Riwaya: Saa za Giza Totoro

Riwaya: Saa za Giza Totoro

SEHEMU YA 16




ILIPOISHIA:
“Kariakoo!” nilijibu bila kufikiria kwa sababu ukweli ni kwamba sikuwa nakujua Kariakoo wala Posta zaidi ya kuwa nasikia tu kwenye bomba.
“Huyo mtoto wa nani, mbona kama namjua!” alisema yule dereva, mapigo ya moyo yakanilipuka paah!
SASA ENDELEA...
“Kwani we..we ni mwenyeji wa Mku..ranga?”
“Hapana! Mi naishi hapahapa Dar.”
“Basi utakuwa umemfananisha, huyu ni mtoto wa aunt yangu Suzy wa Mkuranga, wamekuja kututembelea.”
“Amefanana na mtoto wa dada mmoja anafanya kazi airport, huwa nawabeba mara kwa mara kama gari lake likiwa na matatizo,” alisema yule dereva teksi, mapigo ya moyo yakazidi kunienda mbio.
Kwa ilivyoonesha hakuwa amekosea, mtoto aliyekuwa akimzungumzia ndiyo huyohuyo kwa sababu hata mle ndani ya gari wakati nafanya usafi niliona nyaraka zilizoonesha zinahusu Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere.
Ilibidi nibadilishe mada haraka kwani kama tungeendelea kuzungumza, pengine angepata nafasi ya kumtazama vizuri na pengine kupata uthibitisho kwamba alichokuwa anakihisi ndiyo ukweli.
“Siku hizi Dar foleni imepungua kidogo eeh!”
“Imepungua wapi wakati ndiyo inazidi kuongezeka, yaani zamani mimi nilikuwa naweza kuiga tripu kibao lakini siku hizi, mpaka hesabu ya bosi nashindwa kukamilisha, hakuna kabisa kazi kwa sababu ya foleni,” alisema yule dereva huku gari likiendelea kuchanja mbuga.
Safari iliendelea mpaka tulipofika Kariakoo. Katika kumbukumbu zangu, niliwahi kufika Kariakoo si zaidi ya mara tatu na nakumbuka tulikuwa tukienda kununuliwa nguo za sikukuu na baba kabla hajaanza kuumwa. Kwa hiyo sikuwa naijua vizuri Kariakoo lakini niliamini lazima nitapata majibu.
“Nikushushie sehemu gani?”
“Sehemu yoyote ambayo haina msongamano wa watu wengi, si unajua nina mtoto.”
“Kwani mtoto unampeleka wapi?”
“Nampeleka kwa mama yake, kuna sehemu anatusubiri nikishuka nitampigia simu anielekeze sehemu ya kukutana naye.”
“Sasa kwa nini usipige tu ukiwa bado ndani ya gari? Unajua kutembea na mtoto Kariakoo ni hatari, si unaona watu walivyo wengi.”
“Simu yangu haina vocha, mpaka niteremke nikanunue,” nilimjibu dereva huku nikitoa noti mbili za shilingi elgu kumikumi na kumpa. Niliona nikiendelea kushangaashangaa anaweza kunishtukia, kabla hata hajanijibu vizuri tayari nilishafungua mlango, nikashuka harakaharaka nikiwa nimembeba vizuri yule mtoto.
Hapo tulikuwa kwenye Mataa ya Shule ya Uhuru, nadhani alinishtukia kwa sababu hata nilipoteremka, hakuondoa gari, akawa anaendelea kunitazama naelekea wapi, harakaharaka nikajichanganya kwenye watu wengi na kumuacha kwenye mataa.
Nilikuwa natetemeka mno maana kama ningeshtukiwa sijui nini kingetokea, lazima ningekamatwa na katika kuutafuta ukweli, ingeweza kubainika kwamba mama wa mtoto huyo ameuawa na pengine huo ndiyo ungekuwa mwisho wangu wa kukaa uraiani.
Nilipofika mbali kidogo, niligeuka na kuitazama ile teksi, bado yule dereva alikuwa amesimama palepale kwenye mataa, nikazidi kuongeza mwendo na kutokomea ndanindani kabisa kwenye mitaa ya Kariakoo.
Nilizunguka sana nikiwa hata sielewi naelekea wapi, tukio la yule dereva teksi lilikuwa limenichanganya kabisa kichwa changu. Wanawake wengi niliokuwa napishana nao, walikuwa wakinishangaa kwa nini natembea na mtoto kwenye jua na kwenye maeneo yenye msongamano mkubwa wa watu, hali iliyonipa wakati mgumu sana.
Mara nilipata wazo, nikasogea kwenye duka moja la vipodozi ambalo wauzaji wake wengi walikuwa ni wanawake.
“Shikamoo mama,” nilimwamkia mwanamke mmoja aliyekuwa kama na asili ya ushombeshombe hivi, akaniitikia kwa uchangamfu.
“Samahani, eti hapa kuna choo cha kulipia jirani?” nilimuuliza kimitego.
Bila kujua malengo yangu, alinielekeza mahali kulipokuwa na choo cha kulipia, nikamuomba anishikie mtoto mara moja kwa sababu nisingeweza kwenda naye.
“Mlete tu, haina shida! Mama yake yuko wapi?”
“Yupo pale dukani anachaguachagua nguo,” nilimdanganya, akanipokea mtoto kwa uchangamfu na kuanza kumrusharusha juu, nikaona hiyo ndiyo chansi niliyokuwa naisubiri. Nilitoka na kujifanya nafuata maelekezo ya kule alikonielekeza kwamba ndiyo kuna choo.
Nilitembea harakaharaka, nilipofika eneo hilo nililoelekezwa, niligeuka nyuma kuangalia kama alikuwa akinitazama, wala hakuwa na habari na mimi, akawa anaendelea kucheza na yule mtoto. Nikajichanganya kwenye watu wengi na kuongeza mwendo, nikapotelea kwenye mitaa ya ndanindani.
Nilikatiza mitaa kwa kasi na baadaye nikatokea barabarani, harakaharaka nikasimamisha bodaboda.
“Nipeleke kwenye kituo cha daladala.”
“Unataka kupanda magari ya kwenda wapi?”
“Gongo la Mboto.”
‘Una hela kamili hapo?”
“Nina noti ya shilingi elfu kumi,” nilimjibu yule dereva wa bodabidam, akawa ni kama anasitasita, akaniambia bodaboda haziruhusiwi Kariakoo kwa hiyo anaweza kukamatwa wakati akinishusha na kuanza kutafuta chenji.
“Au nikupeleke mpaka Buguruni, utanipa buku tatu,” aliniambia, nikakubaliana na wazo hilo, nikapanda na muda mfupi baadaye, tukawa tunaelekea Buguruni. Mara kwa mara nilikuwa nageuka nyuma kutazama kama hakuna mtu yeyote anayetufuatilia, bodaboda ikazidi kupasua lami huku nikimsisitiza dereva kuongeza kasi.
Hatimaye tulifika Buguruni, akanishusha na kunirudishia chenji, harakaharaka nikajichanganya kwenye kundi la watu huku nikiwa bado natetemeka sana. Sikujua nini itakuwa hatma ya yule mtoto lakini niliamini tayari yupo kwenye mikono salama kwa sababu wanawake huwa wana huruma sana kwa watoto, tofauti na wanaume.
Niliulizia mahali pa kupata magari ya Gongo la Mboto, msamaria mmoja akanielekeza, basi harakaharaka nikaelekea kituoni, nikapanda kwenye gari na safari ikaanza. Nilienda kushukia Mombasa, nikachukua bodaboda na safari ya kurudi kambini ikaanza.
Hata sikuwa napajua panaitwaje lakini nilimuelekeza dereva kwamba twende nikifika ninapokwenda nitamwambia. Kweli tuliondoka kwa kasi na baada ya kama dakika thelathini, tukawa tumekaribia. Kwa kuwa sikutaka ushahidi, nilimwambia asimame, nikamlipa fedha zake kisha nikaanza kutembea kwa miguu kuelekea pale kambini.
Kwa kuwa tayari nilikuwa najua kwamba ukisogelea tu eneo hilo unaonekana na kamera zilizokuwa zimefungwa kitaalamu kiasi kwamba ni vigumu kwa mtu asiyehusika kujua kwamba kuna kamera, nilikuwa makini na kila kitu nilichokuwa nakifanya.
Nilipofika tu getini, kabla hata sijagonga, mlango mdogo wa pembeni ulifunguka, mlinzi mwenye silaha, aliyevalia sare maalum alinikaribisha kwa kunionesha tu ishara kwamba niingie, nilipoingia geti lilijifunga, nikashusha pumzi ndefu wakati nikitembea harakaharaka kuelekea kule ndani.
Kwa jinsi jengo hili lilivyojengwa, unapoingia tu unaweza kudhani kwamba ni karakana au gereji kubwa na ukiingia unawaona kabisa mafundi waliovaia sare maalum wakiwa bize na kazi zao, nadhani bosi Mute alifanya hivi kwa makusudi kabisa ili kuwapoteza ‘maboya’ watu wanaomfuatilia.
Kwa ndani kulikuwa na geti jingine na huko ndiko mambo yote yalikokuwa yakifanyika. Basi nilipoingia kwenye geti la pili tu, kila mtu aliacha alichokuwa anakifanya, wote wakawa wananitazama.
Kwa mbali nilimuona Bonta akifanya mazoezi ya kunyanyua vitu vizito na wenzake, akanipa ishara kwamba nimfuate pale alipo. Basi niliwapita watu wote bila kumsemesha mtu yeyote, nikaenda mpaka pale Bonta alipokuwa. Nilipomkaribia tu, simu yake ilianza kuita, akaitoa na kuipokea, nikamsikia akisema neno moja tu, ‘sawa’.
“Bosi anakuita, nifuate,” aliniambia, nikagundua kwamba lazima ile simu imetoka kwa Bosi Mute. Tukawa tunatembea kuelekea kulekwenye geti la tatu, ambako kuna ulinzi mkali zaidi.
“Umefikia wapi?”
“Nimekamilisha.”
“Umempeleka wapi?”
“Kariakoo.”
“Umeamuacha kwenye mazingira gani?”
“Kuna mama mmoja muuzaji wa duka la vipodozi ndiyo nimeamuachia.”
“Ulitumia mbinu gani?”
“Nilijifanya nataka kwenda chooni, akanipokea,” nilimwambia, akanitazama usoni kisha akaachia tabasamu, akanipigapiga begani na kuniambia: “Safi sana, naamini bosi atafurahi sana.”
Tuliingia kule ndani, kama kawaida tukakaguliwa na vifaa maalum, tukaingia sehemu ya pili kwenye jengo lenye vioo vitupu, milango ikafunguka yenyewe na kuingia mpaka ndani. Tulienda moja kwa moja mpaka kwenye ofisi ya Bosi Mute.
Tulipoingia tu, alisimama pale alipokuwa amekaa akichezea laptop yake, akatusogelea ambapo Bonta aliinama kutoa heshima, na mimi nikafanya hivyo.
“Nipe ripoti,” alisema, nikashusha pumzi ndefu na kumueleza kama nilivyomueleza Bonta, akafurahi sana ambapo kwa mara ya kwanza nililiona tabasamu kwenye uso wake.
“Karibu sana kwenye himaya yangu, kuanzia sasa utakuwa mwanachama kamili,” alisema huku akinipa mkono, akaniambia taratibu zote za kazi nitapewa na Bonta na kama kuna chochite nahitaji kujua kutoka kwake, milango iko wazi.
Alisogea kwenye kabati la ukutani, akafungua na kutoa burungutu la fedha, akampa Bonta na kumueleza maneno fulani kwa sauti ya chini ambayo mimi sikuyasikia, Bonta akawa anatingisha tu kichwa kuonesha kumuelewa.
“Kwa sasa nakuruhusu ukapumzike, maelezo yote nimempa kiongozi wako hapa,” aliniambia huku akitoa burungutu jingine la fedha na kunikabidhi, nikamshukuru sana huku moyoni nikiwa na furaha kubwa.
“Bosi anasema nikakutafutie chumba kizuri cha kupanga na kununua vitu vyote muhimu unavyotakiwa kuwa navyo ili kuanza maisha ya kujitegemea,” aliniambia Bonta wakati tukiwa tunatoka.
Suruali niliyovaa ilianza kunibana kwani upande wa kushoto kulikuwa na burungutu la fedha alizonipa mwanzo naupande wa pili kulikuwa na burungutu jingine alilonipa muda huo. Moyo wangu ulikuwa na furaha kubwa sana, nikawa najiambia ‘maisha si ndiyo haya!’.
Je, nini kitafuatia?
 
SEHEMU YA 17


ILIPOISHIA:
“Maisha yenyewe mafupi haya, jiachie mdogo wangu, kula bata!” alisema wakati tukiondoka na Bajaj, nikaishia kucheka tu. Moyoni nilijiona kuwa na deni kubwa kwa Bonta mwenyewe na kubwa zaidi kwa Bosi Mute, nikajiapiza kwamba nitafanya chochote atakachoniaagiza, hata kama kitakuwa ni cha hatari kiasi gani.
SASA ENDELEA...
Safari yetu iliishia kwenye Baa ya Cheers, iliyopo Sinza Mori, tukateremka kwenye Bajaj, akamlipa dereva fedha zake kisha tukaingia ndani ya baa hiyo iliyokuwa imechangamka kwelikweli. Tulienda mpaka kwenye moja ya meza zilizokuwa ndani kabisa, kwenye kona.
Tulipokaa tu, wahudumu wa kike kama wanne hivi walitufuata na wote wakawa wanamkumbatia na kumbusu Bonta. Ilionesha ni kama wanamfahamu vizuri, basi naye akawa anawachangamkia.
“Huyu ni mdogo wako nini?”
“Mdogo wangu ndiyo, muacheni bado anasoma,” alisema, wakacheka sana na kugosheana mikono, mmoja akanisogelea na katika hali ambayo sikuitarajia, alinikalia kwenye mapaja yangu, akanibusu mdomoni halafu akaninong’oneza:
“Usiogope, hata kama unasoma mimi sitakupokonya madaftari yako.”
Nilijikuta nikiishia kucheka tu, basi akainuka na kuanza kusikiliza oda iliyokuwa inatolewa na Bonta. Wawilikati yao, walivuta viti na kukaa na sisi, wale wengine wawili wakaenda kutuletea oda zetu kama Bonta alivyoagiza.
Muda mfupi baadaye, meza yetu ilikuwa imejaa vyakula na vinywaji. Bonta akawa ananihimiza nile, kunywa, kucheza muziki na hata kama nitataka mwanamke wa kwenda kulala naye mpaka asubuhi, hakuna tatizo. Kiukweli hayakuwa mazingira niliyoyazoea lakini nilijilazimisha kwenda naye sawa ili nisije kuonekana mshamba.
Nilikula kwanza maana nilikuwa na njaa, nikamfakamia kuku wa kuchoma na chipsi mpaka nikashiba kisawasawa, chupa mbili za bia zikafunguliwa kwa mpigo na kusogezwa mbele yangu. Nilianza kunywa lakini kwa tahadhari kubwa ili nisije nikalewa, stori za hapa na pale zikawa zinaendelea.
Mara kwa mara Bonta alikuwa akigusanisha ndimi na yule mhudumu aliyekaa pembeni yake, wakati mwingine akiingiza mkono wake kwenye sketi yake bila hofu. Yalikuwa ni mambo mageni sana kwangu lakini kama nilivyosema, nilijitahidi kutoshangaa sana, nikawa najifanya kama ni mambo ya kawaida kwangu.
Yule mhudumu mwingine aliyekuwa amekaa pembeni yangu, naye alikuwa akinifanyia vituko vya kila aina, lakini nikawa najitahidi kuvishinda vishawishi kwa sababu ukweli ni kwamba sikuwa namjua mwanamke mpaka katika umri huo.
Nilijikaza na kumaliza chupa ya kwanza, nikaanza kuhisi kichwa kinazunguka. Nikaianza ile chupa ya pili na muda mfupi baadaye, tripu za kwenda chooni zilianza, wanywaji wa pombe watakuwa wanajua vizuri ninachomaanisha. Kadiri nilivyokuwa nikiendelea kunywa, ndivyo kichwa kilivyokuwa kikizidi kuzunguka na ndivyo safari za kuelekea chooni zilivyoongezeka.
Nilikuwa nikibanwa na haja ndogo mara kwa mara. Nilimaliza chupa ya pili, zikafunguliwa nyingine mbili, nikaendelea kunywa huku nikijitahidi nisitapike kwani kuna hali isiyo ya kawaida niliianza kuisikia. Ilifikia mahali, nikisimama kwenda chooni napepesuka kwelikweli, yule mhudumu mmoja akawa ananisaidia.
Muda ulizidi kuyoyoma, watu wakazidi kuongezeka kwenye ile baa, muziki nao ukawa unapigwa kwa sauti ya juu huku Bonta akifakamia pombe kama hana akili nzuri. Nilipomaliza chupa nne, tayari nilikuwa ‘nime-flot’, nikaanza kusikia usingizi mzito na haukupita muda, nikalala kwenye meza.
Bonta akawa anacheka sana huku akiniambia kwamba nisijali, nitazoea taratibu. Baadaye sikuelewa tena kilichoendelea, nilipokuja kuzinduka, nilijikuta nikiwa juu ya kitanda, pale kweye makazi yangu mapya. Nilikuwa nimelala na nguo zangu zote vilevile, na kibaya zaidi, nilikuwa pia nimelala na viatu.
Nilikurupuka kitandani na kusimama, bado nilikuwa na pombe kichwani kwa hiyo nikawa napepesuka. Nilijaribu kuvuta kumbukumbu nimefikaje pale? Kumbukumbu zangu ziliishia pale tulipokuwa kule baa, nikiwa nimelewa sana.
Nilisogea dirishani na kuchungulia nje, kulishaanza kupambazuka! Nikatingisha kichwa na kujisikitikia. Nilitoka mpaka sebuleni, nikakuta kuna hotpot limewekwa mezani huku chini yake kukiwa na kikaratasi kilichokuwa na ujumbe.
“Ukiamka kunywa hii supu, kuna soda za kupunguza pombe kwenye friji na maji, kunywa vyote utajisikia vizuri. Pumzika mpaka nitakapokuja kukuchukua,” ulikuwa ni ujumbe ulioandikwa na Bonta kwani chini kabisa aliandika jina lake.
Nilifanya kama alivyoniambia, nilifunua lile hotpot kubwa na kukuta kuna supu imejaa, ikiwa na nyama kibao. Nikafakamia harakaharaka na baadaye nilienda kwenye friji. Japokuwa lilikuwa jipya, lakini lilishaunganishwa kwenye umeme na kuwashwa.
Nililifungua, nikakuta kuna chupa mbili za zile soda nyeupe na chupa nyingine mbili za maji makubwa. Nilifungua soda moja na kuanza kuinywa. Kwa wale waliowahi kunywa zile soda za kupunguza uchovu wa pombe (club soda) watakuwa wanaeleza jinsi zilivyo na ladha mbaya mdomoni.
