SEHEMU YA 14
ILIPOISHIA:
Ndani ya gari hilo, kulikuwa na mwili wa mwanamke aliyekuwa amepigwa risasi kichwani na kufa papo hapo, lakini siti ya nyuma kulikuwa na mtoto mdogo aliyekuwa amekaa kwenye vile viti maalum vya watoto vinavyofungwa juu ya siti ili kuzuia mtoto asianguke.
SASA ENDELEA...
Nilishtuka kupita kawaida, niligeuka na kutazama huku na kule, kama kawaida, kila mtu alijifanya yuko bize na kazi zake lakini niligundua kwamba karibu wote walikuwa wakinifuatilia kwa makini nitakachokifanya.
Nilifunga mlango haraka, nikanyanyua vifaa vyangu vya kazi na kugeuka huku na kule tena, bado watu walikuwa wakinitazama kwa macho ya chinichini. Kwa kuwa pale mwenyeji wangu alikuwa ni Bonta, ilibidi niweke vifaa vyangu vya usafi na kumfuata.
Alikuwa amekaa kule kwenye vifaa vya mazoezi na mkononi alikuwa na chupa ndogo ya pombe kali huku pia akivuta ‘sigara’. Nilimsogelea mpaka pale alipokuwa amekaa lakini nikagundua kwamba hakuwa akivuta sigara kama nilivyodhani kwa mbali.
Alikuwa akivuta bangi na japokuwa sikuwa nimewahi kuvuta, nilikuwa naijua harufu yake vizuri.
“Braza,” nilimuita huku nikiwa na hofu kubwa ndani ya moyo wangu. Akanionesha kwa ishara kwamba nikae, kweli nikakaa kwenye vile vyuma vya mazoezi huku nikipumua kwa nguvu. Nilishapaniki! Sikia tu hivihivi lakini usiombe kushuhudia aliyefariki kwa kupigwa risasi.
“Huu ni mtihani wa mwisho kwako, bosi anataka kukupima kama una moyo wa kiume,” aliniambia kwa sauti ya chini huku akiendelea kuvuta moshi mwingi na kuumeza kisha kushushia kwa ile pombe iliyoonesha ni kali kwelikweli maana alikuwa akikunja uso anapomeza.
“Pale pembeni ya pipa la taka, kuna mfuko mkubwa, unatakiwa kwenda kuuchukua, utaweka ndani kile ulichokiona kwenye siti ya mbele kisha utaweka juu ya lile toroli. Maelekezo mengine utapewa,” alisema Bonta huku akiwa ‘siriasi’ sana.
Sikuwahi kumuona akiwa kwenye sura kama hiyo, nilishindwa hata nimjibu nini kwani nilihisi mate yakinikauka mdomoni, akanionesha kwa ishara kwamba niiunuke na kuondoka.
Kiukweli kama nisingewahi kushikilia bomba la moja kati ya vifaa vya kufanyia mazoezi, pengine ningeanguka mzima-mzima kwani miguu ilikosa nguvu kabisa, nikawa natetemeka mwili mzima huku miguu ikigongana.
Bonta alinitazama bila kusema chochote, akawa anaendelea kuvuta mibange kwa fujo, nikashusha pumzi ndefu na kusimama vizuri kwa sekunde chache. Sikuwa na uwezo wa kukataa kazi ile ngumu na ya kutisha mno.
Nilipiga moyo konde na kushusha pumzi ndefu kwa mara nyingine, nikaanza kutembea kuelekea kule kwenye pipa la takataka.
Bado nilikuwa najua kwamba watu wote wananitazama na sijui ni nini kilinitokea, lakini nilijikuta nikipata ujasiri wa kuwaonesha waliokuwa wakinitazama kwa macho ya chinichini kwamba na mimi ni mwanaume shupavu.
Nilienda mpaka pale, kweli nikakuta kuna mfuko mkubwa ambao upo katika mfumo wa kama nailoni ngumu, wenye zipu. Nikauchukua na kuelekea kwenye lile gari. Ambacho sikuweza kukizuia ni mapigo yangu ya moyo kwenda mbio.
Basi nilipofika, niliubwaga ule mfuko chini, nikachukua tena vile vifaa vyangu vya kuoshea magari, ikabidi niendelee kujifanya kama naoshaosha lile gari kwa nje. Ilikuwa ni kama kuzuga tu ili nipate ujasiri wa kufanya ile kazi ambayo ama kwa hakika ilikuwa ni mtihani mkubwa mno katika maisha yangu.
Sikutegemea kama naweza kukutana na kitu kama hicho maishani mwangu, kichwani maneno ya mama alipokuwa ananikataza kuja mjini yakawa yanajirudia lakini nilipokumbuka kwamba ni usiku uliopita tu nimetoka kuwaachia kiwango kikubwa cha fedha nyumbani kwa ajili ya matibabu ya baba, nilijikuta nikijiambia ndani ya moyo wangu ‘potelea mbali’.
Nilichukua mfuko na kuuweka vizuri, nikafungua zipu na kuingia nao ndani ya lile gari ambalo lilikuwa likinuka damu, tena damu mbichi. Nilishindwa kumtazama yule mtu kwa jinsi alivyokuwa amefumuliwa kichwa kwa risasi, nikamvalisha ule mfuko huku nikiwa makini nisichafue nguo zangu na damu.
Mwanamke mwenyewe alionesha kuwa mtu wa makamo ya kati, uzuri ni kwamba hakuwa mnene sana kwa hiyo niliweza kumudu kumtoa pale alipokuwa, nikiwa tayari nimeshamvalisha karibu nusu nzima kwenye ule mfuko, kuanzia kichwani mpaka maeneo ya kiunoni.
Huku nikitetemeka, nilitegua siti na kumalizia kumuingiza miguu kwenye ule mfuko, nikaufunga na kuanza kuuvuta kuutoa nje ya gari. Kwa kuwa tayari mwili wote ulikuwa ndani ya ule mfuko, kwa mtu anayetazama kwa mbali angeweza kudhani labda natoa mzigo kwenye gari.
Niliushusha mpaka chini na kuuburuza mpaka pembeni, nikaenda kuchukua lile toroli na kulisogeza huku nikitetemeka mno. Niliunyanyua ule mzigo kwa nguvu zangu zote na kufanikiwa kuuweka juu ya lile toroli. Jasho jingi likawa linanichuruzika mwili mzima.
Nikiwa bado sijui nini cha kufanya, nilishtukia sauti kali ya mtoto akilia kutoka ndani ya lile gari, nikarudi harakaharaka na kufungua mlango wa nyuma, alikuwa akilia akiwa bado palepale kwenye kile kiti chake.
Moyo uliniuma sana kwa sababu nilijua kabisa malaika huyu wa Mungu hana hatia yoyote na mbaya zaidi ni kwamba asingeweza kumuona tena mama yake hapa duniani.
Nilishindwa kuyazuia machozi yasiulowanishe uso wangu. Nikabaki namtazama huku nikiwa hata sijui nifanye nini, machozi yakiendelea kunimwagika kwa wingi. Mara nilishuhudia wanaume wawili waliokuwa wamevalia maovaroli, wakija na kuchukua lile toroli, wakawa wanalisukuma kuelekea upande wa pili.
Sura zao zilikuwa ngeni kabisa kwangu, wakawa wanasukuma toroli bila hata kugeuka nyuma. Mara Bonta naye alikuja na safari hii hakuwa peke yake, alikuwa na wanaume wengine wawili ambao nao sura zao zilikuwa ngeni kwangu. Bonta alikuwa katikati yao, wakanisogelea bila kusema kitu chochote.
Bila kuzungumza chochote, Bonta alinipa ishara kwamba nimtoe yule mtoto kwenye gari, nikafanya hivyo huku bado machozi yakiwa yananibubujika. Nilisimama mbele yao huku nikiwa nimemshika yule mtoto ambaye kwa kumkadiria alikuwa na kama miaka miwili, ambaye alikuwa akiendelea kulia huku akimuita mama yake.
Bonta alimpa ishara mmoja kati ya wale wanaume, nikamuona akifunua koti lake refu, katika hali ambayo sikuitegemea, nilimuona akichomoa bastola, akachomoa na kitu kama kibomba fulani kutoka kwenye mfuko wake mwingine, akawa anakifunga mbele ya mdomo wa bastola kisha akaikoki! Nikabaki nimehamaki nikiwa sijui nini kinachotaka kufanyika.
Nilishangaa yule mwanaume eti akinikabidhi mimi ile bastola, macho yakanitoka pima! Nikamtazama Bonta ambaye sasa hivi alikuwa amebadilika kabisa uso wake, macho yalikuwa mekundu mno.
“Shoot!” alisema, akimaanisha eti nimpige risasi yule mtoto, nikawa narudi nyuma huku nikitingisha kichwa, uso wangu ukiwa umejawa na wasiwasi usiomithilika. Nikiwa naendelea kurudi nyuma, nikiwa hata sijui nataka kufanya nini kwani yule mtoto alikuwa mikononi mwangu lakini pia bastola ilikuwa mkononi mwangu.
Bonta akanipa ishara nitazame upande wa juu, macho yangu yakatua kwa mwanaume aliyekuwa amesimama ghorofani, akiwa ameegamia mabomba ya kwenye ‘balcony’, akivuta sigara na kutoa moshi mwingi. Kwa ilivyoonesha, alikuwepo pale kwa muda mrefu, akifuatilia kila kilichokuwa kikiendelea. Hakuwa mwingine bali bosi Mute.
“Huu ni mtihani wa mwisho kwako, bosi anataka kukupima kama una moyo wa kiume,” maneno aliyoniambia Bonta muda mfupi uliopita yalijirudia kichwani mwangu, nikamtazama Bonta kisha nikamtazama Bosi Mute kule ghorofani, nikawatazama na wale wanaume wengine wawili.
Niligeuka na kutazama huku na kule, kila mtu alikuwa ameacha kila alichokuwa anakifanya na kugeukia pale tulipokuwepo kutazama kilichokuwa kinaendelea. Japo Bonta alikuwa kimya lakini uso wake ni kama ulikuwa unasema ‘mbona unataka kuniangusha?’
Nikiwa bado sijui cha kufanya, nilishtukia wale wanaume wawili wamefyatuka kwa kasi ya upepo, mmoja akanipokonya yule mtoto ambaye bado alikuwa akilia na kumkalisha chini, akamuegamiza kwenye jiwe kubwa la zege, yule mwingine akanishika kwa nguvu na kunirudisha nyuma umbali wa hatua kadhaa.
“Unaishika hivi... kisha unavuta hiki kitufe ukiwa umelenga unapotaka kupiga, vuta pumzi na usizitoe mpaka usikie mlio au mtingishiko kuonesha risasi imetoka,” alisema Bonta ambaye naye alikuwa ameshanisogelea mwilini kabisa na kunishikisha vizuri ile bastola, akakichukua kidole changu kimoja na kukiingiza kwenye ‘trigger’ ya kufyatulia risasi. Kila kitu kilikuwa kikifanyika kwa kasi kubwa mno mpaka nikawa najihisi pengine nipo kwenye ndoto ya kutisha.
“Unatakiwa kufuata maelezo niliyokwambia, vinginevyo kinachoenda kutokea hapa kitakuwa kibaya sana kwenye maisha yako, hebu mtazame tena Bosi Mute,” alisema Bonta, nikageuza shingo na kumtazama kule juu, nikamuona akiwa ametoa bastola na kuielekeza pale tulipokuwepo, Bonta akawageukia wale vijana na kuwapa ishara, wote wakasogea pembeni kabisa.
“Unaweza! Unaweza kabisa, nitazame usoni,” aliniambia Bonta, nikageuka na kumtazama huku nikiendelea kulia, akanipa ishara fulani usoni ya kunitoa wasiwasi na kunihakikishia kwamba ninaweza, akaniambia nielekeze akili zangu pale kwenye tukio vinginevyo bosi Mute atanipiga mimi risasi kwa sababu hawezi kukubali nikatoka nje na kwenda kutoa siri, kwa hiyo sikuwa na cha kufanya zaidi ya kutekeleza nilichoambiwa.
Nilimtazama yule mtoto, bado alikuwa akilia sana huku na yeye akionesha kuwa na hofu kubwa ndani ya moyo wake, kufumba na kufumbua, Bonta naye alikuwa ameshasogea hatua kadhaa na kuniacha nikiwa nimesimama palepale, bastola ikiwa mkononi mwangu na Mute naye akiwa ameshaunyoosha mkono wake weye bastola kunilenga mimi.
“Eeh Mungu wangu, wewe ndiyo unaojua ukweli wa moyo wangu, nisamehe kwa hii dhambi kubwa ninayoenda kuitenda,” nilisema huku nikilia kwa uchungu usiomithilika. Sikuwahi kudhani hata siku moja na mimi nitakuwa muuaji lakini mpaka hapo tulipokuwa tumefikia, nilitakiwa kuchagua jambo moja tu, kuwa muuaji au kuuawa!
Bonta akaanza kunihesabia: “Moja... mbili... ta...!”
Je, nini kitafuatia?
Sent using
Jamii Forums mobile app