Riwaya: Sala ya Sarah

Riwaya: Sala ya Sarah

Dah ila sterling hafi ila tabu atakalopata ni kama looooteee asante mkuu you made my day
 
RIWAYA : SALA YA SARAH

MTUNZI : ALEX KILEO

SEHEMU YA THELATHINI NA TATU

ILIPOISHIA........................

Sarah akatelemka na kwenda kugonga mlango,

"hodi Shoga" Sarah aliita huku akigonga mlango, lakini hakujibiwa

"shoga" Sarah aliita kwa sauti kubwa zaidi huku akiendelea kugonga mlango,

"Ngoja, nakuja shoga" Sauti kutoka ndani ilimjibu, lakini haikuwa sauti ya Dokta Pendo, Sarah akapata wasiwasi, akawa anajiandaa kutoa bastola ili avamie, lakini kabla Hajaichomoa bastola yake mlango ulifunguliwa kwa kasi na Sarah akavutwa ndani, bastola ya yake ikadondoka miguuni kwa Aisha.

Sarah alipomuona Aisha alijikuta akikiasirika, haikuwa hasira ya kuvutwa au kupigwa, ilikuwa ni hasira ya kujilaumu kwanini amekuja kwa Dokta Pendo na kukutana na huyu mwanamke mbaya, Sarah hakuwa alikosa kujiamini kabisa mbele ya Aisha, uoga ukamjaa. Na wakati huo Aisha alifunga mlango kwa ndani kisha akaiokota bastola ya Sarah na kumuelekezea Sarah,

"hii ya leo haina kuremba, ni kumaliza kazi na kupotea" Aisha aliongea na kuikoki bastola huku akiwa hana tabasamu lake kama tulivyomzoea, alikuwa yupo makini kiasi kwamba ndita zilionekana vyema kwenye paji lake la uso.........

***********ENDELEA************

"kwanini utumie bunduki kuniua? Mbona unaweza kunimudu kwa mapigo" Sarah aliongea huku akimuangalia Aisha,

"kwanini tupoteze muda kwa kupigana, acha tu nimalize kazi mapema" Aisha aliongea,

"sawa, najua nakufa muda sio mrefu, je aliyekutuma uniue ni nani?" Sarah alimuuliza Aisha,

"hilo tu, nimetumwa na Harry, unamjua?" Aisha alijibu na wakati huu alianza kutabasamu,

"hapana simjui" Sarah alijibu na kukana kumjua Harry,

"siku chache nyuma nilikuona nae Vin hotel, kwanini unakataa hamjui" Aisha aliuliza,

"yule mwanasheria ndio Harry? Kakupa sababu yoyote ya yeye kutaka kuniua mimi?" Sarah alimuuliza Aisha,

"hajanipa, alafu hapa sio sehemu ya kuulizana maswali" Aisha aliongea,

"sawa, tumekutana mara mbili na Tumepambana, ulinishinda mara zote, lakini leo inaonekana kama unaniogopa na ndio maana unataka kutumia bastola" Sarah aliongea huku akimuangalia Aisha,

"nikuogope kwanini? Mimi sitaki tu kupoteza muda tena kwa ajili yako" Aisha alijibu,

"mbona umeshaupoteza tayari, maana ni muda mrefu toka tumeanza kuongea" Sarah aliongea huku akitabasamu,

"kwa hiyo unanishauri nikupige tu risasi?" Aisha aliuliza huku akiishika vyema bastola mikononi mwake,

"sawa nipige na bastola, ila hautokuwa umeshinda kihalali, ukinishinda kwa ngumi ndio utakuwa ushindi mzuri" Sarah aliendelea kumshawaishi Aisha,

"nimeshakushinda mara mbili, hiyo inaonesha tu huniwezi" Aisha aliongea kwa majivuno,

"wengi walinishinda mara mbili, ila hakuna hata mmoja aliyewahi kunishinda mara tatu" Sarah aliongea huku akitabasamu,

"sawa, mimi nitakushinda mara ya tatu, nataka niweke tofauti kati yangu na hao wengine" Aisha aliongea kisha akazimwaga risasi chini na kuitupa pembeni bastola. Sarah alikuwa na wasiwasi kwa kuwa aliutambua uwezo wa Aisha.

"twende sasa" Aisha aliongea huku akikunja ngumi tayari kupambana na Sarah.

Sarah nae akakunja ngumi kisha akaangalia namna Aisha alivyoiweka miguu yake, alimkadiria hatua.

Aisha akamuendea Sarah na kurusha ngumi nyingi za haraka, lakini hakuna hata moja iliyompata Sarah, nyingine alizikwepa na nyingine ziliishia mikononi mwa Sarah,

"umejitahidi" Aisha aliongea huku akitabasamu, kisha akaachia teke kali lililotua kwenye uso wa Sarah, Sarah akapepesuka na kwenda kujikita ukutani,

"hapo vipi?" Aisha aliuliza huku akicheka,

"Moja bila, unaongoza" Sarah alijibu huku akijifuta damu iliyokuwa ikianza kumchuruzika puani, ila kabla hata hajakaa sawa, Aisha akaachia teke jingine kama lile, Sarah akainama na lile teke likapita, Sarah akainuka na ngumi kali iliyotua kwenye pua ya Aisha, Aisha akaenda chini na damu ikaanza kumtoka puani,

"sasa hapo nimesawazisha, matokeo ni moja moja" Sarah aliongea huku akicheka ila Aisha hakutaka kujibu, sura yake ilionesha ana hasira, hakutegemea kupigwa ngumi ile.

Aisha akajinyanyua na kisha akamuendea Sarah kwa pupa, Sarah akaruka juu, Aisha akapita, Aisha alipogeuka alikutana na teke kali la mdomo lililompeleka chini tena, akatema damu,

"ubao wa matokeo unaonesha mbili kwa moja, nipo mbele" Sarah aliongea huku akijiweka sawa kwa ajili ya kuendelea na pambano, Aisha akasimama na kuhisi huenda hilo pigo alilopigwa muda huu ni makosa yake, alimuendea Sarah hovyo. Aisha akajiweka sawa, kisha akarusha ngumi kali, Sarah akainama, Aisha kwa kasi ya ajabu akampiga Sarah kifuti cha tumbo, Sarah akarudi nyuma na kujishika tumbo lake,

"mbili mbili, nimeshajua ni wapi nilikosea" Aisha aliongea kisha akarusha teke jingine, Sarah akaudaka mguu wa Aisha, kisha ule uliobakia ardhini aliupiga teke kali na Aisha akadondoka chini kama mzigo,

"tatu hiyo" Sarah aliongea huku akiwa ameinamisha kichwa, Aisha akanyanyuka kwa mtindo wa ajabu na kuachia ngumi, Sarah akaiona akaachia teke lilikutana na ile ngumi, Aisha akapuliza mkono kutokana na maumivu aliyoyapata, Sarah akaruka juu na kutua kwenye kifua cha Aisha na teke kali, Aisha akaanguka chini, Sarah akamsogelea na kumpa mkono kwa lengo la kumpa msaada ili Aisha asimame, Aisha akaushika mkono wa Sarah kisha akamvuta ili Sarah aanguke chini, Sarah aliliona hilo, alichofanya ni kuupeleka mguu wake ukutani kisha akamvuta Aisha kwa nguvu na Aisha akakutana na kichwa cha pua, Aisha akahisi kizunguzungu, Sarah akamuachia na kisha akamrushia ngumi kali iliyoenda kwenye paji la uso wa Aisha, Aisha pumzi ikakata, akaanguka chini na kupoteza fahamu.

"aaaaagh hii haikutakiwa, kilichotakiwa ni kuendelea kupambana mpaka asubuhi" Sarah aliongea huku akilaani kitendo cha Aisha cha kupoteza fahamu.

Sarah Akaingia chumbani kwa Dokta Pendo na kuangalia kama yupo lakini hakubahatika kumuona, akarudi sebuleni na kufanya kuokota bastola yake, akazirudishia risasi na kutoka zake nje, akaingia ndani ya gari lake na kuliondoa huku akiwa amekata tamaa ya kupata msaada kutoka kwa Dokta Pendo.

Sarah aliendesha gari yake mpaka nyumbani kwake na kuiingiza ndani ya geti, kisha akatelemka haraka haraka na kukimbilia ndani, alielekea moja kwa moja mpaka katika chumba chake cha siri, akafungua mlango na kuwasha taa, akakuta bado Taita amelala hajitambui, Sarah akamtoa machine zilizokuwa puani ambazo zilikuwa zikimsaidia Taita kupumua, kisha akajaribu kumbeba, akashindwa, akataka kumvuta mkono ili ampeleke nje, akashindwa, Sarah akasimama huku akionesha kuna jambo analifikiria, baada ya dakika moja alitoka kwenye kile chumba na kurudi na kiti cha matairi, akakisogeza jirani na kitanda alicholala Taita, kisha akamsukuma Taita na kuangukia kwenye kile kiti cha matairi, kisha Sarah akashusha pumzi ndefu na kukiendea kile kiti, kisha akaanza kukisukuma kuelekea nje, alikisukuma kile kiti cha magurudumu mpaka nje ya nyumba ila ndani ya uzio, akamuweka Taita chini, akamlaza kwenye marumaru. Aliamua kumtoa Taita nje ili apate hewa ya kutosha kwa maana pale nje ni eneo la wazi,

"mbona unataka kufa mapema hivi, tena kifo kirahisi kisicho hata na majeraha?" Sarah aliuliza huku akimuangalia Taita ambaye hakuwa na fahamu,

"ebu subiri" Sarah aliongea huku akielekea getini na kuhakikisha kama amelifunga vizuri, kisha akarudi mpaka kwenye chumba chake cha siri na kuchukua panga kubwa na mkuki, kisha akatoka navyo mpaka alipokuwa amelala Taita,

"si bora nikutoboe macho kisha mwili wako niukate kate vipande, huenda kifo chako kitakuwa cha maumivu" Sarah aliongea huku akiwa amesimama pembeni ya mwili wa Taita na mkononi alikuwa na panga,

"aaaaagh, bora nikakutupe tu, ufe ingawa kifo chako sijakipenda" Sarah aliongea na kutupa lile panga kwa hasira, kisha akaelekea kwenye gari lake na kuingia, akaliwasha na kulisogeza mpaka jirani na mwili wa Taita, kisha akafungua mlango wa nyuma wa gari na kujitahidi kumnyanyua Taita na kumtupia ndani ya gari, kisha na yeye akaingia kwenye gari yake na kuitoa nje ya geti, kisha akatelemka kwenye gari na kurudi kufunga geti, kisha akarudi kwenye gari na kuliondoa.

*******************

Nyakati hizi za usiku, Sajenti Minja alikuwa njiani kuelekea nyumbani kwake, alikuwa ndani ya gari, alipofika maeneo ya mataa ilibidi asimamishe gari kutokana na taa nyekundu zilizopo mbele yake, Sajenti Minja akaisimamisha gari yake na kuangalia magari mengine yaliyoruhusiwa kupita, sasa hapo ndipo akashtuka, aliiona ile Range Rover nyeusi ikikatiza mbele yake, Sajenti Minja akaitupia jicho ile gari.

Taa za barabarani ziliporuhusu upande alipo Sajenti Minja, Sajenti Minja alishika uelekeo ilipoelekea ile Range Rover nyeusi, kwa bahati nzuri aliiona baada ya mwendo mfupi, akaanza kuifuatilia, mara ya kwanza alidhani ile gari ni ya Sarah, ila aligundua namba za ile gari ni zile namba za ile gari ya mwanzo ambayo mmiliki wake alipambana nae kwenye nyumba iliyoungua, kitu ambacho Sajenti Minja hakukijua ni kuwa huyo Sarah na huyo binti waliyepambana naye mwanzo ni mtu yule yule ambaye ni Sarah.

Sajenti Minja akaongeza mwendo wa gari ili aweze kumdhibiti Sarah.

Sarah wakati akiwa anaendesha gari yake, aliweza kugundua kuna gari inamfuatilia, alichofanya ni kuongeza mwendo wa gari yake, aliamini kuwa gari yake ni moja kati ya magari machache yenye kasi, na kwa hilo Sarah alikuwa sahihi, aliweza kuendesha na kuiacha mbali sana gari ya Sajenti Minja, kisha akabadili uelekeo ili kumpoteza kabisa huyo anayemfuatilia, mara ya kwanza alikuwa anaenda beach kumtupa Taita, ila sasa aliamua kwenda dampo, kuna jalala kubwa alilifahamu ambalo lipo kwenye eneo lililojificha na pia lilikuwa likitisha kutokana na vibaka wengi kuishi eneo hilo.

Sarah alivyofika eneo hilo, alishuka kwenye gari na kuanza kukagua mazingira yale kama kuna mtu yoyote anaweza kuwepo kwenye mazingira yale, alijiridhisha hakuna mtu na pia akiwa amejiaminisha kuwa hata yule aliyekuwa akimfuatilia hawezi tena kufika hapo, Sarah alienda kwenye mlango wa nyuma wa gari yake na kuufungua, akamtoa Taita, kwa kuwa hakuwa na nguvu ya kumbeba, alichofanya ni kumbingirisha tu, alimsukuma mpaka kwenye mtelemko uliopo mwishoni mwa dampo, kisha akauachia hapo mwili wa Taita ukiwa unaseleleka kuelekea bondeni, Sarah akawa amechuchumaa akiuangalia namna unavyobingirita,

"dah, sijapenda, amekufa kirahisi sana" Sarah aliongea peke yake kisha akisimama, alipogeuka nyuma akakuta mtu akiwa amesimama kama hatua kumi kutoka alipo yeye na alikuwa akimuangalia, ila kutokana na giza lile ilikuwa ngumu kuonana sura, Sarah akajipapasa kiunononi kuiangalia bastola yake, hakuikuta, akakumbuka ameisahau ndani ya gari, wakati Sarah akiendelea kutafakari huku akijiuliza yule mtu ni nani usiku ule, pembeni ya yule mtu akaongezeka mtu mwingine, Sarah akachoka kabisa, na muda huo wale watu wawili wanaume wakaanza kupiga hatua kuelekea alipo Sarah, Sarah alipotazama nyuma kuangalia njia nyingine, bahati mbaya hakukuta njia, njia ilikuwa moja tu, ambayo ndiyo hiyo iliyo mbele yake na ubaya kuna wanaume wawili walikuwepo wanamfuata.............

*********ITAENDELEA*********

the Legend☆
 
RIWAYA : SALA YA SARAH

MTUNZI : ALEX KILEO

SEHEMU YA THELATHINI NA NNE

ILIPOISHIA.................

Sarah alivyofika eneo hilo, alishuka kwenye gari na kuanza kukagua mazingira yale kama kuna mtu yoyote anaweza kuwepo kwenye mazingira yale, alijiridhisha hakuna mtu na pia akiwa amejiaminisha kuwa hata yule aliyekuwa akimfuatilia hawezi tena kufika hapo, Sarah alienda kwenye mlango wa nyuma wa gari yake na kuufungua, akamtoa Taita, kwa kuwa hakuwa na nguvu ya kumbeba, alichofanya ni kumbingirisha tu, alimsukuma mpaka kwenye mtelemko uliopo mwishoni mwa dampo, kisha akauachia hapo mwili wa Taita ukiwa unaseleleka kuelekea bondeni, Sarah akawa amechuchumaa akiuangalia namna unavyobingirita,

"dah, sijapenda, amekufa kirahisi sana" Sarah aliongea peke yake kisha akisimama, alipogeuka nyuma akakuta mtu akiwa amesimama kama hatua kumi kutoka alipo yeye na alikuwa akimuangalia, ila kutokana na giza lile ilikuwa ngumu kuonana sura, Sarah akajipapasa kiunononi kuiangalia bastola yake, hakuikuta, akakumbuka ameisahau ndani ya gari, wakati Sarah akiendelea kutafakari huku akijiuliza yule mtu ni nani usiku ule, pembeni ya yule mtu akaongezeka mtu mwingine, Sarah akachoka kabisa, na muda huo wale watu wawili wanaume wakaanza kupiga hatua kuelekea alipo Sarah, Sarah alipotazama nyuma kuangalia njia nyingine, bahati mbaya hakukuta njia, njia ilikuwa moja tu, ambayo ndiyo hiyo iliyo mbele yake na ubaya kuna wanaume wawili walikuwepo wanamfuata.............

*********ENDELEA*********

Sarah akaanza kurudi nyuma huku hofu ikimzidi,

"sister saula, hili chaka uliloingia sio" kijana mmoja aliongea kwa sauti nyembamba iliyotokea puani na kumfanya Sarah ajue kuwa huyo ni teja,

"fasta kabla hatujakugeuza bucha" kijana wa pili aliongea huku akivuta panga kutoka kiunoni mwake.

"ngojeni, mnataka nini?" Sarah aliuliza huku akirudi nyuma,

"toa kila kitu sister" kijana wa kwanza alijibu huku akiwa karibu kabisa na Sarah, Sarah akapiga hesabu za haraka haraka kisha kwa kasi ya ajabu akamruka kijana wa kwanza na kutua mbele ya kijana wa pili yule mwenye panga, yule kijana akabaki na mshangao kwa namna Sarah alivyofanya,

"habari yako" Sarah aliongea huku akimuangalia yule kijana kisha Sarah akaachia teke kali lililomkuta yule kijana usawa wa shavu, yule teja akaenda chini na panga likamtoka mkononi, kisha Sarah akapiga sarakasi ndogo na kuokota lile panga kisha akageuka nalo na kumkuta yule kijana mwingine akija kwa kasi huku akiwa na bisibisi mkononi, Sarah akapiga hatua moja kumuelekea kisha akamuwekea panga shingoni kama anataka kumchinja,

"shida nini baba?" Sarah alimuuliza huku akitabasamu, lakini yule kijana hakujibu kitu, alikuwa akitetemeka tu, Sarah akatoa panga shingoni kwa yule kijana kisha akalitupa panga chini na kuondoka zake kwa mwendo wa haraka na kuwaacha wale vijana wakimuangalia tu huku wasiamini kile walichofanyiwa.

Sarah akaelekea kwenye gari lake na kuingia kisha akaliondoa kwa fujo kurudi nyumbani kwake huku akifungua mziki mzito ndani ya gari.

Sarah alifika nyumbani kwake na kukimbilia kwenye kioo na kujiangalia usoni kama amedhurika na mapigo ya Aisha, hakuona jeraha lolote,

"mpumbavu yule, amekariri pigo la aina moja tu, siku nyingine namuua ili huyo Harry apate fundisho" Sarah aliongea huku akielekea kwenye chumba chake cha siri na kukisafisha kisha akaelekea bafuni kuoga huku akiisubiri siku mpya ambayo aliamini itakuja na habari mbaya kumuhusu Taita.

**************.

Aisha alishtuka asubuhi akiwa amelala sakafuni huku akiwa na maumivu na damu baadhi ya sehemu za mwili,. Aisha akajivuta na kusimama, alijitahidi kuinuka ingawa alihisi mwili ukimuuma, akaenda kukaa kwenye kochi na hapo ndipo kumbukumbu zikamrejea juu ya tukio lililomkuta mpaka akafikia katika hali aliyokuwa nayo muda huo,

"kumbe yule mwanamke ni mwendawazimu" Aisha aliongea baada ya kukumbuka alichofanyiwa na Sarah, na hapo akahisi mlango ukigongwa, Aisha akanyanyuka na akauendea mlango kwa tahadhari sana huku mkononi akiwa na bastola yake, nae mgongaji hakuchoka kugonga mlango, aliendelea tu, na safari hii alizidisha nguvu ya ugongaji.

Aisha akausogelea mlango kisha akaangalia na kugundua upo wazi, akapiga hatua tatu nyuma na kuishika vizuri bastola yake, aliielekezea mlangoni,

"karibu, mlango upo wazi" Aisha aliongea huku macho yakiwa mlangoni, mlango ukafunguliwa na kisha mgongaji akaingia ndani,

"wewe ni mimi, usipige risasi" Harry aliongea baada kuingia ndani na kukutana na mdomo wa bastola,

"kumbe ni wewe boss, nilijua yule malaya amerudi tena" Aisha aliongea huku akikaa kwenye kochi, Harry akamtazama sura yake na kuona jinsi ilivyokuwa nyekundu, Harry hakupata tabu kugundua kuwa sura ya Aisha kuwa vile ni kutokana na kipigo,

"nani, Sarah?" Harry aliuliza,

"ndio huyo huyo" Aisha alijibu huku akiangalia pembeni,

"alikuja muda gani?" Harry aliuliza,

"muda mchache baada ya nyinyi kuondoka" Aisha alijibu,

"hujamuua?" Harry aliuliza swali la kizembe,

"wewe mjinga nini, ningekuwa nimemuua ungenikuta nimeshika bastola namna ile?" Aisha aliuliza kwa jazba baada ya kuhisi Harry anamdhiaki,

"ilikuaje sasa?" Harry aliuliza,

"ameingia hapa na nimemdhibiti vizuri tu, ila nimefanya kosa dogo ndio amefanikiwa kunikimbia" Aisha aliongea,

"umemdhibiti au alikudhibiti? kama wewe uliyemdhibiti upo kwenye hali hiyo, je huyo aliyedhibitiwa yupoje?" Harry aliuliza,

"naona imani imepungua kwangu, ni bora niachane tu na kazi yako kama huniamini" Aisha aliongea,

"nakuamini sana Aisha, ila naona kama kazi imekuwa ngumu kwako ila unashindwa kukubaliana na hilo jambo" Harry aliongea,

"mzee unatakiwa utulie, kazi naifanya mimi, nikishindwa nitakurudishia pesa yako uliyonipa hawali" Aisha aliongea kwa jeuri,

"basi yaishe, tunatakiwa kuondoka muda huu, maana hapa sio kwetu" Harry aliongea huku akinyanyuka kwenye kochi na Aisha nae akasimama kisha wakatoka zao ndani ya ile nyumba ya Dokta Pendo na wakaondoka zao.

**** *********

Dokta Pendo alikuwa bado amefungiwa kwenye chumba kidogo ambacho hakikuwa na hewa ya kutosha, na isitoshe alikuwa amepigwa sana kutokana na kiburi chake cha kutosema ukweli kuhusu njia ya kumshika Sarah, Dokta Pendo alikuwa Hoi bin taaban, hawezi kutembea, miguu ilikuwa imevunjwa na Trigger, Dokta Pendo alibakiwa na sauti ya kuongelea,

"ujue mimi nitakuua, sifanyi utani, nipe namba za Sarah" Trigger aliongea huku akiwa amevaa vest iliyokuwa na damu sehemu kubwa,

"niue tu, maana hicho ndicho kilichobakia, niue, unasubiri nini!?" Dokta Pendo aliongea kwa uchungu huku akilia, Trigger akamrushia konde zito na kumpiga Dokta Pendo ngumi ya mdomo, Dokta Pendo akapiga kelele za maumivu,

"kuua ni jambo dogo tu kwangu, tena kwa mtu jeuri kama wewe uwa nafurahi sana ninapokuua" Trigger aliongea huku akitoa tabasamu la kifedhuli bila kujali maumivu anayoyapata Dokta Pendo,

"najua wewe ni muuaji mzuri, na ndio maana mkamuulia Sarah wazazi wake na pia mkamteka babu yake" Dokta Pendo aliongea kwa hasira, alishaamua liwalo na liwe,

"kumbe mnakaaga na kuongea hayo mambo eeh?" Trigger aliuliza huku akiokota kipande cha nondo, alipania kumpiga nacho Dokta Pendo kichwani,

"Niue, nimalize nikapumzike" Dokta Pendo aliongea huku akikilaza kichwa chake sakafuni, alishajikatia tamaa. Trigger akakinyua juu kile kipande cha nondo, Trigger alidhamiria kummaliza Dokta Pendo, Trigger aliinyanyua nondo juu, kisha akawa anajiandaa kuishusha kichwani kwa Dokta Pendo,

"wewe vipi? Usimpige bwana" Harry aliongea huku akiingia mule ndani, aliongozana na Aisha,

"ana kiburi sana, ananijibu hovyo" Trigger aliongea huku nondo ikiwa bado ipo hewani,

"sasa ukimuua si ndio utaharibu kabisa, utakuwa umeharibu mtego wetu" Aisha aliongea huku akimtazama Trigger,

"Trigger hizo bangi unazotumia kwa sasa hazikupeleki vizuri, unakuwaje sijui, yaani hujielewi kabisa" Harry alimlaumu Trigger,

"kumuacha huyu itakuwa kosa kubwa sana" Trigger aliongea huku akiwa bado anaonesha hasira za wazi kwa Dokta Pendo,

"Aisha ebu mchukue huyo dada na umpeleke kule chumba kingine" Harry aliongea kisha Aisha akaenda sehemu alipo Dokta Pendo na kumnyanyua, cha ajabu Dokta Pendo alishindwa kusimama, alikuwa akilia tu,

"Boss, huyu miguu hana tena, tayari imeshavunjwa" Aisha aliongea huku akimtazama Harry,

"dah, Trigger bangi unazovuta sasa hivi zinakukataa, unakuwa kama kichaa, yaani hueleweki kabisa" Harry alimlaumu Trigger ambaye alikuwa akivaa fulana yake,

"huyu sio wa kuwekwa ndani, tuangalie namna ya kumfikisha hospitali" Aisha aliongea kwa huruma,

"huyu tukimpeleka hospitali itakuja kuwa shida kwetu akipona" Trigger aliongea kwa hasira,

"Aisha ebu toka nje mara moja" Harry aliongea huku anamuangalia Aisha, Aisha akaenda zake nje, ingawa alihisi kuna jambo baya linaweza kutokea juu ya Dokta Pendo. Aisha akaenda zake nje,

"wewe unataka tufanye nini? " Harry alimuuliza Trigger,

"huyu afe tu, hakuna njia nyingine" Trigger alijibu,

"usimuue, maana hapo alipo tayari hana uwezo wa kuishi hata siku mbili, cha msingi ni kwenda kumtupa tu" Harry alitoa ushauri,

"sawa, hilo nalo ni wazo zuri" Trigger aliongea,

"sawa, usiku utafanya hivyo" Harry alimwambia Trigger,

"poa" Trigger aliongea kisha wakawa wamemaliza kwa mtindo huo, wakaachana na kila mmoja akaelekea kwenye jukumu lake.

*******************

Asubuhi hii ilimkuta Sajenti Minja akiwa ofisini kwake na mawazo yalikuwa juu ya ile gari nyeusi ambayo inamilikiwa na mwanamke ambaye alimchukulia ni hatari sana, na mbaya zaidi usiku uliopita aliweza kuiona hiyo gari na alijaribu kuifukuzia lakini hakuipata.

Akiwa kwenye mawazo hayo, alishtuliwa na simu yake iliyokuwa inaita, alipotupia macho kwenye kioo cha simu, alikuta jina la bosi wake, akapokea simu haraka,

"naam mkuu" Sajenti Minja aliongea kikakamavu,

"nenda eneo la dampo kuu, kuna mwili wa mtu umeokotwa" Mkuu wa polisi aliongea na kukata simu.

Sajenti Minja akainuka na kutoka mpaka kwenye gari yake, akaingia na safari ya kwenda dampo kuu ikaanza, ilimchukua dakika kumi kufika dampo kuu.

Alishuka na alikuta kuna askari wengine wakiwa eneo hilo, na ndani ya gari walikuwa wameupakia mwili. Sajenti Minja akawasalimu wenzake, kisha akatupia macho kwenye ule mwili, ndipo alipomuona mtu mzima akiwa amelala, alikuwa ni Taita, ila Sajenti Minja hakuweza kumjua kwa kuwa mwili wa Taita ulikuwa umevimba.

"mmepata habari yoyote kuhusu huu mwili?" Sajenti Minja aliuliza,

"kuna vijana wawili wanadai walimuona mtu aliyekuja kuutupa mwili" askari mmoja alijibu,

"wako wapi?" Sajenti Minja aliuliza,

"wale pale waliokaa pale" askari aliongea huku akiwaoneshea kidole,

"kwanini mmewaacha sasa?" Sajenti Minja aliuliza kwa ukali,

"tumewaona ni mateja, tukahisi wanataka pesa tu" askari alijibu,

"wajinga kabisa nyie, huo ndio ushahidi, niwakute ofisini kwangu wale vijana" Sajenti Minja aliongea huku akielekea mahali ilipo gari yake, kisha akaiwasha na kuondoka.

***************/****

Sajenti Minja alirudi ofisini kwake na kuwakuta wale vijana wakiwa nje ya ofisi yake wakimsubiri, Sajenti Minja akawasalimia kisha akawataka waingie ofisini,

"bila kupoteza muda, mnaweza kunieleza chochote kuhusu ule mwili uliookotwa kule dampo kuu?" Sajenti Minja aliuliza huku akiwatupia jicho,

"sisi tuliona gari nyeusi kali, ikipaki, kisha tukamuona mwanamke akishuka na kwenda kufungua mlango wa nyuma wa gari na kumtoa mtu na kwenda kumtupa" Teja wa kwanza alielezea, kipindi chote Sajenti Minja alikuwa amesisimka mwili kutokana na maelezo ya huyo Teja, kwani mtu anayezungumziwa ndiye yule yule anayemtafuta.

"huyo mwanamke mlifanikiwa kumuona kwa karibu?" Sajenti Minja aliuliza,

"tulimuona vizuri ingawa kulikuwa na giza, Maana tulimfuata" Teja wa kwanza alijibu,

"Mimi mpaka gari yake naijua, nimeikariri vizuri tu" Teja wa pili aliongezea,

"namba za gari yake umezikariri?" Sajenti Minja aliuliza,

"sio namba, ile gari nimeikariri tu, range Rover nyeusi" Teja wa pili alijibu,

"majina yenu" Sajenti Minja aliuliza huku akiwaangalia,

"mi naitwa Juma John" Teja wa pili alijibu na Sajenti Minja akaandika,

"andika salum dengo" Teja wa kwanza akajibu na kisha Sajenti Minja akaandika,

"mnaweza kwenda, ila mkimuona huyo dada au mkiiona gari yake, mje mnipe taharifa, nitawapa pesa" Sajenti Minja aliongea,

"usijali kamanda, tutakutimbia tukimdekshia" Teja wa kwanza aliongea huku wakitoka nje na kumuacha Sajenti Minja akiwaangalia huku akitabasamu.

Wale mateja wakatoka mpaka nje ya ofisi, na wakati huo Sarah alikuwa akiegesha gari yake nje ya ofisi za polisi. Wale mateja wakamuona,

"mzeebaba, yule dada si yule pale" Teja wa kwanza aliongea huku akimtazama Sarah aliyekuwa akatelemka kwenye gari,

"ndio yeye, hata gari ndio lile lile" Teja wa pili alijibu,

"wewe baki hapa mtazame anapoelekea, mimi ngoja nikamtonye kamanda" Teja wa kwanza aliongea huku akielekea ofisini kwa Sajenti Minja. Alipofika aliingia moja kwa moja ofisini, mpaka Sajenti Minja akashtuka,

"Baba kama zali, huyo demu Aliyefanya unyambilisi nae ndio anaingia kituoni, yupo hapo nje" Teja alitoa taharifa iliyomsisimua Sajenti Minja,

"yupo nje?" Sajenti Minja aliuliza kama hakusikia vile,

"Babu tuwahi, tusipoteze muda" Teja aliongea huku akigongesha mikono kwa msisitizo.

Sajenti Minja akanyanyuka na kuanza kuelekea nje, huku yule teja akija kwa nyuma yake na mwendo wake wa kutembea bega moja likiwa chini...........

*********ITAENDELEA**********

the Legend☆
 
Mwanzoni ulinipa shida kidogo, sababu nlikua sijakuzoea. But baada ya kukusoma huwezi nipa shida tena. Tutaenda sawa

the Legend☆
Hivyo eeeh?
Na mie nilikusoma nikaona matani sio rangi yako...usije konda bure..nimefurahi kwa kunielewa..
Nakujaaa... mdogo mdogo...
Some time jokes inasaidia..relief...

Sent using Jamii Forums mobile app
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom