Riwaya: Sala ya Sarah

Riwaya: Sala ya Sarah

Heshima yenu wakuu. Ni hivi; kati ya episodes 70 za hii riwaya, episodes 5 sijafanikiwa kabisa kuzipata. Nazo ni episode ya 35, 38, 40, 43 na ya 45. Ila nyingine zote zipo.

So kitu nlichofkiria kufanya leo ni kuweka as many episodes as possible, ili iwe rahisi kwenu kuunganisha matukio na hatimae kupata mwanga wa yale yaliyojiri katika hizo episodes zilizo-miss.

Samahanini kwa usumbufu wowote utakaojitokeza

the Legend☆
 
RIWAYA : SALA YA SARAH,

MTUNZI : ALEX KILEO

SEHEMU YA THELATHINI NA SITA.

ILIPOISHIA..................

Baada ya kupishana Teja mmoja akatupa jicho nyuma, na wakati huo Sarah alikuwa a akirudisha kitambaa kwenye mfuko wa nyuma wa suruali, wakati anatoa mkono mfukoni, Sarah mkono wake ukatoka na pesa ikadondoka, ila Sarah hakuona isipokuwa kuwa Teja,

"Dada ameangusha pesa" Teja aliongea na kufanya wenzake wageuke nyuma,

"leo umekua mstaharabu, kaiokote ituokoe" Teja mwenzake aliongea,

"kaiokote umrudishie, mkitembea na mimi mnatakiwa kuwa wastaharabu" Sajenti Minja aliongea huku akisimama na kumtupia jicho yule dada ambaye alikuwa amewapa mgongo na anazidi kwenda.

Teja yule aliyeona wakati Sarah akiangusha pesa, aliiendea ile pesa na kuiokota kisha akamkimbilia Sarah, alipofika akamshika bega,

"Dada umeangusha hela" Teja aliongea na Sarah akasimama, akawa anajiandaa kugeuka huku yule kijana Teja akimsubiri na pia Sajenti Minja na yule kijana Teja mwingine walikuwa wakiangalia ...............

********ENDELEA*********

Sarah alisimama ila alisita kugeuka, hiyo sauti iliyomsimamisha aliijua vizuri, Sarah akaamua asonge mbele bila kugeuka nyuma, hata kuongea hakutaka, akamuacha yule kijana Teja akimshangaa tu. Sarah akapotea machoni kwake, yule kijana Teja akageuka na kukuta wenzake wakitabasamu,

"hiyo bahati yako, iweke mfukoni" Sajenti Minja aliongea huku akitabasamu,

"kweli ridhiki mafungu saba" Teja aliongea huku akiiweka pesa mfukoni, kisha wakaondoka mpaka nje ya wodi aliyokuwa amelazwa Taita na bahati nzuri walimkuta yule mama mtu mzima ambaye ni muuguzi,

"vipi mgonjwa anaendeleaje?" Sajenti Minja aliuliza baada ya kumsalimia,

"bado hali yake ni ile ile" Muuguzi alijibu,

"inaelekea alipigwa huyu kabla hajatupwa" Sajenti Minja aliongea,

"hivi baba, uliniambia mgonjwa ni nani yako?" Muuguzi alimuuliza Sajenti Minja,

"sina undugu nae, mimi ni askari tu nafuatilia tukio lililomkuta" Sajenti Minja aliongea huku akitabasamu,

"ooh kumbe ni askari?? sasa haya mambo ya watu kutekwa na kuokotwa naona yamepamba moto, au kuna biashara inafanyika?" Muuguzi aliongea huku Akimtazama Sajenti Minja,

"hakuna anayeyajua, inawezekana kati ya mtekwaji na mtekaji kuna namna walifanya biashara na kwa namna moja ikashindikana" Sajenti Minja alijibu huku akitabasamu,

"au kuna mtu ameingia hapa jijini na anateka tu watu hovyo?" Muuguzi alimuuliza Sajenti Minja,

"hata mimi sijui na ndio maana nafanya uchunguzi, inawezekana unayosema ni sawa, ila sisi kama polisi hatuwezi kuhisi kitu na kutangazia uma, ni lazima tuwe na uhakika na hicho kitu" Sajenti Minja aliongea huku akiona maswali ya muuguzi yanampa kero,

"unajua kwanini nakuuliza hivyo? Kuna mtu mwingine ambaye ameokotwa asubuhi hii" Muuguzi aliongea maneno yaliyomfanya Sajenti Minja ashtuke,

"ameokotwa eneo gani?" Sajenti Minja aliuliza,

"njia ya kwenda nje ya mji, alikutwa mtaroni" Muuguzi alijibu,

"ni mwanamke au mwanaume?" Sajenti Minja aliuliza,

"ni binti, ni daktari, wenzake walikuja na kudai ni daktari, na mwenzake mwingine ametoka hapa muda huu huu" Muuguzi aliongea

"aisee, nae hajakutwa na jeraha lolote mwilini?" Sajenti Minja aliuliza,

"amevunjwa miguu yote, yaani hapa kufikia mchana atakuwa kwenye chumba cha mifupa kwa ajili ya kutibiwa miguu" Muuguzi aliongea,

"yupo wodi namba ngapi?" Sajenti Minja aliendelea kuuliza,

"namba ishirini na tatu" Muuguzi alijibu na wakati huo Sajenti Minja akapiga hatua kuelekea kwenye mlango wa wodi, alipofika alisimama mlangoni na kumuangalia Dokta Pendo aliyekuwa amelala huku akiwa hana fahamu. Ila Sajenti Minja hakuweza kumtambua Dokta Pendo kutokana na mipira aliyovalishwa kwa ajili ya kumsaidia kupumua, na pia umbali ulichangia, kwa maana Sajenti Minja alisimama nje ya mlango na kumtazama Dokta Pendo kwa kupitia kioo kilichokuwepo mlangoni hapo.

"kuna polisi yoyote alikuja hapa kumuangalia zaidi yangu?" Sajenti Minja aliuliza,

"zaidi ya wale polisi waliomleta, hakuna mwingine aliyefika kumuona" Muuguzi alijibu,

"hii hatari sana, itabidi usalama uongezeke hapa, inawezekana kuna watu wabaya wanaweza kuja hapa" Sajenti Minja aliongea huku akiondoka eneo la mlango wa wodi aliyolazwa Dokta Pendo.

.
"suala la usalama linazingatiwa na ndio maana mimi nipo hapa" Muuguzi aliongea,

"kuna mtu yoyote alikuja kumuona huyu mzee?" Sajenti Minja aliuliza huku akinyooshea kidole katika Chumba cha wodi alicholazwa Taita.

"watu wengi wanakuja kumuona, tena mpaka viongozi wa serikali" Muuguzi aliongea,

"ni mtu mzito sana huyo" Sajenti Minja aliongea,

"ni nani?" Teja mmoja aliuliza,

"usikute tumemsaidia waziri mwanangu" Teja mwingine aliongea na kufanya Sajenti Minja na Muuguzi wacheke,

"twendeni bwana, mmeshaanza kelele zenu" Sajenti Minja aliongea huku akiondoka na kufanya wale vijana mateja wamfuate kwa nyuma na wakaondoka zao eneo lile la hospitali.

*********, ***

Sarah alivyotoka pale hospitali alielekea moja kwa moja kwenye gari lake na kuliondoa kwa kasi huku akiwaza wale mateja wamefuata nini pale hospitali?

"au wameitwa kunipeleleza? ila kama wamekuja kunipeleleza mbona hawatanifanya kitu baada ya kuniona? au hawajanijua?" Sarah alikuwa akijiuliza maswali na kujijibu mwenyewe,

"haya sasa kama hawajaja kunichunguza watakuwa wamefuata nini pale? lile eneo la wagonjwa mahututi uwa panahitajika usalama wa kutosha, sasa watu kama wale wamefuata nini pale? au Taita aliokotwa amelazwa pale?" Sarah aliendelea kuwaza huku akiwa anaendesha gari.

"sasa kama Taita atakuwa amepatikana akiwa hai itakuwaje sasa, nmefanya uzembe mkubwa kumuachia, ningejua ningefanya mabadilishano, ningewapa Taita na wao wangenipa babu yangu, sasa kwa hali ilivyo sasa siioni kama babu yangu atakuwa hai, ila kama angekuwa amekufa si wangemtupa kama Dokta Pendo, wangemtupa na watu wangemuokota. Nina imani babu yangu yupo hai ila sijajua suala la usalama wake wa mwili, isije kuwa wamemfanya kama Dokta Pendo" Sarah aliendelea kutafakari huku akijilaumu kwa mambo kadhaa,

"Dokta Pendo utapona shoga yangu, usijali utaishi kwa amani tu, hawa watu nitawamaliza mwenyewe, ahadi ya kisasi Lazima itimie, kisha na historia iandikwe na jina langu likumbukwe na vizazi" Sarah aliongea peke yake huku akaisimamisha gari nje ya geti lake, kisha akashuka na kufungua geti, akaingiza gari ndani ya geti.

************

Baada ya siku mbili, Nyakati za kumi jioni, Harry alikuwa uwanja wa ndege akionekana kumsubiri mtu. Baada ya dakika kumi mlango wa kutokea wageni ulifunguliwa, akatoka kijana mwenye umbo la wastani na pia ni mrefu wa futi sita na inchi 3, mgongoni alibeba begi la kijani na mkononi alikuwa na begi kubwa kiasi, alivaa suruali ya kitambaa nyeusi na shati la rangi ya bluu alilolichomekea vyema kwenye suruali yake hiyo, na chini alivaa viatu vyeusi, vinaitwa moka.

Harry alipomuona alimkimbilia na kumlaki kwa bashasha, yule kijana alijitahidi kutabasamu ila kiukwelie sura yake ilionesha hakuwa na furaha hata kidogo,

"Za safari Vin?" Harry alimsalimu,

"njema, za maisha?" Vin alijibu huku akiangaza angaza mazingira yaliyomzunguka,

"tunamshukuru Mungu, vipi umeshakula?" Harry aliuliza,

"hayo masuala ya kula yatafuata baadae, twende hospitali nikamuone baba" Vin aliongea,

"sawa bosi, twende kwenye gari" Harry aliongea huku akichukua begi mikononi mwa Vin na kushika njia iliyompeleka mpaka alipoegesha gari lake, akamfungulia mlango Vin, kisha Vin akaingia na yeye Harry akaenda upande wa dereva na kuingia, akawasha gari na kuliondoa kwa mwendo mdogo,

"Harry ujue kuna kitu unanificha, Baba yangu kwa ulinzi wake alionao alitekwaje, ni mtu gani alimteka?" Vin aliuliza huku macho yakiwa mbele,

"subiri mwenyewe ahamke, atakusimulia tu" Harry alijibu huku akijichekesha,

"na asipohamka ni nani atanielezea?" Vin alihoji huku akionekana mwenye hasira,

"usiseme hivyo, tuombe tu ahamke" Harry aliongea,

"iko hivi Harry, Baba asipohamka ni wewe ambaye utanieleza haya mambo, kwa hiyo sioni sababu ya kunificha sasa hivi, niambie tu" Vin alimshawishi Harry,

"sawa boss, ni hivi, hizi siku za karibuni baba yako pamoja na sisi ambao tupo chini yake tulipoteza kujiamini kabisa baada ya kuibuka mtu ambaye alikuwa akitufuatilia, mara ya kwanza hatukumchukulia kwa uzito mkubwa, ila alikuja kutuletea athari kubwa sana, aliua wenzetu si chini ya wawili, ameteketeza magari ya baba yako si chini ya mawili na ameshawahi kulipua geti la nyumba ya baba yako" Harry aliongea na kumfanya Vin amgeukie ili kumsikiliza vizuri,

"huyo mtu ana madai yoyote labda kutoka kwa baba?" Vin aliuliza,

"hakuna anayejua" Harry alijibu,

"hakuna anaejua vipi sasa? Wewe ukikaa na baba hamjawahi kulijadili hilo jambo?" Vin aliuliza kwa kufoka baada ya kuhisi Harry anataka kumchezea akili,

"ningekua najua ningekwambia tu, kwanini nikufiche mwanangu?" Harry aliongea kwa sauti ya upole,

"na anawauaje wenzenu, anawateka au anatumia nini?" Vin aliendelea kuuliza,

"aisee amejipanga, anatumia akili nyingi sana, pia ana mitambo ambayo anaweza kujua mtu alipo na akamfuatilia, pia ana simu ambayo anaweza kukupigia ila wewe ukimpigia inaonesha hiyo namba haipo na wala haikuwahi kutumika duniani" Harry aliendelea kutoa maelezo,

"Alafu ana nini kingine cha ziada tofauti na hivyo ulivyovitaja?" Vin alihoji,

"kingine ni mwanamke, tena sio mwanamke, ni kasichana tu kalichokuzidi miaka miwili" Harry aliongea huku macho yakiwa makini na barabara,

"msichana? inaelekea unamjua vizuri, mpaka umri wake umeujua?" Vin aliuliza huku akishangaa,

"ni huyo msichana mwenyewe uwa anajiweka wazi pindi anapokuja kutushambulia" Harry aliongea huku akiingiza gari yake eneo la hospitali,

"nadhani huyo msichana anastahili kufa, hawezi kumnyima raha baba yangu kiasi hiki na isitoshe tayari amemuweka katika hali mbaya kiafya" Vin aliongea huku akishuka katika gari,

"ngoja nitangulie kuingia ili kama nikikuta watu niwaondoe" Harry aliongea huku akipiga hatua za haraka haraka kuingia ndani ya eneo la hospital, na kumuacha Vin akielekea kwenye duka moja liliopo ndani ya uzio wa hospitali na kununua maji ya kunywa, kisha kwa mwendo wa taratibu Vin akawa anaelekea ndani ya jengo la hospitali huku akiwa anajaribu kujenga picha namna hali ya baba yake iliyokuwa.

Wakati Vin akiwa anaingia ndani ya eneo la hospital huku akiwa ana uchungu mkubwa juu ya hali ya baba yake na pia akiwa na hasira na msichana ambaye ameambiwa ndio aliyemtendea ubaya baba yake, ndio wakati huo huo msichana huyo ambaye ni Sarah alikuwa akitoka nje ya hospitali huku akiwa na uchungu mkuu dhidi ya Taita na watu wake baada kumfanyia ubaya Dokta Pendo ambaye mpaka leo bado hujapata fahamu.

Vin aliendelea kupiga hatua huku macho yakiwa mbele na wakati huo Sarah nae ndani ya baibui kubwa jeusi alikuwa akipiga hatua za haraka haraka za kutoka nje.

Na sasa walikuwa wanaelekeana, Vin alikuwa mbele ya Sarah na Sarah alikuwa mbele ya Vin, walikuwa wamebakiza hatua kumi tu kufikiana.

Zikiwa zimebaki hatua tano ili wafikiane, Vin akanyanyua uso wake na kumuangalia Sarah, ghafla tu mapigo ya moyo wake yakabadilika na kuanza kwenda mbio huku moyoni hali fulani ya mshtuko ikimtawala, wakati Vin hali hiyo ikimtazama, kwa upande wa Sarah alihisi kama huyo kijana akimuangalia na yeye ikabidi amtupie jicho, hapo sasa nae Sarah ikamkuta hali ile ile, tena mbaya zaidi mpaka machozi yakawa yanataka kumtoka ila alijizuia huku akishangaa kwanini akutane na hali kama ile?

Walisogeleana mpaka wakawa wanakaribia kupishana, walipopisha Sarah akapiga hatua moja akasimama, Vin nae akahisi yule dada waliyekuwa wakiangaliana amesimama, Vin akasimama huku wakiwa wamepeana migongo na kila mmoja akishangaa ni kwanini hiyo hali imetokea?

Wakiwa bado wamesimama huku wamepeana migongo, ndipo Harry alitokea kwa mbele ya Vin, nyuma ya Sarah. Alikuwa mbali kidogo, ila alipotokea na kuona hilo tukio alisimama ghafla na kutazama, kisha akaamua aanze kusogea jirani na Vin na kipindi anasogea, Sarah hakuwa na habari na hilo, yaani hakuwa akijua kama Harry anajongea eneo lile, Sarah aliendelea kusimama tu huku akijishangaa ile hali iliyomkuta...................

********ITAENDELEA***********

the Legend☆
 
RIWAYA : SALA YA SARAH

MTUNZI : ALEX KILEO

SEHEMU YA THELATHINI NA SABA.

ILIPOISHIA...........

Zikiwa zimebaki hatua tano ili wafikiane, Vin akanyanyua uso wake na kumuangalia Sarah, ghafla tu mapigo ya moyo wake yakabadilika na kuanza kwenda mbio huku moyoni hali fulani ya mshtuko ikimtawala, wakati Vin hali hiyo ikimtazama, kwa upande wa Sarah alihisi kama huyo kijana akimuangalia na yeye ikabidi amtupie jicho, hapo sasa nae Sarah ikamkuta hali ile ile, tena mbaya zaidi mpaka machozi yakawa yanataka kumtoka ila alijizuia huku akishangaa kwanini akutane na hali kama ile?

Walisogeleana mpaka wakawa wanakaribia kupishana, walipopisha Sarah akapiga hatua moja akasimama, Vin nae akahisi yule dada waliyekuwa wakiangaliana amesimama, Vin akasimama huku wakiwa wamepeana migongo na kila mmoja akishangaa ni kwanini hiyo hali imetokea?

Wakiwa bado wamesimama huku wamepeana migongo, ndipo Harry alitokea kwa mbele ya Vin, nyuma ya Sarah. Alikuwa mbali kidogo, ila alipotokea na kuona hilo tukio alisimama ghafla na kutazama, kisha akaamua aanze kusogea jirani na Vin na kipindi anasogea, Sarah hakuwa na habari na hilo, yaani hakuwa akijua kama Harry anajongea eneo lile, Sarah aliendelea kusimama tu huku akijishangaa ile hali iliyomkuta...................

***********ENDELEA***********

Wakati Vin na Sarah wakiwa wamesimama huku wote wakiwa kimya na hakuna aliyekuwa anamuangalia mwenzake, na kipindi hicho Harry nae aliongeza mwendo ili kufika eneo la tukio.

Sarah akaanza kupiga hatua za haraka kuelekea nje, alitembea mpaka katika gari yake na kuingia,

"kwanini moyo wangu umekuwa na hisia nzito juu ya yule kijana?" Sarah alijiuliza huku akiiondoa gari yake kutoka nje ya geti la hospitali na kujaribu kupuuza hisia zisizoeleweka juu ya kijana yule, kitu ambacho hakukijua ni kuwa yule kijana ndiye mdogo wake ambaye hakuwahi kujua ni wapi alipo.

Sarah alielekea moja kwa moja mpaka eneo moja katikati ya mji na kwenda kusimamisha gari yake mbele ya kijiwe kimoja ambacho kilikuwa na watu wa rika mbalimbali wakicheza michezo tofauti kama bao, drafti, na karata, aliposimamisha gari akaangaza macho na kumuona mtu aliyekuwa alimuhitaji, Sarah akapiga honi kisha watu wengi wakageuka kumuangalia mpiga honi, wengi wao baada ya kumuangalia Sarah walirudisha macho yao mbele kuendelea na kazi zao, isipokuwa yule kijana muhusika alipogeuka na kumuona Sarah, aliweka karata chini na kukimbilia kwenye gari la Sarah, alipofika aliingia ndani ya gari,

"sema bosi?" kijana aliongea,

"poa, ndio nimekuja tukaione hiyo nyumba" Sarah aliongea,

"sawa twende" kijana aliongea kisha Sarah akaondoa gari kuelekea kwenda kwenye hiyo nyumba.

"unataka ukaishi wewe?" kijana alimuuliza Sarah,

"kuna babu yangu nataka akaishi uko" Sarah alijibu,

"kwa sasa anaishi wapi?" Kijana ambaye alikuwa ni dalali aliuliza,

"yupo tu, tunaishi nae" Sarah alidanganya,

"ila dada kule ulipopachagua ni mbali, ni nje ya mji kabisa" Kijana aliongea,

"panamfaa kule, maana ni mzee na isitoshe gharama za ndogo za ununuzi wa hiyo nyumba" Sarah aliongea,

"kwa hizo sababu ni sawa. Mzee ataishi peke yake au yupo na mkewe?" Kijana aliuliza, huyu kijana alikuwa na maneno mengi sana,

"yupo kundi kubwa tu la kuishi nalo, ana timu ya mpira" Sarah alijibu na kuwafanya wote wacheke na kipindi hicho gari ilikuwa inasimama nje ya nyumba moja ambayo ilikuwa na uzio bila geti, ila nyumba ilikuwa imekamilika yote, ilikuwa haijapakwa rangi tu.

Sarah baada ya kutelemka katika gari, alianza kuikagua ile nyumba, alianza kwa kuizunguka eneo la nje, baada ya kuridhika akaingia ndani na kuanza kuzungukia kila chumba, baada ya kujiridhisha walitoka mpaka eneo la nje,

"ndio ulisema inauzwa shilingi ngapi?" Sarah alimuuliza kijana dalali,

"anataka million themanini na moja" Dalali alijibu,

"hivi ukiniangalia unaniona nimekaa kitajiri eee? au mgeni sana wa jiji?" Sarah alimuuliza dalali huku akitabasamu,

"kwanini unasema hivyo boss?" Dalali aliuliza,

"hii nyumba sio ya million themanini, mimi nitatoa hamsini, kama haiwezekani ni basi, maana ndiyo iliyopo" Sarah aliongea huku akikaa juu ya tofali lililokuwepo hapo,

"bosi uko unanyonga sana, OK, fanya Sabini na tano" Dalali aliongea,

"Mimi nadhani huanielewa, mimi ninayo hamsini tu. Kama haiwezekani basi biashara ife" Sarah aliongea kwa nyodo huku akimtazama,

"basi kusema kweli kabisa, hii nyumba ni million sitini, zaidi ya hapo haishuki" Dalali aliongea kiunyonge na kumfanya Sarah amcheke,

"hiyo ndiyo bei halali sasa, sasa nitakupa sitini na moja" Sarah aliongea na kumfanya dalali ashangae mwenyewe huku akicheka,

"mbona hueleweki bosi, nikipunguza bei, wewe unaongeza" Dalali aliongea,

"nadhani tangu mwanzo ungeanza na hiyo bei, ungenielewa" Sarah aliongea huku akitabasamu,

"sawa bwana, sasa kuhusu suala la malipo ni mpaka kesho nitakapokukutanisha na mwenye nyumba, muda gani utakuwa free?" Dalali alimuuliza Sarah,

"nitakupigia simu jioni" Sarah alijibu huku akielekea kwenye gari lake,

"sawa bosi, nakuaminia" Dalali aliongea huku nae akielekea kupanda katika gari ya Sarah.

**********************

Vin aliendelea kusimama pale pale, alisikia wakati Sarah akiondoka ila hakutaka kumuangalia, aliendelea kuganda vile vile mpaka Harry alipomfikia,

"mbona hivyo, yule msichana uliyesimama nae unamjua?" Harry alimuuliza Vin,

"Hapana, ni nani?" Vin aliuliza,

"Mimi sijui ndio maana nimekuuliza wswe" Harry aliongea ukweli kwa maana hakumuona kweli Sarah,

"twende, achana nae" Vin aliongea huku akianza kupiga hatua,.

"labda ni malaya tu anataka kukurubuni" Harry aliongea huku nae akimfuata Vin,

"ataniweza sasa? mimi ni mtu ninaejielewa" Vin alijibu huku moyoni akiwa anashangaa ni kwanini moyoni amekuwa mzito baada ya kumuona yule msichana, tena msichana mwenyewe ndio amemuona kwa mara ya kwanza.

"nakuaminia mzee, uko marekani kuna warembo zaidi ya hapa" Harry aliongea huku akijichekesha mbele ya Vin,

"kwetu wanawake ni warembo zaidi" Vin aliongea huku wakiwa wameifikia wodi namba ishirini na moja ambayo ndiyo alikuwa amelazwa Taita. Vin akataka aingie moja kwa moja ndani ya wodi ila yule mama mtu mzima ambaye ni muuguzi, alimzuia,

"haruhusiwi mtu kuingia ilipokuwa Dokta tu" Muuguzi aliongea huku akimshika bega Vin, Vin akasimama huku akimuangalia kwa mbali baba yake, baada ya dakika moja machozi yalikuwa yakitiririka kwenye mashavu ya Vin, alimpenda sana baba yake huyo, na hapo alikuwa akilia huku akimuomba Mungu ampe uhai zaidi baba yake,

"jikaze, atapona tu" Muuguzi aliongea huku akiwa amesimama nyuma ya Vin, Vin akageuka na kumuangalia Muuguzi,

"atapona? wewe unaijua mipango ya Mungu?" Vin alimuuliza Muuguzi huku akiwa na hasira,

"tulia Vin, twende ukapumzike, utarudi baadae" Harry aliongea kinyenyekevu mbele ya Vin na kipindi hicho Muuguzi alikuwa ameogopa na alikaa mbali kabisa,

"sipendagi mtu aongee vitu ambavyo havijui" Vin aliongea huku akianza kuondoka na Harry alikuwa nyuma yake,

"mama tusamehe, endelea kuangalia usalama" Harry aligeuka na kumwambia Muuguzi na kisha akaendelea kusonga mbele kumfuata Vin.

*************************

Baada ya wiki, Dokta Pendo alikuwa amezinduka na alijikuta ana bandeji ngumu kwenye miguu yake yote miwili na wodi alikuwa amehamishwa, alihamishiwa kwenye wodi za kawaida.

Sajenti Minja alifika hospitali pale na kuelekea moja kwa moja kwenye wodi za watu mahututi na kumuona Taita, kisha yule mama Muuguzi akampa taharifa za kuhamishwa kwa Dokta Pendo, Sajenti Minja akaulizia ni wapi alipohamishiwa, akaelekezwa na kwenda moja kwa moja kwenye hiyo wodi, haukuwa muda wa kuangalia wagonjwa ila alijitambulisha yeye ni askari na ameenda pale kikazi, akaruhusiwa kuingia.

Alipoingia na kumuona mgonjwa mwenyewe ilibidi ashangae kwa maana anamfahamu,

"Pendo, vipi?" Sajenti Minja aliongea huku akikaa pembezoni mwa kitanda,

"salama kiasi, karibu" Dokta Pendo aliongea kwa tabu huku miguu yake ikiwa imetundikwa juu,

"nini tatizo tena?" Sajenti Minja aliuliza,

.

"nilitekwa ndugu yangu, kwanza kujikuta mzima hivi nimeshangaa, mi nilikuwa mtu wa kufa" Dokta Pendo aliongea,

"walikuteka unawajua? au sababu za kukuteka unazifahamu?" Sajenti Minja aliuliza,

"kuwajua nawajua kwa sura, ila sababu ya kuniteka ni yule mwanamke uliyekuwa unamfuatilia na niliyekuja kutoa taharifa kuwa aliniteka hawali" Dokta Pendo aliongea,

"kwanini wakuteke wewe na sio yeye?" Sajenti Minja aliuliza,

"waliniteka mimi wakitaka iwe njia ya kumpata yeye, waliamini tuna urafiki na mawasiliano" Dokta Pendo aliongea,

"na ulisikia wakiongea kitu chochote kumuhusu huyo dada?" Sajenti Minja aliuliza,

"waliongea vingi tu ikiwemo kuwa wakimpata lazima wamuue" Dokta Pendo aliongea,

"na huyo dada unavyomjua wewe ni kweli ni mtu mbaya?" Sajenti Minja aliuliza,

"ni mtu mbaya, wewe mwenyewe si ameshawahi kukushambulia? Kwanza namchukia kwa maana yeye ndio amenisababishia mambo yote haya, ameniharibia maisha na sasa siwezi kufanya kazi na nina watu wananitegemea" Dokta Pendo aliongea kwa uchungu huku machozi yakimtoka,

"pole, na tangu muda umehamishiwa hapa, huyo dada amekuja kukuona?" Sajenti Minja aliuliza,

"sitaki hata aje, ni shetani kama inawezekana nipe hata bastola ili akija nimmalizie mbali" Dokta Pendo aliongea kwa chuki huku akiwa bado analia,

"pole sana Dokta, ilo suala lako ngoja nilifuatilie mimi kwa ukaribu zaidi" Sajenti Minja aliongea huku akimfuta machozi Dokta Pendo,

"yaani kila sura yake ikija kichwani kwangu napata maumivu, yaani ameniharibia maisha mbwa huyu" Dokta Pendo aliendelea kulalamika kwa kilio cha kwikwi,

"usijali Dokta, mchana huu unataka ule nini?" Sajenti Minja alimuuliza,

.
. "saa ngapi kwani?" Dokta Pendo aliuliza huku akifuta machozi,

"saa saba na nusu" Sajenti Minja alijibu,

"muda wa kuona wagonjwa umefika, sasa hivi naletewa chakula kwa hiyo usisumbuke kutumia pesa yako" Dokta Pendo aliongea na muda huo mlango wa wodi ulifunguliwa na akaingia yule mama Muuguzi,

"nimekuletea mgeni" Muuguzi aliongea huku akitabasamu na nyuma yake akaingia Sarah huku akiwa na tabasamu pana usoni mwake ila Dokta Pendo alihamaki na sura yake ikaonesha hasira zaidi........

**********ITAENDELEA************

the Legend☆
 
RIWAYA : SALA YA SARAH

MTUNZI : ALEX KILEO

SEHEMU YA THELATHINI NA TISA.

ILIPOISHIA...........................

"sawa, acha mimi nitangulie" Vin aliongea na kisha akaelekea ndani ya jengo la hospitali na kujaribu kumuacha Trigger akiwa amesimama pale nje, kitu kilichomfanya Trigger asiingie hospitali haikuwa ni sigara, ilikuwa ni ile Range Rover nyeusi iliyokuwa imeegeshwa nje ya jengo la hospitali, aliifananisha na gari ya Sarah ingawa hakuwa na uhakika nayo, ila aliamini itakuwa ni yenyewe kabisa,

"huyu malaya kama ni kweli ni yeye, atakuwa amefuata nini huku? Au ameshajua Taita yupo hapa na amekuja kummaliza?" Trigger alikuwa akijiuliza kisha akapiga hatua za haraka haraka kuelekea kwenye mlango wa lile jengo ambao ulikuwa ni wa kioo, ila kabla hajausukuma aliweza kumuona Sarah kupitia kioo, Sarah nae alikuwa anatoka ndani na kuja kwenye ule mlango wa jengo, ina maana Sarah alikuwa akaelekea nje.

Trigger ilimbidi atoke mbio mpaka kwenye gari la Sarah, na kisha akakitoa kidude fulani mfukoni na kukiweka kwenye kitasa cha gari, lock zikaachia, Trigger akafungua mlango na kuingia siti za nyuma, akalala nyuma ya siti.

Sarah akiwa hana hili wala lile, aliweza kutoka nje ya jengo la hospitali, alipolikaribia gari lake akatoa funguo na kobonyeza kisha gari ikapiga alarm ndogo za kutoa lock, Sarah akafungua mlango na kuingia, akatazama simu yake na kisha akaiweka siti ya pembeni yake, Sarah akawasha gari na kuiondoa usiku huo huku akiwa hajui kama Trigger yupo siti ya nyuma yake...................

********ENDELEA********

Sarah aliendelea kuendesha gari huku akiwa hana habari kabisa kama kuna mtu siti ya nyuma, na wakati huo Trigger hakuwa na haraka ya kumdhuru Sarah, alichotaka ni kupajua nyumbani kwa Sarah na ikiwezekana Kama ni kumdhuru, basi amdhuru uko uko.

Wakati Sarah akiendelea kuendesha gari, alisimamisha gari ghafla, Trigger akashuka ila hakutaka kufanya papara, Sarah k akakunja kushoto na kuegesha gari nje ya mgahawa, akatelemka na kuingia ndani ya mgahawa, tena akachagua kiti kilichopo dirishani ili aiangalie gari yake,

"karibu dada, nikuhudumie nini?" Muhudumu alifika na kuuliza,

"ngoja kidogo, nitakuita" Sarah alijibu huku akiitoa simu yake mfukoni, akaibonyeza sehemu yenye majina na kuchagua jina alilonakiri kwa jina "AFANDE" akapiga, ilikuwa ni namba ya Sajenti Minja,

"hallow afande, upo wapi?" Sarah aliuliza baada ya simu kupokelewa,

"naelekea hospital, wewe upo wapi?" Sajenti Minja aliuliza,

"nipo overview restaurant, nina tatizo afande" Sarah aliongea huku macho yakiwa kwenye gari lake,

"tatizo gani tena mrembo?" Sajenti Minja aliuliza kwa shahuku ya kutaka kujua,

"ndani ya gari langu kuna mtu, nahisi aliingia kipindi mimi nipo wodini" Sarah aliongea na kusubiri,

"amejua kama umejua uwepo wake ndani ya gari?" Sajenti Minja aliuliza,

"bado hajajua" Sarah alijibu,

"nakuja hapo overview, jitahidi asijue kama umejua" Sajenti Minja aliongea,

"poa, fanya fasta" Sarah alijibu na kukata simu, kisha akaangaza macho na kumuita muhudumu wa mgahawa,

"niletee sambusa mbili na juisi" Sarah aliagiza kisha akainuka na kuelekea sehemu ya kusafishia mikono, baada ya muda mfupi alirudi na kukuta alichokiagiza kipo mezani, Sarah akaanza kula huku macho yake yakiwa kwenye gari lake, baada ya dakika tano, Sarah aliweza kuiona gari ya Sajenti Minja ikiegeshwa pembeni ya gari yake, Sarah akainuka kwenye kiti na kumuita muhudumu, kisha akampatia malipo yake na Sarah akatoka nje haraka haraka kumuwahi Sajenti Minja,

"yupo wapi" Sajenti Minja aliuliza huku akimtazama Sarah,

"mlango wa nyuma" Sarah alijibu,

"toa lock" Sajenti Minja aliongea huku akiitoa bastola yake. Sarah akatoa lock kwa kutumia remote ndogo iliyoambatanishwa na funguo ya gari.

Sajenti Minja kwa umakini mkubwa alifungua mlango wa gari na kunyooshea bastola, lakini hakukuta mtu,

"mbona hakuna mtu?" Sajenti Minja aliuliza na kumfanya Sarah ashtuke,

"atakuwa ameshakimbia, itakuwa alishtukia mchezo" Sarah alijibu,

"kweli maana naona mchana wa nyayo za viatu hapo kwenye siti. Aliingiaje na ametokaje?" Sajenti Minja aliuliza,

"Mimi sijui bwana" Sarah alijibu,

"ila nadhani atakuwa maeneo haya haya anakufuatilia" Sajenti Minja aliongea,

"inawezekana" Sarah alijibu,

"uligunduaje kuna mtu ndani?" Sajenti Minja aliuliza,

"nilisikia harufu ya perfume na pia nilihisi kuna kitu kama kinagusa gusa siti" Sarah alijibu,

"sasa ni bora nikusindikize nyumbani kwa ajili ya usalama" Sajenti alimwambia Sarah,

"Acha tu, nitafika" Sarah alijibu,

"hapana, panda kwenye gari mimi nitakuja kwa nyuma" Sajenti Minja aliongea,

"yes sir" Sarah alijibu huku akipiga saluti na pia akicheka,

"mjinga kweli wewe, unafurahi huku una matatizo" Sajenti Minja aliongea huku akicheka,

"sio tatizo hilo, kwangu ni kitatizo tu" Sarah aliongea huku akiingia kwenye gari lake,

"kingekuwa kitatizo usingeniita" Sajenti Minja aliongea huku akiwa bado anacheka,

"twende bwana, acha maneno yako" Sarah aliongea huku akiwasha gari yake na kipindi hicho Sajenti Minja alikuwa akielekea kwenye gari yake.

Sarah baada ya kuwasha gari yake, akakitoa kifua kidogo na kugeukia siti ya nyuma na kuanza kukagua kwa kutumia hicho kifaa, alikuwa anaangalia hali ya usalama, baada ya kujiridhisha aliondoa gari na huku nyuma akifuatwa na Sajenti Minja.

Iliwachukua dakika kumi kufika nyumbani kwa Sarah, Sarah akafungua geti na kuingiza gari yake, Sajenti Minja yeye gari aliiweka nje ya geti.

"karibu afande" Sarah aliongea huku akifungua mlango na kisha Sajenti Minja akaingia na kuksribushwa na mandhari nzuri ya sebule ya Sarah,

"asante sana, ni pazuri sana" Sajenti Minja aliongea,

"unatumia kinywaji gani?" Sarah alimuuliza,

"bia" Sajenti Minja alijibu huku akikaa kwenye kochi,

"bia hamna, kama unataka pombe kuna whusky" Sarah aliongea huku akitabasamu,

"basi nipe chochote ila sio pombe" Sajenti Minja aliongea kisha Sarah akamletea juisi tu.

"unaishi na nani hapa?" Sajenti Minja aliuliza,

"mwenyewe tu" Sarah alijibu huku akijitupa kwenye kochi,

"unaishiji mwenyewe kwenye kubwa hivi, huogopi?" Sajenti Minja aliuliza,

"niogope nini sasa?" Sarah aliuliza,

"inatakiwa ukae na mwenzako, au amesafiri unanidanganya tu?" Sajenti Minja aliuliza,

"naishi peke yangu bwana, mbona maswali mengi afande?" Sarah aliuliza huku akitabasamu,

"huwezi jua, labda nataka uwe mke wa afande" Sajenti Minja aliongea na kufanya wacheke,

"suala la kuolewa kwa muda huu sifikirii, maana kuolewa ni kuwa mtumwa wa ndoa, nitashindwa kukamilisha ndoto zangu" Sarah aliongea huku akitabasamu,

"ndoto gani uliyoibakiza? maana maisha mazuri tayari unayo" Sajenti Minja aliuliza,

"ndoto si kuwa na maisha mazuri tu, ndoto ni kukamilisha kile ulichopanga kukifanya kipindi upo mtoto" Sarah alijibu,

"kwa hiyo wewe ndoto yako ni nini?"Sajenti Minja aliuliza,.

"ninayo tu moyoni mwangu, nikiikamilisha nitakwambia" Sarah alijibu,

"sawa mama, acha nirudi hospitali, ila kuwa muangalifu na usalama wako" Sajenti Minja aliongea huku akisimama,

"mbona unaondoka hata juisi haijaisha?" Sarah aliuliza kwa mshangao,

"utamalizia wewe mke wa afande" Sajenti Minja aliongea huku akicheka,

"sawa bwana, mimi hata sikutoi" Sarah aliongea,

"geti nani atafunga?" Sajenti Minja aliuliza,

"rudishia tu" Sarah alijibu na kisha Sajenti Minja akaondoka zake.

Sarah akabaki sebuleni peke yake huku akitafakari ni nani yule aliyeingia kwenye gari yake.

"atakuwa ameingia pale pale hospitali, na walikuwa wananifuatilia, haiwezekani wajue nipo pale, sasa kama watakuwa wamejua pale ninaenda kwa ajili ya kumuona Dokta Pendo, basi hali ya Dokta Pendo itakuwa matatani sana" Sarah aliongea huku akielekea nje kufunga geti.

****************

Trigger wakati yupo, kwenye gari la Sarah, alipata wasiwasi baada ya kumuona Sarah akiongea ndani ya mgahawa na Sajenti simu, wasiwasi uliongezeka zaidi baada ya kumuona Sajenti Minja, maana alikuwa anamjua. Alichofanya Trigger ni kuchomoka kwenye gari na kuondoka zake. Safari yake iliishia hospitali, alipofika alimkuta Harry, ikabidi amtoe nje wakaongee,

"Sarah ametoka hapa muda si mrefu" Trigger aliongea huku akimtazama Harry,

"amefuata nini hapa?" Harry aliuliza,

"Labda bado anamfuatilia Taita, anataka ammalize" Trigger alijibu,

"huenda, ebu imarisheni ulinzi kote, ikiwezekana ongeza vijana wawe eneo la nje ya hospitali" Harry aliongea,

"sawa mkuu, je tumshirikishe Vin juu ya Sarah kuonekana hapa?" Trigger aliuliza,

"hilo suala niachie mimi" Harry alijibu,

"sawa, acha mimi nizunguke zunguke eneo hili la hospitali kuangalia usalama zaidi" Trigger aliongea,

"sawa" Harry alijibu huku akiondoka zake na kumuacha Trigger nae akigeuka na kuondoka zake.

Trigger aliamua kuzunguka tu ndani ya hospitali, hiyo ziara ya ghafla aliita ziara ya kukagua usalama. Wakati Trigger akiwa anapita maeneo tofauti ndani ya hospitali, ndipo alipopita katika wodi moja iliyompa mshtuko, hiyo wodi ndipo aliyolazwa Dokta Pendo, Trigger ilimbidi asimame pale kwa sekunde kadhaa kwa ajili ya kuhakikisha anachokiona, baada ya kujiridhisha, alitoka mbio mpaka alipo Harry, akamtoa nje,

"kuna hatari, yule mwanamke Dokta tuliyemteka na kumtupa, yupo hapa, amelazwa" Trigger aliongea huku akihema juu juu,

"basi itakuwa Sarah ndio alikuja kumuona na ndio maana mkaonana" Harry aliongea,

"hili ni tatizo, wewe unadhani huyu demu akipona itakuwaje, si lazima atatoa taharifa polisi?" Trigger aliuliza,

"huyu ni wa kumalizwa" Harry aliongea,

"ndio maana siku ile nikawaambia tummalize, nyie mkakataa, sasa anakuja kututia presha" Trigger aliongea kwa kulalamika,

"wewe angalia usalama jengo zima, ili tujue namna ya kummaliza, kesho ikiwezekana" Harry aliongea,

"sawa, hii ni mbaya, mbaya sana" Trigger aliongea huku akiondoka kwenda kuangalia usalama ili wajue namna ya kummaliza Dokta Pendo siku inayofuata.

*****************

Siku iliyofuata, Sarah alikuwa bize sana na masuala ya kampuni yake, kwa hiyo hakuweza kwenda kabisa hospitali Nyakati za mchana ila alijitahidi sana kuwasiliana na muuguzi ili kujua maendeleo ya Dokta Pendo.

Ilivyofika jioni, Sarah aliamua kwenda hospitali, hakwenda na gari lake kwa ajili ya usalama, alikwenda na gari ndogo ya ofisi.

Sarah alivyofika hospitali alielekea moja kwa moja kwenye wodi aliyolazwa Dokta Pendo, ila kabla hajafika aliweza kumuona mtu aliyemtia mashaka, alikuwa ni Trigger, tena alikuwa akiranda randa kwenye eneo la ile wodi, hakuweza kuingia kwa kuwa ndani ya ile wodi walikuwepo watu waliokwenda kumtazama Dokta Pendo.

Sarah akasubiri kwa muda mpaka Trigger alipopotea eneo lile, kisha kwa hatua za haraka akaenda kuingia ndani ya wodi, wakati Sarah akiingia na watu waliokuwa ndani walikuwa wanamuaga Dokta Pendo, kwa maana hiyo walikuwa wanaondoka. Watu walivyoondoka, Sarah akamsogelea Dokta Pendo,

"kuna hatari tuondoke" Sarah aliongea kwa sauti ya chini,

"hatari gani?" Dokta Pendo aliuliza,

"wale waliokuteka nimewaona wakiranda nje ya wodi hii" Sarah aliongea,

"acha waniue tu" Dokta Pendo alijibu kijeuri,

"acha ujinga wewe, mimi nakubeba tunaondoka" Sarah aliongea kwa jazba,

"Sarah nilishakuonya Kaa mbali na mimi, usinizidishie matatizo, haya uliyonipa yananitosha, na kama utalazimisha unitoroshe hapa, nitapiga kelele za kuomba msaada" Dokta Pendo aliongea,

"siwezi kukuacha wakuue" Sarah aliongea na kumpiga ngumi ya kisogo Dokta Pendo, Dokta Pendo akapoteza fahamu, Sarah akamuweka kwenye kiti cha matairi na kuanza kumsukuma kuelekea nje.

Sarah alivyotoka tu ndani ya wodi, ndio muda huo Trigger akaingia na bastola mkononi, lakini cha ajabu hajakuta mtu, akahisi kuchanganyikiwa, akatoka mbio na bastola mkononi, akapishana na daktari, daktari akaogopa baada ya kuiona bastola, lakini Trigger hakumdhuru, alimpita tu.

Daktari akahisi hatari, ndipo kuanza kukagua wodi na akakuta wodi moja haina mgonjwa, daktari akahisi mgonjwa ametoroshwa, akakimbilia alarm na kobonyeza, baada ya dakika mbili polisi walijaa eneo la hospital, daktari akawaeleza kila kitu, polisi wakazunguka hospitali nzima, hakuna gari kutoka bila kukaguliwa, na kumbuka Sarah alikuwa bado gari yake ipo ndani ya uzio wa hospitali, alishangazwa na hali ya polisi kujaa eneo lile, akapata hofu huku akihisi huenda imegundulika mgonjwa ameibwa au kuna tukio jingine lisilo la kawaida limetokea.

Sasa Sarah akataka kuwasha gari na kuliondoa kwa kasi, ila alipata mashaka kutokana na gari aliyokuwa nayo leo, haikuwa na kasi kama range Rover yake.

wakati gari yake ikiunguruma huku akiwaza cha kufanya, na muda huo Dokta Pendo alikuwa anazinduka,

"Sarah nirudishe wodini, napiga kelele" Dokta Pendo aliongea huku machozi yakimtoka, alikuwa amekalishwa siti ya nyuma, ila kabla Sarah hajasema kitu, mlango wa gari yake ulifunguliwa ghafla, akashtuka, na kumtazama mtu aliyefungua, alikuwa ni polisi, na tena nyuma ya huyo polisi walisimama polisi wengine wawili,

"shuka chini" Polisi aliongea huku akimmulika Sarah usoni kwa kutumia tochi, Sarah akachoka kabisa na wakati huo sura ya dokta Pendo ilichanua kwa tabasamu..................

**********ITAENDELEA**********

the Legend☆
 
RIWAYA : SALA YA SARAH

MTUNZI : ALEX KILEO

SEHEMU YA AROBAINI NA MOJA

ILIPOISHIA.................

Akiwa amekata tamaa kabisa, Sarah alifungua chumba cha mwisho, alikuta kipo giza ila alihisi kuna mtu anahema kwa nguvu sana, Sarah akapapasa ukutani ili atafute switch ya taa, hakuiona, akaamua kufuata sauti ya mihemo inapotokea, ghafla akamulikwa usoni na tochi yenye mwanga mkali, kisha taa ya chumba kile ikawashwa, alishangaa kumkuta Trigger juu ya kile kiti, yeye ndio aliutengeneza mtego ule wa kumnasa Sarah,

"karibu himayani malaya mtoto" Trigger aliongea huku amekamata bastola yake mkononi, Sarah akataka kurudi mlangoni ili akimbie, ghafla mlangoni akatokea Harry huku nyuma yake akiwa Tekso na Strategic na wote walikuwa na silaha nzito za kivita,

"jisalimishe" Harry aliongea huku akisimama na pia akitoa tabasamu la ushindi. Sarah akazungusha macho kama mtu anayefanya tathmini, ila aliona hawezi kufua dafu mbele ya wanaume wale wenye silaha nzito, Sarah akatoa silaha zake zote na kuzitupa chini, akapiga magoti na Mikono akaiweka juu, Sarah alisalimu amri ingawa hukupenda, aliamua akubaliane na matokeo bila kujua kuwa huenda mwisho wake umekaribia......................

**********ENDELEA***********

"mfunge kamba malaya huyu" Harry aliongea kisha Trigger akanyanyuka na kuchukua kamba na kumsogelea Sarah,

"weka mikono nyuma malaya wewe" Trigger aliongea huku akiivuta mikono ya Sarah kwa nyuma, kisha akamfunga kamba mikononi na kisha akamsukuma kwa mbele, Sarah akaangukia tumbo, kisha Trigger akaishika miguu ya Sarah na kuifunga kwa kamba, sasa rasmi Sarah akawa mateka wa vijana wa Taita.

"katundikeni kwenye chumba cha mateso" Harry aliamrisha kisha Trigger na Tekso wakamkamata Sarah mkono wa kushoto na Tekso alikuwa upande wa kulia wa Sarah , wakaanza kumpeleka, walifika sehemu katika eneo la sebuleni na kuondoa meza, kisha wakakuta kuna mfuniko kama wa chemba, wakauvuta na kumfanya kuuweka pembeni, kisha wakaingia kwa kutumia ngazi wakaanza kushuka chini, muda wote Sarah alikuwa akishangaa namna hiyo sehemu ilivyojificha.

Walipofika chini walikuta korido ndefu, wakaanza kuifuata mpaka katika mlango mmoja uliokuwa na kufuri nzito, Trigger akatoa funguo na kufungua ile kufuri, kisha wakamuingiza Sarah ndani, Kisha wakamfunga katikati ya chumba ambapo sehemu ya juu kulikuwa na vyuma vinaning'inia, wakaifunga mikono ya Sarah juu katika vile vyuma na miguu yake ikabaki ikining'inia, yaani haikufika chini,

"sasa leo nataka unijibu maswali yangu machache" Harry aliongea huku akivuta kiti na kukaa, ila Sarah hakuonesha kuogopa, alitabasamu tu,

"kwanini unataka kutuua?" Harry aliuliza,

"kuwaua? Kama ningetaka kuwaua basi wewe ningeshakuua zamani, bado sijataka kuwaua, bado nangoja nyie mtake kufa wenyewe" Sarah alijibu huku akitabasamu,

"lini sasa wakati wewe hapo ulipo ndio mwisho wako" Trigger aliongea kwa kejeli huku akicheka,

"hakuna anaejua mwisho wangu, na wala huu hautakuwa mwisho wangu" Sarah alijibu kijeuri,

"mpumbavu wewe upo kwetu bado unatujibu jeuri?" Trigger aliongea huku akimrushia Sarah ngumi kali iliyotua kwenye mdomo wa Sarah na kumfanya Sarah ageuze shingo na kutema damu,

"nadhani wewe ni mzuri sana kwenye matumizi ya silaha, ila kwenye matumizi ya ngumi hauna kitu, nimelithibitisha hilo, ngumi yako ni nyepesi sana, kama ya binti wa miaka kumi na mitano" Sarah aliongea huku akitoa kicheko kikubwa cha dharau,

"mpuuzi wewe, leo nitakuua, nitakuua kwa mkono wangu" Trigger aliongea na kumrushia Sarah ngumi mbili zilizomfikia usoni na nyingine ikatua kwenye pua ya Sarah, damu ikawa inamchuruzika Sarah kwenye pua yake,

"hizo ngumi zote zingekuwa ni za mwanaume aliyekamilika, nadhani ningekuwa nimepoteza fahamu au ningekuwa nimeshakufa" Sarah aliongea, ila safari hii hakua akicheka tena, alikuwa akisikitika huku akimuangalia kwa jicho la dharau,

"malaya wewe nitakuua" Trigger aliongea kwa hasira huku akijiandaa kurusha ngumi nyingine,

"tulia wewe, huyo anakupa wendawazimu tu, usiangaike kupambana nae, tutakuwa nae muda wote hapa, utampiga utakavyo na utamtafanya utakavyo, hata mkiamua kumbaka kwa zamu mnaweza" Harry aliongea huku akiwa ameushika mkono wa Trigger na kumuacha,

"Harry una akili sana, nadhani wazazi wako waliona mbali na ndio maana wakaweka dhamira mpaka ukafika chuo kikuu na ukabobea kwenye masuala ya sheria, ila ulichobobea haukitendei haki, unaonea wanyonge kwa sababu ya fedha, umegeuzwa mbwa wa mwenye fedha, unatumiwa kinyume na matarajio ya ulichokisomea, umekuwa mtumwa" Sarah aliongea huku akimtazama Harry,

"binti kuna kitu umsaahau, wazazi wangu walinisomesha kwa juhudi na bidii ili nije kuwa na fedha na niwasahidie kipindi wakizeeka, hicho ndicho ninachokifanya, nipo kwa ajili ya kupata pesa, hujakosea kusema ninatumikishwa kwa ajili ya pesa" Harry alijibu kwa umakini huku akiwa amemkazia macho Sarah,

"unatumikishwa kwa pesa, ila siku ya kifo chako itaandikwa umekufa kwa ajili ya haki" Sarah aliongea huku akitabasamu,

"sasa binti sio kila jambo jema nililolifanya napaswa kulitangaza, kuna mambo mema mengi sana nimeyafanya katika upande wa haki, so usinihukumu kwa kuwa sijawahi kufanya jema mbele yako" Harry aliongea huku nae pia akitabasamu,

"je unaweza kunisaidia kitu ili nikuhesabu kuwa ni mmoja kati ya watu wema niliowahi kukutana nao?" Sarah aliuliza,

"nikusaidie nini?" Harry aliuliza,

"naomba uwe shahidi au uwe mwanasheria wangu katika kesi nitakayoifungua dhidi ya vifo vya wazazi wangu" Sarah aliongea huku akimuangalia Harry,

"utafungua lini sasa wakati huu ndio mwisho wako?" Trigger aliuliza kwa dharau huku akicheka,

"wewe huwezi ujua mwisho wangu kama mwanzo wangu hukuwahi kuujua" Sarah alijibu kwa sauti ya utulivu,

.

"kama ukiweza kutoka hapo, nitakusaidia" Harry alijibu huku akinyanyuka na kuondoka zake, aliamini kabisa Sarah hana ujanja tena wa kutoka pale alipo, na pia aliamini katika ule mchakato wake wa kumuua Sarah ili abakie na amani.

Huku ndani Trigger aliendelea kutamba mbele ya Sarah,

"Mimi usiku nitakupiga tu mpaka nichoke, sina sababu ya kukupiga, nakupiga kufurahisha nafsi" Trigger aliongea huku akiokota mnyonyoro uliokuwa unazagaa sakafuni,

"ukiamua kunipiga, nipige mpaka nife, ukiniacha hai ama ukanivunja kila kiungo changu ila ukaniacha nikipumua, huo utakuwa muendelezo wa makosa yako dhidi yangu, kama tutakutana tena, ndio itakuwa tamati yetu, mmoja lazima afe" Sarah aliongea kwa kujiamini,

"wewe maliza maneno yote, mimi siongei tena, leo nakupiga tu, kesho ndio nitakuuliza maswali" Trigger aliongea kisha akawaruhusu Tekso na Strategic waondoke, akabaki yeye na Sarah, Trigger akamuondoa fulana Sarah na kumuacha mgongo wazi, akaanza kumtandika kwa kutumia ule mnyonyoro, alimtandika sana, Sarah alilia mpaka sauti ikamkauka, mwisho akalegea, macho yakajaa giza na baada ya hapo ubongo haukuwa na mawasiliano tena na dunia, Sarah alilegeza shingo na kufunga macho, lakini Trigger aliendelea kumpiga tu, mpaka aliporidhika, akazima taa ya kile chumba na Kutoka zake kifua mbele, leo alimkamata mwizi wake baada ya arobaini nyingi zisizo na idadi.

***************.

Asubuhi ya leo Sajenti Minja aliamkia hospitali, wakati yupo njiani akielekea hospitali, njiani habari ilikuwa ni kuibwa mgonjwa katika hospitali kubwa na yenye hadhi, magazeti yote na radio zilikuwa ni habari hizo hizo na kila mtu mtaani alikuwa anaongea lake, wapo waliolaani hicho kitendo na wapo pia walituhumu uzembe wa watu wa usalama wa hospitali na wapo wengine waliomlaumu mgonjwa.

Njia nzima Sajenti Minja mawazo yake yalikuwa ni kuwaza hilo tukio, huku akijaribu kutengeneza picha namna hao watu wakiingia hospitali na kufanya uharifu huo.

Sajenti Minja akafika eneo la hospital na kuomba kuonana na mkurugenzi wa hospitali, akaruhusiwa,

"kama nilivyojitambulisha hapo hawali, mimi ni askari na huyo mgonjwa aliyechukuliwa alikuwa na kesi ambayo nilikuwa naipeleleza mimi, kwa hiyo basi, ningependa kuona camera za matukio yote ya jana usiku" Sajenti Minja alizungumza kwa utulivu,

"hakuna shida mkuu, twende chumba cha usalama" Mkurugenzi wa hospitali aliongea huku akisimama na kutangulia kutoka nje huku Sajenti Minja akimfuata kwa nyuma. Safari yao iliishia kwenye mlango mmoja ulioandikwa "security room", mkurugenzi akagonga mlango na ukafunguliwa na kijana mmoja aliyevaa sare za rangi ya blue tupu na kiatu cheusi,

"karibu mkurugenzi" kijana aliongea huku akiwa amesimama mlangoni,

"huyu ni askari mpelelezi, ana kitu anataka kuangalia kwenye record za jana" Mkurugenzi aliongea,

"karibu, pita ndani" Kijana aliongea huku akiacha njia Sajenti Minja apite,

"sasa mimi acha nikuache, nimekufikisha sehemu husika" Mkurugenzi aliongea huku akimpa mkono Sajenti Minja,

"shukran mkurugenzi, nitakuona nikitoka hapa" Sajenti Minja aliongea huku akitabasamu, kisha akaingia ndani na kuoneshwa sehemu ya kukaa, alikaa pembeni ya yule kijana,

"jana usiku ulikuwepo?" Sajenti Minja alimuuliza yule kijana,

"nilikuwepo toka jana mchana" kijana alijibu,

"ok, ebu weka camera ya wodi namba tano kisha uirudishe mpaka Nyakati za jana usiku wakati wa tukio" Sajenti Minja alimwambia yule kijana, yule kijana akairudisha ile camera mpaka muda huo, lakini walionekana wale wageni wa hawali tu waliongia kumuona Dokta Pendo, baada ya hapo camera zikakata mawasiliano,

"huyu aliefanya hili tukio huenda ni mtaalam sana au anayajua mazingira yote ya hapa" Sajenti Minja aliongea huku akisikitika,

"na hata nilipoangalia camera za nje pia sikumuona, nazo zilikuwa zinakata kama hivyo" Kijana aliongea huku akimuwekea Sajenti Minja nae ajionee,

"nashukuru mista, nitarudi tena endapo kutakuwa na ulazima wa kufanya hivyo" Sajenti Minja aliongea huku akisimama na Kuondoka zake, aliweza kupishana na baadhi ya waandishi wa habari wakiwa wapo bize kuhoji wafanyakazi wa hospitali ile.

Sajenti Minja alienda mpaka kwenye gari lake na kuingia, kisha akatoa simu na kumpigia Sarah, simu haikuita, akajaribu tena kupiga namba za Dokta Pendo, pia simu haikuwa hewani, Sajenti Minja akaenda zake ofisini kuendelea na kazi zake.

************************

Dokta Pendo alifungua macho saa mbili asubuhi, hakumkuta Sarah pembeni yake, akadhani huenda yupo jikoni anapika.

Saa tatu asubuhi ikafika lakini hakuona dalili zozote za Sarah kuwepo, akahisi huenda ameenda sokoni.

Saa nne ilipofika hakuona uwepo wa Sarah, Dokta Pendo akajiuliza hata kama sokoni, hilo soko lipo umbali gani? Dokta Pendo akatoa mawazo ya Sarah kuwepo sokoni, akaweka mawazo huenda Sarah ameenda kazini na labda atarudi mchana, akawaza sasa kwanini amshindishe na njaa?

"huyu mwanamke alaaniwe, kwanini anitese hivi??? Si bora angeniacha hospitali?" Dokta Pendo aliongea peke yake huku njaa ikimtafuna, tena kwa kwa kasi ya ajabu.

Mwishowe ikafika saa kumi, Dokta Pendo akaanza kutukana matusi yote makubwa kumuelekea Sarah, kibaya zaidi Dokta Pendo alianza kunyong'onyea kutokana na njaa na pia alikuwa amemeza dawa kali zilizopo kwenye droo ya kitanda pembeni yake. Njaa iliendelea kumuuma na kunyanyuka alikuwa hawezi, akaanza kupiga kelele ili hata mtu akipita amsikie, lakini haikuwezekana kwa sababu nyumba ya Sarah ilijitenga sana, akaamua anywe maji yote yaliyokuwa kwenye chupa pembeni yake.

Saa mbili usiku ikamkuta Dokta Pendo yupo Hoi kitandani, taabani, alichokuwa anakifanya ni kumuomba Mungu huku akilaani kitendo hicho anachofanyiwa na Sarah, kitu ambacho hakukijua ni kuwa muda huo Sarah alikuwa kwenye hali hatari zaidi yake, japo Sarah alikuwa kwenye hatari na akiwa katika hali mbaya kiafya, bado alimuomba Mungu amsaidie Dokta Pendo jambo lolote baya lisimpate.

*****************

Wakati Sarah na dokta Pendo wakiwa katika hali hizo tete, Sajenti Minja mawazo yalikuwa yameaongezeka zaidi baada ya kufokewa na mkuu wake kama mtoto mdogo, alionekana ni mzembe aliyeshindwa kuifanya kazi yake kwa weledi.

Mida hii ya saa tatu usiku, Sajenti Minja alikuwa anajiona ni mtu mwenye hatia sana, aliona jambo lolote baya litalomkuta Dokta Pendo, basi yeye atahusika kwa namna moja au nyingine hata kama hatokuwa mlengwa wa moja kwa moja.

Na muda huu wa saa tatu usiku, Sajenti Minja alikuwa akielekea nyumbani kwa Sarah baada ya kupata wasiwasi kwa maana tokea asubuhi alikuwa akipiga simu na haikuita, na muda huu simu ya Sarah ikawa haipatikani kabisa, Sajenti Minja alikuwa hayupo kwenye hali nzuri kimawazo, kwanza alipanga kumfanya vibaya mtu yoyote atakayehisiwa na kupatikana na hatia juu ya matatizo ya Dokta Pendo.

Saa tatu unusu Sajenti Minja alikuwa anasimamisha gari yake nje ya nyumba ya Sarah, alikuta geti limefungwa, akataka kuondoka ila roho yake ikakataa, akapiga hesabu na kuamua aingie kwa njia isiyo sahihi, akaruka ukuta na kuingia ndani ya uzio wa nyumba, akaelekea kwenye mlango wa sebuleni, akajaribu kuusukuma mlango ukafunguka, akahisi hatari zaidi, akaingia kwa hatua za kunyata, akakuta sebuleni kuko giza, akawasha taa.

Dokta Pendo akiwa chumbani alisikia mtu akiwasha taa, akashukuru Mungu huku akiamini Sarah amerudi, akapanga kumnunia, tena mnuno wa kimataifa.

Sebuleni Sajenti Minja akakuta vitu vyote vipo kwenye utaratibu mzuri, akafungua droo na kuikuta simu ya Sarah,

"atakuwa ameenda kazini amemsahau simu" Sajenti Minja aliongea kwa sauti ya kawaida huku akiifunga droo, akazungusha macho kushoto na kulia, akazima taa akawa anaelekea mlango wa kumtoa sebuleni.

Dokta Pendo aliweza kusikia yote hayo, aliweza kuisikia mpaka sauti ya Sajenti Minja akaitambua, akaona huo ndio wakati wake wa kuwa huru na kutoka mikononi kwa Sarah, aliamua kuwa muwazi kwa Sajenti Minja.

ila kilichomtisha Dokta Pendo ni kuhisi kama Sajenti Minja anataka kuondoka, Dokta Pendo akavuta pumzi ndefu na kupiga kelele kubwa za kutaka msaada................

**********ITAENDELEA*************

the Legend☆
 
RIWAYA : SALA YA SARAH

MTUNZI : ALEX KILEO

SEHEMU YA AROBAINI NA MBILI

ILIPOISHIA.................

Dokta Pendo akiwa chumbani alisikia mtu akiwasha taa, akashukuru Mungu huku akiamini Sarah amerudi, akapanga kumnunia, tena mnuno wa kimataifa.

Sebuleni Sajenti Minja akakuta vitu vyote vipo kwenye utaratibu mzuri, akafungua droo na kuikuta simu ya Sarah,

"atakuwa ameenda kazini amemsahau simu" Sajenti Minja aliongea kwa sauti ya kawaida huku akiifunga droo, akazungusha macho kushoto na kulia, akazima taa akawa anaelekea mlango wa kumtoa sebuleni.

Dokta Pendo aliweza kusikia yote hayo, aliweza kuisikia mpaka sauti ya Sajenti Minja akaitambua, akaona huo ndio wakati wake wa kuwa huru na kutoka mikononi kwa Sarah, aliamua kuwa muwazi kwa Sajenti Minja.

ila kilichomtisha Dokta Pendo ni kuhisi kama Sajenti Minja anataka kuondoka, Dokta Pendo akavuta pumzi ndefu na kupiga kelele kubwa za kutaka msaada................

**************ENDELEA*************

Bahati mbaya kwa Dokta Pendo ni kwamba, nguvu hakuwa nazo, hata sauti haikutoka, akajaribu tena, bado sauti haikutoka, kilichoweza kutoka kwa muda huo ni machozi tu, Dokta Pendo alianza kuuamini ule msemo wa wahenga, "siku ya kufa nyani miti yote huteleza"

Dokta Pendo akajaribu kujivuta, lakini bado mwili ulikataa, nguvu haikuwepo kabisa, tena mbaya zaidi hata mkono tu kuunyanyua alishindwa.

Dokta Pendo akatabasamu, aliamua kukingojea kifo chake kwenye kitanda cha ugenini, hakuwa akiamini kuna msaada mwingine tena, alichokiamini ule ni mchezo, aliyemchezea vile ni Sarah, chuki yake dhidi ya Sarah ikaongezeka Maradufu, akaamua afunge macho na kusubiri kile alichokiita kifo, ndio aliamini ndio msaada uliobakia dhidi ya mateso anayokumbana nayo.

********************

Sarah fahamu zilimrudia saa kumi alfajili, alipofungua macho akajitahidi kupambana na giza la mule ndani, akahisi maumivu makali mgongoni, akakumbuka mateso aliyokuwa anapewa na Trigger ndo yamemuachia maumivu hayo, akataka kupiga hatua, miguu ikawa inaelea, akakumbuka tena alining'nizwa, kitu kingine kilichomshangaza ni kujikuta amefunikwa na nguo kifuani wakati fulana yake ilichanwa na Trigger, akiwa anawaza hayo, alisikia sauti ya mtu akikohoa, tena kikohozi kikavu kabisa, Sarah akageuka shingo ila hakuona mtu kutokana na giza kushamiri ndani ya chumba kile.

Sarah nae akajikoholesha huku akiamini huenda huyo mtu aliyekohoa hawali anaweza kumuongelesha,

"mama umeahamka?" Sauti iliuliza kutoka katika ya giza, sauti hiyo ilionesha imetoka kwa mtu aliyechoka sana,

"ndio, wewe nani?" Sarah aliuliza huku akijifanya amechoka sana, yule mtu hakujibu, badala yake akaenda moja kwa moja sehemu switch ilipo na kuwasha taa, Sarah hakuamini macho yake, alikuwa ni babu yake, alikuwa amechoka sana, Sarah akataka kuuliza kitu ila nafsi ikamzuia akajikuta ameshangaa tu,

"mama hawa watu ni wabaya sana, umewafanya nini mpaka wakakuleta hapa?" babu yake Sarah aliuliza huku akionekana kutomkumbuka kabisa Sarah,

"Mimi sikuwafanya kitu, wamenikamata tu na kunileta huku" Sarah aliongea huku akishangaa hali ya babu yake, huruma ilimjaa,

"pole sana mama, sijui hata kama utqtoka mzima, juzi juzi tu alikuja msichana wa makamo yako, wamempiga wakamvunja miguu yote, wakaenda kumtupa na Sidhani kama yupo hai tena" Babu yake Sarah aliongea kwa huruma na kumfanya Sarah ajue anaezungumziwa ni Dokta Pendo, hapo roho ikamcheza kuhusu hali aliyomuacha nayo Dokta Pendo,

"na wewe kwanini wamekukamata?" Sarah alimuuliza babu yake utasema hajui kweli,

"Mimi wamenikamata kwa ajili ya mjukuu wangu, sasa sijui wanamdai na hawajui alipo au kuna sababu nyingine" babu yake Sarah alijibu na kumfanya Sarah machozi yamtoke,

"sasa mbona hawajakufunga kamba, upo huru alafu unashindwa kutoroka?" Sarah alimuuliza babu yake,

"hata nikitoroka nitapita wapi? Mlango umefungwa kwa nje, na uko nje kuna ulinzi mkali sana" Babu yake Sarah alijibu,

"ndio maana wamekuacha huru, wanajua huwezi fanya kitu" Sarah aliongea kwa upole,

"sijaachwa huru mama, mimi nafungiwa humu, ila kuna upenyo hapa chini uwa napita, humu ninapofungiwa ni padogo sana, ukilala lazima ujikunje sana na uamkapo mwili wote uwa unauma, kwa hiyo mimi nikifungiwa humu uwa natoka usiku sana nalala hapa mpaka panapokucha, kisha narudi humu kwenye kibanda changu" Babu yake Sarah aliongea huku akiwa anamuoneshea Sarah kakibanda kadogo kama cha mbwa,

"kwa hiyo hawajuagi kama unatoka usiku?" Sarah alimuuliza,

"hawajui, siku wakijua watanimaliza" babu yake Sarah alijibu,.

Baada ya hapo waliendelea kuongea mpaka palipokucha, kisha babu yake Sarah akarudi kibandani kwake, Sarah roho ilikuwa inamuuma sana, baada ya babu yake kuingia kibandani, Sarah alilia sana, aliona mateso yote yanayomkuta babu yake, basi chanzo ni yeye,

"mchuma janga hula na wakwao" Sarah aliongea kwa sauti ndogo huku machozi yakitiririka mashavuni mwake.

Sasa muda ukiwa umeenda tangu Sarah aongee na babu yake, mlango ulifunguliwa na Trigger akaingia huku akivuta sigara,

"za asubuhi?" Trigger aliongea kwa kejeli huku akimsogelea Sarah,

"nzuri, karibu tena" Sarah alijibu huku akitabasamu na kumfanya Trigger achoke kabisa, aliamini atamkuta Sarah kwenye hali mbaya sana,

"leo sitokupiga, na kama nitakupiga sitotumia mnyororo kama jana, leo nitatumia njia nyingine" Trigger aliongea huku akiitoa bastola yake na kuitazama,

"huamuzi ni wako, niko himayani kwako, fanya chochote utachojisikia" Sarah alijibu huku akiendelea kutabasamu,

"leo sitokupiga, ila nina maswali machache unatakiwa uyajibu" Trigger aliongea huku akivuta kiti na kukaa mbele ya Sarah,

"uliza" Sarah alijibu,

"endapo tutakuua, itakuwa tumekosea?"Trigger aliuliza,

"kuuawa vitani sio kosa kisheria, na hii iliyo kati yetu ni vita, siogopi kufa na wala sitojuta kufa" Sarah alijibu huku akitabasamu,

"unajua hata kifo cha wazazi wako ni vita, sasa nashangaa wewe unavyotaka kulipa kisasi wakati unajua kuwa kufa vitani ni ushujaa" Trigger aliongea huku akimtazama Sarah,

"vita ni mapambano ya majibizano kutoka pande husika, sasa ile haikua hivyo, mlichofanya nyinyi ni uonevu, kwa maana mlimshambulia mtu ambaye hakuwa akiwashambulia, na mtawajibika kwa hilo" Sarah aliongea huku akiwa amemkazia macho Trigger,

"tutawajibika??? nani atatuwajibisha wakati wewe unafia huku?" Trigger aliuliza kwa madaha,

"kama hutoniua muda huu, kamwe hutopata nafasi ya kuniua tena" Sarah aliongea kwa kujiamini kabisa,

"nitakuua muda ninaotaka, usinipangie" Trigger aliongea huku akinyanyuka katika kiti,

"nisipokupangia muda wa kukuua, basi jiandae kupangiwa muda wa kufa wewe" Sarah aliongea na kufanya Trigger aangushe kicheko kikubwa sana,

"wewe mtoto mpumbavu sana, yaani umedhibitiwa hivyo bado unajiamini?" Trigger aliongea huku akiendelea kucheka,

"endelea kujidanganya" Sarah aliongea,

"nilitaka nisikupe chakula leo, ila nitaagiza uletewe jioni, umenifurahisha sana ndio maana nitakuletea chakula, Trigger aliongea huku akielekea nje, alipofika mlangoni akageuka,

"uwa unapenda chakula gani?" Trigger aliuliza huku akitabasamu,

"nahitaji maji tu, na glucose" Sarah aliongea na kumfanya Trigger azidi kucheka,

"glucose???? Unataka upate nguvu??" Trigger aliongea kwa kejeli huku akitoka nje na kumuacha Sarah akitabasamu tu.

Baada ya nzima ya Trigger kuondoka, Sarah alitupia macho kwenye kile kibanda alichoingia babu yake,

"we mzee" Sarah aliita kwa sauti ya chini,

"nakusikia" Babu yake alijibu,

"toka uko, njoo mara moja" Sarah alimuita yule mzee, babu akaja,

"binti nimesikia maongezi yenu yote, inaelekea mnajuana sana" Babu yake aliuliza kwa uoga,

"nisaidie kitu, ebu nifungue hizo kamba miguuni" Sarah Alimwambia babu yake,

"mama unataka kufanyaje, usije ukaniponza na mimi nikafa" babu yake Sarah aliongea kwa uoga,

"mzee nifungue, acha uoga" Sarah Alimwambia babu yake,

"mama mimi siwezi" Babu yake alijibu hivyo ingawa alikuwa na uwezo wa kumfungua,

"mzee huna watoto? Toka jana nimefungwa miguu inaning'inia, hunionei huruma" Sarah alimuuliza kwa upole,

"sawa nitakufungua miguu, lakini si bado utakuwa unaning'inia tu, mikono ndio ipo juu" Babu yake aliongea,

"nifungue hivyo hivyo tu ili damu ipite vizuri" Sarah alimuomba babu yake, babu aliendelea kuleta mgomo ila mwisho alikubali kumfungua Sarah miguu, Sarah alivyofunguliwa miguu, akaivuta miguu juu mpaka kwenye mikono na kujifungua kamba mikononi, akawa huru, kipindi chote babu yake alipigwa na mshangao kwa maana hakuwahi kuona kitendo kama hicho kabla.

"rudi bandani mzee, hapa hapakufai tena" Sarah aliongea huku akijifuta damu mgongoni mwake.

****************/*****

Sajenti Minja kutwa nzima alishinda na mawazo, ila pia kuna wazo baya lilimjia, alianza kumuhisi Sarah vibaya, na kitu kilichopelekea hiyo ni gari la Sarah, alianza kulitilia mashaka kutokana na kufanana na gari la mwanamke anayemtafuta,

"mara nyingi namba halisi ya gari hukaa kwenye vioo vya gari husika, lazima nikalichunguze lile gari la Sarah" Sajenti Minja aliwaza,

"na kwanini tokea amepotea Dokta Pendo na Sarah nae haonekani na hata simu yake haipatikani, kwanini nisianze kumchunguza na yeye?" Sajenti Minja aliendelea kujiuliza.

Kisha akatoa simu yake na kujaribu kupiga namba ya Sarah, ikawa haipatikani, akajaribu tena na tena lakini jibu likawa ni lile lile, akajaribu kupiga namba ya Dokta Pendo alikadhalika ikawa haipatikani pia, Sajenti Minja akapiga meza kwa hasira.

Nyakati za usiku zilipofika, Sajenti Minja alichukua gari yake na kuelekea moja kwa moja kwa Sarah, alipofika aliegesha gari nje na kisha yeye akaenda getini, akakuta mlango umefungwa kama alivyouacha siku iliyopita, Sajenti akaruka ukuta na kuingia ndani, alipoingia tu kitu cha kwanza alichofanya ni kuangalia namba za gari ya range Rover ya Sarah, akazikuta ni zile zile alizozizoea, na hata alipoangalia kwenye kioo zilikuwa zinarandana na za plate.

Sajenti Minja akaridhika, akaamua aingie ndani, alipofika sebuleni aliikuta kama alivyoiacha siku iliyopita, kila kitu kilikuwa vile vile,

"huyu mwanamke yupo kweli?" Sajenti Minja alijiuliza huku akipepesa macho mule sebuleni.

Mwisho akaanza kuita jina la Sarah, aliita kwa zaidi ya mara tatu hakupata jibu, kitu ambacho hakukijua ni kuwa muda huo Dokta Pendo alikuwa chumbani kwa Sarah na alikuwa ameshapoteza fahamu tangu siku iliyopita.

Sajenti Minja akiwa pale sebuleni akaamua aondoke zake, alipozima taa ya sebuleni akaona kuna sehemu kuna mwanga, yaani taa zinawaka, Sajenti Minja hakudhani kama kuna kitu au mtu, ila aliamua aende hiyo sehemu, kitu ambacho hakukijua ni kuwa hapo anapoelekea ni chumbani kwa Sarah, na mbaya zaidi Dokta Pendo yupo humo.

Sajenti Minja alienda moja kwa moja mpaka mlangoni, akapiga hodi mara mbili lakini hodi yake haikuitikiwa, akaamua kushika kitasa cha mlango na kuusukuma mlango, mlango ukafunguka...............

***********ITAENDELEA************

the Legend☆
 
RIWAYA : SALA YA SARAH

MTUNZI : ALEX KILEO

SEHEMU YA AROBAINI NA NNE.

ILIPOISHIA......................

Sarah alivyofika alimsalimu huku akitabasamu, ila hata kabla maongezi hayajaanza, Vin nae alitokea na kuja kukaa pale pale, Sarah alipomtupia jicho mapigo ya moyo yakaanza kumwenda mbio, na wakati huo hiyo hali ilimkuta Vin.

"Sarah huyu ni Vin, mtoto wa Taita" Harry aliongea huku akitabasamu na kumfanya Sarah astahajabu, maana kabla hajakutana nae hilo jina alishalisikia,

"lakini hausiki kwenye kikao chetu" Sarah aliongea, alikuwa amepaniki,

"Mimi sihusiki, ila nimekuja ili uniambie baba yangu alikufanya nini mpaka umfanyie vile?" Vin aliuliza kwa sauti ya upole,

"kwanini hujaniuliza yeye alinifanya nini mpaka nikaamua kumfanya vile?" Sarah nae aliuliza kwa hasira,

"haya niambie alikufanya nini?" Vin akauliza,

.

"kwa kuwa nimekufundisha kuuliza hilo swali, basi tukikutana siku nyingine hilo ndio liwe swali la kwanza, alafu Harry leo umenikosea kwa mara nyingine tena, huu ndio mwisho wa kukubembeleza" Sarah aliongea kwa hasira huku akisimama aondoke, Vin akamshika mkono kwa nguvu,

"Baba yangu amekufanyia nini mpaka umefanya ateseke vile?" Vin aliuliza huku machozi yakimjaa machoni,

"Mimi sikutaka ateseke vile, mimi nilitaka kumuua ili asiteseke, lakini nashangaa kwa nini hajafa?" Sarah aliongea kwa jeuri huku akijaribu kujinasua mikononi mwa Vin, Vin akamkata Sarah kofi kali la shavu,

"unajua uchungu niliokuwa nao mpaka unanijibu hivyo?" Vin alifoka kwa hasira huku akisimama,

"unanipiga kwa ajili ya yule nguruwe ambaye ni baba yako???, siku akipata fahamu muulize kuhusu mimi, atakujibu" Sarah aliongea kwa hasira na kumsukuma Vin,

"malaya mkubwa, unamuita baba yangu nguruwe?" Vin hasira ziliongezeka, akataka kumpiga kofi jingine, Sarah akaudaka mkono wa Vin, kisha Sarah akataka kutoa bastola ili amtishe Vin, Vin kuona hivyo akatoa bastola yake haraka hata kabla ya Sarah hajatoa yake, kisha bila mtu yoyote kutarajia, Vin akamfyatulia risasi Sarah ya kifua, Sarah akaganda huku asiamini kinachotokea, akiwa ameganda vile vile, Vin akafyatua risasi ya pili iliyopiga paja la Sarah, Sarah akadondoka kutoka ukingoni mpaka chini kwenye maji

"kazi nzuri, umeua" Harry aliongea huku wakiondoka na vin.

Uko chini kwenye bahari, watu waliokuwa hapo walijaa wakiushangaa mwili wa Sarah uliokuwa ukielea juu ya maji...........

***********ENDELEA***********

Mwili wa Sarah ulielea kwa muda wa nusu dakika na watu wakaanza kujaa wakiuzunguka, ghafla bila kutegemea Sarah alifungua macho na kukuta kundi la watu likimtazama, Sarah akakurupuka na kuanza kupiga hatua huku akiuvuta mguu wake, alikuwa ameumia baada ya lile shambulio la risasi. Sarah aliendelea kujivuta huku akiwa amelowa mwili mzima, akajikuta mpaka kwenye gari yake, Range Rover nyeusi na kuingia huku kundi la watu wakimfuatilia na wakishangaa mtu aliyepigwa risasi amewezaje kusimama? Sarah baada ya kuingia kwenye gari yake, aliwasha na kuiondoa kwa kasi, akuwa na furaha kabisa kwa kitendo alichofanyiwa na Harry, hiyo siku Sarah alikuwa na hasira kupita maelezo, njia nzima alikuwa anamuwaza huyo mtu aliyetambulishwa kama mtoto wa Taita, na pia aliwaza usaliti aliofanyiwa na Harry.

"Harry una hali mbaya" Sarah aliongea peke yake huku akikanyaga mafuta ya gari.

**************************

Sajenti Minja aliweza kufika eneo la tukio ambalo mwanamke alipigwa risasi, ila bahati mbaya alikuta mtu aliyepigwa risasi amekimbia na waliompiga risasi wamekimbia.

"sasa huyo mwanamke aliyepigwa risasi amewezaje kukimbia?" Sajenti Minja alimuuliza dada mmoja ambaye ndiye alikuwa shuhuda wa tukio,

"amenyanyuka na ameondoka huku akiuvuta mguu wake na kuingia kwenye gari" Dada alitoa maelezo,

"kwa ulivyomuona, hiyo risasi amepigwa eneo gani?" Sajenti Minja aliuliza,

"itakuwa mguuni kwenye paja, maana ndio alikuwa amepashika" Dada shuhuda aliongea,

"ulisema alivyoinuka alienda kwenye gari lake, hilo gari uliweza kulitambua" Sajenti Minja aliuliza,

"ndio, ni Range Rover Sport nyeusi" Dada shuhuda alijibu na kumfanya Sajenti Minja acheke,

"namba zake ulifanikiwa kuzinakiri?" Sajenti Minja aliuliza,

"hapana, sikuwa na akili ya kuwahi kukariri namba, nilikuwa na mshangao kwa kitendo cha mtu aliyepigwa risasi kuamka na kutembea" Dada shuhuda alijibu,

"je, waliompiga risasi huyo dada uliwaona?" Sajenti Minja aliuliza,

"sikubahatika kuwaona kwa kuwa tukio lilitokea juu na huyo dada akaanguka kutoka kule juu na kufikia kwenye maji" Dada shuhuda alijibu huku akionesha kidole eneo la juu,

"ahaa, kumbe aliporomoka kutoka kule?" Sajenti Minja aliuliza huku akimtazama eneo la juu,

"nilibahatika kuchukua video wakati huyo dada amelala hapo chini" Dada shuhuda aliongea huku akibonyeza simu yake na kumfanya Sajenti Minja ajongee ili aweze kumuona huyo dada ambaye alikuwa akimtafuta kwa muda mrefu, ile video ilimuonesha Sarah akiwa amelala akielekea juu ya maji ila sura ilikuwa chini, alafu video ikaishia hapo hapo.

"sasa mbona fupi, hakuna inayomuonesha uso?" Sajenti Minja aliuliza huku akionekana kukereka,

"simu yangu iliisha charge, hata hapa unapoiona inaweza kuzimika muda wowote" Dada shuhuda aliongea huku akizima data kwenye simu yake,

"nirushie hiyo video" Sajenti Minja aliongea huku nae akitoa simu yake mfukoni na kisha akarushiwa ile video fupi.

Baada ya kumaliza kuchukua ile video, Sajenti Minja alienda mpaka eneo la juu ambapo inasemekana huyo mwanamke alipigwa risasi eneo hilo.

Alimkuta mdada mmoja ambaye inaonekana alikuwa muhudumu hapo, Sajenti Minja akamsalimia,

"Mimi ni polisi, unaweza kuniambia hilo tukio la kupigwa mwanamke risasi lilikuwa?" Sajenti Minja aliuliza baada ya kujitambulisha,

"Mimi kwa kweli nilikuwa bize na mambo yangu, ghafla nikasikia watu wanapiga kelele huku wengine wakikimbia, ndipo nilipoangaza macho nikaona kwenye meza moja wamekaa wanaume wawili na mwanamke mmoja ambaye alikuwa amesimama huku akiwa ameganda, muda huo huo tena mwanaume mmoja yule aliyeshika bastola akamfyatulia risasi yule mwanamke, ilimpata pajani, yule mwanamke akaangukia chini, kisha wale wanaume wakasimama na kuondoka" Muhudumu alitoa maelezo yake,

"kati yao unamjua yoyote?" Sajenti Minja aliuliza,

"siwajui kwa kweli, ila kama nitabahatika kuwaona tena, nitawatambua" Muhudumu aliongea,

"na huyo mwanamke nae ukioneshwa unaweza kumtambua?" Sajenti Minja aliuliza,

"hapana, mwanamke alinipa mgongo, sikuweza kuiona sura yake" Muhudumu alijibu,

"nashukuru, ila inatakiwa ufunge huduma kwa sasa" Sajenti Minja alimwambia Muhudumu,

"ndicho ninachokifanya kwa sasa na ndio maana hujakuta mteja" Muhudumu alijibu na kumfanya Sajenti Minja aelekee zake nje.

Alichofanya Sajenti Minja aliondoka moja kwa moja mpaka kwenye mamlaka ya mapato na kuomba aonane na mkurugenzi, akaoneshwa ofisi na kwenda. Alipofika aliingia moja kwa kwa mkurugenzi na kumkuta akiwa anajiandaa kutoka,

"vipi bwana, wamekuruhusu vipi kuingia wakati ni muda wa kutoka huu?" Mkurugenzi aliuliza huku akivaa koti lake la suti,

"nina shida muhimu, naomba unipe kama dakika tano hivi" Sajenti Minja aliongea huku akikaa kwenye kiti,

.

"sina muda kijana, uje kesho" Mkurugenzi aliongea huku akimuinua Sajenti Minja,

"sijaja kwa tatizo binafsi, nimekuja kiserikali" Sajenti Minja aliongea na kutoa kitambulisho na kukiweka mezani na kumfanya yule mkurugenzi atulie kidogo,

"ooh kumbe umekuja kitaifa?, ungesema mapema" Mkurugenzi aliongea huku akivuta kiti na kukaa,

"usijali boss" Sajenti Minja aliongea,

"kuna tatizo gani?" Mkurugenzi aliuliza huku akivua miwani,

"naomba unitazamie gari aina ya Range Rover Sport zipo ngapi zilizosajiliwa hapa nchini?" Sajenti Minja aliuliza na kumfanya mkurugenzi ashangae,

"sasa hilo tatizo si ungelimaliza huko chini?" Mkurugenzi aliuliza,

"nina sababu zangu za kuja huku, sasa nisaidie tu" Sajenti Minja aliongea huku akitabasamu, na kumfanya mkurugenzi avute computer yake na kuanza kubofya bofya, baada ya dakika tano akamgeukia Sajenti Minja,

"Range Rover tulizozisajili ni kumi na mbili, ila tulizosajili mwaka huu ni mbili, moja ni ya mwanamke anayeitwa Sarah Isack na nyingine ni mzee mmoja wa kiarabu, ila ya huyo mzee sasa hivi haipo, alishaondoka nchini na aliondoka na gari yake" Mkurugenzi aliongea huku akimuangalia Sajenti Minja,

"hiyo ya huyo mwanamke namba zake ni hizi?" Sajenti Minja aliuliza huku akimpatia mkurugenzi karatasi yenye namba za gari la Sarah, mkurugenzi akaangalia na kisha akarudisha macho kwenye computer,

"hakika ndio yenyewe" Mkurugenzi aliongea huku akimrudishia karatasi Sajenti Minja,

"na hii namba ya nani, nani anaimiliki?" Sajenti Minja aliuliza huku akimpatia karatasi ile yenye namba ya siri ya Sarah anayoitumiaga Sarah kipindi anapoenda kufanya tukio. Mkurugenzi akaichukua ile namba na kuiingiza kwenye computer, akabofya bofya vitufe vya computer kisha akawa anasubiri kwa muda,

"hiyo namba haijasajiliwa, ilifutwa usijili wake, ila hakuna sababu yoyote iliyoandikwa kama chanzo cha kufuta hiyo namba" Mkurugenzi alitoa jibu,

"ilikuwa inamilikiwa na nani?" Sajenti Minja aliuliza,

"hakuna record nyingine zaidi ya hiyo niliyokuambia" Mkurugenzi aliongea huku akimgeuzia computer Sajenti Minja ili nae ajionee,

"basi hiyo namba inafanya kazi, tena inatumiwa na mtu anayefanya uharifu" Sajenti Minja aliongea huku akiirudisha computer usawa wa uso wa mkurugenzi,

"sasa hiyo kazi ya kupeleleza ni yenu, hapa msaada wetu umeishia hapo" Mkurugenzi alijibu,

"nashukuru, ila nitarudi tena nikihitaji msaada wako" Sajenti Minja aliongea huku akimpa mkono wa shukran,

"usijali, karibu tena" Mkurugenzi aliongea huku akiweka vitu vyote vizuri juu ya meza.

Sajenti Minja akaelea nje na kuingia ndani ya gari,

"kwa maana hiyo gari ambayo imesajaliwa na ipo ni moja tu, ya Sarah. Au kuna mtu yupo karibu yake uwa anatumia na uwa anabandika namba battle?" Sajenti Minja alijiuliza huku akiwasha gari na kuliondoa,

"sasa bora nimfuatilie Sarah, huenda kuna kitu anakijua, natakiwa niende nae kwa akili sana" Sajenti Minja aliongea huku akiingia ndani ya mgahawa, muda ulikuwa umeenda sana.

Sajenti Minja aliingia mgahawani na kula, alipomaliza akaenda nyumbani, hakuwa na cha kufanya muda huo, akaona bora aende kumuona Sarah huku akiamini kama ni kweli yeye ndiye aliyepigwa bastola, basi lazima amkute na majeraha, Sajenti Minja akatabasamu, akaingia chumbani na kuvaa kaptula fupi na fulana, na juu akavaa koti.

Akatoka na safari ya kwenda kwa Sarah ikaanza, njia nzima alikuwa anawaza kama kweli Sarah atakuwa mtuhumiwa, atamfanyaje?

"sharia itafuata mkondo tu" Sajenti Minja aliongea huku akiwa makini na barabara.

Mishale ya saa mbili na nusu Sajenti Minja alikuwa akiegesha gari yake nje ya nyumba ya Sarah, baada ya hapo akatelemka na kuingia moja kwa moja mpaka mlango wa sebuleni na kupiga hodi, sauti ya kiume toka ndani ikaitikia kisha Sajenti Minja akaingia,

"shikamoo babu" Sajenti Minja alimsalima babu yake Sarah aliyekuwepo sebuleni huku akitazama runinga,

"marhabaa kijana, karibu" Babu yake Sarah aliitikia kichangafu huku kikombe cha kahawa kikiwa mbele yake,

"naona umeshapazoea hapa" Sajenti Minja aliongea huku akikaa juu ya sofa,

"tena sana, Unaona nilivyojitanua" Babu yake Sarah aliongea huku akicheka,

"naona aisee, vipi huyu bibie nimemkuta?" Sajenti Minja alimuulizia Sarah,

"yupo, yupo ndani uko" Babu yake Sarah alijibu na kisha akapaza sauti kumuita Sarah, baada ya sekunde chache Sarah alitokezea sebuleni huku akitembea kwa kuuvuta mguu wake kama umeumia, Sajenti Minja akapata mshtuko ila hakuonesha wazi mshtuko wake,

"karibu afande" Sarah aliongea huku akijitupa juu ya sofa,

"huo mguu vipi?" Sajenti Minja aliuliza,

"nadhani umeteguka" Sarah alijibu,

"babu naomba utupishe kidogo" Sajenti Minja aliongea huku akimuangalia babu yake Sarah,

"kwanini?" Sarah aliuliza,

"babu tupishe muda mchache tu utarudi" Sajenti Minja aliongea huku akiwa bado anamtazama babu yake Sarah,

"kwanini aende?" Sarah aliuliza huku akiwa hamuelewi Sajenti Minja,

"kuna mambo muhimu nataka nikuulize" Sajenti Minja alijibu,

"babu nenda, nitakuita" Sarah Alimwambia babu yake na kisha babu akasimama na kuondoka zake huku akiwa na wasiwasi.

"jioni leo ulikuwa ufukweni?" Sajenti Minja aliuliza na kufanya Sarah apate mshtuko, akahisi Sajenti Minja amemgundua,

"leo nimeshinda nyumbani tu" Sarah alidanganya,

"sasa naongea kama askari na wala sio Joel Minja. Toa hiyo khanga uliyoivaa" Sajenti Minja aliongea huku akiitoa bastola na kumfanya Sarah apate hofu zaidi, Sarah alijua kabisa Sajenti Minja amejua kuwa Sarah yeye alipigwa risasi pajani,

"unataka nikuvulie nguo afande, unataka kunifanya nini?" Sarah aliuliza huku akijifanya ana hasira,

"Sarah fuata amri nikiyokupa, vinginevyo tutaonana wabaya" Sajenti Minja aliongea na kufanya Sarah azidi kupata hofu,

"sheria ndio inasema nimvulie nguo afande?" Sarah aliuliza kwa ukali huku akiwa amesimama,

"toa khanga hiyo, kuna kitu nataka niangalie pajani kwako" Sajenti Minja aliongea kwa ukali huku nae akisimama, Sarah akaona leo kazi anayo,

"sitoi khanga na wala siogopi bastola yako" Sarah aliongea huku akigeuka na kuanza kuondoka huku akiuvuta mguu wake na pia akiamini amefanikisha kumtoka Sajenti Minja,

"unaongea na serikali kama unaongea na bwana wako" Sajenti Minja aliongea kwa hasira huku akiivuta khanga ya Sarah, khanga ikadondoka na Sarah akabaki na kaptula fupi sana iliyoacha kwa asilimia kubwa mapaja yake wazi, kisha Sajenti Minja akamgeuza Sarah kwa kasi wakawa wamegeukiana, macho ya Sajenti Minja yakakimbilia kwenye mapaja ya Sarah kuangalia eneo alilopigwa risasi...........

*********ITAENDELEA**********

the Legend☆
 
RIWAYA : SALA YA SARAH

MTUNZI : ALEX KILEO

SEHEMU YA AROBAINI NA SITA

ILIPOISHIA....................

Baada ya hapo Sarah akaingiza mkono mfukoni na kutoa risasi mbili, moja akaiweka mezani upande wake, na risasi nyingine akaiweka upande wa Trigger pembeni ya bastola aliyomuwekea Trigger, kisha akaitoa stop watch na kuitega sekunde thelathini,

"ikifika sekunde sifuri tunatakiwa kuwahi hizo bastola mezani na kuzitia hiyo risasi, alafu atakayewahi atampiga mwenzake eneo lolote analotaka, mimi nitakupiga kichwani, maana siku yako ya kifo ni leo" Sarah aliongea kwa kejeli na sasa Trigger alishajua lengo la Sarah, Trigger akaachia tabasamu moja baya sana, tabasamu la dharau.

Sekunde zilizidi kuhesabu tu kutoka juu kwenda chini, ilipofika sekunde ya sifuri tu, Sarah kwa kasi ya ajabu akaiwahi bastola yake na kuijaza risasi haraka, alipotaka kuinyanyua ili amfyatulie risasi Trigger, Sarah ndipo aliposhtuka, alikuta tayari mdomo wa bastola ya Trigger upo usawa wa kichwa chake, Sarah akainuka kwa kasi ili akimbie, lakini alichelewa tayari, wakati akiinuka ndio muda huo Trigger alifyatua risasi iliyompiga Sarah na kumtupa mbali............. Sarah akawa yupo chini huku damu ikiwa imejaa kichwani eneo la kisogoni................

************ENDELEA*************


Kichwa chote cha Sarah kilitapakaa damu aliyokuwa ameilalia, sio kwamba alikuwa amepigwa risasi ya kichwa, lah! alipigwa risasi ya bega baada ya kuinuka kwa kasi, lengo la Trigger lilikuwa ni kufumua kichwa cha Sarah, ila baada ya Sarah kuinuka kwa kasi, ile risasi ilipiga bega la Sarah na kumfanya Sarah aanguke chini huku akivuja damu, na ile damu iliyokuwa inavuja kwa wingi ilitapakaa eneo lile na kumfanya Sarah ailalie damu yake na kichwa chake chote kikatapakaa damu.

Baada ya Sarah kuanguka kutokana na pigo la risasi, Sarah akainuka na kuwahi kuokota bastola yake ili ammalize Trigger, lakini alikuta Trigger hayupo muda tu, alishasepa kitambo eneo, Sarah akajikuta anajitukana matusi ya nguoni kwa kufanya uzembe wa kutokummaliza Trigger mapema bila kufanya nae mashindano, Sarah akaenda upande ngazi ilipo ili atelemke, akakuta ngazi imeangushwa chini, Sarah akachoka kabisa, ila akarudi nyuma hatua kadhaa na kwenda mbio mpaka ukingoni kwenye ukuta na kuruka mpaka chini, akahisi maumivu kwenye mkono wake uliopigwa risasi, kisha akaondoka mpaka nje ya nyumba, akaangaza angaza kuona kama ataliona gari la Trigger, lakini hakuiona, akaingia kwenye gari yake na kuiondoa kwa kasi kuwahi nyumbani kwake, ilibidi atumie mwendo wa kasi kwa kuwa alihofu anaweza kupata tatizo kubwa endapo hiyo risasi itaendelea kukaa mwilini mwake. alitumia mkono mmoja tu kuendeshea gari yake.

Alifika nyumbani kwake na kuingia ndani, hakukuta mtu sebuleni, Sarah akapitiliza mpaka kwenye chumba chake cha siri na kuvua fulana, akaenda kwenye sehemu lilipo box lake la huduma ya kwanza, akatoa kisu na mikasi kadhaa, akaenda kukaa mbele ya kioo kikubwa na kisha akaanza kutoa risasi, ingawa alisikia maumivu ila alijitahidi mpaka akafanikisha, alafu akachukua dawa ya maji na kumwagia eneo la jeraha, kisha akaweka pamba na kujifunga bandeji begani, baada ya hapo alitoka na kwenda zake chumbani kwake, alimkuta Dokta Pendo amelala usingizi mzito, Sarah akabadili nguo na kuvaa za kulalia kisha akaingia ndani ya shuka na Kulala.

*****************

.

Trigger alivyompiga risasi Sarah, aliamua kukimbia baada ya kujua Sarah hajafa na kitu kingine ni kuwa Sarah alikuwa jirani na bastola, Trigger hakuona kitu cha kufanya, aliamua kukimbia, alishuka kwenye ngazi na kuitoa ngazi kisha akakimbia mpaka eneo la nje na kuchukua gari yake na kuondoka kwa kasi,

Alipofika kwake alichukua simu na kumtaharifu Harry kila kitu kilichotokea, Harry alishangaa sana, ila alimlaumu Trigger kwanini hakumuua Sarah!? Trigger alijitetea ila ilikuwa ngumu kwa Harry kumuelewa.

"huyu mpuuzi kweli, mbona yeye hakuwahi kumpiga hata ngumi, kazi kulaumu wenzake tu" Trigger aliongea baada ya Harry kukata simu, kisha Trigger akaingia chumbani kwake.

****************

Siku iliyofuata, nyakati za asubuhi, Harry aliamua kumtafuta Aisha, wakakutana kwenye mgahawa waliozoea kukutana,

"Aisha mimi sikuelewi, yaani sijui unachokifanya, hela umekula na Sarah anazidi kunisumbua tu" Harry aliongea kwa kulalamika,

"bado namfuatlia, tena kwa ukaribu sana, hata jana nilikuwa namfuatilia usiku ule wakati akikufuatilia, ila Trigger aliingilia nikaamua kuachana nae, uwa sipendi kuingiliwa kwenye mipango yangu" Aisha aliongea,

"alaah, kumbe ulikuwa unamfuatilia? basi endapo ungeendelea kumfuatilia ungemuua jana, maana Trigger alifanikiwa kumpiga mpaka risasi ila hajamuua" Harry aliongea,

"kwani ni lazima nianze kumuua Sarah? Taita nae si anatakiwa afe? Kwanini nisiangalie ni yupi anaweza kuwa mwepesi kuuawa kwa muda huu?" Aisha aliuliza,

"wote wanatakiwa kufa, fanya uwezavyo ila wote wafe" Harry aliongea,

"sawa, basi niachie hiyo kazi mimi" Aisha aliongea kwa kujiamini,

"sawa, cha muhimu uharakishe kutekeleza hayo yote" Harry aliweka msisitizo,

"nikupe muda gani wa utekelezaji?" Harry aliuliza,

"nimeshakuambia niachie mimi hiyo kazi, kwa hiyo hayo masuala ya utekelezaji yanahitaji mipango yangu, wewe subiri tu taharifa" Aisha alijibu,

"sawa, ila jua maisha yangu yako hatarini" Harry aliongea kwa hofu,

"hata ya kwangu pia, wewe unadhani huyo Sarah endapo nitamuendea hovyo na kunidhibiti, ataniacha?" Aisha aliuliza huku kamtumbulia macho Harry,

"sawa, fanya uwezavyo, na mimi nitafanya niwezavyo" Harry aliongea kwa upole,

"poa, acha nikuache" Aisha aliongea huku akiinuka katika kiti,

"haya" Harry alijibu huku akimuangalia namna Aisha anavyoondoka.

Baada ya dakika tano za Aisha kuondoka, Harry alimpigia simu Tekso, huyu ndiyo yule bwana wa mkuu wa technology katika mamlaka ya Taita. Ilimchukua dakika kumi tu za Tekso kufika, aliongozana na Trigger, walipofika waliagiza chai na kuendelea na maongezi,

"hivi Tekso huwezi kutengeneza bomu dogo lakini lenye mlipuko wa kuleta athari ndani ya umbali wa mita mita tano?" Harry aliuliza huku akimuangalia Tekso,

"udogo wa hilo bomu ni upi unaouzungumzia wewe? Ni kama kiazi mviringo au kama kizibo cha soda?" Tekso aliuliza kwa kujiamini,

"nadhani tupate yenye mlingano na kifungo cha koti la suti" Harry alijibu,

"hiyo inawezekana, nipe wiki moja na pia andaa pesa kidogo kwa ajili ya kununulia vifaa" Tekso aliongea,

"hilo bomu la kazi gani?" Trigger aliuliza,

"nataka ninunue nguo maalum na nitamshawishi Aisha awe anazivaa, na pia kifungo kimoja kitawekwa kinasa sauti ili niweze kumfuatilia" Harry alijibu,

"humuamini tena Aisha?" Trigger aliuliza,

"nahisi nina dalili hizo" Harry alijibu,

"ulimfahamia wapi?" Trigger aliuliza,

"nilikutana nae Congo, alikuwa anatumiwa kama jasus na majeshi ya waasi" Harry alijibu,

.

"mzee mimi niwaache" Tekso aliongea huku akiifunga laptop yake juu ya meza, Tekso kijana mwenye nywele nyingi zisizojua kitana wala chanuo ndani ya muda mrefu,

"umekuja na gari?" Harry alimuuliza,

"hapana, huyu bwana alinipa lift" Tekso aliongea huku akiwa amemshika bega Trigger

"unaenda wapi sasa muda huu?" Trigger alimuuliza,

"kufanya utaratibu wa kutengeneza huo mlipuko" Tekso alijibu,

"sawa, ngoja twende wote, maana sina kazi muda huu" Trigger aliongea huku nae akiinuka, alimfuata Tekso na kumuacha Harry akiwa amekaa pale pale mgahawani.

******************

BAADA YA MWEZI.

Siku hii ya leo, babu yake Sarah alikuwa hana raha kabisa, alikuwa yupo sebuleni na dokta Pendo wakitazamana runinga, Sarah yeye alikuwa yupo kazini.

Na kwa Nyakati hizi hali ya Dokta Pendo ilikuwa njema kiasi kwa maana hakuwa na bandeji ngumu miguuni, tayari zilishatolewa na siku hizi Dokta Pendo alikuwa anafanyishwa mazoezi machache ya kutembea kwa ajili ya kumuweka vizuri miguu yake,

"mzee mbona leo haupo sawa, una nini?" Dokta Pendo alimuuliza babu yake Sarah,

"nipo sawa, hivi ni wapi ulikutana wapi na huyu mwenzako, au alikuweka? Kwa maana mimi nimeanza kukuona wiki iliyopita tu na nikashangaa kuambiwa eti ulikuwepo kabla yangu" Babu yake Sarah aliuliza,

"Mimi ni rafiki yake tu, nipo muda mrefu tangu nimevunjika miguu" Dokta Pendo alijibu,

"ujue binti kuwa muwazi, huyu mwenzako mimi simuamini kabisa, kwanza tulikutana kama mateka, sijajua huyu mwanamke ni nani?" babu yake Sarah aliendelea kuongea,

"kwanza mzee umewaza nini mpaka uongee hivyo?" Dokta Pendo aliuliza huku akitabasamu,

"wewe binti kuwa muwazi, wewe ulitekwa hospitali na Mpaka leo vyombo vya usalama vinakutafuta, usibishe kuhusu hilo" Babu yake Sarah aliongea huku akitupa juu ya meza gazeti lenye habari za kutekwa Dokta Pendo na picha yake, Dokta Pendo akaishiwa pozi,

"ndio ni kweli huyu aliniteka, je unataka kunisaidia?" Dokta Pendo aliuliza kwa utulivu,

"tayari nimeshakusaidia" Babu yake Sarah aliongea huku akiwa hatanii,

"umenisaidiaje sasa, mbona mzee sikuelewi?" Dokta Pendo aliuliza huku akishangaa, ila kabla babu yake Sarah hajajibu, Sarah aliingia huku akitabasamu,

"aisee nimechelewa kidogo, ngoja nibadili nguo haraka twende mazoezini" Sarah aliongea kwa furaha,

"Mimi nilishajikatia tamaa ya kwenda uko mazoezini" Dokta Pendo alijibu huku akitabasamu,

"lakini kwema hapa?" Sarah aliuliza huku akielekea chumbani na kuwaacha hapo sebuleni.

"haya babu nielezee, umenisaidiaje sasa?" Dokta Pendo aliuliza huku akimuangalia babu yake Sarah,

"subiri utaona" Babu yake Sarah aliongea huku akitabasamu na kumfanya Dokta Pendo akae kimya tu, kwa maana hakuelewa kitu.

Baada ya nusu saa Sarah aliweza kutoka chumbani huku akiwa amevaa nguo za mazoezi na kwenda moja kwa moja kwenye friji na kuchukua juisi, akaimiminia kwenye kikombe na kuinywa kwa haraka,

"kuna habari gani mpya?" Sarah aliuliza huku akitabasamu

"hakuna mpya, habari ni zile zile" Babu alijibu huku akijichekesha,

"mmekula mmeshiba?" Sarah aliuliza huku akiendelea kutabasamu,

"tumeshiba mama, ila mama mpaka leo hajawahi kuniambia ni lini utanipeleka kwangu, maana naishi na wewe hata sikujui" Babu aliuliza kwa sauti kavu,

"tatizo nini mzee, si unakula na unalala vizuri tu, hayo masuala ya kujuana yatakuja mbele ya safari" Sarah aliongea huku akiweka utani,

"usiseme hivyo binti, kama suala la kula hata kwangu ningekula na Kulala vizuri tu" Babu aliongea kwa kujiamini,

"mzee usijifanye huna shida, mzee wewe toka amekufa mwanao Isack na maisha yako yalibadilika na kuwa mabaya sana" Sarah alitoa kauli iliyomshangaza babu yake,

"Isack, wewe umejuaje hayo yote?" Babu yake alimuuliza,

"Pendo twendezetu matizi, mzee anazingua" Sarah alipuuza swali la babu yake na kisha akamuongelesha Dokta Pendo,

"mjibu mzee kwanza" Dokta Pendo aliongea huku akicheka,

"twende bwana, ipo siku atapata majibu" Sarah aliongea huku akimsaidia Dokta Pendo kunyanyuka,

"ipo siku ee? Au utanijibia kituoni?" Babu yake Sarah aliuliza kama utani ila alikuwa amedhamilia,

"mzee leo husomeki ujue, umeonja nini?" Dokta Pendo aliuliza kwa utani,

"twende shoga, kwani alitoka leo?" Sarah alimuuliza Dokta Pendo huku wakitoka kwenye mlango wa sebuleni

"alitoka kuanzia asubuhi, amerudi muda sio mrefu" Dokta Pendo alijibu,

"alikuambia alipoenda?" Sarah aliuliza,

"hajaniambia, ila nahisi itakuwa alienda mjini, maana alirudi na gazeti ambalo lina picha yangu inaonesha nimepotea na natafutwa" Dokta Pendo aliongea na kisha akacheka,

"huyu mzee kichaa, ngoja nikirudi niongee nae, maana alivyo na akili finyu anaweza kwenda kutoa taharifa polisi, na hivi wametangaza na donge nono" Sarah aliongea huku akiushika mguu wa Sarah na kuuvusha kwenye geti.

"Sarah" Dokta Pendo aliita baada ya geti kufunguliwa,

"sema shoga" Sarah alijibu huku macho yake yakiwa bize kuuvusha mguu wa Dokta Pendo uliobakia ndani ya chuma cha geti,

"Sarah" Dokta Pendo aliita tena huku macho yakiwa mbele,

"unaniita, nahitika ila hata huongei" Sarah aliongea huku akirudishia geti, kisha akageuza shingo yake kuangalia mbele, kidogo aanguke kwa kitu alichokiona, walikuwa polisi zaidi ya kumi na wote walikuwa na silaha na walizinyoosha kuelekea sehemu aliposimama Sarah na dokta Pendo,

"wewe mtekaji weka mikono juu" Polisi mmoja aliyeonekana kiongozi aliongea huku akiwa amemkazia macho Sarah, Sarah akajikuta akiinua mikono juu huku na hakiwa hataki kuamini kama lile tukio ni la kweli kwa maana limetokea ghafla sana, alilazimisha iwe ndoto lakini haikuwezekana, Sarah maji yalizidi Unga. .........

**********ITAENDELEA***********

the Legend☆
 
RIWAYA : SALA YA SARAH

MTUNZI : ALEX KILEO

SEHEMU YA AROBAINI NA SABA

ILIPOISHIA.............................

Baada ya nusu saa Sarah aliweza kutoka chumbani huku akiwa amevaa nguo za mazoezi na kwenda moja kwa moja kwenye friji na kuchukua juisi, akaimiminia kwenye kikombe na kuinywa kwa haraka,

"kuna habari gani mpya?" Sarah aliuliza huku akitabasamu

"hakuna mpya, habari ni zile zile" Babu alijibu huku akijichekesha,

"mmekula mmeshiba?" Sarah aliuliza huku akiendelea kutabasamu,

"tumeshiba mama, ila mama mpaka leo hajawahi kuniambia ni lini utanipeleka kwangu, maana naishi na wewe hata sikujui" Babu aliuliza kwa sauti kavu,

"tatizo nini mzee, si unakula na unalala vizuri tu, hayo masuala ya kujuana yatakuja mbele ya safari" Sarah aliongea huku akiweka utani,

"usiseme hivyo binti, kama suala la kula hata kwangu ningekula na Kulala vizuri tu" Babu aliongea kwa kujiamini,

"mzee usijifanye huna shida, mzee wewe toka amekufa mwanao Isack na maisha yako yalibadilika na kuwa mabaya sana" Sarah alitoa kauli iliyomshangaza babu yake,

"Isack, wewe umejuaje hayo yote?" Babu yake alimuuliza,

"Pendo twendezetu matizi, mzee anazingua" Sarah alipuuza swali la babu yake na kisha akamuongelesha Dokta Pendo,

"mjibu mzee kwanza" Dokta Pendo aliongea huku akicheka,

"twende bwana, ipo siku atapata majibu" Sarah aliongea huku akimsaidia Dokta Pendo kunyanyuka,

"ipo siku ee? Au utanijibia kituoni?" Babu yake Sarah aliuliza kama utani ila alikuwa amedhamilia,

"mzee leo husomeki ujue, umeonja nini?" Dokta Pendo aliuliza kwa utani,

"twende shoga, kwani alitoka leo?" Sarah alimuuliza Dokta Pendo huku wakitoka kwenye mlango wa sebuleni

"alitoka kuanzia asubuhi, amerudi muda sio mrefu" Dokta Pendo alijibu,

"alikuambia alipoenda?" Sarah aliuliza,

"hajaniambia, ila nahisi itakuwa alienda mjini, maana alirudi na gazeti ambalo lina picha yangu inaonesha nimepotea na natafutwa" Dokta Pendo aliongea na kisha akacheka,

"huyu mzee kichaa, ngoja nikirudi niongee nae, maana alivyo na akili finyu anaweza kwenda kutoa taharifa polisi, na hivi wametangaza na donge nono" Sarah aliongea huku akiushika mguu wa Sarah na kuuvusha kwenye geti.

"Sarah" Dokta Pendo aliita baada ya geti kufunguliwa,

"sema shoga" Sarah alijibu huku macho yake yakiwa bize kuuvusha mguu wa Dokta Pendo uliobakia ndani ya chuma cha geti,

"Sarah" Dokta Pendo aliita tena huku macho yakiwa mbele,

"unaniita, nahitika ila hata huongei" Sarah aliongea huku akirudishia geti, kisha akageuza shingo yake kuangalia mbele, kidogo aanguke kwa kitu alichokiona, walikuwa polisi zaidi ya kumi na wote walikuwa na silaha na walizinyoosha kuelekea sehemu aliposimama Sarah na dokta Pendo,

"wewe mtekaji weka mikono juu" Polisi mmoja aliyeonekana kiongozi aliongea huku akiwa amemkazia macho Sarah, Sarah akajikuta akiinua mikono juu huku na hakiwa hataki kuamini kama lile tukio ni la kweli kwa maana limetokea ghafla sana, alilazimisha iwe ndoto lakini haikuwezekana, Sarah maji yalizidi Unga. .........

***********ENDELEA***********

Sarah akaamua atii amri ya polisi huku akishangaa hao polisi wamepajuaje nyumbani kwake?

"mfungeni pingu huyu muharifu" Kiongozi wa kikosi kile cha polisi alitoa amri ambayo askari wawili walimsogelea Sarah na kuchukua mikono yake na kuifunga pingu.

"naombeni muda kidogo niingie ndani nikaache maagizo" Sarah aliongea kwa huruma huku akimuangalia kiongozi wa kikosi kile cha polisi, ila kabla kiongozi yule hajatoa jibu, babu yake Sarah alitoka ndani huku akiwa kifua wazi na kujongea eneo ambalo Sarah na kiongozi wa polisi walikuwa wamesimama pamoja, Sarah alitegemea babu yake ameenda eneo lile kwa ajili yake, lakini cha kushangaza alishuhudia tukio lililomfungua ubongo, alimshuhudia babu yake akipeana mkono na yule kiongozi wa polisi,

"kazi nzuri mzee, tunamshukuru kwa taharifa yako iliyosaidia kumkamata muharifu" Kiongozi wa polisi aliongea kwa tabasamu pana,

"usijali kiongozi, sisi raia wema lazima tufichue maovu" Babu yake Sarah aliongea huku akitabasamu,

"mzee kumbe ni wewe ndio umeniletea polisi?" Sarah aliuliza huku akimuangalia babu yake,

"mpelekeni bwana, ananipigia kelele" Babu yake Sarah aliongea huku akigeuka nyuma,

"mzee mzigo wako uje uchukue kesho asubuhi, pale pale kituoni ulipotoa taharifa" Kiongozi wa kikosi kile cha polisi alimwambia babu yake Sarah,

"usijali, nitafika hiyo kesho mapema" Babu yake Sarah aliongea huku akirudi zake ndani ya geti.

Wale polisi walimpakia Sarah ndani ya gari huku Sarah akiwa na mawazo dhidi ya babu yake ingawa hakutaka kujenga chuki dhidi yake. Baada ya Sarah kupakiwa ndani ya gari, kupitia kwenye kioo cha gari aliweza kushuhudia Dokta Pendo nae akipakiwa kwenye gari nyingine, alimshuhudia Dokta Pendo akiwa na furaha huku akiongea na baadhi ya askari waliokuwa wanamsaidia kupanda gari. Sarah akawa anajitahidi kuangalia uso wa Dokta Pendo ili ajaribu kumsoma hisia zake, lakini haikuwezekana kwa maana muda wote macho ya Dokta Pendo yalikuwa makini na askari aliokuwa anaongea nao na alionekana akiongea kwa furaha huku akicheka, na hata Dokta Pendo alimpomtazama Sarah, wakikutanisha macho yao Dokta Pendo aliyakwapesha macho yake kwa haraka sana.

Safari iliishia ndani ya kituo cha polisi na Sarah akawekwa lupango. Dokta Pendo alipelekwa moja kwa moja katika ofisi na kuambiwa amsubiri mpelelezi ambaye atakuja kumfanyia mahojiano, lakini hiyo ofisi tayari Dokta Pendo aliijua vizuri hii ofisi, alikumbuka kuwa hii ni mara yake ya pili kuingia ofisini hapo, alijua fika kuwa ofisi hiyo ni ya Sajenti Minja.

Dokta Pendo akiwa amekaa akizungusha macho ndani ya ofisi ile, aliweza kushuhudia mlango ukifunguliwa na aliingia Sajenti Minja, Dokta Pendo akaachia tabasamu laini na kumfanya Sajenti Minja nae atabasamu huku akiwa anashangaa namna Dokta Pendo alivyonenepa. Sajenti Minja akampa mkono Dokta Pendo kisha akaenda kukaa kwenye kiti,

"kwanza pole" Sajenti Minja aliongea kwa utulivu,

"pole ya nini?" Dokta Pendo aliuliza huku akijifanya kushangaa,

"ya kutekwa, au unaona hilo sio tatizo?" Sajenti Minja aliuliza huku akijifanya kutabasamu,

"nani alitekwa??? Wewe unavyodhani Sarah anaweza kuniteka mimi?" Dokta Pendo aliuliza huku akijifanya kushangaa na kumshangaza zaidi Sajenti Minja,

"ndio alikuteka, alikuchukuaje hospitali bila taharifa na kwanini hakuwai kuniambia wewe ulipo ingalikuwa nimeshawahi kufika mara kadhaa nyumbani kwake?" Sajenti Minja aliuliza kwa ukali baada ya kuona kama Dokta Pendo anataka kumtetea Sarah,

"Mimi ndio nilimwambia aniondoe hospitali na mimi ndiye nilimwambia asimwambie mtu yoyote ni wapi nilipo" Dokta Pendo alijibu kwa kujiamini,

"usimtetee Sarah, unamteteaje mtu ambaye amehatarisha maisha yako?" Sajenti Minja aliongea kwa jazba,

"amehatarisha maisha yangu? Kivipi amehatarisha maisha yangu wakati alikuwa akinihudumia kwa kila kitu, ningekuwa kwenye matatizo ningenenepa hivi?" Dokta Pendo alihoji,

"ila inafikia kipindi unatakiwa uwe mkweli Pendo" Sajenti Minja aliongea huku akiwa amepunguza jazba,

"ukweli gani unaoutaka?" Dokta Pendo aliuliza,

"Sarah sio mtu mzuri, nisaidie kuthibitisha hilo" Sajenti Minja aliongea huku akimuangalia Dokta Pendo,

"siwezi kuthibitisha kwa kuwa sijawahi kuuona ubaya wake" Dokta Pendo aliongea huku akicheka,

"sasa alikutoroshaje hospitali na camera zisiweze kuona hilo tukio, si ina maana alizichezea camera, na kama alizichezea, basi hiyo ina maana kuwa yule mwanamke ni muharifu mzoefu" Sajenti Minja aliongea huku akiwa na hasira,

"wewe hujui kitu, usiwe unaongea vitu kwa hisia tu. Sarah hayupo kama unavyomfikiria na siku ile mimi ndio nilimwambia aniondoe hospitali baada ya kuwaona wale watu walioniteka na kunivunja miguu wakiwa wanazunguka zunguka eneo lile, sasa labda huenda wale watu ndio walioharibu camera ili wafanye tukio eneo lile" Dokta Pendo aliongea na kumfanya Sajenti Minja ashushe pumzi ndefu,

"Mimi naona hatutaelewana hapa, ebu ngoja nikupeleke nyumbani ukapumzike, nitakuhoji kesho" Sajenti Minja aliongea huku akinyanyuka kwenye kiti,

"nyumbani wapi?" Dokta Pendo aliuliza kwa mshangao,

"nyumbani kwako" Sajenti Minja alijibu huku akimshangaa,

"nyumbani siwezi kurudi, sio eneo salama kwangu, ninapotaka kwenda ni kwa Sarah tu, hapo ndipo palipo na usalama kwa muda huu" Dokta Pendo alizidi kumvuruga Sajenti Minja,

"sasa hata nikikupekeka kwa Sarah, nani atakuhudumia?" Sajenti Minja aliuliza,

"sasa hata ukinipeleka kwangu nani atanihudumia?" Dokta Pendo aliuliza,

"sasa unatakaje?" Sajenti Minja aliuliza,

"muacheni Sarah, kwa maana yeye ndiye mtu pekee anayeniangalia kwa ukaribu" Dokta Pendo alijibu na kumfanya Sajenti Minja akune kidevu chake,

"ni ngumu kumuacha Sarah kwa kuwa ni mtuhumiwa" Sajenti Minja aliongea huku akiwa bado amesimama,

"mtuhumiwa wa nini? Kama kuondoka hospitali ni mimi ndiye nilietaka, kama hilo ni kosa, basi nikamatwe mimi" Dokta Pendo aliongea,

"basi ngoja nikupeleke hotelini, Sarah tutamuachia baadae, tunataka kumfanyia mahojiano" Sajenti Minja aliongea kwa lengo la kumfanya Dokta Pendo akubali kuondoka,

"naweza kuonana nae muda huu?" Dokta Pendo aliuliza,

"hapana, mtaonana baada ya mahojiano" Sajenti Minja aliongea huku akimtazama Dokta Pendo,

"sawa, naomba msifanye kitu chochote" Dokta Pendo aliongea kwa msisitizo,

"usijali kuhusu hilo, twende nikupeleke hotelini utakaa mpaka jioni Sarah atapokuja" Sajenti Minja aliongea huku akimsaidia Dokta Pendo kumtoa kumpeleka nje, walipofika alimuingiza ndani ya gari na kumpeleka hotel iliyo karibu na kituo cha polisi na kumuacha Dokta Pendo hapo.

********************

Habari ya kukamatwa kwa Sarah ilimfikia Harry, akaamua awaite watu wake, Trigger, strategic, Tekso na Aisha.

"Sarah yupo kituo cha polisi, nimesikia amekamatwa kutokana na lile tukio la kumteka mtu hospitali" Harry aliongea,

"ni jambo zuri, au wewe mkuu unasemaje?" Trigger aliuliza,

"hivi hatuwezi kummalizia pale pale kituoni?" Harry aliuliza,

"inawezekana, kama tutatumia bomu kulipua kituo chote" Tekso aliongea huku akiwa bize kobonyeza lap top yake,

"sasa hapo mtaua mpaka wasiohusika, angalieni njia nyingine tofauti na hiyo ya kulipua" Aisha alitoa ushauri,

"basi tufanye kitu kimoja, Aisha unaweza kuingia ndani mule na kumtorosha Sarah?" Strategic aliuliza na kufanya wenzake wamshangae,

"una lengo gani?" Harry alimuuliza Strategic,

"kama tutafanikiwa kumtoa Sarah mikononi mwa polisi, itakuwa rahisi kumuangamiza akiwa chini yetu" Strategic aliongea,

"je Aisha unaweza kufanya hiyo kazi ya kumtorosha Sarah mikononi mwa polisi?" Harry alimuuliza Aisha,

"inawezekana, ila inahitaji akili sana, kwa hiyo kwa leo haiwezekani mpaka tutengeneze mipango" Aisha aliongea,

"hii kitu inahitajika ifanyike leo, tutakusaidia, nitakupa nguo yenye mawasiliano ambayo tutakuwa tunawasiliana" Tekso aliongea na kisha akamuangalia Harry, na Harry nae akamuangalia Tekso, kuna kitu kinaendelea kati ya hawa watu wawili,

"sawa" Aisha alikubali kisha Tekso akanyanyuka na kuingia kwenye chumba kimoja na kurudi na kizibao, au wengi wamezoea kukiita kijamba koti, kisha akakitupa juu ya meza mbele ya Aisha,

"usiku ukienda kuvamia kituo cha polisi, utavaa hiki kikoti juu ya nguo yako, kineunganishwa na mawasiliano, nitakuwa eneo la polisi kukupa maelekezo" Tekso aliongea huku akikaa kwenye kiti, Aisha akakichukua kile kikoti na kuanza kukikagua, kilikuwa na vufungo vitatu vyenye rangi tofauti,

"hiki kifungo cha juu mbona kikubwa alafu kizito?" Aisha aliuliza baada ya kupata hofu,

"hicho kina camera, njia zote utazopita mimi nitakuwa naziona" Tekso alijibu, lakini ukweli ni kwamba kile kifungo kilikuwa na bomu,

"na hivi vifungo vingine vina nini?" Aisha aliuliza,

"kimoja cha katikati kina kinasa sauti, ila hicho cha chini hakina kitu, ni urembo tu" Tekso aliongea,

"naweza kuondoka na hili koti?" Aisha aliuliza huku akiendelea kulikagua,

"hapana, ikifika muda wa kazi utakuja kulichukua" Tekso alijibu,

"kwanini iwe hivyo?" Aisha aliuliza huku akimuangalia Tekso kwa jicho la udadisi,

"chukua nenda nalo" Harry alijibu baada ya kumuona Tekso akibabaika kutoa jibu,

"beba tu, haina shida" Tekso aliongea huku akitabasamu,

"nadhani tukutane saa mbili usiku, Vin hatakiwi kujulishwa huu mpango, mpaka ufanikiwe ndio tutamjulisha" Harry aliongea huku akiinuka kwenye kiti,

"vipi nikupeleke au una usafiri" Trigger alimuuliza Aisha,

"nipeleke", Aisha alijibu huku akiinuka kisha akatoka huku ameongozana na Trigger, ndani wakabaki Harry na Tekso na Strategic,

"sasa kulikuwa na umuhimu gani wa kumpa Aisha nguo yenye bomu wakati anaenda kumdhibiti Sarah?" Strategic aliuliza,

"Mimi simuamini kabisa, nitatumia mwanya watapokuwa karibu na Sarah wakati wakitoroka, hapo nitalipua bomu, maana hatuna uwezo wa kumfunga Sarah bomu, acha tumtumie Aisha kama mtego" Harry aliongea huku akimuangalia Tekso,

"hatutofanya kosa kipindi hiki, remote ya Bomu nitakuwa nayo mimi" Tekso aliongea huku akiioneha remote ndogo iliyokuwa kwenye mfuko wake wa shati.

***********************

Mishale ya saa nne usiku, ndani ya gari alikuwepo Harry na Trigger waliokuwa siti ya mbele na siti ya nyuma walikuwepo Aisha na Tekso.

Walikuwa wanaelekea maeneo ya kituo cha polisi kwenda kumtorosha Sarah.

Na kwa upande wa kituo cha polisi Sarah alikuwa amewekwa juu ya kiti huku akiwa pembeni yake amekaa Sajenti Minja na askari mwingine ambaye walikuwa walikuwa wanamuhoji Sarah,

"je tukisema una hatia ya kumteka mgonjwa na kumtorosha ndani ya hospitali, utakubali?" Sajenti Minja alimuuliza Sarah, lakini Sarah hakujibu,

"huyu tumpige kidogo ili alainike, la sivyo atatusumbua sana" Askari mwingine aliekuwepo hapo aliongea kwa hasira,

"muache kwanza" Sajenti Minja aliongea huku akimsogelea jirani Sarah,

"sasa mtu gani tunamuuliza maswali muda wote na wala hajibu?" Askari mwingine alihoji huku akiona Sajenti Minja anamlea sana Sarah,

"Sarah, kesho itabidi upelekwe mahakamani, acha tufanye una hatia na una kesi ya kujibu" Sajenti Minja aliongea huku akimtazama Sarah, ila Sarah hakujibu,

"mpige hata kofi" Askari aliongea huku akionekana kutamani sana kumuhadhibu Sarah,

"mpige" Sajenti Minja alimruhusu yule askari, yule askari akawa anamfuata Sarah kwa hasira, ila kabla hajamfikia wakasikia mlio wa bunduki nje ya ofisi, Sajenti Minja na mwenzake wakatizamana,

"kuna nini" Sajenti Minja aliuliza huku akiwa hategemei jibu,

"nipo mimi" Aisha aliongea huku akiingia kwa fujo ndani ya ile ofisi na kufanya watu wote kuchanganyikiwa, Aisha alikuwa na bastola mbili mikononi,

"nipeni huyo mwanamke kwa amani au nipeni kwa kumwaga damu" Aisha aliongea huku bastola akiwa amewaelekezea Sajenti Minja na mwenzie,

"wewe ni nani unayetutisha polisi?" Askari mwingine aliuliza huku akimtazama Aisha, ila Aisha hakujibu alimfyatulia yule askari risasi ya kifua, akadondoka na kufa pale pale,

"mfungue huyo demu, au hujanielewa bado?" Aisha alimuuliza Sajenti Minja huku akitabasamu, wakati huo Sarah alikuwa ahamini ni kwa nini Aisha amekuja kumuokoa?

Sajenti Minja akamsogelea Sarah na kuanza kumuondoa pingu mkononi, kisha alipomaliza, Sarah akasimama,

"Sarah mfunge pingu huyo polisi" Aisha alitoa amri, Sarah akachukua mikono ya Sajenti Minja na kuifunga,

"nifuate" Aisha aliongea na Sarah akawa anamfuata kwa nyuma, njiani alipishana na askari kadhaa wakiwa wamefumgwa kamba na wengine wakiwa wamekufa, Sarah akawa anajiuliza hiyo shughuli yote amefanya Aisha?

Walifanikiwa kutoka mpaka nje, kisha Aisha akamshika mkono Sarah na kuanza kukimbia nae, walikimbia mpaka kwenye daraja walilokubaliana na wenzake, muda wote Tekso alikuwa juu ya jengo moja refu akiwasiliana na Harry huku akimuangalia Aisha,

"mkuu, wameshafika darajani" Tekso aliongea kupitia kifaa maalum, aliongea na Harry,

"walipue" Harry aliongea na kisha Tekso akatoa remote yake ndogo na kuishika mkononi, akatabasamu.

Harry Trigger walikuwa ndani ya gari wakimsubiri Tekso amalize kazi ili waondoke. Wakiwa hapo ukasikika mlipuko mkubwa mpaka gari yao ikatingishika, Harry akatabasamu na kisha akashusha kioo cha gari,

"good job" Harry aliongea huku akitabasamu, kwa maana kazi ilikuwa imeisha rasmi.....................

************ITAENDELEA***********

the Legend☆
 
Asante sana legend.ila story kama either zimerukwa au umechanganya.
Mkuu kisukari kwenye post #285 nilitolea ufafanuzi hilo.

"Heshima yenu wakuu. Ni hivi; kati ya episodes 70 za hii riwaya, episodes 5 sijafanikiwa kabisa kuzipata. Nazo ni episode ya 35, 38, 40, 43 na ya 45. Ila nyingine zote zipo.

So kitu nlichofkiria kufanya leo ni kuweka as many episodes as possible, ili iwe rahisi kwenu kuunganisha matukio na hatimae kupata mwanga wa yale yaliyojiri katika hizo episodes zilizo-miss.

Samahanini kwa usumbufu wowote utakaojitokeza"- the_legend

the Legend☆
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom