RIWAYA : SALA YA SARAH
MTUNZI : ALEX KILEO.
SEHEMU YA ISHIRINI NA SABA.
ILIPOISHIA...................
Ndani ya gari walikuwa na maongezi ya hapa na pale, iliwachukua nusu saa kufika nyumbani kwa Dokta Pendo, walipofika Sarah aliegesha gari yake upande wa pili wa barabara.
Ila waliweza kukuta vijana kadhaa wenye silaha wakiwa wameizunguka nyumba ya Dokta Pendo, hapo Sarah alimtoa kile kitambaa cheusi machoni na dokta Pendo akaweza kuwashuhudia wale vijana,
"wale ni polisi?" Dokta Pendo aliuliza, na wakati huo ndani Alikuwa akitoka Taita na Trigger,
"sio polisi wale, ni watu wako hao wanakutafuta" Sarah alijibu,
"ebu ngoja nishuke nikaongee nao" Dokta Pendo aliongea huku akitaka kufungua mlango,
"subiri kwanza, usiwe na pupa" Sarah alimwambia Dokta Pendo na wakati huo Trigger na Taita waliweza kuiona ile gari ambayo alikuwepo Sarah na dokta Pendo, ila hawakuweza kujua mtu aliyekuwepo ndani ya ile gari, ila waliitilia mashaka, Taita akiwa na Trigger waliamua kuisogelea ile gari huku bunduki zikiwa mkononi, walihisi kabisa mule ndani ya gari hakukuwa na watu wazuri.
Sarah aliweza kuona namna Taita na Trigger wanavyokuja, akawasha gari, lakini gari haikuwaka, akajaribu tena na bado gari haikuwaka, na kipindi hicho Taita na Trigger walibakiza hatua mbili tu waifikie gari ya Sarah, hapo Sarah akapata kihoro, tumbo joto.
Akajaribu tena kuwasha ila gari ikagoma,
"Shuka kwenye gari malaya wewe" Taita aliongea huku mtutu ukiwa usawa wa kichwa cha Sarah, kwa maana hiyo walikuwa tayari wameshamfikia Sarah, Sarah akatabasamu, halikuwa tabasamu la furaha, ila ni tabasamu la kukata tamaa na muda huo Taita alitoa tabasamu la ushindi, Sarah akanyoosha Mikono juu ikiwa ni ishara ya kutii amri..................
***********ENDELEA**********
Sarah akili ikachemka, na vile hujiamini kwa kasi aliyokuwa nayo, alichofanya ni kuushika mkono wa Taita wenye bastola na kuuvuta kwa nguvu mkono wa Taita wenye bastola na kuuvuta kwa nguvu kisha akaachia ngumi nyepesi iliyompiga Taita kooni, Taita akajikuta akiiangusha ile bastola yake mapajani mwa Sarah, kisha Sarah akaikota ile bastola na kumuwekea Taita usawa wa kichwa huku akiwa amemkaba Taita,
"waambie mbwa wako waweke silaha chini na wasogee nyuma" Sarah aliongea huku mdomo wake ukiwa jirani na sikio la Taita, Taita akaona bora atii amri, akajitahidi na kupaza sauti akiwaamuru vijana wake waweke silaha chini na kurudi nyuma, vijana wakatii amri ya mkuu wao, kisha Sarah akatoka ndani ya gari na kumuamuru Taita aingie katika siti za nyuma za gari, Taita akatii kisha nae akaingia na yeye siti za nyuma,
"Dokta Pendo endesha gari" Sarah alimwambia Dokta Pendo ambaye muda wote alikuwa akitetemeka,
"gari si imekataa kuwaka?" Dokta Pendo aliuliza huku akitetemeka,
"we washa bwana, jaribu huenda itakubali" Sarah aliongea na kufanya Dokta Pendo asogee upande wa dereva na kujaribu kuwasha gari, ikawaka,
"tunaelekea wapi?" Dokta Pendo aliuliza,
"nenda eneo lolote lile ambalo unajua kuna pori" Sarah aliongea na kisha Dokta Pendo akaondoa gari, kuna vijana kama wawili walitaka kuokota silaha ili waishambulie gari, Sarah akawawahi na kuwafyatulia risasi, wakafa palepale. Kipindi hicho chote Taita alikuwa tumbo joto, hakuamini kama ametekwa kizembe hivyo, ila hakuwa na cha kufanya.
********************
Sajenti Minja alikuwa bize na lap top yake, bado alikuwa akifuatilia kuhusu ile nyumba iliyoungua, bahati nzuri aligundua kuwa mwenye ile nyumba pia alimuoa mwanamke aliyeitwa margret ambaye alikuwa ni mfanyakazi wa serikali, baada ya kumfuatilia margret kupitia mtandao akagundua kuwa ana undugu wa karibu na Taita, pia akagundua kuwa hata ile hotel iliyojengwa kwenye ile nyumba iliyoungua zamani, ni hotel ya Taita,
Sajenti Minja akakuna kidevu, akaamua amtafute Sarah yule rafiki yake wa kwenye memory card, alimtafuta kwa njia ya mtandao, aliutumia whatsap kwa kuwa alikuwa na namba yake ya simu,
"upo wapi mrembo?" Sajenti Minja aliuliza baada ya salamu,
"nipo marekani, vipi kwani?" Sarah alihoji,
"hakuna kitu, nimekukumbuka tu" Sajenti Minja aliongea,
"bado wewe ni polisi?" Sarah alimuuliza Sajenti Minja,
"bado ndugu yangu, hizi kazi zetu ngumu kuziacha"Sajenti Minja alijibu huku akitabasamu,
"komaa bwana, endeleza mapambano" Sarah aliongea,
"poa bwana, wacha nikuage" Sajenti Minja aliongea,
"poa afande, nashukuru kwa kunikumbuka" Sarah aliongea huku akitabasamu,
"usijali, nitaendelea kukumbuka" Sajenti Minja aliongea,
"poa" Sarah alijibu kisha akakata mawasiliano.
Sajenti Minja akabaki anawaza, swali alilojiuliza kuwa yule binti aliyepambana nae kule pagaleni ni nani?
Mwisho Sajenti Minja akaamua aende Vin hotel, aliamua akamtafute Taita ili aweze kumuuliza maswali machache kuhusu margret na familia yake, aliamini kufanya hivyo kunaweza kumpa mwanga kidogo juu ya kile anachokitafuta.
Akatoka nje ya jengo la polisi na kuelekea moja kwa moja kwenye gari lake, akaingia na kuliondoa.
*******************
Kwenye kambi ya Taita kulikuwa na majonzi makubwa, walikuwa hawajui kiongozi wao yupo kwenye hali gani?
Muda huo aliyekuwa akiumiza kichwa sana ni Trigger, kwa maana tukio zima lilitokea mbele yake, na muda huo bado alikuwa eneo lile lile la nyumbani kwa Dokta Pendo, alikuwa na vijana wake, akawaamuru vijana wakapumzike majumbani mwao, kisha yeye akaingia kwenye gari lake alilokuja nalo na kuamua kwenda moja kwa moja nyumbani kwa Taita.
Wakati akiwa ndani ya gari alijitahidi sana kuwapa taharifa watu muhimu katika kundi lao, hakutaka kuwaambia ukweli, alichowaambia ni kuwa wote wakutane muda huo nyumbani kwa Taita, kuna tukio lisilo la kawaida limetokea.
Baada ya muda Trigger aliwasili nyumbani kwa Taita, akaingiza gari ndani, akaelekea moja kwa moja sebuleni, akawakuta Tekso na Strategic wakiwa wanamsubiri,
"Harry yupo wapi?" Trigger aliuliza,
"bado hajatimba, ila nadhani tunaweza kuendelea na kikao" Tekso alijibu,
"na bosi naye yuko wapi?" Strategic aliuliza lakini Trigger hakuonekana kuwa tayari kujibu hilo swali, na muda huo Harry alikuwa anaingia huku akionekana hajafurahishwa na kikao hicho cha usiku. Harry akawasalimia wenzake na kisha akakaa kwenye kochi,
"nadhani tunaweza kuanza kikao" Trigger aliongea huku akiangalia chini,
"Taita yuko wapi, maana yeye ndio anatakiwa aongoze kikao na sio wewe" Harry aliongea huku akionekana kumshangaa Trigger,
"lengo la kikao ni hilo, kuwajulisha ni wapi alipo Taita" Trigger aliongea na kufanya wenzake watege vizuri masikio yao,
"ukiwa unaeleza kitu unatakiwa uende direct kwenye jambo husika, sio kukatisha katisha maneno" Harry aliongea kwa ukali baada ya kutofurahishwa na mtindo anaoutumia Trigger katika kuongea,
"ok, ni hivi, Taita ametekwa na Sarah muda mchache uliopita" Trigger aliongea na kufanya miili ya wenzake ipigwe na ganzi,
"bado sijakuelewa, unasema?" Harry aliuliza tena kanakwamba hajasikia kilichozungumzwa na mwenzie huyo,
"ilikuwaje kuwaje yaani?" Tekso nae akapandishia swali jingine.
Mpaka kufikia hapo wote walikuwa wamechanganyikiwa, maana walikuwa wanamjua vyema Sarah katika suala zima la kufanya unyama, na hakuna hata mmoja aliyekuwa na imani ya bosi wao huyo kurudi akiwa hai.
"tueleze basi kilichotokea" Harry aliongea baada ya kumuona Trigger akiwa kimya,
Trigger akaeleza kila kitu, hakuficha chochote.
"tunafanyaje sasa?" Tekso aliuliza ila hakuna aliyemjibu, hali ilikuwa mbaya sana kwenye hii kambi,
"sasa mbona hamjibu?" Tekso aliuliza tena, ila safari hii alitumia sauti kubwa kidogo Baada ya kuona wenzie hawakutilia mkazo swali Lake la hawali,
"taratibu basi, hilo swali ulilouliza halihitaji jibu la kukurupuka, linahitaji nafasi ya kufikiria" Strategic alijibu huku akiwa amefunga macho,
"kweli tunahitaji muda kiasi wa kupata cha kufanya kuhusu hili suala" Harry alionekana kumuunga mkono Strategic,
"ndio tufikirie hapa hapa na tupate jibu" Trigger aliongea,
"na hiyo pia haiwezekani, inaweza kutuchukua siku mbili au tatu kuweza kupata fikra sahihi" Strategic aliongea,
"siku mbili au tatu? Wewe una wazimu nini? Siku hizo zote utakuwa unafikiria nini?" Trigger aliongea kwa jazba huku akionekana amekereka kutokana na majibu ya Strategic,
"Trigger kwani wewe unapajua alipopelekwa Taita?" Harry aliuliza huku akimuangalia Trigger,
"sipajui, ningekuwa napajua si ningeshaenda?" Trigger alijibu,
"unajua ni wapi Sarah anapokaa?" Harry akamtupia swali jingine Trigger,
"hapana" Trigger akajibu,
"sasa kwanini Strategic anaposema hili suala itabidi lichukue siku mbili au tatu kuweza kupata fikra sahihi, Wewe unakuwa unapinga wakati unajua kabisa adui tunaepambana nae hatujui pa kumpata?" Harry aliongea huku akimtazama Trigger,
"Tekso si yupo, anaweza kucheza na technolojia tugundue chochote" Trigger aliongea,
"kwani uko alipo Taita ameenda na simu?" Tekso aliuliza,
"simu ameiacha ndani ya gari" Trigger alijibu,
"dah, basi ni ngumu sana kujua alipo" Tekso alijibu na kufanya Trigger achoke kabisa,
"mi nadhani tutawanyike tu, kesho asubuhi tukutane ili tujue cha kufanya, na kila mtu akalale huku akitafuta njia ya kuweza kumpigania Taita" Harry aliongea huku akiwatizama wenzake,
"nyie nendeni, mimi nitabaki hapa nikilinda nyumba, maana hakuna mtu zaidi ya mlinzi" Trigger aliongea,
"sawa, mimi naenda, ila kesho tukutane hapa asubuhi kama nilivyosema" Harry aliongea huku akiinuka kwenye kochi,
"sawa mkuu, naimani kesho tutakuwa na mbinu zozote" Tekso alijibu huku nae akiinuka katika kochi,
"na wewe uende, mimi nataka nifunge mlango" Trigger alimwambia Strategic aliyekuwa bado amekaa,
"taratibu mkuu, kila kitu kinahitaji mpangilio, nasubiri wenzangu wapite mlangoni na mimi ndio nifuate" Strategic alijibu katika sauti tulivu,
"nyanyuka bwana, unajifanya mtu wa mipango wakati umeshindwa kupanga namna ya kumkomboa Taita" Trigger aliongea huku akimvuta Strategic ainuke, strategic akainuka na kuondoka zake huku wakimuacha Trigger akiwa amesimama mlangoni akiwatazama.
*********************
Usiku huu Sajenti Minja aliingia Vin hotel na kuelekea moja kwa moja mapokezi,
"nahitaji Kuongea na meneja wa hapa" Sajenti Minja aliongea huku akionesha kitambulisho chake, dada wa mapokezi akamuelekeza ofisi ya meneja ilipo, akaenda na kumkuta msichana akiwa ndio meneja wa pale, akamsalimu,
"kama nilivyosema hawali, mimi ni askari na hapa nimekuja nikiwa nataka kuonana na mmiliki wa hii hotel" Sajenti Minja aliongea kwa utulivu,
"Mimi hapo sina cha kukusaidia, labda tu nikupe namba yake" meneja aliongea kinyenyekevu,
"pia huo ni msaada" Sajenti Minja aliongea huku akiitoa simu yake na kisha yule dada Meneja akamtajia namba ya Taita, Sajenti Minja akainakiri katika simu yake.
"usimpigie usiku, mtagombana" Meneja alimtahadharisha Sajenti Minja,
"usijali, nitampigia kesho asubuhi" Sajenti Minja alijibu huku akitabasamu na kutoka zake nje, akaelekea kwenye gari yake na kuingia ndani, alipoiwasha ili aondoke, ndipo alishuhudia gari aina ya range Rover likikatiza mbele yake huku likiwa katika mwendo mkali, akalikumbuka hilo gari kuwa ni la muharifu anayemtafuta.
Sajenti Minja nae akaitoa gari yake kwa kasi kuifuata ile Range Rover, alijitahidi kuifanyia ishara zote ili ile Range Rover isimame, badala yake iliongeza mwendo, alafu eneo ilipokuwa inaelekea ni eneo la porini.
Sajenti Minja akaamua atumie akili ili kuweza kuikamata ile gari, akaendelea kuikimbiza kwa nusu saa, akafanikiwa kuipita kisha akaisimamisha kwa ghafla gari yake katikati ya barabara, ile Range Rover nayo ikaminya breki, Sajenti Minja akawasha tochi yake na kummulika dereva wa ile gari, alikuwa ni Dokta Pendo, tena alikuwa na hofu tele.
Sajenti Minja akachomoa bastola yake na kushuka ndani ya gari,
"telemka chini, Mikono ikiwa juu" Sajenti Minja aliongea huku bastola yake akimuelekezea Dokta Pendo, hapo Dokta Pendo akazidi kuchanganyikiwa, akashuka kwenye gari.
"mpo wangapi kwenye gari na mmebeba nini?" Sajenti Minja aliuliza lakini Dokta Pendo hakujibu, ni machozi tu yalimtoka,
"wewe mwanamke si nakuuliza?" Sajenti Minja aliongea kwa ukali, lakini Dokta Pendo hakujibu, aliendelea kulia kimya kimya, sasa Sajenti Minja akahisi ndani ya gari kuna kitu na ndio maana yule dada analia, Sajenti Minja akalisogelea gari na kufungua mlango wa nyuma kwa nguvu.......
*********ITAENDELEA*********
the Legend☆