RIWAYA : SALA YA SARAH.
MTUNZI : ALEX KILEO.
SEHEMU YA THELATHINI NA MOJA.
ILIPOISHIA......................
Sarah akiwa chooni anajiangalia kwenye kioo, alishangaa mtu akisimama nyuma yake na kutabasamu, Sarah akageuka haraka na kumuangalia,
"hujambo mrembo?" Aisha aliongea huku akimsogelea Sarah, tena usogeleaji wa kishari. Sarah akaona bora aondoke, wakati akapiga hatua ili aondoke alikamatwa shingo na Aisha, Sarah akarusha ngumi ikadakwa kisha akapigwa pingu ya mkono mmoja, aliporusha ngumi ya pili ikadakwa na kuunganishwa katika pingu na mkono wa hawali, Sarah akakosa ujanja.
Alipojaribu kurusha teke, Aisha alimdhibiti kwa kumbana ukutani na kisha akatoa kisu chake mfukoni,
"wewe ndio unasumbua mabosi mjini?" Aisha aliuliza huku akitabasamu kisha kisu akakiweka shingoni kwa Sarah, akaanza kukikandamiza taratibu na damu ikaanza kumchuruzika Sarah, Sarah machozi yakaanza kumtoka na kuona ndoto yake ya kulipa kisasi ikimalizwa chooni, tena na mwanamke mwenzake ambaye hata hamjui.................
************ENDELEA************
Ila kile kisu hakikuingia sana shingoni mwa Sarah, kiliingia kidogo na ndio maana kikasababisha ile damu shingoni mwa Sarah.
Aisha akakitoa kile kisu shingoni kwa Sarah na kisha akamuachia Sarah miguu yake, Aisha akaelekea moja kwa moja sehemu ambapo ziliwekwa toilet paper, akakata kipande kidogo na kisha akafutia damu iliyokuwepo kwenye kisu chake.
Muda wote Sarah alijitahidi kujishika shingoni na Mikono yake ingawa alifungwa pingu.
"bahati yako bado sijalipwa pesa yangu, maana siuagi mtu bila kukamilishiwa madai yangu ya hawali" Aisha aliongea huku akimfuata Sarah, alipomfikia alifungua pingu alizomfunga na kuziweka mahali pake, Aisha akawa anapiga hatua ili aondoke, Sarah akamuwahi na kumrushia teke, Aisha akamkwepa, Sarah akaona Kama amedharauliwa vile kwa kufanyiwa udhalilishaji ule na Aisha.
Sarah akarusha ngumi, Aisha akaikwepa tena na kufanya mkono wa Sarah uangukie mgongoni kwake, alichokifanya Aisha ni kukimata kichwa cha Sarah na kukibamiza kwenye kioo cha pale chooni, mpaka kile kioo kikapasuka,
"hao wapuuzi wanavyokusifia nilidhani labda unajua sana kupambana, kumbe fala tu" Aisha aliongea huku akijipangusa mikono yake kisha akawa anatoka zake kuelekea nje.
Sarah akajibandua pale kwenye kioo na kuona damu kidogo ikimchuruzika kwenye kichwa juu ya sikio, akatoa kitambaa chake na kujifuta, kisha nae akatoka nje, ndipo alipomshuhudia kwa mbali Aisha akiondoka kwa mwendo wa madaha huku baadhi ya wanaume wakwale wakimtupia jicho la matamanio kutokana na umbo lake la kike kumvaa vyema, Sarah akajikuta anawachukia wale wanaume bila ya sababu ya msingi,
"wangejua kuwa lile lijanamke ni likatili wala wasingethubu kuliangalia kwa matamanio hivyo" Sarah aliongea peke yake na kumalizia na sonyo la chini chini.
Sarah nae akaamua aelekee nje ili kumuwahi Aisha ili amfuatilie anapoelekea. Sarah akatembea kwa mwendo wa haraka mpaka nje ya mgahawa, akatupa jicho kushoto hakumuona Aisha, akatupa jicho kulia pia hakuona mtu, akasimama kwa muda huku akijilaumu kwa kuchelewa kutoka nje, mwisho nae akaamua aondoke zake, akaelekea sehemu alipoegesha gari lake, uwa anaegesha mbali sana na eneo ambalo huenda.
Sarah alivyopotea eneo lile ndio muda ambao aliibuka Aisha baada ya kujificha katika kichochoro kimoja eneo lile, Aisha uwa hatumiii gari pindi anapokuwa mjini, uwa anatumia njia za mkato sana, ni mwanamke ambaye amezoea sana maisha ya uswahilini na hata tabia zake ni za kiswahili tu.
Aisha alipotoka mafichoni, aliangalia uelekeo alioelekea Sarah kisha akatabasamu huku akitikisa kichwa, alafu mdogo mdogo akaingia zake kichochoni na safari ya kwenda anapopajua yeye ikaanza.
*****************
Sarah alipofika kwenye gari yake aliingia na kufungua eneo la mbele na kutoa dawa, akachukua pamba na kuanza kuipaka kwenye eneo la shingoni na kichwani juu ya sikio ambalo alijeruhiwa na Aisha.
Sarah alipomaliza kujipa huduma ya kwanza, aliwasha gari lake na kuondoka, alikuwa anarudi kwake,
"yule mwanamke ni nani?, alafu ametumwa na nani?" Sarah alijiuliza wakati akiendesha gari yake,
"hii vita inaanza kuwa nzito, maana wanaingizwa wapambanaji, tena wenye uwezo mkubwa" Sarah aliongea huku akimfikiria Aisha namna alivyomdhibiti kiurahisi.
Sarah aliingia nyumbani kwake huku akiwa na hasira, alipofika sebuleni hakutaka hata kupoteza muda, alivua viatu tu na kisha moja kwa moja na kuelekea kwenye chumba cha siri, huku mkononi akiwa amebeba chakula kwa ajili ya mjomba wake, bwana Taita.
Alifika ndani ya chumba na kuwasha taa, Taita alikuwa amelala sakafuni huku akiwa bado amefungwa kamba,
"Sarah hivi si uniachie tu, umetaka hela nimekupa, lakini huniachii, kwanini?" Taita aliuliza kwa upole,
"hela yako naweza kukurudishia, tatizo sio hela, suala la kukuachia ni mimi mwenyewe nikiamua na wala sio pesa yako" Sarah alijibu huku akimfungua Taita ili ale chakula alichomletea,
"basi kama tatizo sio pesa, niache nikafanye shughuli zangu, biashara zangu zinakwama uraiani" Taita aliongea kwa kulalamika,
"ngoja nikuulize kitu, hivi Katika kambi yenu kuna mwanamke hata mmoja?" Sarah alimuuliza Taita,
"mwanamke????? Hapana" Taita alijibu huku akifakamia chakula,
"kuna mwanamke alinivamia leo na kudai ametumwa, sasa ametekwa wapi huyo mwanamke?" Sarah alimuuliza Taita,
"Mimi sijui kwa kweli, kwani wewe unapambana na maadui wangapi?" Taita aliuliza,
"sina adui mimi" Sarah alijibu,
"sasa kama huna adui si uniachie" Taita aliongea,
"nitakuachia, ila siku ninayokuachia itabidi na babu yangu na mwanae wawe huru" Sarah aliongea,
"mbona baba mdogo alishaachiwa, ila babu yako ndio bado" Taita aliongea kwa kujiamini,
"sawa kama mmemuachia, ila mimi shida yangu ni babu" Sarah aliongea,
"nipe simu niwaambie wamuachie" Taita aliongea,
"hupaswi kuwa na haraka, hii shughuli ina utaratibu wake" Sarah aliongea huku akisimama,
"mama mbona unaondoka? Ina maana ndio na leo huniachii?" Taita alilalamika wakati Sarah akitoka, ila leo hakutaka kumfunga Taita Mikono, alimuacha huru tu.
Sarah akaenda sebuleni na kumpigia simu Harry,
"Sarah naongea" Sarah alijitambulisha baada ya Harry kupokea,
"nakusikilza" Harry alijibu huku akipata hofu,
"kesho kutwa naomba tuonane, kuna kitu nataka unisaidie" Sarah aliongea na kufanya Harry ajiulize ni kweli Sarah anahitaji msaada au mtego,
"sawa, tutaonana wapi?" Harry aliuliza,
"sema wewe, nitakuja popote kwa kuwa nina shida" Sarah aliongea kwa utulivu,
"ok, tutakutana Vin hotel, saa mbili usiku" Harry aliongea,
"na iwe hivyo, usiniangushe mwanasheria" Sarah aliongea,
"usijali" Harry aliongea kisha Sarah akakata simu, akatabasamu,
"wewe si ni mwanasheria? Utanisaidia kesi yangu sasa" Sarah aliongea peke yake kisha akatupa simu mezani.
*******************
Siku nyingine tena, Aisha alikutana na Harry katika mgahawa ule ule waliokutana hawali,
"nilikutana na msichana wako, nimemjaribu kabisa, ni mwepesi mno, basi tu sikutaka kumuua" Aisha aliongea huku akitabasamu,
"Sarah??" Harry aliuliza,
"ndio huyo huyo, hana lolote mpaka nikahisi pesa yako naila bure tu, maana hata kupambana hawezi" Aisha aliongea kwa dharau,
"huyo atakuwa sio yeye, ulipambana na mwingine" Harry aliongea huku akiwa haamini,
"kama huamini sawa, ngoja muda ufike tu" Aisha aliongea,
"sasa kwanini hujamuua?" Harry aliuliza,
"uwa siui mpaka malipo yakamilike" Aisha alijibu,
"ungeua tu, au hatuaminiani?" Harry aliuliza,
"kazi haramu hazihitaji kuaminiana" Aisha alijibu,
"sawa, ila sasa tayari nimeshakamilisha malipo yako, na kama utaweza leo usiku anza kazi, nitakutana mahala na Sarah, anadai anataka tuongee" Harry aliongea,
"haina shida, kwa kuwa malipo umekamilisha leo, basi na kazi itaisha leo" Aisha aliongea kwa kujiamini,
"basi sawa, saa mbili usiku nitakuwa nae Vin hotel, uje pale" Harry aliongea,
"nitakuja ila hatutaonana, nitaweka mitego yangu" Aisha aliongea,
"poa, basi baadae, acha niwahi kazini" Harry aliongea huku akisimama na Kuondoka zake, akamuacha Aisha akiendelea kupata juisi.
**************
Mishale ya saa mbili usiku, Sarah akiwa amevaa suruali nyeusi na koti la suti lenye rangi ya njano isiyokoa, alikuwa akiingia pale Vin hotel, alielekea moja kwa moja sehemu ambapo Harry alikuwa amekaa,
"shikamoo" Sarah alimsalimia Harry wakati akikaa,
"marhabaa, Harry aliitikia huku akikishangaa kisarah kilivyo kidogo alafu kinawaendesha,
"bila kupoteza muda, nimekuja kwa jambo moja hapa, nataka nifungue kesi ya mauaji dhidi ya Taita, naomba uwe wakili wangu" Sarah aliongea huku akimtazama Harry, hiyo kauli haikumshangaza tu Harry, ila ilimtisha kabisa, maana alijua kabisa yeye ni mtuhumiwa wa hiyo kesi pia,
"mauaji ya nani?" Harry alituliza akili kisha akauliza,
"vifo vya wazazi wangu" Sarah alijibu na kumuona namna Harry alivyoshtuka,
"hiyo haiwezekani, kama huna cha maana kilichokuleta bora uende tu" Harry aliongea kijeuri,
"kwa hiyo hilo sio la maana?" Sarah aliuliza huku akitabasamu,
"naona huna jipya, siku ukiwa na cha maana utaniita tena" Harry aliongea kijeuri huku akinyanyuka na kuondoka, alijiamini na pia aliamini Sarah hana muda mrefu wa kuishi.
Harry alitoka na kupanda gari yake, akaondoka. Baada ya dakika tano za kuondoka Harry, Sarah alitoka Vin hotel, siku hakuwa na gari, akawa anatembea huku akiamini anaweza kupata bajaj.
Alitembea mwenda mrefu bila kuona bajaj wala boda boda, na kumbuka Vin hotel ilijengwa nje ya mji. Sarah akiwa eneo ambalo kuna miti mingi, ndipo alipoweza kumuona mtu akija nyuma yake, kwa kuwa kulikuwa na giza basi ilikuwa ngumu kumtambua huyo mtu.
Yule mtu akazidi kupiga hatua mpaka akamsogelea Sarah,
"tumekutana tena kwa mara nyingine mrembo" Aisha aliongea na kufanya Sarah amkumbuke, Sarah alishtuka sana,
"ulikuwa unanitafuta, bado hujaridhika na ulichonifanyia?" Sarah alimuuliza,
"nilikuwa sijalipwa, ila leo nimelipwa na nimekuja kuhitimisha kazi" Aisha aliongea,
"hitimisha tu, ruksa" Sarah aliongea na kumfanya Aisha aanze kumsogelea kishari, kwa kujihami Sarah akamrushia ngumi za haraka haraka, Aisha akarudi nyuma, Sarah akamrukia na teke likamkuta Aisha kifuani, akadondoka na kunyanyuka, Sarah akarusha tena ngumi mfululizo, Aisha akarudi nyuma akajikuta ameingia kwenye miti, Sarah akamuendea kasi na kurusha ngumi nyingine, Aisha akamdaka na kuachia kifuti kilichomkuta Sarah tumboni, Sarah akagugumia kwa maumivu,
"wakati unarusha ngumi zako sio kwamba nilikuwa naziogopa, nilitaka nikuvutie huku porini ili nikumalize bila shida" Aisha aliongea kwa dharau, kisha akaachia ngumi mfululizo zilizomkuta Sarah shingoni, Sarah akaenda chini,
"nyanyuka tuendelee" Aisha aliongea huku akizitoa pingu zake mfukoni, Sarah akanyanyuka na kurusha teke kali, Aisha akaudaka mguu wa Sarah kisha akautupa kiufundi, Sarah akajikuta anazunguruka, Aisha akaudaka mkono wa Sarah na kuufunga pingu, Sarah akaona akilegea ataumia, akarusha ngumi kwa ule mkono wake uliobakia, Aisha akainama na kuushika, akautia pingu na ule mkono kisha akamvuta Sarah kwa nyuma na kumtia kabali, Sarah ujanja ukaisha,
"bado sana katika masuala ya kupambana, nenda kajifunzie kuzimu" Aisha aliongea huku akitabasamu na kuchomoa kisu chake, akakipeleka shingoni kwa Sarah, Sarah akataka hata kukurupuka, ila alishindwa, alibanwa kiufundi haswa, kwa mara ya kwanza machozi yakamtoka Sarah katika pambano, hakuwa na msaada ingawa aliuhitaji sana kwa muda huu...........
*********ITAENDELEA***********
the Legend☆