Riwaya: Saa za Giza Totoro

SEHEMU YA 20




ILIPOISHIA:
Nilichoweza kukifanya, ilikuwa ni kuoga tu, usingizi mzito ukanipitia palepale kwenye kochi nilipokaa ili kupumzika kidogo kabla ya kurudia yale mazoezi kama Bonta alivyoniambia. Nilipokuja kuzinduka, tayari kulikuwa kumeshaanza kupambazuka, nikajishangaa imekuwaje?

SASA ENDELEA...
Nilijaribu kuinuka pale nilipokuwa nimelala lakini mwili ulikataa kabisa, viungo vyote vilikuwa vinauma mno. Ilibidi nitulie kwanza, nikashusha pumzi ndefu na kujikaza kiume, nikafanikiwa kusimama huku nikihisi kama mwili wangu unataka kupasuka kutokanana maumivu.

Ni hapo ndipo nilipoelewa ni kwa nini Bonta aliniambia kwamba nikifika natakiwa kuyarudia mazoezi yote kwanza kabla ya kulala. Kwa kuwa bado ilikuwa ni mapema sana, ilibidi nijikaze na kuanza kufanya mazoezi mepesi ili kulainisha viungo. Nilianza kwa kurukaruka taratibu, machozi yakawa yananitoka kutokanana maumivu.

Kadiri nilivyokuwa nazidi kurukaruka, maumivu yalianza kupungua na sasa viungo vikawa vinaanza kulainika, miguu ikaanza kukunjika vizuri, mikono nayo ikawa inaweza kukunjika kwa urahisi.

Nilianza kukimbiakimbia mle ndani na baada ya mwili kukaa sawa, nilirudia mazoezi yote tuliyofanya jana. Japokuwa ilikuwa bado ni asubuhi sana na kulikuw ana baridi, mwili wangu ulikuwa ukitokwa na jasho kama maji. Angalau sasa nilianza kujisikia vizuri, nikaenda bafuni kuoga kisha nikaanza kujiandaa.

Saa kumi na moja na nusu za alfajiri, tayari nilikuwa nimemaliza kujiandaa, nikatoka na kuanza kuelekea kituoni, nikapanda gari na safari ya kuelekea kambini ikaanza. Mpaka nafika, tayari ilikuwa ni saa moja kasoro za asubuhi, watu wengi tayari walikuwa wameshafika wakiendelea na kazi zao.

Kati ya wote tuliokuwa kwenye mazoezi jana, tulikuwa tumefika wanne tu, na wenzangu wote walikuwa wakichechemea kutokana na maumivu. Ile mbinu ya kufanya mazoezi asubuhi ilinisaidia sana kwa sababu angalau mimi ndiyo nilionekana kuwa ‘fiti’ japo bado mwili ulikuwa unauma kwelikweli.

Bonta aliponiona, alikuja kunisalimia huku akiwa na uso wa tabasamu, tukapeana ‘tano’ pale maana hiyo ndiyo ilikuwa salamu yetu kubwa, akaniuliza naendeleaje? Ilibidi nimsimulie kilichotokea, akacheka sana lakini akaniambia kwamba nimemfurahisha sana kwa ukakamavu niliouonesha.

Wale wengine waliendelea kufika mmojammoja na kila aliyekuwa anafika, ungeweza kudhani anaumwa kwa jinsi walivyokuwa wakiugulia maumivu. Wote tulipotimia, tulipelekwa kwenye chumba cha chini kwa chini, ambacho kilikuwa na vifaa vya kufanyia mazoezi kama ‘gym’.

Kumbe vile vyuma pale juu vilikuwa kama geresha tu, kule chini kulikuwa na sehemu kubwa ya kufanyia mazoezi ikiwa na vifaa vyote muhimu. Jamaa mmoja ambaye mara kwa mara nilikuwa namuona na Bonta, ambaye alikuwa na mwili mkubwa kwelikweli, alikuja na kuanza kutufanyisha mazoezi.

Tofauti yake ni kwamba alitufanyisha mazoezi ya kawaida tu ya kujenga mwili, na akatusisitiza kwamba tukiendelea vizuri, na sisi tutakuwa na miili iliyojengeka vizuri kimazoezi kama yeye alivyokuwa.

Niligundua pia kwamba hata mwili wa Bonta, ambao ulikuwa umejengeka vizuri sana, ilikuwa ni kwa sababu ya mazoezi maana alikuwa na kifua kipana, mikono mikubwa yenye misuli na tumbo lililotengeneza kile vijana wanachoita ‘six pack’.
Baada ya kufanya mazoezi kwa karibu saa nzima mfululizo, tulipewa muda wa kupumzika kisha tukaenda kunywa chai.

Kumbe mlemle ndani kulikuwa na kantini ambayo sikuwahi kuigundua, wahudumu wake wote walikuwa wanaume, tukapata kifungua kinywa cha nguvu kisha tukaambiwa tujiandae kwa safari ya kwenda Kazimzumbwi kumalizana na Mamba.

Watu waliposikia jina la Mamba, kila mmoja alionekana kupoteza uchangamfu usoni maana tulikuwa tunajua shughuli pevu tunayoenda kukutana nayo. Kabla hatujaondoka, kila mmoja wetu alipewa ‘ovaroli’ kama yale wanayovaa mafundi, tukavaa na kuingia ndani ya gari.
Kama ungetuona, ungeweza kudhani labda ni mafundi wa kampuni fulani wanaenda kazini lakini kumbe ilikuwa tofauti kabisa. Tulipanda kwenye magari mawili tofauti na yale tuliyotumia jana yake, na safari ya kuelekea msituni ilianza. Tulipofika, tulimkuta tayari Mamba na timu yake wameshafika, wanatusubiri, tukajipanga harakaharaka na bila kupoteza muda, kazi ikaanza.

Asubuhi hiyo tulianza kwa mazoezi ya shabaha tukiwa tumevaa maovaroli yetu, tukawekewa vitu kama sanamu za watu, zilizokuwa na michoro ya maeneo tunayotakiwa kulenga shabaha.

Alianza kwa kutufundisha kwa maelekezo kwanza huku akituonesha pia kwa vitendo, akatuelekeza sehemu za muhimu za kulenga, akatuelekeza maeneo ambayo ukimpiga mtu, unampunguza kasi ya kupambana na wewe lakini pia akatuelekeza maeneo hatari ambayo ukimpiga mtu hawezi kupona.

“Tunapoingia kazini, lazima mjue kwamba lengo letu siyo kuua watu wasio na hatia, kama tumetumwa mzigo fulani basi muhimu ni kuhakikisha mzigo unapatikana bila kusababisha vifo vya watu wasio na hatia, wananchi siyo adui zetu, adui zetu sisi ni polisi,” alisema, nikashtuka sana kusikia maneno hayo.

Kumbe wakati wananchi wa kawaida wakiwaona polisi kama ndiyo watetezi wao, kwa upande wa wahalifu, polisi huwa ndiyo adui yao namba moja. Mamba alitufundisha kabisa kwamba tunapokuwa kwenye kazi, ukimuona polisi hakuna cha ‘msalia mtume’, ni lazima umuondoe vinginevyo yeye atakuondoa wewe.

Niliwafikiria polisi, nikauona ugumu wa kazi yao! Nikazifikiria familia zao, watoto wao, ndugu zao na kadhalika, nikajikuta nawaonea huruma sana.

Hata leo baada ya kupitia mambo mengi sana, ninachoweza kukisema ni kwamba miongoni mwa watu wanaofanya kazi kubwa sana na ambao serikali inatakiwa kuwafikiria sana kwenye suala la maslahi yao, ni polisi.

Nitakueleza baadaye matukio ambayo tulikuwa tukipambana na polisi na utakubaliana na mimi kwamba ni kazi ngumu sana inayohitaji wito na moyo wa kujitoa sana, unahatarisha maisha yako kwa ajili ya kuwalinda watu wengine na mali zao, unapambana na watu wanaofundishwa kwamba wewe ndiye adui yao namba moja! Inahitaji moyo sana.

Mafunzo yaliendelea kwa muda mrefu, ikafika zamu ya kuanza kufanya kwa vitendo kile tulichofundishwa. Wengi wetu tulikuwa na uwezo mdogo sana wa kulenga shabaha na kuna wakati nilimsikia Mamba akisema kwamba hawezi kujivunia kutufundisha kwa sababu anajua ndani ya siku chache tu, wote tutakufa.

“Mkikutana na polisi nyie hakuna atakayerudi hata mmoja! Lazima ujue kulenga siyo kufyatuafyatua tu risasi, mtakufa wote kama kuku,” alisema na kuanza upya kutuelekeza. Lilikuwa somo gumu lakini taratibu tulianza kuelewa, hasa kutokana na msisitizo aliokuwa anautoa.

Kingine nilichogundua ni kwamba kumbe kushika bunduki pekee hakuna maana kama hujui kulenga shabaha! Unaweza kuwa na bunduki na ukazidiwa ujanja na mtu mwenye mshale, cha muhimu zaidi ni kujua unapiga wapi na kwa sababu gani. Baada ya kujifunza shabaha, tulihamia kwenye mazoezi ya viungo, ‘mtiti’ ukawa ni zaidi ya jana yake.

“Wewe unakula nini! Mbona huliilii kama wenzako?” uzalendo ulimshinda Mamba na kuamua kuniuliza. Aliona kila zoezi analotoa, naenda naye sawa kwelikweli, sikumjibu kitu nikawa namtazama tu. Mbinu aliyonipa Bonta ilinisaidia sana. Siku hiyo ilipita, tukaendelea na mazoezi karibu kila siku kwa muda wa siku ishirini na moja.

Huwezi kuamini, baada ya kumaliza mafunzo hayo, tulikuwa ‘tumekwiva’ kwelikweli, hata siku niliyorudi nyumbani kwenda kuwasalimia na kuwapeleka fedha za matumizi, kila mtu alikuwa akinishangaa. Nilikuwa nimebadilika ghafla kutoka kwenye uvulana na kuingia kwenye uanaume.

Mwili wangu ulikuwa umejengeka vizuri kimazoezi, kifua kilikuwa kimepanuka, mikono imejaa na hata kutembea kwangu kulibadilika, nilikuwa kama ‘mjeshi’ flani hivi. Kule kuchekacheka nilikokuwa nao awali, kuliisha, muda mwingi nikawa niko ‘siriasi’ sana.

“Kwani umeingia jeshini nini mwanangu? Maana unatisha siku hizi,” mama aliniuliza, nikashindwa kujizuia kucheka, nikamdanganya kwamba mahali ninapofanya kazi, tunafanya kazi ngumu sana ndiyo maana nimebadilika, basi akawa ananishukuru sana kwa jinsi nilivyoweza kujitoa mhanga kwa ajili ya kumsaidia baba na kuisaidia familia yetu.
Aliniambia kwamba fedha ambazo nimekuwa nikiwatumia, zimesaidia sana kubadilisha maisha ya pale nyumbani na kwamba anajivunia kuwa na mtoto mwenye moyo wa uthubutu kama mimi.

Kuna wakati aliniambia wazi kwamba anajutia uamuzi wake wa mwanzo wa kunikataza kwenda mjini kwa sababu kama ningemsikiliza, tungeendelea kuzama kwenye umaskini na pengine tungempoteza baba mapema zaidi kwa kukosa fedha za kununua dawa na za matunzo.

Nilikuwa namuitikia tu mama lakini ndani ya moyo wangu nilikuwa najua ukweli wa kila kinachoendelea, na kama na yeye angekuwa anajua, kamwe asingeniruhusu nifanye nilichokuwa nakifanya. Basi nilikaa pale nyumbani mpaka mida ya kama saa sita za usiku, nikawaaga kwamba naondoka.

Kila mtu alishangaa na afadhali siku ile nyingine nilienda na Bonta mpaka pale nyumbani, wakawa wananiuliza nitaondokaje? Niliwajibu kwamba nimekuja na teksi ya rafiki yangu kutoka mjini na alikuwa ananisubiri stendi. Haikuwaingia akilini lakini mwisho hawakutaka kunikwaza hasa kutokanana mchango wangu nilioanza kuuonesha kwenye familia, nikaagana nao na kutoka.

Ni kweli nilikuwa nimekuja na teksi kutoka Dar es Salaam lakini nilimwambia dereva anisubiri pale stendi kwa sababu sikutaka niwe gumzo pale kijijini. Kusafiri na teksi kutoka Dar halikuwa jambo dogo. Basi nilienda mpaka stendi ambako nilimkuta dereva akiwa amelala kwenye siti yake, nikamuamsha na muda mfupi baadaye, safari ilianza.

Kwa mujibu wa sheria za bosi Mute, ilikuwa ni makosa kulala nje ya nyumbani kwako, kwa hiyo ilikuwa ni lazima nirudi mpaka Sinza, bila kujali nitafika saa ngapi. Tulisafiri mpaka Dar, yule dereva akanipeleka mpaka Buguruni kama tulivyokuwa yumekubaliana, nikamlipa fedha zake kisha nikapanda bodaboda mpaka nyumbani kwangu, Sinza.

Mpaka naingia ndani, ilikuwa ni karibu saa tisa za usiku, nikaoga na kwenda kulala maana asubuhi nilikuwa natakiwa kuwahi kazini. Nililala kidogo tu, alarm ya kwenye simu ikaniamsha maana niliitegesha iniamshe saa kumi na moja na nusu. Niliamka nikiwa mchovu, nikaenda kuoga na kuanza kujiandaa, nikaenda mpaka kazini.

“Leo kuna kazi usiku, bosi atawapa maelekezo,” aliniambia Bonta nilipoingia tu. Sikuwa najua ni kazi gani lakini moyoni nilijua kwamba kazi imeanza. Kweli mida ya kama saa nne hivi za asubuhi, Bosi Mute alituita kwenye chumba cha mikutano.

Kwa kawaida, alikuwa akiitisha kikao, watu wote wanaacha kila walichokuwa wanakifanya na kwenda kumsikiliza. Muda mfupi baadaye alikuja na kutangaza kwamba siku hiyo kutakuwa na kazi, akawataka watu wote wanaohusika na maandalizi kuhakikisha kila kitu kinakamilika haraka iwezekanavyo.

Watu wengi walionekana kumuelewa haraka, lakini mimi na wale wenzangu tuliomaliza mafunzo pamoja, tulikuwa gizani bado. Akawataka watu wote kutoka isipokuwa sisi ambao sasa tulikuwa tumebatizwa jina la Kikosi B.

Tulibaki tumekaa kwenye viti vyetu, watu wote walipotoka, akatutaka tusogee mbele kulikokuwa na kama ubao mdogo mweupe, akachukua ‘marker pen’ na kuanza kutuelekeza jambo. Kila mmoja akawa na shauku ya kusikia hiyo kazi inahusu nini?

“Leo saa kumi na mbili kwenye benki ya ...(akaitaja jina), kuna mzigo utateremshwa. Mnatakiwa kuhakikisha tunaupata mzigo huo kwa gharama yoyote na kuufikisha kambini kwa sababu ni wa kwetu,” alisema, moyo wangu ukanilipuka paah!

“Tunaenda kuvamia benki?” nilijiuliza nikiwa ni kama siamini. Aliendelea kutuchorea mchongo mzima unavyotakiwa kufanyika, na akasema hatutaenda wote, bali watachaguliwa wachache kati yetu watakaoungana na Kikosi A kwa ajili ya kazi hiyo. Moyoni nikawa namuomba Mungu nisiwe miongoni mwa watakaochaguliwa.
Je, nini kitafuatia?

Sent using Jamii Forums mobile app
 
SEHEMU YA 21


ILIPOISHIA:
“Tunaenda kuvamia benki?” nilijiuliza nikiwa ni kama siamini. Aliendelea kutuchorea mchongo mzima unavyotakiwa kufanyika, na akasema hatutaenda wote, bali watachaguliwa wachache kati yetu watakaoungana na Kikosi A kwa ajili ya kazi hiyo. Moyoni nikawa namuomba Mungu nisiwe miongoni mwa watakaochaguliwa.
SASA ENDELEA...

“Kila mmoja akae tayari, muda wa kuondoka utakapofika mtatangaziwa waliochaguliwa,” alisema Bosi Mute wakati akikamilisha kutupa mchongo wa kazi hiyo. Aliondoka na kutuacha mle ndani, tukawa tunatazamana, kila mmoja akiwa kimya kabisa.

Basi baadaye tulitoka na kila mmoja akaendelea na kazi yake maana licha ya kazi hiyo, kila mtu alikuwa na kitengo chake, mimi nikaelekea kule kwenye kazi yangu ya kuosha magari. Kulikuwa na magari kama matatu hivi yaliyoingia jana yake, basi nikavaa nguo za kazi na kuanza kuyaosha huku mawazo kibao yakiendelea kupita ndani ya kichwa changu.
Ilipofika kama saa tisa hivi za mchana, magari mawili, Toyota Noah, yote yakiwa na rangi nyeusi na vioo vya tinted, yaliwasili na kuingia pale ndani. Nikaona pilikapilika zimeanza, nikajua sasa mambo yamewiva.

Kila mtu aliacha alichokuwa anakifanya na kuanza kuangalia ni nini kinachoendelea, nilimuona Bonta akiwakusanya wale wenzake ambao wote walikuwa wakubwa kwetu. Wakaingia kwenye chumba cha mikutano, sijui walikuwa wakijadiliana nini lakini muda mfupi baadaye, tulianza kuitwa mmojammoja.

Na mimi nilipoitwa, niliacha kila kitu na harakaharaka nikaelekea kwenye kile chumba cha mikutano huku mapigo ya moyo yakinienda mbio kwelikweli. Nilipofika, niliwakuta wenzangu watatu ambao tulikuwa pamoja kwenye Kikosi B, kwa hiyo na mimi nikawa wa nne.

Muda mfupi baadaye, yaliletwa masanduku mawili, yakawekwa pale mezani na Bonta akatuambia kila mmoja anatakiwa kuanza kujiandaa. Masanduku yalifunguliwa, la kwanza lilikuwa na nguo vikiwemo viatu kama vile wanavyovaa wanajeshi na makoti marefu meusi, na lile lingine lilikuwa na bunduki.

Tukaambiwa kila mtu achague vitu vinavyomfaa, tukawa tunatetemeka kwelikweli. Walianza akina Bonta, wakachukua vya kwao, ikafika zamu yetu. Hakukuwa na muda wa kupoteza, kwa hiyo kila mtu alichukua vitu vyake na tukaanza kubadilisha mlemle ndani kama tulivyokuwa tukipewa maelekezo.

Muda mfupi baadaye, kila mmoja alikuwa ameshavaa, kiukweli nguo hizo zilitubadilisha kabisa, sasa tukawa kwenye mwonekano wa kijambazi kwelikweli. Tulipewa pia kofia na miwani myeusi, baada ya kumaliza, Bosi Mute alikuja na kuanza kutukagua mmoja baada ya mwingine.

Ni kama alijua jinsi sisi ambao ndiyo ilikuwa mara yetu ya kwanza tulivyokuwa na hofu, akawa anatutoa hofu na kutuambia tunatakiwa kujiamini. Akaendelea kutupa mchoro wa jinsi kazi inavyotakiwa kufanyika na mwisho akatuambia kwamba Jombi ndiye atakayekuwa kiongozi wa msafara.

Sikuwa namjua sana huyo Jombi zaidi ya kuwa namuona mara mojamoja pale kambini. Alikuwa ni kipande cha mtu, amekwenda hewani halafu ‘amepasuka’ kwelikweli kutokana na mazoezi. Muda wote macho yake yalikuwa mekundu kama ‘nyanya’ na sikumbuki kama nimewahi kumuona akitabasamu au kucheka tangu nianze kumuona.

Kila mmoja alikabidhiwa bunduki yake, wale wakubwa wakachukua mbilimbili, bunduki kubwa na bastola, sisi tukapewa mojamoja. Baada ya hapo, tulitengeneza kama duara hivi, Bosi Mute akiwa katikati, akawa anaendelea kututoa hofu na kusisitiza kwamba anatuamini na hatuwezi kumuangusha.

Baada ya hapo, tulishikana mikono wote kwa pamoja kisha tukagongesheana ngumi na harakaharaka tulitoka kule nje, yale magari yalikuwa yamesogezwa mpaka mlangoni, tukaingia kwa makundi mawili, kila moja likiwa na mchanganyiko wa wakubwa wawili na wadogo wawili. Ukichanganya na madereva, kila gari lilikuwa na watu watano, safari ikaanza.

Tulitoka kwa mwendo wa kasi huku watu wote wakiwa wanatutazama, tukaingia barabarani na magari yakawa yanakimbia kwa kasi kubwa sana. Sikuwa nawajua madereva ni akina nani lakini walionesha kuwa ni wazoefu sana.

Safari yetu iliishia kwenye mtaa mmoja wenye pilikapilika nyingi, eneo ambalo baadaye nilikuja kulitambua kwamba ni Tandika. Tulisimama kwenye barabara ya vumbi ya mtaa huo, mita chache kutoka kwenye barabara ya lami.

Dakika chache baadaye, tuliona yale magari yanayotumika kubebea fedha na kuzisambaza kwenye benki mbalimbali, likipita kwenye barabara ya lami huku nyuma likiwa linasindikizwa na gari la polisi. Kwa wanaoyajua magari ya kubebea pesa watakuwa wanaelewa vizuri, lilikuwa ni kama Hiace ndogo lakini likiwa limezibwa pande zote.

Harakaharaka madereva walipeana ‘signal’, lile gari la mbele ambalo ndiyo nililokuwa nimepanda mimi, likaondoka kwa kasi na kuingia kwenye barabara ya lami, tukawa tunalifuata lile gari lililobeba fedha na lile gari jingine, liligeuza na kupita mtaa wa pili, sikuelewa linaelekea wapi.

Kulikuwa na magari mengine kadhaa katikati yetu, dereva akawa anajaribu kuyapita kwa fujo, mwisho likabakia gari moja mbele yetu, kisha gari la polisi halafu ndiyo lile gari lililobeba fedha.

Jombi ambaye tulikuwa naye kwenye gari moja, alitoa ishara kwamba kila mmoja ajiandae kwa kazi, huku nikitetemeka, niliitoa bunduki yangu niliyokuwa nimeivaa shingoni na kuificha ndani ya koti refu, nikaishika vizuri na kutoa ‘safety lock’, tayari kwa chochote.

“Gari litakaposimama tu, tunawaangusha kwanza hawa waliopo kwenye gari la polisi, wewe na wewe mtabaki kutoa back-up, hakikisha yeyote anayesogea mnamuangusha,” aisema Jombi huku akinioneshea mimi na yule mwenzangu, tukatazamana huku kijasho chembamba kikiwa kinatutoka.

Lile gari la lilikatiza na kuingia upande wa kulia, gari la polisi nalo likafuatia. Dereva wetu alipunguza mwendo kidogo, akalitoa gari barabarani, tukashuhudia yote mawili yakienda na kusimama nje ya tawi dogo la benki. Askari waliwahi kushuka, wakawatawanya watu wote waliokuwa nje ya ile benki.

Kulikuwa na skari kama sita hivi, wote wakiwa na silaha lakini pia kulikuwa na askari wengine kwenye lile gari lenye fedha ambao wao walivaa nguo za tofauti, tukawaona pia walinzi wa ile benki wakiungana nao kuhakikisha hakuna kinachoharibika.

Hata kabla ya tukio lenyewe, nilishajua kwamba hatuwezi kufanikisha tunachoenda kukifanya kwa sababu kwa hesabu za harakaharaka, wao walikuwa wengi kuliko sisi.

Kumbe dereva alikuwa anasubiri tu maelekezo, Jombi alipotoa ishara tu, dereva alikanyaga mafuta kwa nguvu kisha akakata kona na kuelekea pale wale askari walipokuwa wametanda.

Wakati wale askari wakishtuka na kuelekezea mitutu yao kwenye gari letu, lile gari jingine lilitokea upande wa pili, kwa kasi ileile, kwa hiyo wakawa ni kama wamepatwa na kiwewe, ndani ya sekunde chache tu, wote tulikuwa tumeshashuka kwenye magari yote mawili kwa staili ya kikomando kama tulivyofundishwa kule porini, tukawa tumewazunguka wale polisi na walinzi.

Jombi ndiye aliyekuwa wa kwanza kufyatua risasi, na ya kwanza ilimlenga mmoja kati ya wale askari, tena kichwani! Akadondoka chini kama mzigo, kilichofuata baada ya hapo ilikuwa ni kama uwanja wa vita.

Tuliwafyatulia mvua ya risasi kutoka pande mbili, nao wakawa wanajibu mapigo lakini kwa kuwa tulikuwa tumewazunguka, tuliwazidi ujanja. Ndani ya sekunde chache tu, watu wote walikuwa chini, si polisi, si walinzi, watu waliokuwa jirani wakawa wanakimbia huku wakipiga kelele, kila mmoja akiokoa maisha yake.

Kama tulivyoelekezwa, mimi na yule mwenzangu tulibaki kama ‘back-up’ kuhakikisha hakuna mtu anayesogea kwenye eneo la tukio, Jombi, Bonta na wengine kutoka kwenye lile gari, wakakimbilia mpaka kwenye lile gari huku wakiendelea kufyatua risasi.

Kwa kuwa tayari gari lilishakuwa limefunguliwa na sanduku la fedha kutolewa, hawakupata shida, wakaanza kusaidiana kuliburuza huku risasi zikiendelea kurindima.

Dereva wa lile gari letu alilisogeza mpaka pale karibu na lile sanduku kwa kasi mithili ya magari ya mashindano, Akina Jombi wakalibeba lile sanduku lililoonekana kuwa zito kwelikweli na kuliingiza ndani ya gari. Waliingia ndani ya gari na dereva akaondoka kwa kasi kubwa, sekunde chache tu baadaye tayari walishaingia barabarani.

Kimbembe kikabakia kwetu sisi wawili tuliobaki kutoa ‘back-up’ kama tulivyoelekezwa, lile gari la pili lilikuwa limepaki kama mita hamsini hivi kutoka pale tulipokuwepo, kwa hiyo ilikuwa ni lazima tulikimbilie haraka iwezekanavyo na kuungana na wale wenzetu wawili ambao nao walibaki kama ‘back-up’, kibaya ni kwamba wote tulikuwa ni kutoka Kikosi B.

Tukiwa tunalikimbilia kwa tahadhari kubwa huku tukifyatua ovyo risasi, tulishtukia magari mengine mawili ya polisi yakiingia kwa kasi ya kimbunga, askari wengi wakaruka kabla hata hayajasimama na kuanza kutufyatulia risasi kama mvua.
Je, nini kitafuatia?

Sent using Jamii Forums mobile app
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom