Riwaya: Sala ya Sarah

Riwaya: Sala ya Sarah

RIWAYA : SALA YA SARAH

MTUNZI : ALEX KILEO

SEHEMU YA SITINI NA MBILI.

ENDELEA..................

Sajenti Minja na vijana wake wakavamia ndani ya ile nyumba huku wakitumia tochi zao, walikagua nyumba nzima hawakubahatika kukuta mtu katika hiyo nyumba, nyumba yenyewe haikuwa na fenicha yoyote ndani,

"atakuwa ametuzidi akili" Sajenti Minja aliongea huku akitoka nje na baadhi ya askari wakabaki ndani wakiendelea kukagua.

"Mkuu huku nyuma kuna ngazi inayoonesha kuna uwezekano wa huyo mtu kuwepo juu ya nyumba" Askari aliongea na kumfanya Sajenti Minja azunguke nyuma ya nyumba na kukuta ngazi ikiwa imeegeshwa ukutani, Sajenti Minja akapanda mpaka juu ya nyumba na kukuta kuna eneo zuri tu la kukaa watu, na zaidi alikuta kuna viti viwili na meza moja katikati ya vile viti.

Sajenti Minja akasogea kwa karibu huku akiongeza umakini wa macho, akaona damu ikiwa chini ila imeganda, Sajenti Minja akainama na kuigusa ile damu ila hakuambulia kitu, damu ilionekana ya muda mrefu. Sajenti Minja akatupa jicho juu ya meza na kuona ganda la risasi likiwa lipo juu ya meza, Sajenti Minja akahisi eneo hilo kuna mtu alipigwa risasi ila ni siku nyingi sana. Sajenti Minja akatoa simu mfukoni na kupiga picha kadhaa eneo hilo, kisha akatelemka chini,

"hamjabahatika kuona kitu chochote uko ndani?" Sajenti Minja aliuliza askari waliokuwa ndani,

"hakuna kitu mkuu" Askari mmoja alijibu,

"sawa, nyie ondokeni kaendeleeni na shughuli zenu" Sajenti Minja aliwaruhusu askari waondoke, askari wakaondoka na kumuacha peke yake huku akijiuliza ile nyumba ni ya Sarah au ya nani?

,

"atakuwa amekimbia, ila mbona gari yake ameiacha ndani?" Sajenti Minja alijiuliza bila kupata jibu sahihi, akaamua atoke nje na kuanza kuelekea sehemu ilipo gari yake, kwa kuwa aliegesha umbali mrefu kidogo ilimbidi atembee taratibu huku akigeuka kila muda kuiangalia ile nyumba aliyoingia Sarah, ila kabla Sajenti Minja hajaifikia gari yake, alikutana na watu watatu waliomsimamisha, walikuwa ni vijana wawili na mzee mmoja, kati ya wale vijana wawili, Sajenti Minja alimkumbuka kijana mmoja ambaye alimsimamisha hapo hawali na kumuuliza jina la mtaa huo.

Yule mzee na Sajenti Minja wakasalimiana,

"Mimi ni balozi wa huu mtaa, huyu kijana amekuona ukiwa na polisi na umeingia nyumba ile" Mzee aliongea huku akioneshea kwa kidole nyumba aliyoingia Sarah,

"umekuja wakati muafaka mzee, mimi ni afisa wa polisi, kuna mtu aliingia kwenye nyumba ile, huyo mtu anatafutwa na polisi" Sajenti Minja aliongea huku akimpatia balozi kitambulisho chake, balozi akakipokea na kukiangalia, kisha akampa kijana mmoja ambaye nae alikipokea na kukikagua kisha yule kijana akamtupia jicho balozi na kutingisha kichwa chake kwa kukipeleka juu, kuashiria amekubaliana na alichokiona katika kitambulisho,

"mmemkamata?" Balozi aliuliza huku akimrudishia kitambulisho Sajenti Minja,

"hapana, ila kwa namna alivyoingia na kuondoka, inaonesha wazi ni mtu ambaye anaifahamu vizuri ile nyumba" Sajenti Minja aliongea,

"watakuwa vibaka tu, kwa maana mwenye hiyo nyumba tangu ameinunua alirudi mara moja tu kuweka geti la mbele, ila kutokea hapo sijawahi kumuona tena" Balozi alimjibu Sajenti Minja,

"ila huyo mtu tunayemtafuta ameingiza na gari kabisa ndani ya geti, tena hilo geti alifungua na funguo kutoka mfukoni mwake" Sajenti Minja aliongea na kumfanya balozi atoe macho,

"ameingia na gari? ebu twende" Balozi aliongea huku akianza kuondoka na wale vijana wakamfuata na nyuma alikuwepo Sajenti Minja.

Walifika mpaka katika ile nyumba na kuingia, kweli waliikuta gari ndani ya geti, Balozi akazidi kushangaa, kisha Balozi akauendea mlango wa kuingilia sebuleni na kuukuta ukiwa umeharibiwa vibaya na risasi,

"sasa kama mnasema aliingia ndani na nyie mkavunja mlango, kwanini hamkumkuta ndani?" Balozi aliuliza huku akishangaa,

"ndio maana nikasema kuwa huyo mtu anaijua vizuri hii nyumba" Sajenti Minja alijibu,

"ebu twende upande wa nyuma" Balozi aliongea huku akielekea nyuma ya nyumba na Sajenti Minja na wale vijana wakamfuata.

"ebu vuta hilo dirisha" Balozi alimwambia kijana wake ambaye alilivuta dirisha na likanyanyuka zima zima Kama mlango wa mbele wa genge, Sajenti Minja akili zikamwambia huenda Sarah alifanya kitu hicho, sasa swali likabaki ni nani aliyezima taa?

"kwani mzee huyo mmiliki wa hii nyumba ni nani?" Sajenti Minja aliuliza,

"ni kabinti kamoja hivi kadogo dogo, kanaitwa salama sijui" Balozi aliongea,

"hapana mzee, anaitwa Sarah" Kijana mmoja alimrekebisha Balozi huku akimcheka, huo ukawa mwiba kwa Sajenti Minja,

"basi ndiye huyo aliyeingia hapa, anatafutwa na polisi kwa tuhuma za kuua na kuteka, anaitwa Sarah Isack" Sajenti Minja aliongea huku akiitoa simu yake na kumuonesha Balozi picha ya Sarah,

"ndiye huyu haswaaa mmiliki wa hii nyumba, sasa unaponiambia ni muuaji unanichosha kabisa" Balozi aliongea huku akitabasamu kwa mshangao,

"vijana pandeni uko juu ya nyumba alafu mmuambie Balozi kuna nini?" Sajenti Minja alimwambia wale vijana kisha kijana mmoja akapanda na kusema alichokiona, Balozi akazidi kushangaa,

"tulikuwa hatujui kama ni mtu hatari hivyo?" Balozi aliongea,

"mkae mkijua hivyo, na muda wowote akirudi tena hapa, mnitaharifu" Sajenti Minja aliongea huku akiwapa karatasi ngumu yenye namba yake ya simu, kisha akaondoka zake na kumuacha Balozi na vijana wake wakilizungumzia hilo tukio la kushangaza lililotokea mtaani hapo.

********************

Sarah wakati akitoka super market hakuweza kumuona Sajenti Minja, ila baadae wakati akiwa njiani kurudi kwake ndipo alipogundua kuna gari inamfuatilia, hakujua hiyo gari ni ya nani, ilimbidi atulize macho yake na kuiangalia hiyo gari kwa umakini mkubwa na kuitambua hiyo gari ni Sajenti Minja, alichofanya Sarah ni kumpoteza maboya Sajenti Minja.

Sarah alibadili njia na kuelekea upande ilipo ile nyumba, sio kwamba haikua nyumba yake, ile ni nyumba yake ambayo alimnunulia babu yake kutokana na pesa aliyopewa na Taita wakati ule Taita alipokuwa mateka wa Sarah, kama unakumbuka Taita alimpa agizo Trigger la kumpatia pesa Sarah. Sasa Sarah baada ya kuipata ile pesa alinunua nyumba ambayo alifanya kama fidia kwa babu yake baada ya nyumba ya babu yake kuchomwa moto.

OK, tuendelee tulipoishia.
Baada ya Sarah kugundua anafuatiliwa, aliamua aende moja kwa moja kwenye hiyo nyumba, Sarah baada ya kuingiza gari ndani alifunga geti kisha akatoa bidhaa ndogo ndogo alizotokanazo super market na kuziweka kwenye pochi yake kubwa, kisha akadandia ukuta na kumchungulia Sajenti Minja na kumuona akiongea na simu, sarah akahisi huenda Sajenti Minja anaita polisi zaidi.

Sarah akafungua mlango na kuingia ndani, alitaka kuzima taa ili atokee dirisha la nyuma ambalo ni bovu, ila aliona unit za luku ni chache na umeme utazima muda wowote, Sarah akatabasamu na kutokea dirishani, kisha akapanda ukuta na kutua upande wa pili, akapotea eneo hilo na kwenda mtaa wa pili na kuchukua bajaj iliyompeleka nyumbani kwake.

********************

Vin na Strategic wakiwa wamekaa kwenye viti huku wakizitazama zile chupa za chai, waliweza kushuhudia mlango wa mbele ukifunguliwa na akatoka mzee mmoja mwenye mwili mkavu, ingawa umri ulionekana kumtupa kidogo ila bado alikuwa na nguvu za kutembea mwenyewe bila tatizo.

Yule mzee alitembea mpaka alipowafikia Vin na Strategic, kisha Vin na Strategic wakasimama na kumsalimia, akaitikia kwa uchangamfu,

"mbona hamjaweka vinywaji bwana, wekeni msiogope" Mzee aliongea huku akikaa kisha kijana wake yule aliyewapokea wakina Vin akammiminia kahawa kwenye kikombe kidogo,

"Mimi ndio Dokta Innocent Malle, haya na nyie mjitambulishe sasa ili tujuane" Yule mzee aliongea huku akitabasamu,

"Mimi naitwa Vin Denis, huyu ni rafiki yangu tu amenisindikiza, mimi hasa ndio mwenye shida" Vin aliongea huku akitabasamu pia,

"kupitia jina bado sijakujua, huenda ninaweza kukujua baadae baada ya maongezi" Dokta Innocent Malle aliongea na kucheka,

"kweli Dokta" Vin nae alikubaliana nae,

"twende kisomi sasa, nenda moja kwa moja kwenye lengo la wewe kunitafuta mimi" Dokta Innocent Malle aliongea na kunywa kahawa kidogo,

"kuna kitu kina utata kidogo kuhusu maisha yangu, kwanza kabisa mimi ni mtoto wa Taita, lakini bado kuna habari zinasema Taita sio baba yangu ila alinichukua kipindi nipo mdogo na kunifuta kumbukumbu zangu zote, na hiyo kazi ya kufuta kumbukumbu uliifanya wewe" Vin aliongea na kumuangalia Dokta Innocent Malle ambaye muda wote wa maelezo hayo alionekana yupo kawaida, wala hakushtuliwa na maelezo ya Vin,

"ujue kijana mimi ni mtu mmoja mkweli sana, hasa kwenye jambo linalolenga maisha ya mtu moja kwa moja, unaona hii nyumba, hii nyumba nilijenga kwa pesa ya Taita, kipindi kile cha nyuma serikali ilikuwa haina uwezo wa kutoa mshahara na mtu ukanunua Kiwanja kikubwa kama hiki na kujenga nyumba kubwa hivi.

Sasa hapa point yangu ni ipi? ndio, miaka ya nyuma Taita alikuja hospitali na kuniomba nimfanyie kazi ya kumfuta kumbukumbu mtoto mdogo wa umri wa miaka minne, kisheria ni kosa kupoteza kumbukumbu za mtu tena bila sababu ya msingi, ila kwa maelezo waliyonipa ilibidi nikubali kufanya jambo lile Kaa ajili ya kumsaidia mtoto, kwa maana yule mtoto ningemuacha akue huku akiwa na akili na kumbukumbu ya zamani, basi maisha yake yangekuwa mafupi sana, ni lazima tu angeuawa na Taita kwa maana yule mtoto angeutambua na kuukumbuka unyama waliofanyiwa wazazi wake, ni lazima yule mtoto angetaka kulipa kisasi akiwa bado hajakomaa vizuri kimwili na kiakili" Dokta Innocent Malle aliongea na kushushia na kahawa,

"unyama upi waliofanyiwa wazazi wake?" Vin aliuliza huku akimeza mate,

"Harry alikuwa rafiki yangu sana, Harry ndiye aliyeniunganisha na ile kazi ya Taita, kwa hiyo kwa maelezo ya Harry aliniambia kuwa wazazi wa yule mtoto walichomwa moto wakiwa ndani ya nyumba, ila hakuniambiaa ni nani aliyefanya hivyo, ila hapa juzi juzi kabla Harry hajafa alikuja kuniomba nihifadhi familia yake kwa kuwa kuna tatizo, alisema kuna watu wanataka kuiteketeza familia yake, akiwemo baba yako Taita na msichana mmoja aliyemtaja kwa jina la Sarah, na nilipomuuliza ni kwanini Taita ambaye ni rafiki yake wa karibu anataka kumuua? Alinijibu kuwa ni kisa cha miaka ishirini iliyopita, ambacho ndicho hicho cha wazazi wa yule mtoto niliyempoteza kumbukumbu, alidai Sarah ni mtoto aliyeokoka kwenye moto ule na alipotea kwa muda mrefu, ila amerudi na lengo lake inaonekana ni kulipa kisasi kwa Taita na watu walioshiriki kuwaua wazazi wake. Hiyo ndio ilikuwa sababu ya Harry kuwindwa na Sarah.

Na nilipomuuliza kwanini Taita nae anataka amuue, alinijibu kuwa alimwambia Taita Kuwa yeye Harry anataka kuondoka na kukimbia mapambano dhidi ya Sarah, hilo ndilo lilikuwa kosa, na pia anadai kuna siku alimuoneshea Taita bastola wakiwa hospitali, lakini alishangaa kuona akipigwa risasi ingali yeye Harry hakufyatua hizo risasi, na hata bastola yake haikuwa na risasi, huo ndio ukawa uadui kati ya Harry na Trigger na mtoto wa Trigger ambaye nadhani ni wewe" Dokta Innocent Malle aliongea huku akimnyooshea kidole Vin,

"sasa hapo mbona sijapata jibu bado ni nani haswa aliwachoma wazazi wa yule mtoto?" Strategic aliuliza,

"kijana una umelewa mdogo sana, yaani habari yote niliyozungumza na bado hujapata jibu, kwanini hujiulizi ni kwanini Sarah anataka kulipa kisasi cha kifo cha wazazi wake na mlengwa mkubwa ni Taita? hujiulizi kwanini Harry alikubaliana na hoja za Sarah na ndio maana akataka akimbie? Hujiulizi ni kwanini Taita anaficha ukweli kwa yule mtoto aliempotezea kumbukumbu na kumdanganya kuwa yeye ndio baba yake?" Dokta Innocent Malle aliongea,

"mzee, huyo mtoto mwenyewe ndio mimi" Vin aliongea akitegemea Dokta atashtuka,

"mbona ulishajitambulisha mapema, vijana mnapenda sana kurudiarudia mambo na ndio maana mnadumaa kiakili, kisa cha mimi kukupa hii habari yote ni baada ya wewe kusema kuwa Inasemekana ulifutwa kumbukumbu zako ukiwa mdogo, yaani hapo tu ulikuwa umeshajitambulisha, na ndio maana na mimi nikaongea yote ninayofahamu kuhusu hilo tukio" Dokta Innocent Malle aliongea huku akitabasamu,

"kwa hiyo hapo point kubwa ni kwamba mimi sio mtoto wa Taita?" Vin aliuliza,

"hapana, hapo point kubwa ni kwamba ulifutwa kumbukumbu zako wakati ukiwa mtoto, Sasa hilo suala la wewe kuwa sio mtoto wa Taita, hicho ni kijipengele kilichopatikana kwenye maelezo ya point kubwa" Dokta Innocent Malle alijibu huku akitabasamu,

"labda una chochote cha nyongeza?" Vin alimuuliza Dokta Innocent Malle,

"Mimi ndio nilipaswa kukuuliza wewe hilo swali, kwa maana wewe ulikuja kuuliza na mimi kazi yangu ni kujibu" Dokta Innocent Malle aliongea na kumfanya Strategic atabasamu kwa namna mzee huyu alivyokuwa anajibu,

"je ulisikia jina langu la hawali kabla sijafutwa kumbukumbu?" Vin aliuliza huku akiamini huyo mzee hawezi kujibu hilo swali,

"Sebastian Isack, hilo ndilo jina lako nililiandika kwenye daftari la vipimo" Dokta Innocent Malle alijibu na kumfanya Vin atoe macho,

"kwa hiyo mimi na Sarah Isack ni ndugu!? Mbona vipimo Vinapinga?" Vin aliuliza,

"hilo suala sijui, cha muhimu nenda kamuulize Taita, anaweza kukusaidia zaidi, au yule kijana wake mweupe mwenye michoro mwilini" Dokta Innocent Malle alijibu,

"au mzee nikamchukue Sarah uje utupime?" Vin aliuliza,

"hapa ni nyumbani na sio hospitali, alafu mimi ni daktari mstaafu, sio daktari tena" Dokta Innocent Malle alijibu huku akitabasamu,

"nisaidie tu" Vin aliongea,

" wewe unaamini Sarah ni ndugu yako?" Dokta Innocent Malle aliuliza huku akiinuka kwenye kiti,

"si mpaka vipimo vioneshe hivyo" Vin alijibu,

"Sarah sio ndugu yako kijana, jamani muda wangu wa maongezi umeisha, ngoja niende kupumzika kidogo" Dokta Innocent Malle aliongea huku akiondoka na Kijana wake akimfuata kwa nyuma, wakati huo Vin akiwa ameduwaa tu baada ya kuambiwa kuwa Sarah sio ndugu yake,

"utata unaendelea, mzee ameianzisha mwanzo taharifa ya habari" Strategic aliongea huku akipiga mihayo.......

************ITAENDELEA************

the Legend☆
 
RIWAYA : SALA YA SARAH

MTUNZI : ALEX KILEO

SEHEMU YA SITINI NA TATU.

ENDELEA..................

"kumbe mzee unalijua hilo suala, kwanini hukuniambia mapema sasa?" Vin aliuliza wakati mzee akiondoka,

"Mimi sijui chochote, ila si umesema majibu ya vipimo yanasema Sarah sio ndugu yako? Basi labda huenda ni kweli Sarah sio ndugu yako" Dokta Innocent Malle aliongea na kuondoka zake na kumfanya Strategic atabasamu,

"mzee kala chumvi za kutosha, ndio maana anatuvuruga" Strategic aliongea huku akiinuka kwenye kiti,

"ndio tunaondoka au?" Vin aliuliza huku akimuangalia Strategic,

"si ndio, au tunakaa tunasubiri nini wakati mzee ndio ameshamaliza hivyo" Strategic aliongea huku akielekea kwenye geti la kutokea nje na kumfanya Vin amfuate bila kuongeza neno.

Waliondoka mpaka kwenye gari na kuingia, strategic akawasha gari na kuliondoa kwa mwendo wa wastani,

"nadhani umeshajua kuwa Taita sio baba yako, unafanyaje sasa baada ya hapo?" Strategic aliuliza,

"unadhani nitafanya sasa, mimi nafahamu Taita ni baba yangu, hata kama sio baba yangu wa damu, kwa namna alivyonilea tu, naamini yeye ni baba yangu" Vin aliongea huku akitazama chini,

"ila katika maelezo ya yule mzee, amesema pia Taita ndio aliwaua wazazi wako, wewe hilo umelichukuliaje?" Strategic aliuliza,

"sio jambo zuri, ila wazazi wangu siwajui na sijajua upendo wao ulikuwa vipi kwangu, ila kwa namna Taita anavyopenda, naamini inatosha kabisa kuamini hakuna mtu muhimu kwangu kama huyu" Vin aliongea kwa utulivu,

"Sarah anataka kumuua Taita, utamzuiaje wakati umeshajua Sarah ni dada yako?" Strategic aliuliza,

"Sarah sio dada yangu kwa maana hakuna vipimo vilivyothibisha hilo, na kama kweli lengo lake ni kumuua baba yangu, basi ni lazima yeye afe kwanza" Vin aliongea huku macho yake yakiwa mbele,

"aisee upo kwenye mtihani mzito sana" Strategic aliongea kwa huruma,

"mapito tu haya" Vin alijibu na kulalia kiti cha gari.

*******************

Siku ya leo, Sajenti Minja aliamua aende moja kwa moja kwa Taita, alitaka kumuuliza kuhusu kutekwa kwake kwa maana yeye Sajenti Minja ndiye aliyepewa jukumu la kuifuatilia ile kesi, na kitu cha pili alichokuwa anaenda kukiuliza ni kuhusu kifo cha Harry, kwa sababu Harry alikuwa ni mfanyakazi wa kampuni ya Taita.

Sajenti Minja alifika nyumbani kwa Taita na kushangaa kwa namna nyumba ilivyokuwa kubwa.

Sajenti Minja akaenda getini na kumkuta mlinzi, akamsalimu na kujitambulisha huku akimuonesha mlinzi kitambulisho chake, mlinzi akaongozana na Sajenti Minja mpaka sebuleni kwa Taita na kumkuta akiwa amekaa anasoma gazeti. Sajenti Minja akamsalimu na kujitambulisha, akakaribishwa kwenye kochi.

"naona hali yako imeimarika mzee, mara ya mwisho kukuona ulikuwa chumba cha watu mahututi" Sajenti Minja aliongea huku akitabasamu,

"namshukuru Mungu, amenipigania sana" Taita aliongea huku akielekea kwenye friji na kurudi na chupa ya juisi, akampatia Sajenti Minja,

"nashukuru, je unakumbuka ni kipi kilikutokea kabla hujapoteza fahamu?" Sajenti Minja aliuliza,

"nakumbuka machache tu, nakumbuka nilitekwa na watu ambao siwajui, ila hawakutaka kunifanya chochote, walinipiga tu nikapoteza fahamu, zaidi ya hapo sikumbuki kitu" Taita aliongea, ila ulikuwa uongo mtupu,

"na baada ya kutoka hospitali hao watu hawajakusumbua tena?" Sajenti Minja aliuliza,

"hapana, sijui kwa baadae" Taita alijibu,

"Harry alikuwa mfanyakazi wako, je kifo chake familia yake sio muendelezo wa tukio lako? Jibu unavyohisi wewe" Sajenti Minja aliongea,

"siwezi kujua kwa maana walioniteka mimi hawakuniambia chochote wanachohitaji, kwa hiyo inakuwa ngumu kuhisi kitu" Taita alijibu,

"unamfahamu Sarah?" Sajenti Minja aliuliza na kipindi hicho Vin alikuwa anaingia,

"simfahamu" Taita alijibu na kumfanya Vin ashangae kidogo,

"ni nani? Kwa nini uniulize kuhusu yeye?" Taita alimuuliza Sajenti Minja,

"ni mwanamke ambaye anafanya uharifu mwingi hapa mjini, nilitaka kujua kama unamfahamu" Sajenti Minja aliongea huku akishangaa kwanini Taita anadai hamjui Sarah wakati ni mtoto wa dada yake,

"wewe ni polisi?" Vin alimuuliza Sajenti Minja,

"ndio" Sajenti Minja alijibu,

"sasa kwanini unataka kumuhusisha huyo Sarah na baba yangu?" Vin aliuliza,

"sikutaka kumuhusisha, niliuliza tu kama anamfahamu" Sajenti Minja alijibu na kipindi hicho Trigger alikuwa anaingia, Sajenti Minja alipomuona Trigger alishtuka kidogo,

"ni mwanaume mweupe mwenye michoro mwilini, ana kipara na mkononi ana mchoro wa bastola" Sauti hiyo ya mdada wa mapokezi wa hospitali ilimrudia Sajenti Minja kichwani, Sajenti Minja akamtupia jicho Trigger ambaye alikuwa anakaa kwenye kochi pembeni ya Taita,

"kwema hapa?" Trigger alisalimia baada ya kukaa,

"kwema" Sajenti Minja alijibu huku akiweka simu yake vizuri ili ampige picha Trigger bila mtu kujua, kitu kingine alikuwa anamuangalia mikononi ili aweze kuuona mchoro wa bastola, ila hakufanikiwa kwa maana Trigger alivaa shati la mikono mirefu.

"mzee nadhani nimemaliza, nitarudi siku nyingine" Sajenti Minja aliongea huku akinyanyuka na tayari alikuwa ameshafanikisha kumpiga picha Trigger,

"sawa, unaitwa nani?" Taita aliuliza,

"Joel Minja, ila ukinitafuta kwa jina la Sajenti Minja ndio utanipata kwa haraka" Sajenti Minja aliongea huku akitabasamu,

"karibu tena" Taita aliongea na kisha Sajenti Minja akaondoka zake huku akiwa na lengo la kwenda hospitali kumuonesha Daktari picha ya Trigger ili amthibitishie kuwa aliyempiga risasi ndio huyo au sio?

"anataka nini huyu?'' Trigger aliuliza baada ya Sajenti Minja kuondoka,

"unamfahamu?" Taita alimuuliza,

"hapana" Trigger alijibu,

"ni askari, anamfuatilia tukio langu la kuokotwa nikiwa sina fahamu" Taita alijibu,

"anajua chochote?" Trigger aliuliza,

"hamna anachojua" Taita alijibu na kumfanya Trigger atabasamu.

*****************

Sarah baada ya kumtoroka Sajenti Minja katika siku iliyopita, hii siku ya leo aliamka na wazo tofauti kabisa, alipanga aende hospitali ambayo Vin alifanyia vipimo vya DNA, alitaka kwenda kuchunguza ni vipi majibu ya vipimo yawe tofauti.

Sarah hakuwa na gari kutokana na gari yake moja ile Range Rover nyeusi kuiacha kwenye nyumba yake ya zamani na hakutaka kutembea nayo tena kutokana na polisi kuikariri, na gari yake ya pili ndio ile aliyoiacha kwenye nyumba nyumba yake nyingine baada ya kumkimbia Sajenti Minja.

Sarah alitoka nyumbani kwake taratibu mpaka barabarani na kuchukua bajaj iliyompeleka moja kwa moja katika hospitali ambayo Vin alifanyia vipimo vya DNA.

Sarah akamlipa dereva bajaj na kisha akatelemka na kuelekea moja kwa moja ndani ya jengo la hospitali, aliingia ndani na kuwakuta wadada wawili wakiwa eneo la mapokezi,

"karibu" Mdada mmoja muongeaji sana anayeitwa Anita alimkaribisha Sarah,

"asante, nimekuja kufanyiwa vipimo" Sarah aliongea huku akijitahidi kutabasamu,

"andika jina lako hapo, kisha nenda chumba kile kuonana na Daktari" Anita aliongea huku akimpatia Sarah daftari aandike jina lake, Sarah akachukua daftari na kuandika jina, kisha akaelekea katika chumba cha daktari.

"huyu mdada yupo kama mzungu, zile sijui ni nywele zake au amevaa wigi!?" Anita Aliongea wakati Sarah akiingia chumba cha daktari,

"na wewe nae umizidi ufukunyuku, kila mtu akipita lazima umtete kidogo" Lydia shoga yake ambaye uwa pamoja eneo hilo aliongea,

"kwa hiyo nakukera?" Anita aliuliza huku akimtazama lydia,

"ndio, wewe inaelekea hata mimi nikikupa mgongo tu unanisema" Lydia aliongea huku akijinyoosha,

"eeh!! Yamekuwa hayo tena shoga? Basi nitafunga mdomo" Anita aliongea huku akicheka,

"we endelea tu, kuna vingine vya kurithi, wenzio wanarithi mali wewe unarithi umbea" Lydia aliongea huku akiondoka na pia akicheka,

"unaenda wapi sasa?" Anita alimuuliza mwenzake,

"chooni" Lydia alijibu,

"sawa" Anita alijibu kisha akatoa kioo kwenye pochi yake na kujitazama usoni.

Sarah alielekea moja kwa moja mpaka kwenye chumba cha daktari na kumkuta mtu mama mzima akiwa amekaa, Sarah akamsalimu,

"haya dada sema una shida gani?" Daktari ambaye ndiye huyo mama mtu mzima, alimuuliza Sarah,

"nimekuja kupima ujauzito na typhoid" Sarah aliongea na kumfanya daktari atabasamu,

"unahisi dalili gani mpaka uje upime ujauzito?" Daktari aliuliza,

"kichefu chafu tu, alafu nachagua sana chakula" Sarah aliongea huku akiangalia mazingira ya kule ndani,

"jina lako?" Daktari aliuliza huku akiwa ameshikilia karatasi mkononi,

"Sarah isack" Sarah alijibu na kisha daktari akawa anaandika andika katika karatasi,
.

"itabidi upime na maralia, kwa maana hizo dalili ulizosema pia ni dalili za maralia" Daktari aliongea huku akiendelea kuandika,

"eti eeeh?" Sarah aliongea huku akimuangalia daktari,

"Shika hii karatasi, pita nayo mpaka mlango wa mwisho kushoto, utaingia humo kuchukuliwa vipimo" Daktari aliongea huku akimpatia Sarah karatasi, Sarah akatoka nje huku akiendelea kuchunguza ni mtu yupi anaweza kumdadisi na akampa taharifa nzuri juu ofisi ya daktari aliyepigwa risasi, kwa maana Sarah alipanga kuivamia hiyo ofisi na kuifanyia upekuzi, hakujua kama huyo daktari bado yupo hai.

Sarah akaingia katika chumba cha vipimo na kumkuta dada mmoja, wakasalimiana kisha Sarah amampatia yule dada ile karatasi aliyotoka nayo kwa Daktari, yule dada akaichukua na kuisoma, kisha akaanza kumchukua Sarah vipimo kulingana na maelekezo ya karatasi aliyoisoma, baada ya vipimo vyote kukamilika, yule dada alimruhusu Sarah aondoke,

"samahani, baada ya muda gani nifuate majibu?" Sarah alimuuliza yule dada,

"nusu saa tu" yule dada alijibu na kisha Sarah akatoka eneo lile, akaamua arudi kukaa eneo la mapokezi huku akiwa ameshafanya upelelezi wake wa kutosha juu ya ile hospitali na kugundua kuwa haina ulinzi wa kutosha na pia hata camera za kunakiri matukio yanayoendelea hospital hapo, hakuna.

Sarah alijivuta na kukaa kwenye viti vilovyokuwa hapo eneo la mapokezi, kulikuwa na runinga iliyokuwa ikionesha mambo mbalimbali yanayotokea duniani.

"Dada hizo ni nywele zako au umeshonea?" Anita aliuliza na kufanya Sarah ageuke na kutabasamu,

"ni zangu" Sarah alijibu huku akitabasamu,

"una nywele nzuri kweli, mpaka nimezitamani" Anita aliongea huku akitabasamu,

"ni matunzo tu" Sarah alijibu na kukaa kimya.

"nasikia eti mlivamiwa na majambazi siku za karibuni?" Sarah aliuliza huku akawageukia wale wadada wa mapokezi,

"tulivamiwa na mtu tu, sio Jambazi, alivamia chumba cha daktari na kumpiga risasi" Anita alijibu,

"khaa jamani, watu wana roho ngumu, kwa hiyo alivyompiga akamuua?" Sarah aliuliza huku akionesha kuogopeshwa na hilo tukio,

"bahati nzuri daktari hajafa, yupo hai" Anita alijibu na kumfanya Sarah ashtuke, hakutegemea kukutana na hiyo habari,

"aah bora, amepelekwa nje ya nchi kwa matibabu?" Sarah aliuliza,

"yupo hapa hapa hospitali, amelazwa" Anita alijibu,

"na wewe sio unajibu kila swali unaloulizwa, wengine wanaweza kuwa ndio wale wale majambazi wanataka kuja kummalizia" Lydia aliongea kwa sauti ndogo ambayo haikumfikia Sarah, ila aligundua kuna kitu huyo dada anamuonya mwenzake.

"na wewe hujui hata kuhisi watu, huyu dada alivyo hivi anawezaje kuwa Jambazi, kwanza mzuri hadi raha" Anita alimjibu Lydia kisha akamgeukia Sarah na kutabasamu,

"mnatakiwa muweke ulinzi wa kutosha, ipo siku wanaweza kuvamia tena na wakaleta madhara makubwa zaidi" Sarah aliongea kwa utulivu,

"sijui bwana uongozi wenyewe, nadhani wanashughulikia hilo suala" Anita alijibu na kisha ukimya ukatawala. Kipindi chote hicho cha ukimya Sarah alikuwa anafuraha ya kusikia kuwa daktari hajafa na pia alikuwa anataka kujua ni wodi ipi daktari amelazwa ili baadae aje kuongea nae vizuri,

"kuliko kuja baadae kuleta kashkash hapa, ni bora tu nimjulishe Vin kuwa daktari ni mzima" Sarah alijiwazia moyoni kwake na kipindi hicho alitakiwa aende kwa daktari kuchukua majibu yake,

"muda unakimbia, yaani nusu saa imeshafika?" Sarah aliongea huku akitabasamu baada ya kuitwa jina na kutakiwa kuingia chumba cha daktari kufuata majibu.

Baada ya dakika kumi Sarah alitoka kwenye chumba cha Daktari na kuelekezwa aende nje ya jengo ila ndani ya uzio wa geti, kuna duka la dawa, aonyeshe karatasi aliyopewa na Daktari, amuoneshe muuzaji wa duka la dawa na kisha atapatiwa dawa zake.

Sarah alifika ndani ya duka na kumuonesha muuzaji karatasi na kupatiwa dawa husika, Sarah akalipia pesa na kisha akawa anaelekea nje kutafuta usafiri wa kumrudisha kwake huku kichwani akiwa na haraka ya kufika nyumbani na kumpigia simu Vin ili amjulishe kuwa yule daktari aliyepigwa risasi, hakufa.

Wakati Sarah akiwa na haraka zake na kipindi hicho ndicho Sajenti Minja alikuwa ametoka nyumbani kwa Taita huku akija hospitali ili kumuonesha daktari picha ya Trigger ili athibitishe kuwa ndiye mtu aliyempiga risasi.

Sarah akiwa amesimama nje ya geti akisubiri bajaj, alishangaa mtu akiwa amesimama mbele yake kabisa, tena jirani na bastola ikiwa mkononi mwake usawa wa kifua cha Sarah,

"za mwizi arobaini" alikuwa ni Sajenti Minja, aliongea kwa sauti ya dharau na kumfanya Sarah apigwe na butwaa, hakutegemea kama anaweza kufanyiwa shambulio la ghafla namna ile,

"nyoosha mikono mbele" Sajenti Minja aliongea kwa amri na Sarah akatii, hakuwa na ujanja tena. Sarah akanyoosha mikono yake mbele back kisha Sajenti Minja akamfunga pingu, akamkamata mkono mpaka kwenye gari la Sajenti Minja ambalo lilikuwa ng'ambo ya barabara, akamfungulia mlango na Sarah akaingia kwenye siti ya mbele ya gari, Sajenti Minja akatoa pingu nyingine na kumfunga Sarah miguuni, kisha akatoa kamba kwenye buti na kukifunga kiwiliwili cha Sarah kwenye siti, yaani alimbana haswa, kisha Sajenti Minja akaingia kwenye gari na kumtazama Sarah, Sajenti Minja akacheka,

"bila kukufunga namna hiyo kama mbuzi kabebwa kwenye pikipiki, unaweza ukanishangaza, kwa maana wewe sio mtu wa kawaida" Sajenti Minja aliongea na kuwasha gari, Sarah alikuwa kabanwa vibaya, hata kujitingisha alikuwa hawezi.............

***********ITAENDELEA************

the Legend☆
 
RIWAYA : SALA YA SARAH

MTUNZI : ALEX KILEO

SEHEMU YA SITINI NA NNE.

ENDELEA..................

Sajenti Minja akawasha gari yake na safari ya kwenda kituoni ikaanza, njia nzima hakuna aliyemuongelesha mwenzake, Sarah alikuwa akisali msaada utokee, huku Sajenti Minja alikuwa akishangilia kwa kumkamata muharifu wake kwa urahisi namna ile,

"hivi wewe uwaga unanitafutia nini?" Sarah alimuuliza Sajenti Minja, alionekana ana hasira,

"swali gani la kipuuzi hilo unauliza wakati unajua mimi ni polisi na wewe ni muharifu" Sajenti Minja aliongea kwa dharau,

"itafika kipindi nitaanza na wewe kwa maana umekua kama kikwazo kwangu, nitakuondoa wewe kikwazo ili nifanye kazi yangu kwa uhuru" Sarah aliongea kwa hasira,

"sasa haya ni maajabu yametokea, kikwazo ndio kimekuzidi uwezo leo" Sajenti Minja aliongea na kucheka,

"sawa, huu ni mchezo, bado haujaisha, yoyote anaweza kushinda" Sarah aliongea kwa sauti ndogo ila ilimfikia kwa uzuri tu Sajenti Minja,

"mchezo eeh? Kuua watu ni mchezo?" Sajenti Minja aliongea huku akiegesha gari nje ya kituo,

"wewe ndio unaona naua, ila wao ndio wanajua ninachokifanya dhidi yao" Sarah alijibu wakati Sajenti Minja akitelemka katika gari,

"hiyo hainihusu, mimi nipo upande wa sheria tu" Sajenti Minja aliongea huku akifungua mlango wa upande wa Sarah, kisha akamfungua kamba na kisha akamfungua pingu zote, za mikononi na miguuni.

"Sidhani kama utaleta usumbufu eneo hili, mimi sio mkofofi, ila nikichokozwa uwa sio mtu mzuri kabisa" Sajenti Minja alimuonya Sarah mara baada ya kumfungua pingu, kisha akamtelesha na kumshika mkono, wakawa wanaelekea ndani ya kituo.

"twende ofisini kwangu, kuna maswali ya kujibu" Sajenti Minja aliongea huku akiwa bado amemshika mkono Sarah.

Wakaelekea moja kwa moja mpaka ofisini kwa Sajenti Minja na Sarah akawekwa kwenye kochi,

"nina maswali machache tu, Taita ni nani yako?" Sajenti Minja aliuliza,

"mjomba angu" Sarah alijibu,

"mbona yeye anadai hakujui?" Sajenti Minja na Sarah akacheka,

"inaweza kuwa sawa, kwani hajawahi kuona ndugu hawajuani?! " Sarah alihoji,

" kwanini ulimuua Harry?" Sajenti Minja aliuliza,

"Mimi? Ooh sawa ndio ni mimi niliyemuua, ila alitaka mwenyewe kufa" Sarah alijibu huku akitabasamu,

"alitaka mwenyewe kufa? alitakaje kufa?" Sajenti Minja aliuliza,

"aliyesema amechoka kuishi, hana furaha kwa maana familia yake imeuawa yote" Sarah alijibu,

"na mahakamani ukisema huo ushenzi unaweza kupona?" Sajenti Minja aliuliza huku akimshangaa Sarah,

"mahakamani? Sidhani kama naweza kufikishwa mahakamani kwa kitendo hicho" Sarah alijibu kwa kujiamini,

"kwanini uliiua familia ya Harry?" Sajenti Minja aliuliza,

"na wewe upo kama mpuuzi, nitaiuaje familia isiyo na hatia? Najua ni uchungu kiasi gani mtu anaupata anapopoteza familia, nisingeweza kuiua familia Harry" Sarah alijibu,

"sasa kama unajua ni uchungu kupoteza watu muhimu maishani, kwanini ulimuua Harry?" Sajenti Minja aliuliza,

"nilimuua baada ya familia yake kufa, hakuwa na furaha tena, alitaka akaungane na familia yake" Sarah alijibu,

"umesema wewe hujaua familia ya Harry, ni nani ameiua familia ya Harry?" Sajenti Minja aliuliza,

"Taita, Taita na vibaraka wake" Sarah alijibu na kumfanya Sajenti afikirie kidogo, kisha akaitoa simu yake na kubonyeza bonyeza,

"unamjua huyu?" Sajenti aliuliza huku akimuonesha picha ya Trigger,

"Trigger, huyu ndio kiongozi wa mauaji yanayotokea chini ya Taita" Sarah alijibu,.

"unajua kuwa huyu ndiye aliyefanya shambulio la kumuua daktari pale hospitali ulipotoka?" Sajenti Minja aliuliza,

"sijui" Sarah alijibu baada ya kuhisi hilo swali ni la mtego,

"Alafu na yule kijana mwingine anayependa kuvaa suti, ni nani kwa Taita?" Sajenti Minja aliuliza baada ya kumkumbuka Vin na maneno aliyowahi kuambiwa na mlinzi wa Harry kuwa kabla familia ya Harry haijaangamia, mtu wa mwisho kuingia alikuwa ni Trigger na huyo kijana mmoja anapenda kuvaa suti,

"yule anaitwa Vin, hata ile Vin hotel inatokana na jina lake" Sarah alijibu,

"ndiye mtoto wa Taita?" Sajenti Minja aliuliza,

"hapana, yule ni mdogo wangu" Sarah alijibu na kumfanya Sajenti Minja amtolee macho,

"mdogo wako? Au mdogo wako kwa kuwa Taita ni mjomba wako?" Sajenti Minja aliuliza na kumfanya Sarah atabasamu,

"mdogo wangu kwa maana ya kuchangia baba na mama" Sarah alijibu na sasa ikawa zamu ya Sajenti Minja kucheka,

"kivipi?" Sajenti Minja akauliza,

"kivipi, vipi? Hujaelewa nilichokueleza?" Sarah akauliza huku akimshangaa Sajenti Minja,

"iweje Vin awe ndugu yako alafu awe anakaa vyema na Taita, ingali wewe hauishi vyema na Taita?" Sajenti Minja aliuliza,

"yupo gizani yule, na siku akipata mwanga, hakutakuwa na wa kumzuia" Sarah alijibu na kumfanya Sajenti Minja abaki ndani ya Fumbo,

"nitakuuliza swali la mwisho, je ugomvi wako wewe na Taita ulitokana na kifo cha wazazi wako?" Sajenti Minja aliuliza,

"liweke vizuri swali lako hili jibu liwe jepesi, kwa maana wakati wazazi wangu wakifa nilikuwa na miaka sita tu, nisingeweza kugombana na mtu mzima" Sarah alijibu,

"Taita baada ya kuiangamiza familia yako ndipo ulipomchukia?" Sajenti Minja alimuuliza Sarah,

"hilo sio swali, ni jibu" Sarah alijibu,

"na mwisho wa yote ni nini?" Sajenti Minja alimuuliza,

"mwisho ni chini, ama yeye ama mimi" Sarah aliongea huku hasira zikionekana wazi machoni mwake,

"mwisho ni jela, tena kabla vifo havijatokea zaidi, ni lazima ufungwe sasa, ni lazima ushtakiwe Sarah" Sajenti Minja aliongea kwa sauti tulivu,

"hilo halitotokea, mkae mkijua kwamba mimi sishikiki, mimi ni moto. Kama mlishindwa kumkamata Taita na mlijua ana tuhuma, basi msitegemee kunishka mimi, hakuna atayebaki salama" Sarah aliongea kwa hasira na kumfanya Sajenti Minja acheke,

"we mpuuzi kweli, yaani upo mikononi mwa polisi alafu unaleta jeuri?" Sajenti Minja aliuliza huku akicheka,

"labda mniweke ndani ya chupa, tena chupa ya chuma" Sarah aliongea huku bado akiwa na hasira, na kipindi hicho mlango wa ofisi ya Sajenti Minja ulikuwa unagongwa,

"ingia" Sajenti Minja alijibu hodi na kutupia macho mlangoni, aliingia mwanamke aliyevaa kofia ya cap, alipoingia alifunga mlango kwa ndani, wakati Sajenti Minja akishangaa tukio hilo, yule dada aligeuka na mkononi alikuwa na bastola, kisha akaiondoa ile kofia kichwani na kubaki uso wazi, alikuwa ni Aisha,

"afande tulia hivyo hivyo, ukijitingisha sikuachi, si unakumbuka nilichomfanya mwenzako mara ya mwisho ndani ya ofisi hii?" Aisha aliuliza huku akitabasamu na kumfanya Sajenti Minja atulie kama gogo, alikumbuka tukio la Aisha alilowahi kulifanya hapo,

"na wewe unazubaa nini? Nyanyuka na umfunge huyo afande" Aisha aliongea huku akimtazama Sarah, Sarah hakuupenda ule msaada wa Aisha, aliamini unamuongezea matatizo tu, ila kwa muda huo hakuwa na la kufanya, alitaka kuwa huru.

Sarah aliinuka na kwenda kumfunga pingu Sajenti Minja, kisha Aisha akatoa bomu na kuchomoa pin na kumuwekea lile bomu mdomoni mwa Sajenti Minja, kisha akamfunga na plasta ngumu,

"sasa bomu la nini, usimuue bwana" Sarah aliongea kwa ukali huku akimtazama Aisha,

" twende, hii kwa ajili ya usalama wetu" Aisha aliongea huku akifungua mlango kisha wakatoka taratibu huku Aisha akiwaaga polisi wengine kwa furaha zaidi na kumfanya Sarah ashangae huku akijiuliza hilo tukio Aisha alipanga kulifanya kwa kushirikiana na askari wengine au?

Aisha aliongoza nje kwenye gari moja dogo jeusi na kuingia, kisha Sarah nae akaingia upande wa pili,

"kwanini sasa umemuwekea bomu?" Sarah aliuliza huku akimuangalia Aisha,

"ni bomu ndio, ila haliwezi kulipuka kwa kuwa nilishaliharibu, na bila kumfanyia hivyo huenda angepiga kelele baada ya sisi kutoka" Aisha aliongea na kumfanya Sarah ashushe pumzi,

"ulijuaje nipo hapa?" Sarah alimuuliza Aisha,

"nilishajitolea kukusaidia, popote uendapo nipo nyuma yako" Aisha aliongea,

"lakini kumbuka kuwa huu msaada unaonipa unazidi kuniharibia tu, kwa maana hapo umeniongezea kosa polisi, nimeonekana nimemtoroka askari" Sarah aliongea,

"nataka uwe huru ukamilishe kisasi chako" Aisha aliongea,

"na mbona wakati tunatoka polisi ulikuwa ukiagana vizuri na askari?" Sarah alimuuliza Aisha,

"wakati naingia nilijitambulisha ni mpenzi wa Sajenti Minja na niliongea nao kwa ucheshi kabla hawajanielekeza ilipo ofisi ya Minja" Aisha aliongea,

"nishushe hapa" Sarah aliongea na kisha Aisha akasimamisha gari na Sarah akashuka,

"nashukuru, ila nakupa onyo tena, sihitaji msaada kutoka kwako, vinginevyo na wewe utakuwa katika hatari" Sarah aliongea ila Aisha hakujibu kitu, aliondoa gari huku akiongeza sauti ya radio,

"kama ungekuwa hutaki msaada si ungeendelea kubaki polisi, kwanini ulikubali kuondoka na mimi" Aisha aliongea peke yake huku akitabasamu.

Sarah baada ya kuachia na Aisha, alichokifikiria kwa muda huo ni kumpigia simu Vin na kumpa taharifa juu ya daktari aliyepigwa risasi kuwa hajafa. Sarah akaitoa simu mfukoni na kuitafuta namba ya Vin na kupiga.

*******************

Sajenti Minja hakuwa katika hali nzuri, mikono yake ilifungwa pingu iliyoambatanishwa na kiti na mdomoni alikuwa na bomu lilipachikwa na juu ya Bomu kulikuwa na plasta ngumu iliyolizuia bomu lisitoke mdomoni kwa Sajenti Minja. Sajenti Minja hakuweza kutoa hata sauti, muda wote alikuwa kimya huku akimuomba Mungu amletee msaada na pia miale ya machozi ilikuwa ikimchomoza machoni.

Baada ya kukaa muda mrefu bila kupata msaada, Sajenti Minja aliinuka na kiti na kwenda mpaka mlangoni, kwa kuwa mlango ukifunguliwa unafungukia kwa ndani, hiyo ikawa shida shida nyingine, hakuweza kuuvuta mlango, ikabidi augonge mlango kwa kutumia kiti. Baada ya kuugonga kwa muda kidogo, wenzake wa nje walisikia, mmoja wao akaenda na kuusukuma mlango, akamkuta Sajenti Minja akiwa amefungwa kila sehemu, yule askari akakimbilia moja kwa moja kubandua plasta ya mdomoni, Sajenti Minja akakwepesha mdomo na kumuonesha kwa ishara kuwa amfungue pingu, yule askari akafungua pingu Sajenti Minja, kisha Sajenti Minja akaibandua plasta taratibu na kisha akalitoa bomu mdomoni na kutoka nalo nje kwa lengo la kwenda kulitupa baharini, ofisi yao na bahari vilikuwa jirani, baada ya yule askari mwingi kugundua Sajenti Minja amemshika bomu, ikabidi nae aanze kukimbia kutoka nje na wakati huo Sajenti Minja nae alikuwa anaanza kukimbia, tatizo mlango ulikuwa mdogo, wote wakakutaniana mlangoni na kudondoka chini, bomu likamponyoka Sajenti Minja, wakilalamika chini huku wote wakipiga kelele wakijua mwisho wao umefika, lakini wakashangaa bomu halilipuki, mwenzake akanyanyuka bila kuangalia mbele, alitaka akimbie akajikuta akilikanyaga lile bomu, akaanguka tena chini ila bomu halikulipuka, liliseleleka mpaka jirani kwa Sajenti Minja, Sajenti akalitupia jicho na kuona lile bomu lina uwazi mkubwa kwa juu, akashangaa, maana hakuna bomu la namna ile duniani, Sajenti Minja akaliokota na kuliangalia kwa karibu, akagundua ndani ya lile bomu kuna karatasi, akazitoa zote na kuziweka pembeni, bomu halikuwa na kitu, lilikuwa "empty"

Sajenti Minja akajicheka mwenyewe huku akimuangalia mwenzake ambaye alikuwa ameshapoteza fahamu muda mrefu tu mara baada ya kukanyaga bomu.

"hawa wanawake wapumbavu sana" Sajenti Minja aliongea huku akitabasamu, kisha akakumbuka kitu,

"Sarah alivyotoka hospitali alifuata nini?" Sajenti Minja alijiuliza kisha kwa haraka sana akawa anatoka nje, alipanga kwenda hospitali,

"nendeni mkamtoe mwenzenu ofisini kwangu, mlazeni nje chini ya miti" Sajenti Minja aliwaambia askari wawili waliokuwa wamesimama wakipiga soga, kisha Sajenti Minja akaenda kwenye gari yake.......................
.

*********

Vin, Taita na Trigger wakiwa sebuleni wanaongea, simu ya Vin iliita, ilikuwa karibu na Trigger, Trigger akaiokota na kumpa Vin, ila Trigger alibahatika kuona jina la mpigaji, alikuwa ni Sarah,

"vipi?'" Vin aliongea baada ya kupokea simu,

"yule daktari aliyekupima hajafa, nilienda hospitali kufanya uchunguzi" Sarah aliongea na kumfanya Vin ashtuke,

"Daktari hajafa? Yupo wapi?" Vin aliuliza,

"amelazwa pale pale" Sarah alijibu,

'pale pale?, poa ngoja niende" Vin aliongea na kukata simu, kisha akatoka kwa haraka bila kuaga mtu na kufanya Taita amtupie jicho Trigger,

"alikuwa anaongea na Sarah, nimeona jina kwenye kioo" Trigger aliongea,

"Daktari gani ambaye wanamzungumzia?" Taita aliuliza,

"hata mi sijui" Trigger alijibu

"wewe, sio yule uliyempiga risasi juzi ukaondoka na majibu?
" Taita aliuliza kwa mshangao na kumgutusha Trigger,

"ila hata Vin akienda haitomsaidia, majibu si ameyaona na hayaoneshi undugu walionao" Trigger aliongea,

Usiwe mjinga wewe, je huyo daktari akihojiwa na akikutaja wewe kwa Vin, ni picha gani Vin atapata?" Taita aliuliza kwa hasira,

"kwa hiyo?" Trigger aliuliza,

"nenda kammalize muda huu kabla hawajaongea chochote na Vin" Taita aliongea,

"Ila kweli eeh?" Trigger aliuliza na kunyanyuka kwa haraka, nae akatoka ndani kwa kasi kuwahi gari ili aende hospitali na kufika kwa haraka kabla ya Vin.

***, **************

Alitangulia Trigger kufika mapema hospitali, haikuingia ndani, akawa anazunguka nje ya jengo huku akitumia madirisha kumtafuta daktari anayemtaka na mkononi akiwa na bastola.

Vin alifika hospitali na kwenda mapokezi, akajitambulisha na kisha akauliza kama ni kweli Dokta yupo hai, akajibiwa ndio, akaomba kuongea nae kidogo, wadada wa mapokezi wakaenda kumpa ombi la Vin yule daktari, Daktari akakubali kwa maana aliona huo ndio muda muafaka wa kumpatia Vin majibu ya kweli.

Vin akaingia mpaka katika wodi aliyolazwa daktari na kumkuta akiwa amekaa, Daktari alipomuona Vin alifurahi sana, wakasalimiana,

"bora umekuja, maana nilikuwa naweza nitakupataje?" Daktari aliongea,

"nilikuja hata siku ile ulipopigwa risasi, nikakukuta haupo kwenye hali nzuri, pole sana" Vin aliongea kwa furaha,

"sasa kijana kuna mtu alifuata majibu yako, nikampatia kwa sababu alikuja kishari, ila majibu ambayo yamethibitishwa kitabibu yapo" Daktari aliongea na kumfanya Vin atoe macho,

"yapo wapi daktari?" Vin aliuliza huku akitabasamu, ila wakati daktari anataka kujibu alisita na macho akayatupia dirishani ambapo Vin aliupa mgongo upande huo wa dirisha, Vin ikambidi atake kugeuka ili aone daktari anachotaka kusema, ila kabla hajageuka alisikia mlio wa risasi na kushuhudia mwili wa Daktari ukiwa umejaa damu na ilionesha amekufa, Vin akatoa bastola yake na kugeuka upande wa dirishani kwa kasi, akamshuhudia Trigger akiipachika bastola yake kiunoni kisha akatabasamu na kutoka akikimbia. Vin akapigwa na butwaa huku bastola yake ikiwa mkononi, akaona bora atoke nje ajaribu kumfukuzia Trigger, ila Vin hata kabla hajainua mguu, mlango wa wodi ulifunguliwa na Sajenti Minja akiwa mkononi na bastola na nyuma yake walikuwa wafanyakazi wa ile hospitali,

"weka bastola chini, nyanyua mikono juu" Sajenti Minja aliongea kwa amri huku bastola yake akiwa ameelekeza usawa wa kichwa cha Vin...... Vin akanyong'onyea akatupa bastola chini, hakuwa na ujanja kwa maana alikamatwa akiwa na ushahidi wa bastola mkononi.....

***********ITAENDELEA***********

the Legend☆
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom