RIWAYA : SALA YA SARAH.
MTUNZI : ALEX KILEO
SEHEMU YA ISHIRINI.
ILIPOISHIA.
Harry alikuwa na haraka na mchecheto wa kutaka kumuona mtoto wake, na muda huo alikuwa anahesabu kiasi cha pesa ili amkabidhi huyo msamalia mwema atakayekuja, kwake Harry pesa hakuona tamu muda huo, alimuhitaji binti yake tu.
Vijana wa Taita wakiwa getini pamoja na wakuu zao, ndipo walipoiona gari ndogo ikisimama mbele yako na dereva wa gari ile akashusha kioo, ila cha ajabu watu wote pale walikuwa wamepigwa na butwaa na kumfanya Dalali ashindwe kuelewa sababu ya watu wale kumtolea macho,
"Mkamateni mpumbavu huyu" Harry aliwaamrisha vijana wa Taita kwa hasira na kufanya Dalali achoke kabisa, akahisi amegeukwa...........
***********ENDELEA***********
Bumbuwazi likaamia kwa dalali sasa, akawa anajiuliza kule ni kugeukwa ama ni kitu gani? Dalali akiwa bado katikati ya maswali, tayari vijana wa Taita walikuwa wameshamkamata na kumshusha kwenye gari kwa amri ya Harry.
Kipindi chote hicho Taita mwenyewe alikuwa akishangaa huku akiwa hajui ni kwanini msamalia mwema huyo anafanywa hivyo,
"Mpelekeni chumba cha mateso" Harry aliamrisha vijana,
"Mateso tena?" Dalali aliuliza huku akiwa ahamini kinachomtokea,
"Kaa kimya, hutakiwi kuongea" Harry alifoka kwa hasira,
"Lazima niongee kama naona jambo haliendi sawa" Dalali aliongea ila safari hii hakujibiwa kwa mdomo, alijibiwa na makofi kutoka kwa vijana wa Taita waliokuwa wamemshika na kumpeleka ndani, katika chumba cha mateso.
Huku nje alibaki Harry, Trigger, Taita na Tekso ambao walikuwa makini kufuatilia kile kinachofanywa na vijana wao,
"Harry sielewi ni kwanini unamfanya hivi huyu mtu ambaye ni msamalia mwema" Taita aliongea huku mshangao ukijionesha dhahiri machoni pake,
"Hii gari aliyokuja nayo ndio gari ambayo ilikuwa ikinifuatilia siku ile nilipovamiwa nyumbani kwangu" Harry aliongea na kumfanya Taita ashtuke sasa,
"Yeah, gari ndio hili hili tulilokuwa tunalifuatilia kutokana na maelekezo ya yule Dada wa guest kule" Tekso aliongea huku akitingisha kichwa chake,
"Sasa mtekaji si ni mwanamke? kwanini mnataka kumuadhibu huyo mwanaume?" Taita aliuliza swali la kipumbavu,
"Kama gari iliyotumika ni moja, basi inawezekana kabisa wanafahamiana" Tekso alitoa jibu,
"Twendeni ndani tukamuhoji" Harry aliongea huku akielekea ndani na wenzake wakamfuata, walielekea moja kwa moja mpaka ndani ya chumba cha mateso na kumkuta bwana dalali akiwa amewekwa juu ya kiti huku mikono yake ikifungwa kwa nyuma kwa kutumia kamba ngumu.
"Ndugu yangu, hatutaki kukutesa wala kukuumiza, tunachotaka ni ukweli wako tu" Harry aliongea huku akiwa amesimama mbele ya Harry,
"Ukweli upi? Kama ukweli niliouongea umenifikisha hapa na kufanywa mateka" Dalali aliongea huku akitabasamu, halikuwa tabasamu la furaha,
"Hiyo gari uliyokuja nayo ni ya nani?" Harry aliuliza,
"Ni gari yangu" Dalali alijibu,
"Unafanya kazi gani?" Tekso aliingilia kati na kuuliza,
"Mimi ni dalali, tena maarufu sana" Dalali alijibu,
"Ndiyo huyu huyu" Tekso aliongea huku akimgeukia Taita na kufanya Dalali ajiulize maswali kibao,
"Tofauti na wewe, ni nani anayeendeshaga gari yako?" Harry alimtupia swali Dalali,
"Ndio huyo Dada sasa ambaye ndio yupo na huyo mtoto wa kike mnayemtafuta" Dalali alijibu,
"Huyo Dada mna uhusihano naye gani?" Taita aliuliza,
"Mimi ndiye nilimsaidia kupata nyumba ambayo anaishi mpaka sasa, ndipo tukafahamiana mpaka leo" Dalali alitoa jibu na kufanya Harry na Trigger watazamane,
"Unaweza kutupeleka anapoishi?" Trigger aliuliza,
"Ndicho kilichonileta hapa, ila sio bure, maana tangazo lenu linasema msamalia mwema atalipwa" Dalali alijibu,
"Utalipwa" Harry alijibu,
"Sasa kulikuwa na sababu gani ya kunikamata na kunifunga?" Dalali aliuliza,
"Sababu umeshaijua, mfungueni" Trigger alijibu kisha akatoa amri iliyotekelezwa na vijana, Sasa Dalali alikuwa hana kamba tena mwilini, alikuwa huru,
"Tupeleke sasa" Harry aliongea,
"Ngojeni kwanza, ni nani nilikuwa naongea nae kwenye simu?" Dalali aliuliza huku akimtupia macho kila mmoja,
" ni mimi hapa" Harry alijibu,
"Nipe advansi kwanza kabla sijawapeleka uko, alafu mkishampata mtoto wenu mtanimalizia pesa iliyobaki" Dalali aliongea huku akimtazama Harry,
"Twende wewe, ujue tumekuheshimu sana ndio maana hatujakudhuru?" Tekso aliongea huku akimvuta Dalali kwa lengo la kumuinua kwenye kiti,
"Muache kwanza" Harry aliongea kisha akatoa pesa kwenye mifuko yake ya suruali na kumkabidhi Dalali, Dalali akaanza kuzihesabu,
"Hapo sawa, maana hii ni biashara" Dalali aliongea huku akitabasamu,
"Haya tupeleke sasa" Taita aliongea na kisha Dalali akasimama na kutangulia mbele huku wakina Taita wakimfuata kwa nyuma mpaka nje ambapo ndipo kulikuwepo na magari,
"Lete funguo ya gari lako, nitaendesha mimi na wewe utakaa pembeni utakuwa ukinielekeza" Harry aliongea huku akiwa amesimama kwenye mlango wa dereva wa gari la Dalali,
"Sawa, ni wewe tu bosi" Dalali aliongea huku akitabasamu na kumpa funguo Harry. Harry akaingia ndani ya gari na kuiwasha, ila kabla hajaondoka simu yake ilianza kuita, akaitoa mfukoni na kuangalia namba ya mpigaji, haikuwa ngeni, aliikumbuka kuwa ni ile aliyowahi kutumia mtekaji baada ya kumteka mwanae, Harry akapokea na kuweka simu sikioni huku akiwa na wasiwasi,
"Nakupa siri Harry, toka mwenyewe na uangalia kwenye injini,ya hilo gari ulilokuwepo alafu ukimaliza nitakupigia" Sauti ya kike iliongea na kukata simu, Harry akataka amshirikishe dalali ila akasita, akahisi lao moja, Harry akazima gari na kutoka na funguo, akaenda mpaka mbele ya gari na kufungua boneti, hapo ndipo alipoliona Bomu likiwa limepachikwa pembeni ya rejeta, Harry akapiga kelele huku akikimbia na kufanya wenzake wahisi kuna hatari. Dalali akabaki anashangaa huku akiwa ahisi kitu, ila alichofanya ni kufungua mlango ili atoke aulize, alipofungua tu mlango tena kabla hajashusha hata mguu, bomu likaitika, tena lililipuka kwa nguvu na kuirusha ile gari juu angani na kuitupa chini na kuiacha ikiwaka moto.
Muda huo Taita na wenzake walikuwa wamelala chini ya magari yao huku wakiushuhudia ule mchezo wa hatari uliokuwa ukifanyika mbele ya macho yao, na Harry alikuwa kwa mbali akilitazama lile tukio huku akiwa amepoteza matumaini ya kumpata binti yake.
Harry akaanza kuwasogelea wenzake huku akiliangalia lile gari likiteketea na chini alikuwepo yule bwana Dalali akiwa amelala huku akiwa hana miguu na mwili wake ulionekana hauna dalili tena za uhai.
Harry akiwa amewakaribia kabisa wakina Taita, simu yake iliita, alipoiangalia namba alikuta ni ile ya mtekaji, Harry akapokea haraka,
"Kwanini unataka kuniua?" Harry aliuliza kwa hasira baada ya kupokea simu,
"Ningetaka kukuua wala nisingekuambia uangalie kwenye injini, ningelipua tu bomu na ungekufa" Sarah aliongea kisha akacheka,
"Na kwanini hukutaka nife?" Harry aliuliza huku akishangaa jibu la huyo mwanadada,
"Najua hupendi kufa, ila sikutaka ufe kwa sababu nataka nikuumize kihisia, kisaikolojia na kimwili mpaka utakapoona ni bora ufe, hapo ndipo nitakuua" Sarah alijibu katika sauti tulivu na kumfanya Harry jasho limtoke,
"Hivi wewe ni nani na unatutaka nini sisi?" Harry aliuliza kwa upole,
"Mtanijua wakati ukifika, na siku ambayo mtanijua, ndiyo hiyo siku nitaanza kuwaua nyie viongozi wa kakikundi chenu cha kishenzi, acha nidili na vibaraka kwa sasa" Sarah alijibu,
"Nikupe nini ili umuache mwanangu?" Harry aliuliza,
"Sitaki chochote, mwanao nitamrudisha kesho, kesho jioni" Sarah alijibu,
"Nakuomba ufanye hivyo" Harry aliongea,
"Nipe niongee na Taita, namuona yupo upande wako wa kushoto" Sarah aliongea na kufanya Harry ageuke huku akiamini Sarah yupo eneo hilo, Harry akampa simu Taita kisha Harry akamfuata Tekso na kumnong'oneza afanye kitu katika mtandao ili wajue Sarah yupo upande gani? Tekso akatoa simu yake kisha akabonyeza bonyeza na hapo ile sauti ya Sarah ikawa inasikika ndani ya simu mbili, yaani simu ya Harry ambayo alikuwa anaongea nayo Taita, na simu ya pili ni simu ya Tekso.
"Taita, Taita, vijana wako waambie mimi sio mtu wa kawaida, wajiangalie namna ya kunifuata, vinginevyo nitawamaliza wote" Sarah aliongea kisha akaweka kituo,
"Mbona hakuna kijana wangu anaekufuatilia" Taita aliongea huku akiwa hajiamini,
"Toisa nipo nae hapa, au sio kijana wako huyu?" Sarah aliuliza,
"Sina mtu anaeitwa hilo jina" Taita alijifanya hamjui kijana wake,
"Sawa, nitamleta kesho pamoja na mtoto wa Harry, ili umkane akiwa anakusikia. Nawatakia majukumu mema, tchao" Sarah aliongea kisha akakata simu.
Kipindi hicho ambacho Sarah alikuwa akiongea na Taita, tayari Tekso akiwa na vijana wawili walikuwa wanafuatilia eneo ambao mpiga simu huyo alionekana kuwepo, kwa maelezo ya simu ya Tekso yalionesha mpigaji yupo mtaa huo huo, na hata Sarah alipokata simu bado simu ya Tekso iliendelea kusoma alipo mpigaji.
Tekso na wenzake walitembea mpaka katika nyumba moja iliyopo mtaa huo huo na kusimama getini, wakaanza kugonga, ila hawakujibiwa, wakaamua waruke ukuta na kuingia ndani. Bado simu ya Tekso ilikuwa ikaendelea kuonesha na muda huu iliekekeza mpigaji yupo kwenye kajumba cha pembeni yao, baada ya kukachunguza kale kajumba waligundua ni choo cha nje, wakajipanga mlangoni na kuvamia kwa fujo, hawajakuta mtu isipokuwa simu tu iliyokuwa juu ya sinki la choo,
"Aaaagh shit, ichukue hiyo line" Tekso aliongea kwa hasira na kutoka zake nje na kumuacha kijana wake mmoja akiokota mfuko wa nylon na kuuvaa ili aichukue ile simu.
***************
Kitu ambacho Sarah alikifanya ni kufunga vinasa sauti kila sehemu ya gari la Dalali, na pia hata lile bomu aliliweka siku nyingi huku akiamini ni lazima ipo siku lile gari linaweza kumuweka hatiani, ila hakujua kuwa yule Dalali pia anaweza kumuingiza matatizoni.
Na hata Dalali alipowasiliana na Harry, Sarah alisikia kila kitu, alichofanya ni kusogea tu eneo ambalo Harry alimuelekeza Dalali ajongee. Sarah alipofika aliingia kwenye nyumba ya tano kutoka nyumba ya Taita na kuanza kufuatilia namna Taita na wenzake wanavyojipanga kwa ajili ya kwenda kumvamia yeye Sarah.
Sarah alichofanya ni kuilipua ile gari ya Dalali huku Dalali akiwa ndani kwa maana aliamini mtu mwenye ramani ya kuwafikisha maadui kwake ni dalali peke yake, pia alifanya hivyo kwa maana aliona dalali hakuwa mtu mwema tena kwake, Sarah aliiamini sana ile misemo ya "dawa ya ubaya ni ubaya na dawa ya moto, ni moto".
Baada ya hiyo, Sarah akaiweka simu chooni na kuondoka zake baada ya kugundua kuna vijana wa Taita wanamfuata eneo lile.
************
Siku iliyofuata ambayo ndio Sarah aliahidi kumrudisha mtoto wa Harry.
Mida ya saa kumi jioni mlinzi wa Taita aliingia sebuleni huku akiwa amebeba mabox mawili, moja kubwa na jingine dogo, na yote yalikuwa yamefungwa na karatasi za kuwakawaka au karatasi za zawadi "gift paper". Sebuleni walikuwepo wote, walikuwa wanasubiri kupigiwa simu na Sarah, maana waliamini hivyo kwa kuwa Sarah aliwaahidi kuwapelekea mtoto wao.
"Zimetoka wapi?" Taita aliuliza kwa uoga huku akiwa hajiamini kabisa,
"Zimeletwa na gari za airport, zile zinazoletaga bahasha mizigo kutoka kwa Vin" Mlinzi alijibu,
"Aah sawa" Taita alijibu kisha akabeba box moja lile kubwa na kuiondoa ile karatasi ya Zawadi,
"Box zito hilo, sijui vin amenitumia nini?" Taita aliongea kisha akakichomoa kikaratasi kidogo kilicho na maneno kilichokuwa juu ya box, kilikuwa kimeandikwa. "Kubwa ni lako, na dogo ni la Harry"
Baada ya kusoma hivyo, Taita akatabasamu,
"Leo Vin amekukumbuka" Taita aliongea huku akimpa kile kikaratasi Harry aliyekuwa na mawazo, Harry akakisoma kisha lile box dogo akalivutia kwake,
"Fungua tuone zawadi" Trigger alimtania Harry huku akicheka ila Harry wala hakujisumbua kutaka kufungua lile box.
Mzee mzima Taita alikuwa akiendelea kupasua lile box, na sasa ilifika hatua moja tu ya kulifungua ili ajue zawadi iliyomo, macho ya watu wote yalikuwa ndani ya ilo box, Taita akalifungua, wote wakashtuka baada ya kukuta kichwa cha mtu, tena Taita aliruka kidogo adondoke,
"Kitoe" Taita alimwambia Trigger huku Taita akiwa amesimama mbali kabisa, Trigger akakitoa kile kichwa, hapo ndipo wate walipigwa na mshangao, kilikuwa kichwa cha Toisa, kilitisha kwa kweli na puani kiliwekewa karatasi iliyokuwa na maneno yaliyoandikwa "ndio haki ya mwenye dhambi, kila damu yenye dhambi itaigharimu familia yake. Mchuma janga hula na ndugu zake"
Hayo maneno na kilichomo ndani ya box lile kubwa kilimtisha sana Harry pamoja na wengine.
Harry akaamini sasa lile box dogo litakuwa na kichwa cha mwanae. Harry akalifungua kwa pupa na kukuta karatasi iliyoandikwa "leo ni siku ya kukumbukwa katika familia yako, hii Zawadi haijatoka kwa Vin, ni zangu mimi mtu mbaya kabisa"
Baada ya Harry kusoma maneno hayo, nguvu zikaanza kumuishia na kushindwa kufungua box, Trigger akaliendea box na kulifungua, Harry akashindwa hata kuangalia, machozi yalikuwa yakimtoka huku Trigger aliyekuwa jirani na box akibaki na mshangao.............
*********ITAENDELEA**********
the Legend☆