Nilijilazimisha tu kwa sababu bado nilikuwa nimelewa. Nikanywa ya kwanza na kushushia na chupa nzima ya maji. Angalau sasa nilikuwa najisikia vizuri, nilirudi chumbanim nikavua nguo na kuingia bafuni, nikafungulia ‘bomba la mvua’ na kuanza kujimwagia maji.
Kiukweli nilijisikia raha sana kwa sababu hayo ndiyo maisha niliyokuwa nayaota siku zote. Baada ya kuoga, angalau sasa nilikuwa najisikia vizuri, nikatoka na kuanza kuzungukia nyumba yangu kukagua vitu vilivyonunuliwa kwa ajili yangu.
Kila nilichokuwa nakitazama, nilikuwa nikiishia kuchekacheka tu mwenyewe, nikaenda kukaa kwenye masofa mapya pale sebuleni. Haukupita muda, nikapitiwa tena na usingizi kwani bado nilikuwa na uchovu.
Kilichonizindua, ilikuwa ni mlango wa geti uliokuwa ukifunguliwa, nikafunua pazia na kuchungulia nje, nikamuona Bonta akiingia. Hata sikuwa najua kwamba naye alikuwa na funguo, akaingia na kufungua mlango wa ndani, nikampokea kwa uchangamfu.
“Daah! Mdogo wangu ukilewa unakuwa mkorofi sana,” alisema huku akicheka, akakaa na kuanza kunisimulia vituko vyote nilivyokuwa navifanya jana yake. Niliishia kucheka tu kwa sababu mambo mengine yalikuwa ya aibu.
Aliniambia kwamba bosi amesema siku hiyo nipumzike na kuweka vizuri nyumba yangu.
“Nitakuja kukuchukua kesho asubuhi, funguo zako hizo hapo, ilibidi niondoke nazo kwa sababu za kiusalama,” aliniambia huku akinikabidhi funguo alizozitumia kuingilia mle ndani.
Hakukaa sana, akaniaga na kuinuka huku akinisisitiza kwamba natakiwa kwenda kununua nguo nzuri pamoja na simu. Aliniachia bunda la hela pale mezani, basi nikamshukuru sana na kumsindikiza, alipotoka, nilifunga geti kwa ndani na kurudi tena ndani.
Nilianza kwa kuunganisha TV na redio kwa sababu nilikuwa nahitaji kitu cha kuchangamsha nyumba. Sikupata taabu sana kwa sababu kabla baba hajapatwa na haya matatizo, nyumbani tulikuwa na kila kitu. Baada ya kumaliza kuunganisha, ilibakia kazi ya kumtafuta fundi wa kuja kufunga ‘dish’ na vitu vingine vidogo.
Niliendelea kuweka vitu vizuri, nikahakikisha kila kitu kipo kwenye mpangilio safi, kisha nikaoga tena na kutoka kwa ajili ya kwenda kununua simu na nguo kama Bonta alivyoniambia.
Sikuwa mwenyeji wa mitaa ya Sinza kwa hiyo nilitakiwa kuwa makini. Nilitoka mpaka barabarani na uzuri wake ni kwamba kulikuwa na maduka mengi na kila kitu kilikuwa kinapatikana hapohapo.
Baada ya ‘shopping’ ya nguo kadhaa na viatu, nilimalizia na simu, kwa mara ya kwanza katika maisha yangu nikanunua simu ya kisasa (smartphone), nikasajili laini na kununua vocha, kisha nikapitia chakula na kurudi nyumbani.
Ilikuwa ni siku ya furaha mno kwangu, yaani nilijiona kama maisha nimeshayapatia. Niliweka laini kwenye simu, nikawa naisetiseti pale wakati fundi akiendelea kuniunganishia ‘dish’ ili nianze kufaidi utamu wa runinga kubwa (flat screen) na baada ya muda, tayari nilikuwa hewani.
Nikawa naperuzi simu, huku nikijipiga ‘mapichapicha’ nikiwa mle ndani. Japokuwa chakula nilikuwa nimenunua wala sikuwa na haraka, akili zangu zote zilikuwa kwenye simu na TV. Fundi alimaliza kuunganisha ‘dish’ kule juu ya nyumba, nikamlipa fedha zake na kuondoka, akaniacha nikiwa naendelea kujitanua pale sebuleni.
Nilisikiliza muziki, nilitazama runinga, nilichezea simu na kugalagala kwenye masofa, basi ikawa raha tupu. Muda uliyoyoma kwa kasi, giza likaanza kuingia, nikatoka tena na kwenda kununua chakula na kurudi ndani, nikajifungia na kuendelea kuchekelea mafanikio niliyopata. Laiti kama Mungu anetupa binadamu uwezo wa kuona jambo linaloweza kukutokea hata kesho tu, hata sijui ingekuwaje. Nilikuwa nafurahia lakini sikuwa najua ni nini kilichopo mbele yangu.
Basi siku hiyo ilipita, nikalala usingizi mnono pengine kuliko siku yoyote maishani mwangu. Kesho yake asubuhi niliwahi kuamka na kuanza kujiandaa, nikavaa nguo zangu mpya na viatu na kunifanya nipendeze sana.
Muda mfupi baadaye, nilisikia pikipiki la Bonta likinguruma nje ya geti, akapiga honi na harakaharaka nilizima kila kitu na kuiacha nyumba yangu kwenye mazingira salama, nikatoka mpaka nje na kukutana na Bonta.
Alinisifia sana kwa jinsi nilivyokuwa nimependeza, nikapanda kwenye pikipiki na safari ya kuelekea kazini ikaanza. Njiani tulikuwa tukipiga stori za hapa na pale mpaka tulipofika. Tulipoingia tu, tulikuta kuna magari mawili aina ya Landrover Defender kama zile zinazotumiwa na polisi zikiwa zimepaki.
Mwanzo niliogopa lakini nilipoona Bonta wala hashtuki, nilipiga moyo konde. Tuliingia mpaka ndani na muda mfupi baadaye, bosi Mute aliwaita watu wote kwenye chumba cha mikutano. Upande wa chini wa ile gereji kulikuwa na ukumbi mkubwa, wote tukaingia.
Bosi Mute akatueleza kwa kifupi tu kwamba siku hiyo ilikuwa ni siku ya kazi, kwa hiyo wote watakaochaguliwa kwa ajili ya kazi, wanatakiwa kuelekea uwanja wa mazoezi kwa ajili ya maandalizi. Kwa jinsi alivyokuwa akizungumza kwa mafumbo, hata sikuelewa alikuwa akimaanisha nini.
Basi baada ya hapo, Bosi Mute alitoka na kuacha jukumu la kuchagua nani na nani waende kwenye kazi, kwa viongozi wengine. Bado sikuwa najua jinsi ngazi za uongozi zilivyokuwa ila nilichogundua ni kwamba Bonta naye alikuwa ni miongoni mwa viongozi.
Basi watu wote tuliamriwa kukaa katika mistari miwili. Kulikuwa na zaidi ya watu hamsini mle ndani, kuanzia vijana wadogo kama mimi, vijana wakubwa na wenye miili mikubwa kama Bonta na wazee wachache. Basi ilianza kazi ya kuchaguana pale na baada ya muda, watu 12 tulichaguliwa na mimi nikiwa miongoni mwao.
Wale wengine waliruhusiwa kuendelea na kazi, sisi tukaelekezwa kwenda kwenye yale magari pale nje yaliyokuwa yanatusubiri. Mimi niliingia kwenye gari la nyuma, baada ya wote kuingia, msafara wa yale magari mawili na kigari kingine kidogo (carry), vile vinavyotumia kubeba mizigo, uliianza safari ya kuelekea huko mazoezini.
Tulipofika mbele kidogo, magari yaliachana, kila moja likapita njia yake, la kwetu lilipita ile njia ya siku zote na tukaenda kutokezea Mombasa, likakata kona kushoto na kuwa linaelekea Gongo la Mboto. Tulipita Gongo la Mboto, safari ikaendelea mpakakwenye Msitu wa Kazimzumbwi.
“Tumefika guys,” alisema mmoja kati ya watu waliokuwa wamekaa kule mbele wakati akiakata kona na kuiacha barabara ya lami, tukaingia ndani ya msitu huo mpaka ndanindani kabisa. Nilishangaa kugundua kwamba yale magari mengine mawili, yalishafika kabla yetu na kupaki na watu wote kuteremka.
Je, nini kitafuatia?
 
SEHEMU YA 18




ILIPOISHIA:
Suruali niliyovaa ilianza kunibana kwani upande wa kushoto kulikuwa na burungutu la fedha alizonipa mwanzo naupande wa pili kulikuwa na burungutu jingine alilonipa muda huo. Moyo wangu ulikuwa na furaha kubwa sana, nikawa najiambia ‘maisha si ndiyo haya!’.
SASA ENDELEA...
“Bro, naomba na leo twende nyumbani nikapeleke hela za matibabu ya baba,” nilimwambia Bonta wakati akiwasha pikipiki lake kubwa, akiwa amenipakiza.
“Tufanye kwanza tulichoambiwa na bosi, usijali nitakupeleka,” alisema Bonta, nikafurahi sana ndani ya moyo wangu. Kiukweli hakuna kitu nilichokuwa natamani kukifanya kwa kadiri ya uwezo wangu wote kama kuwasaidia nyumbani.
Hali aliyokuwa nayo baba ilikuwa mbaya sana na mpaka muda huo, mimi ndiye niliyekuwa tegemeo. Japokuwa nilijua kabisa kwamba nimeingia sehemu mbaya, lakini kwa kuwa lengo langu la kuisaidia familia lilikuwa limeanza kutimia, niliamua liwalo na liwe.
Bonta alivuta mafuta kwa nguvu, pikipiki likapiga kelele kwa sauti ya juu na kutoa moshi mwingi, nikawasikia wale wafanyakazi wengine wakipiga miluzi kumshangilia Bonta, akaiondoa kwa kasi kubwa.
Tulitoka getini kwa mikwara ya hali ya juu, Bonta akivuta mafuta kwa nguvu na kufanya mlio wa pikipiki uwe kama wa helikopta mbovu, tukaingia barabarani na safari ikaendelea. Sikuwa najua tunaelekea wapi lakini nilichokuwa najua ni kwamba Bonta anaenda kunisaidia kutafuta sehemu ya kuishi.
Breki ya kwanza ilikuwa ni nyumbani kwa Bonta, Kipawa ambapo alipaki pikipiki, tukashuka na kuingia ndani. Tulipumzika kidogo kisha akaniuliza ningependa kuishi sehemu gani ambayo nitakuwa huru?
Ilibidi tu nimweleze ukweli kwamba Dar mimi ni mgeni, kwa hiyo yeye aangalie sehemu inayoweza kuwa nzuri kwangu.
“Unaonaje ukienda kuishi Sinza? Unajua hapa sheria yetu ni moja kwamba lazima kila sehemu awepo mtu anayeishi, lengo ni kusambaa jiji lote, usione mimi nakaa huku Kipawa, pale kuna watu wanaishi Makumbusho, Mwenge, Tegeta, Tabata, Vingunguti na sehemu nyingine kibao, wala huwa hatukai karibukaribu, hiyo ndiyo falsafa ya bosi,” alisema Bonta, nikawa namsikiliza kwa makini.
Niliunga mkono suala la kwenda kuishi Sinza kwa sababu nimekuwa nikisikia sana sifa za Sinza na kiukweli japokuwa nilikuwa siijui vizuri, sifa zake zilinifanya nitamani kwenda kuishi huko.
Baada ya kukubaliana, Bonta alichukua simu yake na kutafuta namba fulani kisha akaiweka simu sikioni. Kumbe alikuwa amempigia dalali wa vyumba, akamueleza kwamba anataka chumba kizuri Sinza, chenye hadhi nzuri.
“Kwa hiyo jioni saa ngapi?” nilimsikia akimuuliza, kisha akakata simu.
“Vyumba vipo, amesema twende saa kumi jioni,” alisema Bonta, nikashusha pumzi ndefu na kuchekelea ndani ya moyo wangu.
“Na mimi naenda kuwa na kwangu, mbona kama miujiza,” nilijisemea ndani ya moyo wangu huku nikitabasamu. Kiukweli sikuwahi kuishi peke yangu, maisha yangu yote yalikuwa ni nyumbani na sikuwahi kuishi nje ya himaya ya baba na mama.
Hakukuwa na muda wa kupoteza, baada ya kupumzika kidogo, tulitoka na Bonta mpaka Keko ambako aliniambia nichague ‘fenicha’ ninazozitaka. Safari hii tlitumia usafiri wa teksi, ile pikipiki yake akaifungia.
Aliniambia natakiwa kuishi maisha ya juu kama alivyokuwa akiishi yeye. Nilibaki nimepigwa na butwaa na nadhani aliligundua hilo, ikabidi yeye ndiyo awe mstari wa mbele kunichagulia kile alichoona kinanifaa.
Tulianza kwenye vitanda, akachagua kitanda kimoja kikubwa, kilichotengenezwa kwa mtindo wa kisasa, akaniuliza kama nimekipenda, nikajibu kwa kutingisha tu kichwa. Unajua kuna wakati furaha ikinizidi, huwa nashindwa kuongea, nakuwa kama nimebanwa na donge kubwa kooni, kama inavyotokea nikiwa na hasira na njia pekee inayoweza kunisaidia, ni kutoa machozi.
Nilitokwa na machozi ya furaha, Bonta akanitazama na kupigwa na butwaa, ilibidi anivute pembeni na kuniuliza nilikuwa na tatizo gani? Ilibidi tu nimweleze ukweli kwamba siamini kinachofanyika, akacheka sana na kunipigapiga mgongoni, akaniambia ‘yajayo yanafurahisha’.
Nilifuta machozi na kurudi kwenye hali yangu ya kawaida, tuliendelea na shopping ya nguvu, tulinunua pia set ya masofa ya kisasa, kabati la nguo, dressing table na meza ya kulia chakula. Vitu vilikuwa vingi sana, nikawa najiuliza tutavibebaje?
Kumbe alishaweka mipango yake vizuri kwani wakati tunaendelea kuchagua, kuna mtu alimpigia simu, nikamsikia akimwambia kwamba apaki pembeni ya barabara. Baada ya kumaliza, akiwa ameshalipa kila kitu kwa kutumia zile fedha alizopewa na Bosi Mute, tulitoka mpaka barabarani, tukakuta kuna gari aina ya ‘Canter’ limepaki.
Akaenda kuzungumza na dereva, nikaona ameanza kulirudisha nyuma, akalipaki vizuri, vijana wa kubeba mizigo wakamsunguka Bonta ambapo alianza kutoa maagizo kibabe, vile vitu vyote tulivyonunua vikaanza kutolewa na kupelekwa kwenye ile Canter huku sisi tukiwa tumesimama pembeni tukihakikisha kila kitu kinaenda sawa.
Baada ya kumaliza, aliwalipa wale wabeba mizigo, sisi tukaingia ndani ya gari na safari ya kuelekea Sinza ikaanza. Mbele kidogo alimweleza dereva kusimamisha gari, tukashuka tena na kuingai kwenye duka kubwa la vifaa vya nyumbani, tukanunua godoro kubwa na vikorombwezo vingine, yakiwemo mapazia, meza ya vioo, mazulia na vifaa vingine.
Tukarudi kwenye gari na safari ikaendelea. Tulienda mpaka Sinza Madukani ambapo gari lilipaki pembeni, mimi na Bonta tukashuka kwenda kukutana na dalali. Alipotuona, alituchangamkia sana, tukaongozana naye mpaka kwenye nyumba aliyopata.
Unajua fedha zinaleta ujeuri sana! Hebu vuta picha, mnaenda kufanya manunuzi ya vifaa kibao vya ndani wakati hata chumba chenyewe hamjakiona! Ninavyojua mimi, watu wengi huwa wanaenda kwanza kukagua nyumba, kupatana na mwenye nyumba na wakikubaliana kiasi wanachoweza kukimudu cha kodim, ndiyo mambo mengine yanafuatia, lakini kwetu sisi ilikuwa kinyume.
Tulipelekwa mpaka kwenye nyumba moja nzuri, iliyokuwa na geti jeusi. Ilikuwa ni nyumba nzuri kwelikweli, nikisema hivyo naomba nieleweke! Kwanza ilikuwa ikijitegemea kwa kila kitu, kulikuwa na geti la peke yake, ndani kulikuwa na sehemu ya ‘parking’ ya magari, korido kubwa iliyopigwa marumaru safi kabisa.
Tuliingia ndani, kulikuwa na sebule kubwa iliyonakshiwa kwa ‘gypsum’, kulikuwana jiko la kisasa, yale yenye makabati ya ukutani, sinki na bomba la maji, lakini pia kulikuwa na sehemu ya kulia chakula na kulikuwa na chumba kikubwa cha kulala, kilichokuwa na choo na bafu humohumo ndani, wanaita self container.
Pia kulikuwa na vyoo vya jumuiya pembeni na kulikuwa na chumba kingine kidogo ambacho yule dalali alisema kinaweza kutumika kama stoo. Mwanzo wakati akiniambia kuhusu chumba, nilijua labda tunaenda kutafuta chumba kimoja maana nilikuwa mwenyewe tu, lakini ilikuwa tofauti kabisa.
Kiukweli nilifuraahi sana, nikawa naona kila kitu kama ni miujiza kweye maisha yangu. Basi baada ya kuikagua vya kutosha na kuridhika nayo, walianza kujadiliana kuhusu malipo, yule dalali akasema eti ni shilingi laki tatu kwa mwezi na wanataka kodi ya miezi kumi.
Wala Bonta hakushtuka, sanasana akaonesha jeuri nyingine kwa kusema yeye atalipa kwa miezi kumi na mbili, nikawa nacheka mwenyewe.
Hakukuwa na muda wa kupoteza, mwenye nyumba alipigiwa simu, akaja na kuandikishiana mkataba ambao sasa pale kwenye jina la mpangaji, liliandikwa jina langu na hata sahihi niliweka ya kwangu, yule mwenye nyumba akawa ananitazama kwa macho ya chinichini, nadhani akiwa haamini kama mimi ndiyo mhusika mwenyewe kwa sababu nilikuwa sifanani kabisa na ‘fujo’ zile za fedha.
Baada ya kukamilisha kila kitu, Bonta alitoa fedha, wakahesabiana pale kisha tukakabishiwa funguo, mwenye nyumba akaondoka zake akiwa anachekacheka tu mwenyewe.
Kwa kuwa nyumba ilikuwa safi sana, hakukuwa na haja ya kufanya usafi, Bonta akamuagiza dalali atafute watu wa kutusaidia kushusha vyombo, tukatoka mpaka barabarani kumchukua yule dereva wa ‘Canter.
Tuliporudi naye mpaka pale kwenye ile nyumba, tayari vijana wenye nguvu kama sita hivi walikuwa wameshajipanga, wanasubiri kushusha mizigo. Kazi ikaanza ambapo Bonta alinisaidia kupanga namna vitu hivyo vitakavyopangiliwa mle ndani.
Kazi ikafanyika haraka na mpaka inafika saa kumi na moja, kila kitu kilikuwa kimeshakamilika, akaniambia twende tukajipongeze kidogo kwenye baa iliyopo jirani, tukafunga vizuri milango na kutoka naye mpaka barabarani, tukaingia kwenye Bajaj na kumuelekeza dereva atupeleke sehemu aliyomtajia ambayo sikuwa naijua.
“Maisha yenyewe mafupi haya, jiachie mdogo wangu, kula bata!” alisema wakati tukiondoka na Bajaj, nikaishia kucheka tu. Moyoni nilijiona kuwa na deni kubwa kwa Bonta mwenyewe na kubwa zaidi kwa Bosi Mute, nikajiapiza kwamba nitafanya chochote atakachoniaagiza, hata kama kitakuwa ni cha hatari kiasi gani.
Je, nini kitafuatia?

Sent using Jamii Forums mobile app
 
SEHEMU YA 19



ILIPOISHIA:
“Tumefika guys,” alisema mmoja kati ya watu waliokuwa wamekaa kule mbele wakati akiakata kona na kuiacha barabara ya lami, tukaingia ndani ya msitu huo mpaka ndanindani kabisa. Nilishangaa kugundua kwamba yale magari mengine mawili, yalishafika kabla yetu na kupaki na watu wote kuteremka.
SASA ENDELEA...
Baada ya wote kuteremka kwenye gari, tulipangwa kwenye mstari mmoja, mwanaume mmoja aliteremka kutoka kwenye lile gari dogo (kirikuu), akatusogelea na kuanza kututazama mmoja baada ya mwingine usoni.
Alikuwa kimya kabisa huku akiwa ‘sirias’ sana, uso wake ukiwa na ndita kibao. Akawa anatutazama mmoja baada ya mwingine usoni na kuhamia kwa mwingine.
“Guys, kutaneni na Mamba, huyu ndiyo mwalimu wa somo letu la leo,” alisema Bonta huku mara kwa mara akinitazama. Yule mwanaume alisogea mbele na kwa muda wa kama dakika mbili hivi, alikuwa kimya kama anayefikiria aanzie wapi.
“Naitwa Mamba! Hapa tumekuja kazini, ambaye anajiona hawezi kazi ni bora aseme mapema, vinginevyo ataliwa na mamba,” alisema kwa sauti nzito na kavu.
Baada ya kusema maneno hayo, alitoa ishara kwa watu waliokuwa ndani ya like gari dogo, wanaume wanne wakateremka, nikawa najiuliza walitoshaje kwenye kigari kidogo kama kile?
Waliteremsha masanduku mawili ya chuma kutoka kwenye kile kigari, wakayasogeza mpaka pale tulipokuwa tumejipanga. Yule mwanaume aliyejitambulisha kama Mamba, japokuwa sijui kama lilikuwa jina lake halisi au la, alifungua sanduku la kwanza, akainama huku akitutazama usoni, akawa ni kama ameshika kitu ndani ya lile sanduku lakini anatupima kuona tutafanya nini atakapokitoa.
Lahaula! Aliinuka na bunduki, zile ndefu kama zinazotumika vitani, akaikoki na kuikamata kama anayetaka kufyatua risasi. Hofu niliyoipata ilikuwa kubwa mno, bado kidogo nitokwe na haja ndogo, bunduki inatisha sana, isikieni tu.
“Hiki ndiyo kifaa cha wanaume! Nikisema wanaumee, wote mnaitikia eeeh! Wanaumee!”
“Eeeh!” wote tuliitikia. Sijui kama na wenzangu walikuwa na hofu kama yangu kwa sababu nakumbuka hata hiyo itikia yangu yenyewe, ilikuwa ni ya sauti ya kutetemeka.
“Wanaumeee!”
“Eeeh!”
“Nimewaambia kwamba hapa tumekuja kazini! Kama kuna mtu anamkumbuka mama yake bora aondoke sasa hivi akamsaidie kuchambua matembele,” alisema Mamba. Nilichojifunza ni kwamba alikuwa na maneno ya shombo sana, ambayo yanaweza kukufanya ukajikuta unapatwa na ujasiri kuliko kawaida.
Mpaka muda huo, niliona kama nikiendelea kutetemeka, naweza kuambiwa mimi ni mtoto wa mama, kwa hiyo nikawa najikaza huku nikiwa makini kufuatilia kila kitu.
“Hii inaitwa manati ya mzungu! Wangapi wamewahi kuitumia?” alisema, wachache kati yetu wakainua mikono juu. Kumbe miongoni mwetu kuna watu walishawahi kutumia bunduki, nikawa najiuliza walizitumia wapi, ilikuwaje, inafananaje ukiibeba? Ni kweli niliona bunduki kule kwa Bonta lakini yenyewe ilikuwa ndogo siyo kama ile aliyoishika Mamba.
“Unapoishika, kwanza hutakiwi kuchekacheka kama mtoto wa kike, lakini pia unatakiwa kuwa makini sana kwa sababu uzembe kidogo tu, tena wa sekunde moja tu, unatosha kukubadilisha jina, ukaitwa marehemu,” alisema huku akitembea nayo, safari hii akiwa ameinyanyua na kuielekeza juu, akawa anatusogelea mmojammoja.
Baada ya kuzungukazunguka, alirudi pale kwenye yale masanduku, akaikoki na kutoa risasi ambazo alizikinga kwenye mkono wake, akairudisha kwenye lile sanduku.
“Ili manati ifanye kazi inatakiwa kuwa na nini?”
“Jiweee!” tulijibu wote, akazichambua zile risasi na kuishika moja, akaiinua juu, akatwambia manati ya mzungu haitumii mawe ya kawaida, bali inatumia mawe ya dukani.
“Hii moja inatosha kabisa kuyakatisha maisha yako! Lakini pia inatosha kuyalinda maisha yako,” alisema Mamba na kuanza kutufundisha jinsi bunduki inavyofanya kazi. Alitufundisha kwanza kwa maneno huku akituonesha, akatufundisha namna ya kuweka risasi kwenye bunduki na kuzitoa, pia akatufundisha namna ya kuikoki, yaani kuzitoa risasi kwenye ‘magazini’ na kuziweka kwenye ‘chemba’, waliowahi kutumia bunduki watakuwa wananielewa. Ili risasi ifyatuke, lazima kwanza uikoki bunduki na kile kitendo cha kukoki ndiyo kinachozitoa risasi kwenye ‘magazini’ na kuziweka kwenye ‘chemba’, tayari kwa kufyatua.
Alitufundisha pia namna ya kutoa ‘safety lock’ na kuirudishia. Mwanzo nilikuwa najua kwamba ukipewa bunduki tu, basi wewe kazi yako ni kufyatua risasi kumbe kulikuwa na mambo mengi sana ya kitaalamu. Ndani ya muda mfupi, nilijikuta nikiwa na shauku kubwa sana ya kuishika mwenyewe kwenye mikono yangu.
Basi baada ya kufundishana kwa maneno, sasa ulifika muda wa vitendo, Mamba alituamuru kupita pale kwenye masanduku mmoja baada ya mwingine na kuchukua bunduki. Nilishangaa bunduki nyingi kiasi kile za kututosha wote, wao wanazipata wapi?
Nilichokuwa najua, ni kwamba wanaoweza kubeba bunduki, ni polisi peke yao, sasa iweje wao wawe na bunduki nyingi kiasi hicho? Wamezipata wapi? Bado kichwa changu kilikuwa na maswali mengi kuliko majibu.
Alituelekeza jinsi ya kuzibeba na akatuambia kwamba kwa sababu wengi wetu hatujui namna ya kuzitumia, tunatakiwa kuzielekezea chini ili hata mtu akifanya uzembe kwa bahati mbaya, ajipige mwenyewe miguuni. Wengi wetu tulikuwa tunatetemeka, hiyo ndiyo ilikuwa mara yangu ya kwanza kubeba bunduki.
Basi tulirudi kujipanga na safari hii, tuligeukia upande wa kule msituni ambako hakukuwa na mtu, akaanza kutuelekeza akiwa nyuma yetu, akawa anapita kwa mmojammoja na kumuelekeza namna ya kuishika na kuielekezea mbele.
Mafunzo yaliendelea kwa muda mrefu, hatimaye karibu kila mtu akawa amepata ujuzi wa namna ya kutumia bunduki. Kwa mujibu wa Mamba, hilo lilikuwa ni somo la kwanza, baada ya hapo kila mmoja alirudisha bunduki yake kwenye yale masanduku, wale wanaume wakaja na kuyabeba na kuyasogeza pembeni.
Akatuambia kwamba siku nyingine tukija, tutajifunza namna ya kulenga shabaha, nikajua basi somo limeishia hapo kumbe ndiyo kwanza limeanza. Kilichofuatia yalikuwa ni mafunzo ya ukakamavu, tulianza kwa kupiga pushapu, hapo nikajua kweli Mamba siyo mtu mzuri.
Wengi wetu hatukuwa na mazoezi ya ukakamavu kwa hiyo suala la kupiga pushapu lilikua mtihani mgumu kwelikweli. Unaweza kuchukulia rahisirahisi lakini kupiga pushapu, tena za ngumi kwa kusimamiwa siyo jambo rahisi.
Akawa akisema chini, wote tunaenda chini, akisema juu, wote tunaenda juu, tatizo likawa idadi ya pushapu tulizotakiwa kupiga. Ilifika mahali mikono yangu ikawa inatetemeka huku ikiuma mno, jasho likiwa limenitoka karibu kila sehemu.
Ugumu haukuwa kwangu pekee, nakumbuka kuna mmoja kati yetu alishindwa kabisa kuendelea, akalala chini huku akilia, Mamba akamfuata na kuanza kumpiga mateke kama mwizi huku akimtolea shombo za kutosha.
Kiukweli ilikuwa siku mbaya sana. Tulipiga pushapu zisizo na idadi mpaka ikafikia hatua kila mmoja akawa analia kimyakimya maana Mamba akikusikia unalia, ujue kazi unayo.
Lilifuata zoezi la kuruka kichurachura, nalo likawa gumu kwelikweli kwa karibu kila mtu. Tuliruka kichura mpaka ikafika mahali aliposema tusimame, ikawa hakuna anayeweza kusimama kwa kunyooka jinsi miguu inavyouma.
Bonta na wenzake walikuwa wamekaa pembeni wakiendelea kuvuta sigara na bangi kwa fujo, huku wakicheka sana jinsi Mamba alivyokuwa akituhenyesha. Tuliendelea na mazoezi mengine ya viungo na mpaka tunamaliza, kila mtu alikuwa nyang’anyang’a.
“Kesho tena tukutane hapahapa!” alisema Mamba wakati akihitimisha mafunzo, tukarudi kwenye magari huku kila mtu akiugulia kivyake, hakuna aliyekuwa na stori na mwenzake, magari yakatoka mpaka barabarani, kile kigari kidogo chenyewe kikaelekea upande tofauti na sisi, hata sijui kilielekea wapi ndani yake akiwepo Mamba na timu yake, sisi tukaanza safari ya kurudi mjini.
“Ukitaka uwe mkali, ukifika nyumbani rudia mazoezi yote mliyofundishwa, ukisema ulale, kesho utashindwa hata kuamka,” Bonta aliniambia huku akinipigapiga mgongoni, nadhani alinionea huruma kwani kila kiungo kilikuwa kikitetemeka kutokana na ‘mtiti’ tuliopewa.
Tulirudishwa mpaka kambini na mpaka tunafika, tayari giza lilishaanza kuingia, tukaenda kusaini kwenye daftari maalum kisha kila mtu akapewa shilingi elfu hamsini, tukaruhusiwa kuondoka. Bonta aliniambia hawezi kuongozana na mimi tena, natakiwa kuanza kuzoea mazingira mwenyewe.
Nilitoka nikiwa nachechemea, kilakiungo kikiuma, wenzangu nao wakawa wanaondoka kila mmoja kivyake. Nilipofika mbele kidogo, nilisimamisha bodaboda na kwenda mpaka Mombasa ambako nilipanda daladala mpaka Sinza. Mpaka naingia ndani, ilikuwa ni tayari saa nne za usiku, nikiwa nimechoka vibaya mno.
Nilichoweza kukifanya, ilikuwa ni kuoga tu, usingizi mzito ukanipitia palepale kwenye kochi nilipokaa ili kupumzika kidogo kabla ya kurudia yale mazoezi kama Bonta alivyoniambia. Nilipokuja kuzinduka, tayari kulikuwa kumeshaanza kupambazuka, nikajishangaa imekuwaje?
Je, nini kitaendelea?

Sent using Jamii Forums mobile app
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom