Riwaya: Saa za Giza Totoro

SEHEMU YA 13





ILIPOISHIA:
Niliporudi kule chumbani, kitu cha kwanza ilikuwa ni kukagua kama ile bunduki ipo palepale lakini cha ajabu ni kwamba haikuwepo. Kwa tafsiri nyepesi ni kwamba Bonta alikuwa ameichukua, sasa amekwenda nayo wapi usiku woye huo? Sikuwa na majibu.
SASA ENDELEA...
Nilipanda kitandani na kujilaza huku mawazo mengi yakipita ndani ya kichwa changu kwa kasi. Ndani ya kipindi kifupi tu, mambo mengi yalikuwa yametokea kwenye maisha yangu kiasi cha wakati mwingine nijihisi kama nipo kwenye ndoto.
Haukupita muda mrefu, nikapitiwa na usingizi mzito uliosababishwa na uchovu mkali niliokuwa nao. Hata sikujua Bonta amerudi saa ngapi lakini nilipokuja kuzinduka, ilikuwa tayari kumeshapambazuka na Bonta alikuwa amelala pembeni yangu, akikoroma kuonesha kwamba naye amechoka sana.
Niliamka kwa kunyata kwani sikutaka kumuamsha, kitu cha kwanza nikainama pale anapoihifadhi ile bunduki yake na kuigusa. Ilikuwepo mahali pake lakini safari hii ilikuwa na kama harufu ya baruti hivi. Sikuelewa hiyo maana yake ni nini.
Nilitoka na kwenda sebuleni, nikafunua mapazia na kuanza kufanya usafi, ikiwa ni pamoja na kuandaa kifungua kinywa kwani Bonta jana yake alishanipa maelekezo yote kwa hiyo ugeni ulishaanza kupungua. Baada ya hapo, nilienda kuoga na kukaa sebuleni, nikawasha runinga kubwa ya kisasa iliyokuwa ukutani.
Muda mfupi baadaye, Bonta aliamka na kitu cha kwanza alichokifanya ilikuwa ni kwenda kwenye friji, akatoa chupa ya pombe kali na kumimina kwenye glasi, akapiga mafunda kadhaa na alipoishusha glasi, ilikuwa tupu.
Akajinyoosha pale kisha akaelekea bafuni kuoga. Ndani ya dakika chache tu, tayari alikuwa ameshaoga na kubadilisha nguo, akaja pale mezani, tukajumuika kwenye kifungua kinywa.
Baada ya kupata kifungua kinywa, tuliondoka pamoja kwa kutumia pikipiki yake na kwenda mpaka kule kazini, ambapo kulikuwa na umbali kidogo. Kama nilivyoeleza, eneo zima lilikuwa limezungushiwa ukuta mrefu na mpaka ufike ndani kabisa, ilikuwa ni lazima upite kwenye mageti mawili, lile la nje kabisa na linalofuatia.
Bonta aliingiza pikipiki yake mpaka ndani, tukateremka na kuanza kutembea kuelekea ndani huku akisalimiana na watu wengine wengi waliokuwa wakiendelea na shughuli za hapa na pale ndani ya eneo hilo ambalo lilikuwa bize kama gereji, karakana au kiwanda fulani.
“Nisubiri hapo,” alisema Bonta, nikasogea pembeni kwenye kundi la vijana wakubwa waliokuwa wakifanya mazoezi ya kunyanyua vyuma. Kila mmoja alikuwa na mwili mkubwa, kifua kipana na mikono iliyojazia kuonesha wameiva kimazoezi kisawasawa.
Walikuwa wakinitazama kwa macho ya chinichini huku wakiendelea na mazoezi yao, na mimi nikawa nawatazama tu. Upande wa pili kulikuwa na kundi lingine la watu waliokuwa wakifanya mazoezi ambao wao walikuwa ni kama wanacheza ‘karate’, huku wakifundishwa na kiongozi wao.
Kundi jingine la watu, lilikuwa bize kufanya usafi na kuhakikisha mazingira ya humo ndani yanakuwa safi, wengine wakawa wanafagia huku wengine wakimwagilia maua. Dakika chache baadaye, Bonta alirejea na kuniambia kwamba ameenda kuonana na bosi na amefurahi kusikia kwamba tumerudi na umeripoti kazini asubuhi hiyo.
“Amesema wewe itabidi ujifunze ufundi makenika, ameniambia nikuunganishe na mafunzi gereji wengine ili uanze kupata uzoefu,” aliniambia huku tukitembea kuelekea upande wa pili wa eneo hilo.
Moyoni nilifurahi sana kwa sababu sasa nilikuwa na uhakika kwamba nitakuwa na kazi ambayo itanisaidia sana maishani mwangu, ikiwa ni pamoja na kuwasaidia wazazi wangu, hususani baba yangu ambaye sasa alikuwa na hali mbaya sana kitandani.
Kweli Bonta alinipeleka kwenye gereji kubwa iliyokuwa ndani ya jengo hilo na kunikabidhi kwa mzee mmoja wa Kidigo, Shekwavi ambaye aliniambia kwamba ndiyo fundi mkuu. Mzee huyo alinipokea vizuri huku mara kwa mara akiniuliza kama kweli nitaweza kazi.
“Nakuona kama upo legelege sana, na hii kazi inahitaji wanaume na siyo wavulana,” aliniambia kwa kejeli, kauli yake hiyo ikauchoma mno moyo wangu. Ni kweli kwa mwonekano wa nje mtu angeweza kuamini kwamba mimi ni legelege lakini ukweli nilikuwa naujua mwenyewe kwamba mimi ni mwanaume wa shoka.
“Unamuona legelege huyu! Ohoo, muangalie hivyohivyo,” alisema Bonta ambaye alikuwa akizunguka huku na kule akiendelea na kazi ya kukagua kama kazi zilikuwa zikifanyika vizuri.
“Msimulie hiyo alama hapo usoni umeipataje,” alisema Bonta huku akicheka, nikajikuta nikitabasamu kwa sababu kauli yake hiyo ilinikumbusha kuhusu lile tukio la yule kondakta mpuuzi aliyetaka kunieletea ubabe na mwisho akaishia kutimua mbio kama mtoto mdogo.
“Eti umefanya nini kwani?” Mzee Shekwavi alizidi kunidadisi lakini sikuwa tayari kumweleza chochote, hakuna kitu nilichokuwa sikipendi kama kudharauliwa. Basi alipoona nimekasirika, hakutaka kuendelea kunihoji, akaanza kunipangia majukumu ya kazi.
Aliniambia kwa siku hizo za mwanzo, kazi yangu itakuwa ni kuosha magari, nje na ndani huku pia nikisaidia kazi nyingine nitakazokuwa natumwa. Nilikubali na bila kupoteza muda, alinionesha gari dogo lililokuwa pembeni kidogo, akaniambia natakiwa kuanza na gari hilo.
Ainielekeza na vifaa vyote vinavyohusika, ikiwemo mpira maalum wa maji ambao unaunganishwa kwenye bomba na kuongeza presha ya maji, sabuni, dawa maalum za kutoa madoa na vifaa vya kukaushia ndani ya gari.
Binafsi niliiona kama ni kazi nyepesi ambayo haiwezi kunishinda chochote na moyoni nikajiapiza kujifanya kwa moyo wangu wote na kwa nguvu zangu zote. Nilianza kuliosha gari hilo upande wa nje na nilijitahidi sana kuling’arisha, lakini nikagundua kwamba kuna kioo kimoja kilikuwa kimetoka.
Basi sikujali sana, nilipomaliza kulisafisha kwa nje, nilihamia kwa ndani na hapo ndipo nilipogundua vitu vilivyonishtua sana moyo wangu. Kwanza niligundua kwamba kile kioo kilichopasuka, kumbe ni kile kilichopo upande wa dereva kwenye mlango wa mbele, lakini pia upande wa ndani, siti yote ilikuwa imelowa damu ambazo sasa zilikuwa zimekauka huku zikiwa zimechanganyikana na vioo ‘vilivyomwagikia’ kwa ndani.
Yaani kwa mazingira yale, ilitosha kabisa kuelewa kwamba kulikuwa na tukio baya lililohusisha gari hilo. Ilibidi nijikaze kiume na kuendelea na kazi kwani kuna wakati nilimuona mzee Shekwavi akinitazama kwa macho ya kuibia.
Nadhani alikuwa anajua kila kitu lakini akataka kuona nitachukua uamuzi gani. Japokuwa nilikuwa nimeshtushwa sana ndani ya moyo wangu, lakini nilijikaza kisabuni, nikaanza kusafisha palepale kwenye ile siti, nikakusanya na kutoa vipande vyote vya vioo, nikachukua ile dawa maalum ya kutoa madoa na kuimwagia kwenye siti yote, nikachukua brasi kubwa na bomba la maji.
Nilianza kusafisha damu zile ambazo nilikuwa najua kabisa kwamba ni za mtu, nikaendelea kupiga brashi kwa nguvu huku nikijifanya kama hakuna chochote kilichotokea. Nilipomaliza, niliendelea na siti ya pembeni yake, napo nikapasafisha, nikahamia siti za nyuma na kuzisafisha na baada ya muda, nilikuwa nimemaliza ingawa pale kwenye siti ya dereva bado kulikuwa na madoa ya damu kwa mbali.
Kumbe hakuwa Shekwavi pekee aliyekuwa akinitazama, ilionesha ni kama gari hilo lilikuwa limewekwa kama kipimo maalum kwa ajili yangu, kwani kumbe Bonta naye alikuwa amekaa sehemu an kujificha akifuatilia kila kilichokuwa kinaendelea na hata wale waliokuwa wakijifanya wanafanya mazoezi, nao walikuwa wakinifuatilia bila mwenyewe kujua.
Nilipomaliza ndipo nilipogundua kwamba kumbe nilikuwa nafuatiliwa, moyoni nikawa najiuliza sasa walitegemea nitakimbia baada ya kuona damu za mtu? Au walitegemea nitapiga kelele?
Nisingeweza kufanya hivyo kwa sababu kuanzia mazingira niliyochukuliwa na kina Bonta na wenzake mpaka muda huo, tayari ndani ya kichwa changu nilishaelewa wao ni watu wa aina gani na nimeingia kwenye kundi la aina gani na sikuona kama kuna tatizo lolote kwa sababu nilikuwa nahitaji fedha, kichwani sina elimu wala sina mtu yeyote ninayefahamiana naye.
Naomba ieleweke kwamba tayari nilishajua kwamba kundi lile linahusika na nini lakini niliamini kazi zangu mimi zitakuwa ni hizo ndogondogo tu, labda za kutumwa kununua vifaa, kusafisha magari, kuhesabu fedha na nyingine za namna hiyo.
Sikuwahi kudhani kwamba kwa kukubali moja, maana yake nimekubali mbili na tatu! Sikufikiria kwamba Bosi Mute ambaye katika hatua hizo za awali alikuwa mtu muhimu sana kwangu, anaweza kuniingiza kwenye kazi ya hatari kama kushika mtutu wa bunduki, tena nikiwa na umri mdogo kiasi hicho na ndiyo maana hata baadaye alipokuja kunigeuka, ugomvi kati yetu ulikuwa mkubwa mno.
Basi kwa kifupi ni kwamba niliendelea kufanya kazi hiyo ya kusafisha magari ambayo ilionesha yamepatikana kwa njia za kumwaga damu kwani kila nililokuwa nasafisha, ndani ilikuwa ni lazima nikute damu, maganda ya risasi, madawa ya kulevya na kadhalika.
Mimi kazi yangu ikawa ni kuyasafisha na kuondoa ushahidi wote, kisha baada ya hapo yanaingizwa gereji ambapo yalikuwa yakifumuliwa na kubadilishwa kila kitu. Yaani gari likitoka, unasema ni jipya kabisa kwani linakuwa limebadilishwa kila kitu.
Nakumbuka siku moja, majira ya mchana nikiwa naendelea na kazi, kuna gari moja liliingizwa kwa kasi kubwa na akina Bonta na kuletwa pale ‘parking’, nikaambiwa natakiwa kulishughulikia kama kawaida lakini tofauti na magari mengine yote, hili lilikuwa na jambo la tofauti ambalo nikiri wazi kwamba ulikuwa ni mtihani mkubwa kwangu.
Ndani ya gari hilo, kulikuwa na mwili wa mwanamke aliyekuwa amepigwa risasi kichwani na kufa papo hapo, lakini siti ya nyuma kulikuwa na mtoto mdogo aliyekuwa amekaa kwenye vile viti maalum vya watoto vinavyofungwa juu ya siti ili kuzuia mtoto asianguke.
Je, nini kitafuatia?

Sent using Jamii Forums mobile app
 
SEHEMU YA 14





ILIPOISHIA:
Ndani ya gari hilo, kulikuwa na mwili wa mwanamke aliyekuwa amepigwa risasi kichwani na kufa papo hapo, lakini siti ya nyuma kulikuwa na mtoto mdogo aliyekuwa amekaa kwenye vile viti maalum vya watoto vinavyofungwa juu ya siti ili kuzuia mtoto asianguke.
SASA ENDELEA...
Nilishtuka kupita kawaida, niligeuka na kutazama huku na kule, kama kawaida, kila mtu alijifanya yuko bize na kazi zake lakini niligundua kwamba karibu wote walikuwa wakinifuatilia kwa makini nitakachokifanya.
Nilifunga mlango haraka, nikanyanyua vifaa vyangu vya kazi na kugeuka huku na kule tena, bado watu walikuwa wakinitazama kwa macho ya chinichini. Kwa kuwa pale mwenyeji wangu alikuwa ni Bonta, ilibidi niweke vifaa vyangu vya usafi na kumfuata.
Alikuwa amekaa kule kwenye vifaa vya mazoezi na mkononi alikuwa na chupa ndogo ya pombe kali huku pia akivuta ‘sigara’. Nilimsogelea mpaka pale alipokuwa amekaa lakini nikagundua kwamba hakuwa akivuta sigara kama nilivyodhani kwa mbali.
Alikuwa akivuta bangi na japokuwa sikuwa nimewahi kuvuta, nilikuwa naijua harufu yake vizuri.
“Braza,” nilimuita huku nikiwa na hofu kubwa ndani ya moyo wangu. Akanionesha kwa ishara kwamba nikae, kweli nikakaa kwenye vile vyuma vya mazoezi huku nikipumua kwa nguvu. Nilishapaniki! Sikia tu hivihivi lakini usiombe kushuhudia aliyefariki kwa kupigwa risasi.
“Huu ni mtihani wa mwisho kwako, bosi anataka kukupima kama una moyo wa kiume,” aliniambia kwa sauti ya chini huku akiendelea kuvuta moshi mwingi na kuumeza kisha kushushia kwa ile pombe iliyoonesha ni kali kwelikweli maana alikuwa akikunja uso anapomeza.
“Pale pembeni ya pipa la taka, kuna mfuko mkubwa, unatakiwa kwenda kuuchukua, utaweka ndani kile ulichokiona kwenye siti ya mbele kisha utaweka juu ya lile toroli. Maelekezo mengine utapewa,” alisema Bonta huku akiwa ‘siriasi’ sana.
Sikuwahi kumuona akiwa kwenye sura kama hiyo, nilishindwa hata nimjibu nini kwani nilihisi mate yakinikauka mdomoni, akanionesha kwa ishara kwamba niiunuke na kuondoka.
Kiukweli kama nisingewahi kushikilia bomba la moja kati ya vifaa vya kufanyia mazoezi, pengine ningeanguka mzima-mzima kwani miguu ilikosa nguvu kabisa, nikawa natetemeka mwili mzima huku miguu ikigongana.
Bonta alinitazama bila kusema chochote, akawa anaendelea kuvuta mibange kwa fujo, nikashusha pumzi ndefu na kusimama vizuri kwa sekunde chache. Sikuwa na uwezo wa kukataa kazi ile ngumu na ya kutisha mno.
Nilipiga moyo konde na kushusha pumzi ndefu kwa mara nyingine, nikaanza kutembea kuelekea kule kwenye pipa la takataka.
Bado nilikuwa najua kwamba watu wote wananitazama na sijui ni nini kilinitokea, lakini nilijikuta nikipata ujasiri wa kuwaonesha waliokuwa wakinitazama kwa macho ya chinichini kwamba na mimi ni mwanaume shupavu.
Nilienda mpaka pale, kweli nikakuta kuna mfuko mkubwa ambao upo katika mfumo wa kama nailoni ngumu, wenye zipu. Nikauchukua na kuelekea kwenye lile gari. Ambacho sikuweza kukizuia ni mapigo yangu ya moyo kwenda mbio.
Basi nilipofika, niliubwaga ule mfuko chini, nikachukua tena vile vifaa vyangu vya kuoshea magari, ikabidi niendelee kujifanya kama naoshaosha lile gari kwa nje. Ilikuwa ni kama kuzuga tu ili nipate ujasiri wa kufanya ile kazi ambayo ama kwa hakika ilikuwa ni mtihani mkubwa mno katika maisha yangu.
Sikutegemea kama naweza kukutana na kitu kama hicho maishani mwangu, kichwani maneno ya mama alipokuwa ananikataza kuja mjini yakawa yanajirudia lakini nilipokumbuka kwamba ni usiku uliopita tu nimetoka kuwaachia kiwango kikubwa cha fedha nyumbani kwa ajili ya matibabu ya baba, nilijikuta nikijiambia ndani ya moyo wangu ‘potelea mbali’.
Nilichukua mfuko na kuuweka vizuri, nikafungua zipu na kuingia nao ndani ya lile gari ambalo lilikuwa likinuka damu, tena damu mbichi. Nilishindwa kumtazama yule mtu kwa jinsi alivyokuwa amefumuliwa kichwa kwa risasi, nikamvalisha ule mfuko huku nikiwa makini nisichafue nguo zangu na damu.
Mwanamke mwenyewe alionesha kuwa mtu wa makamo ya kati, uzuri ni kwamba hakuwa mnene sana kwa hiyo niliweza kumudu kumtoa pale alipokuwa, nikiwa tayari nimeshamvalisha karibu nusu nzima kwenye ule mfuko, kuanzia kichwani mpaka maeneo ya kiunoni.
Huku nikitetemeka, nilitegua siti na kumalizia kumuingiza miguu kwenye ule mfuko, nikaufunga na kuanza kuuvuta kuutoa nje ya gari. Kwa kuwa tayari mwili wote ulikuwa ndani ya ule mfuko, kwa mtu anayetazama kwa mbali angeweza kudhani labda natoa mzigo kwenye gari.
Niliushusha mpaka chini na kuuburuza mpaka pembeni, nikaenda kuchukua lile toroli na kulisogeza huku nikitetemeka mno. Niliunyanyua ule mzigo kwa nguvu zangu zote na kufanikiwa kuuweka juu ya lile toroli. Jasho jingi likawa linanichuruzika mwili mzima.
Nikiwa bado sijui nini cha kufanya, nilishtukia sauti kali ya mtoto akilia kutoka ndani ya lile gari, nikarudi harakaharaka na kufungua mlango wa nyuma, alikuwa akilia akiwa bado palepale kwenye kile kiti chake.
Moyo uliniuma sana kwa sababu nilijua kabisa malaika huyu wa Mungu hana hatia yoyote na mbaya zaidi ni kwamba asingeweza kumuona tena mama yake hapa duniani.
Nilishindwa kuyazuia machozi yasiulowanishe uso wangu. Nikabaki namtazama huku nikiwa hata sijui nifanye nini, machozi yakiendelea kunimwagika kwa wingi. Mara nilishuhudia wanaume wawili waliokuwa wamevalia maovaroli, wakija na kuchukua lile toroli, wakawa wanalisukuma kuelekea upande wa pili.
Sura zao zilikuwa ngeni kabisa kwangu, wakawa wanasukuma toroli bila hata kugeuka nyuma. Mara Bonta naye alikuja na safari hii hakuwa peke yake, alikuwa na wanaume wengine wawili ambao nao sura zao zilikuwa ngeni kwangu. Bonta alikuwa katikati yao, wakanisogelea bila kusema kitu chochote.
Bila kuzungumza chochote, Bonta alinipa ishara kwamba nimtoe yule mtoto kwenye gari, nikafanya hivyo huku bado machozi yakiwa yananibubujika. Nilisimama mbele yao huku nikiwa nimemshika yule mtoto ambaye kwa kumkadiria alikuwa na kama miaka miwili, ambaye alikuwa akiendelea kulia huku akimuita mama yake.
Bonta alimpa ishara mmoja kati ya wale wanaume, nikamuona akifunua koti lake refu, katika hali ambayo sikuitegemea, nilimuona akichomoa bastola, akachomoa na kitu kama kibomba fulani kutoka kwenye mfuko wake mwingine, akawa anakifunga mbele ya mdomo wa bastola kisha akaikoki! Nikabaki nimehamaki nikiwa sijui nini kinachotaka kufanyika.
Nilishangaa yule mwanaume eti akinikabidhi mimi ile bastola, macho yakanitoka pima! Nikamtazama Bonta ambaye sasa hivi alikuwa amebadilika kabisa uso wake, macho yalikuwa mekundu mno.
“Shoot!” alisema, akimaanisha eti nimpige risasi yule mtoto, nikawa narudi nyuma huku nikitingisha kichwa, uso wangu ukiwa umejawa na wasiwasi usiomithilika. Nikiwa naendelea kurudi nyuma, nikiwa hata sijui nataka kufanya nini kwani yule mtoto alikuwa mikononi mwangu lakini pia bastola ilikuwa mkononi mwangu.
Bonta akanipa ishara nitazame upande wa juu, macho yangu yakatua kwa mwanaume aliyekuwa amesimama ghorofani, akiwa ameegamia mabomba ya kwenye ‘balcony’, akivuta sigara na kutoa moshi mwingi. Kwa ilivyoonesha, alikuwepo pale kwa muda mrefu, akifuatilia kila kilichokuwa kikiendelea. Hakuwa mwingine bali bosi Mute.
“Huu ni mtihani wa mwisho kwako, bosi anataka kukupima kama una moyo wa kiume,” maneno aliyoniambia Bonta muda mfupi uliopita yalijirudia kichwani mwangu, nikamtazama Bonta kisha nikamtazama Bosi Mute kule ghorofani, nikawatazama na wale wanaume wengine wawili.
Niligeuka na kutazama huku na kule, kila mtu alikuwa ameacha kila alichokuwa anakifanya na kugeukia pale tulipokuwepo kutazama kilichokuwa kinaendelea. Japo Bonta alikuwa kimya lakini uso wake ni kama ulikuwa unasema ‘mbona unataka kuniangusha?’
Nikiwa bado sijui cha kufanya, nilishtukia wale wanaume wawili wamefyatuka kwa kasi ya upepo, mmoja akanipokonya yule mtoto ambaye bado alikuwa akilia na kumkalisha chini, akamuegamiza kwenye jiwe kubwa la zege, yule mwingine akanishika kwa nguvu na kunirudisha nyuma umbali wa hatua kadhaa.
“Unaishika hivi... kisha unavuta hiki kitufe ukiwa umelenga unapotaka kupiga, vuta pumzi na usizitoe mpaka usikie mlio au mtingishiko kuonesha risasi imetoka,” alisema Bonta ambaye naye alikuwa ameshanisogelea mwilini kabisa na kunishikisha vizuri ile bastola, akakichukua kidole changu kimoja na kukiingiza kwenye ‘trigger’ ya kufyatulia risasi. Kila kitu kilikuwa kikifanyika kwa kasi kubwa mno mpaka nikawa najihisi pengine nipo kwenye ndoto ya kutisha.
“Unatakiwa kufuata maelezo niliyokwambia, vinginevyo kinachoenda kutokea hapa kitakuwa kibaya sana kwenye maisha yako, hebu mtazame tena Bosi Mute,” alisema Bonta, nikageuza shingo na kumtazama kule juu, nikamuona akiwa ametoa bastola na kuielekeza pale tulipokuwepo, Bonta akawageukia wale vijana na kuwapa ishara, wote wakasogea pembeni kabisa.
“Unaweza! Unaweza kabisa, nitazame usoni,” aliniambia Bonta, nikageuka na kumtazama huku nikiendelea kulia, akanipa ishara fulani usoni ya kunitoa wasiwasi na kunihakikishia kwamba ninaweza, akaniambia nielekeze akili zangu pale kwenye tukio vinginevyo bosi Mute atanipiga mimi risasi kwa sababu hawezi kukubali nikatoka nje na kwenda kutoa siri, kwa hiyo sikuwa na cha kufanya zaidi ya kutekeleza nilichoambiwa.
Nilimtazama yule mtoto, bado alikuwa akilia sana huku na yeye akionesha kuwa na hofu kubwa ndani ya moyo wake, kufumba na kufumbua, Bonta naye alikuwa ameshasogea hatua kadhaa na kuniacha nikiwa nimesimama palepale, bastola ikiwa mkononi mwangu na Mute naye akiwa ameshaunyoosha mkono wake weye bastola kunilenga mimi.
“Eeh Mungu wangu, wewe ndiyo unaojua ukweli wa moyo wangu, nisamehe kwa hii dhambi kubwa ninayoenda kuitenda,” nilisema huku nikilia kwa uchungu usiomithilika. Sikuwahi kudhani hata siku moja na mimi nitakuwa muuaji lakini mpaka hapo tulipokuwa tumefikia, nilitakiwa kuchagua jambo moja tu, kuwa muuaji au kuuawa!
Bonta akaanza kunihesabia: “Moja... mbili... ta...!”
Je, nini kitafuatia?

Sent using Jamii Forums mobile app
 
SEHEMU YA 15




ILIPOISHIA:
“Eeh Mungu wangu, wewe ndiyo unaojua ukweli wa moyo wangu, nisamehe kwa hii dhambi kubwa ninayoenda kuitenda,” nilisema huku nikilia kwa uchungu usiomithilika. Sikuwahi kudhani hata siku moja na mimi nitakuwa muuaji lakini mpaka hapo tulipokuwa tumefikia, nilitakiwa kuchagua jambo moja tu, kuwa muuaji au kuuawa!
Bonta akaanza kunihesabia: “Moja... mbili... ta...!”
SASA ENDELEA...
Alipofikisha tatu, nilifumba macho na kuvuta kile kitufe cha kufyatulia risasi lakini cha ajabu, nilipofumbua macho nikiamini nitakuta maskini yule mtoto ameshasambaratishwa na ile risasi, nilishtuka kuona hakuna kilichotokea.
Niliisogeza ile bastola usoni na kuitazama vizuri nikihisi pengine nimekosea wakati wa kufyatua lakini hata sikuwa najua chochote kuhusu bastola. Nikamgeukia Bonta, nikamuona eti anapiga makofi kwa mbali, nikatazama kule juu ya ghorofa, nikamuona Bosi Mute akirudisha bunduki yake chini, naye akawa anapiga makofi.
Niligeuka na kumtazama kila mtu, nikaona karibu wote wanapiga makofi, nikashusha pumzi ndefu nikiwa sielewi kilichokuwa kinaendelea. Nilimuona Bonta akinisogelea kwa hatua za harakaharaka, akaja na kunishika mkono kisha akanikumbatia kwenye kifua chake kikubwa.
“Safi sana!” aliniambia huku nikiwa bado sielewi ni kwa sababu gani ananiambia vile.
“Huu ndiyo mtihani mgumu kuliko yote, mtihani wa pili utakuwa mwepesi sana kwako na naamini utaufurahia,” aliniambia, nikashusha pumzi ndefu na kutaka kumuuliza kitu lakini akanipa ishara kwamba huo siyo muda wa maongezi.
Alisogea mpaka pale yule mtoto alipokuwa amekalishwa chini akiendelea kulia, akamuinua na kumbeba kifuani kwake, akawa anambembeleza. Akamsogeza pale nilipokuwa nimesimama,, akanipa ishara kwamba nimpokee. Nikafanya hivyo huku bado machozi yakiendelea kunitoka.
Ni mtoto huyu ndiye eti niliyetakiwa kumpiga risasi kwa mkono wangu na kumuua! Nilimtazama usoni, naye alikuwa analia, nikambusu kwenye paji la uso kisha nikamkumbatia kwa nguvu sana huku nikiendelea kulia.
“Nifuate!” alisema Bonta, nikawa natembea kumfuata nyuma yake huku nikiwa nimembeba yule mtoto ambaye sasa hivi alishaanza kutulia. Tulipanda ngazi za chuma zilizokuwa ndani ya godauni lililokuwa na magari mengi yakiendelea kurekebishwa, tukatokezea juu kabisa.
Kumbe Bosi Mute alikuwa pia na ofisi nyingine juu kabisa ya godauni na muda ule wakati amenishikia bastola, alikuwa nje ya ofisi hiyo, kwenye ‘balcony’. Tuliingia mpaka ndani ambako tulimkuta akiwa peke yake, akiwa amekaa kwenye kiti cha kuzunguka, mbele yake kukiwa na ‘skrini’ kadhaa kubwa, zote zikiwa zinaonesha matukio yaliyokuwa yakiendelea ndani na nje ya eneo lote hilo.
Kitu ambacho nilikuwa sikijui ni kwamba kumbe eneo lile lote, kuanzia nje, tebna mbali kabisa mpaka ndani, kulikuwa kumefungwa kamera za ulinzi (CCTV) ambazo zilikuwa zikionesha kila kitu kilichokuwa kinaendelea. Nikashangaa sana.
“Kazi nzuri,” alisema Bosi Mute huku akisimama na kunyoosha mkono kunipa, na mimi nikampa kwa heshima. Akaniambia siku nyingine nikipewa bunduki na kuambiwa ni-shoot, sitakiwi kupoteza sekunde hata moja.
Alirudi kukaa pale kwenye kiti chake, akafungua moja kati ya droo nyingi, akatoa bunda la noti za shilingi elfu kumikumi na kulitupa juu ya meza.
“Hakikisha huyo malaika wa Mungu anafikishwa kwenye mikono salama! Tumia akili yako kujua utafanya nini, lakini nataka awe salama lakini asiache alama yoyote inayoweza kumuunganisha na sisi,” alisema Bosi Mute, nikainamisha kichwa kwa adabu kuonesha kukubali, kisha nikachukua lile burungutu la fedha na kuliweka mfukoni.
Bonta naye aliinama kwa adabu kama ishara ya utii kwa Bosi Mute kisha akatangulia yeye kutoka, nikawa namfuata kwa nyumanyuma. Tulishuka mpaka chini, Bonta akanigeukia na kuniambia kwamba mtihani niliopewa natakiwa kuufanya bila msaada wa mtu yeyote.
“Sasa nifanyeje?”
“Unaweza kwenda kumuacha kwenye maeneo ambayo watu wenye roho nzuri watamchukua na kwenda kumlea, unaweza kwenda kumuacha kanisani, msikitini, kwenye vituo vya watoto yatima na kadhalika, lakini hutakiwi kuonekana kama wewe ndiye uliyemuacha,” aliniambia Bonta, kidogo nikashusha pumzi kwa sababu angalau nilipata mwanga wa nini cha kufanya.
‘Nini kilitokea pale? Mbona mlikuwa mnanipigia makofi?”
“Ulipewa bastola isiyo na risasi kwa lengo la kukupima kama una ujasiri wa kuua! Ulipovuta ‘trigger’, ulionesha kwamba kama kungekuwa na risasi, ulikuwa tayari kumuua huyu mtoto, hicho ni kipimo cha juu kabisa katika hizi kazi zetu!” alisema Bonta, sasa nikapata picha ya kilichotokea.
Kumbe walikuwa wanataka kunipima kama nina roho ya kuua! Na kweli kwa hali ilivyokuwa, nilikuwa nimeshamuomba msamaha Mungu wangu kabla hata ya kufanya dhambi kwa sababu kwa sababu ni kweli kama kungekuwa na risasi, ningemuua mtoto wa watu.
Ujue wakati mwingine tunawalaumu tu majambazi au magaidi kuwa wana roho mbaya sana lakini kuna mitihani wanapitia wanajikuta tu tayari roho zao simeshabadilika na kuwa kama wanyama.
Na wasichokijua watu wengi, damu ya mtu ni nzito sana! Unapoanza kumwaga damu ya mtu wa kwanza, akili zako zinakuwa ni kama zimekufa ganzi na kamwe hazitaweza kurudi na kuwa sawa mpaka na wewe ufe! Ni rahisi sana kwa mtu ambaye ameshawahi kuua, kuendelea kuua tena na tena mpaka na yeye atakapouawa kinyama.
Huwezi kuyakatisha maisha ya binadamu mwenzako halafu ukabaki kuwa salama, yaani hata kama hakuna mtu yeyote anayejua, damu ya mtu ni nzito, itakufuata tu na lazima na wewe utaishia kufa kifo cha ajabu ajabu.
Kama huamini, hebu fuatilia historia za watu wote ambao unajua walishawahi kufanya mauaji uangalie mwisho wao ulikuwaje! Bahati mbaya kwangu, ni kwamba nilikuja kuujua ukweli huu tayari ikiwa ni ‘too late!’
Laiti kama ningeujua kabla mambo hayajaharibika, ningekuwa tayari hata nife mimi kuliko kuyakatisha maisha ya mtu mwingine, narudia tena kusisitiza hakuna kosa kubwa kama mauaji na hata kama utaweza kuikwepa mikono ya sheria, bado kuna hukumu fulani ya asili ambayo itakutafuna popote ulipo mpaka na wewe utakapokufa. Nitakuja kukuelezea vizuri hapo baadaye jinsi nilivyoteseka kwa sababu ya uzito wa damu za watu waliopoteza maisha kwenye mikono yangu! Hakika mimi ni mwenye dhambi.
Basi nilitoka na yule mtoto mpaka nje, sikuwa najua kuendesha pikipiki wala gari kwa hiyo njia salama ilikuwa ni kutembea kwa miguu kisha nikatafute usafiri nikiwa nje.
Kabla sijatoka, akili ilinituma kurudi kwanza kwenye lile gari, nikapekuapekua na kukuta kuna kadi ya kliniki ya mtoto pamoja na ‘chuchu’ ya bandia ambayo mtoto huyo alikuwa akiinyonya, nikaisafisha kisha nikamuwekea mdomoni, akawa ananyonya huku akinitazama sana usoni.
Baada ya kutoka nje, nilianza kutembea harakaharaka huku nikiwa nimemkumbatia mtoto huyo kifuani, mkono mmoja nikiwa na bahasha iliyokuwa na kadi yake ya kliniki. Mbele kidogo, nilisimamisha ‘bodaboda’, nikamuelekeza dereva kunipeleka Mombasa.
Nilitaka nikifika pale ndiyo nijue naelekea upande gani kwa sababu bado sikuwa naujua mji na nilikuwa na mtoto wa watu ambaye mama yake ameuawa. Kama mtu angenishtukia na kunikamata, maana yake angehisi kwamba pengine mimi ndiye niliyemuua mama yake au najua wahusika ni akina nani, jambo ambalo lilikuwa la hatari kwelikweli.
Nilitakiwa kuwa makini na hilo nililitambua, basi alinipeleka mpaka Mombasa, pale nikakodi Bajaj na kumuelekeza dereva kwamba anipeleke mjini. Ilikuwa ngumu kidogo kuelewana naye kwa sababu alitaka kujua ni mjini ipi ninayoenda mimi, mwisho tukakubaliana kwamba anisogeze mpaka Buguruni kisha nitajua mwenyewe nini cha kufanya.
Kwa bahati nzuri, yule mtoto alilala muda mfupi baadaye, kwa hiyo njia nzima yeye alikuwa akikoroma tu. Tulienda mpaka Buguruni, nikatoa noti mbili za shilingi elfu kumikumi na kumpa, wala hata sikuulizia chenji, nikateremka na kuvuka barabara. Mbele kidogo nilisimamisha teksi iliyokuwa ikipita bila abiria.
“Unaelekea wapi bosi!”
“Mjini.”
“Posta au Kariakoo!”
“Kariakoo!” nilijibu bila kufikiria kwa sababu ukweli ni kwamba sikuwa nakujua Kariakoo wala Posta zaidi ya kuwa nasikia tu kwenye bomba.
“Huyo mtoto wa nani, mbona kama namjua!” alisema yule dereva, mapigo ya moyo yakanilipuka paah!
Je, nini kitafuatia?

Sent using Jamii Forums mobile app
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom