mpaka gari ilipoegeshwa nje ya nyumba moja nzuri nzuri, Trigger akashuka,

"telemka tumefika, au leo hutaki kushuka" Trigger aliuliza huku akitabasamu na kufanya Sarah akurupuke na kushuka,

"nilikuwa mbali kimawazo" Sarah aliongea huku wakielekea ndani.

Safari yao iliishia ndani ya chumba kimoja ambacho ndani yake alikuwepo babu yake Sarah, Sarah alishtuka ila alijikaza,

"kaendelee na kazi" Trigger alimwambia Sarah kisha Trigger akasimama pale mlangoni, Sarah akamsogelea babu yake,

"babu mimi ni Sarah" Sarah aliongea kwa sauti ndogo ila iliyosikika vyema kwa babu yake,

"Sarah??? Kumbe wewe ni Sarah mjukuu wangu?" Babu yake Sarah aliongea kwa sauti kubwa iliyosikiwa vyema na Trigger, Trigger akachomoa bastola na kumuelekezea Sarah......

"umeharibu babu" Sarah aliongea katika sauti iliyokata tamaa............

*******ITAENDELEA*********

the Legend☆
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom